Mauaji na uzushi wa ugomvi wa barabarani ambao kamwe haukuwepo…!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
Tracie-Andrews_1955790c.jpg

article-0-0D29AB9600000578-772_468x286.jpg

Lee Harvey akiwa na mpenzi wake Tracie Andrew
article-1307801-0AED56D2000005DC-555_468x366.jpg

tracie-andrews-and-lee-harvey.jpg

article-1307801-0AED408E000005DC-200_468x286.jpg

Tracie Andrew akiongea na waandishi wa habari kuelezea tukio hilo
article-1307801-0012A57000000258-180_468x365.jpg

Hata hivyo alitiwa nguvuni akituhumiwa kwa mauaji hayo
article-2019614-0D31CAF000000578-175_468x475.jpg

Maureen Harvey, mama yake Lee Harvey
article-1307801-0AFD3A88000005DC-893_468x619.jpg

Tracie Andrew baada ya kutoka gerezani

Majira ya saa 5:00 usiku, wa siku ya Ijumaa ya January 2, 1997, kitengo cha dharura cha jeshi la polisi kilipokea simu ya kuomba msaada wa haraka katika eneo linalisifika kwa amani nje kidogo ya kijiji cha Alvechurch nchini Uingereza.

Polisi walipofika katika eneo hilo walikuta mwili wa kijana mmoja aliyejulikana kwa jina la Lee Harvey aliyekuwa na umri wa miaka 25 ukiwa umelala nje ya mlango wa dereva wa gari lake aina ya Ford Escort Turbo huku kukiwa na dimbwi la damu. Pembeni alikuwa amesimama mchumba wake Tracie Andrew aliyekuwa na umri wa miaka 27 akiwa amechanganyikiwa kutokana na tukio hilo. Tracie pia alikuwa amelowa damu lakini hakuumia sana zaidi ya kuonekana kuwa na michubuko usoni.

Harvey ambaye alikuwa amechomwa na kisu mara 30, alitangazwa kwamba amekwishakufa pale pale kwenye eneo la tukio, lakini mchumba wake alikimbizwa hospitalini kwa matibabu ambapo pia alihojiwa na askari wa upelelezi kutoka katika kituo cha polisi kilichokuwa karibu cha Bromsgrove. Alimweleza askari huyo wa upelelezi kwamba mpenzi wake aliuawa na watu asiowafahamu katika kile alichikiita ugomvi wa barabarani.

Alisema kwamba yeye na mpenzi wake Harvey walikuwa wanarudi nyumbani kutoka katika matembezi ya usiku ambapo walikwenda katika mji wa Alvechurch, mji ulioko pembezoni mwa barabara kupata vinywaji. Mpenzi wake ndiye naliyekuwa akiendesha gari. Njiani walilipita gari aina ya Ford Sierra, kitendo hicho hakikumfurahisha dereva aliyekuwa akiendesha gari hilo, hivyo alianza kuwafukuza kwa kasi. Hata walipojaribu kubadili barabara, gari hilo liliendelea kuwafuata kwa kasi mpaka likawafikia na kuwapita ambapo baada ya kuwapita, walisimama nmbele yao na kuzuia njia. Ilikuwa imebaki mwendo mfupi tu wafike nyumbani kwao.

Kwa mujibu wa maelezo yake, Tracie alidai kwamba, Harvey na dereva wa Sierra walitoka kwenye magari yao na kuanza kutupiana maneno makali huku wakinyoosheana vidole kiasi cha kutishiana kupigana. Ugomvi huo ulionekana kwisha na dereva huyo wa Sierra alirudi kwenye gari lake, lakini wakati anaingia kwenye gari lake, abiria mmoja kati ya abiria wawili waliokuwa kwenye gari hilo ambaye ana umbo kubwa na mwili wake umejengeka kimichezo. Aliteremka kwa kasi na kumrukia Harvey na kumchoma kwa kisu usoni, shingoni na kifuani. Harvey alianguka chini lakini yule abiria aliendelea kumshambulia pale chini. Tracie alijaribu kuingilia ugomvi ule lakini alisukumwa na abiria yule na kudondoka chini kisha akarudi kwenye ngari lao na kuondoka kwa kasi.

Siku iliyofuata tangu kutokea kwa mauaji hayo, Tracie aliruhusiwa kutoka hospitalini akiwa amepona kabisa. Hata hivyo alihitajika kuzungumza na vyombo vya habari kuhusu tukio hilo. Katika mkutano wake na vyombo vya habari alielezea kwa kirefu juu ya tukio hilo kama alivyowasimulia askari wa upelelezi. "Kwa kweli niliogopeshwa sana na tukio hilo," alisema Tracie, kisha akaendelea…. "Nilimfokea Lee awapuuze na kuachana nao, lakini kama muwajuavyo wanaume jinsi walivyo wala hakunisikiliza. Hata hivyo alikuwa hapendi kuelekezwa namna ya kuendesha gari." Aliongeza Tracie.

"Nilimuona mtu yule akimshambulia Lee, lakini sikujua alikuwa anamshambulia na kitu gani. Niliteremka kwenye gari ili nimsaidie mpenzi wangu, kwani mimi si mwanamke wa kukaa tu na kuangalia mpenzi wangu akishambuliwa bila kuchukua hatua….. Nilimuona Lee akiwa pale chini baada ya kushambuliwa na alikuwa anatoa damu mwilini, nilimfuata yule mtu kukabiliana naye lakini aliniwahi na kunitupa chini. Macho yake yalikuwa ni makali na ya kuogofya………" alimalizia kusema Tracie.

Askari wa upelelezi aliyeongozana naye kwenye mkutano huo wa waandishi wa habari Ian Johnston na yeye alisema: "Naamini baadhi ya watu watasema tukio hilo limetokana na ugomvi wa barabarani, lakini kwetu sisi hayo ni mauaji." Alienda mbali zaidi kwa kuwaomba dereva wa hilo gari aina ya Sierra na abiria aliyehusika na mauaji hayo wajisalimishe Polisi haraka iwezekanavyo. Pia aliomba kama kuna mtu yeyote ambaye aliona tukio hilo la magari kufukuzana katika barabara hiyo ajitokeze kwa ajli ya kuisaidia Polisi.

Siku mbili baada ya kuongea na vyombo vya habari, Tracie alikimbizwa hospitalini baada ya kupoteza fahamu akiwa nyumbani kwake. Si Polisi wala Madaktari waliomhudumia walioweza kuzungumzia hali yake. Lakini kuliibuka minong'ono kwamba alikunywa kiasi kikubwa cha dawa za usingizi. Hata hivyo familia ya Lee Harvey ambayo ndiyo iliyokuwa ikimhudumia, walikanusha madai hayo na kueleza kwamba, Tracie amepatwa na tatizo la kusongeka (Stress).

Wakati huo huo Polisi walikuwa wakiendelea na msako wa gari hilo aina ya Ford Sierra, pamoja na dereva na abiria wake. Mamia ya magari aina ya Foed Sierra yalikuwa yakisimamishwa katika vizuizi vya Polisi vilivyowekwa katika maeneo mbailmbali yanayolizunguka eneo hilo yalipotokea mauaji. Lakini hakuna hata mmoja aliyekumbuka kuona magari mawili aina ya Escort na Sierra yakifukuzana katika barabara hiyo.

Wakati askari huyo wa upelelezi, Detective Superintendent Johnston na timu yake wakiendelea kuwahoji masahidi mbalimbali waliojitokeza, waligundua viashiria vingi ambavyo havikuwa vya kawaida, kuhusiana na maelezo ya Tracie juu ya tukio hilo lililosababisha kifo cha mchumba wake. Baada ya siku tano za kuchimbua ushahidi wa tukio hilo, askari huyo wa upelelezi alianza kupata wasiwasi kwamba, gari hilo aina ya Sierra linalozungumziwa na Tracie huenda liwe ni la kufikirika.
Pia alianza kuchunguza maisha ya uhusiano kati ya Harvey na Tracie.

Rafiki yao mmoja alijitokeza na kudai kwamba uhusiano kati ya wapenzi hao ulikuwa ukikumbwa na vurugu za mara kwa mara. Aliongeza kusema, "Tracie mara nyingi alikuwa akimfukuza Harvey hapo nyumbani kwake na baadae kurudiana naye. Na mpango wao wa kuvishana pete za uchumba ulipata kuahirishwa mara tatu."

Asubuhi ya Januari 7, Tracie aliruhusiwa kutoka hospitalini na hapohapo alikamatwa kwa mahojiano zaidi. Hata hivyo baadae akiwa mikononi mwa Polisi alikimbizwa tena Hospitalini baada ya kujisikia vibaya akiwa katika kituo cha Polisi cha Redditch. Polisi walitoa taarifa fupi juu ya kukamtwa kwake.

"Mapema leo mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 27 amekamatwa na yuko chini ya ulinzi wa Polisi. Kulingana na taratibu za Polisi, alifanyiwa uchunguzi wa kiafya na mtaalamu wa afya wa Polisi na baadae alifanyiwa uchunguzi na daktari mwingine. Kwa sasa anapatiwa matibabu katika hospitali moja ya serikali. Mwanamke huyo hakukamwatwa kwa tuhuma za mauaji, lakini amekamatwa kwa ajili ya kuhojiwa zaidi juu ya mauaji ya Lee Harvey. Mwanamke huyo si mwingine bali ni Tracie Andrew."

Hata hivyo siku tano baadae tangu akamatwe, Tracie Andrew alishitakiwa rasmi kwa mauaji ya mchumba wake Lee Harvey. Kesi ya Tracie ilianza kusikilizwa katika Mahakama ya Birmigham mnamo Julai 1, 1997. Katika maelezo ya awali ya mashitaka mwanasheria David Crigman alilieleza baraza la washauri waliokuwa wakisikiliza kesi hiyo kwamba ataithibitishia mahakama pasi na shaka kwamba Tracie Andrew alimshambulia Lee Harvey kwa kisu cha Ki-Swiss (Swiss army-type penknife) na kumchoma nacho kwa takriban mara 30, na hivyo kumsababishia majeraha makubwa yaliyopelekea kuvuja damu kwa wingi na kusababisha kifo chake.

Silaha hiyo haikupatikana kwa sababu Tracie aliificha katika viatu vyake na hatimaye kuitelekeza katika pipa la taka la hospitali alikopelekwa kutibiwa majeraha aliyoyapata katika purukushani hiyo. Wataalamu wa uchunguzi wa uhalifu waligundua damu ya Harvey iliyoganda kwenye kiatu cha kulia cha Tracie. Pia wataalamu hao wa uchunguzi waligundua mabaki ya nywela za Tracie kwenye kiganja cha mkono wa Harvey na pia kibanio cha nywele cha Tracie kikiwa kimeanguka karibu na ulipolala mwili wa Harvey. Hali hiyo ilionyesha kwamba, kulikuwa na purukushani kati ya wapenzi hao.

Ilidhaniwa kwamba katika purukushani hiyo ndipo Tracie alipopata majeraha usoni kwake. Mwanasheria huyo Crigman aliongeza. "Hakupiga kelele kuomba msaada na wala hakukuwa na gari lililokuwa likiwafukuza kama alivyodai bali ni yeye aliyehusika na tukio hilo……!" Alisema Crigman huku akimnyooshea kidole Tracie.

Mwendesha masitaka katika shauri hilo alidai kwamba mauaji hayo ni kilele cha uhusiano uliokuwa na vurugu kati ya wapenzi hao ambapo Harvey alikuwa akifukuzwa mara kwa mara na Tracie na kurudi kwa wazazi wake. Polisi walikuwa wakiitwa mara kwa mara na majirani zao waliokuwa wakiishi mtaa mmoja katika eneo hilo la Alevchurch, kutokana na kukerwa na kelele zao pale wanapogombana.

Ilidaiwa kwamba jioni ya siku hiyo yalipotokea mauaji Tracie na Harvey waliutumia muda huo wakiwa katika baa ya Malbrook iliyoko katika eneo la Bromsgrove, ambapo watu waliokaa nao karibu walikiri kwamba kulikuwa na hali ya kutoelewana kati ya wapenzi hao. Wakati walipokuwa wakirudi nyumbani, ugomvi wao uliibuka tena ambapo gari lao lilisimama njiani mara kadhaa wakibishana, na mwishowe ndipo wakaanza kushambiliana kitendo ambacho kilipelekea kifo cha Harvey.Mwendesha mashitaka huyo aliita mashahidi kadhaa waliotoa ushahidi kuhusiana na maisha ya vurugu kati ya wapenzi hao.

Mashahidi hao walikuwa ni majirani zao, wahudumu kwenye vilabu vya usiku walivyokuwa wakivitembelea, ambapo walielezea jinsi Tracie alivyowahi kumpiga Harvey na kitu chenye ncha kali hadi kupelekea kumjeruhi shingoni kiasi cha kutoa damu. Pia aliitwa Polisi aliyewahi kwenda katika nyumba ya wapenzi hao baada ya kuitwa na majirani waliokerwa na kelele za ugomvi wao.

Hata hivyo ushahidi mwingie ambao ulikuwa na nguvu ni ule uliotolewa na binti wa miaka tisa kupitia mkanda wa video lakini akiwa amefichwa sura yake. Binti huyo alidai kwamba aliamshwa na kelele za ugomvi kati ya mwanamke na mwanaume waliokuwa wakigombana jirani kabisa na dirisha lake la chumba cha kulala. Alidai kwamba mwanaume huyo alikuwa anaongea kwa ukali na ilionekana kwamba anaongea kwa ukali dhidi ya mtu mwingine aliyekuwa na sauti laini kama ya kike. Mama wabinti huyo alidai kwamba alikuwa sebuleni wakati tukio hilo likitokea, hivyo hakushuhudia chochote.

Pamoja na kutolewa kwa ushahidi huo, hata hivyo wakili aliyekuwa akimtetea Tracie, Ronald Thwaites alimuongoza kujitetea pale mahakamani. Akionekana kutokuwa na wasiwasi, Tracie alikanusha kuhusika na mauaji ya mpenzi wake Lee Harvey. "Nilimpnda sana kuliko kitu chochote hapa duniani.." alisema. Kisha akaendelea kuieleza mahakama kwamba ni kweli mapenzi yao yalitawaliwa na vurugu, lakini zilikuwa ni vurugu za kawaida na za upendo. Aliendelea kuelezea jinsi tukio hilo la kuuawa kwa Lee Harvey lilivyotokea. Maelezo yake alikuwa yanafanana kama vile alivyowaeleza Polisi katika mahojiano ya awali.

Akihojiwa na mwendesha mashitaka, David Crigman, alimuuliza ni kwa nini hakuomba msaada pamoja na kwamba tukio lenyewe lilitokea eneo ambalo si mbali na makazi ya watu. (Kwa mujibu wa maelezo ya akari wa uchunguzi nwa eneo la tukio, Tracie alibaki amesimama katika eneo hilo bila kufanya lolote huku mwili wa Harvey ukiwa umelala chini kwa kati ya dakika 15 hadi 17). Tracie akijibu swali hilo alidai kwamba alikuwa kwenye mshtuko mkubwa.

"Tukio hilo lilinifanya nijihisi kama nafsi yangu imetengana na mwili.." Alisema Tracie. Maelezo hayo yalimfanya mwendesha mashitaka Crigman acheka pale mahakamani…. Kisha akamwambia, "sababu iliyokufanya uchelewe kuomba msaada ni kutokana na kujaribu kukusanya mawazo ya namna ya kutengeneza stori kwa ajili ya kuwadanganya Polisi."

"Kama ungekuwa hujahusika na mauai hayo Tracie, ungekuwa umekimbilia katika nyumba za jirani kuomba japo msaada, lakini pia hukupiga kelele, hukukimbia, hukupiga simu ya kuomba msaada kabla ya mauaji wala hata hukupiga honi….! Kupatwa na mshtuko hakusababishi mtu ashindwe kupiga kelele ya kuomba msaada." Alisema mwendesha mashitaka huyo.

Kesi hiyo iliunguruma kwa siku 21. Wakati baraza la ushauri la wanaume watatu na wanawake tisa walipokamilisha kuipitia kesi hiyo, hapo mnamo June 30, 1997, iliwachukua saa tano kufikia maamuzi ambayo yalimkuta Tracie Andrew kuwa na hatia ya kuhusika mauaji ya mpenzi wake Lee Harvey. Alihukumiwa kifungo cha maisha jela. "Ni wewe pekee unayefahamu kwa usahihi kabisa ni kitu gani kilitokea usiku ule wa mauaji, lakini wote hapa tumeona ni kwa jinsi gani ulihusika na tukio hilo……… Naisikitikia sana familia iliyopoteza kijana wao" alisema Mheshimiwa Jaji Buckley aliyesikiliza kesi hiyo.

Familia ya Harvey haikuridhishwa na hukumu hiyo. Akongea na waandishi wa habari huku akijifuta machozi mama yake Lee Harvey alisema. "Sikuwahi kudhani kwamba mwanangu Lee alifia mikononi mwa mwanamke aliyempenda sana…….. lakini kwa jinsi ushahidi ulivyokuwa ukitolewa hapa mahakamani, niligundua kwamba alihusika na mauaji hayo, nadhani ingekuwa ni vyema sheria ikabadilishwa ili ahukumiwe kunyongwa, na ningehakikisha namchoma mwenyewe sindano ya sumu, kama hilo lingewezekana……"

Hata hivyo mnamo July 2011 Tracie aliachiwa huru baada ya kutumikia kifungo cha miaka 14 jela. Baada ya kutoka jela alianza maisha mapya ya uraiani kwa kubadilisha jina lake na kujiita Tia Carter.

Kitendo cha kuachiwa huru hakikuwafurahisha watu wengi nchini Uingereza akiwemo mama yake Lee Harvey na ili kuonyesha kukasirishwa kwake na jambo hilo alitunga kitabu ili kuonyesha masikitiko yake dhidi ya sheria za nchini humo. Kitabu hicho alikiita, Pure Evil: How Tracie Andrews Murdered My Son, Deceived the Nation and Sentenced Me to a Life of Pain and Misery.

 
Last edited by a moderator:
Haya ni Ijumaa nyingine tena, kama kawaida leo nimewaletea kesi hii iliyowahi kutokea nchini Uingereza.
Hapa mtajifunza jinsi vurugu katika mahusiano zinavyoweza kusababisha umauti, naamini wote tutajifunza kupitia mkasa huu..............
 
Nimependa wazee wa crime scene investigation walivyofanya upelelezi wao chezea polisi wa kidhungu wewe.Sijui ingekuwa bongo angeshikwa kupigwa hadi aseme,japo nafikiri wa murder wengi huwa hawapewi torture sana.
 
Haya ni Ijumaa nyingine tena, kama kawaida leo nimewaletea kesi hii iliyowahi kutokea nchini Uingereza.
Hapa mtajifunza jinsi vurugu katika mahusiano zinavyoweza kusababisha umauti, naamini wote tutajifunza kupitia mkasa huu..............

Ni kweli vurugu mara nyingi si jambo zuri na ni vyema sana kujitahidi kuepuka migogoro isiyo ya lazima!

Tukirudi kwenye kesi yenyewe, tofauti ya Afrika na nchi zilizoendelea, ni kuwa wenzetu wanazijua professional zao vilivyo. Ukiambiwa huyu ni mpelelezi, ujue ni mpelelezi kweli kweli na ukiambiwa huyu ni engineer ujue amebobea kweli kweli. Hakuna sana mianya ya rushwa wala kupendeleana, haki kwa kiasi kikubwa imetawala kesi zao.

Sina uhakika sana kama kwenye nchi zetu tunaweza kuwa na wapelelezi wenye fikra pevu kiasi hiki, hizi tu ndogo ndogo za mabwe pande zinatusumbua, sijui kwenye kesi complicated kama hiyo kama tungeweza kufanya chochote, lol!

Thanks Mtambuzi!
 
Too sad, wale wale tunaowaamini zaidi ndio wanaotutendea matendo ya kikatiri na ya kutisha ambayo yanailetea jamii kizunguzungu na kushindwa kuamini .

Kwa kweli huyu binti ni kiboko alitunga uongo ambao kwa akili za kawaida mtu anaweza akaamini maana mambo ya barabarani nayo ni kero sana e.g the DITO case.

Sasa sijui umwamini nani?

Thanks Mtambuzi!
 
Heshima sana Mkuu Mchambuzi kwa kisa kingine cha kusisimua sana na mafunzo makubwa ndani yake.Ni bahati mbaya visaa hivi haviwafikii wahusika wakuu Wapelelezi,Polisi na TISS yetu huku Tanzania.Wenzetu ulaya na Marekani wamepiga hatua kubwa mno kiasi unashangaa na kujiuliza kama ipo siku tutakaribia hata nusu ya viwango vyao maana kuwafikia ni ndoto za mchana.

Chukulia kisa cha Dr Ulimboka na wapelelezi wetu utaona jinsi wanavyojitahidi kuficha ukweli wakati sisi wananchi wakawaida tayari tushabaini watesaji ni maafisa usalama wa Ikulu.Hapa nyumbani wapelelezi badala ya kufanyakazi zao wanatenda kinyume kabisa cha taaluma zao.
 
Last edited by a moderator:
hapa polisi wetu wasingeambua chochote!ila huu ni ujumbe kwetu mara nyingi Mungu huwa anatuonyesha viashiri ving tu kuwa tulio nao sio sahihi!lakini mambo ya moyo haya bwana huwa tunajipa moyo kuwa ATABADILIKA!SI NI LEO TU!AFTER ALL NIMEMUUDHI!NGOJA TU AMALIZE HASIRA ZAKE!NA WATOTO HAWA NILIO NAO NTAMWACHIA NANI!MUDA WOTE NILIOISHI NAE NTAMWACHAJE!JAMII NAYO ITASEMAJE!SI WATANIONA MI SIO MVUMILIVU!AH NA HIZI MALI JE TULIZOCHUMA!DINI YANGU HAIRUHUSU!na mengine meengi
 
Asante ni nzuri yenye kusisimua.
Lakini kuna mahali umepunja sana,
nini kilifanya afunguliwe baada ya kifungo cha miaka 15
wakati alihukumiwa kifungo cha maisha.

Na binti zako hawajambo wote.
 
mimi nimevutiwa na muendesha mashtaka Bw.Crigman anapocheka kisha kumwambia Tracie Andrews kwamba sababu iliyomfanya achelewe kuomba msaada kwa zaidi ya robo ni kutokana na kujaribu namna ya kutengeneza mawazo ya kubuni story ili kuwadanganya polisi....kweli upelelez ni fani...lol
 
mimi nimevutiwa na muendesha mashtaka Bw.Crigman anapocheka kisha kumwambia Tracie Andrews kwamba sababu iliyomfanya achelewe kuomba msaada kwa zaidi ya robo ni kutokana na kujaribu namna ya kutengeneza mawazo ya kubuni story ili kuwadanganya polisi....kweli upelelez ni fani...lol
\
Hata mimi hiyo kauli imenichekesha sana.......................
 
mkuu ,wiki iliyopita nilitafuta sana case post yako sikuiona,leo nimebahatisha hii,kwani huwa ni msomaji mzuri wa hizi case.Endelea hivyo.
 
Kweli mapenzi yana ua!

Unayempenda sana ndio anaweza kuwa adui yako na kukumaliza.
 
M na shem/wifi yenu tushafikishana hapo so naona ni bora kufanya
immediate bond termination ili chozi lisije mdondoka mamangu.
 
Back
Top Bottom