Achapwa viboko na kunyimwa Form 5 kwa kukataa kuingia chama tawala

Umsolopogaas

Member
Jul 18, 2010
40
11
Siasa ya ujamaa na kujitegemea ilitudumaza - Mtikila
na Ratifa Baranyikwa

Tanzania Daima

Jumapili, 3 Februari 2008




Hivi karibuni Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, alifanya mahojiano na vyombo vya habari, katika mahojiano hayo Mtikila anaelezea kushindwa kwa siasa ya ujamaa na kujitegemea iliyokuwa ikitekelezwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza ya Mwalimu Julius Nyerere. Mtikila pia anaelezea yaliyojiri katika kipindi cha uongozi wa Mwalimu Nyerere na misukosuko mbalimbali aliyokutana nayo katika maisha yake.
Swali: Una nafasi gani hivi sasa katika jamii?
Jibu: Mimi ni Mchungaji, ni mchungaji wa Kanisa la Full Salvation, ndiyo maana ni mchungaji, lakini pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia.
Swali: Maisha yako yamekuwa ya misukosuko sana, unakumbuka msukomsuko wa kwanza uliupata lini?
Jibu: Nilitiwa mbaroni mwaka 1989, hii ilikuwa mara yangu ya kwanza, nilikuwa nawahutubia wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Walikuwa wamegoma, walikuwa wakidai demokrasia ya vyama vingi na haki za binadamu. Wakati nawahutubia nilitiwa mbaroni kwa tuhuma za uchochezi.
Swali: Lini ulianza kujihusisha na harakati za upinzani?
Jibu: Nakumbuka, nikiwa mwanafunzi wa sekondari, Mkuu wa shule ambaye ni Mwafrika wa kwanza, Alexander Thomas Mabelli, alitoa amri kuwa kila mwanafunzi awe mwanachama wa Umoja wa Vijana wa TANU, ambacho kilikuwa chama tawala kwa wakati huo.
Ingawa nilikuwa katibu wa shule, niliyakataa mawazo hayo kwa sababu niliujua ukweli, na nilikataa kwa sababu ningetaka kuwa mwanachama, basi ningefanya hivyo wakati nikiwa nyumbani.
Kwa kuwa nilikataa, nilichapwa fimbo sita mbele ya mkusanyiko wa wanafunzi, niliona si haki, hivyo basi nikafukuzwa shule. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu yangu ya kwanza kupingana na chama tawala.
Ingawa marehemu baba yangu alikwenda kumuomba mkuu wa shule nikaruhusiwa kufanya mitihani yangu ya mwisho ya kidato cha nne, tayari nilikuwa nimepoteza sifa ya nidhamu kwa ajili ya kuendelea na kidato cha tano. Lakini niliamini kuwa nimelinda utu pamoja na msimamo wangu.
Baada ya hapo nilijikita kwenye masuala ya sheria kabla sijakwenda kufanya kazi katika Shirika la Ndege la Afrika Mashariki, baadaye nilianza kujihusisha na biashara.
Mwaka 1982 niliamua kuokoka na kuzaliwa upya kiroho, nikaamua kuhubiri Injili, lakini katika kufanya hayo, nilijihisi kuwa mbinafsi kwa sababu hata sauti ya Mungu ilikuwa ikinijia na kuniambia hivyo.
Nilianza kuzungumza kwa niaba ya wanyonge, nikawaambia watu kuna haja ya kuanza kutambua haki za binadamu na kuzitetea kwenye katiba. Hili nilisema kuwa lilikuwa kinyume cha katiba, hivyo niliingia kwenye matatizo.
Mwaka 1987, nilitawanya karatasi zenye kutetea utu katika mkutano mkuu wa chama tawala, nikawa Mtanzania wa kwanza kufanya hivyo kwenye mkutano kama huo. Nilitoroka kwa kuogopa kukamatwa lakini nilikamatwa rasmi mwaka 1988, hata hivyo sihesabu kama nilikamatwa kwa vile nilishikiriwa kwa saa 24 kisha nikaruhusiwa kwenda nyumbani.
Swali: Hiyo ilikuwa mara yako ya kwanza kukamatwa?
Jibu: Hapana, mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1967. Nilikamatwa nikahukumiwa miaka 25 jela kwa makosa mawili, moja la uchochezi na la pili kutumia lugha ambayo ingesababisha uvunjifu wa amani.
Swali: Maisha yalikuwaje mwaka 1967?
Jibu: Maisha yalikuwa mazuri nilipokuwa shule, kipindi hicho kulikuwa na mkate na siagi, chakula kilikuwa kizuri. Na kiwango cha elimu kilikuwa ni cha kimataifa.
Tulikuwa na walimu kutoka Uingereza, Marekani, Canada, Australia na New Zealand, hivyo tulikuwa na elimu bora kila mahali. Lugha ya ufundishaji ilikuwa Kiingereza, sasa vyote hivi havipo.
Swali: Elimu ya taifa ilikuwaje?
Jibu: Elimu ya taifa ilikuwa mbinu ya kutuweka huru kifikra kutoka katika elimu ya kibepari kama ilivyokuwa ikiitwa, yalikuwa ni mabadiliko kwa sababu masomo yote yalipewa jina la kibepari.
Swali: Hali ya maisha ya watu ilikuwaje wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere?
Jibu: Ilikuwa ni mbaya sana, watu walikuwa hawaaminiani hata katika familia, baba hamuamini mama, vivyo hivyo mama hamuamini baba kwa sababu kulikuwa na kampeni kali ya kigaidi.
Watu walikuwa wakitoweka kimya kimya na hakuna mtu aliyeruhusiwa kuwafikiria, ikitokea wanakutuhumu kama muasi, nawe pia utapotea.
Tuliishi katika utawala wa kimabavu, tulifanywa kufikiria kuhusu mambo ambayo hayakuwepo na tulilazimishwa kuamini yapo.
Swali: Haukumuamini mke wako kwa namna yoyote ile?
Jibu: Si mimi peke yangu, kila mtu aliyekuwa na mke hakumuamini mke wake, tulikuwa tukizungumza kuhusu jambo hilo mitaani, kwenye mabasi na sehemu yoyote ile kwamba usimwamini mtu yeyote.
Hatukuwa tunaongea kuhusu maisha yetu, uchumi wa jamii yetu na vitisho vya kisiasa dhidi ya watu wetu na nchi yetu, tulikuwa tukiogopa kwamba watu wetu wakaribu, wake kwa waume walikuwa ni mawakala wa upande mwingine, ilikuwa ni kesi ya nchi nzima.
Hata mashuleni, watoto wa shule walikuwa hawaruhusiwi kuongelea jambo lolote tofauti na masomo yao, hivyo kitu rahisi cha kulegeza akili za watu ilikuwa ni kuzungumzia kuhusu timu mbili za soka …Simba na Yanga. Ulikuwa wakati mgumu sana kimaisha ambapo tuliishi kama wafungwa, mimi nikiwa mmojawapo.
Swali: Hali ya sasa ikoje kuhusu haki ya watu kujadili maisha yao?
Jibu: Watu bado wanaogopa kuongea ukweli, ingawa hivi sasa wameanza kutembea vizuri. Lakini kwa miaka hii mingi walikuwa wakihofu kuwa bado wapo kwenye umoja, bado wamefungwa pamoja.
Hawawezi kutembea kwa sababu kila wakati walikuwa wakitishwa, ilikuwa lazima kuongea vitu ambavyo watawala walitaka viongelewe.
Hivyo watu bado wanaendelea kuogopa kusema ukweli, lakini wanaendelea kuamka, wanatumia vyombo vya habari na redio kwa maneno ya makeke na maelezo ya habari badala ya habari kutoa onyo kwa kila mtu nchini kutojaribu kuwa kama wasumbufu wanavyosema.
Swali: Ni jinsi gani siasa ya ujamaa na kujitegemea iliharibu muamko wa Watanzania?
Jibu: Kulikuwa kuna kitu katika wazo la ujamaa na ilikuwa ni propaganda, ambayo ilikuwa inaongoza mawazo ya watu, na walikuwa wakijisikia furaha.
Walijisikia kuwa ni haki yao kuwa chini, kutokuwa na sauti, wala msaada, walikuwa wakiamini kuwa ni vibaya na ni kinyume cha taratibu, na kama watageukia upande wa dini ni utakatifu. Walifanikiwa katika hilo kwa kiwango cha juu.
Swali: Je, watu walipata mwamko huo?
Jibu: Ooh! Tuna furaha sana, tuna furaha kubwa sasa kwamba gharama ambazo tulilipa zimeturudishia kitu fulani, watu wanaamka sasa, kweli! Walikuwa wamebadilishwa.
Swali: Je, ni mfumo wa ujamaa ambao ulishindwa au uongozi wa Nyerere ndio ulioshindwa?
Jibu: Katika ujamaa, mara zote si mfumo, tuupeleke kwenye ukweli, mara zote ni binadamu, kama tutaongelea kuhusu ujamaa au ujima katika muungano wa Ki-soviet, tunaongelea kuhusu Marx, Jews na Lenin.
Kama tutaongelea kuhusu mfumo kwa nchi ya China, tunaongelea kuhusu Mao Tse-Tung, katika nchi yetu alikuwa ni Julius Nyerere, alikuwa amebobea katika sera zote, sera za ujamaa hakuna mtu mwingine aliyefanya hivyo- ni yeye pekee.
Kwa hiyo si ujamaa ulioshindwa, bali Nyerere ndiye alishindwa. Watu wanaosema tusimuhusishe Nyerere katika kushindwa kwa ujamaa, hao wanaogopa kusema ukweli.
Swali: Je, kwako kuna mazuri yoyote kuhusu Nyerere unayoweza kuyazungumzia?
Jibu: Kama yangekuwepo ningesema, lakini kwa miaka 41 ya uongozi wake, sikuwahi kuona hata moja.
Ila kulikuwa na machache aliyokuwa akiigiza, yalikuwepo ya kuamini lakini kuwepo kwa hayo hakuwezi kufanya kazi mbele ya watu ambao hawawezi kufikiri na kuona.
Aliniunga mkono kabla ya kifo chake, alisema: 'Tumetambua kwamba tumefanya makosa' hivyo kila kitu alichofanya kwa kivuli cha ujamaa hakikufanikiwa, na alijua kwamba hakitafanikiwa, lakini wakati mwingine alikuwa akisukuma kufanikisha malengo yake.
Wakati dunia ilipoona ukweli alikiri, alisema: "Ni kweli tulifanya makosa." Na siku zote nashangazwa na watu wanaomtenga Nyerere kwa uwazi wake. Alikiri, na kwa sababu mimi ni muhubiri wa Injili tumemsamehe, kwa sababu aliomba msamaha.
Swali: Nini maoni yako kuhusu utawala wa Nyerere kwa ujumla?
Jibu: Tangu siku alipojiuzulu uwaziri mkuu, aliondoka kwa ujanja na kuwa Rais mwaka 1962, siku zote alikuwa mtawala mwenye kutumia mabavu.
Kwa sababu aliona mchezo aliokuwa akiucheza na rushwa ilikuwa inakwenda kumtoa kwenye madaraka kabla ya mchezo wake wa kujiuzuru kutoka kwenye uwaziri mkuu haujajulikana, aliwaangalia watu wote waliokuwa wakimnyoshea kidole, walikuwa ni wa kwanza kupata panga baada ya kuwa rais.
Kwa sababu alijua kwamba wangempinga, alianzisha mfumo wa chama kushika hatamu ili kudhibiti watu ambao wangempinga. Kwa hiyo alikuwa na chembe chembe za utawala wa mabavu.
Ndiyo kusema aliipeleka nchi katika misingi ya kutawala kimabavu.
- end -
 
Back
Top Bottom