Mulyambate ataka kurejea bungeni 2010

jamadari

JF-Expert Member
Feb 13, 2010
295
92
Aliyewahi kuwa mbunge wa jimbo la Meatu mkoani Shinyanga, Jeremeiah Mulyambate ametangaza nia ya kugombea kiti cha ubunge katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Akitangaza nia hiyo, Mulyambete alikanusha uvumi kuwa huenda akahama kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), ikiwa jina lake halitarejeshwa kuwania ubunge.
Akizungumza na Nipashe hivi karibuni, Mulyambate ambaye aliwahi kuwa mbunge kwa miaka 15 mfululizo, alisema ameamua kugombea tena kiti hicho kwa vile ameombwa na wazee wa CCM na upinzani.
Alipinga hoja inayoelekezwa kwake, kwamba baada ya kutumikia ubunge kwa miaka 15, anastahili kuwapisha watu wengine kuonyesha vipaji vya uwakilishi na utumishi.
Katika jimbo la Kisesa, wanachama kadhaa wa CCM wameonyesha nia ama kutajwa katika mchakato wa kutaka kugombea ubunge.
Wanachama hao ni pamoja na Masanja Manani na Nyanvenve Sanani, waliotangaza nia yao hivi karibuni.
Hata hivyo, habari kutoka ndani ya Chadema zimeeleza kuwa Mesharck Jeremeiah Oporukwa anatarajia kuwania ubunge wa Meatu huku Erasto Tumbo akitajwa akiwania jimbo la Kisesa kupitia Chadema.
Naye Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Agrey Mwanri, ametangaza nia ya kuwania tena ubunge wa jimbo la Siha Mkoani Kilimanjaro.
Akitangaza nia hiyo, Mwanri amewakejeli wana-CCM wenye nia kama hiyo kwa kusema hawamnyimi usingizi.
Alifikia hatua hiyo alipokuwa akizungumza na wanajumuiya ya Siha wanaoishi jijini Dar es Salaam juzi.
"Leo ndugu zangu nafurahi kuwaeleza nia yangu hiyo, najua kuna watu wanaotaka nafasi hii...siwezi kuwazuia, lakini kamwe sitonyimwa usingizi kwa sababu wananchi wanaelewa nini nimefanya kwa kipindi changu chote," alisema.
Naye Mbunge wa Ilemela mkoani Mwanza, Antony Diallo ameanza kupata upinzani wa kutetea kiti chake baada ya wanaCCM wawili kujitokeza na kutangaza nia yao ya kugombea ubunge wa jimbo hilo.
Waliotangaza azma hiyo katika ofisi za CCM wilaya ya Ilemela ni John Lupemba na Samson Maganga.
Maganga alisema ameamua kuonyesha nia baada ya kutambua kuwa wananchi wa Ilemela, wanahitaji kiongozi shupavu mwenye uwezo na atakayewaunganisha katika kujiletea maendeleo.
Maganga amewahi kuwa Mweka Hazina wa CCM mkoa wa Mwanza ni msomi mwenye shahada ya uzamili katika uchumi.
Kwa upande wake, Lupemba ambaye ni msomi mwenye shahada katika mambo ya masoko, alisema amefikia uamuzi huo kwa kuwa wananchi wa Ilemela wanakabiliwa na changamoto za kijamii, zinazohitaji mbinu mpya kukabiliana nazo.
Habari hii imeandikwa na Anceth Nyahore, Shinyanga, Moshi Lusonzo, Dar es Salaam na George Ramadhan wa Mwanza.
CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom