Kauli za viongozi wa ccm ni za bendera kufuata upepo

Jan 16, 2007
721
176
Na Salim Said
KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati amesema chama hicho hakina ugomvi wala uadui na wabunge wake wanaoongoza vita dhidi ya mafisadi nchini.

Kauli hiyo imetolewa siku chache baada ya mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kuondoa utata uliotokana na maazimio ya Halmashauri Kuu ya chama hicho ukionyesha kuwa wabunge wanaopiga kelele za ufisadi, wanakichafua chama na serikali yake.

Chiligati ndiye aliyetoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari ambayo ilisisitiza kuwa vita hiyo si ya kikundi cha watu wachache bali ya CCM.

Jana, Chiligati alikuwa ni mtu mwenye kuunga mkono kikundi hicho wakati Mwananchi ilipotaka maoni yake kuhusu wabunge hao ambao wanaonekana kukaidi maazimio ya Nec, huku wakitamba kuwa hakuna anayeweza kuwafunga mdomo.

“CCM haina ugomvi na wabunge wake wala mtu yeyote anayejitoa mhanga kupinga ama kupambana na mafisadi,” alisema Chiligati ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

“Msimamo wa chama chetu ni kwamba rushwa ni adui wa haki, usichukue, kuomba wala kutoa rushwa, huo ndio wimbo wa kila mwana-CCM.

“Hatuna ugomvi wala uadui na mtu yeyote anayepambana na rushwa, ufisadi, uporaji, wizi na ujambazi. Huo ndio msimamo wa CCM.”

Baada ya kikao cha Nec kilichofanyika Dodoma mwezi uliopita, Chiligati alisema CCM imeunda kamati ya watu watatu, inayoongozwa na rais Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kuwachunguza wabunge wenye tabia ya kuishambulia serikali nje ya vikao vya chama.

Habari za ndani ya kikao hicho ambazo baadaye zilivuja kwa vyombo vya habari, zilieleza kuwa Nec ilimweka kitimoto Spika Samuel Sitta kwa madai kuwa anaruhusu mijadala inayokichafua chama na serikali, huku baadhi ya wajumbe wakishinikiza anyang'anywe kadi ya CCM kwa kile kilichoelezwa kuwa anawapa uhuru bungeni watu wanaoishambulia serikali kwa ufisadi.

Kauli hiyo mpya ya Chiligati, inaweza kuwa imetokana na msimamo wa Rais Kikwete ambaye alisema CCM haiwezi kuwafunga midomo wabunge wake.

Katika mazungumzo yake na wananchi aliyoyafanya kwa njia ya televisheni na redio katikati ya wiki iliyopita, Rais Kikwete alisema kuikosoa serikali ni kuifanya ijiangalie na kujirekebisha na hivyo haiwezi kuwazuia wabunge kuikosoa.

Kauli ya Kikwete ilifuatiwa na ya waziri mkuu wa zamani, John Malecela ambaye alimsifu mwenyekiti wake kwa kuruhusu mijadala hiyo na kuongeza kuwa vita dhidi ya mafisadi ni takatifu kwa kuwa ilikuwapo tangu enzi za TANU.

Tangu kumalizika kwa Nec, wabunge ambao wamekuwa wakijinadi kuwa ni makamanda wa vita dhidi ya ufisadi wamekuwa wakikaririwa na vyombo vya habari wakisema kuwa hakuna mtu anayeweza kuwafunga midomo.

Wabunge hao pia walifanya mikutano ya hadhara kwenye majimbo ya baadhi yao na kusisitiza msimamo wao kuwa wataendelea na vita hiyo kwa kuwa ilani ya CCM inawaruhusu.
 
Captain yupo busy sana na mambo ya CCM wakati wizara yake inadidimia. Wizara ya ardhi inaongoza kwa kulalamikiwa kwa huduma mbovu na rushwa, lakini kila kukicha mheshimiwa ni CCM, CCM, CCM....Kazi za maendeleo ya makazi na nyumba utaanza lini?
 
Captain yupo busy sana na mambo ya CCM wakati wizara yake inadidimia. Wizara ya ardhi inaongoza kwa kulalamikiwa kwa huduma mbovu na rushwa, lakini kila kukicha mheshimiwa ni CCM, CCM, CCM....Kazi za maendeleo ya makazi na nyumba utaanza lini?
Huyu jamaa kasuku tu!
 
Back
Top Bottom