Rutashubanyuma
JF-Expert Member
- Sep 24, 2010
- 219,470
- 911,174
Mawakili wa Kujitegemea waaswa kutowakamua wananchi
Imeandikwa na Grace Chilongola, Mwanza; Tarehe: 4th February 2011 @ 23:50
MAWAKILI wa kujitegemea nchini wameaswa kutotanguliza maslahi binafsi pale wananchi wanapohitaji huduma yao na badala yake wafanye kazi katika viwango vya juu ili utetezi wao uwe na maana katika jamii.
Wito huo ulitolewa juzi na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Abbas Kandoro katika sherehe za siku ya sheria ambapo alidai mawakili wengi wa kujitegemea wamekuwa wakitanguliza maslahi wakati wanapokuwa na kazi za kuwatetea wananchi.
Alisema kuwa wananchi wengi wamekuwa wakilalamikia huduma zao na kudai kuwa wamekuwa wakiwatoza fedha nyingi za utetezi na bila ya kuwepo kwa mafanikio katika kesi zao na kuwaacha wakiwa masikini.
Mkuu huyo wa Mkoa alisema amani na utulivu wa nchi ya Tanzania inachangia utendaji kazi mzuri na ili amani hiyo iweze kuendelea mawakili hao wanatakiwa kufanya kazi zao kwa amani zaidi na kuidumisha amani iliyopo.
Akizungumzia utoaji wa elimu ya mfumo wa Mahakama, Mkuu wa Mkoa alisema wananchi walio wengi hawajui mfumo wa Mahakama hali inayosababisha kuondoa kesi zao mahakamani na kuzipeleka serikalini.
Alisema amekuwa akipokea watu wengi ofisini kwake wakilalamikia kutokutendewa haki katika Mahakama ikiwemo kucheleweshwa kwa kesi zao jambo ambalo linahitaji elimu.
Alisema malalamiko hayo yanatokana na wananchi kutokujua namna Mahakama inavyofanya kazi zake na kudai kuwa elimu zaidi inahitajika ili wananchi wawe na uelewa wa kutosha.