Rutashubanyuma
JF-Expert Member
- Sep 24, 2010
- 219,470
- 911,174
Ushuru wa maegesho sasa mpaka ufukweni
Imeandikwa na Oscar Job; Tarehe: 14th January 2011 @ 23:30
KAMPUNI ya Maegesho ya Taifa (NPS), imeanza kukusanya mapato ya uegeshaji katika eneo la ufukwe wa bahari ya Hindi eneo la Coco, Oystebay katika Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, kufuatia agizo lililotolewa na halmashauri ya Jiji.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Hassan Khan, utaratibu huo umeanza rasmi Januari 7 mwaka huu baada ya kupata za kimaandishi, ikiagiza kampuni hiyo kuanza kukusanya mapato kutoka eneo hilo kama ilivyo kwa maeneo mengine ya Jiji.
Khan alisema kuwa, wakati huu ambapo kampuni yake ikiendelea na shughuli zake kama kawaida za ukusanyaji mapato maeneo ya katikati ya Jiji, wamepokea barua hiyo ikiwataka kuifanya kazi hiyo eneo la Coco kwa muda wa saa nne kwa siku.
Ni vyema wananchi wakatambua kuwa kuanzia sasa kampuni hii ya maegesho itaanza kukusanya ushuru wa uegeshaji katika eneo hilo katika hatua ya utekelezaji wa agizo la halmashauri ya Jiji ndani ya mpango wake wa ukusanyaji mapato, alifafanua Khan.
Aidha Khan amewataka wananchi kujihadhari na watu wanajifanya kuwa ni wafanyakazi wa kampuni hiyo na kujishughulisha na ukusanyaji wa mapato huku wakitumia tiketi bandia zinazofanana na tiketi zake na kujipatia fedha kwa njia hiyo.
Katika hatua nyingine, kampuni hiyo imeanza kutumia mashine zake mpya maalumu kwa ajili ya ukataji tiketi za maegesho huku ikielezwa kwamba, zitasaidia kudhibiti mapato yatokanayo na ukusanyaji wa ushuru huo.