Ni kweli mheshimiwa Rais fomu ulichukuwa mwenyewe, lakini je kura nazo ulijipigia mwenyewe?

GENTAMYCINE

JF-Expert Member
Jul 13, 2013
56,689
109,116
UTANGULIZI

Mheshimiwa Rais kwanza nianze kukubali kabisa kauli yako uliyosema kuwa hukutumwa na Mtu kwenda kuchukua Fomu yako ya kugombea Urais kupitia Chama chako cha CCM ila nadhani pia utakuwa umesahau vitu viwili kuwa hata Wewe pia CCM haikukulazimisha kuwania hiyo nafasi lakini labda nikuulize tu swali dogo sana Je Mheshimiwa Rais baada ya Wewe mwenyewe kuchukua Fomu hivi hizo Kura zote takribani Milioni 8 zilizokuweka Madarakani hadi sasa hivi unatiririka Kijeuri hivyo ulijipigia mwenyewe?

Mheshimiwa Rais nadhani leo ndiyo unaweza ukawa mwisho wangu wa kutoa mtazamo wa Uongozi wako na najua fika kuwa huwa unasoma sana threads zangu humu JF japo kila siku unasikika ukitiririka tu kuwa hupendi Mitandao ya Kijamii huku ukisahau kuwa ni Mitandao hii hii ndiyo imekusaidia Wewe kuweza kuzoa hizo Kura zote zile takribani 8,882,935 ( kwa mujibu wa Mzee Lubuva na Tume yake ) na ni Mimi huyu huyu na wana CCM wengine ndiyo tulikuwa tunakesha hasa hapa JF na katika Social Platforms zingine kukupigania, kukutetea na kufanya Propaganda na hata kuweza kuhatarisha maisha yetu na hatimaye ukaibuka mshindi.

Mheshimiwa Rais haya nitakayoyaandika hapa hayaniondolei imani yangu iliyotukuka juu ya Uongozi wako mzuri ambao umeweza kuonyesha uthubutu wako na kiukweli nikupongeze sana kwa angalau kuweza kuirudisha nchi katika mstari wa nidhamu kwani naamini kuwa taifa lolote lenye nidhamu basi hata ustawi wake na wenyewe hasa wa Kimaendeleo huwa ni mzuri na mifano juu ya hili ipo wazi tu kwa nchi kama za China, Korea zote Kaskazini na Kusini na kwa hapa kwetu Africa Rwanda wamefanikiwa katika hili.

Mheshimiwa Rais nimeshawahi kuandika humu humu JF threads zangu kama tatu hivi na zote nikiwa najaribu kukushauri juu ya utendaji wako na pia kuweza kukushauri nini cha kufanya na nimelazimika kufanya hivyo ili tu Kiongozi wangu Wewe uweze kukubalika na pia isije ikatokea ukakengeuka na hatimaye kuweza kupoteza sifa zako zote nzuri ambazo Watanzania tumeshakupa na ambazo sasa naona kama sitojitokeza kukushauri tena kwa mara hii ya mwisho siyo siri Uongozi wako mbele ya macho ya Watanzania wanaojielewa utaonekana ni wa hovyo hovyo kama siyo kituko kitu ambacho siyo kizuri na kitakuharibia.

A. KAULI ZAKO TATA

Mheshimiwa Rais nimekuwa nikijiuliza sana na sipati majibu sahihi hasa pale ninapokusikia unatoa Kauli ambazo kwa upeo wangu huu mdogo sidhani kama kweli zinafaa kutolewa na Head of State ( Mkuu wan chi ) badala yake nadhani kama ningekuwa nazisikia pande zile za Kariakoo shimoni au Tandale au Tandika au Manzese wala nisingekuwa na shaka nazo kwani sisi tunaoishi na kukulia uswahili hizo ndizo kauli zetu na wala hazitushangazi ila zinapotolewa na number one public figure katika nchi huwa zinatupa ukakasi sana.

Naomba nitoe mfano wa nukuu zako tata Mheshimiwa Rais…………

" Nyie askari Polisi mkiona Gari ya Mtu yoyote imeingia katika barabara ya mwendo Kasi wala msipate nayo tabu bali chomoeni tu matairi yake na nendeni mkayauze na mwenye Gari atajua jinsi ya kulitoa pale

" Nyie Wakulima si mmelima wenyewe? Sasa asitokee Mtu akawapangia bei ya kuuza Mazao yenu bali uzeni Nafaka zenu kwa bei muitakayo na atakayeona bei ni kubwa na Yeye akalime

" Ingekuwa ni amri yangu ningeifungia mitandao yote ya Kijamii kasha tukishamaliza kufanya maendeleo ndipo tuifungulie kwani hii mitandao yenu inaturudisha sana nyuma na inakera mno

B. MSHANGAO WA MWAKA

Mheshimiwa Rais huu ni ukweli usiopingika kwamba sasa kwa takribani mwezi mmoja wa Watendaji wako na ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Ndugu Paul C. Makonda amejikuta akiwa matatani mno hasa baada ya Sakata lake la kufoji cheti cha Mtu na kukitumia kwa Masomo yake kitu ambacho Kisheria na Kimaadili ya Uongozi hakitakiwi na ni Kosa la jinai pia.

Mheshimiwa Rais wakati hili likiendelea huku Watu wakiweka ushahidi wote ambao Mimi nilidhani kwa kutumia Vyomba vyako maalum ungeweza tu kutoa maelekezo haraka ili walifanyie Kazi kisha wakupe ukweli kamili Wewe ukaendelea bado kuuchuna ( kunyamaza ) kana kwamba hujui kinachoendelea lakini cha kusikitisha Waziri Mwakyembe alitoa tu Kauli ambayo ilikuwa na utata kwa sisi wapokeaji wengi na ni humu humu katika Mitandao hii hii usiyoipenda Watu wenye akili zetu tukaanza kuichambua na kuipinga ile Kauli ya Waziri Mwakyembe hali ambayo iliwawezesha Wasaidizi wako haraka mno kukuletea mrejesho kutoka kwa Social Media users kuwa maamuzi ya Waziri Mwakyembe yamepokelewa vibaya na Wewe bila kuchelewa ukaitolea maamuzi mara moja bila kuchelewa lakini suala la Makonda hadi sasa unalikwepesha.

Mheshimiwa Rais nasema ni mshangao wa mwaka nikiwa na maana kwamba ni hivi majuzi tu Mkuu wako wa Mkoa Kipenzi wa Mkoa wa Dar es Salaam Ndugu Paul C. Makonda aliweza kukivamia Kituo cha Habari cha Clouds na kusababisha usumbufu mkubwa huku akifaya Utemi wake wote kwa msaada wa wale askari aliokuwa nao kitendo ambacho ni kinyume kabisa na taratibu za nchi yetu na Kosa kubwa tu pia.

Wakati Wadau wa Habari na Wananchi wanaojielewa wakikilaani na kukipinga hiki Kitendo cha Mkuu wako wa Mkoa wa Dar es Salaam jana Mheshimiwa Rais wakati ukimalizia kutoa ile Hotuba yako pale Ubungo Watanzania wote tukiwa tunategemea kuwa hata Wewe pia tukio lile lilikusikitisha na labda ungechukua hatua Kali Kwake Wewe ukaamua kutumia ile platform pale Ubungo kuweza Kumsifu Makonda na Kutukashifu sana sisi Watumiaji wa Mitandao kitu ambacho nakitafsiri kuwa umetutukana kwa Kiwango cha juu na pengine kwa hekima na busara zako tu ungetuomba tu radhi kwani wengi wetu umetuumiza na kutusononesha mno.

Kwa mfano ulio hai tu ni kwamba Mheshimiwa Rais kitendo ulichokifanya jana kwa kumtetea Mkuu wa Mkoa Makonda hasa baada ya tukio la aibu alilolifanya Clouds hakina tofauti na Kitendo cha Mkuu wa Kituo cha Police mahala fulani baada ya kupelekewa mashitaka juu ya Ujambazi uliofanywa na Jambazi fulani mzoefu wa mtaani halafu Yeye badala ya kumchukulia hatua huyo Jambazi sasa anaamua kumsifia huyo Jambazi kwa ujambazi wake alioufanya. Kwa kitendo hiki unadhani huyo Mkuu wa Kituo cha Police ataaminika tena au kupewa ushirikiano na Wananchi wa sehemu husika?

C. CHUKI YAKO ISIYO NA TIJA KWA MITANDAO YA KIJAMII

Mheshimiwa Rais naomba tu leo nikuweke tu wazi kwani nahisi Wasaidizi wako ama hawajui au wanaogopa kukuambia pengine kwa kujua udhaifu wako au madhaifu yako.

Katika dunia ya leo ni vigumu mno kuishi nje ya Mitandao ya Kijamii kwani katika haya mabadiliko makubwa ya njia za Mawasiliano yaliyoratibiwa kwa kiasi kikubwa na ujio wa Utandawazi Mitandao ya Kijamii imeweza sasa kuchukua nafasi kubwa na muhimu sana katika kuhabarisha, kuburudisha, Kuelimisha, Kukosoa, Kujenga na Kupongeza.

Na hata kuonyesha tu kuwa nguvu ya Mitandao ya Kijamii ni kubwa sana katika zama hizi za Kizazi kipya utaweza kuona kuwa hata Rais mwenzako na tena wan chi Kubwa tu na ambayo nina uhakika inatusaidia mno Tanzania kimisaada Donald Trump wa Marekani na yeye ni Mtumiaji mzuri sana wa Social Media na amekuwa hata akitoa maelekezo na taarifa zake muhimu kwa kutumia njia ya Mitandao na hasa hasa Twitter.

Mheshimiwa Rais huwa unanishangaza na wakati mwingine hata kunichekesha hasa pale ambapo kila mara nakusikia kuwa unasema huipendi na unaichukia sana Mitandao ya Kijamii wakati hapo hapo umesahau kuwa hata Wewe katika Taasisi zako karibia zote kumewekwa mifumo mingi ya Kimawasiliano ambayo yote inaingia katika Kapu moja la Mitandao ya Kijamii sasa ukisema kuwa unaichukia kidogo huwa unanifanya nikutafakari upya na kwa mashaka makubwa.

Leo Tanzania imekuwa kila mara ikiomba misaada yake katika nchi za Kitajiri je Mheshimiwa Rais unajua kwamba hizo nchi zote Viongozi wake wanaheshimu mno the power of social media? Kuna faida nyingi sana kuliko hasara za matumizi mazima ya Mitandao ya Kijamii na labda nikusaidie tu kuwa kama ungekuwa unaitumia hii Mitandao ya Kijamii na hapa nisikufiche sana sana huu huu wa JAMIIFORUMS nakuhakikishia Mheshimiwa Rais ungekuwa unafaidika na mengi mno na ungetawala vizuri kwani humu kuna Vichwa vilivyotukuka sana ambavyo vimejaa vision na vingekusaidia siyo katikam kukulazimisha ufanye tuyatakayo bali kuyatafakari na kuyafanyia Kazi.

Mheshimiwa Rais wakati leo ukisema kuwa huipendi Mitandao ya Kijamii hivi leo umesahau kuwa lile Sakata lako la Bomba la Mafuta la TIPPER pale Bandarini na Ufisadi wote uliokuwa ukifanyika pale Mamlaka ya Bandari Tanzania ( TPA ) na ambapo Wewe uliweza kuchukua hatua za haraka zile taarifa zote zilianzia Mitandaoni na hasa hasa hapa JAMIIFORUMS? Je Mheshimiwa Rais kwa mifano hii tu ya uzuri wa Mitandao ya Kijamii hasa katika kuibua uozo hasa huko Serikalini bado utasema Mitandao ya Kijamii ni mibaya na unaomba izimwe?

D. MTIZAMO HASI JUU YA SAKATA ZIMA LA RC MAKONDA

Mheshimiwa Rais kuna hiki kitu huwa kinanikasirisha mno ( hapa lazima niseme ukweli ) ni kwamba kumekuwa na taarifa za kitoto kabisa ambazo Mkuu wako wa Mkoa pamoja na Watoto wenzie anaowatumia wanazieneza kila uchao ambazo binafsi naziona hazina Tija na sana sana ndizo zinatufanya tuzidi kumpuuza Mkuu wako wa Mkoa Makonda.

Mheshimiwa Rais mwambie Makonda kuwa asipende sana kuwahusisha wale wote ambao wanampinga au kumshambulia kwa maovu yake yasiyovumilika kuwa ni Wauza Unga maarufu na Wakubwa au ni Watu wa Upinzani na najua hapa huwa anamaanisha kuwa ni wana CHADEMA.

Kama ni kweli hata Wewe Mheshimiwa Rais umelishwa sumu hii ya Uwongo na Makonda na ukaiamini basi nitaanza kuwa na mashaka na Wewe kama Kiongozi wetu. Napinga na nitapinga kwa nguvu zangu zote kuwa wote tunaompinga Makonda na kutaka ang’olewe ni Drug Barons ( Wauza Unga wakubwa ) na ni Wapinzani wa kutoka UKAWA na hasa CHADEMA kwa kuweka wazi kuwa Mimi binafsi sijawahi sit u kuuona huo Unga kwa macho yangu haya halisi au kuutumia au kuuza na kama haitoshi Mimi ni Mwana CCM tena niliyetukuka kabisa na nimeweza kuliweka hili wazi muda mrefu sana humu JF na hakuna asiyejua hili.

Tunachokitaka hapa kwa Makonda ni kwamba ama aweke wazi Vyeti vyake au kwa Uungwana tu aachie ngazi ili wawekwe Watu wanaostahili kuwa hapo Kisheria na ambao naamini wapo wengi na wanajulikana kutokana na historia zao za Uongozi zilizotukuka. Aache kuwapotosha Watu tafadhali katika hili na awe mkweli Kwako.

E. USHAURI WANGU WA MWISHO KWAKO MHESHIMIWA RAIS

Mheshimiwa Rais nakuomba sana pale ambapo utakuwa unaona umekwama na hujui nini cha kufanya basi usisite kuwaona akina Mzee Mwinyi au Mkapa au Kikwete ili na wao waweze kukusaidia kwani naamini kuwa bado kuna mambo mengine utahitaji hekima na busara zao ukizingatia kuwa walikutangulia Kiuongozi na kustaafu Kwao hakumaanishi kuwa hata uzoefu wao nao umestaafu.

Watumie sana Washauri wako kwani kuna hisia imeniijia kuwa yawezekana ukawa una very competent Presidential Advisers lakini ama Wewe huambiliki ( namaanisha Mbishi ) huwa huwasikilizi au hao Washauri wako wanakuogopa au hata wanakuingiza chaka ili uharibikiwe zaidi halafu nchi ikikushinda wakucheke.

Nakuomba jikite sana katika Kuuvaa Udiplomasia hasa katika matendo yako na hapa niseme tu ukweli japo najua utakuuma ila kama utaweza nakuomba jaribu kuiiga tu kidogo Diplomasia aliyojaaliwa nayo Waziri Mkuu aliyejiuzuru Mzee Edward Ngoyai Lowassa kwani japo Mimi ni Mwana CCM na nakumbuka tena nakiri kuwa wakati wa Kampeni nilikuwa mstari wa mbele katika kumpiga Madongo humu ila Lowassa ana aina ya Diplomasia ya ajabu sana ambayo imeweza kumfanya aendelee kuheshimiwa na hata Wana CCM ( japo hatuwezi kukuonyesha machoni ) usije ukatuchenjia bure tukatafutana mjini hapa.

Imarisha sana Kitengo chako kizima cha Habari na Mawasiliano ambacho sina shaka na aliyepo sasa Kamarada Gerson Msigwa kwani kuna wakati mwingine Mheshimiwa Rais aina yako ya uwasilishaji huwa inanifanya ninapokuangalia moyo wangu uweze kwenda mbio kwa hofu kuwa muda wowote utagogesha tu besela ( namaanisha kuwa utakosea ). Ninachokisema hapa ni kwamba jaribu sana kupenda kusoma katika Script yako na usiwe unatamka tu maneno yako kwani kuna muda mwingi huwa unatoka sana katika lengo Kihotuba kitu ambacho kwa Wabobezi wakubwa wa Mawasiliano, Habari na Saikolojia kama GENTAMYCINE huwa unatusikitisha na tunashikwa na butwaa pia.

Mwisho nikuambie tu Mheshimiwa Rais kuwa Kitendo chako cha jana kusema tena kwa yale Majigambo kuwa una imani na Mkuu wako wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul C. Makonda na kwamba achape tu Kazi na hutomng’oa madarakani ulifanya Kosa moja kubwa mno la Kiutawala na impact yake hasa Kiutendaji Kazi wa Makonda mwenyewe utashuka na pia umeweza kutengeneza chuki kubwa Kwake na inaweza hata ikamuathiri asiweze kupata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa Watendaji wake kitu ambacho ni cha hatari hasa ukizingatia kuwa Mkoa wenyewe ni huu wa Dar es Salaam. Na tambua ya kuwa haiwezekani Watanzania walio wengi wote wampinge Makonda bali jua ya kuwa Kitendo hicho kinamaanisha kuwa ana Kasoro fulani hivyo kwa Ustawi wako kama Kiongozi wan chi unapashwa kutafakari na kuchukua hatua za haraka kulikabili.

Yangu ni hayo tu Mheshimiwa Rais na ni matumaini yangu kuwa utalisoma vizuri sana na kwa uangalifu kama si utulivu mkubwa hili bandiko langi / uzi wangu ( thread yangu ) kisha uuelewe na kama ukitaka kunipata Mimi huwa napatikana sana humu humu JF full time.

Akhsante sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph MAGUFULI na nikutakie tu kila la kheri katika Uongozi na Utawala wako. Mwenyezi Mungu awe nawe na akuongoze vyema Amen / Inshaallah.

ANGALIZO KWA PLAGIARISTS WOTE POPOTE PALE MLIPO

Kuna wale wenzangu na Mie ambao hupenda sana kusubiri hadi GENTAMYCINE aje na thread humu halafu wanazikopi na kuzipeleka katika Mitandao yao bila kunifanyia ACKNOWLEDGEMENT na kusema wameanzisha wao tafadhalini jamani huwa naumiza sana Kichwa changu hiki hadi kuja na hizi analysis ( chambuzi ) hivyo kwa kunitia tu moyo msione Wivu kunitaja tu kwani huwa naumia mno nikiona threads zangu nyingi zikitambaa katika social platforms zingine bila kupewa heshima yangu stahiki kitu ambacho kina afya pia Kitaaluma na Kiueledi.

Nawatakieni kila la kheri na majukumu mema nyote akhsanteni.

Nawasilisha.



 
Naomba wasukuma mtusaidie hapa, kuna hiki kitendawili cha kisukuma tupeni tafsiri yake kinaenda hivi:
Mtegaji: kalagu.
Mteguaji: kize!
Mtegaji: kwimbila nchiba. Mteguaji: imala mimbo!
Hiki kitendawili nimekuwa nakisikia, nikiwauliza maana yake wanaishia kucheka! Karibuni wasukuma mtujuze hapa!
 
Asante sana bro, mchango katika kupigania chama tunaujua sana wana JF, kiukweli umegombana sana na watu humu na mpaka wengine kukutukana lakini lengo lako ni mkulu aingie pale Magogoni, Binafsi napenda kukiri pia nimempigania sana mkulu humu JF na kwingineko mtaani nahisi ni wapiga kura wengi sana niliwabadirisha wakampigia kura mkuu kulingana na ushawishi wangu kwenye vijiwe vya kahawa na mtaani...

Ni wakati sasa wakumuonyesha mkuu nguvu yetu inamanufaa kwa taifa hili kuliko anavyofikiri..
Binafsi nilishaacha kumuunga mkono baada tu ya miezi nane ya utawala wake, ni bora kura yangu ikarudi kwa wazungurusha mikono au mzee Rungwe kuliko kurudia makosa...

Tofauti ya kura 2mil ni ndogo sana kubadirisha game kuliko anavyofikiri, ukawa wanahitaji vitu viwili au vitatu muhimu sana kwa sasa kumuangusha jamaa na nina uhakika kwa nguvu yetu hii mpya tutaiangusha CCM asubuhi sana 2020..Mwafaaa...
 
Back
Top Bottom