Nyambala
JF-Expert Member
- Oct 10, 2007
- 4,465
- 1,170
M. M. Mwanakijiji
SIJUI kama mwenzangu umegundua kuwa siku za karibuni wanasiasa wetu na watawala wetu walioshindwa wameanza kulalamika kuwa kuna udini unaingizwa katika kampeni hizi huku baadhi yao wakidai kuwa kuna watu wanawashawishi watu kupiga kura kwa misingi ya dini.Ukiwasikiliza vile unaweza kuamini kabisa kuwa hawajui jinsi gani suala la udini limeingia kwenye kampeni na sasa wameshtuka kuwa linaweza kuwagharimu uchaguzi, kuzaa vurugu na hata kusababisha machafuko nchini. Lakini mtu mwenye hekima hana budi kujiuliza tulifikaje mahali ambapo dini inaonekana kuwa sehemu ya kampeni hii?
Labda nitumie fursa hii kukumbushia tu matukio kadhaa ambayo yatatudokeza kwanini kuna hisia za kuingizwa kwa mambo ya kidini katika kampeni hizi. Sote tunafahamu kuwa Dk. Slaa kwa muda wa miaka kumi na mitano amekuwa ni mbunge wa Jimbo la Karatu na ni jambo linalojulikana kuwa aliingia katika siasa akitoka kuwa padri wa Kanisa Katoliki akiwa ameshika nafasi mbalimbali kuanzia jimboni kwake hadi makao makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki pale Kurasini.
Alipotaka kugombea ubunge kwa tiketi ya CCM kule Karatu, CCM ilimuengua kwa kumpendekeza mtu mwingine na Dk. Slaa akaamua kuhamia CHADEMA wakati huo kikiwa bado ni chama kichanga kabisa. Kuingia kwake CHADEMA kulidhaniwa kutakuwa ni mwisho wake kisiasa na wananchi wa Karatu baada ya uchaguzi mmoja tu wangemtema na kurudisha CCM. Miaka kumi na tano imepita na Dk. Slaa amekuwa ni mbunge wa Karatu huku chama chake kikishika na Halmashauri ya Karatu mojawapo ya halmashauri chache ambazo zimeshikiliwa na upinzani.
Katika kipindi chote hicho cha miaka kumi na mitano suala la kuwa Dk. Slaa alikuwa ni padre halijawahi kuwa jambo la kuwakwaza watu. Aliposimama kuwanyoshea vidole mafisadi bungeni alimtaja miongoni mwao mtu ambaye alikuwa ni Mkristu, Gavana David Balali.
Suala la kuwa aliwahi kuwa Padri halikuwa suala kubwa. Na aliposimama pale Mwembe Yanga alitaja majina ya watu mbalimbali kuwatuhumu vitendo vya ufisadi. Hakukuwa na mtu yeyote aliyesimama na kusema ‘imekuwaje mbunge aliyewahi kuwa padri kufanya jambo hili"?
Ukweli ulibakia ni kuwa Watanzania hawakujali dini ya Dk. Slaa wala hali yake ya upadre. Watanzania walitamani na hatimaye walipata mwanasiasa mwenye ujasiri wa kuita embe embe, chungwa chungwa, na kitunguu kitunguu!
Hadi pale chama chake kilipompendekeza kuwa mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muuangano wa Tanzania. Hapo ndipo tulipoona wabaguzi wa kidini wakianza kujitokeza na kufanya suala la upadri wa Dk. Slaa kuwa hoja.
Kwanza walianza kuhoji ana "udaktari" wa kitu gani? Wakaanza kubeza kuwa udaktari wake ni wa "Elimu ya Kanisa" na hivyo siyo elimu hasa na wengine wakajenga hata hoja kuwa labda hastahili kuitwa daktari. Licha ya maelezo ambayo yalitolewa wakati ule na kuwapa watu elimu kuwa shahada ya uzamivu aliyonayo inatoka kwenye chuo kinachotambulika na siyo ya kununua kama ya kina fulani bado wengine hawakuridhika.
Wakatoka kwenye hoja hiyo wakaongeza kuwa Dk. Slaa bado ni padri wa Kikatoliki na magazeti yenye mrengo wa kifisadi yakaandika kwa mmbwembwe na kuwatisha baadhi ya wananchi kuwa Dk. Slaa atakuwa ni mtumishi wa Baraza la Maaskofu. Licha ya maelezo ya utaratibu unaotumika kwa padri kuacha upadri bado wenye hisia za udini wakaendeleza hoja hiyo.
Lengo lao walikuwa wanataka kuonesha kuwa mtu aliyewahi kuwa padri hastahili kuwa Rais wa Muungano. Lakini kwa kufanya hivyo wakaenda mbele zaidi kwani wakaanzisha ile hisia dhidi ya "ukatoliki" wa mtu ambayo imekuwepo kwenye baadhi ya watu.
Suala hili la udini liliwahi kutumika katika historia ya Wamarekani pale Seneta John F. Kennedy alipotaka kugombea urais wa taifa hilo kubwa wakati wa kilele cha vita baridi. Ilimlazimu Seneta Kennedy kutetea ukatoliki na kutofautisha na nafasi yake ya urais aliyokuwa anagombea.
Katika chakula cha jioni kwenye mji mmoja huko Marekani Seneta Kennedy aliwaondoa hofu Wamarekani kwa kuwaambia kuwa "mimi siyo mgombea Mkatoliki wa nafasi ya urais wa Marekani, bali ni mgombea wa nafasi ya urais wa Marekani ambaye pia ni Mkatoliki".
Waliokuwa na hofu hasa Waprotestant ambao ni wengi katika Marekani waliondolewa hofu hiyo na Kennedy akachaguliwa kuwa Rais wa 35 wa Marekani. Na hadi leo amebakia kuwa ni miongoni mwa marais waliopendwa sana Marekani.
Kumbe suala la dini ya mtu halipaswi kuwa sehemu kabisa ya mjadala wa siasa za kidemokrasia. Vigezo vya msingi vilivyoainishwa na Katiba yetu ndivyo pekee vinatakiwa kuzingatiwa wakati wa kufikiria nani awe rais wetu. Na ni kutokana na uelewa potofu wa makada wa CCM na mashabiki walioeneza siasa hizo za udini CCM ikajikuta imetegwa ikategeka.
Wakaanza kuzungumzia "kama alikosa uaminifu katika upadre ataweza vipi kuwa mwaminifu kwa taifa". Hawakujua wanauliza nini; hawakujua wanapandikiza mbegu za chuki za kidini, utengano na hisia ya shuku. Lakini kilichonikera mimi zaidi ni kuwa katika muda wote huo hakuna kiongozi yeyote wa juu wa CCM na serikali yake aliyejitokeza kukemea tabia hiyo ya makada wao.
Hakuna aliyesimama na kusema kuwa suala la upadri wa Dk. Slaa siyo hoja na suala la imani yake halihusu wananchi. Mpaka pale wachache wetu tulipojenga hoja za kuonesha upuuzi wa hoja za kibaguzi zilizopandikizwa.
Lakini juhudi zetu zilikuwa zimechelewa. Tayari madhara yalikuwa yameshafanyika; walioamini kuwa Dk. Slaa ni kibaraka wa Wakatoliki wakaendelea kuamini hivyo na hao hadi sasa wamekwazika kwa Dk. Slaa kugombea urais.
Wale ambao tayari wameaminishwa kuwa Wakristu ndio maadui zao basi wakaona ndani ya Dk. Slaa mtu ambaye atawakilisha maslahi ya Wakristu. Na jambo baya zaidi lililotokea ni kuwa Dk. Slaa anagombea dhidi ya mgombea wa CCM ambaye ni Muislamu. Hisia zikaanza kujengeka kuwa kuonesha mapungufu ya serikali ya Rais Kikwete au kuhoji maamuzi yake ilikuwa ni sawa na kumshambulia kwa sababu ni "Mwislamu".
Matokeo yake kimetokea kitu gani? Baadhi ya Wakristu wakaanza kuona kuwa Dk. Slaa hatendewi haki na anashambuliwa kwa sababu ya Ukatoliki wake na hasa pale tuhuma zilikuwa zikiongozwa na viongozi wa CCM ambao pia ni Waislamu (Makamba na Kinana) na Waislamu nao wakaona kuwa Kikwete anashambuliwa kwa sababu ni Mwislamu na hasa baada ya kauli ya viongozi wa Kikristu kama Mch. Kakobe.
Na kwa kadiri siku zinavyoendelea kila kundi linazidi kwenda mbali ya jingine na kugawa mashabiki wao vivyo hivyo. Hata hivyo ukweli ni kuwa fikra za namna hii zinatokana na ujinga yaani, kutokujua. Hata hivyo uzuri wa ujinga ni kuwa huweza kuondolewa kwa kuelimishwa.
Ndugu zangu, anayedhani kuwa Wakristu wa Tanzania watahama sijui waende sayari ya Zebaki anajidanganya na yule anayedhani kuwa Waislamu wa Tanzania watahamia Zuhura nao wanajidanganya.
Ni wapuuzi wale wote wanaofikiria kuwa nchi hii itakuja kumegwa kwa ajili ya vikundi mbalimbali kuridhishwa. Ni taifa letu sote. Ni taifa la Wandengereko na Wazinza kama lilivyo taifa la Wambulu na Wabarbaig; ni taifa la Wamwera na Wagweno kama lilivyo taifa la Wasafwa na Wamatengo!
Ni taifa la Wahindi na Waarabu kama lilivyo leo hii taifa la Washirazi na Wakomoro. Historia imetufunga pamoja milele kiasi kwamba wanaodhani kuwa tunaweza kutenganishwa kwa sababu za dini na ukabila wanajidanganya na sala yao hata shetani hawezi kuitekeleza!
Hakuna mwenye haki zaidi katika taifa hili au mwenye kustahili zaidi. Hakuna mtu ambaye ati kwa vile babu yake alipigania uhuru basi yeye anastahili zaidi!
Ni katika kutambua ukweli huu ndipo wale wachache ambao tunajitambua kuwa ni Watanzania kwanza tunasimama na kuyabeza makundi yote mawili. Tanzania itatawaliwa na Watanzania wote. Lakini katika kutambua hili hatutaogopana ati kwa sababu fulani ni Mkristu au Mwislamu mwenzetu basi hatutamkemea.
Lakini vile vile hatutaogopana ati kwa sababu mtu ni tofauti na sisi katika dini au kabila, basi tutamkandamiza. Yote ni ya hatari kwa mustakabali wa taifa. Binafsi napenda kuona viongozi wa Kikristu wakimkemea Mkapa na kutaka awajibike kwa yale aliyoyafanya na kuliomba taifa pasipo kumuonea haya na ningependa viongozi wa Kiislamu wakimkemea Kikwete pasipo kupepesa macho. Na ni matarajio yangu kuwa endapo Dk. Slaa atashinda Wakristu wa Tanzania hawatajaribu kummezea pale akianza kuleta yale yale tuliyoyakataa chini ya Kikwete na Mkapa.
Ni lazima tuwe na ujasiri wa kuweka Tanzania mbele kuliko dini zetu, makabila yetu na vyama vyetu. Ni kutokana na ukweli huo naamini mkorogano wa sasa umeletwa na CCM na ni CCM wenyewe wausafishe.
Kwanza ni lazima wakiri kuwa Dk. Slaa ana haki ya kugombea kama Rais wa Muungano licha ya kwamba aliwahi kuwa padri na kuwa suala la yeye kuwa padri si kikwazo wala sababu ya kutokuchaguliwa.
Pili, CCM iache mara moja hizi siasa zenye kudokeza ubaguzi wa kidini au kikabila ambazo imezifanya miaka kadhaa huko nyuma (tunakumbuka walivyosakama CHADEMA kuwa ni chama cha kikabila).
Endapo CCM haitasahihisha makosa yake yenyewe katika kupandikiza mbegu za chuki za kidini kupitia makada wake kama alivyofanya kiongozi wao wa Umoja wa Vijana Benno Malisa huko Geita mwishoni mwa juma basi wajue kuwa baadhi ya Watanzania wataona kuwa njia pekee ya kujibu mashambulizi hayo ni wao wenyewe vile vile kuendeleza siasa za kidini.
Hii itakuwa ni hatari kwa taifa na Watanzania wote ni lazima tusimame katika ulinzi kuwakataa wana CCM wenye kupandikiza mbegu za chuki za kidini kwa kisingizio chochote na wakati huo huo kuwakana wapinzania ambao watasimama na kutoa mashambulizi ambayo yana misingi ya kidini dhidi ya CCM.
Ni katika kufanya hivyo tu ndipo tutajikuta tunalipa taifa letu nafasi ya kuendelea kwani katika hili sote hatima yetu ni moja; nchi moja, hatima moja!
Natamani nione viongozi wetu wa kisiasa na kidini wakiandaa maandamano ya umoja wa kitaifa yenye kushinikiza umoja wetu zaidi na siyo tofauti zetu mbalimbali. Ni kwa kufanya hivyo tu watawala na viongozi wenye hisia za ubaguzi wataumbuliwa na ajenda zao za utengano kufichuliwa.