KICHAKA
Member
- Jun 17, 2009
- 58
- 9
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Machi 14, 2010
Machi 14, 2010
Utangulizi
Historia yangu
Tangu nikiwa mdogo nimejihusisha katika harakati mbalimbali zinazohusu kutetea haki za makundi ambayo nimekuwa nayo na jambo hili kwa kiasi kikubwa ndilo lililonisukuma kusomea taaluma ya sheria. Ninao uzoefu wa kina baada ya kufanya kazi za ndani ya nchi na kimataifa. Nimefanya kazi na Umoja wa Mataifa nchini Msumbiji sambamba na hapa Tanzania katika mahakama ya kesi za mauaji ya kimbari ya huko Rwanda, ICTR.
Katika maisha yangu nimeweza pia kuwa kiongozi katika ngazi mbalimbali. Kwa sasa nashikilia nafasi ya Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha na Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM Taifa. Nafasi hizi nimezipata kutokana na historia ya uwajibikaji wangu usiotiliwa shaka na moyo wangu wa kujitoa katika kusaidia kufanikisha majukumu yanayokuwepo mbele yetu katika taasisi yoyote niliyobahatika kufanya nayo kazi.
Nini maana ya Historia Hii
Kwa nini nilifungua kesi
· Imani yangu kuwa binadamu wote sawa na kwamba haki ya binadamu inayokwapuliwa hupatikana katika vyombo vya sheria. (Katika shahada yangu ya pili nimesomea masuala haya ya haki za binadamu na demokrasia)
· Utambuzi wangu kuhusu mahakama kuwa chombo cha kutenda haki, kinachosimamia haki za kila mtu anayedhulumiwa na kunyanyaswa bila kubagua. Nikiwa mhitimu wa taaluma ya sheria na pia muhanga wa tukio kupigwa na kutishiwa bastola nililofanyiwa na Christopher Ole Sendeka, niliamini njia muafaka ni hii ya kutumia mahakama kupata haki yangu.
· Tafakari niliyofanya baada ya kubaini kuwa, mshtakiwa Ole Sendeka ana rekodi ya tuhuma za uhalifu wa kutishia na tabia nyingine chafu katika jamii. Katika tafakari hii nilitazama matukio na historia yake na kubaini kuwa, amekuwa akifanya matukio mengi lakini kwa kutumia mfumo wa kimila na mifumo ambayo siyo rasmi, amekuwa akifanikiwa kuzima matukio hayo. Nitataja matukio machache kama ifuatavyo;
I. Kumtishia kwa bastola ndugu Paulo Yamat ya tarehe 20 Mei 2001. Baada ya tukio hili kesi yenye RB namba KIB/IR/282/2001 ilifunguliwa na kisha kufutwa baada ya Sendeka kutumia vikao vya wazee wa kimila. Maelezo ya vikaohivyo yapo..
II. Tukio la kumchokoza, kumtishia na kugombana kati yake na Marehemu Mzee Soipe aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri na mzee wa Kimila.
III. Tena, kuna tuhuma za kumpachika mimba mwanafunzi na kumfanya kupoteza haki yake ya kusoma. Upo ushahidi wa kesi aliyofunguliwa kuhusiana na tuhuma hii lakini ilifungwa katika mazingira ya kutatanisha. Nisisitize hapa, juzi nilikuwa nikimuona Mama Salma akizungumza na chama cha walimu wanawake, ambao walikuwa na kampeni ya kupambana na mimba mashuleni, nadhani nitumie fursa hii kumuomba Mama Salma aanze na Simanjiro maana huko kuna viongozi wasiotambua maana ya elimu na ambao wanaonyesha mfano mbaya kwa jamii yetu.Inawezekana tabia hii pia akawa anaifanya kwa kuwa yeye mwenyewe alipata division 0 katika matokeo yake ya kidato cha sita, hivyo anaona wengine hawana haki ya kupata elimu bora kwa kuwa yeye alishindwa.
IV. Akiwa mkuu wa utawala wa UVCCM alipata tuhuma za kumpiga aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM wakati huo na sasa Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es Salaam ndugu Guninita
V. Akiwa na nafasi hii hii ya ubunge, zipo tuhuma za yeye kumtemea mate mbunge mwenzake. Lakini la kuashangaza hapa ni kuwa, vyombo vya habari hasa vya swaiba wake Mengi, vimemfanya mtu huyu kuonekana katika jamii kuwa ni mwenye haki na mtetezi wa wanyonge. Hii ni hali mbaya sana kwa kuwa inapotosha ukweli na kuwafanya wananchi wa nchi hii kutopata watu wa kweli wa kuwaamini na wanaoweza kusimama na kuwa mfano bora wa jamii yetu.
Kwa mtindo huo huo usio rasmi aliweza kuwatumia wazee wa kimila, viongozi wa kidini na watu wengine maarufu katika maeneo yetu ya Umasaini ili niitwe katika vikao vyetu vya kimila ili niweze kumsamehe. Hii imekuwa historia yake, na amefanya mfumo huo kuwa kinga yake. Ni wazi katika mfumo huo amefanikiwa. Binafsi sikuona umuhimu wa kuendeleza orodha ya wahanga ambao wamekwapuliwa haki zao na Sendeka kwa kutumia mbinu ya mila. Niliamua kwenda mahakamani kutafuta haki yangu ili iwe fundisho kwake na kwa wale wote waliopewa dhamana ya uongozi wa wananchi na wenye mali. Tena nililenga kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kuheshimu utawala wa sheria.
Nini matokeo
· Matumizi ya vyombo vya habari ambavyo vilikuwa vina lengo la kuandika habari potofu na zile tu ambazo zinanikandamiza mimi. Hapa nazungumzia vyombo vya habari vya IPP. Na kwanza nitambue uwepo wa waandishi kutoka katika vyombo hivi, najua wazi kuwa nafasi yenu katika mioyo yenu ni safi sana na wala hamkuhusika kwa mioyo yenu kufanya jambo hili ambalo ni kinyume na taaluma yenu. Ndio maana nimewaita hapa pamoja na wenzenu, najua kulikuwa tu na mashinikizo fulani yaliyosababisha taarifa za Televisheni na habari za magazeti ya kampuni hii kuwa na mlengo huo wa kunikandamiza mimi. Ndugu waandishi wa habari, niwakumbushe tu jambo hili; hivi kweli zipo kesi ngapi nchini ambazo hazipati kuonyeshwa katika televisheni na badala yake iwe hii ya kwangu tu? Mnaweza kujiuliza hii ililenga nini?Mimi ni kijana mdogo tu kutoka katika jamii ya wafugaji, sasa nguvu ile ya kunikandamiza vile ililenga kitu gani?
· Kuingia kwa mfanyabiashara Reginald Mengi tangu siku ya kwanza ya kutajwa kesi ambapo yeye mwenyewe alihudhuria mahakamani na kisha kufuatia taarifa za kupotosha jamii kuhusiana na kesi hiyo. Vyombo vya IPP, vilinihusisha mimi kutumwa na wanasiasa na hasa Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kwenda kumshtaki Sendeka. Lengo la kumuingiza Lowassa katika kesi hii lilikuwa kujitafutia umaarufu kwa Sendeka mwenyewe na kutafuta huruma na kusaka misaada ya kumsaidia katika kesi ile hasa kwa wabaya wa mheshimiwa Waziri Mkuu mstaafu. Upotoshaji huu ni wazi ulilenga kupotosha maana nzima ya kesi yangu na kukwapua haki yangu mahakamani. Naomba nisisitize hapa, kabla ya kufungua kesi hii na kwa kuwa ilitokea katika kikao ambacho Lowassa alikuwepo kama kiongozi rasmi, yeye binafsi akiwa na Askofu Laizer waliniiita nami nikaitikia wito wa kuwaona. Hoja yao ilikuwa nijadiliane na Sendeka ili nimalize jambo hilo kwa taratibu zetu. Nilitafakari yote waliyonieleza lakini, mwisho niliwashukuru na kuwaeleza msimamo wangu wa kuamini katika utawala wa sheria. Lakini pia ndugu waandishi nieleze pia kidogo, mimi nafahamu vizuri sana athari za kutofautiana ama kisiasa au kibiashara kwa mzee Mengi na baadhi ya watu hapa nchini, mfano anaweza kuwa rais mstaafu Benjamin Mkapa ambapo mtaona namna ambavyo amejitahidi kupitia vyombo vyake kumchafulia taswira kiongozi huyo wa nchi hii. Sawa tu mimi ni kijana wa familia duni, lakini naamini katika nguvu ya Mungu kwa kuwa katika yeye siku zote haki ya mtu haipotei. Haya nayaona kama majaribu na pepo wa Ibilisi tu, mwisho nitabakia nimesimama na nikiwa imara zaidi.
Kutokana na mambo haya niliyoyaeleza hapo juu, naamini ilikuwepo mbinu chafu iliyochezwa kuhakikisha kuwa sipati haki yangu mahakani. Kwa mfano ni pale ndugu Telele ambaye alikuwa shahidi muhimu wa serikali dhidi ya Sendeka kukanusha ukweli wa kuona tukio la shambulio la Sendeka na baadaye kuwa ni mhusika na mjumbe wa kamati ya maandalizi ya mapokezi ya Sendeka baada ya kutangazwa kufutiwa mashtaka.
Nilijiuliza pia tangu siku ya kwanza nilipoingia mahakamani pale nilipomuona Mzee Mengi ambaye ni mmiliki mkubwa wa vyombo vya habari nchini, nikajiuliza kulikoni? Nikatafakari na kuwaza labda mzee huyu ambaye ni mchimbaji mkubwa wa madini ya Tanzanite wilayani Simanjiro ni swahiba wa karibu wa Sendeka katika maslahi yao binafsi. Najua uwekezaji huu wa Mengi wilayani kwetu hauna manufaa ya wazi kwa wakazi wa Simanjiro zaidi yake yeye na swahiba wake Sendeka. Labda hiki ndicho kilichomleta yaani kusimamia maslahi ya mdau mwenzake katika kutafuna maliasili za Simanjiro.
Naomba ieleweke kuwa, kesi yangu haikuwa na haitakuwa na mahusiano ya aina yoyote ya kisiasa ama ya kundi fulani. Sikushinikizwa, sikutumwa na wala sikumtuma Sendeka kunishambulia baada ya kushindwa nguvu ya hoja. Sikulazimishwa kwenda mahakamani kumshitaki kama ambavyo vyombo vya habari vya IPP na washirika wao wanavyotaka kuiaminisha jamii ya Kitanzania.
Nimesimamia hili kwa sababu naamini mahakama ndicho chombo kinachoweza kumsaidia mnyonge yeyote hapa nchini kupata haki yake. Imani hii nitabaki nayo siku zote za maisha yangu na nitakuwa tayari kuwasaidia wengine kuipata haki hiyo kwa namna ninavyoweza kutokana na taaluma yangu ya sheria na utashi wangu binafsi.
Hitimisho
Baada ya kushauriana na wakili wangu, ndugu zangu na wengi wenye mapenzi mema nami ambao wanaamini katika mfumo wa sheria, haki na uhuru wa mahakama; nimeamua yafuatayo;
1. Kuiomba serikali kwa kuwa ndiye mshtaki katika kesi hii kufikiria namna ya kukata rufaa katika kesi hii kwa kuwa inaonyesha kulikuwa na mazingira yaliyojengwa mapema kabisa ili kupoteza maana ya kesi hii wakati ikisikilizwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha. Mnaweza kuona hata tukio la shahidi mmoja aliyetakiwa kutoa uashahidi na serikali kisha anakuwa mmoja wa wana kamati ya maandalizi ya mapokezi ya mashatakiwa.
2. Ni wazi kuwa binafsi sijaridhishwa na hukumu iliyotolewa naamini kuwa Sendeka ana kesi ya kujibu. Lakini nisisitize pia hapa, ninayo imani kubwa na sekta ya mahakama na vyombo vingine vya dola hapa nchini hivyo kuteleza katika ngazi moja siyo kuwa ni mwisho wa mahakama hiyo kutoa haki katika kesi hii. Naamini mahakama na vyombo vinavyohusika vya serikali vitaungana nami kama ambavyo vimeshafanya katika jitihada za kutafuta haki yangu mpaka ipatikane.
Nawaombeni ndugu zangu wana habari kuwa, tujenge Tanzania yenye kujali habari zilizofanyiwa utafiti na za kweli. Tufikirie mara mbili mbili kabla ya kuandika na tutazame kwa mfano; kama ingekuwa ni wewe, ndugu yako ama mtu mwingine yeyote anafanyiwa jambo na kisha wanaoandika wanapindisha ukweli, je ungefurahia jambo hilo?
Niwafahamishe pia ndugu zangu wa Simanjiro, mimi nimelelewa vema kwa mila zetu, naziheshimu sana. Tena nathamini sana maamuzi ya wazee wangu wa Kimila na kufungua kwangu kesi hakukulenga na hakutalenga kuwadharau ama kuwapotezea heshima. Nilibaini kuwa huu ni uamuzi sahihi wenye lengo la kusaidia jamii yetu dhidi ya wapotoshaji wa mila. Mila zetu hazihamasishi ukorofi na tabia ya kutisha ama kupiga watu. Mila zetu zinahubiri upole, udugu na urafiki na sio mmoja kujigeuza mkubwa kwa kila anayekutana naye na wakapingana kwa hoja.
Nakushukuruni kwa kunisikiliza na asanteni sana.
James Millya