Dotto C. Rangimoto
JF-Expert Member
- Nov 22, 2012
- 1,985
- 1,282
KAKOBE USIPOTOSHE, TANGANYIKA SI URITHI TOKA KWA MUNGU.
Askofu Kakobe mara kadhaa amenukuliwa akilalamika juu ya mfumo wa Muungano uliopo, haridhishwi na mfumo huu na anachotaka hadhi ya Tanganyika kama nchi ikiwa na serikali yake irudi.
Sina ugomvi ama shaka juu ya yeye kutaka Tanganyika irudi ikiwa na hadhi yake kama nchi, ila nina shaka na ugomvi juu ya moja ya hoja zake anazotumia kutimiza lengo lake. Hoja yake ni kwamba Tanganyika ni urithi kutoka kwa Mungu na kero za muungano ni matokeo ya laana ya kupuuza mipaka tulopewa na Mungu.
Kabla ya kuingia ukoloni Afrika, na tena kabla hata ya kuingia ukristo Afrika, hatukuwa na mipaka tulokuwa nayo sasa, bali kulikuwa na tawala za jadi chini ya kabila moja ua makabila mengi yenye tamaduni zilizo fanana na walioamua kuishi pamoja.
Mkataba wa Berlin uliofanyika chini ya uenyekiti wa Chancellor Otto von Bismarck mwaka 1884-1885, mkutano ulifuatia na utiaji saini mkataba ulioligawanya bara la Afrika na kuweka mipaka. Mipaka ambayo ilipelekea baadhi ya wamasai kuwa wakenya na wengine kuwa watanganyika, mipaka ambayo ulipelekea baadhi ya wamakonde kuwa wasumbiji na wengine kuwa watanganyika.
Kakobe anatumbia kuwa Tanganyika iliyowaweka baadhi ya wanyasa kuwa wamalawi na baadhi yao kuwa watanganyika ni urithi na mpango wa Mungu. Mungu yupi? Huyu Bismarck aliyeitisha kikao cha kuligawa bara la Afrika? Mungu yupi alituletea laana ya kutugawa badala ya kutuunganisha?
Hivi kwanini tunaheshimu nchi na jina tuliopewa na wazungu badala ya kuheshimu jina na nchi tuliyounda sisi wenyewe kwa hiyari yetu? Hivi Afrika kuna nchi yenye thamani na ya kujivunia kama waafrika zaidi Tanzania? Hakuna, Tanzania ni zao la akili zetu, maarifa yetu na kujitambua kwetu, Tanganyika ni zao la wazungu na Zanzibar ni zao Sultani.
Wazungu walitumia ukristo kupora na kututawala, Kakobe anapita njia ileile ambayo kanisa ilipita, njia ya kutuzubaisha akili kwa kutumia neno la Mungu, njia ya kutufanya kukumbatia biblia na kufumba macho kwa kusali, kufumbua tumebakiwa na biblia, lakini dhahabu, alamasi na rasilimali zetu zingine zikabebwa na wazungu, zikawatajirisha, na sasa hivi wanajiita wahisani na misaada yao ya masharti.
Wanatuwekea masharti wakati biashara ya utumwa, kuwatumia watumia watumwa kama nguvu kazi, na ukoloni ndio msingi wa utajiri wa Ulaya na Amerika, na wasasa wanazidi kujitajirisha kwa kutumia ukoloni mambo leo na kuletea hadithi za wahisani wenye huruma nasi huku moyoni wanamitego ilo jificha kwenye masharti.
Kuhusu muungano kinacho tushughulisha ni ubinafsi, umimi na ubaguzi, kinyume na hapo hakuna haja ya Zanzibar na hakuna haja ya Tanganyika, bali haja hasa yenye mantiki ni Tanzania. Hili litawezekana endapo ile dhana ya utaifa wa Tanganyika na Zanzibar sanjari na ubinafsi ama umimi ukiondoka katika nyoyo zetu.
Pamoja na hayo, Kakobe kasema haya kanisani, kanisa ambalo linakusanya watu wenye misimamo tafauti ya kisiasa, kanisa lenye wanachama wa vyama tafautitafauti vya siasa na wasio na chama kabisa!
Sasa Kakobe anaitaka Tanganyika kwa kutumia mgongo wa dini, nasema ni wa wakupuuzwa, atafute jukwaa la kisiasa lakini si jukwaa la dini sababu katika kanisa wako watu wa misimamo tafauti ya kisiasa.
NDANI YA KANISA KUNA.
1. Watu wanaotaka serikali moja kama mimi, yaani kusiwe na Zanzibar wala Tanganyika bali kuwe na Tanzania tu.
2. Kuna watu wanaotaka serikali mbili, yaani serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
3. Kuna watu wanaotaka serikali tatu kama Kakobe, yaani Serikali ya Tanganyika, Zanzibar na Serikali ya muungano.
4. Kuna watu wanaotaka Muungano wa mkataba
5. Kuna watu wasiotaka Mungano kabisa!
SASA askofu anapoleta siasa katika kanisa, ikiwa ndani ya kanisa kuna mchanganyiko huo ni kuligawa kanisa, na kama ikitokea ndio msimamo wa kanisa lake, na ikitokea kanisa lingine likiwa na msimamo tafauti na wa kanisa la kakobe, au kukatokea dini nyingine ikawa na msimamo tafauti na msimamo wa dini ya Kakobe, ndio mwanzo makanisa haya au dini hizi kushambuliana Kisiasa na pia kupambana kuhakikisha watu wao ndio wanapata madaraka ya serikalini ili kufanikisha maslahi yao ya kisiasa.
Tukifikia huko tutaanza kuchagua viongozi kwa misingi ya dini zetu na madhehebu yetu ili wakafanikishe kupita kwa misimamo ya makanisa, misikiti na dini zetu, tukifika huko na hasa ikitokea dini fulani mtu wao hakushinda na wakamua kutokubali, basi nchi itachafuka, na mtu kama Kakobe, uwezo wa kuruka Marekani na kutulia huko anao, ni mimi na wewe ndio tutabaki katika nchi iliyochafuka huku tukishuhudia dada zetu, mama zetu, watoto zetu au wadogo zetu wakifa na kutaabika, Kakobe na familia yake watakuwa wanakula bata Marekani.
HUYU KAKOBE ASHUGHULIKIWE KWA MUJIBU WA SHERIA HARAKA INAVYOWEZEKANA, SI WA KUACHWA HIVIHIVI TU.
Huu ndio msingi wa sababu wa kanisa na msikikiti kuambiwa kuacha siasa, kama mchungaji au shekhe anataka siasa asitumie mimbari za dini, akiwa katika mimbari za dini asilete misimamo ya kisiasa, bali atumie jukwaa la siasa kufanya siasa na atumie jukwaa la dini kufanya kazi za dini. Kiongozi wa dini hatakiwi kuwa na msimamo wa kisiasa lakini anaweza kuishauri serikali, wanasiasa na waumini wake juu mambo ya nchi na siasa bila kuwa na msimamo au bila kuwapa msimamo ambao utapelekea kuligawa taifa kwa misingi ya dini.
Mathalani anaweza kuwashauri na Kuwahimiza waumini juu ya umuhimu wa kupiga kura, kufuatilia siasa za nchi yao, kuchagua viongozi waadilifu na wasiopokea rushwa, umuhimu wa kutafakari juu ya mfumo wa serikali na uendeshaji nchi, nk
Lakini kingozi wa dini hapaswi kusema chagua fulani, au chama fulani, au kwa upande wa mfumo wa muungano kuwa mfumo fulani ndio mzuri na sahihi na ule si sahihi na haufai, mambo hayo ni ya wanasiasa na ni waumini wenyewe wenye itikadi tafauti kuamua juu ya hayo na si kuamuliwa au kushurutishwa au kuamriwa na kiongozi wa dini.
Neno la KIONGOZI wa dini huhesabika kama amri, na kwa kauli ya Kakobe ilikuwa amri kwa waumini wake wafuate maneno yake na jambo hili sio SAHIHI HATA KIDOGO.
ASKOFU AU SHEKHE hakatazwi kufanya saisa midhali ni mtanzania, ila SIASA afanye nje ya msikiti au kanisa, na fanye hivyo bila kutumia wadhifa wake wa kanisani au msikitini.
MCHUNGAJI msigwa ni mwanaisiasa anayefanya VIZURI SANA, lakini hatumii uchungaji wake au kanisa lake kijinufaisha kisiasa, bali anatumia jukwaa la siasa kufanya siasa na anatumia jukwaa lake la dini kufanya uchungaji wake.
Kwanini KAKOBE ASIFANYE KAMA MSIGWA? Mbona Mchungaji Msigwa tunamuelewa vizuri tu? NAREJEA TUACHE UJINGA.
MUUNGANO WETU NA NENO.
1
Neno limeota meno, lajazua tafarani,
Siyaoni mapatano, sote vipembe kichwani,
Mwana ashikwe mkono, asipotee njiani,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
2
Hakika nimekubali, heshima kwa muungano,
Usitafute kibali, hubiri utengamano,
Tuwashinde majahili, wanotaka utengano,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
3
Hekima zao wahenga, zimenikumbusha mbali,
Zanifikirisha ngenga, za wenzetu majahili,
Wanawaza kujitenga, sasa wamekuwa nduli,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
4
Niambie yafaani, maneno ya utengano,
Liwapi yenye thamani, nataka yako maono,
Zanzibar ya Sultani, au wetu Muungano?
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
5
Zanzibar si thamani, kuuzidi muungano,
Tanganyika izikeni, hatutaki utengano,
Mipaka ya wakoloni, isilete mapambano,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno,
6
Tanganyika ni Berlini, ni zao la wakoloni,
Zenj mno ithamini, ni fahari ya Sultani,
Tanzania ya Amani, na Nyerere tambueni,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
7
Tanzania imefuta, mipaka ya wakoloni,
Pomoya imetuleta, wa bara na visiwani,
Waasisi mwawateta, mna wazimu rasini?
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
8
Kila nikiyatazama, naona yako na meno,
Na kinywa mmehasama, ndimi kama msumeno,
Chombo chaenda mrama, yaacheni mabishano
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
9
Kiongozi huongoza, watu wakamfuata,
Tena huyasikiliza, yanoleta vutavuta,
Kwa hekima huyamaliza, bila kuwata utata
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
10
Mtawala hutawala, wananchi wakaogopa,
Akisema nyote lala, kitandani wajitupa,
Sasa wachoke kulala, wababe hutapatapa,
Halikidhi mahitaji, neno likiota meno.
Dotto Rangimoto Chamchua.(Njano5)
whatsapp/call 0622845394 Morogoro