X-PASTER
JF-Expert Member
- Feb 12, 2007
- 11,610
- 1,810
WE THIO LAFKI YANGU TEENA!
NILIRUDI nyumbani jioni baada ya mizunguuko yangu ya kimaisha. Kwa kawaida mwanangu mdogo, Lubna, (jina la kitoto tunapenda kumwita Lu), hunikimbilia kwa shangwe kuja kunipokea, lakini siku ile nilishangaa alikuwa "kauchuna". Nikamuuliza: "Lu, vipi mwanangu?" Kimya! "Hujambo?" Kimya!
Baada ya kumhojihoji ili kumdadisi nifahamu tatizo lilikuwa nini, alitoa maneno ya ukali akisema: "We thio lafki yangu teena!"
Waliokuwepo waliangua kicheko na kusema tu, "Lu bwana!"
Nilimuuliza kwa nini mimi sio rafiki yake, nikagundua sababu. Kumbe nilikuwa nimemfinya asubuhi kabla sijaenda kazini, kwa sababu alikuwa hataki kwenda shuleni (chekechea) eti kwa sababu alikuwa amechoka sana ile asubuhi.
Nilichokifanya ni kutoa kafuko ambako ndani kalikuwa na vituvitu vya kutafuna, kama ilivyo kawaida nikirudi nyumbani. Nikasema: "Sawa kama mimi thio lafki yako".
Lu alipoona kale kafuko akajua mna vitu. Akawa anatafuta suluhu. Akaja mbio huku akisema: "Thalamaleku, baba!" Waliokuwepo wakaangua kicheko tena. Bila ya kuwajali waliokuwa wakicheka, alisema: "Nilikuwa nadanganya tu baba, wewe ni lafki yangu".
Kwa nini alifanya hivyo? Alijua kwamba uadui wake kwangu ungemkosesha maslahi, walau kwa kipindi kile kifupi cha neema.
Wengi waliokuwepo waliangua kicheko tu, wakiishia kusema: "Lu bwana!...Watoto bwana!... blah...blah...blah! Lakini kwa watu wa fasihi kila tukio lina maanisho (implication) katika maisha, na vile vile kwa watu wa fasihi maisha yote ni tamthilia (drama), unaweza kuyafanyia uchambuzi. Nilikuwa nafikiria niandike nini kwenye JF Leo, lakini tukio lile dogo kwangu likawa na maanisho kubwa zaidi katika maisha yetu leo kuliko wale waliokuwa wakicheka tu walivyolichukulia.
Juzi hapa kuna kigogo mmoja wa chama fulani alikuwa amealikwa na chama tawala kuhudhuria mkutano mkuu wa Chama hicho Kizota, Dodoma. Alishangiliwa sana na wana CCM kwa nyimbo na vigelegele... Na inasemekana kuwa amesema kwamba CCM haikamatiki. CCM Chama Kubwa... Sasa baadhi ya wapinzani wanajiuliza, amesalimu amri!?
Kwani mwaka 1995 alishindwa, mwaka 2000 aligaragazwa na Mh. Mkapa, na mwaka 2005 ndio kabisaa Kikwete akammaliza. Hivyo CCM ni chama imara, hakishikiki. "Kweli CCM inagaragaza upinzani".
Mheshimiwa wa inji hii inasemekana aliongeza, "Kila mwaka wa uchaguzi inakula kwangu, sasa nimechoka" alisema kwa hamasa huku akiendelea kuisifia CCM na uongozi wake.
Kwa maneno yake amesema, hana sababu ya kuacha kumsifia Rais Kikwete kwani ndiye Rais pekee anayemjua. Amefanya kazi kubwa sana katika kipindi cha miaka mitano hususan katika harakati za kupambana na ufisadi na mafisadi nchini.
Zile hasira zake kwa chama tawala wakati ule zilikuwa za kweli au ilikuwa ni ile ile "we thio lafki yangu teena!"
Sasa hivi kila kona unayokwenda watu wanalalamika hali ngumu za kimaisha, ufisadi kila mahala. Utamkuta mtu jicho limemtoka: "Hatukubali. Ngoja elfu mbili na kumi inakuja. Huyu sasa basi. Mimi kura yangu kwa dk Maslaha tu safari hii. Eeh, ndio! Mfxyz%£*&! Kshxnz$!!! kabisa! Blah...blah...blah...!"
Ukimkuta mtu utadhani mkali kweli, lakini ngoja fulana na vitenge vitolewe. Ona watu watakavyobadilika rangi. Angalia watu watakavyorudisha kadi na kuomba radhi. Cha kuchekesha, wengine ni wasomi wazuri na pia wapo wanasiasa wenye wafuasi wengi tu... Wapo pia mashehe na maaskofu. Wakati wa kaneemeka kwa muda mfupi ndio waja huo.
Ukiwa nje ya mchezo ndio unafaidi. Miye sina chama lakini ninapo pa kupiga kura. Usiniulize wapi, kwa sababu wenye busara zao wameshatupa uhuru wa kuchagua tunapopapenda. Nauliza tu wale wanaojidai wana hasira, hasira hizo ni za kweli au ni zile zile za "We thio lafki yangu teeeeeena!" Vifuko vikitolewa tu, "Thalamaleku baba!"
Haya, tutaona!