Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,410
- 33,290
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka (kulia), akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana. (PICHA: OMAR FUNGO)
Tanzania imetangaza kuwasilisha maombi Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa (UN), jijini New York, nchini Marekani, kudai umiliki wa eneo la ziada nje ya maili 200 za Ukanda wa Kiuchumi Baharini (EEZ) katika Bahari Kuu ya Hindi, ili iweze kulifanyia utafiti zaidi kuhusu rasilimali zilizoko chini ya bahari kwa lengo la kuinua uchumi wa nchi.
Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, rasilimali hizo ni pamoja na mafuta, gesi na madini.
Eneo hilo linatokana na ongezeko lingine tena maili 150 na hivyo kufanya jumla ya mpaka hadi maili 350, ambazo ni sawa na kilomita 560 kutoka kwenye baseline.
Waziri Tibaijuka alisema maombi hayo yanatarajiwa kupelekwa na jopo la wataalamu kutoka Tanzania Bara na Zanzibar na wajumbe wawili kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, litaongozwa na Waziri Tibaijuka.
Alisema wanatarajia kuwasilisha andiko la utafiti wa kisayansi la kudai eneo hilo katika Shirika la UN Linaloshughilikia Mikataba Sheria za Baharini (UNCLOS) kesho na kwamba, baadaye Aprili, mwaka huu, watakwenda tena UN kutetea andiko hilo.
Alisema baada ya kutetea andiko hilo huko UN, Kamisheni ya Masuala ya Baharini itafanya uamuzi kuhusu maombi yao na kwamba, anaamini hatua waliyoifikia watafanikiwa.
Waziri Tibaijuka alisema kazi ya kukamilisha andiko hilo iliyoanza mwaka 2007 na kugharimu zaidi ya Sh. bilioni 5.2, imesimamiwa na wizara yake na tafiti zimefanyika kwa kutumia wataalamu kutoka sekta za ardhi, maji, mawasiliano, sayansi na teknolojia, sheria na wataalamu wa masuala ya baharini kutoka vyuo vikuu.
SOURCE: NIPASHE