Uchaguzi 2020 Hotuba ya Tundu Lissu kutangaza nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania - Juni 08, 2020

CHADEMA

JF-Expert Member
Apr 13, 2013
488
2,468


Hotuba ya Tundu Lissu, FULL TEXT:

KWANINI NAGOMBEA URAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA?

Wananchi na raia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania popote walipo, ndani na nje ya nchi yetu;

Wanachama, wapenzi na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA);

Marafiki wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika ukanda wa Afrika Mashariki, ukanda wa Kusini mwa Afrika, Umoja wa Afrika na katika jumuiya ya kimataifa kwa ujumla;

UTANGULIZI

Kama ambavyo imekuwa jadi ya nchi yetu, siku ya Jumapili ya mwisho ya mwezi Oktoba wa kila mwaka wa tano, sisi raia wa Tanzania hupiga kura ili kuwachagua viongozi wetu wa ngazi mbali mbali. Sasa kipindi hicho kimewadia. Huu ni mwaka wa Uchaguzi Mkuu, na tarehe 25 Oktoba 2020, Jumapili ya mwisho ya mwezi huo, sisi wananchi katika wingi wetu, tutafurika katika vituo vya kupigia kura katika sehemu mbali mbali za nchi yetu kwa lengo la kufanya hiyo sala ya raia walio huru, yaani kuchagua viongozi wetu.

Kama ambavyo nimewahi kugusia siku za nyuma, sasa napenda kuwataarifu kwamba nimetangaza rasmi nia yangu ya kugombea nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Tayari nimeshawasilisha taarifa rasmi ya kutangaza nia hiyo kwa Katibu Mkuu wetu wa Chama, kama ilivyoelekezwa kwenye maelekezo yake kwa wanachama wa chama chetu. Nina wajibu wa kutaja kile ambacho kimenisukuma kutaka kugombea nafasi ya juu kabisa ya uongozi katika mfumo wetu wa kikatiba, yaani Rais wa Jamhuri ya Muungano.

NCHI IKO NJIA PANDA

Kwa kipindi cha miaka mitano itakayoishia Oktoba mwaka huu, nchi yetu imetawaliwa na Serikali ya Rais John Pombe Magufuli na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa namna ambayo imeiweka nchi yetu katika mtihani mkubwa kiuchumi, kisiasa na kidiplomasia. Kwa mtihani huo, nchi yetu iko katika njia panda na, kwa vyovyote vile itakavyokuwa, Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utakuwa na umuhimu mkubwa katika historia ya nchi yetu.

UCHUMI UMEANGUKA

Badala ya kuzingatia mazingira haya halisi ya kiuchumi ndani na nje ya nchi yetu, Rais Magufuli ameendesha uchumi wetu bila sera au mipango madhubuti ya uchumi, bali kwa kutumia amri za Ikulu na za majukwaa ya kisiasa. Bila sera inayoeleweka au mipango thabiti ya kiuchumi au kibiashara, sasa Serikali yetu imejiingiza kwenye biashara, kuanzia ya kununua na kuuza mazao ya biashara, mabenki, uchimbaji madini hadi biashara ya kuendesha shirika la ndege.

Kwa kutumia njia hizo za amri za kisiasa, vyombo vya ulinzi na usalama, vikiwemo Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ), Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Idara ya Usalama wa Taifa na Ujasusi (TISS) pamoja na Mamlaka ya Kodi (TRA) vimetumika kukamata kwa nguvu na kutaifisha mali za wafanya biashara wetu wa ndani na makampuni ya wawekezaji kutoka nje.

Hata wakulima wadogo wa vijijini hawajaachwa salama, kama ilivyotokea kwenye zao la korosho kwenye mikoa ya Kusini mwaka jana ambako wakulima walinyang’anywa mazao yao kwa nguvu za kijeshi na ukatili mkubwa kwa amri ya Rais Magufuli mwenyewe. Badala ya kulipwa bei kubwa kama walivyoahidiwa na Rais, wakulima hao walidhulumiwa fedha zao na wameachwa katika umaskini mkubwa. Hivi ndivyo ilivyotokea pia kwa wafanya biashara wa maduka ya fedha za kigeni ambao walivamiwa na askari wa Jeshi la Wananchi na maafisa wa Benki Kuu na kunyang’anywa fedha na mali zao nyingine.

Ili kupata fedha za kuendeshea miradi yake ya miundo mbinu, Serikali ya Rais Magufuli imekusanya kodi kutoka kwa kila mwananchi na kila mfanya bishara, mkubwa na mdogo, kwa ukatili mkubwa. Wafanya biashara wamebambikiziwa kodi kubwa ambazo hazilingani na mapato yao au hali ya biashara zao. Wasioweza kulipa kodi hizo za kubambikiza sio tu wamefilisiwa, bali wengi wao wameshtakiwa kwa makosa makubwa ya kiuchumi ambayo hayana dhamana. Wengi wanaozea katika magereza mbali mbali ya nchi yetu kwa sababu ya kushindwa kulipa gharama kubwa wanazodaiwa kulipa ili kununua uhuru wao. Wengine hata wamefia magerezani au kutokana na mshtuko wa kunyang’anywa mali zao bila utaratibu.

Matokeo ya sera hizi za kiuchumi za Rais Magufuli yameonekana wazi. Uchumi wetu umeanguka; wafanya biashara wengi na wawekezaji kutoka nje ya nchi wamefunga biashara au kusitisha uwekezaji wao; na wengine wamekimbiza biashara na mitaji yao nchi za nje. Hali hii imesababisha mapato ya serikali kuanguka vibaya; ukosefu mkubwa wa ajira na umaskini wa wananchi wetu, hasa vijana na wanawake, umeongezeka. Hali ya kiuchumi ya wananchi wetu leo ni mbaya zaidi kuliko ilivyokuwa wakati Rais Magufuli anaingia madarakani mwaka 2015 na kabla ya hapo.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utaamua kama Rais Magufuli atapata fursa ya miaka mitano mingine ya kuendelea kuharibu uchumi wetu na kuwafukarisha wananchi wetu, au kama tutaanza na mwanzo mpya wa kiuchumi kwa nchi yetu kwa kumuondoa yeye na chama chake madarakani.

NCHI YA WAJANE, YATIMA NA VILEMA

Tangu mwaka 1984, nchi yetu imekuwa na Hati ya Haki za Binadamu katika Katiba yetu, ambayo imeweka na kufafanua haki mbali mbali za binadamu na wajibu wa wananchi. Ndani ya miaka mitano ya utawala huu, utaratibu wote wa haki za binadamu na utawala wa sheria umechanwa chanwa vipande na Serikali ya Rais Magufuli na vyombo vyake vya ulinzi na usalama.

Tanzania imekuwa nchi ya vilio na machozi ya wajane, yatima na vilema wa viungo na wa kisaikolojia wa miaka mitano ya utawala wa Rais Magufuli. Upotezaji watu, utekaji nyara, utesaji na ukandamizaji wa wakosoaji wa serikali kwa kuwafungulia kesi za kubambikiza za uchochezi, makosa ya mtandao au utakatishaji fedha. Mauaji ya wananchi wasio na hatia yoyote na wapinzani wa serikali na chama tawala. Haya ni baadhi tu ya matendo mabaya yaliyokithiri sana katika Tanzania ya Magufuli.

Hakuna aliyeachwa salama. Viongozi wa kisiasa, kama marehemu Alfons Mawazo, Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Geita, aliyekatwa katwa mapanga na kutupwa bararabani mchana kweupe. Au Diwani Simon Kanguye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko Mkoa wa Kigoma, aliyechukuliwa na watu wanaosemekana kuwa maafisa usalama wa taifa na kutokomezwa kusikjulikana. Wanaharakati wa mitandaoni na waandishi habari, kama Ben Saanane, msaidizi wa Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, aliyenaswa na ‘watu wasiojulikana’ na kupotezwa hadi leo. Au mwandishi habari Azory Gwanda, aliyechukuliwa nyumbani kwake na watu waliojitambulisha kuwa askari polisi na hadi leo hajulikani alipo. Hawa ni baadhi tu ya wahanga wa Tanzania ya Magufuli.

Wapo pia wasanii, kama wanamuziki wa kizazi kipya Roma Mkatoliki na Ney wa Mitego, waliokamatwa na kuteswa katika nyumba za siri za kutesea watu, kabla ya kuachiliwa huru baada ya siku kadhaa. Au wafanyabiashara na matajiri, kama Mo Dewji aliyedakwa nje ya hoteli na kupotezwa kabla ya kutupwa mita mia kadhaa kutoka Ikulu ya Dar es Salaam. Wanafunzi, kama Aquilina Aquiline, aliyepigwa risasi na askari polisi wakati akiwa kwenye dala dala kuelekea chuoni kwake. Orodha ya wahanga wa utawala huu ni ndefu na ya kuhuzunisha.

Matumizi ya nguvu za kijeshi dhidi ya wananchi wanaotekeleza haki na wajibu wao kikatiba yamekuwa makubwa. Utamaduni wa kutowawajibisha wale wote wanaohusika na mauaji na mateso haya ya Watanzania umekithiri. Imekuwa ni jambo la kawaida kwa vyombo vya usalama vya nchi yetu kuua au kujeruhi raia wasiokuwa na hatia bila hatua zozote kuchukuliwa dhidi ya wahusika. Ukweli kwamba natolea tangazo hili la nia ya kugomea Urais nikiwa uhamishoni barani Ulaya, badala ya kulitolea nikiwa ndani ya nchi nilikozaliwa na kukulia, ni ushahidi tosha wa majanga makubwa ambayo yameikumba nchi yetu katika miaka hii mitano ya utawala wa Rais Magufuli.

Uchaguzi Mkuu huu utaonyesha ni kwa kiasi gani wananchi wa Tanzania hawako tayari tena kuendelea kuonewa, kudhalilishwa na kunyanyaswa na wale waliowapa dhamana ya kuwaongoza, au kama bado wako tayari kuendelea kuwa kwenye minyororo hii. Uchaguzi Mkuu huu utaamua kama vilio hivi vya wajane, yatima na vilema vitapata Mfariji Mkuu wa kuvituliza, atakayefuta machozi ya wanaolia na atakayeponya majeraha na makovu mengi ya Tanzania ya Magufuli, au kama Mtesaji Mkuu atapata miaka mingine mitano ya kuongeza majeraha, vilio na machozi haya.

UTAWALA WA KIIMLA

Tangu nchi yetu ilipoingia katika mfumo wa kidemokrasia wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992, mfumo huo wa kidemokrasia umekua na kukomaa kama ushahidi wa chaguzi mbali mbali zilizofanyika tangu wakati huo unavyodhihirisha. Hata hivyo, tangu aingie madarakani, Rais Magufuli ametangaza vita kubwa dhidi ya mfumo wa kidemokrasia wa vyama vingi vya siasa. Yeye mwenyewe alitangaza hadharani, wakati wa maadhimisho ya miaka 39 ya CCM mwezi Februari 2016, kwamba atahakikisha hakuna tena vyama vya upinzani ifikapo mwaka 2020, yaani mwaka huu.

Wote tumeshuhudia utekelezaji wa ahadi yake hiyo kwa vita kubwa ambayo imeendeshwa dhidi ya viongozi, wanachama na wafuasi wa vyama halisi vya upinzani, hasa CHADEMA na, kwa upande wa Zanzibar, ACT Wazalendo. Mfumo wa vyama vingi vya siasa umewekwa kwenye hatari kubwa na ya kipekee. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utaamua kama Rais Magufuli anafanikiwa kutekeleza azma yake ya kuua mfumo wa kidemokrasia wa vyama vingi na kuirudisha nchi yetu katika zama za giza za mfumo wa chama kimoja, au kama mfumo huo wa kidemokrasia utadumu na kushamiri katika nchi yetu.

BUNGE DHAIFU

Sambamba na vita dhidi ya mfumo wa kidemokrasia wa vyama vingi, Rais Magufuli ameendesha vita kubwa dhidi ya Bunge na Mahakama. Historia ya Bunge letu la tangu Uhuru sio ya kujivunia sana. Ukiachia miaka michache ya mwanzo ya Uhuru na miaka kumi ya utawala wa Rais Jakaya Kikwete, Bunge letu lilikuwa bubu, kiziwi, kipofu na butu. Bunge lilianza kupata nguvu baada ya kuingia kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992 na hasa kuanzia Uchaguzi Mkuu wa kwanza wa vyama vingi wa mwaka 1995. Baada ya hapo mamlaka, hadhi na heshima ya Bunge letu iliongezeka, hasa katika miaka kumi ya Rais Kikwete iliyoishia mwaka 2015.

Ni heshima kubwa kwa marais wa nchi yetu wa wakati wa vyama vingi, hasa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, kwamba wakati wa utawala wao, Bunge letu lilipata nguvu na heshima kubwa mbele ya wananchi na katika jamii ya kimataifa. Ni heshima kubwa kwa Maspika wa Bunge letu wa kipindi hicho, hasa marehemu Samuel John Sitta na Mheshimiwa Anna Semamba Makinda, kwamba katika uongozi wao wa Bunge letu, Bunge lilipata sauti ya kusemea, masikio ya kusikia, macho ya kuona na meno ya kuuma katika kutekeleza wajibu wake wa kuisimamia na kuishauri serikali.

Bunge la Tanzania ya Magufuli, chini ya uongozi dhaifu wa Spika Job Yustino Ndugai, limeingiliwa, kuvurugwa na kutekwa nyara na Serikali ya Magufuli kwa namna ambayo halina tofauti tena na Bunge la Tanzania ya zama ya chama kushika hatamu, hasa la kati ya miaka ya 1965 na 1985. Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 utaamua kama tutarudi kwenye Bunge linalojitambua, kama la marehemu Spika Sitta na la Mama Makinda, au kama tutaongezewa miaka mingine mitano ya Bunge lililopoteza mwelekeo kama hili la Spika Ndugai.

MAHAKAMA MATEKA

Rais Magufuli ameingilia na kuvuruga uhuru wa Mahakama ya Tanzania kwa namna ambayo haijawahi kutokea katika historia yetu yote. Amewatisha na kuwadhalilisha hadharani majaji wa mahakama zetu za juu. Ameondoa baadhi ya majaji kinyume na utaratibu uliowekwa na Katiba ya nchi yetu. Ameingilia utendaji wao wa kazi kwa kuwaelekeza namna ya kufanya kazi zao wakati yeye sio mwanasheria. Ametoa ahadi za kuizawadia Mahakama endapo itawatia hatiani watuhumiwa wa kesi za kubambikiza za serikali yake. Ameahidi hadharani kuwapandisha vyeo mahakimu waliowafunga wapinzani wa CCM na kuwafanya Majaji wa Mahakama Kuu.

Matokeo ya vitendo hivi vya Rais Magufuli ni kwamba, Mahakama imekuwa sehemu kubwa ya kukandamizia haki za binadamu za wananchi wetu. Badala ya kuwa chombo cha kulinda Katiba yetu, haki za binadamu na utawala wa sheria, Mahakama imegeuzwa na utawala huu kuwa chombo cha kukandamizia haki kwa kunyima watuhumiwa wa kesi za kubambikizia dhamana ; kuwarubuni majaji na mahakimu wetu ili watoe adhabu kali kwa wapinzani wa serikali, au watumie visingizio vya kiufundi vya kisheria ili kukwepa kutenda haki ya msingi kwa mujibu wa sheria.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utaamua kama tutaendelea kuwa na Mahakama inayotumika kukanyaga haki za wananchi, au tutakuwa na Mahakama itakayolinda misingi muhimu ya kikatiba na haki za binadamu za wananchi wetu.

‘FUNGO WA KIMATAIFA’

Ndugu wananchi,

Rais wa nchi yoyote ile ni Mwanadiplomasia Mkuu wa nchi yake. Kwa takriban robo karne ya uongozi wake, Baba wa Taifa aliiweka Tanzania yetu katika ramani ya kidiplomasia ya kimataifa. Tulitengeneza marafiki na washirika wa maendeleo katika pande zote mbili za Vita Baridi. Tulitengeneza mshikamano na mahusiano ya karibu na nchi za Afrika Mashariki. Tulikuwa mstari wa mbele katika harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika; na tulikuwa kinara katika harakati za kuunganisha nguvu za Bara la Afrika na Ulimwengu wa Tatu.

Nchi yetu na viongozi wake waliheshimika kila mahali duniani. Tuliielewa na kuiheshimu dunia, na dunia ilituelewa na kutuheshimu. Kwa sababu ya kuwa na mahusiano hayo mema na jumuiya ya kimataifa, nchi yetu ilifaidika sana na fursa na misaada mbali mbali ya jumuiya ya kimataifa. Tulijengewa reli ya TAZARA na Wachina; na tulijengewa Kitivo cha Uhandisi cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na vyuo kadhaa vya ufundi na Wajerumani Magharibi. Tuliletewa chakula cha njaa cha mahindi ya yanga na unga wa dona na Wamarekani na tulijengewa shule za sekondari za kilimo na Wakuba. Msingi wa diplomasia ya kimataifa uliowekwa na Baba wa Taifa uliendelezwa na warithi wake katika Ikulu yetu.

Hata hivyo, tangu aingie madarakani mwaka 2015, Rais Magufuli ameharibu mahusiano yetu na jumuiya ya kimataifa. Ametutenganisha na kila rafiki tuliyekuwa naye miaka ya nyuma. Ametutenganisha na majirani zetu katika Jumuiya ya Afrika Mashariki; na ndugu zetu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambao tuliwatolea damu yetu ili wajikomboe, na katika Umoja wa Afrika. Ametufarakanisha hata na mashirika muhimu ya kimataifa kama Umoja wa Mataifa na taasisi zake kama WHO. Ametugombanisha na Umoja wa Ulaya na marafiki zetu wa kihistoria kuanzia China iliyoko mashariki hadi Marekani iliyoko magharibi.

Sasa nchi yetu inasemwa vibaya katika mabaraza ya kimataifa na inatengwa au kuwekewa vikwazo katika misaada, fursa na manufaa mengi yatokanayo na diplomasia yenye busara na akili. Leo kila chombo cha habari cha kimataifa kinachoandika habari za Tanzania kinaanza kwa kutaja jinsi Rais wetu asivyoendana na taratibu zinaoeleweka na kukubalika kimataifa. Kama nilivyosema miaka miwili na nusu iliyopita, nchi yetu imekuwa ‘fungo wa kimataifa.’ Fungo ni mnyama wa jamii ya nguchiro ambaye akifukuzwa anatoa harufu mbaya inayowafukuza wale wote wanaomkimbiza.

Badala ya kujirudi na kujirekebisha, viongozi wa serikali yetu, wamekuwa wanawatukana marafiki zetu wa tangu Uhuru kwa kuwaita ‘mabeberu’ na kufukuza au kuwasumbua mabalozi na wawakilishi wao hapa kwetu. Uchaguzi Mkuu wa mwaka utaamua kama sisi tutaendelea kujifanya kisiwa katika bahari pana ya mahusiano ya kidiplomasia ya kimataifa, au tutajirudi na kutambua kwamba sisi ndio tunaoihitaji dunia kuliko dunia inavyotuhitaji sisi.

KATIBA MPYA

Mwaka 1978 Rais wetu wa kwanza Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitamka, katika mahojiano na Shirika la Habari la Uingereza (BBC), kwamba alikuwa na mamlaka, kwa mujibu wa Katiba na sheria za yetu, ya kuwa dikteta. Katiba aliyokuwa anaizungumzia Baba wa Taifa wakati huo ni hii hii tuliyonayo leo. Na sheria alizokuwa anazizungumzia bado zipo na nyingine nyingi zimeongezwa katika kipindi hiki cha Tanzania ya Magufuli.

Katika miaka mitano ya utawala wake, Rais Magufuli ametufundisha somo kubwa na lisilosahaulika la umuhimu wa Katiba Mpya na kuwa na mfumo wa kisheria ulio wa haki na unaozingatia haki na utu wa binadamu. Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu utaamua kama tumelielewa somo hili kubwa na tuko tayari kuendelea kuwa na katiba na sheria zinazotengeneza watawala wenye mamlaka ya kidikteta, au kama tutarudi kwenye mchakato wa kutengeneza Katiba Mpya uliovurugwa na wanaCCM mwaka 2014.

SASA, BAADA YA YOTE HAYA NILIYOYALALAMIKIA, JE, NI KITU GANI NITAKIFANYA TOFAUTI ENDAPO NITAPATA HESHIMA, IMANI NA DHAMANA YA KUWAONGOZA WANANCHI KAMA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO?

  • Endapo nitachaguliwa kuwa Rais, Serikali yangu itaandaa sera thabiti za kiuchumi zitakazohakikisha kwamba Serikali inabakia kama mwangalizi wa shughuli za kiuchumi zinazoendeshwa na sekta binfasi. Aidha, Serikali itakuwa msimamizi wa maslahi ya jumla ya wananchi ili kuhakikisha usalama wa bidhaa na udhibiti wa bei za bidhaa na huduma muhimu kwa ustawi wa wananchi.
  • Vile vile, Serikali yangu itafanya mageuzi makubwa ya mfumo wa utozaji kodi ili kuondoa utitiri wa kodi na hali ya sasa ambapo TRA inatumika kuangamiza biashara na mitaji ya wafanya biashara na wajasiri amali, badala ya kuhakikisha biashara zao zinashamiri na kuendelea kukua, kutengeneza ajira zaidi kwa wananchi wetu na kuongeza mapato ya kikodi ya Serikali.
  • Endapo nitapata dhamana ya kuiongoza nchi yetu, nitamaliza kabisa vitendo hivi kikandamizaji kwa kufutilia mbali sheria zote za kikandamizaji ambazo zimetumika kuumiza wananchi wetu na wakosoaji wa Serikali.
  • Aidha, Serikali yangu itafanya mageuzi makubwa ya mfumo mzima wa vyombo vya ulinzi na usalama ili kuvifanya kuwa walinzi wa Katiba, haki za binadamu na uhuru wa wananchi kufanya shughuli zao kwa mujibu wa Katiba.
  • Serikali yangu haitatumia vyombo vya ulinzi na usalama dhidi ya wapinzani wake wa kisiasa na wakosoaji wake au vyombo huru vya habari. Serikali itaendeshwa kwa kufuata misingi ya utawala wa sheria zinazoendana na matakwa ya Katiba na ya mikataba ya kimataifa ambayo nchi yetu imeikubali kwa kuiridhia.
  • Endapo nitapata dhamana ya kuwa Rais wa nchi yetu, nitakuwa Mfariji Mkuu. Sitakimbilia mafichoni kijijini kwetu Mahambe endapo nchi yetu na wananchi wetu watakabiliwa na majanga, yawe ya asili kama matetemeko ya ardhi, au yawe ya maradhi kama COVID-19. Kama Rais, nitakuwa mstari wa mbele kuwapa waliofikwa na majanga hayo faraja na misaada na afueni za kibinadamu watakazohitaji. Tofauti na sasa kamwe sitawasimanga, kuwakejeli au kuwatweza waliofikwa na maafa.
  • Tofauti na Rais Magufuli, endapo nitachaguliwa katika nafasi hii ya juu kabisa katika nchi yetu, nitatii, kulinda na kuhifadhi mfumo wa vyama vingi vya siasa kwa kuondoa vikwazo na vizingiti vyote vya kikatiba, kisheria na kiutendaji vinavyozuia wananchi kufurahia haki zao zote za kidemokrasia. Katika uongozi wangu, mazuio ya mikutano ya hadhara na maandamano ya kisiasa ya wananchi, wawe kwenye vyama vya siasa au katika taasisi zao nyingine, yataondolewa. Kazi ya vyombo vya usalama itakuwa kulinda mikutano na maandamano hayo, badala ya kuwa vyombo vya kudhibiti wapinzani wa kisiasa wa chama na serikali iliyoko madarakani.
  • Endapo nitapata ridhaa ya wananchi wa Tanzania kuwaongoza kama Rais, nitarudisha hadhi, heshima na madaraka ya Bunge kama mhimili huru wa dola wenye mamlaka yanayolingana na ya Serikali ndani ya mipaka yake iliyowekwa na Katiba. Nitaondoa vikwazo na vizuizi vyote vya kikatiba, kisheria na kiutendaji ambavyo vimelizuia Bunge letu kutekeleza wajibu wake wa kuisimamia na kuiwajibisha Serikali na kuwawakilisha wananchi.
  • Endapo nikuwa Rais nitaifungulia Mahakama kutoka katika kifungo chake cha sasa kwa kuondoa kivuli cha Urais wa Kifalme na vizuizi na vizingiti vingine vyote vya kikatiba, kisheria na kitaasisi ambavyo vimeikabili kwa muda mrefu.
HAJA YA MARIDHIANO YA KITAIFA

Ndugu wananchi,

Mahatma Gandhi, mwasisi wa Taifa la India, aliwahi kusema : ‘Jicho kwa jicho itatufanya wote kuwa vipofu.’ Makosa mawili hayatengenezi jambo moja la haki; kama ambavyo waongo wawili hawatengenezi mkweli mmoja. Ninaamini kwamba matatizo makubwa na ya msingi ya matumizi mabaya ya madaraka na uonevu waliofanyiwa wananchi hayawezi kutatuliwa kwa kulipiza kisasi dhidi ya wale waliotutesa na kutukandamiza. Visasi ni upanga wa walio waoga na dhaifu, sio ngao ya walio jasiri. Kwa hiyo, kama Rais, Serikali yangu haitalipiza visasi vya mabaya mengi ambayo wananchi wetu, mimi mwenyewe na viongozi na wanachama wenzangu wamefanyiwa na utawala huu na hata na serikali za nyuma.

Badala ya kulipiza visasi, Serikali yangu itarudisha, kujenga na kuimarisha mapatano na maridhiano ya kitaifa yatakayojengwa katika misingi ya ukweli juu ya makosa yaliyofanyika; msamaha kwa wanaotubu makosa yao, na fidia kwa wahanga wa makosa hayo.

NIMEJIANDAA KWA MAJUKUMU

Nitaendelea kufafanua masuala haya na mengine mengi katika siku, wiki na miezi inayofuatia; na wakati wa kampeni ya Uchauzi Mkuu endapo nitapata ridhaa ya Chama changu ya kuwa mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano. Itoshe tu kusema, kwa sasa, kwamba ninaamini ninazo sifa zote stahiki za kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Kwa zaidi ya miaka 20 nimetetea haki na maslahi ya wananchi wa Tanzania katika maeneo mbali mbali ya nchi yetu. Nilikuwa wa kwanza kupigia kelele ukandamizaji mkubwa na dhuluma walizofanyiwa wananchi wa maeneo mbali mbali ya nchi yetu yenye utajiri wa madini. Nilikuwa wa kwanza kuonyesha matatizo makubwa yaliyoko kwenye sekta ya madini na maeneo mengine ya rasilmali asili za nchi yetu.

Kwa miaka saba, kabla ya risasi 16 za ‘watu wasiojulikana’ wa utawala wa Magufuli hazijaniondoa Bungeni na Tanzania, niliongoza mapambano ya haki, utawala wa sheria na demokrasia kama Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni. Niliongoza na kuratibu harakati za kupigania Katiba Mpya Bungeni na katika Bunge Maalum la Katiba kati ya 2011 na 2014. Nimekuwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS) kabla ya uongozi wangu kukatishwa kikatili na waitwao ‘watu wasiojulikana’ Septemba 7, 2017. Msimamo wangu katika masuala yote muhimu ya nchi yetu na ya watu wetu unajulikana wazi na wote na haujawahi kutetereka.

Katika utumishi wa kitaaluma na kisiasa wa zaidi ya miaka ishirini, nimetembelea kila mkoa na karibu kila wilaya ya nchi yetu. Kwa sababu hiyo, ninaifahamu Tanzania kwa undani na ninawafahamu Watanzania. Ninaelewa hofu zao, na ninaelewa matumaini yao. Muhimu zaidi, ninafahamu hifadhi kubwa ya nguvu, akili na ubunifu wa Watanzania ambao umejificha kwa sababu ya watu wetu kulazimishwa kuishi katika mazingira ya kikandamizaji na yaliyojaa hofu na kutojiamini.

Katika kipindi hicho hicho, nimetembelea, kusoma na kufanya kazi katika nchi mbali mbali za dunia. Nimeishi, kusoma na kufanya kazi katika Afrika yetu, Ulaya na Marekani ya Kaskazini. Katika mabara yote ya dunia hii, ni Bara la Australia peke yake ndiyo sijalitembelea bado. Ninaelewa masuala ya kimataifa kwa upana. Kwa sababu hizo, nitaleta katika Urais wa nchi yetu sio tu ufahamu wa Tanzania na Watanzania, bali pia uelewa wa mifumo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii ya kimataifa na nafasi yetu katika mifumo hiyo.

Kwa sababu nimekuwa mmojawapo wa wahanga wakubwa wa Tanzania ya Magufuli, ninafahamu maana ya kuishi chini ya utawala wa aina hii ambao tumekuwa nao kwa miaka mitano sasa. Nina uwezo wa kuwafuta machozi wale waliofanywa wajane na yatima na vilema wa utawala huu. Nina uwezo wa kutibu majeraha na makovu mengi ambayo wamesababishiwa watu wetu wengi.

SIFA ZA KUGOMBEA URAIS

Ninafahamu kwamba baadhi yenu mna hofu kubwa na ya halali kabisa juu ya mimi kuwa na sifa za kikatiba na kisheria za kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano. Hii ni kufuatia uamuzi wa Spika Ndugai wa kunifutia Ubunge mwezi Juni ya mwaka jana. Nitalitolea suala hili ufafanuzi wa kina wa kikatiba na kisheria endapo utahitajika. Itoshe tu kusema kwamba mtu anayekosa sifa za kugombea Urais (au Ubunge) kwa kukiuka masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ni yule tu ambaye amepatikana na hatia ya kukiuka Sheria hiyo na chombo pekee kilichoanzishwa kwa mujibu wa Sheria hiyo, yaani Baraza la Maadili.

Katika utumishi wangu wote kama kiongozi wa umma, mimi sijawahi kutuhumiwa, kushtakiwa, kuitwa kwenye shauri, kutolewa ushahidi wowote dhidi au kwa niaba yangu, na kuhukumiwa na Baraza hilo la Maadili kwa kosa lolote lile chini ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma. Aidha, sijawahi kutuhumiwa, kushtakiwa, kuitwa kwenye kesi, kutolewa ushahidi dhidi ya au kwa niaba yangu, kuhukumiwa na kuadhibiwa kwa kosa lolote linaloweza kunifutia sifa za kugombea nafasi yoyote ile ya uchaguzi wa umma kwa mujibu wa Katiba na sheria zetu za Uchaguzi.

Spika Ndugai ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo, licha ya dhamana hiyo kubwa ya uongozi aliyonayo kitaifa, yeye sio Baraza la Maadili, na wala sio Mwenyekiti au mjumbe wake. Kwa sababu hiyo, uamuzi wa Spika Ndugai wa kunifutia ubunge haujaniondolea sifa za kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania au nafasi nyingine yoyote ya uongozi.

Kwa hiyo, wananchi wenzangu, nawaombeni wote mniunge mkono katika safari hii ngumu iliyopo mbele yetu ya kuhakikisha kwamba:


  • Tunatibu majeraha na makovu mengi na makubwa ya Taifa letu;
  • Tunawatunza wajane, yatima na vilema wengi wa miaka hii mitano;
  • Tunafuta machozi na kutupilia mbali hofu tulizojazwa katika miaka hii ya adha kubwa;
  • Tunawaweka huru wafungwa na mateka wa utawala huu, tunaleta haki, amani ya moyo na nafuu ya Maisha kwa watu wote na kulirudisha Taifa letu katika misingi ya utu, haki na ubinadamu;
  • Tunaziba nyufa ambazo zimeligawa Taifa letu ; na
  • Tunajenga Taifa letu na kuwatoa wakulima, wafanyakazi, watumishi wa umma, wafanya biashara, wamachinga, mama lishe, vijana wasiokuwa na ajira, wake kwa waume wa Jamhuri ya Muungano kutoka kwenye lindi la umaskini, ukandamizaji, hofu na kukosa matumaini walilogubikwa na Tanzania ya Magufuli.
Nelson Rolihlahla Mandela, Rais wa kwanza wa Afrika Kusini huru na ya kidemokrasia alisema yafuatayo siku alipoapishwa Rais wa nchi hiyo tarehe 10 Mei 1994 : ‘Isijetokea kamwe, kamwe na kamwe kwamba nchi hii nzuri itashuhudia tena ukandamizaji wa mtu mmoja dhidi ya mwenzake na kubebeshwa dharau ya kuwa fungo wa kimataifa.’ Maneno haya yanaihusu nchi yetu kwa sasa.

Nawashukuruni sana kwa uvumilivu wenu na Mwenyezi Mungu awape baraka zote.

Tundu A.M. Lissu (MB)

Tienen, Ubelgiji

8 Juni 2020

 
Back
Top Bottom