The Sheriff
JF-Expert Member
- Oct 10, 2019
- 617
- 1,801
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amefungua Mkutano wa Kitaifa wa Haki, Amani na Maridiano ulioandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) leo tarehe 05 Aprili, 2022 katika Ukumbi wa Hazina Jijini Dodoma.
=========
Updates:
RAIS SAMIA AMEELEZA HAYA:
Binafsi nikiwa mdau wa demokrasia ya vyama vingi naona kukutana hapa kama fursa adhimu ya kujadiliana, kushauriana na kujenga muafaka, umoja na mshikamano wa kitaifa.
Nilikuwa naangalia ndani ya chumba hiki kuanzia kwa Komredi Kinana mpaka mstari wa mwisho – wote ni Watanzania. Hapa kuna wageni wasio Watanzania lakini tumewapa jina Wadau au washiriki wa Kisiasa.
Nataka leo tuzungumze Kitanzania ili tuone tunapozungumza Maridhiano, ambayo ndiyo nataka kuanza nayo, tuone tunazungumza vipi, tunaridhiana wapi, katika maeneo yepi, tunakwenda mpaka wapi. Na haya Maridhiano ndiyo sasa.
Tukitoka kwenye Maridhiano tunakwenda kwenye Haki. Haki zetu ni zipi kama Watanzania. Haki zetu kama Vyama vya Siasa ni zipi. Tutazizungumza haki zetu na pale tulipobinya haki hizo tuweze kuzifungua. Lakini kwa mazingira yetu ya Kitanzania.
Tukitoka hapo sasa tunakwenda kudumisha Amani ya nchi yetu. Hakuna atakayetusaidia kwenye hili - ni sisi. Tutasaidiwa kukusanyika hapa, tutasaidiwa maposho na usafiri lakini haya matatu, ni sisi. Kwahiyo kaeni, zungumzeni tuone tunaenda vipi.
Unapozungumza Haki, ujue ya kwako inapoishia basi ya mwenzako ndiyo inapoanzia. Usije kujadili ya kwako ukataka kubinya ya mwenzako.
USHIRIKIANO NA USHIRIKISHWAJI TOKA SERIKALINI UPO 'GUARANTEED'
Tulichagua kuingia mfumo huu wa Vyama Vingi tukijua kwamba ndani ya mfumo huu tutakwenda kupata maendeleo ya haraka kwasababu macho yapo mengi, vyama vipo vingi na maono yapo mengi.
Ndiyo maana tukasema vyama vingi hivi kazi yake ni kuangalia yanayoendelea, yanayofanywa na serikali na kutoa maoni yao kwamba “Jamani, mmepanga hivi, mnakwenda hivi – lakini mbona tunaona hivi?”
Kwa Serikali kazi yetu ni kuwashirikisha katika hayo. Nami nataka nitoe ahadi kwenu kwamba tutashhirikishana katika haya. Kwasababu Tanzania hii haitajengwa na mtu mmoja. Haitajengwa na chama kimoja. Wote kama Watanzania lazima tujadili mambo yetu – iwe sera, iwe sheria, iwe dira.
Na tukikubaliana tunaenda kutekeleza wote kama Watanzania. Atakayekiuka hapo ni mkosa. Awe ametoka kokote kule, ni mkosa.
Kwahiyo niseme kuwa ushirikiano au ushirikishwaji kutoka Serikalini ni guaranteed.
Nafurahi kuwa katika mkutano huu wamealikwa watu mbalimbali: Taasisi za kijamii, vyama vingine, washirika wetu wa maendeleo. Ni utanuzi wa wigo wa mawazo. Na nimeambiwa hapa leo mtazungumza Mapendekezo ya Rasimu ambayo imetayarishwa na wenzetu.
MAENDELEO HAYAFANYWI NA CCM NA RAIS WAO PEKEE
Ndugu zangu, leo siyo siku ya kusema makubwa sana. Makubwa mtazungumza wenyewe. Kuna vichwa vingi hapa, vyenye akili kuliko zangu. Nimekuja hapa kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye nina wajibu na dhima ya ulezi na ulinzi wa Amani ya nchi hii. Ndiyo maana nikaitwa Amiri Jeshi Mkuu.
Matumaini yangu kwenu ni kuwa mtajadili vyema na kuleta mapendekezo yatakayokwenda kuweka Amani katika nchi yetu. Nasema Amani kwakuwa jitihada tunazofanya kujenga uchumi wetu, nchi yetu, underlying condition ni Amani, Maelewano na Mshikamano.
Maendeleo yale hayafanywi na Chama cha Mapinduzi na Rais wao peke yao, hapana. Maendeleo yale yanafanywa na kila Mtanzania.
TUTAKUWA TUMERUDI UCHUMI WA KATI IFIKAPO 2025
Twendeni tukalinde maendeleo yanayoendelea sasa hivi. Tanzania yetu ilikwenda tukafika Uchumi wa Kati na kisha tukarudishwa kwa uwezo wa Mungu, wala si kwa uwezo wa mtu. Kwa sasa kazi yetu ni kupambana kurudi tulipokuwa, tusije tukarudishwa tukaambiwa hatufai kuwa kule.
Kwa mipango na jinsi ninavyoiendesha Serikali, nina imani tutakapofika 2025 kama hatujafika tutakuwa tunatarajia kwani mwaka ninatarajia mwaka ujao tunakwenda kukua kwa asilimia 5; miaka miwili inayokuja tutakwenda kufika kwenye 6.8 tuliyokuwa tukikua before. Kwahiyo, hiyo si nguvu ya mtu mmoja. Ni nguvu yetu wote Watanzania.
UPO UTAYARI WA KUBADILISHA SHERIA YA VYAMA VYA SIASA, ILA KAMA HAIPO 'CONTROVERSIAL'
Mwenyekiti amaeomba mwaka huu tukiwa tunaadhimisha miaka 30 ya Mfumo wa Vyama Vingi, Julai mwaka huu tuwe tumekuwa tumefanya maboresho ya Sheria za Vyama vya Siasa. Sasa inategemea mtakavyotuletea na sisi tutakavyochuja kwa mazingira yetu. Lakini kama haitakuwa controversial.
Kama itakuwa controversial itabidi tukutane – vikao baada ya vikao mpaka tufike. Kama haitakuwa controversial tunaweza kuimaliza kwenye muda huo ili tukasema kwamba Sheria yetu ya Vyama vya Siasa tumeibadilisha baada ya miaka 30. Hili halina shida.
SUALA LA RUZUKU KWA TCD LINAZUNGUMZIKA
Kuhusu suala la Ruzuku kutoka serikalini kwa TCD. Aaah! Kwa bajeti ijayo umechelewa Mwenyekiti kwasababu nimeshaweka sealing na tumeshagawa bajeti. Ila, linazungumzika. Linazungumzika.