MBUNGE WA CUF MAGDALENA SAKAYA, WAJUMBE WA BARAZA KUU CUF, OFISA WA HAKI ZA BINADAMU NA SHERIA NA VIONGOZI WAANDAMIZI WA WILAYA NA KATA WANYIMWA DHAMANA BAADA YA KUPEWA MASHARTI MAGUMU.
Hakimu wa mahakama ya wilaya ya Urambo Mkoani Tabora Mhe. Bulugu amewanyima dhamana viongozi waandamizi wa CUF.
Viongozi waliopandishwa kizimbani NA KUNYIMWA DHAMANA ni;
1. Magdalena Sakaya Mbunge wa Viti Maalum
2. Wajumbe wa baraza kuu watatu Mhe Yasin Mrotwa, Mhe Doyo Hassan na Bi. Zainab Nyumba.
3. Hashim Bakari Ofisa Haki za binadamu na sheria CUF Taifa,
4. Amir Kirungi Mgombea wa CUF katika jimbo la Urambo magharibi 2010,
5. Viongozi waandamizi saba 7 wa kata na wilaya Mrisho Swedi, Singu Yustu, Changu Salum, Idd S Matola, Msafiri Alkado, Ukiwa Juma na Peter Charles.
Kiongozi wa kwanza wa kwanza kupandishwa kizimbani alikuwa ni IDD S MATOLA katika kesi ya jinai namba 60/ 2011. Dhamana yake iliwekwa wazi na wadhamini walisimama kuanza taratibu. Hakimu Bulugu alimtaka mwendesha mashtaka athibitishe hati za dhamana na mwendesha mashtaka alijiridhisha na kumjulisha hivyo hakimu. Hakimu Bulugu naye aliziomba na alipoziona aliweka pingamizi kuwa hati husika hazijapitia kwa mtendaji wa kata kwa uthibitisho.
Hali hiyo iliua sintofahamu na ilimbidi wakili wa mshtakiwa Mhe Twaha Taslima aingilie kati na kumtaka hakimu aziruhusu hati hizo kwani zimethibitishwa na mtendaji wa kijiji ambaye mahakama zote zinamtambua.
Hakimu Bulugu akijibu hoja ya Mhe. Twaha Taslima alieleza kuwa mahakama yake imejiwekea utaratibu huo na ni lazima ufuatwe, hata pale wakili wa mtuhumiwa alipozidi kutoa utetezi kuwa dhamana kwa makosa ya kawaida hutumika hati za dhamana kutoka kwa mtendaji wa kijiji na siyo lazima kata- hakimu Bulugu alikataa katakata na kudai utaratibu wa kupokea barua za utambulisha kutoka kwa mtendaji wa kata ndio utakaoutumika japo alikiri kuwa umeanza hivi karibuni kwatika mahakama yake na kuwa wananchi watauzoea.
Ilipoitwa kesi ya jinai namba 57/2011 ambayo washtakiwa ni Mhe Sakaya na wenzake 11 isipokuwa IDD S. MATOLA washtakiwa wote 11 walipanda kizimbani.
Mwendesha mashtaka alieleza hana pingamizi na dhamana kwa kuwa hali ya Kata ya Usinge ambako vurugu zilitokea na viongozi hao kuhusishwa kwa sasa pako shwari lakini mwendesha mashtaka akaweka pingamizi kuwa ni muhimu mahakama izuie watuhumiwa wote wanaotoka nje ya Usinge wasiende usinge kwa Shughuli zozote hadi kesi itakapoisha.
Wakili wa watuhumiwa wote 12 Mhe Twaha Taslima aliiomba mahakama itupilie mbali ombi la upande wa mashtaka la kuwazuia wateja wake wanaotoka nje ya Using e wasifike Usinge kwa sababu ;
1. Mahakama haina uwezo wa kuzuia watu wasitembee maeneo kadhaa ndani ya jamhuri ya muungano wa Tanzania.
2. Pili baadhi ya washtakiwa wanaotoka nje ya Usinge wana shughuli za kijamii wanazozifanya katika maeneo hayo kwani ni viongozi na lazima waendelee na shughuli za kijamii, kisiasa na kimaendeleo mahali kokote.
Hakimu Bulugu alitumia dakika 12 kupitia vifungu vya sheria na kisha akatoa uamuzi kuwa washtakiwa hawawezi kuzuiwa kwenda Usinge siku zote bali wale wanaotoka nje ya Usinge hawataruhusiwa kukanyaga huko hadi siku 7 zipite na ikiwa pana ulazima wa kufanya hivyo itampasa mhusika akaombe barua kutoka kwa OCD.
Baada ya kutoa uamuzi huo hakimu Bulugu alitoa uamuzi wa dhamana na kudai dhamana kwa watuhumiwa itakuwa na masharti yafuatayo kwa pamoja;
1. Watuhumiwa watapaswa kujidhamini kwa barua zenye commitment ya TZS 3,000,000/- .
2. Kila mtuhumiwa atadhaminiwa na mdhamini mmoja ANAYEISHI ndani ya wilaya ya Urambo mwenye hati ya nyumba ya thamani ya TZS 3,000,000/- au atakayewasilisha mahakamani shilingi 3,000,000/- taslimu.
3. Kila mtuhumiwa lazima awe na barua ya utambulisho kutoka kwa mtendaji wa kijiji iliyothibitishwa na kata na siyo kijiji ambayo haijathibitishwa na kata kama ilivyozoeleka.
Baada ya kutoa masharti hayo magumu, wakili wa washtakiwa Mhe Twaha Taslima aliiomba mahakama ilitizame suala hilo kwa upana kwani sharti la kutaka hati ya utambulisho iliyothibitishwa na mtendaji wa kata ni suala geni na linafanyika kwa kesi ya kina Sakaya tu.
Hakimu Bulugu alibakia na msimamo huo wa mahakama na akaiahirisha kesi hiyo hadi 15 Juni 2011 ambapo watuhumiwa hao watarudishwa.
Hii ina maana kuwa mhe Sakaya na viongozi waandamizi wa CUF watakaa gerezani kwa siku 9 zaidi na hii itakamilisha siku 20 za kukaa gerezani kwa kunyimwa dhamana.
Hata hivyo , wananchi kadhaa waliohojiwa na waandishi wa redio kadhaa zilizohudhuria mahakamani walisema kuwa hadi ijumaa iliyopita watu walidhaminiwa kwa barua za kutoka kwa watendaji wa vijiji tu na walishangazwa na utaratibu mpya ulioanza katika kesi ya kina Sakaya na kuwakosesha dhamana.
Alipokuwa akihojiwa nje ya mahakama hiyo Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania Bara Mhe Julius Mtatiro alikiri kushangazwa na uamuzi huo wa mahakama na akasema hawezi kuingilia sana suala hilo kwa undani na kuwa kazi yake kama Naibu Katibu Mkuu kwa sasa ni kuhakikisha kuwa masharti hayo magumu yaliyotolewa na mahakama yanatafutiwa ufumbuzi.
Wakili wa washtakiwa MHE TWAHA TASLIMA amesema anaanzisha utaratibu kuhakikisha viongozi hao wanapata dhamana haraka iwezekanavyo kabla ya terehe 15 Mei 2011.
Hii ni mara ya pili kwa mhe Sakaya na wenzie kunyimwa dhamana katika kesi hiyo kwani tarehe 30 Mei 2011 walipandishwa kizimbani katika mahakama ya Urambo na hakimu Bulugu aliwanyima dhamana baada ya upande wa mashtaka kuwasilisha hati ya pingamizi ya dhamana kwa mahakama kwa madai kuwa washtakiwa wakiachiwa watahatarisha amani ya wananchi wengine.
Mhe Sakaya na viongozi waandamizi wa CUF walikamatwa tarehe 28 Mei 2011 katika kata ya Usinge wilaya ya Urambo baada ya polisi kuua kijana mmoja kwa risasi na kujeruhi wengine katika rapsha iliyoanzishwa na polisi kwa wananchi waliokuwa wanatawanyika kurudi majumbani walipokuwa wakimsikiliza mhe Sakaya na Ujumbe wake ambao walikwenda katika kijiji hicho kutatua matatizo ya wafugaji kunyanganywa mifugo yao na askari wa maliasili na polisi.
Mtatiro alibainisha kuwa akifika Dar Es Saalam atawaeleza watanzania juu ya Ukatili usiomithilika unaofanya na vyombo vya dola kwa wananchi walio katika vijiji vinavyopakana na hifandhi ndani ya wilaya ya Urambo.
Taarifa hii imeandikwa na;
Mohammed Mtutuma.
Msaidizi Maalum wa Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara (CUF).
Urambo.