JK: Atakayegoma hana kazi
Afafanua mgomo wa wafanyakazi ni batili
Aeleza yu tayari kuzikosa kura zao Oktoba
Asema hata wakigoma miaka 8 hawalipwi
Tucta waahidi kutoa tamko la mgomo leo
Rais Jakaya Kikwete
Rais Jakaya Kikwete, amesema mgomo wa wafanyakazi uliopangwa kufanyika kuanzia kesho nchini kote ni batili na ni kinyume cha sheria na kuonya kuwa atakayeshiriki atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu za kazi.
Mgomo huo umeitishwa kwa lengo la kuishinikiza serikali kutekeleza madai yao mbalimbali, ikiwamo nyongeza ya kima cha chini cha mshahara kutoka sh. 104,000 kufikia sh. 315,000 kwa mwezi.
Amesema mgomo huo ni batili kwa vile umeitishwa katikati ya majadiliano kati ya serikali na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) kuhusu madai ya wafanyakazi, ambayo alisema yamepangwa kuendelea Mei 8, mwaka huu.
Alisema kiwango cha nyongeza ya mshahara kinachoombwa na wafanyakazi kupitia Tucta, hakiwezi kutekelezeka hata kama mgomo huo utafanyika kwa miaka minane mfululizo.
Rais Kikwete alisema hayo alipozungumza na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam jana kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee na kusema kama kuna mtumishi yeyote wa serikali anayeona hawezi kufanya kazi mpaka alipwe mshahara wa Sh. 315,000 kwa mwezi, ni heri aache kazi, badala ya kujisumbua kugoma.
Alisema iwapo wafanyakazi wanaofikiria kumnyima kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu kwa vile serikali imeshindwa kutekeleza matakwa yao magumu, yuko tayari wamnyime, lakini kamwe serikali haiko tayari kuwadhulumu wananchi 39,650,000 kwa ajili tu ya kuwanufaisha wachache Sh. 315,000.
Na bahati mbaya mgomo uliotangazwa na Tucta siyo halali kabisa. Umeitishwa katikati ya majadiliano. Mmekubaliana tarehe 8 mkutane, wewe mgomo tarehe 5, na wamekubali wenyewe, alisema Rais Kikwete na kuongeza:
Lakini ninachowaambia kama mgomo wenyewe ni kwa ajili ya 315,000, hata wakigoma, wakakaa miaka minane, mshahara huo haupo. Hatuwezi kuulipa. Anayeona kwamba hawezi kufanya kazi kwenye serikali, ambayo haiwezi kumlipa kima cha chini cha 315,000 aache kazi.
Tusipoteze muda wa kudai kisichowezekana, hamtakipata. Kama ukisema wewe kama si wa 315,000, basi hutaki kufanya kazi serikalini, basi ondoka kwa usalama. Huna sababu ya kugoma kwa sababu hata ukigoma ukimaliza mgomo, 315,000 hazipo, alisema huku akishangiliwa na wazee kwa maneno: Sema usiogope sema.
Alisema kauli ya Tucta kwamba, mgomo hautakuwa na muda hadi hapo madai ya wafanyakazi ya kulipwa mshahara wa Sh. 315,000, hawana sababu ya kusumbuka kwani hayatatekelezwa na kuwashauri waache kazi serikalini na waende watakakopata waajiri ambao wataweza kuwatekelezea mshahara mzuri.
Rais Kikwete alisema Tucta wamejitwalia mamlaka ya kisheria ya kutangaza kima cha chini cha mshahara, wakati mwenye mamlaka hayo kwenye sekta binafsi, ni Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana na kwenye sekta ya umma, ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi).
Alisema daima serikali inawajali na kuwapenda sana wafanyakazi kwa vile bila kuwajali shughuli serikalini haziwezi kufanyika na kwamba, itaendelea kuongeza mishahara kwa kadiri uwezo utakavyoruhusu.
Alisema atakayegoma kesho, atakuwa amekiuka taratibu na kanuni za ajira na kwamba, atachukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu na kanuni za utumishi serikalini.
Kama dereva kagoma atachukuliwa hatua kwa mujibu wa mwenye teksi, kama ni dereva wa daladala kagoma kwa mujibu wa mwenye daladala, alisisitiza.
Pia, alisema yule atakayekwenda kazini, akaacha kufanya kazi, naye pia atachukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa kanuni.
Mimi ndiye mwajiri mkuu kwa upande wa serikali, nawaomba myasikilize yangu. Mkiamua kumsikiliza Mgaya (Naibu Katibu Mkuu wa Tucta) shauri yenu. Mtapoteza maslahi yenu na Mgaya hamtamuona. Na hatakuwapo kuwatetea. Yeye ana ajenda yake, tuna wasiwasi na kama ameyatimiza ya waliomtuma, ameshawafanyia kazi, alisema.
Katika mkutano wa jana, viongozi waliohudhuria ni pamoja na Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohamed Shein, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Jenerali Davis Mwamunyange, Mkuu wa Jeshi Polisi, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Profesa Juma Kapuya na Naibu wake, Dk. Makongoro Mahanga na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi.
Rais Kikwete aliingia ukumbini hapo na kutoa hotuba hiyo iliyochukua takriban saa moja na nusu kuanzia saa 11:00 jioni, huku wazee wengi wakiwa wamevalia sare za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kumshangilia kila wakati.
Kabla ya Rais Kikwete kutangaza kuwa mgomo wa kesho ni batili, Rais wa Tucta, Ayoub Omari, alisema hatma ya mgomo wao itajulikana leo baada ya Kamati ya Utendaji ya Shirikisho kukutana.
Kesho (leo), tutakuwa na kikao cha Kamati ya Utendaji, baadaye tutatoa tamko la pamoja kama mgomo utakuwapo kesho au la, alisema Omari.
Alisema Kamati ya Utendaji ya Tucta inakutana leo baada ya majadiliano yaliyoanza takriban mwezi sasa kati ya Shirikisho na serikali kupitia Kamati yake ya Usuluhishi na Upatanishi kuhusu maslahi ya wafanyakazi kufikia tamati kati ya jana au leo.
Hata hivyo, alisema kufikia jana, majadiliano hayo yalikuwa yanaendelea vizuri na kwamba, yameanza kutoa mwanga unaoonyesha mambo yanayodaiwa na wafanyakazi kufikia mahala pazuri.
Majadiliano yanaendelea vizuri sana. Kuna mwangaza mzuri tu wa kufikia mahala pazuri. Kama nilivyokwambia, sisi si watu wa uhasama. Nia yetu si kugoma, ila watu wanyonge kupata haki yao, alisema Ayubu.
Majadiliano hayo yalianza kufanyika siku tatu, baada ya Rais Jakaya Kikwete kupitia hotuba yake ya mwisho wa mwezi Machi, mwaka huu kwa taifa, kuwasihi wafanyakazi kupitia Tucta kuacha mgomo na kukubali kurejea kwenye meza ya mazungumzo ili kumaliza mvutano kati yao na serikali kuhusu maslahi yao.
Katika hotuba yake hiyo, Rais Kikwete aliwasihi wafanyakazi kufikiria upya uamuzi wao wa kutaka kugoma, badala yake wakubali kufanya mazungumzo na serikali kwani inawajali, kuwathamini na inajiandaa kuongeza tena mishahara katika bajeti yake ijayo.
Machi 2, mwaka huu, Ayubu alikaririwa na gazeti hili akisema walifikia uamuzi wa kutangaza kugoma nchi nzima, kutokana na serikali kutaka kutumia jukwaa la mazungumzo lisilostahili.
Ayubu alisema Baraza la Ushaurikazi, Uchumi na Masuala ya Jamii (Lesco), ndiyo lilikuwa jukwaa sahihi la mazungumzo, lakini tangu mwaka 2008, serikali haikutaka kuliitisha.
Rais Kikwete alisema tangu serikali yake iingie madarakani, imechukua hatua thabiti za kuendeleza haki na maslahi ya wafanyakazi, mambo ambayo yanathibitisha kwamba inawapenda, kuwathamini na kuwajali.
Rais Kikwete alisema wameongeza mshahara wa kima chini mara tatu, kuanzia mwaka 2006 kutoka sh. 65,000 hadi 104,000 sasa.
Rais Kikwete alisema hivi sasa wanajiandaa kuangalia makundi mengine na hata baadhi ya yale waliyoongeza siku za nyuma watayaangalia tena.
Habari hii imeandikwa na Muhibu Said na Richard Makore.
CHANZO: NIPASHE