Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,354
- 33,192
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda Nora Damian JUMLA ya watumishi wapya 9,000 wanatarajiwa kuajiriwa mwaka huu katika sekta ya afya kuziba pengo la uhaba wa watumishi linalozikabili halmashauri nyingi nchini. Akizungumza Dar es Salaam jana wakati wa mkutano wa 12 wa wadau wa sekta ya afya kuhusu tathmini ya huduma za afya nchini, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda alisema wizara hiyo ina uhaba wa asilimia 42 ya watumishi. Tunaandaa mazingira ya kuweka vivutio vya ziada kama mishahara posho na nyumba, ili kuwafanya watumishi wetu wasikimbie vituo vyao vya kazi,alisema Dk Mponda. Alisema wizara yake ina changamoto nyingi katika kutoa huduma zilizo na uwiano, zitakazomfikia kila mtu na kwamba wameongeza udahili kwa wanafunzi wanaochukua masomo ya afya na wataajiriwa watakapomaliza masomo yao. Alisema kwamba, maeneo mengi yenye mazingira magumu nchini ndiyo yanaongoza kwa kuwa na uhaba mkubwa wa watumishi. Hata hivyo, alisema watumishi wengi wamekuwa hawaripoti kwenye vituo wanavyopangiwa hasa katika maeneo hayo ambako kati ya mwaka 2007 hadi 2010 asilimia 37 ya watumishi hawakuripoti kwenye vituo vyao vya kazi. Waziri huyo alisema changamoto nyingine inayowakabili ni vifo vya uzazi pindi mama anapokuwa mjamzito hadi anapojifungua na mtoto wake. Licha ya changamoto hizo, waziri huyo alisema pia wamepata mafanikio makubwa hasa katika kupambana na magonjwa mbalimbali kama malaria, kifua kikuu, virusi vya ukimwi na ukimwi ambapo maambukizi yamepungua kutoka asilimia 12 mwaka 1990 hadi asilimia 5.6 mwaka huu. Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika lisilo la kiserikali lijulikanalo kama (Sikika) Irenei Kiria akizungumza kwa niaba ya asasi za kiraia, aliitaka serikali kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kama ya sherehe safari na posho na kutenga fedha za kutosha katika sekta ya afya ili kuokoa wananchi. Katika bajeti ya mwaka huu wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imetenga Sh 515 milioni kwa ajili ya sherehe fedha ambazo zinatajwa kuwa zingeweza kuhudumia afya za wananchi. Alisema serikali imekuwa haitengi fedha za kutosha katika sekta ya afya kwa kisingizio kwamba ina wafadhili wengi ambapo katika bajeti ya mwaka huu, asilimia 97 ya fedha zimetolewa na wafadhili huku serikali ikichangia asilimia tatu. Kama serikali inawaachia wafadhili maana yake inajiondoa katika jukumu lake la kikatiba la kuhudumia wananchi,alisema Kiria. Alisema serikali inakwenda kinyume na mkataba wa Abuja wa mwaka 2001 ambao unaelekeza nchi wanachama kutenga asilimia 15 ya bajeti katika matumizi ya sekta ya afya. Alisema pia bajeti ya afya imekuwa ikishuka siku hadi siku ambapo kwa mwaka 2010/11 ilikuwa asilimia 11 lakini mwaka 2011/12 imeshuka hadi kufikia asilimia 8.9. Asasi hizo pia zililalamikia serikali kwa kushindwa kuajiri watumishi wa afya wa kutosha kama inavyoombwa na halmashauri husika na uhaba wa mashine za kupima chemchembe za damu kwa waathirika wa virusi vya ukimwi maarufu kama CD4. Kiria alisema baadhi ya wilaya nchini kama za Misenyi, Sumbawanga na Temeke zilipelekewa watumishi wachache tofauti na idadi waliyoomba. |
chanzo: Gazeti la Mwananchi