TAARIFA KWA WANANCHI WA TANZANIA.
Ndugu wanahabari,
Tarehe 15 Septemba 2007 tulitoa Orodha ya Mafisadi yenye kuonyesha ufisadi, wizi na/au ubadhirifu wa mabilioni ya fedha za umma unaowahusisha viongozi na watendaji wa juu katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano na watu wengine walio kwenye uongozi wa umma. Hadi sasa Serikali haijatoa majibu ya kuridhisha kuhusiana na tuhuma hizi nzito licha ya madai ya kufanya hivyo kutoka kwa wananchi, taasisi zisizo za kiserikali, viongozi mbali mbali ndani na nje ya Serikali na Chama cha Mapinduzi (CCM) na hata wawakilishi wa nchi wafadhili walioko Tanzania.
Ndugu wanahabari,
Siku hiyo kwenye mkutano wetu wa hadhara kule Mwembe Yanga Wilaya ya Temeke tulisema yafuatayo kuhusiana na ufisadi ndani ya BOT , na tunaomba kuyaweka hapa ili kuweka kumbukumbu ziwe sahihi pamoja na historia ya jambo hili;
(i)Gavana Balali ameruhusu na/au kuidhinisha na/au kunyamazia ufujaji wa fedha za umma unaodaiwa kufikia Shilingi 522, 459, 255,000 katika ujenzi wa majengo ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyoko barabara ya Mirambo, Dar es Salaam na Gulioni, Zanzibar.
(ii) Gavana Balali aliidhinisha na/au kuruhusu na/au kunyamazia malipo ya Dola za Marekani 118,396,460.36 zilizopelekwa katika akaunti isiyojulikana ya Benki ya Nedbank Ltd. ya Afrika Kusini kama malipo ya madeni ya kampuni muflisi ya Meremeta Ltd. iliyokuwa inachimba dhahabu katika eneo la Buhemba wilaya ya Musoma, Mkoa wa Mara. Hata hivyo, nakala ya usajili iliyotolewa na Msajili wa Makampuni wa Uingereza na Wales inaonyesha kwamba kampuni hiyo iliandikishwa nchini Uingereza tarehe 19 Agosti 1997 na ilifilisiwa huko huko Uingereza tarehe 10 Januari 2006.
(iii) Gavana Balali aliruhusu na/au kuidhinisha na/au kunyamazia malipo ya Dola za Marekani 13,736,628.73 kwa kampuni ya Tangold Ltd. Katika hotuba yake Bungeni ya tarehe 27 Juni 2007, Waziri wa Madini na Nishati Mheshimiwa Nazir Karamagi alidai kwamba "… mali na madeni ya MEREMETA yamehamishiwa kwenye kampuni mpya ya TANGOLD ambayo inamilikiwa na Serikali kwa asilimia mia moja." Hata hivyo, barua ya BRELA ya tarehe 4 Julai 2007 inatamka wazi kwamba "Tangold Limited ni kampuni ya kigeni iliyosajiliwa kwa mara ya kwanza nchini Jamhuri ya Mauritius, na baadae kuandikishwa nchini Tanzania kama tawi la kampuni ya kigeni.
(iv) Gavana Balali aliruhusu na/au kuidhinisha na/au kunyamazia mkopo usio na riba wa Dola za Marekani 5,512,398.55 kwa kampuni ya Mwananchi Gold Co. Ltd. kati ya mwaka 2004 na tarehe 30 Juni 2006. Kati ya fedha hizo, deni la dola 2,807,920 limedhaminiwa kwa dhahabu ghafi ambayo ingenunuliwa kutokana na fedha za mkopo zilizotolewa na Benki Kuu yenyewe! Kwa maana rahisi ni kwamba kampuni ya Mwananchi Gold haijatoa dhamana yoyote inayoeleweka kwa mabilioni ya shilingi ilizokopeshwa na Benki Kuu chini ya Gavana Balali.
(v)Gavana Balali aliruhusu na/au kuidhinisha na/au kunyamazia malipo ya shilingi 131,950,750,000 kwa watu wasiojulikana wanaodaiwa kuingiza fedha za kigeni nchini. Vile vile Gavana Balali anadaiwa kuidhinisha malipo ya shilingi bilioni 4,228,658,000 kwa watu wasiojulikana wanaodaiwa kuingiza fedha za kigeni nchini. Waziri wa Fedha Zakia Meghji mwenyewe amekiri kuwepo kwa matumizi mabaya ya fedha za umma katika akaunti za malipo ya madeni ya nje katika barua yake kwa Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF).
IMF yenyewe katika taarifa kwa vyombo vya habari ya tarehe 27 Juni 2007 imetamka kwamba "Serikali (ya Tanzania) imekwisha kusimamisha malipo kutoka akaunti hiyo hadi uchunguzi huo utakapokamilika." Wakati Serikali ikitoa taarifa hizi kwa IMF imekataa kata kata kutoa taarifa hizi kwa umma wa Watanzania wala wawakilishi wao Bungeni.
(vi) Kwa mujibu wa barua ya wakaguzi kampuni ya Mkono & Co. Advocates wamekwishalipwa shilingi 8,128,375,237 kwa fedha taslimu na BOT kwa kesi hiyo ambayo bado iko mahakamani. Malipo haya ni sawa na asilimia 13.5 ya deni lote inalodaiwa Benki Kuu (BOT) Hoja ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu ni kuwa kesi hii haina muda maalumu wa kumalizika na hivyo inawezekana kabisa malipo ya wanasheria yakazidi kiasi cha fedha inachodaiwa Benki Kuu.
Ndugu wanahabari,
Ukiangalia kwa makini juu ya tuhuma tulizozitoa utaona ya kuwa Rais Kikwete amechukua hatua kwenye tuhuma moja tuu ya wizi na au ufisadi wa kiasi cha shilingi 133 Bilioni ,na kunyamazia tuhuma nyingine na wizi mwingine ambao ni mkubwa zaidi ,kwani taarifa zinaonyesha kuwa zaidi ya shilingi trilioni 1.3 zimeibiwa ama zimefujwa ndani ya (BOT) ,na kilichofanyiwa kazi ni chini ya asilimia kumi tuu (10%
.
Kwa hiyo basi tunamtaka Rais Kikwete afanye yafuatayo kama kweli ana nia na dhamira ya kukabiliana na mafisadi waliopo ndani ya serikali yake na Chama chake ambacho ndicho chama tawala;
1.Sisi tunaamini kuwa Dr. Daudi Ballali anayo mambo mengi ambayo anayafahamu na kwa kukamatwa mara moja na kuwekwa chini ya ulinzi ,kutaweza kusaidia kwenye kutafuta ushahidi na pia jambo hili litaweza kumwepusha na wale wote waliohusika kwenye ufisadi huu kumdhuru ili kuficha ama kupoteza ushahidi.Na pia serikali iache kukaa kimya na iseme wazi kuwa Ballali anaumwa nini na yupo hosipitali gani na nchi gani .
2.Wakurugenzi wa makampuni yaliyotajwa kwenye ufisadi na ripoti ya ukaguzi iliyoshughulikia eneo moja la akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) wakamatwe mara moja na kuwekwa chini ya ulinzi na hatua za kisheria zichukuliwe juu yao , kitendo cha kuwaweka chini ya ulinzi kitasaidia kwenye upelelezi na wao hawatapata nafasi ya kuharibu ama kuupotosha ushahidi .
3.Rais Kikwete awafukuze kazi mara moja aliyekuwa waziri wa fedha Mhe.Basil Mramba na Katibu Mkuu wa wizara ya fedha Gray Mgonja, kwani hawa wanahusika moja kwa moja kwenye ama kuidhinisha malipo hayo au kunyamazia ufisadi huo.
Na pia kitendo cha yeye Gray Mgonja kuendelea kuwa mjumbe wa bodi ya Benki Kuu (BOT) kwa wadhifa wake wa kuwa katibu mkuu hazina na kujichukulia hatua mwenyewe ni kitendo ambacho hakiwezekani ,kwani anahusika moja kwa moja na upotevu wa fedha za wananchi masikini wa Tanzania .
4.Kwenye uchunguzi wetu tumegundua kuwa ufisadi huu ulihusisha mabenki ambayo yapo hapa nchini mwetu, na tunawataka wenye Benki hizo wahakikishe kuwa wanawajulisha watanzania jinsi walivyohusika na ufisadi huo kwani waliweza kujipatia faida kwenye fedha za kifisadi na kama hawatafanya hivyo tutawatangazia wananchi wa Tanzania hatua madhubuti za kuchukuliwa dhidi ya Benki hizo ,kwani zinajihusisha na wizi wa fedha za wananchi masikini na wafanyakazi ambao wamekuwa wakikatwa kodi kubwa kwenye mishahara yao midogo .
5.Tunasisitiza kuwa Rais Kikwete aiweke taarifa ya ukaguzi wa fedha kwenye akaunti ya EPA hadharani kama alivyowaahidi wananchi wa Tanzania mara moja ili kuepusha hisia kwamba kuna jambo linalofichwa kwenye taarifa hiyo na/au inafanyiwa marekebisho ya kuficha baadhi ya ufisadi uliofanyika ndani ya Benki Kuu (BOT).
6.Muda ambao Rais Kikwete ameutoa wa miezi sita kwa ajili ya kufanyika kwa uchunguzi baada ya ripoti ya ukaguzi ndani ya akaunti ya EPA unakinzana na kauli yake ambayo aliitoa Bungeni ya kuwa kama ukaguzi ukishafanyika na kubaini kuwepo kwa kasoro ama ukiukwaji wa taratibu , hakuna sababu ya kufanya uchunguzi mwingine tena bali ni kuwachukulia hatua za kisheria mara moja wahusika. Hivyo tunamtaka Rais atembee kwenye maneno yake na sio vinginevyo.
7 . Kama Rais Kikwete asipowawajibisha wahusika wote wa ufisadi uliotokea ndani ya Benki Kuu , basi viongozi wakuu wa vyama hivi watawapa watanzania maelekezo ya juu ya hatua zinazofaa kuchukuliwa .
Tunawashukuru sana kwa kutusikiliza .
Imetolewa na Kamati ya Ufundi ya ushirikiano wa vyama vya;
CHADEMA – Benson Kigaila. ………………………………..
CUF – Wilfred Lwakatare (Mwenyekiti). ………………………………
NCCR MAGEUZI – Sam Ruhuza. ……………………………...
TLP – Benedicto Mtungirehi. ……………………………….