Mbunge CCM afikishwa kizimbani kwa rushwa; Lengo pia ni Kushawishi wenzake kukiuka sheria

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
KUNA MWANA JAMII FORUM ALITAKA KUJUA SABABU YA MBUNGE KUWEKWA RUMANDE.

JUMANNE, JUNI 05, 2012 06:28 NA OTILIA PAULINUS


badwel%201.jpg
Badwel akiwa chini ya ulinzi wa polisi kwa tuhuma za rushwa.
Badwel akila kiapo cha utii bungeni
badwel2.jpg



*Ni Omary Badwel wa Jimbo la Bahi
*Aliomba Sh milioni 8 akapewa Sh milioni 1
*Lengo kushawishi wenzake wakiuke sheria
*Wabunge wenzake wamruka, wasema hawahusiki

MBUNGE wa Bahi, Omary Badwel (CCM), amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.

Badwel alifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka mawili ambayo ni kushawishi ili apewe rushwa ya Sh milioni 8 na kupokea rushwa ya Sh milioni 1.

Badwel pia ni Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), inayoongozwa na Mbunge wa Vunjo, Augustine Mrema (TLP).

Akisoma shitaka la kwanza, Wakili kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Janeth Machullya aliyekuwa akisaidiana na Ben Linkolin, mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Faisal Kahamba, alidai kuwa, kati ya Mei 30 na Juni 2 mwaka huu, katika maeneo tofauti ya Jiji la Dar es Salaam, mshitakiwa alivunja kifungu cha 15 (1) (a) cha Sheria namba 11 ya Makosa ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya mwaka 2007.

Alidai kuwa, siku ya tukio, mshitakiwa akijua kuwa ni kosa kisheria, alishawishi apewe Sh milioni 8 kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Sipora Liana.

Mwendesha mashitaka huyo alidai kuwa, Badwel aliomba rushwa hiyo ili awashawishi wajumbe wa kamati yake kupitisha hesabu za Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani.

Katika shitaka la pili ambalo lilisomwa mahakani hapo na Wakili huyo kutoka Takukuru, inadaiwa kuwa, kati ya Juni 2 mwaka huu katika Hoteli ya Peacock, iliyopo Ilala, Dar es Salaam, mjumbe huyo wa LAAC alijifanya kuwa ni Ofisa wa Umma kutoka TAKUKURU na kupokea rushwa ya Sh milioni moja kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga.

Lengo la kufanya hivyo lilikuwa ni kuwashawishi wajumbe wa Kamati ya LAAC kupitisha hesabu za Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga.

Hata hivyo, mshitakiwa alikana mashitaka yote mawili na upande wa Jamhuri uliomba tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo.

"Kwa kuwa mheshimiwa Hakimu upelelezi juu ya kesi hii tayari umeshakamilika, tunaiomba mahakama ipange tarehe nyingine ya kutajwa,"aliomba Wakili kutoka Takukuru, Ben Linkolin.

Wakati upande wa Jamhuri ukiomba tarehe ya kujatwa, Wakili wa Mshtakiwa, Mpare Mpoki, alimuombea mteja wake dhamana ili asirudishwe rumande.

"Kwa niaba ya mshitakiwa tunaomba dhamana, kwani mshitakiwa ana wadhamini wa kuaminika na wako tayari kuja mahakamani kwa siku na saa ambayo watahitajika," alisema Mpoki.

Pamoja na hayo, Hakimu hakuwa na pingamizi katika ombi hilo na kusema kuwa mashitaka yote mawili yana dhamana.

"Makosa yote mawili yana dhamana, kwa hiyo, masharti yake ni lazima awe na wadhamini wawili ambao kila mmoja atawasilisha hati ya Sh milioni 4 mahakamani pamoja na hati ya kusafiria," alisema Kahamba.

Mshitakiwa yupo nje kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana. Kesi hiyo iliahirishwa hadi Juni 18 mwaka huu itakapotajwa tena.

Wakati huo huo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya LAAC ambaye pia ni Mbunge wa Kinondoni, Idd Azan (CCM), aliwaambia waandishi wa habari katika ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam jana, kwamba suala la Badwel ni lake binafsi.

Alisema kuwa, tuhuma hizo hazina uhusiano na kamati yake, kwa kuwa wao wanafanya kazi kwa ushirikiano na kwamba kama kuna mjumbe wa kamati hiyo anafanya kazi kwa masilahi yake binafsi kwa kutumia jina la kamati, wao haliwahusu.

"Sisi tunafanya kazi kwa kanuni na taratibu za Bunge, kwa hiyo hata sisi tuliposikia taarifa za tukio hilo, tulishangaa ila kwa kuwa jambo hilo limeshafikishwa mahakamani, sina la kusema," alisema Azan.


 
Back
Top Bottom