Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,354
- 33,191
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba.
Chama cha Wananchi (CUF) kimesema serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ni wavivu wa kufikiri, hali ambayo kila mwaka inawafanya washindwe kupata vyanzo vingine vya mapato.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, amesema serikali imeg'ang'ania kuongeza kodi katika sigara, pombe, mvinyo, na ushuru wa magari.
Jana Lipumba aliainisha vyanzo mbalimbali vya mapato ambavyo alisema kama serikali ingeviwekea kipaumbele vingeweza kuwakwamua wananchi kutoka katika umaskini.
Kadhalika, alisema mapato ya ndani ya serikali yaliyotangazwa kukusanywa kwenye bajeti ya mwaka huu 20010/2011 yanayofikia trilioni sita hayawezi kufikiwa.
Lipumba alisema kama wao wangepewa fursa ya kuandaa bajeti wangejikita katika kukusanya mapato kutoka sekta ya madini.
Sekta nyingine ambazo alisema zinatoa mapato mengi ni magogo yanayouzwa nje ya nchi na kuondoa misamaha ya kodi mbalimbali ikiwemo ya wafanyakazi wa serikali kutolipa ushuru wanapoagiza magari.
Eneo lingine ni kudhibiti matumizi mabovu ya fedha za serikali ambapo alisema asilimia 30 ya fedha hizo zinaliwa na watu wachache.
Alisema makampuni ya madini amekuwa yakisingizia kuwa hayapati faida wakati katika soko la dunia bidhaa hiyo inaonekana kupanda bei kila kukicha.
Upande wa magogo yanayouzwa China, alisema wao wana takwimu sahihi na wanajua wananunua kiasi gani kuliko serikali ya Tanzania ambayo inawauzia hatua ambayo alisema ni hatari.
Alitoa mfano kuwa takwimu inazojua serikali ya Tanzania ni ndogo mara 10 ya zile wanazojua China.
Alisema serikali kuendelea kuongeza kodi katika sigara na vinywaji mbalimbali hakuwezi kuongeza mapato ambayo yatatumika kulikwamua taifa kiuchumi pamoja na kuondoa umaskini wa kipato kwa Watanzania.
Kuhusu kilimo, alisema bado serikali haijatenga bajeti ya kutosha na hivyo inaonyesha wakulima wataendelea kuteseka kwa muda mrefu.
Alitoa mfano kuwa nchi za Afrika zilikubaliana kuwa bajeti ya kilimo ifikie asilimia 10, lakini Tanzania imetenga asilimia 7.8 tu.
CHANZO: NIPASHE