The Informer
Senior Member
- Jun 14, 2010
- 119
- 29
RAIA Mwema, KULIKONI na Dira ndiyo magazeti huru yaliyobaki sasa hivi. Buriani MWANAHalisi, limenunuliwa na Rostam na sasa kila siku linaandika habari za kuwabeba mafisadi. Toleo la sasa Kubenea kaandika stori -- "Kikwete kumwangukia Rostam." Total bullshit...
Lowassa, Chenge waivuruga CCM
MWANDISHI WETU
Dodoma
GENGE la wanasiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) linalomuunga mkono Waziri Mkuu wa zamani aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa, kwa lengo la kuhakikisha kuwa mwanasiasa huyo mwenye tuhuma mbalimbali anakuwa Rais wa Tanzania kwenye uchaguzi wa 2015 limepata pigo kubwa baada ya kinara wa kundi hilo, Rostam Aziz, kujiuzulu kama Mbunge wa Igunga.
Rostam, ambaye alikuwa anategemewa sana na kundi hilo kutokana na utajiri wake mkubwa wa pesa, hivi karibuni alitangaza kuachana na siasa ikiwa ni baada ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC) kutaka viongozi wote wenye tuhuma za ufisadi kuondoka kwenye chama hiko.
Kitendo cha Rostam kujiuzulu kimechukuliwa kwa hisia tofauti na kundi linalomuunga mkono Lowassa, huku ikionekana kuwa waziri mkuu huyo wa zamani sasa ni dhahiri kuwa naye anatakiwa kufuata nyayo za Rostam na kung'atuka mwenyewe kabla ya kufukuzwa.
Kiongozi mwingine wa kundi hilo, Andrew Chenge, naye yuko kwenye shinikizo kubwa kujiuzulu nyadhifa zake zote za uongozi ndani ya CCM.
Lowassa ambaye ameelezwa kuanza kuonyesha wazi wazi kuwa na malengo mazito zaidi ya kisiasa, ameelezwa kutokua tayari kuachia nafasi yake ya ubunge, hata kama atajitoa katika nafasi zake za uongozi ndani ya CCM.
Habari kutoka kwa watu waliokaribu na Lowassa zinaeleza kwamba mwanasiasa huyo ameapa kung'ang'ania nafasi yake ya ubunge na kwamba uongozi mwengine yulo tayari kutimuliwa apate nafasi ya kulipa kisasi.
Mbali ya Lowassa na Rostam, mwanasiasa mwengine aliyetajwa wazi kutakiwa kujitoa ni Mbunge wa Bariadi Magharibi na mwanasheria mkuu wa zamani Andrew Chenge ambaye yeye ameelezwa kuyumba katika kuamua.
"Huyu mzee (Lowassa) sasa ameamua kupambana hadi dakika ya mwisho ili wamfukuze na yeye kupata nafasi ya kulipa kisasi kwa yeyote atakayehusika na kutimuliwa kwake mkiwamo nyie waandishi na hata uongozi wa juu wa CCM," anasema mwana CCM ambaye anakiri kuwa anamuunga mkono Lowassa.
Shabiki huyo wa Lowassa ametoboa siri nzito kwamba kundi la Lowassa linalohusisha wanasiasa kadhaa wakiwamo wabunge na viongozi wa CCM mikoani, limepania hata kulipa kisasi kwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete.
"Lowassa sasa ameamua kutoa makucha yake kwamba ana hasira sana na Mwenyekiti wetu Rais Kikwete na anajitapa kuwa ameandaa mkakati kambambe wa kuhakikisha anamaliza vibaya ngwe yake iliyobaki," anasema mbunge mmoja ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC).
Katika moja ya mikakati hiyo, tayari baadhi ya viongozi ndani ya CCM wameshaanza kutoa matamshi ya wazi kumdhalilisha Rais Kikwete ikiwamo ile ya kuwakejeli wana CCM wanaomuunga mkono kwa kusema "wanajipendekeza kwa Rais".
Hatua nyingine imeelezwa ni kuhakikisha vyombo vya habari vinamchafua kwa kipindi chote cha uongozi wake kilichosalia ikiwa ni pamoja na kuandaa taarifa za uongo zikimhusisha Rais Kikwete na kashfa ili kupotosha vita dhidi ya ufisadi ndani ya CCM iliyobeba jina la "uvuaji gamba".
"Jamaa wanapanga hata kutunga uongo kumhusisha Rais na kashfa ili kuupotosha umma kwamba CCM wote ni mafisadi ili dhana ya uvuaji gamba isiwe na maana tena," anaeleza mbunge mwingine wa CCM mjini Dodoma.
Imeelezwa kwamba hata baadhi ya wabunge wameshaanza kuingiza hoja kichini chini zinazolenga kumchafua Rais Kikwete na baadhi wamekua wakidai kwamba anaendelea na mahusiano na mafisadi hadi sasa.
Wajumbe wa NEC ambacho kinatarajia kufanya kikao chake hivi kariburini wamejipanga kuhakikisha kuwa kama alivyoondoka Rostam, Lowassa na Chenge nao lazima wang'oke ili wasiendelee kukichafua chama kwa tuhuma mbali mbali za ufisadi.
Wakati Lowassa amechafuka kwa kashfa ya Richmond na familia yake kuwa na tuhuma za kumiliki mali nyingi zisizoweza kuelezeka, ikiwemo kununua jumba la thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1 kwenye mtaa wa matajiri London, Chenge amehusishwa kwenye kashfa ya rada na kumiliki akaunti ya benki nje ya nchi yenye zaidi ya shillingi bilioni 2 kinyume na maadili ya uongozi wa umma.
Wajumbe kadhaa wa NEC, wakiwemo baadhi ya wenyeviti wa CCM wa mikoa ambao wanajulikana kuwa wako kwenye kundi la Lowassa nao wamejipanga kuwatetea kina Lowassa na Chenge wasifukuzwe kwenye chama.
Wafuasi wa kundi hilo tayari wameanza kampeni za kuwachafua viongozi wanaoheshimika kwenye CCM, akiwemo Waziri wa Afrika Mashariki Samuel Sitta, kwa lengo la kuzua tafrani ndani ya chama tawala.
"Lengo la kundi hili, ikiwemo baadhi ya wenyeviti wa CCM, ni kutaka kuleta mgogoro mkubwa ndani ya CCM ili ionekane kuwa chama kinabidi kiwafukuze viongozi wote wakuu. Wafuasi wa Lowassa na Chenge wanadhani kuwa wanaweza kuwaokoa viongozi hawa wawili kwa kuzua mgogoro ndani ya chama na kuleta maasi," alisema mjumbe mmoja wa NEC kutoka mkoa wa kusini Tanzania.
Viongozi na wanachama wengi wa CCM wameonesha kuvutiwa na uongozi mahiri wa Secretariati ya CCM iliyo chini ya Katibu Mkuu Wilson Mukama, naibu katibu mkuu John Chiligati na katibu wa uenezi Nape Nnauye.
"Nape, Chiligati na Mukama wameonesha ujasiri mkubwa sana wa kusimamia maamuzi ya NEC ya kutaka mafisadi wote watimuliwe kwenye CCM," alisema mkumbe wa mkutano mkuu wa CCM kutoka Dar es Salaam ambaye aliomba kutotajwa jina.
"Huyu kijana Nape ametia fora kwa kuwa makini sana na kuwajibu hawa mafisadi kila mara wanapojaribu kujitutumua na kutaka kuleta maasi ndani ya CCM."
Viongozi wa CCM wamesema kuwa kikao kijacho cha NEC kitatakiwa kufanya maamuzi magumu kwa kuwafukuza Lowassa na Chenge kwenye chama ili wasiendelee kukichafua chama na kuleta makundi ndani ya CCM kuelekea kwenye uchaguzi wa 2015.
"Zama za mafisadi kukiweka chama chetu mfukoni sasa imepita. Hiki chama kinarudi kuwa mikononi mwa wakulima na wafanyakazi, hivyo basi Lowassa na Chenge lazima watimuliwe kwani kuwepo kwao kunazidi kukichafua chama na kuendekeza siasa za visasi, chuki na uasi," alisema kada mmoja wa CCM.
Lowassa, ambaye aliishambulia serikali ya Rais Jakaya Kikwete Bungeni hivi karibuni kuwa inaogopa kufanya maamuzi magumu sasa anaelekea kutafunwa na dhana yake mwenyewe baada ya kutakiwa yeye mwenye kufanya maamuzi magumu na kuiga mfano wa Rostam wa kujiuzulu badala ya kusubiri aibu ya kufukuzwa na wajumbe wa NEC.
<Source: KULIKONI, Julai 29, 2011>