nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Saturday, 22 October 2011 09:31 |
Patricia Kimelemeta SERIKALI imezitaka hospitali na taasisi binafsi zinazotoa huduma ya afya nchini kutoa bure kwa wazee, walemavu, watoto chini ya miaka mitano na wananchi wasiokuwa na uwezo wa kulipia huduma hiyo. Hatua hiyo imekuja baada ya kuwapo kwa malalamiko kwa hospitali hizo kudaiwa kutoza kiwango kikubwa cha fedha jambo ambalo limesababisha wananchi wengi kushindwa kumudu na kukimbilia kwenye hospitali za Serikali. Akizungumza kwenye Mkutano wa Chama cha Watoa Huduma ya Afya Binafsi (APHFTA) Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Lucy Nkya, alisema kutokana na hali hiyo, hospitali na taasisi hizo zinapaswa kupunguza gharama ili kila mmoja aweze kupata matibabu hata kama maeneo hayo hakuna hospitali au vituo vya afya vya Serikali. Dk Nkya alisema ili kufikia malengo ya milenia mwaka 2015, Serikali imepanga kuboresha sekta ya afya ikiwamo kutoa huduma bure kwa makundi maalum ambayo ni walemavu, wazee, wasiojiweza na watoto chini ya umri wa miaka mitano. Gharama zinazotozwa na hospitali, taasisi na vituo binafsi vya afya ni kubwa, wananchi wengi wanashindwa kumudu jambo ambalo limesababisha kwenda umbali mrefu kutafuta hospitali za Serikali, kutokana na hali hiyo Serikali imewataka kupunguza gharama hizo, alisema Dk Nkya. Aliongeza kuwa hadi sasa idadi ya hospitali na taasisi hizo ni kubwa, hivyo basi kwa pamoja wanaweza kutoa huduma hiyo na kupunguza mrundikano wa wagonjwa katika hospitali za Serikali. Waziri alisema ili kuyafikia malengo ya milenia, ni wajibu wa sekta binafsi kushirikiana na Serikali kwa suala zima la utoaji huduma bora za afya, iwe mijini au vijijini, jambo ambalo linaweza kuleta maendeleo na wananchi kuwa na imani na Serikali yao. |