nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Waandishi Wetu
Toleo la 238
9 May 2012
WAKATI Chama cha Mapinduzi (CCM) kikikanusha taarifa za wabunge na mawaziri wake kuhamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), upepo mkali unazidi kuvuma miongoni mwa wanachama wake kubebwa na upepo wa mageuzi, wengine kwa malengo mazuri na baadhi kuficha uchafu wao.
Raia Mwema limefahamishwa kuwapo mtafaruku ndani ya vyama vyote viwili, kuhusiana na wimbi la wanachama wa CCM kuhamia CHADEMA, kutokana na sababu mbalimbali, huku baadhi ya wananchi wakiwasukuma wabunge wao kuhama.
Taarifa za hivi karibuni zimeeleza kwamba baadhi ya mawaziri walioondolewa katika mabadiliko ya hivi karibuni, wamekuwa wakipata mashinikizo kutoka kwa wapiga kura wao wakiwataka kutoka CCM na kuhamia CHADEMA, wakidai kuwa wameonewa.
Mbali ya kuwapo taarifa hizo, habari zinasema kwamba CHADEMA nao wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kujiweka karibu na mawaziri hao, huku baadhi ya viongozi na wanachama wa chama hicho kinachokua kwa kasi wakihadharisha upokeaji wa viongozi ‘wachafu' watakaokichafua na hata kupunguza imani waliyonayo wananchi.
Tayari CCM kupitia Katibu wake wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, imekanusha vikali taarifa zilizotolewa na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kwamba kuna wabunge 70 wa CCM na mawaziri saba wanataka kuhamia CHADEMA.
Nape alimtaka Mbowe kuwa makini kutokana na nyadhifa alizonazo ndani ya chama hicho cha upinzani, akisema kwamba Mbowe ameitoa kauli hiyo bila kufanya utafiti.
Mbowe alipokuwa mjini Arusha alihutubia mkutano wa hadhara hivi karibuni na kueleza kuwa, miongoni mwa walioomba kujiunga CHADEMA ni mawaziri walioteuliwa wiki iliyopita na Rais Jakaya Kikwete, akisema kuna wimbi kubwa la wanachama watakaohamia CHADEMA.
Kutokana na kuwapo hofu ya CHADEMA kuingiliwa na kutekwa na mafisadi, Mbowe aliwatoa wafuasi wake hofu kwa kusema; "..msiwe na hofu na wale wanaojiunga na chama kutokea CCM, kwa kuwa kuna wengi walitoka huko na ni wapigania haki wazuri. Mfano, Katibu Mkuu, Dk. Willbrod Slaa, Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje na Makamu Mwenyekiti wetu, Said Amour Arfi, ambaye alikuwa TLP kabla ya kujiunga CHADEMA."
Miongoni mwa mawaziri walioondolewa na Kikwete ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami, ambaye kashfa ya ukaguzi wa magari ndani ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ilimponza, na sasa wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini alikotoka wamecharuka.
Habari za kutoka Moshi Vijijini zinaeleza kwamba baadhi ya wananchi kwenye baadhi ya kata nyingi wameanza kurudisha kadi za CCM na kujiunga CHADEMA baada ya mbunge wao kutoswa, wakiamini kwamba hakutendewa haki.
Mmoja wa wananchi hao aliyejitambulisha kwa jina la Fadhili Msangi wa Mabigini, alituma ujumbe mfupi wa maneno akidai kwamba yeye na wenzake wanaamini kwamba mbunge wao ameonewa akasema; "Ameondolewa kiujanja ujanja kwa kisingizio cha kuwajibika! Kwa nini Mkuchika (George), Maghembe (Jumanne) na Lazaro Nyalandu aliyekiuka kiapo kwa kusambaza dokezo la serikali wasiwajibishwe pia?"
Imedaiwa kwamba wananchi hao wamemtaka mbunge wao atoe msimamo ili waamue nini cha kufanya, lakini Dk. Chami alipoulizwa na Raia Mwema, alikataa kuzungumzia suala hilo kwa sasa akisema anaandaa ziara jimboni kwake atakapotoa msimamo na kuwaelimisha wapiga kura wake kilichotokea.
"Binafsi sina taarifa sahihi ya hicho unachoniambia. Inawezekana ikawa ni hasira tu za watu, ama mbinu nyingine za kutaka kunichafua, lakini kwa sasa niacheni nitapanga ratiba ya ziara jimboni ili nipate picha ya hali halisi huko na huko ndiko mahali pa kutolea msimamo wangu na kuwaelimisha wapiga kura na wananchi," alisema Dk. Chami Jumanne ya wiki hii.
Kutokana na kutowapata baadhi ya wabunge na mawaziri wanaotajwa, hatutawataja majina, lakini hali ndani ya CHADEMA nako si shwari baada ya kuwapo hofu ya chama hicho kutekwa na mafisadi kutoka CCM na wanaohama kwa maslahi binafsi.
Taarifa ndani ya CHADEMA zinaeleza kwamba, baadhi ya wanachama wamekuwa wakitahadharisha wimbi la mageuzi nchini wakisema ni muhimu kuendelea kuwapokea wanachama ambao ni wananchi wa kawaida wenye nia ya dhati, tofauti na wanasiasa ambao wanakimbilia madaraka.
"Lazima tuwe na tahadhari maana wenzetu walikuwa wakitupiga vita wakiwa viongozi ndani ya CCM, sasa wanaona umma unatuunga mkono wanaanza kujipendekeza kwetu, lazima tuwe waangalifu, pamoja na kuwa wengine watatusaidia, lakini wengine ni hatari kwetu. Tuwe makini kufungua milango na madirisha wataingia mbu na hata nyoka," anasema Maria Mremi wa Urafiki, Dar es Salaam.
Tayari Mbowe na viongozi wengine wa CHADEMA walishaweka msimamo mara kadhaa wakisema kwamba chama chao kimeshakomaa na kwamba watakuwa makini katika kupokea wanachama wa CCM, lakini hawatasita ‘kuvuna' wanachama kutoka chama chochote, ikiwa ndio njia ya kujiimarisha.
Hofu kubwa iliyojitokeza ni baada ya kuhamia CHADEMA kwa wana CCM ambao wanafahamika kuwa karibu sana na Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kuhusishwa na kashfa ya mradi wa kuzalisha umeme kupitia kampuni ya Richmond Development LLC, ya Marekani, Edward Lowassa, ikionekana kama mkakati mahsusi.
Wana CCM hao, James Millya, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana (UVCCM) mkoani Arusha, na mwenzake Ally Bananga, walijiondoa CCM na kuhamia CHADEMA wakiaiminika kutangulizwa na Lowassa ‘kumsafishia' njia na ‘kupima upepo' kabla ya kiongozi huyo kuhamia CHADEMA.
Mbowe katika mkutano wa Arusha aligusia suala hilo akasema,; "Sasa wanaowataja akina Ole Millya, Bananga na wengine watashangaa kusikia orodha na majina ya wana CCM watakaojiunga CHADEMA," kauli ambayo inazidi kuweka uzito wa taarifa kwamba vigogo zaidi watajiunga CHADEMA.
Hata hivyo, wiki kadhaa zilizopita Mbowe aliliambia Raia Mwema kwamba atakuwa mtu wa mwisho kufanya jambo ambalo litakishushia chama chake heshima mbele ya umma na kukanusha taarifa za kuwapo mazungumzo na Lowassa.
Mbowe alisema hakuna mkakati wala mazungumzo rasmi kati ya CHADEMA na Lowassa ama mwakilishi wake kuhusiana na yeye ama mfuasi wake kuja CHADEMA.
"Hatujawahi kuwa na mazungumzo yoyote au mkakati wowote na Lowassa au mwakilishi wake kuhusu yeye au mtu mwingine yeyotekuja CHADEMA. Nilikutana na Lowassa nje ya Bunge katika misa ya Sokoine (Marehemu Edward Moringe) kule Dakawa na
hatukuzungumza chochote," alisema.
Mbowe ambaye amekuwa akipambana kujenga upinzani kwa takriban miaka 20 sasa, amesema atakuwa mtu wa mwisho kujihusisha na jambo lolote ambalo linaweza kuishushia heshima CHADEMA, pamoja na kuwa atatumia kila fursa atakayoipata kuibomoa CCM kwa kupangua makada wake kwani "ndio njia pekee ya kukijenga CHADEMA."
Lakini wakati hayo yakiendelea, ndani ya CCM wanadaiwa kuendelea ‘kuomba' Lowassa aondoke ili kurahisisha mpango wa Chama hicho wa kujisafisha, maarufu kama kujivua gamba.
Taarifa za uhakika zinabainisha kuwa CCM imekuwa ikifuatilia nyendo za Lowassa kwa karibu na wamekuwa wakiamini kwamba kama ataondoka na kundi lake basi chama hicho kinaweza kurejea katika umoja wake na hivyo kuanza upya kuimarisha nguvu zake za ndani dhidi ya kambi ya upinzani.
Mbowe pia amewahi kubeza taarifa za mafisadi kuiteka CHADEMA akiuita huo ni umbea wenye lengo la kuichafua CHADEMA kwa kuihusisha na mafisadi, kutokana na chama hicho kupata umaarufu kwa kupambana na ufisadi kwa vitendo.
Kwa upande mwingine, gazeti hili katika matoleo yake yaliyopita liliwahi kuandika habari ya namna UVCCM ilivyokuwa ikitumika ‘kumzunguka' Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kwa kuhujumu baadhi ya uamuzi wa CCM na sehemu ya uamuzi wa Serikali, habari ambayo iliwahi kuzungumziwa pia na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Membe katika mahojiano yake aliyowahi kufanya na gazeti hili alieleza kuwa baadhi ya vigogo waliohusika katika kashfa ya Richmond wamejipanga kumhujumu Kikwete kwa njia mbalimbali lakini akisisitiza azma yao hiyo haitafanikiwa na wala kumpotezea mwelekeo wa namna ya kuongoa nchini Kikwete.
Toleo la 238
9 May 2012
- Wapiga kura wataka wabunge wao wahamie upinzani
- Mafisadi nao sasa wataka kukimbilia huko kujiokoa
- CHADEMA nao wajipanga kudhibiti uchafu
WAKATI Chama cha Mapinduzi (CCM) kikikanusha taarifa za wabunge na mawaziri wake kuhamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), upepo mkali unazidi kuvuma miongoni mwa wanachama wake kubebwa na upepo wa mageuzi, wengine kwa malengo mazuri na baadhi kuficha uchafu wao.
Raia Mwema limefahamishwa kuwapo mtafaruku ndani ya vyama vyote viwili, kuhusiana na wimbi la wanachama wa CCM kuhamia CHADEMA, kutokana na sababu mbalimbali, huku baadhi ya wananchi wakiwasukuma wabunge wao kuhama.
Taarifa za hivi karibuni zimeeleza kwamba baadhi ya mawaziri walioondolewa katika mabadiliko ya hivi karibuni, wamekuwa wakipata mashinikizo kutoka kwa wapiga kura wao wakiwataka kutoka CCM na kuhamia CHADEMA, wakidai kuwa wameonewa.
Mbali ya kuwapo taarifa hizo, habari zinasema kwamba CHADEMA nao wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kujiweka karibu na mawaziri hao, huku baadhi ya viongozi na wanachama wa chama hicho kinachokua kwa kasi wakihadharisha upokeaji wa viongozi ‘wachafu' watakaokichafua na hata kupunguza imani waliyonayo wananchi.
Tayari CCM kupitia Katibu wake wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, imekanusha vikali taarifa zilizotolewa na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kwamba kuna wabunge 70 wa CCM na mawaziri saba wanataka kuhamia CHADEMA.
Nape alimtaka Mbowe kuwa makini kutokana na nyadhifa alizonazo ndani ya chama hicho cha upinzani, akisema kwamba Mbowe ameitoa kauli hiyo bila kufanya utafiti.
Mbowe alipokuwa mjini Arusha alihutubia mkutano wa hadhara hivi karibuni na kueleza kuwa, miongoni mwa walioomba kujiunga CHADEMA ni mawaziri walioteuliwa wiki iliyopita na Rais Jakaya Kikwete, akisema kuna wimbi kubwa la wanachama watakaohamia CHADEMA.
Kutokana na kuwapo hofu ya CHADEMA kuingiliwa na kutekwa na mafisadi, Mbowe aliwatoa wafuasi wake hofu kwa kusema; "..msiwe na hofu na wale wanaojiunga na chama kutokea CCM, kwa kuwa kuna wengi walitoka huko na ni wapigania haki wazuri. Mfano, Katibu Mkuu, Dk. Willbrod Slaa, Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje na Makamu Mwenyekiti wetu, Said Amour Arfi, ambaye alikuwa TLP kabla ya kujiunga CHADEMA."
Miongoni mwa mawaziri walioondolewa na Kikwete ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami, ambaye kashfa ya ukaguzi wa magari ndani ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ilimponza, na sasa wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini alikotoka wamecharuka.
Habari za kutoka Moshi Vijijini zinaeleza kwamba baadhi ya wananchi kwenye baadhi ya kata nyingi wameanza kurudisha kadi za CCM na kujiunga CHADEMA baada ya mbunge wao kutoswa, wakiamini kwamba hakutendewa haki.
Mmoja wa wananchi hao aliyejitambulisha kwa jina la Fadhili Msangi wa Mabigini, alituma ujumbe mfupi wa maneno akidai kwamba yeye na wenzake wanaamini kwamba mbunge wao ameonewa akasema; "Ameondolewa kiujanja ujanja kwa kisingizio cha kuwajibika! Kwa nini Mkuchika (George), Maghembe (Jumanne) na Lazaro Nyalandu aliyekiuka kiapo kwa kusambaza dokezo la serikali wasiwajibishwe pia?"
Imedaiwa kwamba wananchi hao wamemtaka mbunge wao atoe msimamo ili waamue nini cha kufanya, lakini Dk. Chami alipoulizwa na Raia Mwema, alikataa kuzungumzia suala hilo kwa sasa akisema anaandaa ziara jimboni kwake atakapotoa msimamo na kuwaelimisha wapiga kura wake kilichotokea.
"Binafsi sina taarifa sahihi ya hicho unachoniambia. Inawezekana ikawa ni hasira tu za watu, ama mbinu nyingine za kutaka kunichafua, lakini kwa sasa niacheni nitapanga ratiba ya ziara jimboni ili nipate picha ya hali halisi huko na huko ndiko mahali pa kutolea msimamo wangu na kuwaelimisha wapiga kura na wananchi," alisema Dk. Chami Jumanne ya wiki hii.
Kutokana na kutowapata baadhi ya wabunge na mawaziri wanaotajwa, hatutawataja majina, lakini hali ndani ya CHADEMA nako si shwari baada ya kuwapo hofu ya chama hicho kutekwa na mafisadi kutoka CCM na wanaohama kwa maslahi binafsi.
Taarifa ndani ya CHADEMA zinaeleza kwamba, baadhi ya wanachama wamekuwa wakitahadharisha wimbi la mageuzi nchini wakisema ni muhimu kuendelea kuwapokea wanachama ambao ni wananchi wa kawaida wenye nia ya dhati, tofauti na wanasiasa ambao wanakimbilia madaraka.
"Lazima tuwe na tahadhari maana wenzetu walikuwa wakitupiga vita wakiwa viongozi ndani ya CCM, sasa wanaona umma unatuunga mkono wanaanza kujipendekeza kwetu, lazima tuwe waangalifu, pamoja na kuwa wengine watatusaidia, lakini wengine ni hatari kwetu. Tuwe makini kufungua milango na madirisha wataingia mbu na hata nyoka," anasema Maria Mremi wa Urafiki, Dar es Salaam.
Tayari Mbowe na viongozi wengine wa CHADEMA walishaweka msimamo mara kadhaa wakisema kwamba chama chao kimeshakomaa na kwamba watakuwa makini katika kupokea wanachama wa CCM, lakini hawatasita ‘kuvuna' wanachama kutoka chama chochote, ikiwa ndio njia ya kujiimarisha.
Hofu kubwa iliyojitokeza ni baada ya kuhamia CHADEMA kwa wana CCM ambao wanafahamika kuwa karibu sana na Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kuhusishwa na kashfa ya mradi wa kuzalisha umeme kupitia kampuni ya Richmond Development LLC, ya Marekani, Edward Lowassa, ikionekana kama mkakati mahsusi.
Wana CCM hao, James Millya, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana (UVCCM) mkoani Arusha, na mwenzake Ally Bananga, walijiondoa CCM na kuhamia CHADEMA wakiaiminika kutangulizwa na Lowassa ‘kumsafishia' njia na ‘kupima upepo' kabla ya kiongozi huyo kuhamia CHADEMA.
Mbowe katika mkutano wa Arusha aligusia suala hilo akasema,; "Sasa wanaowataja akina Ole Millya, Bananga na wengine watashangaa kusikia orodha na majina ya wana CCM watakaojiunga CHADEMA," kauli ambayo inazidi kuweka uzito wa taarifa kwamba vigogo zaidi watajiunga CHADEMA.
Hata hivyo, wiki kadhaa zilizopita Mbowe aliliambia Raia Mwema kwamba atakuwa mtu wa mwisho kufanya jambo ambalo litakishushia chama chake heshima mbele ya umma na kukanusha taarifa za kuwapo mazungumzo na Lowassa.
Mbowe alisema hakuna mkakati wala mazungumzo rasmi kati ya CHADEMA na Lowassa ama mwakilishi wake kuhusiana na yeye ama mfuasi wake kuja CHADEMA.
"Hatujawahi kuwa na mazungumzo yoyote au mkakati wowote na Lowassa au mwakilishi wake kuhusu yeye au mtu mwingine yeyotekuja CHADEMA. Nilikutana na Lowassa nje ya Bunge katika misa ya Sokoine (Marehemu Edward Moringe) kule Dakawa na
hatukuzungumza chochote," alisema.
Mbowe ambaye amekuwa akipambana kujenga upinzani kwa takriban miaka 20 sasa, amesema atakuwa mtu wa mwisho kujihusisha na jambo lolote ambalo linaweza kuishushia heshima CHADEMA, pamoja na kuwa atatumia kila fursa atakayoipata kuibomoa CCM kwa kupangua makada wake kwani "ndio njia pekee ya kukijenga CHADEMA."
Lakini wakati hayo yakiendelea, ndani ya CCM wanadaiwa kuendelea ‘kuomba' Lowassa aondoke ili kurahisisha mpango wa Chama hicho wa kujisafisha, maarufu kama kujivua gamba.
Taarifa za uhakika zinabainisha kuwa CCM imekuwa ikifuatilia nyendo za Lowassa kwa karibu na wamekuwa wakiamini kwamba kama ataondoka na kundi lake basi chama hicho kinaweza kurejea katika umoja wake na hivyo kuanza upya kuimarisha nguvu zake za ndani dhidi ya kambi ya upinzani.
Mbowe pia amewahi kubeza taarifa za mafisadi kuiteka CHADEMA akiuita huo ni umbea wenye lengo la kuichafua CHADEMA kwa kuihusisha na mafisadi, kutokana na chama hicho kupata umaarufu kwa kupambana na ufisadi kwa vitendo.
Kwa upande mwingine, gazeti hili katika matoleo yake yaliyopita liliwahi kuandika habari ya namna UVCCM ilivyokuwa ikitumika ‘kumzunguka' Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kwa kuhujumu baadhi ya uamuzi wa CCM na sehemu ya uamuzi wa Serikali, habari ambayo iliwahi kuzungumziwa pia na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Membe katika mahojiano yake aliyowahi kufanya na gazeti hili alieleza kuwa baadhi ya vigogo waliohusika katika kashfa ya Richmond wamejipanga kumhujumu Kikwete kwa njia mbalimbali lakini akisisitiza azma yao hiyo haitafanikiwa na wala kumpotezea mwelekeo wa namna ya kuongoa nchini Kikwete.