LEGE
JF-Expert Member
- Oct 14, 2011
- 5,123
- 9,168
MISS TANZANIA
SEHEMU YA KWANZA
MTUNZI: PATRICK .C.K
==========
Haki zote zimehifadhiwa hairuhusiwi kunakili, kuchapa maandiko ya kitabu hiki bila idhini ya wahusika wakuu.
“Patrick amka darling, inakaribia saa nne sasa”, alisema Veronika kwa sauti laini ya kubembeleza.
“‘Mmmmhhh” Akaguna Patrick ,akajigeuza upande wa pili na kulivuta zaidi shuka.
“Amka ukaoge” Alizidi kubembeleza Veronika. Kwa uvivu Patrick akaamka na kuelekea bafuni kuoga.Dakika chache baadae alitoka akiwa amechangamka.
"Kweli maji ni dawa nzuri ya uchovu. Sasa najisikia safi kabisa.Nadhani kwa sasa itabidi nipunguze muda wa kufanya kazi. Nimekuwa nikifanya kazi kwa masaa mengi sana kwa siku kiasi kwamba nakosa hata muda wa kupumzika. Naogopa tukija kuoana nisije kushindwa kutimiza majukumu yangu kama mume kwa sababu ya uchovu” akasema Patrick na kumfanya Vero atabasamu halafu akatoa kicheko cha chini chini na kusema.
“Kweli mpenzi jitahidi kwa sasa kupata muda wa kutosha wa kupumzika.”
“Nitajitahidi baby”
Baada ya kuhakikisha sasa yuko safi Vero akamshika mkono Patrick na kumpeleka sebuleni kupata stafstahi.
“Patrick dear nataka unisindikize Supermarket nikafanye manunuzi ya vitu vya ndani. Si unajua kesho Andrew na vicktoria wameahidi kututembelea”Akasema Veronika wakati wakiendelea kupata chai.
“Mhh! Vero nenda mwenyewe mimi niache nipumzike".Patrick akajibu.
“Jamani dear usifanye hivyo naomba unisindikize ,mimi naona uvivu kwenda peke yangu”
"Haya mama, tumalize chai twende ili tuwahi kurudi”
“Nashukuru dear”.
Katika vitu ambavyo Veronika alibarikiwa kuwa navyo ni uwezo wake mkubwa wa kushawishi.
* * * *
Veronika Rugi alikuwa ni msichana mrembo mwenye mvuto wa aina yake.Binti huyu licha ya kujaliwa kichwa kizuri chenye nywele laini, nyingi na ndefu, alikuwa na uso mpana wa mviringo ulionakshiwa na macho mapana yenye kurembua muda wote.
Midomo mizuri ,laini ambayo akikupiga busu hutatamani abanduke mdomoni. Mtoto huyu alijaliwa shingo murua ambayo iliungana na kiwiliwili kilichokuwa na kifua chenye kupendeza kilichobeba chuchu changa zenye kusisimua,zenye kuwatoa udenda wakware. Kimwana huyu mwenye uzuri usiopimika alijaliwa umbo la utatanishi kuanzia kiunoni kushuka chini. Ni wasichana wachache sana waliopewa upendeleo wa namna hii na manani..
Pamoja na sifa hizo zote za nje lakini bado alikuwa na sifa lukuki za ndani.Kikubwa zaidi kinachomfanya apendwe na kila mtu ni uwezo wake mkubwa wa kuelewa mambo.Ni binti mwenye roho nzuri ya huruma na upendo asiyependa kujivuna wala kujikweza licha ya uwezo mkubwa familia yake ilionao.
Ni binti mwenye heshima kwa watu wa rika zote ,mcheshi,asiyependa ubinafsi na zaidi ya yote ni mtu anayejua kupenda. Veronika ambaye bado anaishi na mama yake mzazi baada ya baba yake kufariki miaka kadhaa iliyopita ,alikuwa ni mtoto wa tatu na wa mwisho katika familia ambayo haikubahatika kuwa na mtoto wa kiume.
Dada mkubwa wa Veronika aliyeitwa Loniki hivi sasa anafanya kazi katika shirika la ndege la British airways ,ameolewa na anaishi nchini Uingereza.
Mtoto wa pili kuzaliwa katika familia hii ni binti mrembo sana Sarah ambaye aliwahi kushika nafasi ya tatu katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa.naye amekwishaolewa na ni afisa mahusiano wa benki moja mpya kabisa nchini iitwayo African meckat bank.
Mtoto wa tatu na wa mwisho ni Veronika ambaye bado hajaolewa ,ila alikuwa katika hatua za mwisho za kukamilisha maandalizi ya ndoa yake na mchumba wake Patrick.
Ni hivi karibuni tu amehitimu shahada yake ya kwanza ya biashara katika chuo kikuu cha dar es salaam.Yeye ndiye msimamizi mkuu wa miradi yote ya familia kwa sasa.
* * *
“Patrick mpenzi nilisahau kukwambia toka mapema kuwa dada Loniki alifurahi sana kusikia tunataka tukafanye shopping ya harusi yetu nchini Uingrereza. Ameahidi kuwa yeye na mumewe watagharamia safari nzima ya kwenda na kurudi na gharama zote za
manunuzi. Amesisitiza kuwa tusitumie hata shilingi yetu. Kwa maana hiyo wiki hii nataka niende tena kufuatilia yale maombi yetu ya viza pale ubalozini. Nadhani kama Mungu akijaalia basi ndani ya wiki mbili zijazo tutakuwa tumeshakamilisha taratibu zote zinazotakiwa.” Alisema Vero huku akijiegemeza karibu zaidi na kifua cha Patrick.
Muda huo ilipata saa mbili za usiku , bado walikuwa wakipunga hewa safi baada ya mlo wa jioni.
“Wow! Hongera sana Vero kwa kuwa na ndugu wakarimu na wenye upendo wa hali ya juu sana kama ulivyo wewe. Tena umeongea kuhusu Loniki nimekumbuka zile CD alizonitumia wiki iliyopita. Unajua sijatazama hata moja.Hebu twende ndani nikaitazame ile filamu mpya ya Jack bauer.”
Akasema Patrick huku akijiinua toka pale walipokuwa wameketi na kuelekea sebuleni. Vero naye akakusanya vitu vyote vilivyokuwapo chini naye akaingia ndani.
“Vero mbona ile CD ya Jack bauer siioni hapa au Andrew aliichukua?Akauliza Patrick baada ya kuitafuta CD ile bila kuiona.
“Yawezekana Andrew aliichukua kwa sababu siku ile aliing’ang'ania sana.Nakumbuka kuna CD alizichukua hapo nadhani na hiyo nayo ilikuwapo”. Akasema Vero
Patrick akalifunga kabati ,akaelekea katika friji akafungua na kujimimia Juice katika glasi. Vero alikuwa ameketi sofani akitazama Luninga.
“Patrick , Miss Tanzania mwaka huu itakuwa na ushindani mkubwa sana kwa sababu mabinti ni warembo kupita maelezo. Mhh………..” Akasema Vero huku amekodoa macho yake katika Luninga kubwa iliyokuwamo humo sebuleni.
“Kwani fainali za miss Tanzania ni lini?” Patrick akauliza
“Ni jumamosi ijayo na itafanyikia pale Diamond Jubilee. Kutapambwa na onyesho kali la Malaika band,vile vile wana Fm academia na wasanii wengine kibao watakuwepo.Nataka kesho nikakate tiketi zetu za V.I P ili tusikose nafasi siku hiyo” Alisema Vero.
Akiwa na juice yake mkononi Patrick akajisogeza taratibu kuelekea mahali alipokaa Veronika . Kabla hajafika sofani alisimama akapiga funda la juice kisha akaelekeza macho yake katika luninga
“Naitwa Neema, ni mrembo toka kanda ya kaskazini. Ni miss Arusha. Napendelea sana muziki wa dini, kusoma na michezo mbali mbali. Nategemea kuwa mwanamitindo wa kimataifa. Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitajikita zaidi katika kuwasaidia watoto yatima kwani naelewa mateso na machungu wanayoyapata kwa kutokuwa na wazazi wao. Naombeni kura zenu namba yangu ya ushiriki ni ishirini.”
Alikuwa ni mrembo wa Arusha akijinadi katika kipindi maalum cha kuwatambulisha washiriki wa kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Tanzania kilichorushwa moja kwa moja na televisheni ya Taifa.
“Du! Si mchezo” Aliguna Patrick huku akiisogelea zaidi Luninga
“Nimekwambia Patrick warembo wa mwaka huu si mchezo. Hebu kaa uangalie jinsi watoto walivyo wazuri ” Akasema Vero.
“Naitwa Happy Kibaho. Ni mrembo wa wilaya ya Ilala. Napendelea sana muziki laini,kusoma hadithi ,magazeti, kutazama luninga,na wanyama. Nategemea kuwa mwanasheria .Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitaelekeza nguvu zangu zote katika kuwasadia vijana wajasiria mali ikiwa ni pamoja na kuwatafutia wafadhili, nitaitumia kofia yangu kuiomba serikali ielekeze nguvu zake zaidi katika kuwasaidia vijana hawa katika kuwapatia mitaji na kuwatafutia masoko ya bidhaa zao wanazozizalisha ili kupambana na ongezeko la vijana wasiokuwa na ajira. Ninaomba kura zenu ili niweze kulitwaa taji hili la miss Tanzania kwani nina vigezo vyote vya kulitwaa taji hili. Namba yangu ya ushiriki ni 6.”
“Whaaaat!!!!........................” Patrick Akapiga ukelele mkubwa “Nooooooooooo!!..I cant bel……………………” ghafla glasi aliyoishika ikamponyoka ikaanguka na kuvunjika. Taratibu nguvu zikaanza kumwishia akadondokea sofani kisha akapoteza fahamu.
“Patrick , Patrick what’s wrong!!!...”Alihamaki Veronika huku akimsogelea Patrick pale sofani na kumtingisha.
“Patrick darling what’s wrong with you? Alizidi kuuliza Vero huku akimtingisha.
“Ooh ! Nooo...!!!!...Wake up Patrick” Alipiga ukelele baada ya kugundua kuwa Patrick hakuwa na fahamu. Vero akataharuki asijue afanye nini. Hakukuwa na mtu yoyote wa karibu ambaye angeweza kumsaidia .
Alitoka kutaka kwenda kuwaita majirani ,akafika mlangoni na kurudi tena ndani mpaka sofani alipolala Patrick.
“Patrick ! Patrick dear what’s wrong with you. Whats’s wrong Patrick!!!!!!!!!” Vero aliongea peke yake huku machozi yakimtiririka.
Pale pale akapata wazo la kumpeleka Patrick hospitali. Kwa nguvu zake zote akamuinua Patrick na kumpakia garini , akakimbia kufungua geti kisha akaingia garini na kuondoka kwa kasi ya ajabu pasi na kufunga mlango wowote wa nyumba. Kwa kasi ya ajabu Vero aliendesha gari hadi hospitali ya karibu maarufu kama Dr Heneriko hospital. Si mbali sana na makazi ya Patrick.
Huku akilia akapaki gari na kuingia ndani ,akawaomba msaada wauguzi .Haraka haraka wauguzi wakamchukua Patrick na kumuwahisha katika chumba maalum kwa ajili ya kumpatia huduma ya haraka.
“Hurry up !.hurry up.! Ooh Patrick what’s wrong with you?” Alilalamika Vero huku akiwaomba manesi waharakishe. Muda wote huo machozi hayakumkauka. Veronika alizuiliwa asiingie katika chumba cha huduma ya kwanza akaachwa hapo nje na mmoja kati ya manesi akiendelea kumfariji.
“Jipe moyo dada yangu Patrick atapona tu. Mtumaini Mungu.” Nesi yule alimbembeleza Vero kwa upole. Dakika kama 20 hivi baadae dokta Heneriko alimwita Vero ofisini kwake na kumuomba awe mvumilivu wakati wakiendelea kuishughulikia hali ya Patrick.
Dokta alitaka kufahamu nini hasa kilichopelekea Patrick kupoteza fahamu.
“Unajua dokta , Patrick ni mpenzi wangu na tuko katika maandalizi ya harusi yetu. Mimi siishi naye kwa sasa ila huja kwake kila mwisho wa wiki. Leo hii toka asubuhi alikuwa akilalamika kuwa alihisi uchovu mwingi . Tulitoka kidogo kisha tukarudi na akaendelea kupumzika. Usiku tukiwa sebuleni tukiangalia Tv nikaona mwenzangu akipiga ukelele akaishiwa nguvu na kuangukia sofani akapoteza fahamu. Kwa kweli sina hakika mpaka sasa ni kitu gani hasa kilichopelekea hali ile kutokea. Naomba Dokta ufanye kila linalowezekana ili Patrick apone. Niko tayari kutoa kiasi chochote cha pesa ili mradi apone.” Vero alishindwa kujizuia akaangua kilio.
“Nyamaza Vero, Hali ya Patrick inaendelea vizuri. nina hakika muda si mrefu atazinduka. Kwa hiyo yawezekana kuwa kuna habari yoyote aliyoitazama ambayo ilimpelekea Patrick kupata mstuko?
“Sidhani dokta kwa sababu wakati tunaangalia Tv hakukuwa na taarifa yoyote ya kutisha au kustusha inayoweza kupelekea mtu kupata mstuko hadi kupoteza fahamu. Tulikuwa tukiangalia washiriki wa miss Tanzania wakijinadi. Ni hilo tu” Vero akajibu.
Dokta Heneriko akanyamaza kimya kwa sekunde kadhaa kisha akasema,
“Kwa kumbukumbu zako toka umekuwa naye kuna siku yoyote tukio kama hili limewahi kumtokea zaidi ya leo?
“Hapana dokta tangu mimi nimekuwa naye halijawahi tokea tukio kama hili Patrick kupoteza fahamu.”
“Ok Vero hivi sasa waweza kwenda kupumzika na kutuacha sisi tuendelee kumuhudumia mgonjwa wako. Iwapo kutakuwa na mabadiliko yoyote tutakupigia simu kukutaarifu.Na kama itahijika kumuhamisha kumpeleka katika hospitali kubwa zaidi tutakutaarifu pia. Lakini kwa sasa hali yake inaendelea vizuri,mapigo ya moyo wake yako sawa na kila kitu kinaonekana kufanya kazi vizuri. Huu ulikuwa ni mstuko wa kawaida tu ambao unaweza kumtokea mtu yeyote na hasa akiwa na msongo wa mawazo.” Akasema Doctor Henry.
“No Dokta ,siwezi kwenda nyumbani bila kujua hali ya mpenzi wangu iko vipi. Nitalala hapa hapa . Nataka niwe wa kwanza kuniona pindi atakapofumbua macho. Samahani dokta naweza kuitumia simu yako kuongea na mama yangu na kumtaarifu juu ya ugonjwa wa Patrick”
Dokta Heneriko hakuwa na kipingamizi akamruhusu Vero aitumie simu yake. Vero akampigia simu mama yake na kumtaarifu juu ya tukio lile ,halafu akawapigia simu ndugu zake wote bila kumsahau Andrew rafiki mkubwa wa Patrick pamoja na Alois kaka yake Patrick. Wazazi wa Patrick walikuwa safarini nje ya nchi.
* * * *
Ilimchukua kama nusu saa toka Andrew apate taarifa ya ugonjwa wa patrick,kuwasili pale hospitali. Akiwa na mpenzi wake Vick walishuka garini na kukimbia kuelekea mapokezi. Mara tu baada ya kuingia hapo mapokezi walilakiwa na sura yenye kusawajika ya Vero. Alipowaona Andrew na Vick wakiingia humo hospitali Vero aliangua kilio ambacho kiliwachanganya zaidi Andrew na Vick.
“Where is Patrick??” Andrew akauliza huku akijikaza lakini ni wazi alikuwa akitetemeka
“Calm down Vero tuambie Patrick yuko wapi?” Aliuliza tena Andrew .Vick akamkumbatia Vero huku naye machozi yakimtoka.
Andrew alimfuata muuguzi aliyekuwa mapokezi na kumuuliza juu ya hali ya Patrick. Hakuridhika na jibu alilolipata ,kwa kasi akakimbia hadi katika ofisi ya Dokta Heneriko lakini hakumkuta. Taratibu akatoka humo ofisini jasho likimtiririka na kurudi mapokezi.
Tayari Alois kaka yake Patrick alikwisha wasili hapo hospitali akiwa ameongozana na mke wake nao wote waliungana na Vick katika kumbembeleza Vero. Andrew akawasalimia kisha akamvuta mkono alois wakasogea pembeni kidogo.
“Hebu niambie Andrew kitu gani kinachoendelea hapa na Patrick yuko wapi ? Aliuliza Alois huku naye jasho likimtiririka
“Brother Aloia hata mimi mpaka muda huu sielewe chochote kwani toka nimefika hapa muda mfupi uliopita sijaweza kuongea lolote na Vero. Ila kwa maelezo niliyoyapata toka kwa muuguzi ni kwamba Patrick yuko katika chumba cha huduma ya kwanza akipatiwa matibabu. Nasikia ni mstuko ndio uliopelekea akapoteza fahamu”
Mara dokta Heneriko akatokea. Muuguzi aliyekuwapo mapokezi akamtambulisha kwa akina Andrew.
“Dokta hawa ni ndugu zake Patrick wamefika sasa hivi na walitaka kupata taarifa juu ya maendeleo ya mgonjwa wao’.
Dr henry akawasalimu wote halafu akawaomba Alois na Andrew wamfuate ofisini kwake..
“Vijana wangu kwanza poleni sana kwa matatizo ‘ “Ahsante sana dokta tumeshapoa” Wakajibu kwa pamoja
“sasa vijana wangu nimewaiteni hapa ili tuongelee zaidi suala la ndugu yenu.. Patrick aliletwa hapa kwangu usiku huu akiwa amepoteza fahamu. Kwa haraka nikisaidiana na madokta wenzangu tumejitahidi kumpatia huduma ya kwanza na mpaka sasa maendeleo yake ni mazuri. Tumejitahidi kuyashusha mapigo ya moyo yaliyokuwa juu sana na kwa sasa yako kawaida. Taratibu anaanza kurejewa na fahamu zake ingawa bado anahitaji kupumzika zaidi kwani bado fahamu hazijarejea vizuri. Maendeleo yake ni mazuri na baada ya muda mfupi ujao basi atarejea na fahamu zake zote.” Alois akashusha pumzi nzito kwa kusikia taarifa ile ya dokta. Akatoa leso na kujifuta jasho lililokuwa likimtirirka kwa kasi muda huo.
“Thanks God” Alisema Alois huku ameinua mikono juu ishara ya kumshukuru Mungu
“Kwa hivi sasa bado ataendelea kuwapo katika uangalizi maalum mpaka hapo hali yake itakapokuwa nzuri kabisa.Tatizo lililompata ni mstuko wa moyo. Ni tatizo la kawaida kutokea. Ila hali yake itakapokuwa nzuri tutamshauri aonane na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo ili aweze kumfanyia uchunguzi zaidi katika moyo wake ”
Baada ya kupata maelezo ya kutosha toka kwa dokta, Alois na Andrew waliridhika kabisa na dokta akawashauri waende kupumzika mpaka kesho . Alois alikubaliana na wazo hilo lakini akashauri andrew awarudishe kwanza Vero na Vick nyumbani wakapumzike.Yeye atabaki pale kuangalia hali ya Patrick inavyokwenda.
Wakati wakiendelea kujadili mama yake Vero akatokea. Akawasalimu wote aliowakuta hapo kisha kwa wasiwasi akataka kujua juu ya hali ya Patrick. Alipewa maelezo mafupi ya hali ya mgonjwa halafu akaomba aonane na dokta Heneriko, akaongea naye na kupewa kwa muhtasari juu ya hali ya Patrick na maendeleo yake na akahakikishiwa uangalizi wa hali ya juu.
“Ok . sasa utaratibu gani unaoendelea hapa? Aliuliza Bi stella Rugi mama yake na Vero.
“Tumepanga kuwa Andrew awarudishe nyumbani Vero na vick wakapumzike ,mimi nitaendelea kubaki hapa hapa na kufuatilia hali ya mgonjwa” Akasema alois
“Vizuri ,basi msipate shida ,Vero na Vick nitaondoka nao mimi na kwenda nao nyumbani kwangu , Andrew nenda nyumbani kwa Patrick ukahakikishe kuko salama .Alois utaendelea kubaki hapa kumwangalia mgonjwa .Nitakuwa nakupigia simu mara kwa mara ili kujua maendeleo ya mgonjwa ." akasema mama yake Vero
“sawa mama tumekuelewa .” Andrew na alois waliitika kisha wote wakatawanyika na kumwacha Alois hapo hospitali
Saa saba usiku Patrick akarejewa na fahamu zake kamili. Kitu cha kwanza kuhisi ni harufu kali ya dawa akageuza shingo kutazama pande zote akatambua kuwa pale alikuwa hospitali. Taratibu akavuta kumbukumbu za nyuma na mara akakumbuka kitu kilichopelekea yeye kuwepo pale.
“I saw her. I real saw her. she’s alive” Alijikuta akitamka maneno haya huku jasho likikimtiririka na mapigo yake ya moyo kwenda kasi .
Muuguzi aliyekuwa akimuangalia aliingia ndani na kumkuta tayari Patrick amerejewa na fahamu na amekaa kitandani. Haraka akaenda kumwita daktari. Dk heneriko alikuja kwa kasi na kumpima akagundua kuwa bado mapigo ya moyo wa Patrick yalikuwa juu sana.
“‘Lazima kuna kitu kinamsumbua huyu si bure”Akawaza dokta Heneriko.
“Patrick “Dokta akamwita baada ya kumaliza kumfanyia vipimo.
“naam dokta”Aliitika Patrick kwa sauti yenye kukwaruza.
“Pole sana “
“Ahsante sana dokta”
“Patrick kijana wangu usijali utapona tu hali yako inaendelea vizuri. Unahitaji kupumzika sasa mpaka asubuhi tutakapochukua tena vipimo vingine”
“Sawa dokta.” akajibu Patrick
“Endelea pumzika Patrick na iwapo utahitaji kitu chochote muuguzi yuko hapo nje na atakuwa akija hapa mara kwa mara kukuangalia. Tena nimekumbuka kaka yako yuko nje muda sijui kama ungependa kumwona?” Akasema dokta heneriko.
“Ndiyo dokta naomba uniitie..” Dokta Heneriko akafungua mlango na kutoka. Alois alikuwa amesinzia katika sofa lililoko mapokezi Mara akastuliwa na sauti ya Dokta Heneriko.
“Alois ,Patrick amekwisha rejewa na fahamu zake kamili kwa hiyo unaweza kwenda kumwona. Ila tafadhali usijaribu kumuuliza chochote kuhusiana na kilichopelekea yeye kupoteza fahamu. Ongea naye maongezi mengine ya kawaida. sawa?”
“sawa dokta” Alijibu Patrick huku akifikicha macho yaliyojaa usingizi. Muuguzi aliyekuwepo mapokezi akampeleka hadi katika chumba alimolazwa Patrick.
“Vipi Patrick unajisikiaje kwa sasa? Akasema Alois
“Sasa hivi sijambo brother najisikia vizuri. nashukuru kwa kuja kuniona”
“Usijali Patrick kwa sasa endelea kupumzika. bado unahitaji mapumziko ya kutosha. Mimi niko hapo nje.i”
“Vero yuko wapi?” Akauliza Patrick
"Vero amechukuliwa na mama yake. Andrew amekwenda nyumbani kwako kuhakikisha kuko salama" akasema Alois.
"Naomba umpigie simu na umwambie kwamba niko salama, asiwe na mawazo" akasema Patrick
"Sawa Patrick ngoja nimfahamishe" akasema Alois.
* * *
Baada ya kulia sana hatimaye kiusingizi kikaanza kumchukua na taratibu akajikuta akianza kulala. Hazikupita hata dakika kumi toka aanze kusinzia simu yak ikaanza kuita na kumstua toka usingizini. Alipoiangalia simu yake ilikuwa imeandika jina Alois. Aliogopa kuipokea simu ile akabaki akiiangalia ikiiendelea kuita. Mikono ilikuwa ikimtetemeka . Alihofia pengine simu ile inaweza kuwa imebeba ujumbe mbaya kuhusu Patrick.
Simu iliita ikakatika ,ikaanza kuita tena. Akaamua kuipokea. “Haloo” Akaita Vero
“Haloo Vero unaendeleaje ? akasema Alois.
“naendelea vizuri shemeji vipi huko kwema ? Akasema vero huku mapigo yake ya moyo yakienda kwa kasi isiyo ya kawaida.
“Huku kwema tu shemeji. Nataka nikufahamishe kuwa Patrick tayari amekwisha rejewa na fahamu zake na nimetoka kuongea naye muda si mrefu. Kwa hivi sasa anaendelea kupumzika. Amenituma nikwambie kwamba usiwe na wasi wasi yeye ni mzima wa afya.” Vero akashusha pumzi ndefu akakaa kimya kwa sekunde kadhaa kisha akamuaga Alois na kukata simu. Alipokata simu akaanza tena kulia kwa kwikwi.. Vick ambaye alikuwa katika usingizi mzito akaamka baada ya kustushwa na kilio cha Vero.
“Vero nini tena"?
“Patrick anaendelea vizuri.Alois amenipigia simu sasa hivi na kunifahamisha.”
“sasa kama hajambo unalia nini?
“Huwezi jua Vick ni jinsi gani nisivyopenda kumuona Patrick akiumwa kwa jinsi ninavyompenda.. Ninalia kwa mateso ninayoyapata juu yake.” Vick akambembeleza vero hadi akanyamaza kisha akajilaza kitandani na kuanza kutafakari.juu ya tukio zima..
Alikumbuka walikuwa sebuleni wakiangalia luninga ambapo warembo wanaotarajia kuwania taji al miss Tanzania walikuwa wakijinadi . Alivuta picha na kumuona Patrick akiwa katika friji akijimiminia kinywajii katika glasi ambapo muda huo Miss arusha Neema alikuwa akijinadi. Alikumbuka kumuona Patrick alivyovutiwa ghafla na kipindi hicho cha warembo. Toka Neema hakumbuki ni mrembo gani aliyefuatia kujinadi ila anachokumbuka ni kwamba Patrick alipiga ukelele mkubwa wa kushangaa kitu halafu akaanguka na kupoteza fahamu.
“Ni dhahiri ni mstuko ndio uliomfanya Patrick aanguke na kupoteza fahamu .Lakini je ni kitu gani hasa ambacho kilimstua Patrick kiasi cha kupoteza fahamu?Je mstuko huu una uhusiano wowote na kipindi kile tulichokuwa tukitazama ? hapana . Patrick nimekuwa naye muda mrefu sasa na tabia yake ninaifahamu vizuri. Kuhusu wanawake siwezi kumsemea vibaya hana tabia hiyo ya kuwa na wanawake wengine nje ya mahusiano yetu. Nina uhakika na hilo. Sasa ni kitu gani kilichomstua ? Any way siwezi kupata jibu kwa sasa mpaka hapo atakaponiambia yeye mwenyewe kwani nina hakika hawezi kunificha kitu chochote.” Alikuwa akiwaza Vero na taratibu usingizi ukamchukua akalala.
* * * *
Saa kumi na mbili asubuhi iliwakuta Vero ,Vick na mama yake vero tayari wakiwa hospitali.Hali ya Patrick ilikuwa ikiendelea vizuri . Alfajiri hiyo tayari alikwisha hamishwa toka katika chumba cha uangalizi maalum na kuwekwa katika chumba cha mapumziko ya kawaida. Wakiongozwa na alois ambaye alilala hapo hospitali walielekea moja kwa moja chumbani na kumkuta Patrick tayari amekwishaamka. Bila kupoteza muda Vero akamkumbatia na kumpiga mabusu mfululizo.
“Pole sana my dear. Unajisiaje kwa sasa? akauliza Vero huku akitabasamu
“Najisikia vizuri sana” akajibu Patrick huku akijinyoosha nyoosha pale kitandani.
Baada ya kusalimiana kilifuata kipindi cha vicheko na utani wa hapa na pale kisha Vick na mama yake Vero wakaomba waondoke kwa ajili ya kwenda kujiandaa na mishughuliko ya siku. Vero alimwinua Patrick na kumpeleka bafuni ambako alimwogesha na kumrudisha tena chumbani , akamwandalia kifungua kinywa . Patrick alijisikia faraja kubwa kwa namna binti huyu alivyokuwa akimjali na kumuhudumia.
* * * *
“Andrew kwa kipindi kirefu sasa umekuwa ni msiri wangu mkubwa. Mambo yangu mengi ambayo sihitaji mtu mwingine kufahamu wewe wayajua.Urafiki wetu ni zaidi ya undugu. Naomba sana kile nitakachokuambia hapa usimwambie mtu yeyote yule.Itabaki kuwa siri yako mpaka pale muda muafaka utakapofika.” Patrick aliongea taratibu huku akijiweka vizuri sofani.
Ni siku ya kwanza tangu ameruhusiwa kutoka hospitali kwa sababu ya mstuko uliopelekea apoteze fahamu. Andrew rafiki mkubwa wa Patrick alikuwa kimya akiwa na shauku kubwa ya kutaka kulisikia lile ambalo rafiki yake alikuwa tayari kumwambia.
“I saw Happy ”akasema Patrick kisha akatulia na kuyaacha maneno yale yamwingie Andrew.
“What !! ” akauliza Andrew kwa mshangao
“I saw Happy ” Patrick alirudia tena kisha akainamisha kichwa chini na kuzama katika mawazo mazito. Andrew akainuka na kuanza kuzunguka zunguka mle chumbani huku akionekana dhahiri alikuwa ameshtushwa mno na kauli ile ya Patrick.
“Umemuona wapi?”andrew akauliza huku amejishika kichwa.
’‘Nimemuona kwenye luninga .Kulikuwa na kipindi cha kuwanandi warembo wanaoshiriki kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Taifa .Happy ni miss Ilala.”
“are you sure” Andrew akahoji
“I'm sure Andrew na hiyo ndiyo sababu iliyonifanya nikapata mstuko na kupoteza fahamu”Andrew akavuta pumzi ndefu ,akainuka akaanza kuzunguka zunguka humo ndani kisha akakaa. Vijana hawa wote kwa sasa walikuwa katika wakati mgumu sana.
Ni Andrew pekee aliyefahamu kilichokuwa kikiendelea kati ya Patrick na Happy na ndio maana alichanganyikiwa asijue afanye nini. Alimuonea huruma sana Patrick kwa wakati huu mgumu alionao.
“Vero aligundua chochote “Andrew akauliza tena
“sina hakika kama aligundua kitu chochote kwa wakati ule” akajibu Patrick
“ kwa hiyo tufanye nini sasa” Andrew akahoji.
Patrick akainuka na kwenda katika friji akjimiminia maji baridi kwenye glasi akapiga funda kubwa kisha akavuta pumzi ndefu na kusema.
“Nataka kuonana na Happy"
Kimya cha sekunde kadhaa kikapita hapo sebuleni kisha Patrick akaendelea
“Nataka kabla ya kuonana naye kwanza tumfanyie uchunguzi anaishi wapi,na nani ,anafanya kazi gani,ana mchumba au hana,na chochote kile tunachoweza kukifahamu kuhusu yeye. Uchunguzi huu nataka uwe wa siri na yeye Happy asiweze kufahamu kuwa anachunguzwa. Ikiwezekana tunaweza hata kuajiri mtu wa kuifanya kazi hii niko tayari kumlipa kiasi chochote cha pesa anachohitaji. Nakukabidhi kazi hii Andrew nina imani itafanyika ipasavyo. Tuko pamoja? Akasema Patrick.Andrew akavuta pumzi ndefu na kusema
“Nimekuelewa Patrick lakini suala hili haliwezi kuathiri maandalizi ya harusi yako ambayo tayari yanaelekea mwishoni?
“Hahahah ! usihofu kuhusu hilo my friend. I know what I’m doing ,ok?” akasema Patrick huku akicheka
“Una maana gani Patrick unaposema unajua unachokifanya ? Ninafahamu kuwa ndoto zako za siku nyingi ni kuwa na Happy katika maisha yako na kwa sasa umekwisha kuwa na uhakika kuwa yupo na kwa wakati wowote unaweza kumuona . Nina wasiwasi sana na huu ujio wa Happy katikati ya maandalizi ya Harusi yako unaweza kutibua kila kitu." akasema Andrew kwa wasi wasi
“Kwa ajili ya Happy niko tayari kwa lolote linaloweza kutokea. All these years I’ve been hurting myself thinking about her na mpaka sasa nimeshindwa kabisa kuifuta kumbukumbu ya Happy moyoni mwangu. Siwezi kuendelea kuutesa moyo wangu Andrew.I have to face her.” Akasema Patrick
“Patrick nafikiri unahitaji kufikiri zaidi kuhusu suala hili, si suala jepesi kama unavyolifikiri. Ni suala ambalo linagusa hisia za watu wengi .Hi…..” Andrew hakuendelea zaidi Patrick akadakia.
“Andrew I've made my decision and its final. Nilivyoamua nimeamua. Nitapambana kadiri ninavyoweza ili kuonana tena na Happy . I love her and I know she loves me too.” akasema Patrick. Andrew akamuangalai rafiki yake kwa makini na kusema.
“Patrick miaka mingi imepita tangu mpotezane na Happy na kila mmoja ameendelea na maisha yake. Tayari uko na Vero na kwa sasa bado kama mwezi mmoja na nusu hivi ufunge ndoa na Vero ,ndoa ambayo sehemu kubwa ya maandalizi yake yamekamilika. Huoni kuwa utakuwa unamnyima haki zake Vero kama ukihamishia mawazo yako yote kwa Happy .? Nina imani Vero anakupenda kwa dhati ya moyo wake na nina imani vile vile hata wewe unampenda Vero Kwa nini utake kumtesa Vero kiasi hiki ?
“Andrew nafahamu unachokisema .Ni kitu cha msingi sana lakini kama ungeigia viatu vyangu na kuona nini kilichomo ndani. Nina imani kubwa hata wewe ungefanya kama mimi ninavyotaka kufanya. Happy ni msichana wangu wa kwanza ambaye nilimpenda kupita ninavyojipenda mwenyewe. Ni kweli niko katika mahusiano na hivi karibuni ninatarajia kufunga ndoa na Vero lakini bado sura ya Happy haijaweza kunitoka moyoni mwangu. Please Andrew naomba msaada wako katika hili.Nisaidie nionane na Happy tafadhali.” akasema Patrick
“Nimekuelewa Patrick lakini bado moyo wangu una wasiwasi sana juu ya kinachoweza kutokea hapo mbeleni. Nafahamu kuwa endapo utaingia matatizoni basi ni sisi sote tutakuwa katika matatizo. Tatizo langu ni lako na lako langu ndio maana tunahitaji sana kushauriana kwa kina kabla ya kufanya jambo.”
“Andrew najua una wasiwasi mwingi kuhusu mimi na Vero.Hilo ni kubwa linalokuumiza kichwa. Hata mimi sijisikii vizuri kumtesa Vero binti aliyeyatoa maisha yake kwangu.Binti anayenipenda kwa dhati ya moyo wake. Ni vero huyu huyu ndiye aliyeirudisha tena furaha ndani ya moyo wangu na kuliondoa wingu zito la ukiwa lililokuwa limenifunika. Nampenda Vero lakini ni lazima nionane na Happy .” akasema Patrick.
Andrew akainuka kitini akachukua chupa ya mvinyo na kujimiminia katika glasi akanywa mafunda kadhaa kisha akamgeukia Patrick.
“Ok Patrick kwa sababu umekwishaamua basi hatuna budi kufanya hivyo. Mimi nitaianza kazi hiyo kesho. Nitamtafuta mtu ambaye ataifanya kazi hiyo kwa ustadi mkubwa. Usijali kuhusu hili ndugu yangu” Patrick alifurahi akainuka na kumkumbatia rafiki yake.
* * * *
Saa kumi na mbili za jioni Veronika alirejea katika shughuli zake na kumuaga mama yake kuwa alikuwa akaienda kumwangalia Patrick nyumbani kwake. N i siku ya tatu sasa toka Patrick atoke hospitali. Hali yake haikuwa ikiendelea vizuri sana.Muda mwingi alikuwa akionekana ni mtu mwenye mawazo mengi . Hali hii ilimpa wasiwasi mwingi Vero kiasi cha kumfanya awe karibu naye kila wakati ili kujaribu kumchangamsha na kumrudisha katika hali yake ya kawaida.
Ingawa Patrick alijitahidi kwa kila jinsi ili Vero asione hali hii ya mawazo mengi aliyokuwa nayo lakini mara nyingi alishindwa na kujikuta akitoa machozi. Vero aliigundua hali hii na kwa kiasi kikubwa ikamuongezea udadisi juu ya kinachoendelea . alijua ni lazima liko jambo ambalo linamchanganya Patrick
“Haloo sweetie” Alisema Vero baada ya kuingia ndani kwa Patrick
“Haloo vero ” akasema PatrickVero akamfuata Patrick kitandani akamkumbatia na kumpiga busu zito.
‘Unaendeleaje mpenzi”
“Naendelea vizuri Mungu ananisaidia sana. Muda si mrefu nitapona kabisa”.
Baada ya kujuliana hali Vero alimwandalia Patrick Juice kisha yeye akaelekea jikoni kufanya maandalizi ya chakula cha jioni.Patrick alipata faraja kubwa baada ya Vero kuwasili Ni wazi Patrick husikia furaha kubwa moyoni awapo na Vero. Ilimuuma sana baada ya kugundua kuwa alimpenda Vero lakini kwa ghafla Happy ametokea na kuanza taratibu kuzihamisha hisia zake. Chakula kilipokuwa tayari kikawekwa mezani,wakala kisha wakapumzika na baadae wakaelekea kulala.
“Vero dear tayari umekwisha kata tiketi za kuingia Miss Tanzania Jumamosi? Patrick akauliza
“Tayari mpenzi Nimekwishaziandaa . Utaweza kwenda na hali hii ? Naona kama hali yako inazidi kudhoofu siku hadi siku”
“Usijali mpenzi wangu lazima nihudhurie. Nina imani ndani ya siku mbili tatu zijazo hali yangu itakuwa shwari ”akajibu Patrick
Vero akanyamaza kimya akajaribu kuvuta kumbukumbu nyuma siku ile Patrick alipoanguka na kupoteza fahamu alikuwa akitazama kipindi cha wagombea wa miss Tanzania . Hakutaka kukubaliana kuwa kuna kitu chochote kinachoendelea baina ya Patrick na mashindano yale. Alijitahidi kuilazimisha akili yake ikubaliane na taarifa ya daktari kuwa Patrick alipoteza fahamu kwa sababu ya uchovu mwingi uliokuwa ukimkabili kiasi cha kuufanya ubongo wake ushindwe kufanya vizuri kazi yake.
“Lakini pamoja na taarifa ile ya daktari lakini kuna kitu kiko moyoni mwa Patrick ambacho kinamyima raha na kuisumbua akili yake . Ni kwa sababu hiyo tu ndiyo maana amepoteza furaha yote aliyokuwa nayo kabla. Chakula chenyewe mpaka abembelezwe. Mara kadhaa nimemfuma mwenyewe kwa macho yangu akilia. Ingawa anajitahidi sana kuificha hali hii lakini nimekwishafahamu . Anyway nitajitahidi kumuuliza ili anieleze kama kuna jambo lolote linalomsibu.” Veronika alizama ghafla katika mawazo.
“Unawaza nini mpenzi wangu”Patrick akauliza
“Nothing.Siwazi chochote zaidi yako.Unajua Patrick hali yako kwa sasa inanipa wasiwasi sana. Tangu umetoka hospitali umebadilika. Ni kitu gani kinakusumbua mpenzi hebu niambie. Hali hii inanifanya hata mimi nihisi kama vile ninaumwa pia. Au kama kuna kitu nimekukosea niambie Patrick ili nijirekebishe. Tangu tumeanza mapenzi yetu sijawahi hata siku moja kukuona katika hali hii” Vero akashindwa kujizuia akaanza kulia kwa kwikwi.
Patrick akamvutia Vero kwake akambusu na kumwambia
“Usihofu kitu baby hakuna kitu kingine kinachonisumbua .Kama daktari alivyosema kuwa natakiwa kupumzika sana .Uchovu ndio uliopelekea tatizo lile kutokea.”Akasema Patrick huku akizichezea nywele laini za Vero.
‘Hapana dear najua lazima kuna kitu kinachokusumbua akili na hutaki kuniambia”
“ my dear angel ,wewe ndiye maisha yangu.Wewe ndiye uliyeyashika maisha yangu. Nimekukabidhi funguo za moyo wangu. Wewe ndiye mfariji wangu,wewe ndiye furaha yangu,wewe ndiye kila kitu kwangu sasa kwa nini nikufiche kitu?Hakuna kitu nimewahi kukuficha wewe mpenzi wangu na haitakuja tokea nikawa na tatizo nikashindwa kukwambia. Sasa nisipokwambia wewe nitamwambia nani tena?”
Patrick alijitahidi kumtoa Vero wasiwasi aliokuwa ameanza kuwa nao juu yake na mara moja akaazimia moyoni kubadilika kitabia ili Vero asije akaendelea kumdadisi. Taratibu akaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ya ucheshi na uchangamfu mkubwa kitu ambacho Vero alikifurahia sana.
Ni jumamosi angavu ndani ya jiji la Dar es salaam, jiji lililojaa kila aina ya pilika na purukushani. Jua lilikuwa likielekea magharibi na kulipisha giza lichukue nafasi yake.Jioni hii iliwakuta Patrick na Veronika wakiwa katika pilika pilika za kujiandaa kuelekea katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa katika ukumbi wa Diamong jubilee.
Patrick ndiye aliyekuwa katika pilika pilika nyingi zaidi jioni hiyo. Siku hii ilikuwa ni moja kati ya siku zake kubwa kabisa katika maisha yake. Ni siku ambayo aliamini ingemkutanisha tena na kiumbe ampendaye kwa dhati ya moyo wake.
Alikuwa ndani ya suti nzuri ya gharama kubwa. Suti hii huwa anaivaa kwa nyakati maalum kama hizi. Hakika alikuwa amependeza vilivyo kijana huyu. Wakiwa katika harakati z a kumalizia kujiandaa simu yake ikaita. Alkuwa ni Andrew.
“Haloo Andrew”
“Hallo Patrick vipi mko tayari? aliuliza Andrew huku akicheka kichinichini.
“Tupo tayari Andrew na muda wowote toka sasa tunaweza kuanza safari ya kuelekea ukumbini”
“Ok Patrick sisi tayari tumekwishajiandaa na muda wowote tutakuwa njiani pia kuelekea huko na tutawasubiri nje ya ukumbi ili tuingie pamoja.Ila ndugu yangu nakuomba kitu kimoja katu usihamaki. Wala usionyeshe aina yoyote ya mstuko pindi utakapomuona Happy . Najua tu lazima kunaweza kutokea na kitu kama mstuko fulani utakaomuona Happy lakini naomba ujaribu kujizuia kwa sababu pale tutakuwa tuko na Vero na Vick kwa hiyo wanatakiwa wasihisi kitu chochote. Mimi nitakuwa macho kuhakikisha kuwa hakuna kitu chochote kitakachoharibika “
“Usihofu Andrew nalifahamui hilo na niko makini nalo sana..” akasema Patrick Baada ya kumaliza kujiandaa na kuhakikisha kuwa wako safi wakaingia garini na kueleka Diamond Jubilee.
* * * *
Ukumbi wa Diamond jubilee ulikuwa umefurika watu pasi mfano.Pamoja na ukumbi kufurika watu bado watu walikuwa wakimiminika ukumbini hapo kwa lengo la kushuhudia mchuano wa kumtafuta mrembo wa Taifa atakayeliwakilisha Taifa katika mashindano ya dunia. Patrick, Vero, Andrew na Vick waliwahi sana kuingia ukumbini na kuchukua moja kati ya meza za mbele kabisa. Patrick moyo ulikuwa ukimdunda sana usiku huo.
Andrew alilifahamu hilo na hivyo akawa makini sana katika kuhakikisha kuwa hakuna kitu kitakachoharibika .Toka wameingia ukumbini Patrick alikuwa kimya .
“Patrick are you ok? Vero akauliza baada ya kuona Patrick yuko kimya sana.
“Yes I’m ok Vero usihofu.”
Mara muongoza shughuli akatokea jukwaani na kuanza kutangaza.
“Mabibi na mabwana mliohudhuria mashindano haya makubwa ya urembo nchini napenda kuwakaribisha sana katika usiku huu wa pekee kabisa kwetu sote. Ni usiku wa pekee kwa sababu leo tutaandika historia mpya kabisa katika mashindano ya urembo hapa nchini na ulimwengu kwa ujumla. Kwa mwaka huu kamati nzima ya Miss Tanzania imeazimia kufanya mabadiliko makubwa sana na nyie wote mlioko hapa ndio mtakaokuwa mashahidi wa kile kitakachotokea usiku wa leo. Nasema karibuni sana katika usiku huu na tujumuike sote mimi naitwa Mc Thora kwa wale ambao hawanifahamu.."
“Mabibi na mabwana kabla hatujaendelea mbele na ratiba yetu ningependa kwanza kumkaribisha jukwaani mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainments ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu. Mabibi na mabwana makofi kwa Mr Petty.s Woris”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainments akapanda jukwaani akiwa amevalia nadhifu kabisa.
“viongozi mbali mbali ,watazamaji wote mliohudhuria mashindano haya usiku huu mabibi na mabwana asalaam aleikhum. Ni furaha ilioje kwetu sisi kama Masimulizi entertainments kudhamini mashindano makubwa kama haya ya urembo hapa nchini. Kama wote mnavyoshuhudia mashindano ya mwaka huu yamekuwa na utofauti mkubwa na mengine yaliyotangulia. Maandalizi yake yamekuwa mazuri , zawadi zimeboreshwa na ushindani miongoni mwa washiriki umeongezeka mara dufu.
Kwa kuwa ni mara yetu ya kwanza kudhamini mashindano makubwa kama haya bado kunaweza kuwa na kasoro kadhaa ambazo nina imani kwa kushirikiana na wadau wote wa urembo hapa nchini tutasaidiana kuzitatua. Nina imani bado tutaendelea kudhamini na kuandaa matamasha mengi na makubwa zaidi hapa nchini ili kuzidi kuukuza wigo wa burudani hususani sanaa hii ya urembo .
Mwisho kwa niaba ya uongozi na wafanya kazi wote wa Masimulizi entertainments napenda kuwatakia wote utazamaji mzuri wa mashindano haya usiku huu.Ahsanteni sana.”
Baada ya kumaliza kusema machache akarudisha kipaza sauti kwa muongoza shughuli kisha akashuka jukwaani.
“Mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mkurugenzi wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu.. Mabibi na mabwana kwa mujibu wa ratiba yetu kinachofuata kwa sasa ni kuwatambulisha majaji wa mchuano huu ambao ndio watakaofanya kazi kubwa na ngumu ya kutuchagulia mrembo mwenye sifa ya kuwa mrembo wa taifa. Majaji tulionao usiku huu ni saba. Ningeomba jaji utakaposikia jina lako likitajwa basi usimame ili watu wakufahamu.
Wa kwanza ni Mr Ernest Namesha, wa pili ni ndugu Mecky , tunaye pia Mr Boniventure Gregory, anayefuatia ni Mr Samweli Nathaniel, tunaye pia dada yetu mpendwa usiku huu naye ni dada Esther mathias, pia tunaye Mrs Coletha brown, tunaye vile vile bi Susan Abrahams na wa mwisho ni ndugu Jacob Lyimo. Hawa ndio majaji wetu ambao watakuwa wakifanya kazi ngumu ya kumchagua mrembo wa Taifa usiku huu wa leo.”
“Mabibi na mabwana baada ya kuwafahamu majaji wa mchuano huu wa leo sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 katika show maalum waliyoiandaa “ wimbo ukaanza kupigwa na warembo wakaanza kutoka huku wakicheza kwa staili yenye kuvutia sana.
Makofi nderemo na vifijo vikatawala ukumbini. Patrick alielekeza macho na akili yake yote jukwaani na bila kukosea alimuona Happy ambaye alikuwa amependeza kupindukia Jasho likaanza kumtiririka akatoa kitambaa na kujifuta. Alikuwa kimya kabisa.
Baada ya show ya warembo kukamilika ziliendelea burudani nyingine toka kwa wasanii mbali mbali kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana baada ya kupata burudani hizo zakukata na shoka sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 ili muwatambue. Watapita hapa jukwaani mmoja mmoja .”
Warembo wakaanza kutoka nyuma ya jukwaa na kuanza kupita mbele ya watazamaji. Kidogo Patrick atamke kitu baada ya kusikia jina la Happy likitajwa. Happy akapita jukwaani huku kelele za shangwe zikisikika.
Happy alikuwa akionekana kama malaika usiku huu. Alikuwa amependeza vilivyo. Kila mtu aliustaajabia uzuri wa binti huyu mwenye kila sifa ya kuwa mrembo wa Taifa na dunia. Kelele zile za mashabiki zilizidi kumchanganya Patrick na kumfanya ahisi kuchanganyikiwa. Andrew alikuwa makini sana kwa lolote ambalo lingeweza kutokea.
Baada ya kupita jukwaani kujitambulisha kwa mashabiki zikafuata burudani za aina yake toka kwa wanamuziki. Kisha Muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana mambo yanazidi kupamba moto. Mambo ni bam bam na kama nilivyowaeleza toka mwanzo kuwa Masimulizi entertainment wameleta mageuzi makubwa katika mashidano ya mwaka huu .
Kwa sasa napenda kuwaleta kwenu warembo wote 26 wakiwa katika vazi la ufukweni. Mhh ! hapa pana kazi kweli kweli .mabibi na mabwana hebu tuwashangilie hawa warembo wetu watakapokuwa wakipita jukwaani katika vazi la ufukweni.”
Warembo wakaanza kupita jukwaani wakiwa katika vazi la ufukweni. Siyo siri walikuwa wamependeza vilivyo. Baada ya kumaliza kupita na vazi la ufukweni zikafuata tena burudani halafu warembo wote wakapita tena kwa mara nyingine na vazi la ubunifu.
Kelele zilikuwa kubwa sana kila walipopita warembo Neema wa Arusha na Happy wa Ilala. Warembo hawa walionekana kuchuana vilivyo. Kisha pita na vazi la ubunifu muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana tayari tumewashudia warembo wetu 26 wakipita hapa mbele yetu wakiwa katika mavazi tofauti tofauti. Kwa sasa ule wakati mliokuwa mkiusubiri kwa hamu kubwa unaelekea kuwadia.K wa hivi sasa tutakwenda kuwafahamu warembo 10 bora ambao wameonekana kufanya vizuri zaidi . Naomba sasa nimkaribishe Mrs Coletha brown ili aje atutangazie wale warembo wetu kumi waliofanya vizuri zaidi.Karibu sana mama.”
Mrs Coletha brown akapanda jukwaani akiwa na karatasi yenye majina ya warembo kumi waliofanya vizuri na ambao wataendelea na mchuano.
“mabibi na mabwana napenda kuchukua nafasi hii kwanza kuwapongeza waandaaji wa mashindano haya ambayo kwa mwaka huu yameboreshwa kwa kiwango cha juu kabisa. Mabibi na mabwana kazi yetu usiku wa leo imekuwa ni ngumu sana . Warembo wote wako katika hali ya ushindani wa hali ya juu mno. Lakini tumeweza kuwapata wale kumi ambao ni bora zaidi na ambao nitaenda kuwataja hivi punde.
Nambari 12 Nelea shulo,nambari 9Saida abdi,nambari 4 Upendo timelo,Nambari 20 Neema ,Nambari 11 Esther stevens,Nambari 6 Happy Kibaho, nambari 22 Elimeena kimuo, nambari 26 bahati udhoka,nambari 16 Winifrida mwasajuki,na mwisho ni namba 13 genevieve alphonse.”
Kelele za kushangilia zikasikika ukumbini. Warembo waliofika hatua ya kumi bora wakajipanga mstari. wakapiga picha ya pamoja kisha zikafuata burudani .baada ya burudani mc akapanda tena jukwaani.
“Mabibi na mabwana bado tunaendelea na mchakato wetu wa kuifikia ile hatua kubwa kabisa ambayo kila mmoja wetu aliyeko hapa ana hamu ya kuishuhudia. Kila mmoja anatamani amfahamu mrembo wetu mpya wa Taifa. Kwa sasa tutaenda kuwatafuta wale watano bora ambao kutoka kwao tutampata mrembo wetu. Atapanda tena Mrs Coletha kuja kututangazia warembo watano bora .” mrs Coletha akapanda tena jukwaani akiwa ameongozana na watu wawili wa miraba minne wanaomlinda.
“mabibi na mabwana kama nilivyowaambia awali kuwa kazi yetu leo imekuwa ngumu sana hasa kutokana na jinsi warembo wote walivyo na vigezo vya juu mno kiushindani.Lakini pamoja na wote kuwa na ushindani wa juu tumeweza kufanikiwa kuwachuja na kupata wale watano ambao wameonekana kuwa ni bora zaidi. Warembo waliopita hatua ya tano bora ni mrembo nambari 16 Winifrida mwasajuki,nambari 20 Neema i,nambari 13 Genevieve alphonse,nambari 26 Bahati udhoka na mwisho ni nambari 6 Happy Kibaho .” Kelele kubwa zikasikika zikishangilia.
Kila mtu pale ukumbini alikuwa ameridhika na kazi waliyoifanya majaji. Hakukuwa na aina yoyote ya upendeleo. Baada ya kuwatambua warembo wote waliofanikiwa kuingia hatua ya tano bora hatimaye kikafuata kipindi cha maswali. Ni Happy kibaho tena ndiye aliyejibu swali vizuri zaidi na kuwafanya watu wote ukumbini kumshangilia kwa nguvu.
Kila mtu aliamini kuwa Happy ni lazima angeibuka kuwa mrembo wa Taifa. Patrick jasho lilikuwa likimtiririka mwilini. Alijitahidi kwa kila alivyoweza ili asiweze kuonyesha hali yoyote ya utofauti pale mezani.
Baada ya kipindi cha maswali kumalizika ikafuata burudani moja kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana ule wakati uliokuwa ukisubiriwa na kila mtu hapa ukumbini naona sasa umewadia. Huu ni wakati wa kumtambua mrembo wetu mpya wa Taifa. Napenda nichukue fursa hii kuwashukuru sana majaji kwa kazi ngumu waliyoifanya usiku huu kwa kutuchagulia mrembo mpya wa Taifa. Kabla sijamkaribisha jaji mkuu kuja kutangaza mshindi wa shindano hili napenda kumkaribisha mrembo anayemaliza muda wake ili aweze kuongea machache na kuwaaga rasmi kabla hajalivua taji la Miss Tanzania.”
Helen Daudi mrembo anayemaliza muda wake alipanda jukwaani huku akishangiliwa vilivyo. Alipewa kipaza sauti na kusogea mbele.
“mabibi na mabwana ,wageni waalikwa,waheshimiwa majaji ,waandaaji na wadhamini wote wa mashindano haya habari za usiku. Napenda kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha mimi kutimiza moja ya ndoto zangu nayo ni kuwa mrembo wa Tanzania.
Nawashukuru vile vile wazazi wangu na ndugu zangu kwa kunipa moyo toka katika hatua za awali za kinyang’anyiro hiki hadi nilipobahatika kuchukua taji. Mabibi na mabwana kulivaa taji la Miss Tanzania ni mzigo mkubwa. Nimeshuhudia mimi mwenyewe uzito wa taji hili kubwa la urembo hapa nchini. Yapo mengi ambayo unapaswa kulifanyia taifa hili ukiwa kama mrembo wa Taifa. Kuna mazuri na magumu yake. Zipo changamoto nyingi ambazo yakubidi upambane kufa na kupona ili uweze kushinda. Napenda kuishukuru kamati nzima ya Miss Tanzaina kwa ushirikiano mkubwa walionipa katika kipindi chote nilichokuwa nimevaa taji hili. Sintaweza kumtaja mmoja mmoja lakini napenda niwashukuru wote kwa ujumla
.Napenda niwashukuru vile vile wadau wote wa sanaa hii ya urembo hapa nchini kwa sapoti yao kubwa waliyonipa. Wamenisaidia sana kuifahamu sanaa hii ya urembo vizuri.Nawashukuru pia wananchi wote wa Tanzania kwa kunikubali Nawapenda wote na ninaahidi kushirikiana na mrembo atakayevaa taji hili usiku huu katika yale yote mazuri niliyokuwa nimeyafanya kwani kulivua taji hili si mwisho wa kuendeleza yale yote niliyokwisha yafanya wakati niko na taji.
Mwisho kama binadamu kuna wakati naweza kuwa nimemkosea huyu na yule kwa namna moja au nyingine. Napenda kuchukua nafasi hii kwa dhati kabisa kuwaomba msamaha wale wote niliowakosea.Tusameheane na kuanzia usiku huu tuanze maisha mapya.Ahsanteni sana.” Alimaliza kutoa machache mrembo huyu akarudi katika kiti chake cha heshima huku akishangiliwa na watu.’
“naam mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mrembo anayemaliza muda wake. Na sasa ule wakati tuliokuwa tukiusubiri kwa hamu kubwa ndio umewadia.Ni hivi punde tutaenda kumfahamu mrembo wetu mpya. Naomba sasa nimwite Mr Jackob Evarist ili aweze kututajia washindi wetu.”Mr jacob akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana kama alivyotangulia kusema Mrs Coletha brown kuwa mchuano wa leo ulikuwa mgumu sana. Tunamshukuru Mungu kuwa tumeweza kumpata mrembo wa taifa licha ya kuwa na wakati mgumu hasa kutokana na kila mrembo alivyokuwa amejiandaa. Mabibi na mabwana nitaanza kuitangaza nafasi ya tatu hadi moja.” Alitulia kidogo kisha akaendelea.
“Nafasi ya tatu imekwenda kwa mrembo nambari 16 winifrida mwasajuki” alitulia kwanza na kumpisha mrembo huyu apite mbele huku akishangiliwa.
“nafasi ya pili imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 20 Neema Jaspa” Kelele za shangwe zikasikika. Miss Arusha Neema Jaspa binti mwenye ngozi nyeusi yenye kung’aa akapita jukwaani akiwa ndani ya tabasamu kubwa. “
Na sasa mabibi na mabwana ni nafasi ya kwanza.Nafasi ya kwanza imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 6 Happy .”
Tangu ukumbi wa Diamond jubilee ujengwe hakujawahi tokea shangwe kubwa kama hii ya usiku huu ya kuushangilia ushindi wa Happy .Mrembo huyu alifanikiwa kuzikonga nyoyo za watu vilivyo. Patrick alishindwa kujizuia akainuka na kushangilia kwa nguvu sana.
Jukwaani Happy machozi yalikuwa yakimtoka. Hakuamini kama ni yeye ndiye aliyetangazwa mshindi wa shindano hili hasa kutokana na upinzani mkubwa uliokuwepo miongoni mwa washiriki. Watu waliKumbatiana na kupeana mikono ya hongera kuashiria kukubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji ya kumchagua Happy kuwa mrembo wa Taifa. Kila mmoja aliamini kuwa Happy alistahili kulitwaa taji lile.
Baada ya kama dakika kumi hivi za hoi hoi na nderemo muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana nafikiri hoi hoi na nderemo hizi zote ni kuonyesha jinsi gani wote kwa pamoja tunavyokubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji.Happy kibaho ndiye miss Tanzania wetu mpya. Kinachofuata sasa ni mrembo anayemaliza muda wake kulivua taji na kumvisha mrembo mpya.”
Zoezi hili likafanyika huku likishangiliwa kwa nguvu sana.na baada ya zoezi hili kukamilika muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“Mabibi na mabwana tukio linalofuata sasa ni la kumkabidhi Miss Tanzania funguo za gari lake. Tunamuomba mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu apande jukwaani na kumkabidhi Miss Tanzania funguo hizo.”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainment akapanda jukwaani na bila kupoteza muda akamkabidhi Happy funguo za gari ambalo ni zawadi ya kwanza kwa miss Tanzania. Akiwa katika tabasamu pana sana alipita jukwaani huku akizipunga funguo hewani .Kelele za kushangilia zilisikika.
Baada ya zoezi hilo zikafuata burudani mbili kisha mashindano yakafungwa rasmi na taratibu umati wa watu ukaanza kuondoka maeneo hayo ya Diamond jubilee kila mmoja akiwa amesuuzika vilivyo na ushindi wa Happy kibaho .
Happy sasa alikuwa akipiga picha na watu mbali mbali huku akisongwa na waandishi wa habari wakitaka kufahamu mawili matatu ingawa mkurugenzi wa Miss Tanzania alijitahidi kuwazuia kwani Happy angefanya mkutano na waandishi wa habari hapo kesho lakini haikusaidia kitu.
Patrick ambaye alionekana kuchanganyikiwa kadiri muda unavyosonga alitoa simu yake na kuanza kubonyeza namba kisha akajitenga na akina Andrew ambao kwa sasa walikuwa wamesimama wakijiandaa kuondoka.
Patrick aliitumia njia ile ya kujifanya anapiga simu ili aweze kuondoka mahala pale bila kutiliwa mashaka kwani lengo lake kuu lilikuwa kujaribu kupata nafasi ya kuonana na Happy .
Andrew alielewa mara moja nini kilichokuwa kikiendelea akawaomba Vero na Vick waondoke mahala pale waelekee katika magari. Lengo lilikuwa kuwatoa wasiwasi akina Vero.
Patrick alikuwa akipigana vikumbo na waandishi wa habari waliokuwa wakichukua picha na kumuuliza Happy maswali mawili matatu. Alijitahidi sana kupenya na hatimaye akajikuta yuko mahala ambako anaweza kumuona Happy kwa ukaribu.
Jasho lilikuwa likimtiririka na moyoni alikuwa na wasi wasi mwingi lakini hii haikukumkatisha tamaa ya kuonana na Happy . Alijisogeza taratibu na hakuna mtu yeyote aliyeweza kuwa na shaka naye kuwa si mwandishi wa habari tena toka katika chombo cha habari kikubwa hapa nchi au nje ya nchi kutokana na muonekano wake.
“Hongera sana Happy madame Tanzanie” Akasema Patrick wakati huo akiwa uso kwa uso na Happy . Happy kwa wakati huo hakujua aliyekuwa akiongea naye .Alijua wote ni waandishi wa habari. Lakini neno lile “Madame Tanzanie” likamstua na kumfanya ainue uso wake na kumtazama vizuri mtu yule aliye mpa salamu ile.
Kwanza alihisi sauti ile ni kama si ngeni masikioni mwake .mbele yake alikuwa amesimama kijana nadhifu akiwa ndani ya tabasamu lenye kuonyesha aina Fulani ya wasi wasi. macho yake yakakutana na macho ya Patrick na kwa kasi ya umeme kumbukumbu ya ghafla ikamjia kichwani “Noooooo!!!!!!!!!!! Pa...t…….” Akaanguka na kupoteza fahamu.
Kizaa zaa cha ghafla kikatanda hapo ukumbini. Kwa sekunde kadhaa ikatokea taharuki kubwa. Kila mtu akapatwa mstuko kwa kitendo cha Miss Tanzania kupoteza fahamu ghafla.
Haraka haraka walinda usalama wakamwinua na kumkimbiza katika gari la wagonjwa ambalo lilikuwa nje tayari kabisa kwa dharura kama hii.Kwa kasi ya ajabu gari lile likaondoka kuelekea Hospitali. Watu waliokuwa bado wako ukumbini hawakuamini kilichotokea ghafla vile.
Waandishi wa habari wakalichukua tukio lile kama lilivyotokea.
Patrick nusura akili imruke kwa kitendo cha Happy kupoteza fahamu.Taratibu alihisi kuishiwa nguvu lakini tayari Andrew alikuwa ameshafika ,akamshika mkono na kumtoa nje ya ukumbi .
* * * *
Saa kumi na moja asubuhi miss Tanzania Happy alizinduka. akaangaza huku na huku akatambua kuwa alikuwa hospitali. Taratibu akaanza kukumbuka kilichotokea na kumfanya awepo pale hospitali mida ile.Akalikumbuka tukio zima lililotokea usiku.
“That’s him..I saw him ”Happy akajikuta akiongea kwa sauti na kuwastua watu waliokuwemo mle chumbani. Miongoni mwa watu waliokuwa wakifuatilia kwa karibu hali ya Happy ni mdogo wake Margreth .Alikuwepo pia mkurugenzi wa Miss Tanzania pamoja na watu wengine kadhaa.
Mara tu waliposikia kuwa ameamka mkurugenzi wa Miss Tanzania akamwita daktari ambaye alikuja na kumpima. Baada ya vipimo vyote kuonyesha hakuna tatizo zaidi ya mstuko wa kawaida daktari alimuomba Happy aendelee kupumzika na asibughudhiwe.
Daktari akawaomba wote waliokuwa pale Hospitali kwa ajili ya Happy waende kupumzika na kumwacha mgonjwa apumzike kwani bado alihitaji mapumziko ya kutosha.
Ni margreth pekee ndiye aliyebaki ili kumsaidia dada yake.
Baada ya watu wote kutawanyika Happy akageuza kichwa na kumwita margreth.
“ Pole sana Happy.Unaisikiaje sasa ”akasema Margreth
“I’m ok magie." akajibu happy. Margreth akamuangalia kwa makini kisha akamuuliza.
"Happy kitu gani kilitokea mpaka ukapoteza fahamu?..Happy akamuanglai mdogo wake usoni halafu akasema.
"Maggie I saw Patrick yesterday”
“Whaaaaat!!!!!”akauliza margreth kwa mstuko. ' Patrick !!....Patrick yupi ? akauliza Margreth.
" Patrick mpenzi wangu wa zamani" akasema Happy
"Happy Patrick is dead....hakuan namna ambayo ataweza kurudi.Inawezekana ulimafananisha na mtu" akasema Margreth.
"Hapana margreth..I saw him with my own eyes. It was him.." akasisitiza Happy
“Sister are u ok?Magie akauliza tena.
“Sina tatizo magie ni kweli nilimuona Patrick jana wakati nikiongea na waandishi wa habari Alikuja mbele yangu na kunisalimu .Alitamka maneno Fulani ambayo yalinifanya nistuke na nilipomtazama vizuri alikuwa ni yeye.
Nina hakika ni yeye kwani ni mtu ambaye yuko moyoni mwangu kwa miaka mingi na kila siku ninaangalia picha yake hivyo siwezi kuwa nilimfananisha. Ninaamini nilimuona Patrick na ndio maana nikastuka hadi kupoteza fahamu. I’m confused Maggie .Totaly confused.” Kimya kikatanda mle chumbani .
“Margreth tafadhali usimwambia mtu yeyote juu ya habari hii.”
“Usijali sister siwezi mweleza mtu" akasema Margreth.
“Sasa maggie naomba unisaidie kitu kimoja.”Akasema Happy .
“Nikusaidie nini Happy?” akauliza Margreth. ‘
"Nataka kuonana na Patrick” Akasema Happy huku macho yake yamefunikwa na machozi.
“Pumzika kwanza sister ukitoka Hospitali tutaongea kwa undani juu ya suala hili. Kwa sasa bado unahitaji mapumziko ya kutosha na huhitaji kuwaza sana juu ya suala hili.”akasema Margreth.
“Thanks Maggie I understand “akasema Happy.
Mara mlango wa chumba alimolazwa Happy ukafunguliwa wakaingia wazazi wa Happy ambao walikuwa safarini lakini kutokana na matatizo aliyoyapata mtoto wao ikawabidi waahirishe safari yao na kurudi Tanzania haraka.Mama yake akamkumbatia huku machozi yakiwatoka wote . Baada ya kusalimiana Happy akawahakikishia wazazi wake kuwa kwa sasa alijisikia mzima kabisa na pengine mchana wa siku hiyo angeruhusiwa kurudi nyumbani.
Wakiwa katika maongezi akaingia muuguzi akiwa na sinia la dawa. akawaomba radhi wote waliokuwa mle ndani kuwa alihitaji kumuhudumia mgonjwa hivyo akawaomba watoke nje kwa dakika kadhaa. Alipohakikisha wote wametoka akamkaribia Happy .
“Samahani dada Happy nina ujumbe wako ambao nimeambiwa ni wa muhimu na nyeti sana .Aliyenipa ujumbe huu amenionya kwamba nisikupe mahala penye watu .”
“Nani aliyekupa ujumbe huu?
“simfahamu ila ni kijana mmoja alikuwa amevaa suti nyeusi na hakujitambulisha jina lake .yeye alisema ukishausoma tu utakuwa umefahamu.” Yule muuguzi akatoa bahasha toka katika mfuko wake wa koti na kumpatia. Baada ya kumpatia dawa muuguzi yule alitoka na kumwacha Happy jasho likimtiririka. Hakujua ni nani aliyeleta ujumbe ule.
Aliishika bahasha ile na kuifungua taratibu. Ilikuwa ni kadi nzuri iliyomtakia uponaji wa haraka. Ndani ya kadi ile kikaanguka kikadi kidogo . Akakiokota na kukisoma.Nusura apatwe na wazimu baada ya kuisoma kadi ile. Margreth akaingia mara akastukia dada yake amesimama ghafla na kumkumbatia.
“Dada kuna nini? akauliza margreth kwa mshangao.
“Its Patrick”
“Patrick!!!!”
“Yes .Look at this” akasema Happy akimuonyesha Margreth ile bussines card
“Mhhh”margreth akaguna.
Wakati margreth akiisoma ile kadi mlango ukagongwa na likaingia kundi la warembo. Wote wakafurahi baada ya kumkuta Happy ni mwenye furaha namna ile.
* * * *
MISS TANZANIA AZIMIA JUKWAANI , HAPPY KIBAHO MISS TANZANIA MPYA , ZENGWE LATAWALA UKUMBINI MISS TANZANIA AZIRAI.
Hivyo vilikuwa ni baadhi ya vichwa vya habari vilivyotanda katika magazeti mengi kwa siku hiyo. Karibu magazeti yote yalijaribu kuandika kwa kina juu ya tukio la kuzimia kwa miss Tanzania ukumbini, lakini hakuna hata gazeti moja lililoweza kuandika au kuufahamu ukweli juu ya tukio lile.
Akiwa katika kibanda cha kuuzia magazeti asubuhi hiyo Andrew alinunua karibu kila gazeti lililotoka siku hiyo na kupitia habari ya kuanguka kwa Happy. Lengo lake kubwa ni kutaka kufahamu kama kuna mtu yeyote aliyeweza kumtilia shaka Patrick kuwa ndiye aliyekuwa chanzo cha tukio lile la kuanguka Happy ukumbini. katika magazeti yote hakukuta habari yoyote iliyomuhusisha Patrick na tukio lile.
Akatoa simu yake na kumpigia Patrick.Simu ikapokelewa na Vero
“Hallo shemeji”akasema Vero.
“Shemeji mambo vipi? habari za toka jana ? Andrew akauliza
“nzuri tu shemeji”
“Vipi jamaa bado kalala?
“Ameingia maliwatoni kidogo anakuja sasa hivi” Muda huo huo Patrick akatokea Vero akampa simu na kumwambia Andrew anahitaji kuongea naye.
Hallow Andrew vipi ? Akasema Patrick
“Poa Patrick vipi maendeleo yako ?
“Nashukuru Mungu Andrew naendelea vizuri. Hebu nipe habari’
“Habari ni ndefu kidogo lakini kwa ufupi tu ni kwamba leo sijalala kabisa. Baada ya kuachana pale ukumbini nikamrudisha Vick kwake halafu nikaanza kufuatilia Happy alipelekwa hospitali gani. Kwa msaada wa rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari nilifanikiwa kujua mahala Happy Alikopelekwa.
Unajua walificha juu ya mahala alikopelekwa Happy kwa kuwakwepa waandishi wa habari. Alipelekwa katika hospitali moja ya kanisa maeneo ya msasani. Mpaka saa kumi na mbili nilikuwa pale hospitali na ndipo nilipopata taarifa kuwa tayari Happy alikuwa amezinduka.
Kuna muuguzi mmoja anafahamiana na Vick pale na ndiye huyo aliyenipa msaada mkubwa sana. Nilimpa kiasi Fulani cha pesa yule muuguzi na kumuomba aipeleke business card yako kwa Happy na kumwambia apige namba zile zilizoandikwa katika business card hasa muda wa mchana.
Yule muuguzi akajitahidi na kuifikisha kadi ile .Baada ya kuhakikisha tayari Hapy ameipata mimi nikaondoka. Kabla sijafika nyumbani nikaona nipite kwanza katika kibanda cha magazeti ili nione magazeti yanasema nini lakini hakuna chochote kibaya.
Kwa hiyo Patrick nina imani muda wowote Happy anaweza akakupigia simu. Mimi kwa sasa nakwenda nyumbani kupumzika tutaonana baadae ila be carefull brother’ akasema Andrew.
Patrick akavuta pumzi ndefu kisha akasema
“Sijui nikushukuruje Andrew kwa msaada huu mkubwa . thanks a lot. Dont worry I’ll be careful. see you later” Patrick akakata simu kisha akaelekea jikoni ambako Vero alikuwa akiandaa stafstahi akamsaidia kuandaa mlo wa asubuhi kitendo ambacho Vero alikifurahia sana.
* * * *
Saa sita kamili mchana Happy akaruhusiwa kutoka hospitali.Akiwa na furaha isiyokifani huku ameongozana na mama yake pamoja na mdogo wake kipenzi Margreth bila kumsahau mwenyekiti wa kamati ya Miss Tanzania pamoja na wajumbe kadhaa wa kamati hiyo na ujumbe wa watu toka Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano hayo walilakiwa na kundi kubwa la warembo waliokuwa wakisubiri atoke kwani walikwisha taarifiwa kuwa angeruhusiwa mchana.
Walitumia kama robo saa kusalimiana na kupongezana vile vile kupeana pole kwa yaliyotokea. Kisha akapanda gari na kuelekea nyumbani kwao.Happy alikuwa ni mwenye furaha sana mchana huo.
Ni margreth pekee ndiye aliyefahamu siri ya furaha ile aliyokuwa nayo dada yake.Akiwa garini Happy akafumba macho kana kwamba amelala lakini alikuwa amezama katika mawazo na mara akajikuta akitamka kwa sauti.
"Thanks God I found him" Mama yake aliyekaa kiti cha mbele aligeuka na kumuangalia mwanae bila kusema kitu. Margreth yeye alikuwa katika lindi la mawazo na hasa akijaribu kuvuta taswira ya kinachoenda kutokea huko mbeleni.
Anafahamu wazi kuwa katika dunia hii Patrick ndiye mwanaume pekee ambaye Happy anampenda . Licha ya kupotezana kwa muda mrefu lakini bado taswira ya Patrick haikufutika moyoni mwake.
Kwa sasa Happy tayari ana pete ya uchumba ambayo amevishwa na mchumba wake aitwaye Mike cambell raia wa Marekani. Mike ni kijana anayependwa sana na kila mtu katika familia ya akina Happy . Pamoja na kuwa na pete ya uchumba kidoleni bado Happy ameshindwa kuifuta kabisa kumbukumbu ya Patrick moyoni mwake.
Kuonekana kwa Patrick ni wazi kunaweza kusababisha mvurugano mkubwa ambao ni vigumu kujua hatma yake itakuwa nini. Ni wazi Mike alimpenda Happy kupita maelezo. Hiki ni kitu kilichomuumiza kichwa Margreth.
Baada ya mzunguko mrefu hatimaye wakawasili nyumbani ambako walilakiwa na kundi jingine la warembo,ndugu jamaa marafiki na waandishi wa habari wote walifika kumpongeza na kumpa pole Happy . Kisha salimiana na kupongezana Happy akaomba aachwe kidogo apumzike.
Happy akaoga na kupata chakula kisha akaingia chumbani kwake kupumzika.Kitu cha kwanza kabisa ambacho alikifanya ni kuitazama tena ile business card kwa makini .akaichukua simu yake na kuandika namba zile zilizoandikwa pale juu kisha akapiga.
Mapigo ya moyo wake yalikuwa yakienda kwa kasi ya aina yake alipoiweka simu sikioni akaisikia ikiita. Mikono ilianza kuloa jasho kwa wasi wasi.Hakujua angeongea nini baada ya kuisikia sauti ya Patrick. Hakujua Patrick angekuwa katika hali gani mara atakapoisikia sauti yake.
Wakati akisuburi kujibiwa na sauti ambayo aliamini moja kwa moja ingekuwa ni ya Patrick akasikia kitu ambacho hakukitarajia. Ilikuwa ni sauti ya mwanamke ndiye aliyepokea simu ile ya Parick.
“hallow” Ikasema sauti ya upande wa pili.
Happy mikono ilimtetemeka,akapatwa na kigugumizi cha ghafla kilichomfanya ashindwe kuongea.
“hallow naongea na nani?” ikauliza tena ile sauti ya mwanamke.
Happy akashindwa ajibu nini akabaki ameiweka simu sikioni.
“Haloo nani mwenzangu?Ikauliza tena.. Tayari Happy chozi lilikuwa likimtoka. Mara akasikia simu ikikatwa. Kitendo kile kikamuuma akajitupa kitandani machozi yakimtoka.
“Oooh Lord why me?? Why me God? I love Patrick .Yes ni yeye tu ndiye mwanaume ninayempenda kwa dhati ya moyo wangu .Nimetengana naye muda mrefu sana na sielewi maisha yake kwa sasa nadhani tayari ana mke .Sielewi kama ninaweza vumilia nikisikia Patrick ana mke.’ akawaza Happy
“Patrick I’ll fight for you and I must win you back. You are mine Patrick . I lost you once and now I’ve found you I’ll never loose you again” Happy alikuwa akiongea peke yake maneno haya huku machozi yakimchuruzika.
* * * *
Patrick leo huamki? akasema Vero huku akimtingisha Patrick ambaye alikuwa amelala tangu alipokula chakula cha mchana. Patrick akajigeuza na kuangalia saa kubwa ya ukutani. Ilionyesha ni saa kumi na moja za jioni.
“Oh nimelala sana” akasema Patrick kwa uchovu
“Ni vizuri hata hivyo ukipata mapumziko ya kutosha” akasema Happy. Happy akaelekea jikoni akaleta juice na kummiminia Patrick katika glasi.
“Halafu nimekumbuka kuna mtu alikupigia simu nikaipokea lakini cha ajabu hakutaka kuongea kitu chochote . Nimemuuliza zaidi ya mara mbili yeye ni nani lakini hakunijibu.” akasema Happy na kumfanya Patrick astuke.
Mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi.. Kijasho kikaanza kumtoka .akaichukua simu na kuziangalia namba zile zilikuwa ni ngeni kabisa kwake. Hakufahamu zilikuwa ni namba za nani lakini akahisi huenda Happy ndiye aliyepiga.
Kwa mujibu wa maelezo ya Andrew ni kwamba alimuelekeza Happy apige mida ya mchana. Vero akainuka akatoka mle chumbani,Patrcik akaitumia nafasi hiyo kupia zile namba. Simu ikaita bila kupokelewa,ikakatika. Akapiga tena mambo yakawa ni yale yale. Akapiga kwa mara ya tatu simu ikapokelewa.
“Hallow” Ilikuwa ni sauti tamu sana ya mtoto wa kike. Sauti hii Patrick hajaisahau mpaka hvi sasa. Ni sauti ya Happy. Kabla Patrick hajaongea lolote simu ikakatika. Patrick akaipiga tena na safari hii akaambiwa kuwa simu anayopiga haipatikani tena. Akajaribu kupiga tena na tena lakini simu haikuwa ikipatikana.
Patrick akaitupa simu kitandani kwa hasira .Hakuelewa sababu ya Happy kumkatia simu. Sauti aliyoisikia ilikuwa ni ya Happy. Patrick akasimama na kuzunguka zunguka humo chumbani Vero akarejea na kumshangaa kwa namna alivyobadilika ghafla.. Vero akamtazama akapatwa na wasiwasi.
“Patrick dear kuna kitu gani kibaya mbona umebadilika ghafla hivyo? Patrick akastuka na kumtazama Vero..
“Usiogope Vero.Mimi niko sawa kabisa." akasema Patrick lakini ndani ya moyo wake Vero alifahamu kabisa kwamba kuna ambo linamsumbua Patrick.
“Relax my dear jitahidi usiumize kichwa chako kwa mawazo .Kaa chini tuendelee kupanga mipango ya harusi yetu.” Patrick akastuka kwa ndani baada ya kuisikia habari ile ya harusi. Toka amemuona Happy alisahau kabisa kama anatakiwa kuendelea na mipango ya harusi yake na Vero. Kijasho kikamtoka.
" Vero naomba niendelee kupumzika nitakapoamka tutaendelea na majadiliano." akasema Patrick na kupanda kitandani. Akafumba macho na kurejesha kumbu kumbu za nyuma. Akakumbuka toka siku ya kwanza aliyokutana na Happy.
SEHEMU YA KWANZA
MTUNZI: PATRICK .C.K
==========
Haki zote zimehifadhiwa hairuhusiwi kunakili, kuchapa maandiko ya kitabu hiki bila idhini ya wahusika wakuu.
“Patrick amka darling, inakaribia saa nne sasa”, alisema Veronika kwa sauti laini ya kubembeleza.
“‘Mmmmhhh” Akaguna Patrick ,akajigeuza upande wa pili na kulivuta zaidi shuka.
“Amka ukaoge” Alizidi kubembeleza Veronika. Kwa uvivu Patrick akaamka na kuelekea bafuni kuoga.Dakika chache baadae alitoka akiwa amechangamka.
"Kweli maji ni dawa nzuri ya uchovu. Sasa najisikia safi kabisa.Nadhani kwa sasa itabidi nipunguze muda wa kufanya kazi. Nimekuwa nikifanya kazi kwa masaa mengi sana kwa siku kiasi kwamba nakosa hata muda wa kupumzika. Naogopa tukija kuoana nisije kushindwa kutimiza majukumu yangu kama mume kwa sababu ya uchovu” akasema Patrick na kumfanya Vero atabasamu halafu akatoa kicheko cha chini chini na kusema.
“Kweli mpenzi jitahidi kwa sasa kupata muda wa kutosha wa kupumzika.”
“Nitajitahidi baby”
Baada ya kuhakikisha sasa yuko safi Vero akamshika mkono Patrick na kumpeleka sebuleni kupata stafstahi.
“Patrick dear nataka unisindikize Supermarket nikafanye manunuzi ya vitu vya ndani. Si unajua kesho Andrew na vicktoria wameahidi kututembelea”Akasema Veronika wakati wakiendelea kupata chai.
“Mhh! Vero nenda mwenyewe mimi niache nipumzike".Patrick akajibu.
“Jamani dear usifanye hivyo naomba unisindikize ,mimi naona uvivu kwenda peke yangu”
"Haya mama, tumalize chai twende ili tuwahi kurudi”
“Nashukuru dear”.
Katika vitu ambavyo Veronika alibarikiwa kuwa navyo ni uwezo wake mkubwa wa kushawishi.
* * * *
Veronika Rugi alikuwa ni msichana mrembo mwenye mvuto wa aina yake.Binti huyu licha ya kujaliwa kichwa kizuri chenye nywele laini, nyingi na ndefu, alikuwa na uso mpana wa mviringo ulionakshiwa na macho mapana yenye kurembua muda wote.
Midomo mizuri ,laini ambayo akikupiga busu hutatamani abanduke mdomoni. Mtoto huyu alijaliwa shingo murua ambayo iliungana na kiwiliwili kilichokuwa na kifua chenye kupendeza kilichobeba chuchu changa zenye kusisimua,zenye kuwatoa udenda wakware. Kimwana huyu mwenye uzuri usiopimika alijaliwa umbo la utatanishi kuanzia kiunoni kushuka chini. Ni wasichana wachache sana waliopewa upendeleo wa namna hii na manani..
Pamoja na sifa hizo zote za nje lakini bado alikuwa na sifa lukuki za ndani.Kikubwa zaidi kinachomfanya apendwe na kila mtu ni uwezo wake mkubwa wa kuelewa mambo.Ni binti mwenye roho nzuri ya huruma na upendo asiyependa kujivuna wala kujikweza licha ya uwezo mkubwa familia yake ilionao.
Ni binti mwenye heshima kwa watu wa rika zote ,mcheshi,asiyependa ubinafsi na zaidi ya yote ni mtu anayejua kupenda. Veronika ambaye bado anaishi na mama yake mzazi baada ya baba yake kufariki miaka kadhaa iliyopita ,alikuwa ni mtoto wa tatu na wa mwisho katika familia ambayo haikubahatika kuwa na mtoto wa kiume.
Dada mkubwa wa Veronika aliyeitwa Loniki hivi sasa anafanya kazi katika shirika la ndege la British airways ,ameolewa na anaishi nchini Uingereza.
Mtoto wa pili kuzaliwa katika familia hii ni binti mrembo sana Sarah ambaye aliwahi kushika nafasi ya tatu katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa.naye amekwishaolewa na ni afisa mahusiano wa benki moja mpya kabisa nchini iitwayo African meckat bank.
Mtoto wa tatu na wa mwisho ni Veronika ambaye bado hajaolewa ,ila alikuwa katika hatua za mwisho za kukamilisha maandalizi ya ndoa yake na mchumba wake Patrick.
Ni hivi karibuni tu amehitimu shahada yake ya kwanza ya biashara katika chuo kikuu cha dar es salaam.Yeye ndiye msimamizi mkuu wa miradi yote ya familia kwa sasa.
* * *
“Patrick mpenzi nilisahau kukwambia toka mapema kuwa dada Loniki alifurahi sana kusikia tunataka tukafanye shopping ya harusi yetu nchini Uingrereza. Ameahidi kuwa yeye na mumewe watagharamia safari nzima ya kwenda na kurudi na gharama zote za
manunuzi. Amesisitiza kuwa tusitumie hata shilingi yetu. Kwa maana hiyo wiki hii nataka niende tena kufuatilia yale maombi yetu ya viza pale ubalozini. Nadhani kama Mungu akijaalia basi ndani ya wiki mbili zijazo tutakuwa tumeshakamilisha taratibu zote zinazotakiwa.” Alisema Vero huku akijiegemeza karibu zaidi na kifua cha Patrick.
Muda huo ilipata saa mbili za usiku , bado walikuwa wakipunga hewa safi baada ya mlo wa jioni.
“Wow! Hongera sana Vero kwa kuwa na ndugu wakarimu na wenye upendo wa hali ya juu sana kama ulivyo wewe. Tena umeongea kuhusu Loniki nimekumbuka zile CD alizonitumia wiki iliyopita. Unajua sijatazama hata moja.Hebu twende ndani nikaitazame ile filamu mpya ya Jack bauer.”
Akasema Patrick huku akijiinua toka pale walipokuwa wameketi na kuelekea sebuleni. Vero naye akakusanya vitu vyote vilivyokuwapo chini naye akaingia ndani.
“Vero mbona ile CD ya Jack bauer siioni hapa au Andrew aliichukua?Akauliza Patrick baada ya kuitafuta CD ile bila kuiona.
“Yawezekana Andrew aliichukua kwa sababu siku ile aliing’ang'ania sana.Nakumbuka kuna CD alizichukua hapo nadhani na hiyo nayo ilikuwapo”. Akasema Vero
Patrick akalifunga kabati ,akaelekea katika friji akafungua na kujimimia Juice katika glasi. Vero alikuwa ameketi sofani akitazama Luninga.
“Patrick , Miss Tanzania mwaka huu itakuwa na ushindani mkubwa sana kwa sababu mabinti ni warembo kupita maelezo. Mhh………..” Akasema Vero huku amekodoa macho yake katika Luninga kubwa iliyokuwamo humo sebuleni.
“Kwani fainali za miss Tanzania ni lini?” Patrick akauliza
“Ni jumamosi ijayo na itafanyikia pale Diamond Jubilee. Kutapambwa na onyesho kali la Malaika band,vile vile wana Fm academia na wasanii wengine kibao watakuwepo.Nataka kesho nikakate tiketi zetu za V.I P ili tusikose nafasi siku hiyo” Alisema Vero.
Akiwa na juice yake mkononi Patrick akajisogeza taratibu kuelekea mahali alipokaa Veronika . Kabla hajafika sofani alisimama akapiga funda la juice kisha akaelekeza macho yake katika luninga
“Naitwa Neema, ni mrembo toka kanda ya kaskazini. Ni miss Arusha. Napendelea sana muziki wa dini, kusoma na michezo mbali mbali. Nategemea kuwa mwanamitindo wa kimataifa. Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitajikita zaidi katika kuwasaidia watoto yatima kwani naelewa mateso na machungu wanayoyapata kwa kutokuwa na wazazi wao. Naombeni kura zenu namba yangu ya ushiriki ni ishirini.”
Alikuwa ni mrembo wa Arusha akijinadi katika kipindi maalum cha kuwatambulisha washiriki wa kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Tanzania kilichorushwa moja kwa moja na televisheni ya Taifa.
“Du! Si mchezo” Aliguna Patrick huku akiisogelea zaidi Luninga
“Nimekwambia Patrick warembo wa mwaka huu si mchezo. Hebu kaa uangalie jinsi watoto walivyo wazuri ” Akasema Vero.
“Naitwa Happy Kibaho. Ni mrembo wa wilaya ya Ilala. Napendelea sana muziki laini,kusoma hadithi ,magazeti, kutazama luninga,na wanyama. Nategemea kuwa mwanasheria .Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitaelekeza nguvu zangu zote katika kuwasadia vijana wajasiria mali ikiwa ni pamoja na kuwatafutia wafadhili, nitaitumia kofia yangu kuiomba serikali ielekeze nguvu zake zaidi katika kuwasaidia vijana hawa katika kuwapatia mitaji na kuwatafutia masoko ya bidhaa zao wanazozizalisha ili kupambana na ongezeko la vijana wasiokuwa na ajira. Ninaomba kura zenu ili niweze kulitwaa taji hili la miss Tanzania kwani nina vigezo vyote vya kulitwaa taji hili. Namba yangu ya ushiriki ni 6.”
“Whaaaat!!!!........................” Patrick Akapiga ukelele mkubwa “Nooooooooooo!!..I cant bel……………………” ghafla glasi aliyoishika ikamponyoka ikaanguka na kuvunjika. Taratibu nguvu zikaanza kumwishia akadondokea sofani kisha akapoteza fahamu.
“Patrick , Patrick what’s wrong!!!...”Alihamaki Veronika huku akimsogelea Patrick pale sofani na kumtingisha.
“Patrick darling what’s wrong with you? Alizidi kuuliza Vero huku akimtingisha.
“Ooh ! Nooo...!!!!...Wake up Patrick” Alipiga ukelele baada ya kugundua kuwa Patrick hakuwa na fahamu. Vero akataharuki asijue afanye nini. Hakukuwa na mtu yoyote wa karibu ambaye angeweza kumsaidia .
Alitoka kutaka kwenda kuwaita majirani ,akafika mlangoni na kurudi tena ndani mpaka sofani alipolala Patrick.
“Patrick ! Patrick dear what’s wrong with you. Whats’s wrong Patrick!!!!!!!!!” Vero aliongea peke yake huku machozi yakimtiririka.
Pale pale akapata wazo la kumpeleka Patrick hospitali. Kwa nguvu zake zote akamuinua Patrick na kumpakia garini , akakimbia kufungua geti kisha akaingia garini na kuondoka kwa kasi ya ajabu pasi na kufunga mlango wowote wa nyumba. Kwa kasi ya ajabu Vero aliendesha gari hadi hospitali ya karibu maarufu kama Dr Heneriko hospital. Si mbali sana na makazi ya Patrick.
Huku akilia akapaki gari na kuingia ndani ,akawaomba msaada wauguzi .Haraka haraka wauguzi wakamchukua Patrick na kumuwahisha katika chumba maalum kwa ajili ya kumpatia huduma ya haraka.
“Hurry up !.hurry up.! Ooh Patrick what’s wrong with you?” Alilalamika Vero huku akiwaomba manesi waharakishe. Muda wote huo machozi hayakumkauka. Veronika alizuiliwa asiingie katika chumba cha huduma ya kwanza akaachwa hapo nje na mmoja kati ya manesi akiendelea kumfariji.
“Jipe moyo dada yangu Patrick atapona tu. Mtumaini Mungu.” Nesi yule alimbembeleza Vero kwa upole. Dakika kama 20 hivi baadae dokta Heneriko alimwita Vero ofisini kwake na kumuomba awe mvumilivu wakati wakiendelea kuishughulikia hali ya Patrick.
Dokta alitaka kufahamu nini hasa kilichopelekea Patrick kupoteza fahamu.
“Unajua dokta , Patrick ni mpenzi wangu na tuko katika maandalizi ya harusi yetu. Mimi siishi naye kwa sasa ila huja kwake kila mwisho wa wiki. Leo hii toka asubuhi alikuwa akilalamika kuwa alihisi uchovu mwingi . Tulitoka kidogo kisha tukarudi na akaendelea kupumzika. Usiku tukiwa sebuleni tukiangalia Tv nikaona mwenzangu akipiga ukelele akaishiwa nguvu na kuangukia sofani akapoteza fahamu. Kwa kweli sina hakika mpaka sasa ni kitu gani hasa kilichopelekea hali ile kutokea. Naomba Dokta ufanye kila linalowezekana ili Patrick apone. Niko tayari kutoa kiasi chochote cha pesa ili mradi apone.” Vero alishindwa kujizuia akaangua kilio.
“Nyamaza Vero, Hali ya Patrick inaendelea vizuri. nina hakika muda si mrefu atazinduka. Kwa hiyo yawezekana kuwa kuna habari yoyote aliyoitazama ambayo ilimpelekea Patrick kupata mstuko?
“Sidhani dokta kwa sababu wakati tunaangalia Tv hakukuwa na taarifa yoyote ya kutisha au kustusha inayoweza kupelekea mtu kupata mstuko hadi kupoteza fahamu. Tulikuwa tukiangalia washiriki wa miss Tanzania wakijinadi. Ni hilo tu” Vero akajibu.
Dokta Heneriko akanyamaza kimya kwa sekunde kadhaa kisha akasema,
“Kwa kumbukumbu zako toka umekuwa naye kuna siku yoyote tukio kama hili limewahi kumtokea zaidi ya leo?
“Hapana dokta tangu mimi nimekuwa naye halijawahi tokea tukio kama hili Patrick kupoteza fahamu.”
“Ok Vero hivi sasa waweza kwenda kupumzika na kutuacha sisi tuendelee kumuhudumia mgonjwa wako. Iwapo kutakuwa na mabadiliko yoyote tutakupigia simu kukutaarifu.Na kama itahijika kumuhamisha kumpeleka katika hospitali kubwa zaidi tutakutaarifu pia. Lakini kwa sasa hali yake inaendelea vizuri,mapigo ya moyo wake yako sawa na kila kitu kinaonekana kufanya kazi vizuri. Huu ulikuwa ni mstuko wa kawaida tu ambao unaweza kumtokea mtu yeyote na hasa akiwa na msongo wa mawazo.” Akasema Doctor Henry.
“No Dokta ,siwezi kwenda nyumbani bila kujua hali ya mpenzi wangu iko vipi. Nitalala hapa hapa . Nataka niwe wa kwanza kuniona pindi atakapofumbua macho. Samahani dokta naweza kuitumia simu yako kuongea na mama yangu na kumtaarifu juu ya ugonjwa wa Patrick”
Dokta Heneriko hakuwa na kipingamizi akamruhusu Vero aitumie simu yake. Vero akampigia simu mama yake na kumtaarifu juu ya tukio lile ,halafu akawapigia simu ndugu zake wote bila kumsahau Andrew rafiki mkubwa wa Patrick pamoja na Alois kaka yake Patrick. Wazazi wa Patrick walikuwa safarini nje ya nchi.
* * * *
Ilimchukua kama nusu saa toka Andrew apate taarifa ya ugonjwa wa patrick,kuwasili pale hospitali. Akiwa na mpenzi wake Vick walishuka garini na kukimbia kuelekea mapokezi. Mara tu baada ya kuingia hapo mapokezi walilakiwa na sura yenye kusawajika ya Vero. Alipowaona Andrew na Vick wakiingia humo hospitali Vero aliangua kilio ambacho kiliwachanganya zaidi Andrew na Vick.
“Where is Patrick??” Andrew akauliza huku akijikaza lakini ni wazi alikuwa akitetemeka
“Calm down Vero tuambie Patrick yuko wapi?” Aliuliza tena Andrew .Vick akamkumbatia Vero huku naye machozi yakimtoka.
Andrew alimfuata muuguzi aliyekuwa mapokezi na kumuuliza juu ya hali ya Patrick. Hakuridhika na jibu alilolipata ,kwa kasi akakimbia hadi katika ofisi ya Dokta Heneriko lakini hakumkuta. Taratibu akatoka humo ofisini jasho likimtiririka na kurudi mapokezi.
Tayari Alois kaka yake Patrick alikwisha wasili hapo hospitali akiwa ameongozana na mke wake nao wote waliungana na Vick katika kumbembeleza Vero. Andrew akawasalimia kisha akamvuta mkono alois wakasogea pembeni kidogo.
“Hebu niambie Andrew kitu gani kinachoendelea hapa na Patrick yuko wapi ? Aliuliza Alois huku naye jasho likimtiririka
“Brother Aloia hata mimi mpaka muda huu sielewe chochote kwani toka nimefika hapa muda mfupi uliopita sijaweza kuongea lolote na Vero. Ila kwa maelezo niliyoyapata toka kwa muuguzi ni kwamba Patrick yuko katika chumba cha huduma ya kwanza akipatiwa matibabu. Nasikia ni mstuko ndio uliopelekea akapoteza fahamu”
Mara dokta Heneriko akatokea. Muuguzi aliyekuwapo mapokezi akamtambulisha kwa akina Andrew.
“Dokta hawa ni ndugu zake Patrick wamefika sasa hivi na walitaka kupata taarifa juu ya maendeleo ya mgonjwa wao’.
Dr henry akawasalimu wote halafu akawaomba Alois na Andrew wamfuate ofisini kwake..
“Vijana wangu kwanza poleni sana kwa matatizo ‘ “Ahsante sana dokta tumeshapoa” Wakajibu kwa pamoja
“sasa vijana wangu nimewaiteni hapa ili tuongelee zaidi suala la ndugu yenu.. Patrick aliletwa hapa kwangu usiku huu akiwa amepoteza fahamu. Kwa haraka nikisaidiana na madokta wenzangu tumejitahidi kumpatia huduma ya kwanza na mpaka sasa maendeleo yake ni mazuri. Tumejitahidi kuyashusha mapigo ya moyo yaliyokuwa juu sana na kwa sasa yako kawaida. Taratibu anaanza kurejewa na fahamu zake ingawa bado anahitaji kupumzika zaidi kwani bado fahamu hazijarejea vizuri. Maendeleo yake ni mazuri na baada ya muda mfupi ujao basi atarejea na fahamu zake zote.” Alois akashusha pumzi nzito kwa kusikia taarifa ile ya dokta. Akatoa leso na kujifuta jasho lililokuwa likimtirirka kwa kasi muda huo.
“Thanks God” Alisema Alois huku ameinua mikono juu ishara ya kumshukuru Mungu
“Kwa hivi sasa bado ataendelea kuwapo katika uangalizi maalum mpaka hapo hali yake itakapokuwa nzuri kabisa.Tatizo lililompata ni mstuko wa moyo. Ni tatizo la kawaida kutokea. Ila hali yake itakapokuwa nzuri tutamshauri aonane na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo ili aweze kumfanyia uchunguzi zaidi katika moyo wake ”
Baada ya kupata maelezo ya kutosha toka kwa dokta, Alois na Andrew waliridhika kabisa na dokta akawashauri waende kupumzika mpaka kesho . Alois alikubaliana na wazo hilo lakini akashauri andrew awarudishe kwanza Vero na Vick nyumbani wakapumzike.Yeye atabaki pale kuangalia hali ya Patrick inavyokwenda.
Wakati wakiendelea kujadili mama yake Vero akatokea. Akawasalimu wote aliowakuta hapo kisha kwa wasiwasi akataka kujua juu ya hali ya Patrick. Alipewa maelezo mafupi ya hali ya mgonjwa halafu akaomba aonane na dokta Heneriko, akaongea naye na kupewa kwa muhtasari juu ya hali ya Patrick na maendeleo yake na akahakikishiwa uangalizi wa hali ya juu.
“Ok . sasa utaratibu gani unaoendelea hapa? Aliuliza Bi stella Rugi mama yake na Vero.
“Tumepanga kuwa Andrew awarudishe nyumbani Vero na vick wakapumzike ,mimi nitaendelea kubaki hapa hapa na kufuatilia hali ya mgonjwa” Akasema alois
“Vizuri ,basi msipate shida ,Vero na Vick nitaondoka nao mimi na kwenda nao nyumbani kwangu , Andrew nenda nyumbani kwa Patrick ukahakikishe kuko salama .Alois utaendelea kubaki hapa kumwangalia mgonjwa .Nitakuwa nakupigia simu mara kwa mara ili kujua maendeleo ya mgonjwa ." akasema mama yake Vero
“sawa mama tumekuelewa .” Andrew na alois waliitika kisha wote wakatawanyika na kumwacha Alois hapo hospitali
Saa saba usiku Patrick akarejewa na fahamu zake kamili. Kitu cha kwanza kuhisi ni harufu kali ya dawa akageuza shingo kutazama pande zote akatambua kuwa pale alikuwa hospitali. Taratibu akavuta kumbukumbu za nyuma na mara akakumbuka kitu kilichopelekea yeye kuwepo pale.
“I saw her. I real saw her. she’s alive” Alijikuta akitamka maneno haya huku jasho likikimtiririka na mapigo yake ya moyo kwenda kasi .
Muuguzi aliyekuwa akimuangalia aliingia ndani na kumkuta tayari Patrick amerejewa na fahamu na amekaa kitandani. Haraka akaenda kumwita daktari. Dk heneriko alikuja kwa kasi na kumpima akagundua kuwa bado mapigo ya moyo wa Patrick yalikuwa juu sana.
“‘Lazima kuna kitu kinamsumbua huyu si bure”Akawaza dokta Heneriko.
“Patrick “Dokta akamwita baada ya kumaliza kumfanyia vipimo.
“naam dokta”Aliitika Patrick kwa sauti yenye kukwaruza.
“Pole sana “
“Ahsante sana dokta”
“Patrick kijana wangu usijali utapona tu hali yako inaendelea vizuri. Unahitaji kupumzika sasa mpaka asubuhi tutakapochukua tena vipimo vingine”
“Sawa dokta.” akajibu Patrick
“Endelea pumzika Patrick na iwapo utahitaji kitu chochote muuguzi yuko hapo nje na atakuwa akija hapa mara kwa mara kukuangalia. Tena nimekumbuka kaka yako yuko nje muda sijui kama ungependa kumwona?” Akasema dokta heneriko.
“Ndiyo dokta naomba uniitie..” Dokta Heneriko akafungua mlango na kutoka. Alois alikuwa amesinzia katika sofa lililoko mapokezi Mara akastuliwa na sauti ya Dokta Heneriko.
“Alois ,Patrick amekwisha rejewa na fahamu zake kamili kwa hiyo unaweza kwenda kumwona. Ila tafadhali usijaribu kumuuliza chochote kuhusiana na kilichopelekea yeye kupoteza fahamu. Ongea naye maongezi mengine ya kawaida. sawa?”
“sawa dokta” Alijibu Patrick huku akifikicha macho yaliyojaa usingizi. Muuguzi aliyekuwepo mapokezi akampeleka hadi katika chumba alimolazwa Patrick.
“Vipi Patrick unajisikiaje kwa sasa? Akasema Alois
“Sasa hivi sijambo brother najisikia vizuri. nashukuru kwa kuja kuniona”
“Usijali Patrick kwa sasa endelea kupumzika. bado unahitaji mapumziko ya kutosha. Mimi niko hapo nje.i”
“Vero yuko wapi?” Akauliza Patrick
"Vero amechukuliwa na mama yake. Andrew amekwenda nyumbani kwako kuhakikisha kuko salama" akasema Alois.
"Naomba umpigie simu na umwambie kwamba niko salama, asiwe na mawazo" akasema Patrick
"Sawa Patrick ngoja nimfahamishe" akasema Alois.
* * *
Baada ya kulia sana hatimaye kiusingizi kikaanza kumchukua na taratibu akajikuta akianza kulala. Hazikupita hata dakika kumi toka aanze kusinzia simu yak ikaanza kuita na kumstua toka usingizini. Alipoiangalia simu yake ilikuwa imeandika jina Alois. Aliogopa kuipokea simu ile akabaki akiiangalia ikiiendelea kuita. Mikono ilikuwa ikimtetemeka . Alihofia pengine simu ile inaweza kuwa imebeba ujumbe mbaya kuhusu Patrick.
Simu iliita ikakatika ,ikaanza kuita tena. Akaamua kuipokea. “Haloo” Akaita Vero
“Haloo Vero unaendeleaje ? akasema Alois.
“naendelea vizuri shemeji vipi huko kwema ? Akasema vero huku mapigo yake ya moyo yakienda kwa kasi isiyo ya kawaida.
“Huku kwema tu shemeji. Nataka nikufahamishe kuwa Patrick tayari amekwisha rejewa na fahamu zake na nimetoka kuongea naye muda si mrefu. Kwa hivi sasa anaendelea kupumzika. Amenituma nikwambie kwamba usiwe na wasi wasi yeye ni mzima wa afya.” Vero akashusha pumzi ndefu akakaa kimya kwa sekunde kadhaa kisha akamuaga Alois na kukata simu. Alipokata simu akaanza tena kulia kwa kwikwi.. Vick ambaye alikuwa katika usingizi mzito akaamka baada ya kustushwa na kilio cha Vero.
“Vero nini tena"?
“Patrick anaendelea vizuri.Alois amenipigia simu sasa hivi na kunifahamisha.”
“sasa kama hajambo unalia nini?
“Huwezi jua Vick ni jinsi gani nisivyopenda kumuona Patrick akiumwa kwa jinsi ninavyompenda.. Ninalia kwa mateso ninayoyapata juu yake.” Vick akambembeleza vero hadi akanyamaza kisha akajilaza kitandani na kuanza kutafakari.juu ya tukio zima..
Alikumbuka walikuwa sebuleni wakiangalia luninga ambapo warembo wanaotarajia kuwania taji al miss Tanzania walikuwa wakijinadi . Alivuta picha na kumuona Patrick akiwa katika friji akijimiminia kinywajii katika glasi ambapo muda huo Miss arusha Neema alikuwa akijinadi. Alikumbuka kumuona Patrick alivyovutiwa ghafla na kipindi hicho cha warembo. Toka Neema hakumbuki ni mrembo gani aliyefuatia kujinadi ila anachokumbuka ni kwamba Patrick alipiga ukelele mkubwa wa kushangaa kitu halafu akaanguka na kupoteza fahamu.
“Ni dhahiri ni mstuko ndio uliomfanya Patrick aanguke na kupoteza fahamu .Lakini je ni kitu gani hasa ambacho kilimstua Patrick kiasi cha kupoteza fahamu?Je mstuko huu una uhusiano wowote na kipindi kile tulichokuwa tukitazama ? hapana . Patrick nimekuwa naye muda mrefu sasa na tabia yake ninaifahamu vizuri. Kuhusu wanawake siwezi kumsemea vibaya hana tabia hiyo ya kuwa na wanawake wengine nje ya mahusiano yetu. Nina uhakika na hilo. Sasa ni kitu gani kilichomstua ? Any way siwezi kupata jibu kwa sasa mpaka hapo atakaponiambia yeye mwenyewe kwani nina hakika hawezi kunificha kitu chochote.” Alikuwa akiwaza Vero na taratibu usingizi ukamchukua akalala.
* * * *
Saa kumi na mbili asubuhi iliwakuta Vero ,Vick na mama yake vero tayari wakiwa hospitali.Hali ya Patrick ilikuwa ikiendelea vizuri . Alfajiri hiyo tayari alikwisha hamishwa toka katika chumba cha uangalizi maalum na kuwekwa katika chumba cha mapumziko ya kawaida. Wakiongozwa na alois ambaye alilala hapo hospitali walielekea moja kwa moja chumbani na kumkuta Patrick tayari amekwishaamka. Bila kupoteza muda Vero akamkumbatia na kumpiga mabusu mfululizo.
“Pole sana my dear. Unajisiaje kwa sasa? akauliza Vero huku akitabasamu
“Najisikia vizuri sana” akajibu Patrick huku akijinyoosha nyoosha pale kitandani.
Baada ya kusalimiana kilifuata kipindi cha vicheko na utani wa hapa na pale kisha Vick na mama yake Vero wakaomba waondoke kwa ajili ya kwenda kujiandaa na mishughuliko ya siku. Vero alimwinua Patrick na kumpeleka bafuni ambako alimwogesha na kumrudisha tena chumbani , akamwandalia kifungua kinywa . Patrick alijisikia faraja kubwa kwa namna binti huyu alivyokuwa akimjali na kumuhudumia.
* * * *
“Andrew kwa kipindi kirefu sasa umekuwa ni msiri wangu mkubwa. Mambo yangu mengi ambayo sihitaji mtu mwingine kufahamu wewe wayajua.Urafiki wetu ni zaidi ya undugu. Naomba sana kile nitakachokuambia hapa usimwambie mtu yeyote yule.Itabaki kuwa siri yako mpaka pale muda muafaka utakapofika.” Patrick aliongea taratibu huku akijiweka vizuri sofani.
Ni siku ya kwanza tangu ameruhusiwa kutoka hospitali kwa sababu ya mstuko uliopelekea apoteze fahamu. Andrew rafiki mkubwa wa Patrick alikuwa kimya akiwa na shauku kubwa ya kutaka kulisikia lile ambalo rafiki yake alikuwa tayari kumwambia.
“I saw Happy ”akasema Patrick kisha akatulia na kuyaacha maneno yale yamwingie Andrew.
“What !! ” akauliza Andrew kwa mshangao
“I saw Happy ” Patrick alirudia tena kisha akainamisha kichwa chini na kuzama katika mawazo mazito. Andrew akainuka na kuanza kuzunguka zunguka mle chumbani huku akionekana dhahiri alikuwa ameshtushwa mno na kauli ile ya Patrick.
“Umemuona wapi?”andrew akauliza huku amejishika kichwa.
’‘Nimemuona kwenye luninga .Kulikuwa na kipindi cha kuwanandi warembo wanaoshiriki kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Taifa .Happy ni miss Ilala.”
“are you sure” Andrew akahoji
“I'm sure Andrew na hiyo ndiyo sababu iliyonifanya nikapata mstuko na kupoteza fahamu”Andrew akavuta pumzi ndefu ,akainuka akaanza kuzunguka zunguka humo ndani kisha akakaa. Vijana hawa wote kwa sasa walikuwa katika wakati mgumu sana.
Ni Andrew pekee aliyefahamu kilichokuwa kikiendelea kati ya Patrick na Happy na ndio maana alichanganyikiwa asijue afanye nini. Alimuonea huruma sana Patrick kwa wakati huu mgumu alionao.
“Vero aligundua chochote “Andrew akauliza tena
“sina hakika kama aligundua kitu chochote kwa wakati ule” akajibu Patrick
“ kwa hiyo tufanye nini sasa” Andrew akahoji.
Patrick akainuka na kwenda katika friji akjimiminia maji baridi kwenye glasi akapiga funda kubwa kisha akavuta pumzi ndefu na kusema.
“Nataka kuonana na Happy"
Kimya cha sekunde kadhaa kikapita hapo sebuleni kisha Patrick akaendelea
“Nataka kabla ya kuonana naye kwanza tumfanyie uchunguzi anaishi wapi,na nani ,anafanya kazi gani,ana mchumba au hana,na chochote kile tunachoweza kukifahamu kuhusu yeye. Uchunguzi huu nataka uwe wa siri na yeye Happy asiweze kufahamu kuwa anachunguzwa. Ikiwezekana tunaweza hata kuajiri mtu wa kuifanya kazi hii niko tayari kumlipa kiasi chochote cha pesa anachohitaji. Nakukabidhi kazi hii Andrew nina imani itafanyika ipasavyo. Tuko pamoja? Akasema Patrick.Andrew akavuta pumzi ndefu na kusema
“Nimekuelewa Patrick lakini suala hili haliwezi kuathiri maandalizi ya harusi yako ambayo tayari yanaelekea mwishoni?
“Hahahah ! usihofu kuhusu hilo my friend. I know what I’m doing ,ok?” akasema Patrick huku akicheka
“Una maana gani Patrick unaposema unajua unachokifanya ? Ninafahamu kuwa ndoto zako za siku nyingi ni kuwa na Happy katika maisha yako na kwa sasa umekwisha kuwa na uhakika kuwa yupo na kwa wakati wowote unaweza kumuona . Nina wasiwasi sana na huu ujio wa Happy katikati ya maandalizi ya Harusi yako unaweza kutibua kila kitu." akasema Andrew kwa wasi wasi
“Kwa ajili ya Happy niko tayari kwa lolote linaloweza kutokea. All these years I’ve been hurting myself thinking about her na mpaka sasa nimeshindwa kabisa kuifuta kumbukumbu ya Happy moyoni mwangu. Siwezi kuendelea kuutesa moyo wangu Andrew.I have to face her.” Akasema Patrick
“Patrick nafikiri unahitaji kufikiri zaidi kuhusu suala hili, si suala jepesi kama unavyolifikiri. Ni suala ambalo linagusa hisia za watu wengi .Hi…..” Andrew hakuendelea zaidi Patrick akadakia.
“Andrew I've made my decision and its final. Nilivyoamua nimeamua. Nitapambana kadiri ninavyoweza ili kuonana tena na Happy . I love her and I know she loves me too.” akasema Patrick. Andrew akamuangalai rafiki yake kwa makini na kusema.
“Patrick miaka mingi imepita tangu mpotezane na Happy na kila mmoja ameendelea na maisha yake. Tayari uko na Vero na kwa sasa bado kama mwezi mmoja na nusu hivi ufunge ndoa na Vero ,ndoa ambayo sehemu kubwa ya maandalizi yake yamekamilika. Huoni kuwa utakuwa unamnyima haki zake Vero kama ukihamishia mawazo yako yote kwa Happy .? Nina imani Vero anakupenda kwa dhati ya moyo wake na nina imani vile vile hata wewe unampenda Vero Kwa nini utake kumtesa Vero kiasi hiki ?
“Andrew nafahamu unachokisema .Ni kitu cha msingi sana lakini kama ungeigia viatu vyangu na kuona nini kilichomo ndani. Nina imani kubwa hata wewe ungefanya kama mimi ninavyotaka kufanya. Happy ni msichana wangu wa kwanza ambaye nilimpenda kupita ninavyojipenda mwenyewe. Ni kweli niko katika mahusiano na hivi karibuni ninatarajia kufunga ndoa na Vero lakini bado sura ya Happy haijaweza kunitoka moyoni mwangu. Please Andrew naomba msaada wako katika hili.Nisaidie nionane na Happy tafadhali.” akasema Patrick
“Nimekuelewa Patrick lakini bado moyo wangu una wasiwasi sana juu ya kinachoweza kutokea hapo mbeleni. Nafahamu kuwa endapo utaingia matatizoni basi ni sisi sote tutakuwa katika matatizo. Tatizo langu ni lako na lako langu ndio maana tunahitaji sana kushauriana kwa kina kabla ya kufanya jambo.”
“Andrew najua una wasiwasi mwingi kuhusu mimi na Vero.Hilo ni kubwa linalokuumiza kichwa. Hata mimi sijisikii vizuri kumtesa Vero binti aliyeyatoa maisha yake kwangu.Binti anayenipenda kwa dhati ya moyo wake. Ni vero huyu huyu ndiye aliyeirudisha tena furaha ndani ya moyo wangu na kuliondoa wingu zito la ukiwa lililokuwa limenifunika. Nampenda Vero lakini ni lazima nionane na Happy .” akasema Patrick.
Andrew akainuka kitini akachukua chupa ya mvinyo na kujimiminia katika glasi akanywa mafunda kadhaa kisha akamgeukia Patrick.
“Ok Patrick kwa sababu umekwishaamua basi hatuna budi kufanya hivyo. Mimi nitaianza kazi hiyo kesho. Nitamtafuta mtu ambaye ataifanya kazi hiyo kwa ustadi mkubwa. Usijali kuhusu hili ndugu yangu” Patrick alifurahi akainuka na kumkumbatia rafiki yake.
* * * *
Saa kumi na mbili za jioni Veronika alirejea katika shughuli zake na kumuaga mama yake kuwa alikuwa akaienda kumwangalia Patrick nyumbani kwake. N i siku ya tatu sasa toka Patrick atoke hospitali. Hali yake haikuwa ikiendelea vizuri sana.Muda mwingi alikuwa akionekana ni mtu mwenye mawazo mengi . Hali hii ilimpa wasiwasi mwingi Vero kiasi cha kumfanya awe karibu naye kila wakati ili kujaribu kumchangamsha na kumrudisha katika hali yake ya kawaida.
Ingawa Patrick alijitahidi kwa kila jinsi ili Vero asione hali hii ya mawazo mengi aliyokuwa nayo lakini mara nyingi alishindwa na kujikuta akitoa machozi. Vero aliigundua hali hii na kwa kiasi kikubwa ikamuongezea udadisi juu ya kinachoendelea . alijua ni lazima liko jambo ambalo linamchanganya Patrick
“Haloo sweetie” Alisema Vero baada ya kuingia ndani kwa Patrick
“Haloo vero ” akasema PatrickVero akamfuata Patrick kitandani akamkumbatia na kumpiga busu zito.
‘Unaendeleaje mpenzi”
“Naendelea vizuri Mungu ananisaidia sana. Muda si mrefu nitapona kabisa”.
Baada ya kujuliana hali Vero alimwandalia Patrick Juice kisha yeye akaelekea jikoni kufanya maandalizi ya chakula cha jioni.Patrick alipata faraja kubwa baada ya Vero kuwasili Ni wazi Patrick husikia furaha kubwa moyoni awapo na Vero. Ilimuuma sana baada ya kugundua kuwa alimpenda Vero lakini kwa ghafla Happy ametokea na kuanza taratibu kuzihamisha hisia zake. Chakula kilipokuwa tayari kikawekwa mezani,wakala kisha wakapumzika na baadae wakaelekea kulala.
“Vero dear tayari umekwisha kata tiketi za kuingia Miss Tanzania Jumamosi? Patrick akauliza
“Tayari mpenzi Nimekwishaziandaa . Utaweza kwenda na hali hii ? Naona kama hali yako inazidi kudhoofu siku hadi siku”
“Usijali mpenzi wangu lazima nihudhurie. Nina imani ndani ya siku mbili tatu zijazo hali yangu itakuwa shwari ”akajibu Patrick
Vero akanyamaza kimya akajaribu kuvuta kumbukumbu nyuma siku ile Patrick alipoanguka na kupoteza fahamu alikuwa akitazama kipindi cha wagombea wa miss Tanzania . Hakutaka kukubaliana kuwa kuna kitu chochote kinachoendelea baina ya Patrick na mashindano yale. Alijitahidi kuilazimisha akili yake ikubaliane na taarifa ya daktari kuwa Patrick alipoteza fahamu kwa sababu ya uchovu mwingi uliokuwa ukimkabili kiasi cha kuufanya ubongo wake ushindwe kufanya vizuri kazi yake.
“Lakini pamoja na taarifa ile ya daktari lakini kuna kitu kiko moyoni mwa Patrick ambacho kinamyima raha na kuisumbua akili yake . Ni kwa sababu hiyo tu ndiyo maana amepoteza furaha yote aliyokuwa nayo kabla. Chakula chenyewe mpaka abembelezwe. Mara kadhaa nimemfuma mwenyewe kwa macho yangu akilia. Ingawa anajitahidi sana kuificha hali hii lakini nimekwishafahamu . Anyway nitajitahidi kumuuliza ili anieleze kama kuna jambo lolote linalomsibu.” Veronika alizama ghafla katika mawazo.
“Unawaza nini mpenzi wangu”Patrick akauliza
“Nothing.Siwazi chochote zaidi yako.Unajua Patrick hali yako kwa sasa inanipa wasiwasi sana. Tangu umetoka hospitali umebadilika. Ni kitu gani kinakusumbua mpenzi hebu niambie. Hali hii inanifanya hata mimi nihisi kama vile ninaumwa pia. Au kama kuna kitu nimekukosea niambie Patrick ili nijirekebishe. Tangu tumeanza mapenzi yetu sijawahi hata siku moja kukuona katika hali hii” Vero akashindwa kujizuia akaanza kulia kwa kwikwi.
Patrick akamvutia Vero kwake akambusu na kumwambia
“Usihofu kitu baby hakuna kitu kingine kinachonisumbua .Kama daktari alivyosema kuwa natakiwa kupumzika sana .Uchovu ndio uliopelekea tatizo lile kutokea.”Akasema Patrick huku akizichezea nywele laini za Vero.
‘Hapana dear najua lazima kuna kitu kinachokusumbua akili na hutaki kuniambia”
“ my dear angel ,wewe ndiye maisha yangu.Wewe ndiye uliyeyashika maisha yangu. Nimekukabidhi funguo za moyo wangu. Wewe ndiye mfariji wangu,wewe ndiye furaha yangu,wewe ndiye kila kitu kwangu sasa kwa nini nikufiche kitu?Hakuna kitu nimewahi kukuficha wewe mpenzi wangu na haitakuja tokea nikawa na tatizo nikashindwa kukwambia. Sasa nisipokwambia wewe nitamwambia nani tena?”
Patrick alijitahidi kumtoa Vero wasiwasi aliokuwa ameanza kuwa nao juu yake na mara moja akaazimia moyoni kubadilika kitabia ili Vero asije akaendelea kumdadisi. Taratibu akaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ya ucheshi na uchangamfu mkubwa kitu ambacho Vero alikifurahia sana.
Ni jumamosi angavu ndani ya jiji la Dar es salaam, jiji lililojaa kila aina ya pilika na purukushani. Jua lilikuwa likielekea magharibi na kulipisha giza lichukue nafasi yake.Jioni hii iliwakuta Patrick na Veronika wakiwa katika pilika pilika za kujiandaa kuelekea katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa katika ukumbi wa Diamong jubilee.
Patrick ndiye aliyekuwa katika pilika pilika nyingi zaidi jioni hiyo. Siku hii ilikuwa ni moja kati ya siku zake kubwa kabisa katika maisha yake. Ni siku ambayo aliamini ingemkutanisha tena na kiumbe ampendaye kwa dhati ya moyo wake.
Alikuwa ndani ya suti nzuri ya gharama kubwa. Suti hii huwa anaivaa kwa nyakati maalum kama hizi. Hakika alikuwa amependeza vilivyo kijana huyu. Wakiwa katika harakati z a kumalizia kujiandaa simu yake ikaita. Alkuwa ni Andrew.
“Haloo Andrew”
“Hallo Patrick vipi mko tayari? aliuliza Andrew huku akicheka kichinichini.
“Tupo tayari Andrew na muda wowote toka sasa tunaweza kuanza safari ya kuelekea ukumbini”
“Ok Patrick sisi tayari tumekwishajiandaa na muda wowote tutakuwa njiani pia kuelekea huko na tutawasubiri nje ya ukumbi ili tuingie pamoja.Ila ndugu yangu nakuomba kitu kimoja katu usihamaki. Wala usionyeshe aina yoyote ya mstuko pindi utakapomuona Happy . Najua tu lazima kunaweza kutokea na kitu kama mstuko fulani utakaomuona Happy lakini naomba ujaribu kujizuia kwa sababu pale tutakuwa tuko na Vero na Vick kwa hiyo wanatakiwa wasihisi kitu chochote. Mimi nitakuwa macho kuhakikisha kuwa hakuna kitu chochote kitakachoharibika “
“Usihofu Andrew nalifahamui hilo na niko makini nalo sana..” akasema Patrick Baada ya kumaliza kujiandaa na kuhakikisha kuwa wako safi wakaingia garini na kueleka Diamond Jubilee.
* * * *
Ukumbi wa Diamond jubilee ulikuwa umefurika watu pasi mfano.Pamoja na ukumbi kufurika watu bado watu walikuwa wakimiminika ukumbini hapo kwa lengo la kushuhudia mchuano wa kumtafuta mrembo wa Taifa atakayeliwakilisha Taifa katika mashindano ya dunia. Patrick, Vero, Andrew na Vick waliwahi sana kuingia ukumbini na kuchukua moja kati ya meza za mbele kabisa. Patrick moyo ulikuwa ukimdunda sana usiku huo.
Andrew alilifahamu hilo na hivyo akawa makini sana katika kuhakikisha kuwa hakuna kitu kitakachoharibika .Toka wameingia ukumbini Patrick alikuwa kimya .
“Patrick are you ok? Vero akauliza baada ya kuona Patrick yuko kimya sana.
“Yes I’m ok Vero usihofu.”
Mara muongoza shughuli akatokea jukwaani na kuanza kutangaza.
“Mabibi na mabwana mliohudhuria mashindano haya makubwa ya urembo nchini napenda kuwakaribisha sana katika usiku huu wa pekee kabisa kwetu sote. Ni usiku wa pekee kwa sababu leo tutaandika historia mpya kabisa katika mashindano ya urembo hapa nchini na ulimwengu kwa ujumla. Kwa mwaka huu kamati nzima ya Miss Tanzania imeazimia kufanya mabadiliko makubwa sana na nyie wote mlioko hapa ndio mtakaokuwa mashahidi wa kile kitakachotokea usiku wa leo. Nasema karibuni sana katika usiku huu na tujumuike sote mimi naitwa Mc Thora kwa wale ambao hawanifahamu.."
“Mabibi na mabwana kabla hatujaendelea mbele na ratiba yetu ningependa kwanza kumkaribisha jukwaani mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainments ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu. Mabibi na mabwana makofi kwa Mr Petty.s Woris”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainments akapanda jukwaani akiwa amevalia nadhifu kabisa.
“viongozi mbali mbali ,watazamaji wote mliohudhuria mashindano haya usiku huu mabibi na mabwana asalaam aleikhum. Ni furaha ilioje kwetu sisi kama Masimulizi entertainments kudhamini mashindano makubwa kama haya ya urembo hapa nchini. Kama wote mnavyoshuhudia mashindano ya mwaka huu yamekuwa na utofauti mkubwa na mengine yaliyotangulia. Maandalizi yake yamekuwa mazuri , zawadi zimeboreshwa na ushindani miongoni mwa washiriki umeongezeka mara dufu.
Kwa kuwa ni mara yetu ya kwanza kudhamini mashindano makubwa kama haya bado kunaweza kuwa na kasoro kadhaa ambazo nina imani kwa kushirikiana na wadau wote wa urembo hapa nchini tutasaidiana kuzitatua. Nina imani bado tutaendelea kudhamini na kuandaa matamasha mengi na makubwa zaidi hapa nchini ili kuzidi kuukuza wigo wa burudani hususani sanaa hii ya urembo .
Mwisho kwa niaba ya uongozi na wafanya kazi wote wa Masimulizi entertainments napenda kuwatakia wote utazamaji mzuri wa mashindano haya usiku huu.Ahsanteni sana.”
Baada ya kumaliza kusema machache akarudisha kipaza sauti kwa muongoza shughuli kisha akashuka jukwaani.
“Mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mkurugenzi wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu.. Mabibi na mabwana kwa mujibu wa ratiba yetu kinachofuata kwa sasa ni kuwatambulisha majaji wa mchuano huu ambao ndio watakaofanya kazi kubwa na ngumu ya kutuchagulia mrembo mwenye sifa ya kuwa mrembo wa taifa. Majaji tulionao usiku huu ni saba. Ningeomba jaji utakaposikia jina lako likitajwa basi usimame ili watu wakufahamu.
Wa kwanza ni Mr Ernest Namesha, wa pili ni ndugu Mecky , tunaye pia Mr Boniventure Gregory, anayefuatia ni Mr Samweli Nathaniel, tunaye pia dada yetu mpendwa usiku huu naye ni dada Esther mathias, pia tunaye Mrs Coletha brown, tunaye vile vile bi Susan Abrahams na wa mwisho ni ndugu Jacob Lyimo. Hawa ndio majaji wetu ambao watakuwa wakifanya kazi ngumu ya kumchagua mrembo wa Taifa usiku huu wa leo.”
“Mabibi na mabwana baada ya kuwafahamu majaji wa mchuano huu wa leo sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 katika show maalum waliyoiandaa “ wimbo ukaanza kupigwa na warembo wakaanza kutoka huku wakicheza kwa staili yenye kuvutia sana.
Makofi nderemo na vifijo vikatawala ukumbini. Patrick alielekeza macho na akili yake yote jukwaani na bila kukosea alimuona Happy ambaye alikuwa amependeza kupindukia Jasho likaanza kumtiririka akatoa kitambaa na kujifuta. Alikuwa kimya kabisa.
Baada ya show ya warembo kukamilika ziliendelea burudani nyingine toka kwa wasanii mbali mbali kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana baada ya kupata burudani hizo zakukata na shoka sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 ili muwatambue. Watapita hapa jukwaani mmoja mmoja .”
Warembo wakaanza kutoka nyuma ya jukwaa na kuanza kupita mbele ya watazamaji. Kidogo Patrick atamke kitu baada ya kusikia jina la Happy likitajwa. Happy akapita jukwaani huku kelele za shangwe zikisikika.
Happy alikuwa akionekana kama malaika usiku huu. Alikuwa amependeza vilivyo. Kila mtu aliustaajabia uzuri wa binti huyu mwenye kila sifa ya kuwa mrembo wa Taifa na dunia. Kelele zile za mashabiki zilizidi kumchanganya Patrick na kumfanya ahisi kuchanganyikiwa. Andrew alikuwa makini sana kwa lolote ambalo lingeweza kutokea.
Baada ya kupita jukwaani kujitambulisha kwa mashabiki zikafuata burudani za aina yake toka kwa wanamuziki. Kisha Muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana mambo yanazidi kupamba moto. Mambo ni bam bam na kama nilivyowaeleza toka mwanzo kuwa Masimulizi entertainment wameleta mageuzi makubwa katika mashidano ya mwaka huu .
Kwa sasa napenda kuwaleta kwenu warembo wote 26 wakiwa katika vazi la ufukweni. Mhh ! hapa pana kazi kweli kweli .mabibi na mabwana hebu tuwashangilie hawa warembo wetu watakapokuwa wakipita jukwaani katika vazi la ufukweni.”
Warembo wakaanza kupita jukwaani wakiwa katika vazi la ufukweni. Siyo siri walikuwa wamependeza vilivyo. Baada ya kumaliza kupita na vazi la ufukweni zikafuata tena burudani halafu warembo wote wakapita tena kwa mara nyingine na vazi la ubunifu.
Kelele zilikuwa kubwa sana kila walipopita warembo Neema wa Arusha na Happy wa Ilala. Warembo hawa walionekana kuchuana vilivyo. Kisha pita na vazi la ubunifu muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana tayari tumewashudia warembo wetu 26 wakipita hapa mbele yetu wakiwa katika mavazi tofauti tofauti. Kwa sasa ule wakati mliokuwa mkiusubiri kwa hamu kubwa unaelekea kuwadia.K wa hivi sasa tutakwenda kuwafahamu warembo 10 bora ambao wameonekana kufanya vizuri zaidi . Naomba sasa nimkaribishe Mrs Coletha brown ili aje atutangazie wale warembo wetu kumi waliofanya vizuri zaidi.Karibu sana mama.”
Mrs Coletha brown akapanda jukwaani akiwa na karatasi yenye majina ya warembo kumi waliofanya vizuri na ambao wataendelea na mchuano.
“mabibi na mabwana napenda kuchukua nafasi hii kwanza kuwapongeza waandaaji wa mashindano haya ambayo kwa mwaka huu yameboreshwa kwa kiwango cha juu kabisa. Mabibi na mabwana kazi yetu usiku wa leo imekuwa ni ngumu sana . Warembo wote wako katika hali ya ushindani wa hali ya juu mno. Lakini tumeweza kuwapata wale kumi ambao ni bora zaidi na ambao nitaenda kuwataja hivi punde.
Nambari 12 Nelea shulo,nambari 9Saida abdi,nambari 4 Upendo timelo,Nambari 20 Neema ,Nambari 11 Esther stevens,Nambari 6 Happy Kibaho, nambari 22 Elimeena kimuo, nambari 26 bahati udhoka,nambari 16 Winifrida mwasajuki,na mwisho ni namba 13 genevieve alphonse.”
Kelele za kushangilia zikasikika ukumbini. Warembo waliofika hatua ya kumi bora wakajipanga mstari. wakapiga picha ya pamoja kisha zikafuata burudani .baada ya burudani mc akapanda tena jukwaani.
“Mabibi na mabwana bado tunaendelea na mchakato wetu wa kuifikia ile hatua kubwa kabisa ambayo kila mmoja wetu aliyeko hapa ana hamu ya kuishuhudia. Kila mmoja anatamani amfahamu mrembo wetu mpya wa Taifa. Kwa sasa tutaenda kuwatafuta wale watano bora ambao kutoka kwao tutampata mrembo wetu. Atapanda tena Mrs Coletha kuja kututangazia warembo watano bora .” mrs Coletha akapanda tena jukwaani akiwa ameongozana na watu wawili wa miraba minne wanaomlinda.
“mabibi na mabwana kama nilivyowaambia awali kuwa kazi yetu leo imekuwa ngumu sana hasa kutokana na jinsi warembo wote walivyo na vigezo vya juu mno kiushindani.Lakini pamoja na wote kuwa na ushindani wa juu tumeweza kufanikiwa kuwachuja na kupata wale watano ambao wameonekana kuwa ni bora zaidi. Warembo waliopita hatua ya tano bora ni mrembo nambari 16 Winifrida mwasajuki,nambari 20 Neema i,nambari 13 Genevieve alphonse,nambari 26 Bahati udhoka na mwisho ni nambari 6 Happy Kibaho .” Kelele kubwa zikasikika zikishangilia.
Kila mtu pale ukumbini alikuwa ameridhika na kazi waliyoifanya majaji. Hakukuwa na aina yoyote ya upendeleo. Baada ya kuwatambua warembo wote waliofanikiwa kuingia hatua ya tano bora hatimaye kikafuata kipindi cha maswali. Ni Happy kibaho tena ndiye aliyejibu swali vizuri zaidi na kuwafanya watu wote ukumbini kumshangilia kwa nguvu.
Kila mtu aliamini kuwa Happy ni lazima angeibuka kuwa mrembo wa Taifa. Patrick jasho lilikuwa likimtiririka mwilini. Alijitahidi kwa kila alivyoweza ili asiweze kuonyesha hali yoyote ya utofauti pale mezani.
Baada ya kipindi cha maswali kumalizika ikafuata burudani moja kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana ule wakati uliokuwa ukisubiriwa na kila mtu hapa ukumbini naona sasa umewadia. Huu ni wakati wa kumtambua mrembo wetu mpya wa Taifa. Napenda nichukue fursa hii kuwashukuru sana majaji kwa kazi ngumu waliyoifanya usiku huu kwa kutuchagulia mrembo mpya wa Taifa. Kabla sijamkaribisha jaji mkuu kuja kutangaza mshindi wa shindano hili napenda kumkaribisha mrembo anayemaliza muda wake ili aweze kuongea machache na kuwaaga rasmi kabla hajalivua taji la Miss Tanzania.”
Helen Daudi mrembo anayemaliza muda wake alipanda jukwaani huku akishangiliwa vilivyo. Alipewa kipaza sauti na kusogea mbele.
“mabibi na mabwana ,wageni waalikwa,waheshimiwa majaji ,waandaaji na wadhamini wote wa mashindano haya habari za usiku. Napenda kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha mimi kutimiza moja ya ndoto zangu nayo ni kuwa mrembo wa Tanzania.
Nawashukuru vile vile wazazi wangu na ndugu zangu kwa kunipa moyo toka katika hatua za awali za kinyang’anyiro hiki hadi nilipobahatika kuchukua taji. Mabibi na mabwana kulivaa taji la Miss Tanzania ni mzigo mkubwa. Nimeshuhudia mimi mwenyewe uzito wa taji hili kubwa la urembo hapa nchini. Yapo mengi ambayo unapaswa kulifanyia taifa hili ukiwa kama mrembo wa Taifa. Kuna mazuri na magumu yake. Zipo changamoto nyingi ambazo yakubidi upambane kufa na kupona ili uweze kushinda. Napenda kuishukuru kamati nzima ya Miss Tanzaina kwa ushirikiano mkubwa walionipa katika kipindi chote nilichokuwa nimevaa taji hili. Sintaweza kumtaja mmoja mmoja lakini napenda niwashukuru wote kwa ujumla
.Napenda niwashukuru vile vile wadau wote wa sanaa hii ya urembo hapa nchini kwa sapoti yao kubwa waliyonipa. Wamenisaidia sana kuifahamu sanaa hii ya urembo vizuri.Nawashukuru pia wananchi wote wa Tanzania kwa kunikubali Nawapenda wote na ninaahidi kushirikiana na mrembo atakayevaa taji hili usiku huu katika yale yote mazuri niliyokuwa nimeyafanya kwani kulivua taji hili si mwisho wa kuendeleza yale yote niliyokwisha yafanya wakati niko na taji.
Mwisho kama binadamu kuna wakati naweza kuwa nimemkosea huyu na yule kwa namna moja au nyingine. Napenda kuchukua nafasi hii kwa dhati kabisa kuwaomba msamaha wale wote niliowakosea.Tusameheane na kuanzia usiku huu tuanze maisha mapya.Ahsanteni sana.” Alimaliza kutoa machache mrembo huyu akarudi katika kiti chake cha heshima huku akishangiliwa na watu.’
“naam mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mrembo anayemaliza muda wake. Na sasa ule wakati tuliokuwa tukiusubiri kwa hamu kubwa ndio umewadia.Ni hivi punde tutaenda kumfahamu mrembo wetu mpya. Naomba sasa nimwite Mr Jackob Evarist ili aweze kututajia washindi wetu.”Mr jacob akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana kama alivyotangulia kusema Mrs Coletha brown kuwa mchuano wa leo ulikuwa mgumu sana. Tunamshukuru Mungu kuwa tumeweza kumpata mrembo wa taifa licha ya kuwa na wakati mgumu hasa kutokana na kila mrembo alivyokuwa amejiandaa. Mabibi na mabwana nitaanza kuitangaza nafasi ya tatu hadi moja.” Alitulia kidogo kisha akaendelea.
“Nafasi ya tatu imekwenda kwa mrembo nambari 16 winifrida mwasajuki” alitulia kwanza na kumpisha mrembo huyu apite mbele huku akishangiliwa.
“nafasi ya pili imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 20 Neema Jaspa” Kelele za shangwe zikasikika. Miss Arusha Neema Jaspa binti mwenye ngozi nyeusi yenye kung’aa akapita jukwaani akiwa ndani ya tabasamu kubwa. “
Na sasa mabibi na mabwana ni nafasi ya kwanza.Nafasi ya kwanza imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 6 Happy .”
Tangu ukumbi wa Diamond jubilee ujengwe hakujawahi tokea shangwe kubwa kama hii ya usiku huu ya kuushangilia ushindi wa Happy .Mrembo huyu alifanikiwa kuzikonga nyoyo za watu vilivyo. Patrick alishindwa kujizuia akainuka na kushangilia kwa nguvu sana.
Jukwaani Happy machozi yalikuwa yakimtoka. Hakuamini kama ni yeye ndiye aliyetangazwa mshindi wa shindano hili hasa kutokana na upinzani mkubwa uliokuwepo miongoni mwa washiriki. Watu waliKumbatiana na kupeana mikono ya hongera kuashiria kukubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji ya kumchagua Happy kuwa mrembo wa Taifa. Kila mmoja aliamini kuwa Happy alistahili kulitwaa taji lile.
Baada ya kama dakika kumi hivi za hoi hoi na nderemo muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana nafikiri hoi hoi na nderemo hizi zote ni kuonyesha jinsi gani wote kwa pamoja tunavyokubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji.Happy kibaho ndiye miss Tanzania wetu mpya. Kinachofuata sasa ni mrembo anayemaliza muda wake kulivua taji na kumvisha mrembo mpya.”
Zoezi hili likafanyika huku likishangiliwa kwa nguvu sana.na baada ya zoezi hili kukamilika muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“Mabibi na mabwana tukio linalofuata sasa ni la kumkabidhi Miss Tanzania funguo za gari lake. Tunamuomba mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu apande jukwaani na kumkabidhi Miss Tanzania funguo hizo.”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainment akapanda jukwaani na bila kupoteza muda akamkabidhi Happy funguo za gari ambalo ni zawadi ya kwanza kwa miss Tanzania. Akiwa katika tabasamu pana sana alipita jukwaani huku akizipunga funguo hewani .Kelele za kushangilia zilisikika.
Baada ya zoezi hilo zikafuata burudani mbili kisha mashindano yakafungwa rasmi na taratibu umati wa watu ukaanza kuondoka maeneo hayo ya Diamond jubilee kila mmoja akiwa amesuuzika vilivyo na ushindi wa Happy kibaho .
Happy sasa alikuwa akipiga picha na watu mbali mbali huku akisongwa na waandishi wa habari wakitaka kufahamu mawili matatu ingawa mkurugenzi wa Miss Tanzania alijitahidi kuwazuia kwani Happy angefanya mkutano na waandishi wa habari hapo kesho lakini haikusaidia kitu.
Patrick ambaye alionekana kuchanganyikiwa kadiri muda unavyosonga alitoa simu yake na kuanza kubonyeza namba kisha akajitenga na akina Andrew ambao kwa sasa walikuwa wamesimama wakijiandaa kuondoka.
Patrick aliitumia njia ile ya kujifanya anapiga simu ili aweze kuondoka mahala pale bila kutiliwa mashaka kwani lengo lake kuu lilikuwa kujaribu kupata nafasi ya kuonana na Happy .
Andrew alielewa mara moja nini kilichokuwa kikiendelea akawaomba Vero na Vick waondoke mahala pale waelekee katika magari. Lengo lilikuwa kuwatoa wasiwasi akina Vero.
Patrick alikuwa akipigana vikumbo na waandishi wa habari waliokuwa wakichukua picha na kumuuliza Happy maswali mawili matatu. Alijitahidi sana kupenya na hatimaye akajikuta yuko mahala ambako anaweza kumuona Happy kwa ukaribu.
Jasho lilikuwa likimtiririka na moyoni alikuwa na wasi wasi mwingi lakini hii haikukumkatisha tamaa ya kuonana na Happy . Alijisogeza taratibu na hakuna mtu yeyote aliyeweza kuwa na shaka naye kuwa si mwandishi wa habari tena toka katika chombo cha habari kikubwa hapa nchi au nje ya nchi kutokana na muonekano wake.
“Hongera sana Happy madame Tanzanie” Akasema Patrick wakati huo akiwa uso kwa uso na Happy . Happy kwa wakati huo hakujua aliyekuwa akiongea naye .Alijua wote ni waandishi wa habari. Lakini neno lile “Madame Tanzanie” likamstua na kumfanya ainue uso wake na kumtazama vizuri mtu yule aliye mpa salamu ile.
Kwanza alihisi sauti ile ni kama si ngeni masikioni mwake .mbele yake alikuwa amesimama kijana nadhifu akiwa ndani ya tabasamu lenye kuonyesha aina Fulani ya wasi wasi. macho yake yakakutana na macho ya Patrick na kwa kasi ya umeme kumbukumbu ya ghafla ikamjia kichwani “Noooooo!!!!!!!!!!! Pa...t…….” Akaanguka na kupoteza fahamu.
Kizaa zaa cha ghafla kikatanda hapo ukumbini. Kwa sekunde kadhaa ikatokea taharuki kubwa. Kila mtu akapatwa mstuko kwa kitendo cha Miss Tanzania kupoteza fahamu ghafla.
Haraka haraka walinda usalama wakamwinua na kumkimbiza katika gari la wagonjwa ambalo lilikuwa nje tayari kabisa kwa dharura kama hii.Kwa kasi ya ajabu gari lile likaondoka kuelekea Hospitali. Watu waliokuwa bado wako ukumbini hawakuamini kilichotokea ghafla vile.
Waandishi wa habari wakalichukua tukio lile kama lilivyotokea.
Patrick nusura akili imruke kwa kitendo cha Happy kupoteza fahamu.Taratibu alihisi kuishiwa nguvu lakini tayari Andrew alikuwa ameshafika ,akamshika mkono na kumtoa nje ya ukumbi .
* * * *
Saa kumi na moja asubuhi miss Tanzania Happy alizinduka. akaangaza huku na huku akatambua kuwa alikuwa hospitali. Taratibu akaanza kukumbuka kilichotokea na kumfanya awepo pale hospitali mida ile.Akalikumbuka tukio zima lililotokea usiku.
“That’s him..I saw him ”Happy akajikuta akiongea kwa sauti na kuwastua watu waliokuwemo mle chumbani. Miongoni mwa watu waliokuwa wakifuatilia kwa karibu hali ya Happy ni mdogo wake Margreth .Alikuwepo pia mkurugenzi wa Miss Tanzania pamoja na watu wengine kadhaa.
Mara tu waliposikia kuwa ameamka mkurugenzi wa Miss Tanzania akamwita daktari ambaye alikuja na kumpima. Baada ya vipimo vyote kuonyesha hakuna tatizo zaidi ya mstuko wa kawaida daktari alimuomba Happy aendelee kupumzika na asibughudhiwe.
Daktari akawaomba wote waliokuwa pale Hospitali kwa ajili ya Happy waende kupumzika na kumwacha mgonjwa apumzike kwani bado alihitaji mapumziko ya kutosha.
Ni margreth pekee ndiye aliyebaki ili kumsaidia dada yake.
Baada ya watu wote kutawanyika Happy akageuza kichwa na kumwita margreth.
“ Pole sana Happy.Unaisikiaje sasa ”akasema Margreth
“I’m ok magie." akajibu happy. Margreth akamuangalia kwa makini kisha akamuuliza.
"Happy kitu gani kilitokea mpaka ukapoteza fahamu?..Happy akamuanglai mdogo wake usoni halafu akasema.
"Maggie I saw Patrick yesterday”
“Whaaaaat!!!!!”akauliza margreth kwa mstuko. ' Patrick !!....Patrick yupi ? akauliza Margreth.
" Patrick mpenzi wangu wa zamani" akasema Happy
"Happy Patrick is dead....hakuan namna ambayo ataweza kurudi.Inawezekana ulimafananisha na mtu" akasema Margreth.
"Hapana margreth..I saw him with my own eyes. It was him.." akasisitiza Happy
“Sister are u ok?Magie akauliza tena.
“Sina tatizo magie ni kweli nilimuona Patrick jana wakati nikiongea na waandishi wa habari Alikuja mbele yangu na kunisalimu .Alitamka maneno Fulani ambayo yalinifanya nistuke na nilipomtazama vizuri alikuwa ni yeye.
Nina hakika ni yeye kwani ni mtu ambaye yuko moyoni mwangu kwa miaka mingi na kila siku ninaangalia picha yake hivyo siwezi kuwa nilimfananisha. Ninaamini nilimuona Patrick na ndio maana nikastuka hadi kupoteza fahamu. I’m confused Maggie .Totaly confused.” Kimya kikatanda mle chumbani .
“Margreth tafadhali usimwambia mtu yeyote juu ya habari hii.”
“Usijali sister siwezi mweleza mtu" akasema Margreth.
“Sasa maggie naomba unisaidie kitu kimoja.”Akasema Happy .
“Nikusaidie nini Happy?” akauliza Margreth. ‘
"Nataka kuonana na Patrick” Akasema Happy huku macho yake yamefunikwa na machozi.
“Pumzika kwanza sister ukitoka Hospitali tutaongea kwa undani juu ya suala hili. Kwa sasa bado unahitaji mapumziko ya kutosha na huhitaji kuwaza sana juu ya suala hili.”akasema Margreth.
“Thanks Maggie I understand “akasema Happy.
Mara mlango wa chumba alimolazwa Happy ukafunguliwa wakaingia wazazi wa Happy ambao walikuwa safarini lakini kutokana na matatizo aliyoyapata mtoto wao ikawabidi waahirishe safari yao na kurudi Tanzania haraka.Mama yake akamkumbatia huku machozi yakiwatoka wote . Baada ya kusalimiana Happy akawahakikishia wazazi wake kuwa kwa sasa alijisikia mzima kabisa na pengine mchana wa siku hiyo angeruhusiwa kurudi nyumbani.
Wakiwa katika maongezi akaingia muuguzi akiwa na sinia la dawa. akawaomba radhi wote waliokuwa mle ndani kuwa alihitaji kumuhudumia mgonjwa hivyo akawaomba watoke nje kwa dakika kadhaa. Alipohakikisha wote wametoka akamkaribia Happy .
“Samahani dada Happy nina ujumbe wako ambao nimeambiwa ni wa muhimu na nyeti sana .Aliyenipa ujumbe huu amenionya kwamba nisikupe mahala penye watu .”
“Nani aliyekupa ujumbe huu?
“simfahamu ila ni kijana mmoja alikuwa amevaa suti nyeusi na hakujitambulisha jina lake .yeye alisema ukishausoma tu utakuwa umefahamu.” Yule muuguzi akatoa bahasha toka katika mfuko wake wa koti na kumpatia. Baada ya kumpatia dawa muuguzi yule alitoka na kumwacha Happy jasho likimtiririka. Hakujua ni nani aliyeleta ujumbe ule.
Aliishika bahasha ile na kuifungua taratibu. Ilikuwa ni kadi nzuri iliyomtakia uponaji wa haraka. Ndani ya kadi ile kikaanguka kikadi kidogo . Akakiokota na kukisoma.Nusura apatwe na wazimu baada ya kuisoma kadi ile. Margreth akaingia mara akastukia dada yake amesimama ghafla na kumkumbatia.
“Dada kuna nini? akauliza margreth kwa mshangao.
“Its Patrick”
“Patrick!!!!”
“Yes .Look at this” akasema Happy akimuonyesha Margreth ile bussines card
“Mhhh”margreth akaguna.
Wakati margreth akiisoma ile kadi mlango ukagongwa na likaingia kundi la warembo. Wote wakafurahi baada ya kumkuta Happy ni mwenye furaha namna ile.
* * * *
MISS TANZANIA AZIMIA JUKWAANI , HAPPY KIBAHO MISS TANZANIA MPYA , ZENGWE LATAWALA UKUMBINI MISS TANZANIA AZIRAI.
Hivyo vilikuwa ni baadhi ya vichwa vya habari vilivyotanda katika magazeti mengi kwa siku hiyo. Karibu magazeti yote yalijaribu kuandika kwa kina juu ya tukio la kuzimia kwa miss Tanzania ukumbini, lakini hakuna hata gazeti moja lililoweza kuandika au kuufahamu ukweli juu ya tukio lile.
Akiwa katika kibanda cha kuuzia magazeti asubuhi hiyo Andrew alinunua karibu kila gazeti lililotoka siku hiyo na kupitia habari ya kuanguka kwa Happy. Lengo lake kubwa ni kutaka kufahamu kama kuna mtu yeyote aliyeweza kumtilia shaka Patrick kuwa ndiye aliyekuwa chanzo cha tukio lile la kuanguka Happy ukumbini. katika magazeti yote hakukuta habari yoyote iliyomuhusisha Patrick na tukio lile.
Akatoa simu yake na kumpigia Patrick.Simu ikapokelewa na Vero
“Hallo shemeji”akasema Vero.
“Shemeji mambo vipi? habari za toka jana ? Andrew akauliza
“nzuri tu shemeji”
“Vipi jamaa bado kalala?
“Ameingia maliwatoni kidogo anakuja sasa hivi” Muda huo huo Patrick akatokea Vero akampa simu na kumwambia Andrew anahitaji kuongea naye.
Hallow Andrew vipi ? Akasema Patrick
“Poa Patrick vipi maendeleo yako ?
“Nashukuru Mungu Andrew naendelea vizuri. Hebu nipe habari’
“Habari ni ndefu kidogo lakini kwa ufupi tu ni kwamba leo sijalala kabisa. Baada ya kuachana pale ukumbini nikamrudisha Vick kwake halafu nikaanza kufuatilia Happy alipelekwa hospitali gani. Kwa msaada wa rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari nilifanikiwa kujua mahala Happy Alikopelekwa.
Unajua walificha juu ya mahala alikopelekwa Happy kwa kuwakwepa waandishi wa habari. Alipelekwa katika hospitali moja ya kanisa maeneo ya msasani. Mpaka saa kumi na mbili nilikuwa pale hospitali na ndipo nilipopata taarifa kuwa tayari Happy alikuwa amezinduka.
Kuna muuguzi mmoja anafahamiana na Vick pale na ndiye huyo aliyenipa msaada mkubwa sana. Nilimpa kiasi Fulani cha pesa yule muuguzi na kumuomba aipeleke business card yako kwa Happy na kumwambia apige namba zile zilizoandikwa katika business card hasa muda wa mchana.
Yule muuguzi akajitahidi na kuifikisha kadi ile .Baada ya kuhakikisha tayari Hapy ameipata mimi nikaondoka. Kabla sijafika nyumbani nikaona nipite kwanza katika kibanda cha magazeti ili nione magazeti yanasema nini lakini hakuna chochote kibaya.
Kwa hiyo Patrick nina imani muda wowote Happy anaweza akakupigia simu. Mimi kwa sasa nakwenda nyumbani kupumzika tutaonana baadae ila be carefull brother’ akasema Andrew.
Patrick akavuta pumzi ndefu kisha akasema
“Sijui nikushukuruje Andrew kwa msaada huu mkubwa . thanks a lot. Dont worry I’ll be careful. see you later” Patrick akakata simu kisha akaelekea jikoni ambako Vero alikuwa akiandaa stafstahi akamsaidia kuandaa mlo wa asubuhi kitendo ambacho Vero alikifurahia sana.
* * * *
Saa sita kamili mchana Happy akaruhusiwa kutoka hospitali.Akiwa na furaha isiyokifani huku ameongozana na mama yake pamoja na mdogo wake kipenzi Margreth bila kumsahau mwenyekiti wa kamati ya Miss Tanzania pamoja na wajumbe kadhaa wa kamati hiyo na ujumbe wa watu toka Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano hayo walilakiwa na kundi kubwa la warembo waliokuwa wakisubiri atoke kwani walikwisha taarifiwa kuwa angeruhusiwa mchana.
Walitumia kama robo saa kusalimiana na kupongezana vile vile kupeana pole kwa yaliyotokea. Kisha akapanda gari na kuelekea nyumbani kwao.Happy alikuwa ni mwenye furaha sana mchana huo.
Ni margreth pekee ndiye aliyefahamu siri ya furaha ile aliyokuwa nayo dada yake.Akiwa garini Happy akafumba macho kana kwamba amelala lakini alikuwa amezama katika mawazo na mara akajikuta akitamka kwa sauti.
"Thanks God I found him" Mama yake aliyekaa kiti cha mbele aligeuka na kumuangalia mwanae bila kusema kitu. Margreth yeye alikuwa katika lindi la mawazo na hasa akijaribu kuvuta taswira ya kinachoenda kutokea huko mbeleni.
Anafahamu wazi kuwa katika dunia hii Patrick ndiye mwanaume pekee ambaye Happy anampenda . Licha ya kupotezana kwa muda mrefu lakini bado taswira ya Patrick haikufutika moyoni mwake.
Kwa sasa Happy tayari ana pete ya uchumba ambayo amevishwa na mchumba wake aitwaye Mike cambell raia wa Marekani. Mike ni kijana anayependwa sana na kila mtu katika familia ya akina Happy . Pamoja na kuwa na pete ya uchumba kidoleni bado Happy ameshindwa kuifuta kabisa kumbukumbu ya Patrick moyoni mwake.
Kuonekana kwa Patrick ni wazi kunaweza kusababisha mvurugano mkubwa ambao ni vigumu kujua hatma yake itakuwa nini. Ni wazi Mike alimpenda Happy kupita maelezo. Hiki ni kitu kilichomuumiza kichwa Margreth.
Baada ya mzunguko mrefu hatimaye wakawasili nyumbani ambako walilakiwa na kundi jingine la warembo,ndugu jamaa marafiki na waandishi wa habari wote walifika kumpongeza na kumpa pole Happy . Kisha salimiana na kupongezana Happy akaomba aachwe kidogo apumzike.
Happy akaoga na kupata chakula kisha akaingia chumbani kwake kupumzika.Kitu cha kwanza kabisa ambacho alikifanya ni kuitazama tena ile business card kwa makini .akaichukua simu yake na kuandika namba zile zilizoandikwa pale juu kisha akapiga.
Mapigo ya moyo wake yalikuwa yakienda kwa kasi ya aina yake alipoiweka simu sikioni akaisikia ikiita. Mikono ilianza kuloa jasho kwa wasi wasi.Hakujua angeongea nini baada ya kuisikia sauti ya Patrick. Hakujua Patrick angekuwa katika hali gani mara atakapoisikia sauti yake.
Wakati akisuburi kujibiwa na sauti ambayo aliamini moja kwa moja ingekuwa ni ya Patrick akasikia kitu ambacho hakukitarajia. Ilikuwa ni sauti ya mwanamke ndiye aliyepokea simu ile ya Parick.
“hallow” Ikasema sauti ya upande wa pili.
Happy mikono ilimtetemeka,akapatwa na kigugumizi cha ghafla kilichomfanya ashindwe kuongea.
“hallow naongea na nani?” ikauliza tena ile sauti ya mwanamke.
Happy akashindwa ajibu nini akabaki ameiweka simu sikioni.
“Haloo nani mwenzangu?Ikauliza tena.. Tayari Happy chozi lilikuwa likimtoka. Mara akasikia simu ikikatwa. Kitendo kile kikamuuma akajitupa kitandani machozi yakimtoka.
“Oooh Lord why me?? Why me God? I love Patrick .Yes ni yeye tu ndiye mwanaume ninayempenda kwa dhati ya moyo wangu .Nimetengana naye muda mrefu sana na sielewi maisha yake kwa sasa nadhani tayari ana mke .Sielewi kama ninaweza vumilia nikisikia Patrick ana mke.’ akawaza Happy
“Patrick I’ll fight for you and I must win you back. You are mine Patrick . I lost you once and now I’ve found you I’ll never loose you again” Happy alikuwa akiongea peke yake maneno haya huku machozi yakimchuruzika.
* * * *
Patrick leo huamki? akasema Vero huku akimtingisha Patrick ambaye alikuwa amelala tangu alipokula chakula cha mchana. Patrick akajigeuza na kuangalia saa kubwa ya ukutani. Ilionyesha ni saa kumi na moja za jioni.
“Oh nimelala sana” akasema Patrick kwa uchovu
“Ni vizuri hata hivyo ukipata mapumziko ya kutosha” akasema Happy. Happy akaelekea jikoni akaleta juice na kummiminia Patrick katika glasi.
“Halafu nimekumbuka kuna mtu alikupigia simu nikaipokea lakini cha ajabu hakutaka kuongea kitu chochote . Nimemuuliza zaidi ya mara mbili yeye ni nani lakini hakunijibu.” akasema Happy na kumfanya Patrick astuke.
Mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi.. Kijasho kikaanza kumtoka .akaichukua simu na kuziangalia namba zile zilikuwa ni ngeni kabisa kwake. Hakufahamu zilikuwa ni namba za nani lakini akahisi huenda Happy ndiye aliyepiga.
Kwa mujibu wa maelezo ya Andrew ni kwamba alimuelekeza Happy apige mida ya mchana. Vero akainuka akatoka mle chumbani,Patrcik akaitumia nafasi hiyo kupia zile namba. Simu ikaita bila kupokelewa,ikakatika. Akapiga tena mambo yakawa ni yale yale. Akapiga kwa mara ya tatu simu ikapokelewa.
“Hallow” Ilikuwa ni sauti tamu sana ya mtoto wa kike. Sauti hii Patrick hajaisahau mpaka hvi sasa. Ni sauti ya Happy. Kabla Patrick hajaongea lolote simu ikakatika. Patrick akaipiga tena na safari hii akaambiwa kuwa simu anayopiga haipatikani tena. Akajaribu kupiga tena na tena lakini simu haikuwa ikipatikana.
Patrick akaitupa simu kitandani kwa hasira .Hakuelewa sababu ya Happy kumkatia simu. Sauti aliyoisikia ilikuwa ni ya Happy. Patrick akasimama na kuzunguka zunguka humo chumbani Vero akarejea na kumshangaa kwa namna alivyobadilika ghafla.. Vero akamtazama akapatwa na wasiwasi.
“Patrick dear kuna kitu gani kibaya mbona umebadilika ghafla hivyo? Patrick akastuka na kumtazama Vero..
“Usiogope Vero.Mimi niko sawa kabisa." akasema Patrick lakini ndani ya moyo wake Vero alifahamu kabisa kwamba kuna ambo linamsumbua Patrick.
“Relax my dear jitahidi usiumize kichwa chako kwa mawazo .Kaa chini tuendelee kupanga mipango ya harusi yetu.” Patrick akastuka kwa ndani baada ya kuisikia habari ile ya harusi. Toka amemuona Happy alisahau kabisa kama anatakiwa kuendelea na mipango ya harusi yake na Vero. Kijasho kikamtoka.
" Vero naomba niendelee kupumzika nitakapoamka tutaendelea na majadiliano." akasema Patrick na kupanda kitandani. Akafumba macho na kurejesha kumbu kumbu za nyuma. Akakumbuka toka siku ya kwanza aliyokutana na Happy.