CUF yairarua CHADEMA

Paparazi Muwazi

JF-Expert Member
Dec 23, 2007
310
79
Yasema ni wababaishaji wasio na agenda
:: Yawahusisha Zitto, Kiwelu na watuhumiwa EPA
:: Wao wakiri kuwa na undugu na wanaotuhumiwa
:: Mbatia naye awataja kuwa ni waongo wa hoja

Benedict Sichalwe na Eliya Mbonea

CHAMA Cha Wananchi (CUF) kimewatuhumu viongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa ni mafisadi, wanafiki na waongo na hivyo hawawezi kuaminiwa na Watanzania kuongoza mageuzi ya kisiasa nchini.

Chama hicho kimeibua tuhuma hizo nzito kufuatia kauli za viongozi wa Chadema wa kitaifa na taarifa iliyotolewa na viongozi wa Chadema wa Mkoa wa Tanga kukituhumu CUF kwamba kinashirikiana na CCM kudhoofisha upinzani wa kweli.

Akizungumza na Rai katika mahojiano maalumu, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa wa CUF, Ismail Jussa, alisema Watanzania hawana haja ya kuelezwa ni chama kipi na viongozi wapi wamekuwa mstari wa mbele kupambana kufa kupona kuleta mabadiliko ya kisiasa Tanzania na wapi ni wanafiki.

“Viongozi takribani wote wa CUF tumeonja sulubu za CCM na serikali zake katika kupigani mabadiliko. Mwenyekiti Prof. Ibrahim Lipumba, Makamu Mwenyekiti Machano Khamis, Katibu Mkuu Seif Sharif Hamad, Manaibu Katibu Mkuu, Juma Duni na Wilfred Lwakatare, Kiongozi wa Upinzani Bungeni Hamad Rashid na wajumbe wengi wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa wa CUF wamekwenda jela na hata kuchezea vipigo vya vyombo vya dola kuleta mageuzi hapa nchini. Ni kiongozi gani wa Chadema aliyejitoa muhanga kama huu kwa ajili ya Watanzania,” aliuliza Jussa.

Aliongeza kwamba ni muhanga wa wanachama wa CUF wa Januari 26 na 27, 2001 uliofungua mlango wa mageuzi ya msingi ya kidemokrasia hapa nchini na kuhoji tena ni kipi cha maana kimefanywa na CHADEMA hata leo wawe na uthubutu wa kuisema CUF ni kibaraka wa CCM.

Jussa alisema ili kuongoza mageuzi ya aina yoyote yale, ni lazima wale walio mstari wa mbele kuyapigania wawakilishe taswira ya mageuzi hayo na waonekane kuwa ni tofauti na wale wanaowapinga.

“Mahatma Gandhi, mmoja kati ya viongozi ninaowaheshimu sana ulimwenguni alisema “Be the change you want to see” (Onyesha mabadiliko unayoyataka katika nafsi yako kwanza). Sasa ni vipi mafisadi wa CHADEMA wanaweza kupambana na mafisadi wa CCM?”, alihoji Jussa.

Akitoa ushahidi wa madai yake, aliwataka viongozi wa Chadema kuwaeleza Watanzania wana ushirikiano gani na watuhumiwa wa ufisadi wa EPA hadi kwenda kuwachukulia dhamana mahakamani huku wakiwadanganya wananchi kwamba wao wanapambana na ufisadi.

“Viongozi wa ngazi ya juu wa Chadema, Grace Kiwelu na Anthony Komu ni miongoni mwa waliowachukulia dhamana watuhumiwa wa EPA. Kabwe Zitto aliripotiwa na gazeti moja kuwa alikwenda Mahakama ya Kisutu na kunong’ona na Katibu wa Fedha na Uchumi wa CCM wa Mkoa wa Kigoma anayeitwa Maranda ambaye ni mshtakiwa pia. Alizungumza naye hadi alipopewa onyo na Hakimu na kulazimika kutoka nje. Wana siri gani hawa?” aliuliza Jussa.

Hata hivyo alipozungumza gazeti hili juu ya tuhuma hizo, Mbunge wa viti maalumu Grace Kiwelu alikiri kwenda mahakamani na kumchukua Ester Komu kwa madai kuwa ni ndugu.

“Ester Komu ni mtoto wa mjomba wangu, mahakamani nilikwenda kama ndugu. Hayo ni mambo mawili tofauti nawaomba CUF wasikihusishe chama changu na masuala ya undugu,” alisema Kiwelu na kuongeza:

“Kama wanataka wafanye uchunguzi wao ili wabaini kweli ni ndugu au siyo ndugu yangu. CUF hawana jipya zaidi ya kutapatapa baada ya kukataa kuwaunga mkono uchaguzi mdogo wa Mbeya vijijini,” alisema Kiwelu.

Pia Zitto Kabwe alipoulizwa kuhusu kuwepo Kisutu na kuzungumza na mtuhumiwa wa EPA alisema; yeye alienda kufatilia suala la wanafunzi wa vyuo vikuu waliokuwa wameshikwa kufuatia migomo ya wanafunzi. Akiwa pale alikutana na Maranda na kisha kuamua kumsalimia kwa kuwa ni mjomba wake.

Jussa alieleza pia kwamba viongozi wa juu wa Chadema wamekuwa wakijaribu kutumia rushwa kuwarubuni viongozi mashuhuri wa CUF kukihama chama hicho na kujiunga na chama chao.

Alitaja tukio mojawapo kwamba wakiwa safarini nchini Afrika Kusini mwaka jana, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alimfuata mjumbe wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la CUF kutoka Mkoa wa Mara, Mustafa Wandwi, na kumuuliza iwapo alishapokea salamu zake kutoka kwa Ofisa mmoja wa CHADEMA za kumtaka ajiunge na chama hicho pamoja na mzigo wa shilingi milioni moja.

“Wandwi alimjibu kwamba hakuwahi kupokea salamu wala fedha hizo. Mbowe alionekana kushangazwa. Hiyo maana yake ni kwamba fedha hizo zililiwa. Sasa hapo kuna ufisadi wa aina mbili, kwanza Mbowe kutaka kutumia rushwa kuwahonga viongozi wa CUF kukihama chama chao na pili Ofisa mwengine wa CHADEMA kuiba fedha aliyopewa kwa ajili ya kumpatia Wandwi. Hivi kweli watu wa aina hii wanataka watuaminishe kwamba wanaweza kupambana na ufisadi?” aliendelea kuhoji.

Jitihada za gazeti hili kumpata Mbowe ili afafanue kuhusu tuhuma hizi hazikuzaa matunda kufuatia yeye kuwa katika mikutano ya Oparesheni Sangara lakini akaahidi kuzungumza nasi siku nyingine.

Jussa pia aliyataja matukio mengine ya kurubuni wanachama wao, yanayofanywa na CHADEMA kuwa yamekuwa yakifanywa mikoani na wilayani, ambapo viongozi wa CUF kuitwa na wale wa CHADEMA wakiwemo baadhi ya wenyeviti na makatibu wa wilaya na madiwani na kuwapa ahadi za fedha ili wahame CUF na wajiunge na CHADEMA.

Alisema Makamu Mwenyekiti wa CUF alipofanya ziara ya Mikoa ya Mwanza na Tabora mwaka jana, viongozi wa CUF wa wilaya za Mwanza mjini na Urambo wakiwamo madiwani walimweleza kwamba viongozi wa ngazi ya taifa wa CHADEMA waliwaita katika vikao vya ndani na kuwataka wajiunge na chama hicho huku wakiwaahidi fedha.

Alipoulizwa iwapo haoni kuwa hilo ni jambo la kawaida kwa viongozi wa chama kimoja cha siasa kuwashawishi viongozi na wanachama wa chama kingine kujiunga nao ili kujiimarisha, alisema hana tatizo na hilo na anaukubali kuwa ni utaratibu wa kawaida katika demokrasia ya vyama vingi. Hata hivyo, alisema tatizo siyo kushawishi bali ni kuwarubuni kwa kutoa rushwa.

“Kuvutia wanachama ni jambo la kawaida lakini si kwa njia ya rushwa. Rushwa ni rushwa tu, na ufisadi ni ufisadi tu. Hauwezi kuwa haramu unapofanyika katika njia moja lakini ukawa halali ukifanywa kwa njia nyingine,” alisema Jussa.

Kwa upande mwingine, alisema hata kwa hilo la kushawishiana kwa njia za kawaida linaweza kukubalika inapokuwa kila chama kinafanya mambo yake kivyake. Lakini alisisitiza kuwa CUF, CHADEMA, NCCR na TLP waliingia makubaliano ya ushirikiano na hivyo kuwafuata viongozi wa chama kimojawapo kwenda chama kingine itakuwa ni usaliti wa kisiasa kwa wale unaoshirikiana nao.

Akitoa mfano wa hilo, Jussa alisema Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Kabwe Zitto, alimfuata Mbunge wa Chake Chake wa CUF, Fatma Maghimbi, na kumtaka aachane na CUF na kujiunga na CHADEMA.

Akizungumzia juu ya madai ya Jussa, mara baada ya kumpata Mwenyekiti wa CHADEMA Freeman Mbowe na kudai asingeweza kutolea ufafanua maswali hayo kulingana na eneo alilokuwa, Rai ilimtafuta Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe ambapo alitoa ufafanuzi wa madai hayo akisema siku zote chama chake kimekuwa kikifanya mikutano yenye lengo la kupata wanachama wapya na si wanachama wa kununua kama ilivyodaiwa na CUF.

“CHADEMA haina fedha za kununua watu inapata ruzuku Sh. milioni 60 kwa mwezi wakati CUF wanapata Sh. milioni 170 ukiangalia nani anaweza kuwa na fedha za kununua watu. CUF hawataki siku zote kuona vyama vingine vya siasa vikikua hususani CHADEMA, wamejigeuza wao wana hati miliki ya upinzani,” alisema Zitto

Akizungumzia suala la kutowaunga mkono Mbeya vijini Naibu Katibu Mkuu huyo alitanabaisha wazi kwamba tangu awali katika mazungumzo waliyoyafanya CUF hawakuonyesha ushirikiano

“Hawa CUF wanapolalamika eti tuwaunge mkono Mbeya vijijini kwa vile wanakubalika siyo kweli tukiwa kwenye Oparesheni Sangara tumefika kila mahali, kama ni chama kinachopaswa kulalamika kuungwa mkono ni TLP kwani kila tulipokuwa tukiingia tunakuta wapo,”alisema Zitto na kuongeza:

“Kama utakumbuka mwaka 2005 NCCR- Mageuzi waliiwekea CUF pingamizi Zanzibar kwa kitendo hicho CUF ilihamasisha wananchi wapige kura za maruhani. CHADEMA tumekataa kuwaunga mkono lakini hatujawaambia wananchi wapigie kura za maruhani wala kuwaambia wananchi wasipige kura,” alisema Zitto.

Akijibu madai ya kuzungumza na Fatma Magimbi, Zitto alisema ni kweli alizungumza na mama huyo Machi 2005 akiwa ametumwa na chama chake kwa lengo la kutafuta mwanamke kutoka Visiwani atakayeweza kusimama kwa nafasi ya mgombea mwenza wa chama chao.

“Si kuzungumza Magimbi pekee yake nilizungumza pia na Naila Jidawi na mwanamke mwingine ninayemkumba kwa jina moja la Ruaida. Lengo letu lilikuwa ni kutaka kuwa na makamu wa rais mwanamke kutoka Zanzibar. Tena wakati huo nilikuwa kijana mdogo sikuwa na wadhifa wowote ndani ya chama nilikuwa na miaka 28,” alisema Zitto.

Akifafanua zaidi juu ya suala la Mwananchi Gold Mining na Rais Mstaafu Benjamin Mkapa kuwatetea Zitto alisema mpaka sasa hajaona tuhuma zozote juu ya kampuni ya Mwananchi kujihusisha na ufisadi.

“Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati za Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, BoT, Kampuni ya Mwananchi gold mining, pamoja na wengine wote hawa wanaripoti kwenye kamati nimechunguza na kufuatulia kwa kina sijaona mahali wana tuhuma za ufisadi.

“Mpaka hivi sasa sijaona chochote cha kuishitaki Mwananchi Gold Mining sijaona chochote cha kushitaki juu ya Jaji Warioba hata kimoja. Nilikutana na BoT, NBC wakanielekezea kuhusu Mwananchi nimekaa na Jaji Warioba kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge mimi si mwanasiasa wa aina ya kwamba kwa vile nipo upinzani basi nipinge tuu, hapana ni mwanasiasa ninayetaka baadaye nije kuwa na heshima katika kuitumia nchi yangu kwa hiyo sitakiwi kumuonea wala kumpendelea mtu,” alisema Zitto.

“Hakuna rushwa kwenye Mwananchi Gold Mining ilikuwa na malengo mazuri kabisa kwa taifa hili. Ndani ya Mwananchi kuna matatizo madogo madogo ya kawaida tu ambayo ukiingia hata maeneo mengine utayakuta,”

Akielezea juu ya Mkapa alisema wapo watu wengi wametaka kiongozi huyo mstaafu aondolewe kinga ya kutoshitakiwa.

“Uzoefu unaonyesha si kila nchi zote duniani zilizowaondolea kinga marais wao wastaafu zilifanikiwa. Kwa jambo hili nasema tusiingie kichwakichwa kwa kumuondolea Mkapa kinga, lazima tujiulize je, kuna tija kwa upande wa taifa kuondoa kinga ya rais mstaafu?” alihoji Zitto na kuongeza:

“Lazima ukumbuke rais mstaafu alifanya mambo mengi sana kwa taifa sasa tunau hakika wa kile tunachokiamini. Nimuhimu tukaelewa kwamba Rais Mkapa si sawa na Mramba, Yona wala ‘Babu Seya’. Mkapa ni Rais mstaafu aliyetia saini mtu kunyongwa. Katika hili lazima tuwe na uhakika wa kile tunachotaka kukifanya kwa taifa letu kama kina tija yoyote,” alisema Zitto.

Hata hivyo Jussa aliendelea kukituhuma chama hicho kwa kusema kwamba kama mtu akitaka kujua CHADEMA hawana agenda ya kisiasa yenye malengo yanayoeleweka katika mapambano dhidi ya ufisadi bali wanawalaghai Watanzania tu, aangalie undumila kuwili katika suala hilo.

“Hebu angalia karibu vitendo vingi vya ufisadi vilivyoibuliwa vilifanywa wakati wa utawala wa Rais Benjamin Mkapa. Watanzania wanapodai kwa nguvu kuwa Rais mstaafu Mkapa aondoshewe kinga ya Kikatiba na baadaye aweze kushtakiwa, Zitto ananukuliwa na Nipashe akisema haungi mkono kumshtaki Mkapa kwa sababu hatua hiyo haitokuwa ufumbuzi wa matatizo ya ufisadi,” alibainisha.

Jussa anataja mfano mwingine wa undumila kuwili wa viongozi wa CHADEMA kuwa ni pale Zitto huyo huyo alipojitokeza hadharani kumtetea Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba, kwamba hahusiki na ufisadi wa Kampuni ya Mwananchi Gold na kwamba iwapo atakamatwa kwa tuhuma hizo, yeye (Zitto) yuko tayari kumtetea kwa njia zozote na hata kumchukulia dhamana.

“Huyu Zitto na wenzake wamekuwa siku zote wakitaka watuhumiwa wa rushwa wafikishwe mahakamani na kwamba Mahakama iachiwe kuamua hatima yao. Kwa kweli, kwa wengine wamefikia hata kuwahukumu kwenye majukwaa ya kisiasa kabla hata hawajafikishwa mahakamani. Kwa nini sasa inapokuja kwa Jaji Warioba hawataki kuiachia Mahakama ifanye kazi yake na wanajaribu kuiingilia hata kabla kesi hiyo haijafikishwa huko? Au wanataka kutuambia kuwa Mwananchi Gold ni safi?” alishangaa Jussa. Akizungumzia malumbano kati ya CUF na Chadema kuhusiana na uchaguzi mdogo wa kujaza kiti cha ubunge kilicho wazi cha Mbeya Vijijini, Jussa alisema hakutegemea kama Zitto angefikia hatua ya kusema uongo hadharani kwamba Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, hakuwahi kumuandikia barua Mbowe kumuomba chama chake kimuunge mkono mgombea wa CUF.

Jussa alitoa nakala ya barua ambayo Lipumba alimuandikia Mbowe pamoja na ushahidi wa kupokelewa barua hiyo Makao Makuu ya CHADEMA kwa njia ya dispatch book (kitabu cha kutia sahihi kuthibitisha kupokelewa barua).

Wakati huo huo; Mwenyekiti wa Chama cha NCCR Mageuzi, James Mbatia amesema hoja za kwamba chama chake ni kibaraka inatokana na umasikini wa mawazo ya wanasiasa wababaishaji ambao si wakweli.

Akizungumza kwa simu na RAI wiki hii, Mbatia alisema kwamba tatizo kubwa unaolikabili taifa la Tanzania kwa sasa ni umaskini mkubwa wa fikra na hoja walizonazo wanasiasa hasa wanaotumia uongo kama mtaji wa siasa.

Mbatia alisema; “Sifa ya kiongozi mwoga ni uongo. Watu hawasemi ukweli na hilo linatokana na tatizo kubwa linalolikabili taifa ambalo ni umasikini mkubwa wa fikra na mawazo ya wanasoasa wanaotumia uongo kuwadanganya Watanzania”.

Mwenyekiti huyo alisema wakati alitoa hoja yake kama maoni yake juu ya suala la kuwapo kwa Tume ya maridhiano kama njia muafaka ya kulinusuru taifa katika sakata la ufisadi, hoja hiyo imegeuzwa kwa kutaka kumfanya aonekane ni kibaraka wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

“Sasa tunapokuwa na hoja kama hizo zinazozuia watu kutoa maoni yao, nini manna ya haki ya kujieleza ambayo ni ya kikatiba kwa kila mtu kuwa nayo?” alihoji Mbatia.

Akizungumzia juu ya ushirikiano na vyama vingine vya kambi ya upinzani, Mbatia alikanusha kwa chama chake kuwa kibaraka dhidi ya vyama vingine hasa katika uchaguzi.

“Mwaka 2000 mgombea wa CUF (Chama cha Wananchi) alimwekea pingamizi mgombea wa NCCR na mwaka 2003 wagombea wa NCCR waliwawekea pingamizi wagombea wa CUF kule Pemba. Pamoja na hiyo kuwa haki za wagombea, lakini iligeuzwa na kupotoshwa kuwa mimi ndiye niliyeiwekea pingamizi CUF,” alisema Mbatia na kuongeza;

“Jambo la msingi ambalo Watanzania wanapaswa kuelewa ni kuwa wagombea wanapochuana katika nafasi za kuomba kura, haki ya kuwekeana pingamizi ni ya msingi kama utagundua udhaifu wa wagombea wenzako ili kupunguza kazi ya ushindi”.
 
MTAFUTANO KUWANIA MAJIMBO 2010

:: Wabunge waliopo madarakani wahaha kuwakwamisha vijana
:: Vijana wnaotaka kuwania waelezwa kusaka silaha ili kujilinda
:: Manumba: polisi imejizatiti kuwakabili wnasiasa wahalifu

Na Waandishi Wetu

SIKU chache baada ya gazeti hili kuandika kuhusu mapambano ya kuwania nafasi za ubunge katika uchaguzi mkuu unaofanyika mwakani, utafiti zaidi umebaini kuwa vyama mbalimbali vya siasa viko katika harakati za kuweka mikakati ya kuhakikisha vinafanikisha kupata viti vingi katika Bunge lijalo.

Baadhi ya mikakati hiyo ni ya wazi na mingine ni ya kificho na yote inalenga kuweka ramani nzuri ya vyama husika ikiwa ni maandalizi yanayolenga kuchukua serikali hasa kwa mwaka 2015. Inaelezwa upo ugumu kwa CCM kuvuka salama mwaka huo, kwa kuwa wanachama wa chama hicho kutoka Visiwani Zanzibar wameshaanza kutaka kuweka msimamo kuhusu kupewa nafasi ya kuwania urais baada ya Kikwete, ili kurejesha utamaduni uliozoeleka na chama hicho ambao ulikiukwa mwaka 2005.

Katika kuelekea katika uchaguzi wa mwaka 2010, CCM nayo imebaini umuhimu wa kuwatumia vijana, mbinu inayotumiwa na Chadema. Kuanzia juzi CCM kwa kushirikiana na UVCCM sambamba na Ikulu, inafanya semina ya vijana wake wapatao 80 Kisiwani Zanzibar. Duru za siasa zinaonyesha kuwa wengi katika vijana hao watatarajiwa kuwania nafasi za ubunge katika majimbo wanayotoka.

Mkakati huo wa CCM unalenga kupambana kwa uwazi kabisa na Chadema, chama ambacho katika siku za hivi karibuni kimekuwa kikipata vijana wengi. Inaelezwa kuwa, upo uwezekano wa wabunge mbalimbali kujikuta wanashindwa kama watakabiliana na wagombea vijana ambao wengi hawana uchafu wowote. Hali kama hii ndiyo inayoleta ushawishi wa kada wa CCM Kijana Nape Nnauye kuwania jimbo la Ubungo ili kukwaana na kijana mwenzake John Mnyika wa Chadema.

Mbunge wa sasa wa Jimbo la Ubungo Charles Keenja ambaye pia anaelezwa kubakia na nia ya kuwania jimbo hilo licha ya kushinda kwa tabu mwaka 2005, alipoulizwa kuhusu mkakati wa kuwatumia makada vijana jimboni kwake na kama hana nia ya kuwania tena nafasi hiyo alisema; “hili swali uliloniuliza (la kwamba anagombea) ni zito sana na lina gharama sawa na dola milioni moja.”

Chadema kinatumia vijana hasa kutoka katika vyuo vikuu na safari hii kinatumia oparesheni Sangara kupita katika majimbo ya vijana kinaotaka wagombee ikiwa ni hatua za kuwatangaza, huku pia mbinu nyingine ikiwa ni kufahamu nini kinahitajika katika majimbo hayo kabla ya uchaguzi huo.

Katika hali nyingine ipo hofu kwa wabunge waliopo, hofu inayotokana na joto la wanasiasa vijana wanaotaka kuwania ubunge. Tukio lililotokea Monduli kati ya Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole Sendeka kumpiga konde na kisha kumtishia bastola mwenyekiti wa UVCCM mkoa wa Arusha James Ole Millya linaelezwa kubainisha namna wabunge waliopo majimboni wanavyohaha kuhusu hatma ya nafasi zao katika uchaguzi ujao.

Yapo maeneo ambayo wagombea vijana wameshaanza kujiandaa na watakabiliana na matukio ambayo mara nyingi yamekuwa yakifanywa kimya kimya. Baadhi ya matukio hayo ni kutishana kwa silaha ambako kumekuwa kukifanywa kati ya wagombea kwa wagombea. Kutokana na hali hii, baadhi ya vijana ambao wana nia ya kuwania ubunge walioapata nafasi ya kuzungumza na gazeti hili, walieleza nia yao ya kutaka kumiliki silaha kabla ya uchaguzi mkuu ujao kwa sababu ya kujenga mazingira ya kujilinda dhidi ya wapinzani wao.

Kamishna wa Makosa ya Jinai nchini, Robert Manumba alipoulizwa kuhusu hali hii aliliambia Rai kwa njia ya simu kuwa, wao kama polisi wamejiandaa vema kukabiliana na kila mtu anayevunja sheria. Kwa mujibu wa Manumba, jeshi hilo halitamvumilia yeyote aliyepewa kibali cha kumiliki silaha kisha akaitumia kinyume cha taratibu.

Zipo pia taarifa kutoka katika kambi ya upinzani zinazoonyesha kuwepo mikakati ya baadhi ya wabunge kukimbia majimbo ili kuhamia majimbo ya mjini. Sababu ya kufanya hivi ni hofu inayotokana na kushindwa kufanikisha maendeleo waliyoahidi, huku kipindi kilichobaki ni kifupi. Wabunge wengi waliopo madarakani ambao gazeti hili lilifanikiwa kuzungumza nao, hawakutaka kuweka wazi kama watawania tena nafasi zao. Vile vile wagombea wapya wanaonyesha nia kwa mtindo wa kimya kimya kwa hofu ya kutotaka kutokea matukio kama yale ya Ole Sendeka na Ole Millya
 
Naona malengo ya CCM yanaanza kutimia, wameshawagombanisha wapinzani na sasa wanaanza kufarakana na hakuna anayefikiria tena suala la kushirikiana wakati uchaguziw a serikali za mitaa unakaribia. CCM wanajiandaa na mpaka utakapofika wakati wa uchaguzi wapinzani watakuwa wamemalizana wenyewe kwa wenyewe kiasi kwamba CCM itachukua viti kwa ulaini
 
Hili suala la CHADEMA kuwanunua wapinzani mbona si jambo jipya,wamewahi na wanaendelea kufanya hivyo.Mfano mzuri katika uchaguzi wa udiwani kati ya kati (Arusha)CHADEMA walimuonga mgombea udiwani wa TLP bwana Simba iliagombee kupitia Chadema.
 
Heeh. Kumbe CHADEMA wanamapesa mengi kuliko CCM. Hivi wanahonga au wanahama tu wenyewe toka vyama vingine vya upinzani? Hebu tupe undani wa hiyo habari ya Arusha kuhusu kilichotokea

Hivi CHADEMA waliwahonga pia Dr Slaa na Balozi Ngaiza watoke CCM kugombea kupitia CHADEMA ubunge!

Hivi kwanini watu wanatoka CUF, TLP na NCCR kwenda CHADEMA hawatoki CHADEMA kwenda kwenye vyama hivyo?


.....ndiyohiyo
 
DUh Haya madai ya Jussa mazito.....!!! ...Always CCM will be the winner....
 
MTAFUTANO KUWANIA MAJIMBO 2010

:: Wabunge waliopo madarakani wahaha kuwakwamisha vijana
:: Vijana wnaotaka kuwania waelezwa kusaka silaha ili kujilinda
:: Manumba: polisi imejizatiti kuwakabili wnasiasa wahalifu

Na Waandishi Wetu

Source: R*$T@& ^2!2 Int. (RAI)
 
Ushirikiano wa upinzani: Mimba changa inayotaka kuharibika

2008-09-13 09:24:33
Na Simon Mhina


Yale matumaini ya Watanzania ya kupata upinzani wenye nguvu kuliko huu walio nao hivi sasa, yanaonekana kufifia kutokana na dosari ndogo lakini kubwa zilizojitokeza baina ya vyama hivyo hivi karibuni.

Februari mwaka 2007, vyama vine vya upinzani vyenye wabunge CUF, TLP, Chadema na NCCR-Mageuzi, vilikubaliana kuwa na ushirikiano wa kisiasa.

Tofauti na siku zilizopita, ambapo walikuwa wanakubaliana kwa mdomo tu, safari hii wakaita vyombo vya habari wakatiliana saini, kwa maana kwamba makubaliano hayo yalikuwa na nguvu zaidi na hivyo kuwa na hadhi ya kuitwa mkataba.

Wenyeviti wa Taifa wa vyama hivyo, Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) , Augustine Mrema (TLP), Freeman Mbowe (CHADEMA) na James Mbatia (NCCR) kila mmoja kwa nyakati tofauti, alijaribu kuelezea faida za ushirikiano huo.

Wananchi wengi, akiwemo Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa walitoa taarifa za kupongeza ushirikiano huo, ambao ulikuwa katika nyanja za kisiasa.

Lakini kwa tafakuri ya kawaida, siasa ni jambo lenye mapana na marefu. Hata hivyo, kwa vile hatima ya siasa ni sanduku la kura, wananchi walijawa na furaha pale waliposikia viongozi wao wakitamba kwamba wakati wa Uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 20010 watasimamisha mgombea mmoja.

Dalili za ukweli juu ya jambo hilo zlichomoza mapema kwani siku chache baadaye palitokea chaguzi ndogo za ubunge kule Tunduru na baadaye Kiteto, ambapo vyama hivyo viliachiana nafasi.

Viongozi hao walienda mbali zaidi, kwamba kila jambo lenye hadhi ya kitaifa, walikuwa wakilitolea msimamo wa pamoja.

Lakini ghafla mambo yamegeuka. Umoja uliojengwa na kushamiri japo kwa kipindi kidogo kinachokaribia miaka miwili, unataka kubomoka kwa kipindi cha mwezi mmoja na nusu. tu.

Sio siri, kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe na uchaguzi mdogo wa marudio kujaza pengo lake, ndivyo vimeleta dosari hizo.

Sina sababu ya kurudia yaliyojiri katika msiba huo, lakini kwa kifupi ni kwamba safari hii, wapinzani ambao walikuwa wanatoa msimamo wao kwa pamoja, wakagawanyika. Vyama vitatu vikaonekana vimeweka mgomo baridi.

Vyama hivyo NCCR, TLP na CUF vikaitisha mkutano wa waandishi wa habari kuelezea kile Profesa Lipumba alichokiita ``sintofahamu`` zilizojitokeza kwenye msiba huo.

Katika kikao hicho nilimuuliza James Mbatia kuwa ``Tumezoea kuwaona viongozi wote wanne kwenye mikutano yenu, leo vipi Mbona Mbowe simuoni?``

Mbatia akajibu kwamba alipewa taarifa, lakini hakuhudhuria.

Siku ya pili nilikutana na Mbowe nikamuuliza habari hizo, akamkana Mbatia na kusisitiza kuwa hakualikwa.

Mpaka hapo bila shaka utagundua kuna tatizo. Na tatizo lenyewe linatokana na unafiki wa kisiasa.

Kwa vile inafahamika kuwa Tarime ni jimbo la upinzani, hivi sasa kila chama kinafanya jaribio la kuhakikisha chenyewe ndicho kinapata nafasi.

Japokuwa wenyewe wanajitetea kwamba muungano huo hauzuii kila chama kufanya shughuli zake, lakini dalili mbaya wakati wa kila chama kinafanya `shughuli zake` zimeanza kujionyesha.

Chadema na NCCR Mageuzi wamepigana juzi. Dk. Sengodo Mvungi alipigwa mawe wakati anahutubia.

Kabla ya kujadili hilo, lazima tujiulize kwanini hizo `shughuli` za kisiasa Tarime zinafanyika wakati huu?

Kwa nini ulipotamngaza uchaguzi wa Tunduru na baadaye Kiteto, mbona NCCR, TLP na CUF havikwenda kufanya hicho kinachoitwa `shughuli za kisiasa` katika maeneo hayo?

Jambo jingine la kujiuliza, kwanini NCCR wapigane na Chadema, kwanini NCCR wasipigane na TLP ambao nao wana mgombea? Katika makubaliano ya vyama hivyo, imeelezwa wazi kwamba lengo hasa la umoja huo, ni uchaguzi wa 2010, ili kuweka mgombea mmoja wa kiti cha urais.

Mrema wa TLP amesisitiza kwamba lazima wapinzani wataweka mgombea urais mmoja, binafsi ameapa kwamba hatogeuka.

James Mbatia naye ameniambia kwamba yaliyotokea Tarime ni mambo madogo, ambayo hayawezi kuzima dhana nzima ya ushirikiano wenye kuleta maslahi ya kitaifa.

Lakini kama watashindwa kuweka mgombea wa Ubunge mmoja kule Tarime kama ambavyo dalili zinajionyesha, wataweza kuweka mgombea urais mmoja?

Kama anavyosisitiza Mrema? Au hayo maslahi ya kitaifa anayosema Mbatia yanaanzia wapi na yanaishia wapi?

Lipumba yeye anaonekana kuunga mkono harakati za kisiasa kwa kila chama katika uchaguzi wa Tarime.

Juzi, Lipumba ameniambia hivi: ``Unajua ushirikiano ule haukumaanisha kuua madaraka ya kila chama, kila chama kinabaki na mamlaka yake kamili kwa mujibu wa sera zake na Katiba yake. Tulichokubaliano ni ushirikiano na wala sio muungano.``

Profesa Lipumba hakuishia hapo, akaongeza :``Unajua kila chama kikiendelea kujiimarisha, baadaye tukiweka mgombea mmoja pia tutapata nguvu kubwa zaidi zilizoimarika.``

Mrema naye akamuunga mkono akisema: ``Ni vema kila chama kikaendelea na taratibu za kutafuta mgombea kwa mujibu wa Katiba yake, alafu siku ya siku ndipo tutakaa na kuchuja katika wagombea wote, ni yupi anauzika.``

Maneo ya viongozi hawa maarufu kisiasa, yana mantiki, lakini hayana dalili za nia njema. Hivi kunaweza kutokea mgombea Tarime akauzika na kubwaga chama `kinachomiliki` Halmashauri?

Jibu linaweza kuwan ndio, kwa sababu hata Mrema aliwahi kuibwaga serikali nzima ya Benjamin Mkapa iliyohamia Temeke kumuwekea kigingi asichaguliwe ubunge mwaka 1996. Watu wakamchagua.

Lakini ni ukweli usiopingika kwamba watu wa aina ya Mrema sasa hivi hawapo, tutajidanganya tukiendelea kubahatisha.

Kama kweli wapinzani wana nia njema, kwanza kwa nini wanashindwa kukutana na kukaa meza moja?

Kwa nini hilo la ``kila chama kujiimarisha`` halisemwi wote wakiwa wamekaa meza moja? Badala yake kila mtu safari hii anasema kivyake.

Mbatia yeye amesema kinachotokea ni mgongano ya kimaslahi kwa kila chama.

Kwani wakati wanatia saini makubaliano, hawakujua kila chama kina maslahi? Hiyo migongano mbona haikutokea Kiteto?

Na mwaka 20010 hiyo migongano itakuwa imeenda likizo?

Mbowe kwa upande wake, yeye naona amepigwa na butwaa. Na Chadema yake nayo naona imeduwaa, sasa sijui `inatunga sheria` au inajihisi imeumbuka! Kilichomduwaza Mbowe (kamanda wa anga) huenda ni kushuka ardhini na kujikuta askari wake wa miguu wamelala.

Kifo cha Wangwe kilichotokea akiwa amesimamishwa uongozi ndani ya Chadema, kilitumiwa kama kombora la kumtungua kamanda wa anga.

Kombora hilo japokuwa limetengenezwa na `baruti feki za kuokoteza` lakini ni kombora! Linalipuka na kutoa moshi!

Lakini yote tisa, kinachofanya wapinzani wasikutano ni kitu gani hasa? Jibu ni kwamba ni kwa vile kila chama kina ajenda yake ya siri.

Alafu hawa jamaa wanashangaza, kwa vile hawasemi kwamba panapokuwa na haja ya kukutana, nani anawaita wenzake?

Kwa hili la sasa anayepaswa kulaumiwa ni Mbowe.Chama chake ndicho kilikuwa na Mbunge Tarime, amechukua hatua gani ya kuwaita wenzake na kuwauliza ``Mtaendelea kutuachia Tarime au mnataka tuweke mgombea wa chama kingine miongoni mwetu?``
Huku kuduwaa kwake kunaweza kutafsiriwa kuwa woga au kiburi.


Source: Nipashe
 
Ushirikiano wa vyama vya upinzani uvunjike kwa masilahi ya taifa

Samson Mwigamba

KICHWA cha makala yangu ya leo ni lazima kiwape shida wasomaji wangu, hasa wanaharakati wa mabadiliko.

Kwa wanaharakati wa mabadiliko kauli iliyobebwa na kichwa cha makala hii, lazima iwe ni kauli iliyotolewa na ama fisadi, mfuasi wa mafisadi au mnazi wa chama kilichopo madarakani asiyependa kuona chama hicho kiking’oka karibuni.

Hivyo itashangaza kuona leo ikitolewa na kalamu iliyojipambanua tangu mwanzo kuwa ipo kwenye harakati za kweli za kuikomboa nchi hii kutoka mikononi mwa chama dola kilichotekwa na mafia waitwao mafisadi kwa faida yao wenyewe, familia zao na wapambe wao.

Kwa kusoma kichwa cha makala hii huenda msomaji yule aliyenipigia simu wakati fulani, akionyesha hofu na mimi, akaona unabii wake unatimia.

Msomaji huyo katika ujumbe wake aliuliza: “Ni kweli umedhamiria kupigana hii vita na utaendelea na mapambano? Usije ukawa kama yule mhariri wenu wa zamani ambaye naye alianza hivi hivi akiwa shupavu kweli kweli katika vita hii dhidi ya utawala dhalimu wa chama dola.

Lakini, taratibu akadakwa na leo anawatumikia wale aliowaponda sana.”

Naomba kuwahakikishia wasomaji wangu akiwamo huyu aliyekuwa na wasiwasi kwamba kwa maandishi yangu, mafisadi wanaweza kunitafuta na hatimaye wakanivuta upande wao kwa njia yoyote ile, kwamba mimi ni mpambanaji.

Kutulia kwangu ni pale vita itakapomalizika, nchi ikatulia na Watanzania wote wakafaidi kile walichojaliwa na Mwenyezi Mungu.

Kama sivyo, basi pumzi ya uhai initoke na kuuacha huu mwili wa udongo ukirudi kuwa udongo, hapo nitatulia. Vinginevyo, nitaendelea kupigana vita.

Hata ningeacha kuandika leo kwa sababu yoyote ile au magazeti yote yangenunuliwa na mafisadi na kuanza kuwashabikia kama tunavyoona kwa baadhi ya magazeti makini ya zamani, nitaendeleza vita kwa njia nyingine.

Nimeamua kutumia makala nzima kueleza kwa kinagaubaga mawazo yangu kuhusu ushirikiano wa vyama vya upinzani ambao umepigiwa upatu sana na Watanzania kwa muda mrefu.

Waandishi kama Yusuph Halimoja, wametumia muda mwingi kuwaasa viongozi wa vyama vya upinzani kuungana ili Chama Cha Mapinduzi (CCM) king’oke.

Mwaka 2005 kulikuwa na shinikizo kubwa la wananchi kutaka vyama viungane na kufanya muungano kama ule wa NARC ya Kenya na hatimaye kuing’oa CCM madarakani.

Ukiachia mbali moto uliowashwa na mtandao wa Jakaya Kikwete, wa kuwaaminisha kwamba Kikwete alikuwa ni chaguo la Mungu, nadiriki kusema hata upinzani kutoungana na kusimamisha wagombea wengi kiasi kile, iliwakatisha tamaa Watanzania wengi na kuamua kukipigia Chama Cha Mapinduzi kura.

Huenda hata huo pia ulikuwa ni moja ya mikakati yao. Huenda, wanamtandao waliotoa pesa iliyotokana na ufisadi na kuwapandikiza wagombea wengi kiasi kile ili kuwapa ujumbe Watanzania kwamba viongozi wa vyama vya upinzani wana uchu wa madaraka ndiyo maana kila mmoja wao anataka kuwa rais.

Leo, napenda kuwaambia kwamba ni vema ushirikiano wa vyama vinne vya upinzani (CHADEMA, CUF, NCCR-MAGEUZI na TLP) ukavunjika kwa masilahi ya taifa.

Katika kueleza msimamo wangu, napenda kuwarejesha nyuma kwenye historia ya hivi karibuni iliyopigiwa upatu na Watanzania.

Hii ya wenzetu wa Kenya. Vyama vingi vilipoanzishwa kule havikufua dafu kwa KANU. Baada ya chaguzi mbili za vyama vingi, vyama vya upinzani vikaamua kuungana kwa mujibu wa sheria ya nchi yao na hatimaye profesa wa siasa akakabidhi urais wa nchi kwa mwakilishi aliyetokea upinzani, ndiyo ukawa mwisho wa chama dola.

Lakini nini kilitokea baadaye? Kukazuka mgogoro wa chama hiki kudai kupewa mawaziri wachache, kile kikidai kunyimwa wizara nyeti, hiki hapa kikidai makubaliano yamekiukwa na mambo kadha wa kadha mpaka wakagombana.

Walisambaratika na kumlazimisha rais aliyetokana na upinzani kuanzisha ushirikiano mpya na rais aliyeondoka madarakani na hivyo kufifisha vita dhidi ya ufisadi na kusababisha serikali iliyokuwa madarakani ionekana ya ufisadi sawa na ile serikali iliyopita. Huo ndiyo ushirikiano wa vyama vya upinzani unaotafutwa na Watanzania.

Nawatahadharisha Watanzania. Kwamba hatuhitaji ushirikiano wa vyama vya upinzani wenye lengo la kuing’oa CCM madarakani. Tunahitaji Tanzania mpya yenye kutoa fursa kwa kila raia kufaidi rasilimali za nchi hii na kujiletea maendeleo bila kujali katokea kundi gani.

Ushirikiano wa CHADEMA, CUF, NCCR na TLP hautafanikisha hayo. Mwaka huu serikali ina mpango wa kupeleka bungeni muswada wa sheria ya kuruhusu vyama kuungana.

Sina shaka ndani ya dhamira yangu kwamba wanafanya hivyo sasa baada ya kujiandaa kutumia muungano wowote wenye nguvu utakaoanzishwa ili kuvimaliza vyama vya upinzani.

Serikali ya CCM imepigiwa kelele muda mrefu lakini haikutaka sheria hiyo itungwe. Kinachowasukuma kufanya hivyo sasa wakati ambapo serikali yao iko katika wakati mgumu mbele ya wananchi kuliko kipindi chochote kile ni nini?

Ni kwa sababu tayari wana watu wao ndani ya CHADEMA, ndani ya CUF, ndani ya NCCR-Mageuzi na ndani ya TLP, ambao watawatumia kuvisambaratisha vyama hivi kwa urahisi sana.

Nawapa unabii mwingine ambao naamini utatimia. Kama vyama hivi vitaungana, hatimaye vikaamua kusimamisha mgombea mmoja wa urais na hata wa ubunge ama udiwani, basi karibu uchaguzi mkuu wa 2010 CCM itatumia watu wake ndani ya vyama hivyo.

Watavuruga huo ushirikiano na hatimaye vyama vitatengana katika hatua za mwisho mwisho na CCM kutumia nafasi hiyo kuwaeleza Watanzania kwamba, “Mmeona! vyama vya upinzani nia yao ni madaraka tu. Wanaanza kugombea madaraka kabla hawajachaguliwa, je, wakichaguliwa?”

Na sasa chukulia kwamba tayari vyama vyote vinne vimeshaungana na vimemteua mgombea mmoja kugombea urais.

Wakati mgombea huyo ameshapitishwa na tume ya uchaguzi, ndipo unaibuka mgogoro mkubwa na hatimaye muungano huo unavunjwa.

Kwa sababu muungano uliomsimamisha mgombea huyo umevunjwa, hana tena sifa ya kuwa mgombea urais. Tume ya uchaguzi inamfuta kutoka kwenye orodha ya wagombea. Nini kitatokea, kila msomaji anaweza kujibu hilo swali.

Dalili za unabii huu kutimia tayari zimeshaonekana. Baada tu ya kifo cha Chacha Zakayo Wangwe, aliyekuwa mbunge, kumetokea mparaganyiko mkubwa.

Vyama vinne vya upinzani vilivyo kwenye ushirikiano vimeparaganyika. Kwa mara ya kwanza CHADEMA wamelalamikia mwenyekiti wao kuandikiwa habari za uongo halafu CUF, NCCR na TLP wakatoa tamko la kuwapongeza wanahabari wale wale kuhusu kitu hicho hicho tena wakipingana hadharani na malalamiko ya CHADEMA.

Kwa mara ya kwanza vyama vya CUF, NCCR na TLP wamealikana kutoa tamko la pamoja halafu wakawapa CHADEMA taarifa kwamba watakutana na waandishi wa habari na kwamba kwa vile CHADEMA ndiyo wafiwa, basi watawakilishwa na vyama hivyo vitatu.

Lakini, makubaliano yaliyosainiwa na vyama hivyo vinne vya upinzani yanasemaje? “Kwamba viongozi wakuu wa vyama vyetu watatoa maazimio na matamko ya pamoja kuhusu masuala mbalimbali ya kitaifa na kimataifa pale itakapohitajika”.

Hakuna kipengele cha kwamba katika baadhi ya mambo chama kitawakilishwa na vyama vingine. Na kama waliona mwenyekiti mwenzao atakuwa katika majonzi, mbona mara nyingi tumeona Freeman Mbowe akiwakilishwa na kiongozi mwingine wa kitaifa wa CHADEMA kwenye matamko ya huko nyuma?

Mbona tumeona mara nyingi James Mbatia akiwakilishwa na kiongozi mwingine wa kitaifa wa NCCR katika matamko ya huko nyuma? Katika hili kulikuwa na agenda gani?

Kitu hicho kinajidhihirisha zaidi katika mwenendo mzima ulioendelea baada ya hapo. Tukapata taarifa za viongozi wa vyama vingine kuwa mstari wa mbele kumshambulia mwenyekiti wa taifa wa CHADEMA kwamba kahusika na kifo cha Wangwe kiasi cha kumwandikia Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) amchunguze.

Tangu hapo naomba kama kuna mtu aliwahi kusikia kwamba viongozi vya vyama vinne vya upinzani vilivyo kwenye ushirikiano wamekutana na kuzungumza na hatimaye kutoa tamko la pamoja kwenye vyombo vya habari anisaidie. Tulichoshuhudia ni kila chama kinatafuta kuweka mgombea wake kule Tarime.

Katika kufuatilia kwamba kuna nini na kwa nini vile vitatu vinaonekana kuwa pamoja bado, ila vinaonekana kujitenga na CHADEMA, ndipo nikaambiwa kwamba vyama vingine vinalalamika kuchukuliwa wanachama wao na CHADEMA.

Wanaona kama ushirikiano unaijenga zaidi CHADEMA kuliko vyama vyao. Na hata wanadhani CHADEMA, inafanya kuwashawishi wanachama wao kuhamia kwao. Hoja mufilisi!

Huwezi kuwazuia watu kufuata sera za chama kingine. Kama CHADEMA, wameanza kuwanunua wanachama kwa fedha kama Chama cha Mafisadi, tuambieni.

Lakini, kama watu wanavutwa wenyewe na sera na mwenendo wa CHADEMA, hiyo ni hoja mufilisi. Inaonyesha kabisa kwamba hawa wakiungana na kuing’oa CCM tutashuhudia ya NARC.

Nawashauri Watanzania tuwaruhusu wapinzani wavunje ushirikiano wao halafu wajijenge kama chama kimoja kimoja na ndipo tutakapoona chama chenye mwelekeo wa kuleta maendeleo tukipe kura.

Hata Marekani, kwao demokrasia ya vyama vingi, vyama tunavyovisikia havikupata nguvu kwa kuungana na vingine bali kwa kujijenga.

Democratic Party ilianzishwa mwaka 1792 na baadaye ikazinduliwa upya kama ilivyozinduliwa upya CHADEMA, mwaka 1828.

Republican Party ilianzishwa mwaka 1854 na inaendelea hadi leo, Libertarian Party (1971), Constitution Party (1992) na Green Party (1996).

Hivyo ni vyama vilivyosimamisha wagombea kwenye uchaguzi wa rais. Lakini kuna vyama vingine 17 vilivyosimamisha wagombea katika chaguzi za hivi karibuni, vyama vingine 29 ambavyo havijasimamisha wagombea kwenye chaguzi za hivi karibuni, vyama vya majimbo 32 ambavyo vimesimamisha wagombea kwenye chaguzi za hivi karibuni na vyama 61 ambavyo ni kama vimekufa.

Hatuwezi kulazimisha vyama vya upinzani viungane ili tu kuing’oa CCM madarakani halafu baada ya hapo nchi ipate shida kubwa zaidi kama ilivyotokea Kenya.

Kibaki na Raila waliungana kwa lengo la kuing’oa tu KANU na baadaye wakaanza kugombania madaraka wao kwa wao kiasi cha hatimaye mwaka jana kusababisha mauaji makubwa.

Muungano wa namna hiyo hatuuhitaji Tanzania. Na hatuwezi kulazimisha kupunguza idadi ya vyama. Vitapungua vyenyewe kama tunavyoona Marekani kwamba 61 vimekufa vyenyewe, 32 vya majimbo na 17 vya kitaifa bado vipo vipo lakini havina nguvu hata ya kusimamisha wagombea urais wakati 29 hata kusimamisha wagombea kwenye chaguzi mbalimbali imekuwa shida na kati ya vitano vilivyosimamisha wagombea urais ni viwili ndivyo vinavyosikika.

Natamani chama kama CHADEMA, ambacho kimejipambanua hivi karibuni kuwa chama makini chenye sera nzuri zilizopata kusifiwa hata na Mwalimu Nyerere wakati wa uhai wake na ambacho hivi karibuni kimewaonyesha Watanzania kwamba kumbe inawezekana kuiondoa CCM na tukaongozwa na chama kingine na kujipatia maendeleo ambayo hatukuwahi kuyaota wakati wote wa CCM, kipate ukubali kutoka kwa Watanzania.

Wakipokee kama kilivyopokelewa Tarime na kufanya mabadiliko makubwa. Chama kipewe nafasi ya kujipanua na mwaka 2010 kuwe na uchaguzi wenye ushindani kama tunaoushuhudia Tarime.

Vyama vingine viendelee kusimamisha wagombea urais, ubunge na udiwani kwa kuwa ni haki yao lakini mchuano uwe kati ya vyama viwili kama tunavyoona kule Tarime na hapo ndipo tutakuwa tunaelekea huko kwenye maendeleo.

Kwamba hakuna chama hadi sasa kinachoweza kutamba kuwa kimeshinda Tarime hadi mwisho wa dakika 90, vivyo hivyo kwenye urais, ubunge na udiwani mwaka 2010 kusiwe na chama kitakachokuwa na uhakika wa ushindi. Tukifikia hapo, tutakuwa ‘tumewini’.

Na kitakachoshinda kiwe na nafasi pana ya kutekeleza sera zake kilizokuwa kinazitangaza ili kudhihirisha kwa Watanzania kwamba ni chama bora huku kikitambua kwamba kosa moja, uchaguzi unaofuata kinapigwa chini.

Sitaki vyama viungane halafu vifanikiwe kuing’oa CCM na baadaye vitumie muda mwingi kugombea vyeo au kugombea sera ya chama gani itekelezwe na serikali. Natamani kila chama kijijenge kama vile vya Marekani na kitakachoshindwa kujijenga kijifie chenyewe.

Kila la heri wana Tarime kwa kuonyesha mfano wa kuigwa na taifa zima. Juma lijalo tutasemezana kidogo baada ya matokeo ya uchaguzi.

Bila kujali ni chama gani kitashinda tutakuwa na machache ya kuongea tukipongezana, kupeana pole, kukosoana na kadhalika.

Nawatakia uchaguzi wa amani na utulivu lakini pia nawatakia ujasiri wa kuchagua mnayemtaka na kulinda kura zenu asipewe msiyemtaka.

Aluta continua! Kalamu itasema ukweli daima, unafiki kwake mwiko!

Chanzo:Tanzania Daima
 
Wapinzani onyesheni uongozi Tarime

Lula wa Ndali-Mwananzela Septemba 17, 2008




UONGOZI mzuri hauonekani wakati watu wanashangilia, wakati watu wanakubeba juu juu au kuimbiwa nyimbo za sifa.

Uongozi mzuri hauonekani wakati wa kampeni za uchaguzi ambapo maelfu ya watu wakiwa na bendera za chama chako wakiandamana kufuata msururu wa magari ya kampeni. Kwa hakika uongozi hauonekani wakati wa ushindi au hata dalili za ushindi. Uongozi mzuri huonekana wakati wa dharura, vurugu, migogoro au wakati mambo kwa namna moja au nyingine, yanakwenda kombo.

Uongozi mzuri hauonekani kwa maneno mazuri, kauli kali, au hoja tupu. Uongozi hauonekani kwa mtu kutoa maneno ya kulaani, kupinga, kuhoji au hata kukebehi mambo mazito wakati wa mgogoro. Uongozi huonekana katika hatua zinazochukuliwa wakati mambo yanakwenda kombo. Maneno, kauli, hoja n.k zinakuwa na nguvu pale tu zinapoendana na hatua zilizo dhahiri na za makusudi zenye lengo la kutatua mgogoro au kukabiliana na tatizo lililopo.

Kwa wiki kadhaa sasa tangu Mbunge wa Tarime Chacha Zakayo Wangwe afariki dunia, vyama vya upinzani ambavyo tulividhania kuwa viko katika “ushirikiano” vimeonyesha rangi yao ya kweli. Ushirikiano waliokuwa nao ni wa kutafuta sifa, na umoja waliokuwa nao ni wa chuki dhidi ya adui mmoja. Ushirikiano wao haukujengwa katika kuheshimiana, kukubaliana, kusaidiana na hata katika kupanga mkakati wa kumshinda adui yao mmoja.

Kile ambacho tulidhania kuwa ni ushirikiano hakikuwa hicho, bali geresha ya kutuzuga kama vile ushirikiano tunaoona wa mafisadi ndani ya chama tawala. Ushirikiano wao ni ushirikiano kwa kadiri ya kwamba unakidhi malengo yao kama mtu mmoja mmoja au kama chama kimoja kimoja na si ushirikiano wenye kukidhi lengo lao moja kubwa.

Kwa maneno mengine, tulichoshuhudia tunaweza kukiita ni “ushirikiano wenye mashaka”. Kuna picha moja inayowaonesha wanyama wakiwa katika tafrija mwituni, wakila na kunywa na kucheza dansi. Wanyama hao ambao wengine kwa asili ni maadui kama simba na swala, mbuzi na chui, wote walikuwa wanafurahia tafrija hiyo na kwa nje mtu angeweza kusema kuwa “hatimaye mwituni amani, umoja, na mshikamano vinatawala”.

Lakini kwa kuangalia kwa karibu utaona kuwa uzuri na usalama wa tafrija hiyo upo tu pale ambapo kinacholiwa ni chakula kingine na kila mgeni ameshiba. Muda ambapo utafika na mmoja akaanza kusikia njaa na chakula kilichoandaliwa kimeisha ni wazi kuwa wale wenye nguvu wataanza kufikiria ni “kitoweo” gani kilichopo karibu.

Mfano wa hili unaonekana katika filamu ya vikatuni ya Madagascar iliyotoka mwaka 2005 ambamo wanyama waliokuwa kwenye zoo ya New York walijikuta wanarudishwa Afrika na kwa bahati mbaya kujikuta wanatupwa kwenye visiwa vya Madagascar.

Wanyama hao wakiwemo Alex (simba) na pundamilia aitwaye Marty walijikuta wanachanganyika na wanyama wengine wa mwituni ambao hawakuwahi kuwa kifungoni. Wale wanyama wa zoo hawakuwahi kuishi maisha ya mwituni na hasa Alex ambaye akiwa kwenye zoo alikuwa analetewa minofu ya nyama bila kuwahi kuwinda. Wakiwa kisiwani Madagascar wakifiria jinsi watakavyorudi kwao New York, Alex akawa ana hamu sana ya minofu ya nyama.

Siku moja njaa ikiwa inamuuma sana alimuangalia rafiki yake wa karibu Marty na kuanza kujiwazia jinsi gani angekuwa mtamu kama angemnyofoa kidogo. Katika njozi yake hiyo akajikuta anamuona Marty kama kipande cha paja la ng’ombe na kama mtu anayetembea akiwa usingizini akaanza kumfukuza Marty. Kilichooneshwa ni kuwa simba atakuwa simba hata ukimpa mafunzo na semina elekezi.

Njaa ilimdhihirisha kuwa simba ataendelea kuwa simba akibanwa na njaa. Tunachoshuhudia Tarime sasa hivi ni kudhihirishwa kuwa ushirikiano wa vyama vya Chadema, CUF, TLP na NCCR-Mageuzi msingi wake haukuwa wa kina kwani dhoruba ilipokuja (kifo cha Wangwe) kila mmoja ikabidi atafute njia yake ya kutokea.

Nasikitishwa na maneno yanayorushwa na Wapinzani ambao miezi michache iliyopita walikuwa wakisimama pamoja tena kwa umoja. Leo hii kuna dalili ya kupoteza jimbo na wengine kupata ruzuku basi imekuwa kila mtu na lwake.

Hiki kinathibitisha nilichosema hapo juu kuwa uongozi hauonekani wakati mambo yanakwenda vizuri. Wakati Zitto Kabwe alipofungiwa na wabunge wa CCM mwaka jana wengi wetu tuliguswa na umoja ulioonyeshwa na Wapinzani na hata kwenye uchaguzi mdogo wa Kiteto tuliweza kuwaona walivyoshirikiana. Lakini wakati ule mambo yalikwenda vizuri. Lakini sasa, ni balaa.



Freeman Mbowe
Freeman Mbowe ameshindwa kuonyesha uongozi unaotakiwa hasa baada ya yale yaliyokikumba chama chake na msiba uliotokea wa kumpoteza Wangwe. Ukimya wake tangu kifo cha Wangwe kwa hakika unapiga kelele. Hajajitokeza hata mara moja kutoa pole, kusema rambirambi au kuonyeshwa kwa namna fulani kuwa msiba ule umemgusa zaidi ya kujitokeza kuandamana na viongozi wenzake Tarime.

Wakati wa msiba ule uongozi wake ulihitajika zaidi kwa mashabiki na wapenzi wa chama hicho, lakini kwa yeye kukaa kimya kunaonyesha jambo moja tu kuwa tofauti yake na Wangwe haikuwa ya kisiasa au mtazamo wa mambo bali ilikuwa ni ya kibinafsi.

Na hata sasa wakati chama chake kinataka kikubaliwe kuongoza Jimbo la Tarime tena, wengine tunajiuliza kwa kustahili gani? Misiba hutokea duniani na mengine ina utata wa kila aina, lakini ukimya kwa mtu aliyekuwa karibu yako ni sababu tosha ya watu kuhoji mwelekeo wako wa uongozi. Wakati uongozi wake unahitajika Mbowe hakuonyesha uongozi huo.

Ni matumaini yangu kuwa licha ya kuwa ameangushwa chini na kugaragazwa atasimama na kuuleta uongozi unaohitajika kule Tarime na kwa Chadema. Vinginevyo asipoangalia atabakia kuwa yule kiongozi atakayetolewa methali. Haitoshi kuibukia Mwanza kuzungumzia mambo ya ufisadi na kuendeleza ukimya katika msiba mkubwa kabisa uliowahi kukikuta chama chake. Hili ni doa analohitaji kulipangusa vinginevyo likikauka halitoki.

Swali kubwa ambalo wapiga kura wa Tarime wanahitaji kupata jibu ni je, Chadema bado kinastahili kura yao? Je, Mbowe hatimaye atasimama mbele ya wana Tarime na kuzungumza nao na kwa upande wa Taifa kutoa kauli ya kiongozi au ndiyo ameamua kununa?

James Mbatia na Dk. Sengodo Mvungi. Kati ya vitu ambavyo vilidhihirisha jinsi gani urafiki wa wapinzani hawa ulikuwa ni wenye mashaka ni maneno yaliyokuwa yanatolewa na viongozi hawa wawili wa NCCR Mageuzi.

Ni rahisi kuona kuwa kati ya vyama ambavyo vingetamani kushinda Tarime ni chama hicho. Sababu kubwa ni kuwa katika uchaguzi uliopita wa 2005 NCCR haikufanikiwa kupata kiti hata kimoja.

Hivyo, wao kwa kiasi kikubwa wanatamani wapate kiti hicho kwa sababu moja kubwa nayo ni ruzuku ili waweze angalau kuwa na mahali pa kuanzia au kutokea. Lakini na wao hatuna budi kuhoji uwezo wao wa kuongoza kuwa badala ya kuona haja ya kushirikiana kupata ushindi kwa mgombea anayekubalika zaidi wao wakaanza kwenda na kurusha madongo kwa Chadema ili kukichafua chama hicho ili watu wa Tarime waanze kukubali mgombea wao.



Sengondo Mvungi
Ilipofikia mahali kuwa wanaosadikiwa kuwa ni wanachama wa Chadema walipowavurumusha kina Mvungi toka Tarime ni wazi kuwa kukubalika kwao au kwa hoja zao kuna shaka. Wakati huu viongozi hawa walitakiwa kuonyesha uongozi kwa kuweka maslahi ya Tarime mbele zaidi kuliko manufaa ya chama kujipatia mbunge. Kwa tamaa kama ya Alex wakaamua kuwaangalia marafiki zao na kuona “mnofu” mkubwa! Wakati walipotakiwa kuonyesha uongozi wao wanaleta mapozi ya kisiasa.

Augustine Mrema na TLP. Kiongozi mwingine ambaye bila ya shaka wananchi hawana budi kumshangaa ni Mrema ambaye naye kwa kuona kuwa chama chake kinahitaji angalau mbunge mmoja baada ya yule waliyekuwa naye kuvuliwa ubunge na Mahakama. Katika kufikia lengo hilo yeye kama kina Mbatia na Mvungi akaamua kwenda nje ya ule ushirikiano na kutaka kusimamisha mgombea wa chama chake huko Tarime.

Kwanini? Bila ya shaka sababu yake haina tofauti kubwa sana na ile ya hao wenzake hapo juu. Wote wanataka kutumia nafasi hii ya machozi ili wao wajinufaishe. Njia pekee ni ya kuonyesha kuwa Chadema hakistahili kupewa uongozi wa Tarime tena na hivyo chama kingine. Badala ya kumeza viburi vyao na kuamua kusimamisha mgombea mmoja viongozi hawa wakati huu wa zahma wamejikuta wakiweka sifa, majina na ujiko wao mbele zaidi kuliko maslahi ya Tarime au ya Upinzani mzima. Wakati walipotakiwa kuongoza wao wameamua kujiuza!

Profesa Ibrahim Lipumba na CUF. Hapa kuna kitu cha kushangaza nacho kinahitimisha mtazamo wangu wa uzugaji wa ushirika wa ulaghai ambao tuliushuhudia. Mara nyingi nimekuwa nikiamini kuwa kama kuna chama ambacho kinaweza kwa kweli hatimaye kushika madaraka ya Tanzania ni CUF. Lakini hilo litatokea endapo tu kitaweza kupenya Tanzania Bara na kukubalika.

Hilo lingewezekana kabisa endapo chama hicho kingeweza kuingia katika ushirikiano na chama cha Bara cha Upinzani ambacho kina nguvu nacho ni Chadema. Vyama hivi viwili vingeweza kufanya TANU na ASP ya upinzani. Vyama hivi viwili vingeweza kukubali kufa na kujiunga pamoja na kutengeneza ngome mpya ya upinzani nchini.

Cha kushangaza CUF ndio kwanza wameanza kuamka siku hizi na kuanza kujikita taratibu Bara. Kwenye sakata la Tarime nilishangazwa wao nao walipojikuta wanachukua ushirika wa TLP na NCCR na hivyo kutengeneza Pembetatu ya Maslahi. Wao kama TLP na NCCR wameamini kuwa wangeweza kusimamisha mgombea wao au kuunga mkono ushirika wao huo wa utatu na kusimamisha mgombea mmoja bila kumshirikisha yule wa Chadema.



Ibrahim Lipumba
Huo ndio ulikuwa mpango hadi siku hizi chache ambapo CUF Tarime wameamua kuachana na maamuzi ya CUF Taifa na wao kumuunga mkono mgombea wa Chadema. Wakati CUF walipotakiwa kuonyesha uongozi wameshindwa na badala yake wao kama TLP na NCCR wameweka maslahi yao mbele.

Tatizo kubwa ambalo naweza kuliona ni kuwa vyama hivi bado vinaongozwa kwa mtindo wa wanasiasa kuwa watendaji wa vyama vya kisiasa. Havina wataalamu wa mikakati ya kisiasa (political strategists) na matokeo yake viongozi wa kisiasa ndio pia wataalamu wa mikakati ya kisiasa.

Ndugu zangu siasa ni sayansi na sanaa. Siyo kila kitu kinafanywa kwenye majukwaa, kwani vingine vinapaswa kufanywa kwenye usiri wa wataalamu wa mambo mbalimbali. Vyama hivi vya upinzani ambavyo tulivitarajia kuwa tishio kwa CCM na hatimaye labda kuweza kuwa mbadala wa utawala vinazidi kuthibitisha kuwa licha ya vipaji vingi vya mtu mmoja mmoja ndani ya vyama hivyo, kama taasisi havijawa tayari kuikabili CCM na vipaji vilivyomo ndani ya chama hicho.

Ni kwa sababu hiyo sitoshangaa CCM wakishinda Tarime na wapinzani wakaja na wimbo wa “wizi wa kura” wenye kibwagizo cha “walitumia vyombo vya dola”. Saa na wakati kama huu Watanzania wanaangalia kwa makini kile wapinzani wanachofanya na siku si nyingi watakapoanza kuimba wimbo huo, wasishangae wakabakia wao na wapiga debe wao wakiitikia wimbo uliopitwa na wakati.

Ni mkosi wenye bahati kuweza kusimama wakati huu mgumu kwa Tarime. Wakati huu vyama hivi vinne vilitakiwa kuonyesha umoja zaidi, kuaminiana zaidi na ushirikiano kupita wakati mwingine wowote. Wakati huu walitakiwa kusimama kama kitu kimoja na badala yake sasa watajikuta wananyongwa mmoja mmoja.

Natoa wito kwa viongozi wa vyama hivi vya upinzani kutoendelea na hizi kampeni zilizogawanyika kwani wakiendelea hivi naweza kutabiri matokeo ya kura za Tarime kwa uhakika wa asilimia mia moja. Endapo vyama vya upinzani vitaamua kugawana kura basi mgombea wa CCM atashinda kwa kura chache ukilinganisha na jumla ya kura za wagombea wote wa upinzani.

Viongozi hawa na vyama vyao waache nyodo za kisiasa na kiburi cha tamaa ya madaraka. Wakae pamoja tena kwa haraka na kumaliza tofauti zao. Waende Tarime na waamue kuona jinsi gani wanaweza kuhakikisha mgombea wao mmoja ndiye anasimama na kuungwa mkono na tofauti zao kuzimaliza au kuziweka kiporo hadi baada ya uchaguzi huo mdogo. Viongozi hawa waamue kuweka umoja wao mbele kuliko kujiweka kimbelembele mmoja mmoja. Waamue kuhakikisha kuwa Jimbo la Tarime linabakia kuwa mikononi mwa Upinzani.

Wakiweza kukaa chini, kupanga mkakati wa ushindi na hatimaye kumsimamisha mgombea mmoja basi watawapa watu wa Tarime zawadi inayowastahili, zawadi ya kuhakikisha kuwa atakayemrithi Wangwe ni mtu anayekubalika na watu wengi zaidi. Kwa kufanya hivyo wataonyesha kuwa wao ni viongozi kweli kweli na si wanaonyatia marafiki zao wajikwae ndipo na wao watwae.



Chanzo: Raia Mwema
 
Mrema alalamikia Chadema, Jukwaa la wahariri

2008-11-10 13:44:49
Na Muhibu Said


Ufa umezidi kudhihirika katika ushirikiano wa kisiasa wa vyama vya upinzani nchini, baada ya Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema, kukituhumu Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwamba kimekuwa kikiendesha kampeni nchi nzima kwa lengo la kumsambaratisha kisiasa yeye na chama chake.

Amedai kampeni hizo dhidi yake na chama chake, zimekuwa zikifanywa na Chadema kwa kutumia ripoti ya uchunguzi wa habari za msiba wa aliyekuwa Mbunge wa Tarime, marehemu Chacha Wangwe (Chadema), iliyotolewa hivi karibuni na Kamati ya Hiari ya Wahariri.

Kamati hiyo iliyoundwa na Jukwaa la Wahariri, ndiyo iliyofanya uchunguzi huo.

Ushirikiano wa vyama vya upinzani ulioanzishwa Oktoba 10, mwaka jana, hadi sasa unaundwa na vyama vya CUF, Chadema, TLP na NCCR-Mageuzi, kati ya vyama 15 vya kambi vyenye usajili wa kudumu.

Hivi karibuni, Baraza Kuu la Uongozi wa CUF Taifa, lilimuagiza Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad kuviandikia vyama vya Chadema, TLP na NCCR-Mageuzi kuvitaka vieleze kama bado vina nia ya dhati ya kuendelea na ushirikiano huo, baada ya baadhi ya viongozi wa vyama hivyo kutamka kwa nyakati tofauti kwamba, ushirikiano huo umekufa.

Mrema alitoa madai hayo dhidi ya Chadema alipozungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya TLP, Magomeni, jijini Dar es Salaam jana.

``Chadema kampeni wanayoifanya hivi sasa nchi nzima, wanaitumia ripoti hii, ambayo inalenga kuniangamiza mimi na chama changu kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.

Maana leo kuna watu wanasafishwa na wengine wanalindwa. Hivi sasa naambiwa Chadema wako Mwanza wanaendelea na kampeni hiyo,`` alidai Mrema.

Hata hivyo, Mrema alisema anatarajia leo kuweka bayana undani wa kampeni hizo za Chadema anazodai kwamba zinafanywa dhidi yake na chama chake, atakapozungumza na waandishi wa habari.

Alidai Kamati ya Hiari ya Wahariri licha ya wajumbe wake kufahamu anakoishi, iliko ofisi yake na namba yake ya simu, haikujishughulisha kumtafuta ili kumhoji, badala yake iliishia kutoa ripoti, ambayo imemtuhumu kuwa alihusika katika kutumia msiba wa Wangwe kama mradi wa kisiasa kwa kutamka kwamba, Chadema ndio waliomuua Wangwe na kuwashawishi baadhi ya wananchi wa Tarime washushe bendera yake na wapandishe bendera ya TLP.

Alisema kitendo hicho, mbali ya kudhihirisha nia mbaya, ajenda ya siri ya kamati dhidi yake na kutaka kumchonganisha na Chadema na Mbowe, kimemdhalilisha na kumvunjia hadhi na heshima aliyoijenga kwa muda mrefu.

SOURCE: Nipashe
 
By Mkinga Mkinga

Chadema has turned down a request by the Civic United Front (CUF) to support its candidate in the coming Mbeya Rural parliamentary by-election.

As the Chadema refused to join an opposition alliance to wrest the seat from the ruling Chama cha Mapinduzi (CCM), representatives of CUF and three other parties met in Dar es Salaam yesterday to strategise on how to win the January 25 poll.

The four opposition parties declared their support for the CUF candidate, Mr Daudi Mponzi.Addressing a joint press conference, NCCR-Mageuzi chairman James Mbatia, Tanzania Labour Party (TLP) Augustine Mrema, and PPT-Maendeleo's Peter Mziray said their main objective was to defeat CCM in the by-election.

The ruling party's candidate is the Reverend Luckson Mwanjale. He seeks to succeed Mr Richard Nyaulawa, whose death last November, occasioned the by-election.But Chadema dissociated itself from the joint opposition candidate plan, accusing CUF of blocking its own aspirant for the Mbeya Rural seat.

Speaking to The Citizen by telephone yesterday, the Chadema secretary-general, Dr Willibrod Slaa, said discussions between the two parties had failed to yield an agreement on a joint opposition election strategy and other matters.

"Last September, before the Tarime parliamentary by-election, we met at opposition leader in Parliament Hamad Rashid's residence in Dar es Salaam for discussions led by our two chairpersons, Prof Ibrahim Lipumba and Mr Freeman Mbowe, but failed to reach a consensus on the issue," Dr Slaa said.

Chadema had sought to know if CUF was ready for opposition solidarity, but Prof Lipumba said they needed to discuss the matter in their party so that the decision executive council members could make that decision.

"Until today, nothing has come out of that solidarity bid. Instead, CUF fielded a candidate in Tarime against our own though its leaders were aware that Chadema is more popular in area," the secretary-general added. He said CUF's Tarime district management team criticised the headquarters for opting to field a candidate instead of supporting Chadema's.

Dr Slaa added that after the Tarime by-election, Chadema wrote a letter to CUF seeking to know its position on the solidarity talks that had been held at Mr Rashid's residence, but received no response on the matter.

"Instead they wrote requesting for our support in the Mbeya Rural by-election campaigns. CUF was an impediment to our party, so how can we support them?" Dr Slaa asked.

"We won't assist CUF in the campaigns, as if we do so people will think we are crazy. Let the other parties support them and not Chadema,"

Yesterday, CUF's national chairman Lipumba said the leaders of the other three parties would join them on the campaign trail in Mbeya to ensure that their candidate wins the poll.

Prof Lipumba said the disagreement with Chadema had started during the Tarime by-election campaigns, but fortunately the opposition party had retained the seat.

"But I'm now happy that we have the support of our opposition colleagues and are now finalising plans before leaving for the Mbeya by-election campaigns."

NCCR Mageuzi chairman James Mbatia said they would fully support the CUF candidate in the Mbeya Rural by-election to defeat CCM.

"This has been our dream for very long time, but it has all along been sabotaged. We have now corrected our mistakes and decided to fully support CUF because they have majority support in the constituency," Mr Mbatia said.

"We need to increase number of opposition members in the national assembly, we have our supporters in Mbeya rural which we can influence them to vote for CUF."

TLP chairman Augustine Mrema said the opposition parties had decided to forget their differences and support CUF, which came second to CCM in the 2005 elections.

"We all have a very good network in the area and should make the CUF candidate win the election," he said.

On the failure to forge opposition unity, Mr Mrema said: "Every human being has his own way of pursuing issues, and we all have our weaknesses. We have now resolved our differences and will assist the CUF candidate to win election in Mbeya Rural seat.".
 
CUF Itawaongoza na kuiteka Tanganyika toka mikononi mwa CCM kama ilivyofanikiwa kuiteka Zanzibar kutoka mikononi mwa CCM. kitakachowakwamisha kuchukua serikali ni nguvu za ziada ambazo CCM imeshika hatamu zake.

La kujiuliza ni lini wananchi wa Tanganyika watakapo amua kula sahani moja na nguvu hizo kama wenzao wa Pemba na kuwawacha watawala kuwa wa kimabavu kama huko Zenji,hilo ndilo la kujiuliza.

CUF naweza kusema ni chama ambacho kimekuwa gifted ,kinapendwa kiaaina na wananchi walio wengi ,hili halina ubishi.
 
Kifupi, CUF au Chadema ni kichaa aliyeiba nguo za mwenzake na sasa hivi kichaa huyo anafukuzwa na mwenziwe akiwa Uchi..nimeshindwa kujua kichaa ni nani kati yao..

Habari hii yote inapokelewa na wananchi kwa jicho tofauti na vyama hivi vinavyofikiria.. Sisi tunawaona wote ni vichaa na watu wasioweza kupewa dhamana ya wananchi..
Umoja wa Upinzani unakuja na sura mpya na yenye nuru kuliko nguvu ya chama kimoja...Upinzani ni sawa na ndoa ambayo heshima yake hutokana na kuwepo watu wawili walioshikamana kama mme na mke hivyo hata siku moja ndoa hiyo ikivunjika na sababu zikatolewa kumponda mmoja wao ni dhahiri msemaji hujiumbua yeye mwenyewe..
Hakuna Mtanzania hata mmoja anayejiunga na CUF au Chadema kwa sababu ya kujitoa mhanga wala hakuna kipimo cha maumivu kinachodhihirisha kwetu nani mgombea wa kweli..
Na kibaya zaidi ya yote ni kwamba Usiri na mipango yote ambayo waliiweka ktk makubaliano ya Upinzani sasa hivi yanatoka nje, hii kuonyesha ni jinsi gani viongozi hawa hawatakiwi kuaminiwa hata kidogo.
Siri za ndami ya nyumba zinapotoka nje siku zote msikilizaji humwona msemaji kuwa chizi au kichaa.. huwezi kutoa siri za nyumbani kwako kabla hujauliza na hata kama umeulizwa la msingi ni kujiuliza kwanza uta accomplish kitu gani kumbomoa mwenzako kwa matusi wakati wananchi wanaona kabisa kuwa huwezi kuiweka ndoa.. Problem ni wewe kushindwa kuwa ktk ndoa..Who did what, haiwezi kutusaidia hata kidogo wala kwenda jela sio kithibitisho cha kutetea wananchi ikiwa sababu zilikuwa kutoa matusi kwa ki/viongozi wa CCM au baraza la Mapinduzi..

Hakuna mtu hata mmoja Tanzania hii amekwenda Jela kwa sababu ya kupigania haki yetu isipokuwa maslahi yake binafsi..huwezi kwenda jela kwa kutumia matusi ama lugha chafu kisha udai kuwa umepigania haki ya wananchi...stupid! ni ukosefu wa heshima na upunguani kutoheshimu Jamhuri ya Muungano wetu hata kama hukubaliani na katiba ya nchi yetu.
Kumbukeni tu CUF na Chadema - U all Losers - bigtime losers - ndivyo wananchi wanavyowaona.. mtaacha ndoa hii na hakuna mwananchi (watoto wenu) watawaamini tena..
 
Back
Top Bottom