‘Watanzania wanyonge’ wataka Paul Makonda agombee na kupewa Urais 2030

Lucas Mwashambwa

JF-Expert Member
Jul 28, 2022
15,302
9,729
Ndugu zangu Watanzania, uchapakazi wa Mheshimiwa Makonda, ujasiri wake, uzalendo wake, kujitoa kwake kutetea wanyonge, ushupavu na umadhubuti wake umewakosha na kukonga mioyo ya Watanzania mitaani.

Ambao kwa sasa wana kiu ya kutaka kuona Paul Makonda anagombea urais na kuchaguliwa kwa kishindo kumpokea kijiti cha urais Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan mwaka 2030.

Sauti zinaendelea kupazwa na wananchi kupitia mitandao ya kijamii, vyombo vya habari, sauti za wananchi vilingeni na magengeni kuona kuwa siku moja Taifa hili linawekwa mikononi mwa Paul Makonda kama mkuu wa nchi, kiongozi wa serikali na Amiri Jeshi Mkuu wetu.

Kutokana na kuona namna anavyochapa kazi bila kuchoka wala kupumzika, wala kupata hata muda wa kula chakula cha mchana. Muda wote yupo kazini kuwasikiliza wananchi kwa unyenyekevu na upole wa hali ya juu sana na kuchukua hatua papo kwa papo kwa kuwaita watu wa serikali kutoa majibu.

Nami naunga mkono kuwa ili kazi nzuri anazofanya Mheshimiwa Rais ziwe na muendelezo mzuri na kuendelea kwa kasi hii hii, basi ni vema mwaka 2030 kumpa ushirikiano na kumuunga mkono Paul Makonda kushika nchi.

Kwa hakika ndugu zangu, nawaambieni ya kuwa kwa huyu mwamba na jasiri kuwahi kutokea kusini mwa jangwa la Sahara, hakika nchi itakwenda mchaka mchaka katika maendeleo.

Maendeleo yatakimbia kwa kasi na kukimbizwa kama mashindano ya mbio ndefu, watumishi wa umma watachapa kazi kama nyuki, cheo kitakuwa dhamana na wananchi watabaki mabosi huku kila mtu akifurahia kuzaliwa Tanzania kama ilivyo sasa chini ya uongozi wa Rais Wetu Mpendwa, Kipenzi cha Watanzania, Mama Samia Suluhu Hassan.

Jiulize kama leo ni Mwenezi wa Chama anaitetemesha na kuiteka nchi kiasi hiki kwa uchapakazi wake, vipi tukimpa Urais ili aendeleze pale alipoishia mama yetu mpendwa na mchapa kazi aliyetukuka? Kwa sababu ni lazima anapotoka mchapa kazi kama Mama Samia, tukakikishe nchi inakwenda katika mikono ya mchapa kazi na jasiri aina ya Makonda ili kazi zisisimame na kusua sua.

Tanzania inamhitaji sana Mheshimiwa Paul Makonda 2030 kuliko wakati mwingine wowote ule. Ndio maana jana nilisema alindwe kwa nguvu zote na gharama zozote zile ili aje kutupatia matokeo makubwa na chanya Watanzania. Tuendelee kumuombea afya njema tu.

Ni lazima Makonda aandaliwe na kuwekwa tayari kwa nafasi za juu, maana amejaliwa kipawa na kalama ya uongozi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Nyote mnajionea namna kifua chake kilivyojaa ujasiri wa hali ya juu.

Angalieni namna mchaka mchaka unavyopigwa huko kwenye ziara zake, angalieni namna watu nyuso zao zilivyo na tabasamu zimuonapo Paul Makonda, angalieni namna watu wanalivyo na imani na matumaini na Mheshimiwa Makonda. Hapo hata mwaka mmoja tu hajamaliza ofisini.

Vipi akipewa miaka kumi kama Rais wa nchi? Mnafikiri Tanzania hii ya Rais wetu mpendwa Mama Samia itakuwa wapi? Ikumbukwe kwanza atakuta kazi kubwa imefanywa na Mheshimiwa Rais Mama Samia, ambapo atakuta umeme ni wa uhakika baada ya kuwa tayari bwawa la Mwalimu Nyerere limeshakamilika.

Mnafikiri nani ataipita kiuchumi Tanzania hii yenye rutuba nzuri ya kutosha na yenye kukubali kila aina ya mazao, yenye mlima mrefu barani Afrika, yenye mbuga za wanyama wa kila aina, yenye madini ya Tanzanite yanayopatikana Tanzania pekee, yenye madini ya kutosha karibu kila ukanda, yenye rasilimali watu ya kutosha, yenye mito, maziwa na bahari kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na hata usafiri wa majini.

Yenye bandari kila kanda, yenye faida ya kuzungukwa na nchi zaidi ya saba ambazo zinategemea kupitishia mizigo yao katika bandari yetu, yenye misitu mingi kwa ajili ya kutengenezea vitu vya aina mbalimbali badala ya kuagiza nje na hivyo kupunguza hazina ya pesa za kigeni. Mnafikiri Tanzania ya kijana jasiri na imara mwamba Paul Makonda itakuwaje?

Mnafikiri Tanzania ya Makonda yenye utajiri wa makaa ya mawe ya kutosha, vivutio vya utalii, kimondo cha pili kwa ukubwa duniani baada ya kile cha Marekani, hamuoni Tanzania hiyo itatiririsha maziwa na asali katika mabomba yake kwa kila kaya? Kumbuka, kwa sasa anachofanya Rais Samia ni kuweka misingi mizuri ya kiuchumi, ambapo ni wakati huo wa Urais wa Makonda miradi ya kimkakati itakuwa imeanza kutoa na kuleta faida.

Tujiandae kumpa nchi Mheshimiwa Paul Makonda mwaka huo wa 2030 ili dunia ikae chini na kuishangaa Tanzania ikipaa kama ndege vita kiuchumi, na kupokea wageni watakao kuwa wanapanga foleni na kupishana pale airport wakija kuitembelea Tanzania na kujifunza.

Paul Makonda, chapa kazi sana kaka yangu. Mama amekuamini na anaimani na matarajio makubwa sana kutoka kwako. Chama tunakuamini sana na tuna matarajio makubwa sana kutoka kwako.

Chapa kazi na kila upitapo waambie wananchi na Watanzania mambo makubwa aliyoyafanya mama yetu na Rais wetu Mama Samia. Waeleze mabilioni aliyoyapeleka katika maeneo yao. Waambie kila mwezi mama yao na Rais wao anatoa zaidi ya bilioni 33 ili watoto wao wasome bure.

Waambie Rais wao ametiririsha zaidi ya trilioni sita katika sekta ya afya pekee, waambie Rais wao ameongeza bajeti ya kilimo kufikia bilioni mia tisa tisini ili wakulima wapate pembejeo kwa bei nzuri, waambie mama yao ameagiza zaidi ya tani laki moja za sukari kuja kuingiza sokoni, waambie mama yao anawapa mikopo wanafunzi wote wa elimu ya juu wenye sifa bila ubaguzi.

Waambie mama yao ametoa maelfu ya ajira kwa vijana na muda siyo mrefu anakwenda kumwaga mitaani zaidi ya elfu ishirini na tatu katika sekta ya elimu na afya.

Waambie watumishi wa umma wachape kazi, maana mama yao yupo pamoja nao na ataendelea kuwaongeza mishahara na kuwalipa madai yao, lakini nao wahakikishe kuwa wanachapa kazi kwa bidii na uadilifu wa hali ya juu na wasifanye kazi kwa mazoea. Waambie mama amefanya mengi ambayo huwezi kumaliza kuyataja.

Kazi iendelee, mama ametufikia na kuwafikia Watanzania kwa utumishi wake uliotukuka wa kugusa maisha ya Watanzania wanyonge wasio na sauti.

Lucas Hebel Mwashambwa, kijana mzalendo na mpenda nchi yangu.

0742-676627.
 
Back
Top Bottom