Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,890
- 6,898
Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsa Vuai Nahodha
Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsa Vuai Nahodha, amewanyooshea vidole maafisa wa Idara ya Uhamiaji ni vinara wa rushwa katika utoaji wa hati za kusafiria na kuwaingiza wahamiaji haramu nchini.
Katika kuthibisha kuwa vigogo hao wanahusika na rushwa, Nahodha alisema tayari ana majina ya maafisa nane wa makao makuu ambao wametajwa na wateja kuwa wamekuwa vinara wakuu wa kupokea rushwa katika Idara ya Uhamiaji.
Waziri Nahodha alisema hayo mjini Morogoro wakati akifungua mkutano wa siku tatu wa tathmini ya utendaji wa kazi kwa viongozi na watendaji wakuu wa idara hiyo kutoka makao makuu, mikoani na mipakani.
Alisema kuwa idara ya uhamiaji hivi sasa inahusishwa na urasimu,vitendo vya rushwa, kuingiza na kukumbatia wahamiaji haramu pamoja na ukosefu wa maadili ya kazi.
"Kuna vitu ambayo vinaweza kutolewa maamuzi kwa hata siku moja au tatu, lakini nyinyi maafisa wetu mnawazungusha mpaka mwezi mmoja ili kutaka kujiharalishia vitendo vya rushwa," alisema. Kuhusu kukithiri kwa rushwa katika Idara hiyo,Waziri Nahodha alisema kuwa ilifanyika tathmini kwa idara za serikali zinazoongoza kwa rushwa na Uhamiaji ilitajwa kushika nafasi ya tatu.
Alifafanua kuwa maafisa hao wamekuwa wakijihusisha katika kupokea rushwa kwa kuwaombea hati za uraia wa Tanzania baadhi ya wageni kwa kupindisha sheria na taratibu zilizopo za kuomba uraia baada kupewa fedha na wageni hao.
"Kuna afisa mmoja alikuja ofisini kwangu akitaka niidhinishe uraia wa Tanzania kwa Mhindi mmoja katika barua ya kumuombea, alitaja kuwa alichimba visima viwili vya maji kusaidia wananchi," alisema Nahodha na kuongeza:
"Visima hivyo hata Mtanzania anaweza kuvichimba,nilikataa kufanya hivyo najua tayari alishampa rushwa." "Na mwingine alileta hati ambayo haijakamilika na kueleza kuwa huyo ni mwekezaji ana bekari ya mikate hivyo nimpe hati ya uraia wa Tanzania. Hivi kuwa na bekari ni uwekezaji unaojitosheleza kumpatia uraia?" alihoji.
Waziri huyo alisema Idara ya Uhamiaji hivi sasa imekosa uadilifu na maadili kwa kuwa kila mtu anajifanyia anachotaka huku wakimpelekea yeye (Waziri) kazi ambazo zinapaswa kufanywa na maofisa. "Kuna maafisa wanawaambia wateja wao kuwa faili lako lipo kwa Waziri baada ya kuchukua kitu kidogo, na wale wanakuja kwangu moja kwa moja wakitaka nishughulikie mafaili yao wakati mimi sikai na mafaili hayo," alisema
Kuhusu maofisa wa Uhamiaji waliopo mipakani, alisema wanajihusisha na vitendo vya kuwaingiza wahamiaji haramu, baada ya kuwapatia fedha kiasi kisichopungua Dola za marekani 1,000, hali inayosababisha wahamiaji kuzagaa nchini.
Alisema licha ya kuwaingiza wahamiaji hao, pia maafisa hao wamekuwa wakiwalinda jambo ambalo alisema alikubaliki na ni kinyume cha maadili.
Kadhalika, alisema vitendo hivyo ni aibu ikizingatiwa kuwa idara hiyo ni sehemu ya ulinzi na usalama wa nchi. "Ninawapa mwezi mmoja maofisa wa mikoa mlete taarifa ya namna mlivyodhibiti uingiaji wa wahamiaji haramu na changamoto, ikishindikana sitakubali niadhibiwe na Bunge.
Nnyinyi ndio mtakuwa wa kwanza na nalisema hili si kama natania au ni mazoea ya wanasiasa, mtaona wenyewe," alionya. Hata hivyo, alisema ili kumaliza tatizo hilo, Idara ya Uhamiaji inapaswa kuanza kushirikiana na Jeshi la Polisi na Magereza kwani vyombo hivyo viko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Kwa upande wake, Kamishna wa Uhamiaji, Magnus Ulunga, alikiri kuwa baadhi ya maofisa wa idara hiyo wanajihusisha na rushwa na kuongeza kuwa tatizo hilo pia lipo katika idara nyingine za Serikali.
IPPMedia