Hadithi ya kusisimua: Jini mauti

Hadithi ya kusisimua: Jini Mauti-14

ILIPOISHIA

ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:
Hata usiku wa siku hiyo tulipokutana kwenye uwanja wa wachawi, sikuonekana kuwa na furaha, nilionekana kuwa mnyonge sana, bibi alifahamu kila kitu kilichotokea, akaamua kunifuata. Endelea sasa…

“Davina…”
“Abeee.”
“Hongera sana,” alisema bibi.
“Hongera sana,” alinipongeza, kidogo nikashtuka.
“Hongera ya nini?” niliuliza.

Badala ya kujibu swali hilo, bibi akaanza kucheka, kicheko kikubwa kilichoonesha ni jinsi gani alifurahi. Sikujua ni kitu gani kilichomfurahisha, nilibaki nikimshangaa, alichokifanya ni kuondoka mahali hapo.

Baadaye kukaanza kutolewa taarifa kwamba kulikuwa na mtu miongoni mwetu ambaye alifanya kazi nzuri sana ya kumleta mtu mmoja pale uwanjani, mtu ambaye kwa siku hiyo angetumika na kuwa nyama kwa ajili ya wachawi.

Sikujua mtu huyo alikuwa nani, nikabaki nikiangalia tu kila kilichokuwa kikiendelea. Baada ya dakika kadhaa, akaletwa mvulana mmoja mbele yetu, nilipomwangalia, nilihisi kumfahamu ingawa sikuwa na uhakika kwa kuwa mahali pale kulikuwa na mwanga hafifu.

Nilichokifanya ni kusogea mbele ili nimuone vizuri. Sikuamini mara baada ya kufika mbele na kugundua kwamba yule mtu niliyekuwa nikimwangalia alikuwa Thomas.
“Thomas….” niliita huku nikionekana kushtuka.

Thomas hakuongea kitu, alibaki akiniangalia tu, alionekana kama zezeta. Nilimsogelea zaidi na kumshika, nikataka azungumze kitu chochote kile, alikuwa kimya, nilipomfumbua mdomo, ulimi wake ulikuwa umekatwa.

Nililia sana, niliumia sana lakini cha kushangaza wachawi wenzangu walikuwa wakicheka tu. Nilitamani Thomas azungumze kitu chochote kile lakini haikuwa hivyo, alibaki kimya tu kitu kilichonifanya nione kwamba tayari nilimpoteza mtu niliyekuwa nikimpenda sana.

Siku hiyo, hatukufanya kazi zaidi ya kusherehekea tu, nililazimishwa kuwa na furaha lakini ilishindikana kabisa. Sherehe ilipofikia mwisho, Thomas akachukuliwa na kupelekwa katika sehemu moja ambayo huko ndipo walipohifadhiwa misukule na hata watu walioandaliwa kwa ajili ya kuliwa nyama.

Asubuhi ilipofika, nikaamka, nikajiandaa na kwenda shule. Nilionekana kuwa na mawazo mno, njiani nilishindwa kuvumilia, nilikuwa nikibubujikwa na machozi tu, sikuamini kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Nilipofika shuleni, kitu cha kwanza kabisa kukutana nacho, wanafunzi wengi walikuwa wakilia, vilio vilitawala kila kona, sikutaka kuuliza kulikuwa na nini, nilifahamu kila kitu nikajua tu kwamba taarifa zilikuwa zimetolewa kwamba Thomas alikuwa amefariki dunia.

Nilishindwa kuvumilia, nililia sana kwa ajili ya Thomas lakini nikashindwa kuyazuia tena machozi yangu mahali hapo, nikaanza kulia, tena kwa maumivu makali mno.
Kwa kuwa wengi walifahamu kwamba nilikuwa kwenye uhusiano na Thomas, wakaanza kunionea huruma, wakanifuata na kuanza kunibembeleza ninyamaze kitu kilichonifanya nilie zaidi.

Walimu wakatutangazia kwamba tulitakiwa kwenda msibani hivyo maandalizi yalitakiwa kufanyika. Baada ya dakika kadhaa tayari kila kitu kilikuwa tayari na hivyo kuanza kuelekea huko.

Tulipofika tukaanza kusikia sauti ya vilio mahali hapo, watu wengi walikuwa wakilia hali iliyoonesha kwamba Thomas alikuwa mtu aliyependwa mno, tukakaa katika sehemu maalum ambayo ilitengwa kwa ajili ya wanafunzi na walimu, tukakaa hapo huku tukiendelea kulia kama kawaida.

Msibani hapo hakukuwa na watu wa kawaida tu, nilipopiga macho huku na kule, nikafanikiwa kuwaona wachawi wengine nao wakiwa mahali hapo kuhakikisha amani inatawala. Katika hili ngoja nikwambie kitu kimoja, mara nyingi kunapokuwa na msiba wa mtu aliyechukuliwa msukule huwa wachawi waliohusika ambao walimchukua marehemu ni lazima wawepo hapo ili kuhakikisha kwamba kila kitu kinakuwa sawa.

Watu wanaposogea kule kulipokuwa na jeneza, kila mmoja alikuwa akimwagiwa unga usoni ili wale waliokuwa na nguvu ya kugundua kwamba yule aliyezikwa hakuwa mtu bali gogo au nyoka mkubwa, waweze kuuona mwili wa marehemu.


Je, kiliendelea nini? Usikose wiki ijayo.


 
Hadithi ya kusisimua: Jini Mauti-15

ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:

Watu wanaposogea kule kulipokuwa na jeneza, kila mmoja alikuwa akimwagiwa unga usoni ili wale waliokuwa na nguvu ya kugundua kwamba yule aliyezikwa hakuwa mtu bali gogo au nyoka mkubwa, waweze kuuona mwili wa marehemu. Endelea…

Ndivyo ilivyokuwa, wakati tunasimama na kuanza kuelekea kwenye jeneza kuaga, tayari wachawi wakakimbia na kuelekea kule, wakajipanga mstari, walikuwa uchi wa mnyama, kila aliyekuwa akilisogelea jeneza lile, alipuliziwa unga fulani usoni mwake, unga wenye nguvu uitwao Yakumonzi wenye rangi ya njano.

Waliponiona nasogea kule lilipokuwa jeneza, hawakunimwagia unga ule, nilikuwa mtu wao, wakaniacha na hivyo kuangalia ndani ya jeneza. Nilichokifikiria ndicho kilichokuwa, kulikuwa na mgomba mkubwa ndani ya jeneza, sikushtuka, nikazidi kulia niliamini kwamba Thomas alikuwa nyuma ya mlango.

Nilipotoka hapo, sikutaka kubaki nje, nilichokifanya ni kwenda ndani kwao huku nikilia, nilipofika sebuleni, nikakaa kwenye kochi na kuangalia nyuma ya mlango. Nilimuona Thomas akiwa amesimama na mchawi mmoja.

“Thomas wangu! Thomas wangu kwa nini hili limetokea?” nililia huku nikiuliza, macho yangu yalikuwa yakiwaangalia wawili hao waliokuwa nyuma ya mlango.
“Nyamaza Davina, kazi ya Mungu haina makosa,” aliniambia Anita, tayari alikuwa ameingia ndani ya sebule ile.
***
Nilitakiwa kusahau kila kitu, nilitakiwa kusahau kuhusu Thomas, kitendo kile cha kufariki dunia huku akiwa mbele ya macho yangu kiliniumiza sana. Mlinzi na dada wa kazi walichukuliwa na kupelekwa polisi, walitakiwa kuelezea kilichokuwa kimetokea.

Hawakujua kitu, walipoulizwa kama Thomas alimchukua mtu na kwenda naye chumbani, hakukuwa na aliyekumbuka chochote kile. Nguvu kubwa ya kichawi ikawasahaulisha kila kitu, hawakutakiwa kukumbuka kitu chochote kile kuhusu mimi.
Walichokikumbuka ni kwamba Thomas alitembelewa na mtu mmoja ambaye aliingia naye ndani, walipotakiwa kusema alikuwa nani, walisahau kabisa. Hiyo ilikuwa ni kazi ya bibi, alitaka kuwasahaulisha kila kitu na kweli alifanikiwa.

Sikuwahi kuhisi kama hapo baadaye ningekuwa na furaha kabisa, kila siku nilikuwa mtu wa huzuni kwani kuchukuliwa kwa Thomas na kufanywa msukule, hakika kuliniumiza sana moyoni mwangu.

Baada ya miezi mitatu, kidogo nikaanza kusahau kuhusu Thomas, nikaendelea na maisha yangu na niliendelea kuroga kama kawaida. Ndugu yangu, kiukweli kwa kipindi hicho nilipenda sana kuroga, niliufurahia uchawi kuliko kitu chochote kile.

Maisha yaliendelea kusogea mbele, baada ya kipindi fulani, Mudi akanifuata na kunisisitizia kwamba bado alikuwa akinipenda mno. Sikutaka kukubaliana naye hata mara moja, nilimwambia ukweli kwamba kwa kipindi hicho sikutaka kuwa na mwanaume yeyote yule.

Mudi alikuwa king’ang’anizi, aliendelea kunisumbua lakini na mimi nikaweka msisitizo wangu kwamba haiwezekani kuwa naye. Mpaka tunafunga shule na kuingia kidato cha tatu, bado Mudi aliendelea kuniambia kwamba alikuwa akinipenda sana.

Niliendelea kumwambia kwamba sikutaka kuwa naye hata mara moja. Alilia sana lakini sikutaka kuwa na huruma hata mara moja, nilimwambia ukweli kwamba sikutaka kuwa na mwanaume yeyote yule.

“Mchawi huyo hapo,” nilimsikia mwanafunzi mmoja.
“Nani? Davina? Kumbe ndiye mchawi mwenyewe?” aliuliza mwanafunzi mwingine.
Kwanza nilishtuka, sikutegemea kusikia maneno kama hayo.

Nikageuka na kuwaangalia wasichana hao, walikuwa wamekaa chini na msichana ambaye alisema kwamba mimi nilikuwa mchawi alikuwa Agape, yule msichana aliyekuwa akimtaka Thomas.

Nilikasirika mno, sikuweza kuvumilia, kweli nilikuwa mchawi lakini sikutaka mtu aniambie kwamba mimi ni mchawi hivyo nikaanza kumfuata. Alijua kwamba namfuata yeye, alichokifanya ni kusimama kibabe na kuanza kuniangalia.

Itaendelea wiki ijayo.

 
Hadithi ya kusisimua: Jini Mauti-16

ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:

Nilikasirika mno, sikuweza kuvumilia, kweli nilikuwa mchawi lakini sikutaka mtu aniambie kwamba mimi ni mchawi hivyo nikaanza kumfuata. Alijua kwamba namfuata yeye, alichokifanya ni kusimama kibabe na kuanza kuniangalia…

“Agape sipendi ugomvi na yeyote yule, nani mchawi?” nilimuuliza, nilionekana kuwa na hasira mno.
“Wewe hapo,” alinijibu kijeuri.

“Una uhakika mimi mchawi? Umewahi kuniona nikikuroga?” nilimuuliza.
“Kwani nani asiyejua kwamba wewe mchawi? Hebu acha kuwaroga watu, mtoto mdogo unakuwa mchawi,” aliniambia Agape.

Nilikasirika sana lakini sikuwa na jinsi, nilichokifanya ni kugeuka nyuma na kuanza kuondoka mahali hapo huku nikilia. Moyoni niliumia mno, ni kweli nilikuwa mchawi lakini hakutakiwa mtu yeyote kuniita mimi mchawi.

Nikawa na hasira na Agape, sikutaka kumpenda hata mara moja, kila nilipomuona, moyo wangu uliwaka kwa hasira. Nilirudi nyumbani huku nikiwa kwenye hali ya hasira, hata kula sikula vizuri, nilichokifanya ni kwenda kulala.

Usiku niliamshwa na bibi, alikuja kunichukua kama kawaida yake. Nikajiandaa, nikachukua ungo wangu kisha kuondoka chumbani humo. Tulipofika kwenye uwanja wa kukutania, tayari siku hiyo kuliwekwa kiti kikubwa ambacho bibi alinitaka niende kukikalia, yaani ningeanza kazi kama malkia wa wachawi.

Nilipokikalia kiti kile, nikaanza kusikia nguvu za ajabu mwilini mwangu, kiti kile kilinipa nguvu ambazo sikuwahi kuzipata hapo kabla. Watu wote wakainamisha vichwa vyao chini kama kunipa heshima.

Kwa kuwa nilifahamu ratiba nzima, nikaanza kuwapa ratiba nzima juu ya mahali wapotakiwa kwenda kufanya kazi kwa usiku wa siku hiyo. Baada ya kuwaambia, wakaondoka na kwenda kwenye majukumu yao huku nikibaki peke yangu ambapo nilipanda kwenye ungo na kuanza kuelekea katika nyumba aliyokuwa akiishi Agape.

Sikuchukua muda mrefu, nikafika katika nyumba hiyo isiyokuwa na kinga yoyote ile, nikaanza kuelekea ndani mpaka katika chumba alichokuwa akilala. Nikaingia ndani kupitia pembe ya nyumba ile huku nikiwa mtupu kabisa.

Nilimuona Agape akiwa kitandani, alikuwa kwenye usingizi mzito, nilichokifanya ni kumfuata kisha kumuinua, nikamuweka kwenye ungo na kuondoka naye.

Sehemu ya kwanza kabisa kwenda naye ilikuwa Morogoro, kule kulikuwa na shamba kubwa la mchawi mwenzetu kikongwe, shamba la hekari kumi ambapo kila siku watu walikuwa wakichukuliwa kisha kulimishwa huko.

Nilipomfikisha Agape, kitu cha kwanza kabisa akapewa jembe hivyo kuanza kazi ya kulima shambani hapo huku akiwa na wenzake. Agape aliniona lakini hakunifahamu kabisa, alilima kwa takriban saa moja, tena kwa umbali mkubwa, alipomaliza, nikamchukua na kumrudisha nyumbani kwao.

Asubuhi nilipofika shuleni nilitaka kusikia kuhusu Agape, alikuwa akijisikiaje. Taarifa ambazo zilisambaa kwa rafiki zake wa darasa lake ni kwamba asingeweza kufika shule kwani alihisi viungo vyote kuuma huku akihisi kama kutaka kuumwa.
“Na ndiyo akome sasa,” nilijisemea.

Mudi, yule mvulana aliyekuwa akinitaka hakukata tamaa, kila siku ilikuwa ni lazima kuniambia kwamba alikuwa akinipenda sana na kutaka kuwa mpenzi wake. Sikumpenda lakini kutokana na ung’ang’anizi wake, nikajikuta nikianza kuvutiwa na mvulana huyo.

Maneno yake matamu, ahadi zake za kuvutia ikiwepo ya kunitunza na kunijali, nikajikuta nikiingia mikononi mwake. Kwa kipindi hicho sikukumbuka chochote kuhusu Thomas, nilimsahau kabisa.

“Nataka tukutane usiku,” aliniambia Mudi.
“Wapi?”
“Utaweza kuja kwenye ile Baa ya Mawele?”
“Ipi? Ile ya Sinza?”
“Ndiyo!”

“Mmmh!”
“Nini tena?”
“Wanafunzi na baa wapi na wapi?”

Itaendelea wiki ijayo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom