Yafahamu matangazo feki ya kazi na namna ya kuyaepuka

JamiiCheck

Member
Nov 3, 2023
54
40
1709620994643.jpeg

Kupata kazi ni lengo linalohitaji jitihada na tahadhari, lakini katika ulimwengu wa leo wa mtandao, kuna hatari ya kukumbana na matangazo ya kazi feki. Kutambua ishara za matangazo haya na kujifunza jinsi ya kuepuka kushawishiwa ni muhimu kwa mafanikio ya kutafuta ajira.

Matangazo ya kazi feki yanaweza kuwa na vipengele mbalimbali. Katika andiko hili tumegusia vipengele vifuatavyo:

Kuwekwa Mshahara Mkubwa usio wa kawaida: Tangazo linalotangaza mshahara usio wa kawaida kwa kazi fulani linaweza kuwa ishara ya tangazo feki. Mara nyingi, watu hutoa mshahara mkubwa sana ili kuvutia waombaji, lakini ukweli ni kwamba kazi hiyo haistahili kulipwa kiwango kikubwa kama hicho.

Kukudai Taarifa Binafsi: Tangazo linalokuhitaji utoe taarifa zako binafsi kama vile namba za akaunti za benki au namba za kitambulisho cha taifa kabla ya mchakato wa mahojiano kinaweza kuwa tangazo feki. Kampuni halali zinapaswa kufanya mchakato wa mahojiano kabla ya kuhitaji taarifa kama hizo.

Tangazo Lisilokamilika: Ikiwa tangazo halina maelezo kamili kuhusu kazi au kampuni, au ina makosa ya kisarufi au ya kiuandishi, basi inaweza kuwa ishara ya tangazo feki. Kampuni halali zitakuwa na maelezo kamili na ya kina kuhusu kazi wanayoitoa.

Mchakato wa Ajira Usio wa Kawaida: Tangazo ambalo linahitaji waombaji kufanya mambo yasiyo ya kawaida kama vile kulipa ada ya maombi au kuhudhuria semina ya malipo kabla ya kupewa kazi ni ishara ya wazi ya tangazo feki. Katika hili pia tangazo feki la kazi huweza kutaka ili kuendelea kutuma maombi basi ulitume kwa watu wengine ili uruhusiwe kwenda hatua nyingine. Kampuni halali hazitatoza ada kwa waombaji wa kazi wala kukutaka usambaze tangazo lao kwa wengine.


Jinsi ya Kuepuka
Chunguza Kampuni
: Fanya utafiti kuhusu kampuni inayotoa tangazo la kazi. Angalia tovuti yao, maoni ya wateja, na habari nyingine mtandaoni ili kujiridhisha kwamba ni kampuni halali.

Pima Uwiano wa Mshahara: Linganisha mshahara unaotangazwa na viwango vya mshahara vya wastani katika tasnia hiyo. Ikiwa mshahara unaonekana kuwa wa juu sana, basi huenda ikawa ni ishara ya tangazo feki.

Usitoe Taarifa zako Binafsi kabla ya muda: Usitoe taarifa za kibinafsi kama vile namba zako akaunti za benki au namba za kitambulisho chako cha taifa kabla ya kujiridhisha kwamba tangazo la kazi ni halali na kampuni ni halali.

Fanya Mawasiliano na Kampuni: Ikiwa una shaka kuhusu tangazo la kazi au kampuni inayotoa kazi, wasiliana nao moja kwa moja kupitia barua pepe au simu ili kuthibitisha uhalali wa tangazo hilo.

Kumbuka daima kuwa makini na tahadhari unapotafuta kazi mtandaoni na epuka kutoa taarifa za kibinafsi kwa watu au kampuni ambazo haujathibitisha uhalali wao.

Kufikia Jukwaa la JamiiCheck, bofya HAPA.
 
Back
Top Bottom