Xinjiang machoni mwangu: Mandhari ya kuvutia ya milima ya Tian Shan mjini Xinjiang yaniacha kinywa wazi

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,014
1,040
2.jpg

Katika safari yangu ya mkoa unaojiendesha wa Xinjiang Uygur, nimebahatika kutembelea kwenye vivutio kadhaa, ila cha kwanza ambacho nina hamu sana ya kukielezea na ambacho kiliniwacha kinywa wazi kwa kushangaa ni mlima maarufu sana wa Tianshan.

Ilituchukua takriban mwendo wa saa mbili hivi hadi kufika kwenye mlima wenyewe, unaweza kuona ni mwendo mrefu lakini njiani tulisimama kidogo na kujionea maporomoko ya maji pamoja na kufurahia mandhari ya kupendeza kabisa. Kama ilivyo maeneo mengi ya utalii nchini China, mipango ya usimamizi imewekwa vizuri na matembezi yameandaliwa kwa mpango maalumu. Katika sehemu ya kuingilia watalii au wageni, yamewekwa mabasi maalumu yanayowapeleka watalii kwenye Ziwa la Tianchi (Ziwa la Mbinguni) ambalo lipo kwenye mlima Tianshan.

Mchanganyiko wa mlima na ziwa unaleta sura ya kipekee. Tian Shan (Milima ya Mbinguni) ambayo inapendeza sana, mandhari yake ya kushangaza iliwachochea hata watunzi wa zamani na kujikuta wanatunga mashairi. Eneo lake lina mvuto mkubwa ambalo limefunikwa na rangi ya kijani. Mwanzo nilipofika na kuangalia milima hiyo nilijua kwamba miti na majani yote ilikuwa ni ya asili yaani iliota yenyewe, lakini loo! Kumbe haikuwa hivyo, baadaye nikatanabahi kuwa ukijani huu haukupatikana bure tu, kwani kwa mujibu wa mtembezaji wetu, mlima huo awali ulikuwa jangwa tupu. Akaendelea kutuelezea kwamba iliwachukua wenyeji miaka thelathini kupanda miti na majani na sasa ukienda unaweza kushangaa kuona milima yote ina rangi ya kuvutia ya kijani. Hali ya hewa kwenye maeneo ya mlima ni baridi kiasi, unaweza kudhani kwamba bado upo kwenye majira ya baridi, lakini hali halisi ni kwamba mimi nimetembelea wakati wa majira ya joto, hivyo kama na wewe utabahatika kutembelea siku moja usisahau kuchukua koti la kujisitiri na baridi.

Baada ya kufika tukaanza kutembezwa kwenye ziwa kwa kutumia boti ndogo ya utalii ili kujionea na kufurahia zaidi mandhari ya asili aliyotujaalia Mungu, huku tukikaribishwa chai ya maziwa na lozi, zabibu na jujube (tende). Ili kuhakikisha eneo hili la urithi wa dunia linaenziwa, mamlaka zimepiga marufuku shughuli za ufugaji, na uvuvi na badala yake watu hao wamepatiwa kazi nyingine za kufanya, ni rahisi kwasababu sasa mkoa wa Xinjiang umeendelea na una fursa nyingi za ajira kama vile viwandani, kwenye kampuni n.k.

Kusema kweli hii ni safari ambayo niliifurahia sana, hasa baada ya kuona hamasa ya wenyeji ya kutunza mazingira huku wakiingiza fedha kutokana na vivutio hivyo. Kama jina la mlima au ziwa linavyoitwa yaani Ziwa la Mbinguni, ni kweli ukienda utajihisi kama upo peponi kwani mazingira yake yanakufanya utulize akili na moyo pia.

Kwa siku hiyo safari yangu ya matembezi haikuishia hapo, baada ya kupata chakula cha mchana tulifunga safari moja kwa moja hadi kwenye kampuni ya pamba ya rangi ya Xinjiang. Kama nilivyosema awali kwamba huu ni mkoa uliobarikiwa na Mungu kwani una hazina nyingi sana. Najua wengi wetu tumezoea kuona pamba nyeupe ikiota mtini kwake. Kama pamba ina rangi nyingine basi tuliamini kwamba labda imepakwa rangi. Lakini pamba ya hapa Xinjiang yenyewe haiko hivyo, kwani kuna baadhi ambazo si nyeupe na rangi yake ni ya asili na wala sio ya kupakwa.

Kampuni hii inalima na kuvuna pamba za rangi mbili, yaani rangi ya kahawia na rangi ya kijani. Na hizi za rangi ya kahawia pia zipo za aina mbili yaani kahawia iliyokoza na nyepesi. Hii ni pamba ambayo ina ubora wa hali ya juu, na uzuri wake ni kwamba ina mchango mkubwa katika kuzuia uchafuzi wa mazingira. Kwa mujibu wa mhusika aliyetukaribisha kwenye kampuni hiyo, kwa mwaka jana pekee mavuno yake yalifika tani elfu 51.6. Na kazi ya uvunaji kwa kiasi kikubwa inafanywa na mashine na kiasi fulani inafanywa na watu. Kwani tunafahamu kuwa mashine haiwezi kufanya kazi zote kuna baadhi ya kazi ambazo lazima zitamhitaji binadamu.

Baada ya kutupa maelezo ya kina kuhusu uendeshaji mzima unavyokuwa na kufahamishwa jinsi pamba inavyovunwa hadi kutengezwa nyuzi au bidhaa nyingine, tulitembea duka la maonesho ya bidhaa za pamba kama vile, taulo, nguo za watoto, foronya za mito, fulana, nguo za ndani hata midoli pia, n.k na sisi angalau tukapata kufanya manunuzi ya bidhaa hizo adimu.

Kwa hiyo nikiwa bado naendelea kufahamu na kuelimika na mambo mengi mazuri ya mkoa huu wa Xinjiang, pia kwa upande wa pili nafurahia na kuburudika na safari nzima, kwani wahenga wanasema “kazi na dawa” kweli nipo kazini lakini ndani yake napata burudani safi kabisa.
 
Back
Top Bottom