Polisi waua watatu

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,322
33,126
headline_bullet.jpg
Wadaiwa walikuwa ni majambazi
headline_bullet.jpg
Aua shemeji yake kwa deni la 1,500/-
headline_bullet.jpg
Mwingine aua kwa wivu wa mapenzi



Nyombi2.jpg

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Advocate Nyombi.



Watu watatu kati ya watano wanaodhaniwa kuwa majambazi, wameuawa kwa kupigwa risasi na askari polisi waliokuwa doria wilayani Rungwe mkoani Mbeya.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Advocate Nyombi, alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea Juni 3, mwaka huu, katika kijiji cha Nditu wilayani humo.
Nyombi alisema siku ya tukio, polisi walifanya doria usiku katika barabara ya Katumba hadi Mwakaleli, baada ya kuwapo kwa taarifa za kuwepo watu waliodhaniwa kuwa majambazi.
Watu hao walidaiwa kuwepo katika eneo hilo kwa lengo la kuwavizia wafanyabiashara wa mbao.
Alisema usiku huo wakati askari hao wakiwa katika doria, waliona watu watano waliovaa makoti meusi, wakiwa wanatembea barabarani kuelekea upande walipokuwa askari.
Nyombi alisema kuona hivyo, askari polisi walijiandaa, huku wakijificha kando ya barabara.
Alisema watu hao walipokaribia, polisi waliwasimamisha na kuwataka wajitambulishe, lakini kabla ya kutekeleza agizo hilo, `waligeuzia kibao’ askari na kuwataka wajitambulishe kwanza.
“Watu hao waliwataka askari wajitambulishe kwanza ili wawafahamu wanaowahoji,” alisema.
Kwa mujibu wa Nyombi, askari waliokuwa doria walipojitambulisha kuwa ni polisi, watu hao walianza kuwarushia risasi, na ndipo askari wakajibu mashambulizi kwa kurusha risasi dhidi yao (majambazi).
“Katika mapambano hayo, watu watatu walijeruhiwa na baadaye kufa, lakini wengine wawili walifanikiwa kutoroka na kukimbia,” alisema.
Nyombi alisema watu waliouawa walipekuliwa na polisi, mmoja alikutwa na bunduki aina ya Short gun Pump-action, maganda mawili ya
risasi na risasi nane zilizokuwa ndani ya mfuko wa koti. Wengine wawili walikutwa na panga kila mmoja. Nyombi alisema ufuatiliaji uliofanyika muda mfupi baada ya tukio hilo uliwezesha kumtambua mmoja wa marehemu hao, kuwa ni Barick Martin (24), mkazi wa kijiji cha Lufilyo wilayani humo.
Alisema mtu huyo alitambuliwa kirahisi kwa sababu ni mkazi wa eneo hilo, na kwamba watu waliomfahamu walidai kuwa ni miongoni mwa wahalifu sugu.
Nyombi alisema taarifa zinazohusiana na Barick zilionyesha kuwa aliwahi kufungwa jela miaka mitatu na kuachiwa huru April 26, mwaka huu. Kwa mujibu wa Nyombi, marehemu wengine wawili bado hawajatambuliwa na polisi wanaendelea na msako ili kuwapata waliokimbia.
Hata hivyo, habari zilizothibitishwa na Nyombi zilisema jambazi mwingine alikamatwa baada ya kukutwa kwa mganga wa kienyeji mjini Rungwe, akipata tiba kutokana na majeraha ya risasi.
Matukio ya mauaji wiki hii yameendelea kutokea mkoani Mbeya, ambapo katika kipindi cha wiki moja iliyopita, zaidi ya watu sita wameuawa katika maeneo tofauti.
Baadhi yao walidaiwa kushambuliwa na wananchi wenye hasira, huku kikongwe mmoja akichinjwa na wauaji kuondoka na kichwa chake ambacho hakijapatikana hadi sasa.
Katika tukio jingine mkoani Singida, mkazi wa kijiji cha Mgungira wilayani Singida, Jacob Karim, anatuhumiwa kumuua shemeji yake kwa kumkata kwa mundu kichwani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Celina Kaluba alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kusema kwamba wanamtafuta mtuhumiwa huyo ili sheria ichukue mkondo wake.
Tukio hilo linadaiwa kutokea wakati Karim na shemeji yake, Joseph Francis (26), wakinywa pombe ya kienyeji aina ya mtukuru.
Habari zilizolifikia Nipashe zilidai kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo ili kumdhibiti Francis asimdai deni la Sh.1,500.
Baada ya kufanya mauaji hayo, mtuhumiwa huyo alitoroka na hakuna taarifa rasmi zinazothibitisha mahali alipo.
Kamanda Kaluba alisema tukio hilo lilitokea Juni Mosi mwaka huu katika kitongoji cha Mahambe kilichopo kijijini hapo.
Alisema ubongo wa Francis ulitapakaa ardhini baada ya mtuhumiwa huyo kutenda kosa hilo.
Kaluba alisema siku ya tukio, marehemu alikutana na mtuhumiwa kwenye klabu ya pombe za kienyeji katika kitongoji hicho ambako Francis alimtaka Karim kumrejeshea fedha alizomkopesha. Alisema baada ya mtuhumiwa kudaiwa deni hilo, kuliibuka malumbano kiasi cha kutaka kupigana, lakini watu waliokuwepo waliwaamulia.
Alisema baada ya kuachanishwa, Francis aliondoka kwenda kijiji cha jirani kwa ajili ya matembezi ya kawaida.
Kamanda Kaluba alisema mtuhumiwa naye aliondoka eneo hilo na kwenda nyumbani kwake, ambapo alichukua mundu na kumsaka shemeji yake, hadi alipompata majira ya saa 3.00 usiku.
“Wakati shemeji marehemu akiwa njiani kurudi nyumbani kwake, mtuhumiwa alimvamia na kuanza kumkata kichwani, hali iliyomsababishia kifo papo hapo, kisha akatoroka,” alisema.
Katika tukio jingine, polisi wilayani Serengeti mkoa wa Mara, inamtafuta mtu mmoja anayetuhumiwa kumchoma kisu mfanyakazi wa idara ya maji katika mamlaka ya mji mdogo wa Mugumu kwa madai ya kumfumania.
Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mara, Robert Boaz, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kumtaja aliyeuawa kuwa ni Lazaro Msiba (35), ambaye alichomwa kisu tumboni na kifuani.
Boaz alisema tukio hilo lilitokea Juni 2, mwaka huu katika mtaa wa Bomani mjini humo.
Taarifa ambazo hazijathibitishwa zinadai kuwa, marehemu alifukuzwa na mtuhumiwa wa mauaji aliyefahamika kwa jina moja la Maganja na kuingia ndani ya nyumba ya Bhoke Nyamberi ambamo mauaji hayo yalifanywa.
Lakini taarifa nyingine zinadai kuwa mtu huyo (marehemu) alikutwa kwenye chumba cha Bhoke aliyefahamika kwa jina la Pendo.
Pendo anadaiwa kuwa rafiki wa mke wa mtuhumiwa, na haikujulikana mara moja sababu iliyowafanya wawili hao kukutana chumbani kwake, wakati yeye (Pendo) akiwa hayupo.
Ilidaiwa kuwa mtuhumiwa ambaye ni mfanyabiashara wa duka la viatu katika soko kuu la mjini humo, alifika nyumbani hapo kwa kutumia usafiri wa pikipiki za kukodi maarufu kama bodaboda.
Ilielezwa kwamba aliingia ndani ya chumba hicho, kisha sauti za watu waliokuwa wakiongea zilisikika hadi nje kwa majirani, ingawa haikufahamika mazungumzo yalihusu kitu gani.
Hata hivyo, sauti ya mke wa mtuhumiwa wa mauaji aliyekuwepo nyumbani kwa Pendo, akiwa na marehemu, ilisikika akiomba msamaha, kisha purukushani na vishindo vilisikika kutoka ndani ya chumba hicho.
“Inahisiwa kuwa wakati huo, mtuhumiwa alikuwa akimchoma visu marehemu,” alidai mtu mmoja aliyeshuhudia tukio hilo.
Pia ilielezwa kuwa mtuhumiwa wa mauaji hayo alionekana akiwa ameshika kisu kilichotapakaa damu, ambapo aliwatishia watu waliokuwa eneo la jirani, wakimpigia yowe.
Vitisho hivyo vilisababisha umati wa watu waliokuwepo kutawanyika na mtuhumiwa huyo kutoweka.
Watu hao walimshuhudia Lazaro akitoka chumbani kwa shida, hali iliyomfanya apepesuke na kutokwa damu kifuani wakati akipumua.
Hata hivyo, alipofika mlangoni, alidondoka na kufa papo hapo, huku kichwa kikiwa nje na kiwiliwili kilibaki ndani ya chumba.
Taarifa ilitolewa polisi ambapo askari walifika katika eneo la tukio na kufanya uchunguzi.
Wakati huo huo, imebainika kuwa mtuhumiwa mara baada ya kufanya unyama huo alitimua mbio na kuacha duka wazi ambalo linadaiwa lilifungwa na kaka yake.
Kuna taarifa kuwa alikimbilia kijijini kwao Kisangura, kisha akatoweka.
Mazishi ya marehemu huyo yanatarajiwa kufanyika leo nyumbani kwao Chumwi-Majita, Musoma vijijini.
Hakuna mtu anayeshikiliwa na polisi hadi sasa kuhusiana na tukio hilo.
Habari hii imeandikwa na Emmanuel Lengwa, Mbeya, Wilbroad Tungaraza, Serengeti na Elisante John, Singida.



CHANZO: NIPASHE

Polisi wa Kibongo kwa kujichukulia sheria Mkononi kiboko jamani
 
Back
Top Bottom