Dr kisanji maskini

AHAKU

Member
Jan 28, 2010
26
1
Nimei down load kutoka mtandao wa gazeti la Mwananchi

Tanzia:Kapumzike Dk Kisanji waliokujua watakuenzi
Na Abeid Poyo
HAKUNA awezaye kukizuia kifo pindi kinapomtembelea mwanadamu. Laiti uwezo huo ungekuwapo, wadau wa elimu nchini wangekuwa wa mwanzo kukizuia kifo kisimchukue marehemu Dk Joseph Kisanji aliyefariki hivi karibuni.

Kwa wale wadau wa elimu, taja Mtandao wa Elimu Tanzania (TenMet), jina la Kisanji (65) halitokosekana katika orodha ya watu walioupa uhai na hata kuupandisha chati mtandao huo kwa kiwango kikubwa.

Amekufa akiwa mratibu wa Ten Met, asasi ya kiraia iliyo mstari wa mbele katika harakati za kuhakikisha fursa za elimu bora ya msingi kwa kuhakikisha kuwa watoto wote wa Kitanzania wanapata fursa ya kupata elimu ya msingi iliyo bora.

TenMet pamoja na shughuli zake nyingi inasifiwa kwa kuwa kinara wa kuandaa machapisho, mikutano na mijadala ya kitaifa ya elimu ya kila mwezi inayowaleta pamoja wadau mbalimbali wa elimu.

Wanaomjua wanakiri alikuwa na mchango na ubunifu mkubwa katika harakati za kukuza sekta ya elimu. Hakika kuondoka kwake ni pigo kwa wadau na wanaharakati wa elimu nchini.

"Tanzania imepoteza kifaa cha elimu, imempoteza mtu muhimu katika sekta ya elimu. Alikuwa na utashi wa kuona Tanzania ikikua kielimu, kiuchumi na kijamii," ni maneno ya Florence Katabazi, Afisa Uchechemuaji wa sera za elimu nchini, mmoja wa watu aliofanya nao kazi kwa karibu wakati wa uhai wake.

Shirika maarufu la kielimu Tanzania HakiElimu kwa kutambua mchango wa Kisanji katika kukuza sekta ya elimu nchini, halikuchelewa kumpamba siku chache tu baada ya kifo chake. Kupitia taarifa ya tanzia iliyoitoa katika vyombo vya habari, shirika hilo lilisema:

"Atakumbukwa kwa nia thabiti na jitihada zake nyingi katika kuboresha elimu hapa Tanzania. Mchango wake wenye manufaa umekwenda zaidi ya Tanzania hasa kwa jinsi alivyotetea utu na ubinadamu kwa jumla."

Kitaaluma Dk Kisanji alikuwa msomi bobezi wa taaluma ya elimu hususan elimu maalum iliyomtambulisha katika dunia ya wasomi wa fani hiyo.

Kwa historia hiyo ya elimu, halikuwa jambo la ajabu kwake kutoa machapisho kadhaa ya kielimu yaliyokuwa yakiwazungumzia watu kutoka makundi mbali mbali ya ulemavu.
Moja ya machapisho haya ni pamoja na Attitudes and Beliefs about Disability in Tanzania.

Kwa waliobahatika kukaa naye japo kwa kupiga soga wanajua utamu wa kumsikiliza pale anapoyadadavua makundi ya walemavu na hata majina wanayostahiki kuitwa.

Kisanji hakuwa mtetezi wa watu wenye ulemavu pekee, kama ulivyo wajibu wa asasi aliyokuwa akiiongoza, yeye na wadau wengine walikuwa mstari wa mbele kushajiisha serikali kutoa haki na usawa katika upatikanaji wa elimu kwa makundi yote ya kijamii.

Akizungumza na gazeti hili siku za nyuma, aliwahi kunukuliwa akiwapigia chapuo watoto wa jamii za wafugaji, alisema:

"Bado hakuna mafanikio yoyote katika kuzisaidia jamii za wafugaji kupata elimu iliyo bora, wengi bado hawaendi shule na hii inatokana zaidi na desturi yao ya kuhama hama kwa ajili ya kutafuta malisho ya mifugo yao."

Aliongeza kuwa asilimia kati ya 60 hadi 70 ya watoto wa jamii za wafugaji wataendelea kushindwa kwenda shule iwapo hakutakuwa na mikakati maalum ya kuwajengea watoto shule za bweni ili kuwazuia kuhama mara kwa mara wakiwafuata wazazi wao ambao huhama kutafuta malisho ya mifugo.

"Suala muhimu hapa ni kuwajengea watoto shule za bweni katika maeneo hayo, hii itawafanya waweze kubaki shule wakati wazazi wao wakihama na mifugo.

“Pia suala la kuhamasisha wazazi katika jamii hizo linahitaji kupewa kipaumbele cha hali ya juu kwa sasa, wanatakiwa wabadilike kimawazo na mitazamo," alisema Kisanji.

Kwa mtazamo wake mtalaa uliopo sasa hauruhusu makundi fulani ya kijamii kushiriki katika elimu huku yakiendelea na mfumo wao wa maisha na tamaduni zao, suala ambalo linatakiwa liangaliwe kwa kina.

Mchango wa marehemu Kisanji ulikwenda mbali zaidi ya kuitumikia TenMet na wadau wengine wa elimu. Kwa mfano, yeye ndiye kinara na mwanzilishi wa kituo maarufu cha elimu kwa mtandao maarufu kwa Kiingereza kama Tanzania Global Develeopment Learning Centre chenye makazi yake katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha cha IFM jijini Dar es Salaam.

Pamoja na kuishi kwa zaidi ya robo karne nchini Uingereza akifanya kazi na kufundisha katika vyuo vikuu kama vile Chuo Kikuu cha Manchester, Kisanji hakuwa mwathirika wa uzungu, alikuwa mtu rahisi aliyejichanganya na kila mtu, tabia iliyo ngeni kwa baadhi ya wasomi nchini.

Hata hivyo, Katabazi anasema urahisi huo haukufanya kuwa mtu mwepesi kusukumwa hasa na watu wasioitakia mema Tanzania, watu waliokuwa wakiendekeza matumbo yao badala ya maendeleo ya walio wengi.

"Alikuwa mwafrika halisi na mzalendo, alikuwa akikwaruzana na watu wasiopenda maendeleo, watu waliotaka kujaza matumbo yao,"anaongeza Katabazi

Kwa wakubwa serikalini si ajabu kwao kutoufahamu mchango wake na ndio maana hatukuwasikia japo wakitoa salamu za rambirambi kuhusu marehemu Kisanji.

Inawezekana hakuwa maarufu au kwa kuwa hakuwa msomi aliyejipendekeza kwa vizito. Hata hivyo kwa wanaoufahamu mchango wake na hata kuujali kama vile wadau wa elimu na wapenda maendeleo kwa ujumla, kifo chake kimeacha pengo kubwa.

Ameshiriki na kutoa mchango katika mikusanyiko mingi ya kitaaluma. Baadhi ya machapisho aliyowahi kuyatoa ni pamoja na Special Education in Africa, Interface between Culture and Disability in the Tanzanian Context na EFA by 2015: A tantalizing prospect for Tanzania.

Kazi nyingine ni Historical and Theoretical basis of Inclusive Education, Historical Perspectives on Attitudes Towards Disability, Folklore Based Analysis for a Culture –Speific Concept of Inclusive.

Dk Kisanji, baba wa watoto tisa alifariki Machi 4 mwaka huu jijini Dar es Salaam na kuzikwa mkoani Mbeya.
 
R.I.P Dr. , harakati alizoanzisha tuziendeleze. Wanasiasa hawatakuimba kama si m1 wao ama muumini wao.
 
Back
Top Bottom