nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
THURSDAY, 20 OCTOBER 2011 19:27 NEWSROOM
* Awakana CHADEMA, awaonya Watanzania
MFANYABIASHARA maarufu nchini, Jaffer Sabodo, amesema hajahama na wala hana mpango wa kukihama Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho amekuwa mwanachama kwa zaidi ya miaka 40.
Sabodo alisema baadhi ya kauli kali ambazo amekuwa akizitoa dhidi ya CCM, hazina maana kuwa anaichukia, isipokuwa zinalenga kukikosoa Chama ili kiendelee kuwa imara katika kuwaongoza Watanzania na kuharakisha maendeleo yao. Hayo aliyasema jana alipozungumza na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara), John Chiligati nyumbani kwake, Upanga, Dar es Salaam na kuwataka wana CCM na wananchi kwa jumla wasimwelewe vibaya.
"Siwezi kuondoka CCM ambako nimekuwa mwanachama kwa zaidi ya miaka 40, CCM bado Chama kizuri, kina uzoefu wa kuongoza, isipokuwa ndani yake kuna baadhi ya viongozi hawaitakii mema, ndiyo maana wakati mwingine nakemea kwa kuwa siko tayari kuona Chama changu kikiteketea," alisema Sabodo. Alisema haoni chama mbadala cha CCM ambacho kinaweza kushika dola na kuongeza kuwa, "Vyama vyote vya upinzani havina uzoefu wa kuongoza nchi."
Alitoa toa wito kwa wananchi kutofanya makosa ya kufanya majaribio ya kuwapa ridhaa wapinzani kuunda serikali. "Nawaomba Watanzania wenzangu, tusifanye majaribio ya kuwapa CHADEMA au chama kingine chochote zaidi ya CCM kuongoza serikali kwa kuwa havina uzoefu, hatuwezi kufanya majaribio ya kuliweka rehani Taifa," alisema mfanyabiashara huyo.
Kuhusu msaada wa sh. milioni 100 alizotoa hivi karibuni kwa CHADEMA za kuchimba visima vya maji, alisema ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kuwa visima vitakavyochimbwa vitasaidia wananchi wote bila kujali itikadi zao za siasa.
Alisema amepanga kuchimba visima 200 katika majimbo yote nchini, bila kujali wabunge wa majimbo hayo wanatoka vyama gani kwa kuwa lengo lake ni kuwasaidia Watanzania na kutekeleza kwa vitendo Ilani ya uchaguzi ya CCM.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Chiligati alimshukuru Sabodo kwa kutoa msimamo wake huo kwa kuwa unamaliza minong'ono ya baadhi ya wanachama wa CCM na wananchi kwa jumla juu ya msimamo wa mfanyabiashara huyo ndani ya Chama.
"Nitawajulisha wanachama wenzako wa CCM na wananchi kwa jumla, kwamba bado uko nao kwa hali na mali ndani ya Chama chetu kwa ajili ya ustawi wa taifa letu, kauli yako imemaliza minong'ono kwamba umehama au una mpango wa kuhama CCM," alisema.
.