CCM wadhibitiwa Arusha kwa kuandamana bila kibali
John Mhala, Arusha
Daily News; Saturday,October 11, 2008 @20:09
John Mhala, Arusha
Daily News; Saturday,October 11, 2008 @20:09
Viongozi kadhaa wa CCM Wilaya na Mkoa wa Arusha juzi jioni walidhibitiwa na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kwa madai ya kuandamana bila kibali. Waliokumbwa na dhahma hiyo ni pamoja na Katibu wa CCM wa Wilaya ya Arusha, Mohamed Nyawenga, ambaye alichaniwa nguo baada ya kurushia ngumi polisi hao.
Wengine waliokumbwa na tafrani hiyo ni Mbunge wa Arusha, Felix Mrema, aliyechaniwa shati, Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Arusha, Semmy Kiondo na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Jerry Siayi.
Mgombea udiwani wa Kata ya Sombetini, Alphonce Mawazo, alijeruhiwa mkono katika tukio hilo.Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha Basilio Matei alithibitisha kuwapo kwa tukio kwa kusema chanzo chake ni maandamano yaliyofanywa na wana-CCM baada ya kumaliza mkutano wa kampeni kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa udiwani wa Sombetini unaofanyika leo.
Matei alisema maandamano hayo hayakuwa rasmi kwani muda wa mwisho wa kufanya mikutano na mikusanyiko ni saa 12 jioni lakini wana CCM hao walifanya maandamano zaidi ya muda huo.Hata hivyo kauli ya Kamanda Matei ilipingwa na Katibu Mwenezi Kiondo aliyesema viongozi wa CCM na wafuasi wao hawakuandamana bali walikuwa wakienda kwa miguu katika ofisi ya kata kufanya tathmini.
Kiondo alisema inasikitisha kwamba FFU hao wengi wao walikuwa wamelewa na walikuwa wamejikita zaidi katika kuwapiga.Katibu huyo alisema kuwa viongozi wote waliripoti Polisi na kupewa cheti cha PF3 ili kwenda kupata matibabu hospitali na wamefungua kesi katika Kituo Kikuu cha Polisi mjini hapa juu ya suala hilo.