Simulizi: Miss Tanzania

Madame S

JF-Expert Member
Mar 4, 2015
17,172
34,282
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 1
MTUNZI : PATRICK.CK
“Patrick amka darling inakaribia saa nne sasa”Alisema Veronika kwa sauti laini ya kubembeleza.
“‘Mmmmhhh”Akaguna Patrick ,akajigeuza upande wa pili na kulivuta zaidi shuka.
“Amka ukaoge”Alizidi kubembeleza Veronika.Kwa uvivu Patrick akaamka na kuelekea bafuni kuoga.Dakika chache baadae alitoka akiwa amechangamka.
"Kweli maji ni dawa nzuri ya uchovu.Sasa najisikia safi kabisa.Nadhani kwa sasa itabidi nipunguze muda wa kufanya kazi .Nimekuwa nikifanya kazi kwa masaa mengi sana kwa siku kiasi kwamba nakosa hata muda wa kupumzika.Naogopa tukija kuoana nisije kushindwa kutimiza majukumu yangu kama mume kwa sababu ya uchovu” akasema Patrick na kumfanya Vero atabasamu halafu akatoa kicheko cha chini chini na kusema
“Kweli mpenzi jitahidi kwa sasa kupata muda wa kutosha wa kupumzika.”
“Nitajitahidi baby”
Baada ya kuhakikisha sasa yuko safi Vero akamshika mkono Patrick na kumpeleka sebuleni kupata stafstahi.
“Patrick dear nataka unisindikize Supermarket nikafanye manunuzi ya vitu vya ndani .Si unajua kesho Andrew na vicktoria wameahidi kututembelea”Akasema Veronika wakati wakiendelea kupata chai.
“Mhh ! Vero nenda mwenyewe mimi niache nipumzike ”Patrick akajibu
“jamani dear usifanye hivyo naomba unisindikize ,mimi naona uvivu kwenda peke yangu”
‘haya mama ,tumalize chai twende ili tuwahi kurudi”
“Nashukuru dear”
Katika vitu ambavyo Veronika alibarikiwa kuwa navyo ni uwezo wake mkubwa wa kushawishi.

* * * *

Veronika Rugi alikuwa ni msichana mrembo mwenye mvuto wa aina yake.Binti huyu licha ya kujaliwa kichwa kizuri chenye nywele laini ,nyingi na ndefu ,alikuwa na uso mpana wa mviringo ulionakshiwa na macho mapana yenye kurembua muda wote.Midomo mizuri ,laini ambayo akikupiga busu hutatamani abanduke mdomoni .Mtoto huyu alijaliwa shingo murua ambayo iliungana na kiwiliwili kilichokuwa na kifua chenye kupendeza kilichobeba chuchu changa zenye kusisimua,zenye kuwatoa udenda wakware.Kimwana huyu mwenye uzuri usiopimika alijaliwa umbo la utatanishi kuanzia kiunoni kushuka chini.Ni wasichana wachache sana waliopewa upendeleo wa namna hii na manani..
Pamoja na sifa hizo zote za nje lakini bado alikuwa na sifa lukuki za ndani.Kikubwa zaidi kinachomfanya apendwe na kila mtu ni uwezo wake mkubwa wa kuelewa mambo.Ni binti mwenye roho nzuri ya huruma na upendo asiyependa kujivuna wala kujikweza licha ya uwezo mkubwa familia yake ilionao.Ni binti mwenye heshima kwa watu wa rika zote ,mcheshi,asiyependa ubinafsi na zaidi ya yote ni mtu anayejua kupenda.
Veronika ambaye bado anaishi na mama yake mzazi baada ya baba yake kufariki miaka kadhaa iliyopita ,alikuwa ni mtoto wa tatu na wa mwisho katika familia ambayo haikubahatika kuwa na mtoto wa kiume.Dada mkubwa wa Veronika aliyeitwa Loniki hivi sasa anafanya kazi katika shirika la ndege la British airways ,ameolewa na anaishi nchini Uingereza.Mtoto wa pili kuzaliwa katika familia hii ni binti mrembo sana Sarah ambaye aliwahi kushika nafasi ya tatu katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa.naye amekwishaolewa na ni afisa mahusiano wa benki moja mpya kabisa nchini iitwayo African meckat bank.Mtoto wa tatu na wa mwisho ni Veronika ambaye bado hajaolewa ,ila alikuwa katika hatua za mwisho za kukamilisha maandalizi ya ndoa yake na mchumba wake Patrick.Ni hivi karibuni tu amehitimu shahada yake ya kwanza ya biashara katika chuo kikuu cha dar es salaam.Yeye ndiye msimamizi mkuu wa miradi yote ya familia kwa sasa.

* * *

“Patrick mpenzi nilisahau kukwambia toka mapema kuwa dada Loniki alifurahi sana kusikia tunataka tukafanye shopping ya harusi yetu nchini Uingrereza.Ameahidi kuwa yeye na mumewe watagharamia safari nzima ya kwenda na kurudi na gharama zote za manunuzi.Amesisitiza kuwa tusitumie hata shilingi yetu.Kwa maana hiyo wiki hii nataka niende tena kufuatilia yale maombi yetu ya viza pale ubalozini.Nadhani kama Mungu akijaalia basi ndani ya wiki mbili zijazo tutakuwa tumeshakamilisha taratibu zote zinazotakiwa.” Alisema Vero huku akijiegemeza karibu zaidi na kifua cha Patrick.Muda huo ilipata saa mbili za usiku , bado walikuwa wakipunga hewa safi baada ya mlo wa jioni.
“Wow! Hongera sana Vero kwa kuwa na ndugu wakarimu na wenye upendo wa hali ya juu sana kama ulivyo wewe.Tena umeongea kuhusu Loniki nimekumbuka zile CD alizonitumia wiki iliyopita.Unajua sijatazama hata moja.Hebu twende ndani nikaitazame ile filamu mpya ya Jack bauer.”
Akasema Patrick huku akijiinua toka pale walipokuwa wameketi na kuelekea sebuleni .Vero naye akakusanya vitu vyote vilivyokuwapo chini naye akaingia ndani.
“Vero mbona ile CD ya Jack bauer siioni hapa au Andrew aliichukua?Akauliza Patrick baada ya kuitafuta CD ile bila kuiona.
“Yawezekana Andrew aliichukua kwa sababu siku ile aliing’ang'ania sana.Nakumbuka kuna CD alizichukua hapo nadhani na hiyo nayo ilikuwapo.”Akasema Vero
Patrick akalifunga kabati ,akaelekea katika friji akafungua na kujimimia Juice katika glasi .Vero alikuwa ameketi sofani akitazama Luninga.
“ Patrick ,Miss Tanzania mwaka huu itakuwa na ushindani mkubwa sana kwa sababu mabinti ni warembo kupita maelezo.Mhh………..”
Akasema Vero huku amekodoa macho yake katika Luninga kubwa iliyokuwamo humo sebuleni.
“kwani fainali za miss Tanzania ni lini?”Patrick akauliza
“Ni jumamosi ijayo na itafanyikia pale Diamond Jubilee.Kutapambwa na onyesho kali la Malaika band,vile vile wana Fm academia na wasanii wengine kibao watakuwepo.Nataka kesho nikakate tiketi zetu za V.I P ili tusikose nafasi siku hiyo”Alisema Vero
Akiwa na juice yake mkononi Patrick akajisogeza taratibu kuelekea mahali alipokaa Veronika .Kabla hajafika sofani alisimama akapiga funda la juice kisha akaelekeza macho yake katika luninga
“Naitwa Neema ni mrembo toka kanda ya kaskazini.Ni miss Arusha.Napendelea sana muziki wa dini,kusoma na michezo mbali mbali.Nategemea kuwa mwanamitindo wa kimataifa.Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitajikita zaidi katika kuwasaidia watoto yatima kwani naelewa mateso na machungu wanayoyapata kwa kutokuwa na wazazi wao.Naombeni kura zenu namba yangu ya ushiriki ni ishirini.”Alikuwa ni mrembo wa Arusha akijinadi katika kipindi maalum cha kuwatambulisha washiriki wa kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Tanzania kilichorushwa moja kwa moja na televisheni ya Taifa.
“Du! Si mchezo”Aliguna Patrick huku akiisogelea zaidi Luninga
“nimekwambia Patrick warembo wa mwaka huu si mchezo .Hebu kaa uangalie jinsi watoto walivyo wazuri ”Akasema Vero
“Naitwa Happy kibaho.Ni mrembo wa wilaya ya Ilala .Napendelea sana muziki laini,kusoma hadithi ,magazeti,kutazama luninga,na wanyama.Nategemea kuwa mwanasheria.Iwapo nitachaguliwa kuwa miss Tanzania nitaelekeza nguvu zangu zote katika kuwasadia vijana wajasiria mali ikiwa ni pamoja na kuwatafutia wafadhili,nitaitumia kofia yangu kuiomba serikali ielekeze nguvu zake zaidi katika kuwasaidia vijana hawa katika kuwapatia mitaji na kuwatafutia masoko ya bidhaa zao wanazozizalisha ili kupambana na ongezeko la vijana wasiokuwa na ajira.Ninaomba kura zenu ili niweze kulitwaa taji hili la miss Tanzania kwani nina vigezo vyote vya kulitwaa taji hili .Namba yangu ya ushiriki ni 6.”
“Whaaaat!!!!!!!!!!!!!!........................”Patrick Akapiga ukelele mkubwa
“Nooooooooooo!!!!!!!!..I cant bel……………………”ghafla glasi aliyoishika ikamponyoka ikaanguka na kuvunjika .Taratibu nguvu zikaanza kumwishia akadondokea sofani kisha akapoteza fahamu.
“Patrick ,Patrick what’s wrong....!!!!!!!!!!!...”
Alihamaki Veronika huku akimsogelea Patrick pale sofani na kumtingisha.
“Patrick darling what’s wrong with you?
Alizidi kuuliza Vero huku akimtingisha.
“Ooh ! Nooo...!!!!...Wake up Patrick”Alipiga ukelele baada ya kugundua kuwa Patrick hakuwa na fahamu.Vero akataharuki asijue afanye nini.Hakukuwa na mtu yoyote wa karibu ambaye angeweza kumsaidia .Alitoka kutaka kwenda kuwaita majirani ,akafika mlangoni na kurudi tena ndani mpaka sofani alipolala Patrick.
“Patrick ! Patrick dear what’s wrong with you.Whats’s wrong Patrick!!!!!!!!!”Vero aliongea peke yake huku machozi yakimtiririka.Pale pale akapata wazo la kumpeleka Patrick hospitali.Kwa nguvu zake zote akamuinua Patrick na kumpakia garini ,akakimbia kufungua geti kisha akaingia garini na kuondoka kwa kasi ya ajabu pasi na kufunga mlango wowote wa nyumba.Kwa kasi ya ajabu Vero aliendesha gari hadi hospitali ya karibu maarufu kama Dr Heneriko hospital.Si mbali sana na makazi ya Patrick.Huku akilia akapaki gari na kuingia ndani ,akawaomba msaada wauguzi .Haraka haraka wauguzi wakamchukua Patrick na kumuwahisha katika chumba maalum kwa ajili ya kumpatia huduma ya haraka.
“Hurry up !.hurry up.! Ooh Patrick what’s wrong with you?”Alilalamika Vero huku akiwaomba manesi waharakishe.Muda wote huo machozi hayakumkauka.
Veronika alizuiliwa asiingie katika chumba cha huduma ya kwanza akaachwa hapo nje na mmoja kati ya manesi akiendelea kumfariji.
“Jipe moyo dada yangu Patrick atapona tu.Mtumaini Mungu.”Nesi yule alimbembeleza Vero kwa upole.
Dakika kama 20 hivi baadae dokta Heneriko alimwita Vero ofisini kwake na kumuomba awe mvumilivu wakati wakiendelea kuishughulikia hali ya Patrick.Dokta alitaka kufahamu nini hasa kilichopelekea Patrick kupoteza fahamu.
“Unajua dokta ,Patrick ni mpenzi wangu na tuko katika maandalizi ya harusi yetu.Mimi siishi naye kwa sasa ila huja kwake kila mwisho wa wiki .Leo hii toka asubuhi alikuwa akilalamika kuwa alihisi uchovu mwingi .Tulitoka kidogo kisha tukarudi na akaendelea kupumzika.Usiku tukiwa sebuleni tukiangalia Tv nikaona mwenzangu akipiga ukelele akaishiwa nguvu na kuangukia sofani akapoteza fahamu.kwa kweli sina hakika mpaka sasa ni kitu gani hasa kilichopelekea hali ile kutokea.Naomba Dokta ufanye kila linalowezekana ili Patrick apone.Niko tayari kutoa kiasi chochote cha pesa ili mradi apone.”
Vero alishindwa kujizuia akaangua kilio.
“Nyamaza Vero,Hali ya Patrick inaendelea vizuri. nina hakika muda si mrefu atazinduka.Kwa hiyo yawezekana kuwa kuna habari yoyote aliyoitazama ambayo ilimpelekea Patrick kupata mstuko ?
“Sidhani dokta kwa sababu wakati tunaangalia Tv hakukuwa na taarifa yoyote ya kutisha au kustusha inayoweza kupelekea mtu kupata mstuko hadi kupoteza fahamu.Tulikuwa tukiangalia washiriki wa miss Tanzania wakijinadi.Ni hilo tu”Vero akajibu
Dokta Heneriko akanyamaza kimya kwa sekunde kadhaa kisha akasema
“Kwa kumbukumbu zako toka umekuwa naye kuna siku yoyote tukio kama hili limewahi kumtokea zaidi ya leo?
“Hapana dokta tangu mimi nimekuwa naye halijawahi tokea tukio kama hili Patrick kupoteza fahamu.”
“Ok Vero hivi sasa waweza kwenda kupumzika na kutuacha sisi tuendelee kumuhudumia mgonjwa wako.Iwapo kutakuwa na mabadiliko yoyote tutakupigia simu kukutaarifu.Na kama itahijika kumuhamisha kumpeleka katika hospitali kubwa zaidi tutakutaarifu pia.Lakini kwa sasa hali yake inaendelea vizuri,mapigo ya moyo wake yako sawa na kila kitu kinaonekana kufanya kazi vizuri.Huu ulikuwa ni mstuko wa kawaida tu ambao unaweza kumtokea mtu yeyote na hasa akiwa na msongo wa mawazo.”Akasema Doctor Henry.
“No Dokta ,siwezi kwenda nyumbani bila kujua hali ya mpenzi wangu iko vipi.Nitalala hapa hapa .Nataka niwe wa kwanza kuniona pindi atakapofumbua macho.Samahani dokta naweza kuitumia simu yako kuongea na mama yangu na kumtaarifu juu ya ugonjwa wa Patrick”
Dokta Heneriko hakuwa na kipingamizi akamruhusu Vero aitumie simu yake.
Vero akampigia simu mama yake na kumtaarifu juu ya tukio lile ,halafu akawapigia simu ndugu zake wote bila kumsahau Andrew rafiki mkubwa wa Patrick pamoja na Alois kaka yake Patrick.Wazazi wa Patrick walikuwa safarini nje ya nchi.

* * * *

Ilimchukua kama nusu saa toka Andrew apate taarifa ya ugonjwa wa patrick,kuwasili pale hospitali.Akiwa na mpenzi wake Vick walishuka garini na kukimbia kuelekea mapokezi.Mara tu baada ya kuingia hapo mapokezi walilakiwa na sura yenye kusawajika ya Vero.Alipowaona Andrew na Vick wakiingia humo hospitali Vero aliangua kilio ambacho kiliwachanganya zaidi Andrew na Vick.
“Where is Patrick??”Andrew akauliza huku akijikaza lakini ni wazi alikuwa akitetemeka
“Calm down Vero tuambie Patrick yuko wapi?”Aliuliza tena Andrew .Vick akamkumbatia Vero huku naye machozi yakimtoka.
Andrew alimfuata muuguzi aliyekuwa mapokezi na kumuuliza juu ya hali ya Patrick.Hakuridhika na jibu alilolipata ,kwa kasi akakimbia hadi katika ofisi ya Dokta Heneriko lakini hakumkuta.Taratibu akatoka humo ofisini jasho likimtiririka na kurudi mapokezi.Tayari Alois kaka yake Patrick alikwisha wasili hapo hospitali akiwa ameongozana na mke wake nao wote waliungana na Vick katika kumbembeleza Vero.
Andrew akawasalimia kisha akamvuta mkono alois wakasogea pembeni kidogo.
“Hebu niambie Andrew kitu gani kinachoendelea hapa na Patrick yuko wapi ?Aliuliza Alois huku naye jasho likimtiririka
“Brother Aloia hata mimi mpaka muda huu sielewe chochote kwani toka nimefika hapa muda mfupi uliopita sijaweza kuongea lolote na Vero.Ila kwa maelezo niliyoyapata toka kwa muuguzi ni kwamba Patrick yuko katika chumba cha huduma ya kwanza akipatiwa matibabu.Nasikia ni mstuko ndio uliopelekea akapoteza fahamu”
Mara dokta Heneriko akatokea.Muuguzi aliyekuwapo mapokezi akamtambulisha kwa akina Andrew.
“Dokta hawa ni ndugu zake Patrick wamefika sasa hivi na walitaka kupata taarifa juu ya maendeleo ya mgonjwa wao’
Dr henry akawasalimu wote halafu akawaomba Alois na Andrew wamfuate ofisini kwake..
“Vijana wangu kwanza poleni sana kwa matatizo ‘
“Ahsante sana dokta tumeshapoa”Wakajibu kwa pamoja
“sasa vijana wangu nimewaiteni hapa ili tuongelee zaidi suala la ndugu yenu..Patrick aliletwa hapa kwangu usiku huu akiwa amepoteza fahamu.Kwa haraka nikisaidiana na madokta wenzangu tumejitahidi kumpatia huduma ya kwanza na mpaka sasa maendeleo yake ni mazuri.Tumejitahidi kuyashusha mapigo ya moyo yaliyokuwa juu sana na kwa sasa yako kawaida.Taratibu anaanza kurejewa na fahamu zake ingawa bado anahitaji kupumzika zaidi kwani bado fahamu hazijarejea vizuri.Maendeleo yake ni mazuri na baada ya muda mfupi ujao basi atarejea na fahamu zake zote.”
Alois akashusha pumzi nzito kwa kusikia taarifa ile ya dokta.Akatoa leso na kujifuta jasho lililokuwa likimtirirka kwa kasi muda huo.
“Thanks God”Alisema Alois huku ameinua mikono juu ishara ya kumshukuru Mungu
“kwa hivi sasa bado ataendelea kuwapo katika uangalizi maalum mpaka hapo hali yake itakapokuwa nzuri kabisa.Tatizo lililompata ni mstuko wa moyo.Ni tatizo la kawaida kutokea.Ila hali yake itakapokuwa nzuri tutamshauri aonane na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo ili aweze kumfanyia uchunguzi zaidi katika moyo wake ”
Baada ya kupata maelezo ya kutosha toka kwa dokta,Alois na andrew waliridhika kabisa na dokta akawashauri waende kupumzika mpaka kesho .Alois alikubaliana na wazo hilo lakini akashauri andrew awarudishe kwanza Vero na Vick nyumbani wakapumzike.Yeye atabaki pale kuangalia hali ya Patrick inavyokwenda.
Wakati wakiendelea kujadili mama yake Vero akatokea.Akawasalimu wote aliowakuta hapo kisha kwa wasiwasi akataka kujua juu ya hali ya Patrick.Alipewa maelezo mafupi ya hali ya mgonjwa halafu akaomba aonane na dokta Heneriko,akaongea naye na kupewa kwa muhtasari juu ya hali ya Patrick na maendeleo yake na akahakikishiwa uangalizi wa hali ya juu.
“Ok . sasa utaratibu gani unaoendelea hapa? Aliuliza Bi stella Rugi mama yake na Vero.
“Tumepanga kuwa Andrew awarudishe nyumbani Vero na vick wakapumzike ,mimi nitaendelea kubaki hapa hapa na kufuatilia hali ya mgonjwa”Akasema alois
“Vizuri ,basi msipate shida ,Vero na Vick nitaondoka nao mimi na kwenda nao nyumbani kwangu , Andrew nenda nyumbani kwa Patrick ukahakikishe kuko salama .Alois utaendelea kubaki hapa kumwangalia mgonjwa .Nitakuwa nakupigia simu mara kwa mara ili kujua maendeleo ya mgonjwa ." akasema mama yake Vero
“sawa mama tumekuelewa .”Andrew na alois waliitika kisha wote wakatawanyika na kumwacha Alois hapo hospitali
Saa saba usiku Patrick akarejewa na fahamu zake kamili.Kitu cha kwanza kuhisi ni harufu kali ya dawa akageuza shingo kutazama pande zote akatambua kuwa pale alikuwa hospitali.Taratibu akavuta kumbukumbu za nyuma na mara akakumbuka kitu kilichopelekea yeye kuwepo pale.
“I saw her. I real saw her. she’s alive” Alijikuta akitamka maneno haya huku jasho likikimtiririka na mapigo yake ya moyo kwenda kasi .
Muuguzi aliyekuwa akimuangalia aliingia ndani na kumkuta tayari Patrick amerejewa na fahamu na amekaa kitandani.Haraka akaenda kumwita daktari.Dk heneriko alikuja kwa kasi na kumpima akagundua kuwa bado mapigo ya moyo wa Patrick yalikuwa juu sana.
“‘Lazima kuna kitu kinamsumbua huyu si bure”Akawaza dokta Heneriko.
“Patrick “Dokta akamwita baada ya kumaliza kumfanyia vipimo.
“naam dokta”Aliitika Patrick kwa sauti yenye kukwaruza.
“Pole sana “
“Ahsante sana dokta”
“Patrick kijana wangu usijali utapona tu hali yako inaendelea vizuri .Unahitaji kupumzika sasa mpaka asubuhi tutakapochukua tena vipimo vingine”
“Sawa dokta.” akajibu Patrick
“Endelea pumzika Patrick na iwapo utahitaji kitu chochote muuguzi yuko hapo nje na atakuwa akija hapa mara kwa mara kukuangalia.Tena nimekumbuka kaka yako yuko nje muda sijui kama ungependa kumwona?”Akasema dokta heneriko.
“Ndiyo dokta naomba uniitie..”
Dokta Heneriko akafungua mlango na kutoka.
Alois alikuwa amesinzia katika sofa lililoko mapokezi Mara akastuliwa na sauti ya Dokta Heneriko.
“Alois ,Patrick amekwisha rejewa na fahamu zake kamili kwa hiyo unaweza kwenda kumwona.Ila tafadhali usijaribu kumuuliza chochote kuhusiana na kilichopelekea yeye kupoteza fahamu.Ongea naye maongezi mengine ya kawaida.sawa?”
“sawa dokta”Alijibu Patrick huku akifikicha macho yaliyojaa usingizi.Muuguzi aliyekuwepo mapokezi akampeleka hadi katika chumba alimolazwa Patrick.
“Vipi Patrick unajisikiaje kwa sasa?Akasema Alois
“Sasa hivi sijambo brother najisikia vizuri.nashukuru kwa kuja kuniona”
“Usijali Patrick kwa sasa endelea kupumzika.bado unahitaji mapumziko ya kutosha.Mimi niko hapo nje.i”
“Vero yuko wapi?” Akauliza Patrick
" Vero amechukuliwa na mama yake.Andrew amekwenda nyumbani kwako kuhakikisha kuko salama" akasema Alois.
" Naomba umpigie simu na umwambie kwamba niko salama,asiwe na mawazo" akasema Patrick
" Sawa Patrick ngoja nimfahamishe" akasema Alois

TUKUTANE SEHEMU IJAYO..........................
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 2
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Alois ,Patrick amekwisha rejewa na fahamu zake kamili kwa hiyo unaweza kwenda kumwona.Ila tafadhali usijaribu kumuuliza chochote kuhusiana na kilichopelekea yeye kupoteza fahamu.Ongea naye maongezi mengine ya kawaida.sawa?”
“sawa dokta”Alijibu Patrick huku akifikicha macho yaliyojaa usingizi.Muuguzi aliyekuwepo mapokezi akampeleka hadi katika chumba alimolazwa Patrick.
“Vipi Patrick unajisikiaje kwa sasa?Akasema Alois
“Sasa hivi sijambo brother najisikia vizuri.nashukuru kwa kuja kuniona”
“Usijali Patrick kwa sasa endelea kupumzika.bado unahitaji mapumziko ya kutosha.Mimi niko hapo nje.i”
“Vero yuko wapi?” Akauliza Patrick
" Vero amechukuliwa na mama yake.Andrew amekwenda nyumbani kwako kuhakikisha kuko salama" akasema Alois.
" Naomba umpigie simu na umwambie kwamba niko salama,asiwe na mawazo" akasema Patrick
" Sawa Patrick ngoja nimfahamishe" akasema Alois

ENDELEA…………………………

Baada ya kulia sana hatimaye kiusingizi kikaanza kumchukua na taratibu akajikuta akianza kulala.Hazikupita hata dakika kumi toka aanze kusinzia simu yak ikaanza kuita na kumstua toka usingizini.Alipoiangalia simu yake ilikuwa imeandika jina Alois.Aliogopa kuipokea simu ile akabaki akiiangalia ikiiendelea kuita.Mikono ilikuwa ikimtetemeka .Alihofia pengine simu ile inaweza kuwa imebeba ujumbe mbaya kuhusu Patrick.Simu iliita ikakatika ,ikaanza kuita tena.Akaamua kuipokea.
“Haloo”Akaita Vero
“Haloo Vero unaendeleaje ? akasema Alois.
“naendelea vizuri shemeji vipi huko kwema ? Akasema vero huku mapigo yake ya moyo yakienda kwa kasi isiyo ya kawaida.
“Huku kwema tu shemeji.Nataka nikufahamishe kuwa Patrick tayari amekwisha rejewa na fahamu zake na nimetoka kuongea naye muda si mrefu.Kwa hivi sasa anaendelea kupumzika.Amenituma nikwambie kwamba usiwe na wasi wasi yeye ni mzima wa afya.”
Vero akashusha pumzi ndefu akakaa kimya kwa sekunde kadhaa kisha akamuaga Alois na kukata simu.Alipokata simu akaanza tena kulia kwa kwikwi..Vick ambaye alikuwa katika usingizi mzito akaamka baada ya kustushwa na kilio cha Vero.
“Vero nini tena?
“Patrick anaendelea vizuri.Alois amenipigia simu sasa hivi na kunifahamisha.”
“sasa kama hajambo unalia nini?
“Huwezi jua Vick ni jinsi gani nisivyopenda kumuona Patrick akiumwa kwa jinsi ninavyompenda..Ninalia kwa mateso ninayoyapata juu yake.”
Vick akambembeleza vero hadi akanyamaza kisha akajilaza kitandani na kuanza kutafakari.juu ya tukio zima..Alikumbuka walikuwa sebuleni wakiangalia luninga ambapo warembo wanaotarajia kuwania taji al miss Tanzania walikuwa wakijinadi .Alivuta picha na kumuona Patrick akiwa katika friji akijimiminia kinywajii katika glasi ambapo muda huo Miss arusha Neema alikuwa akijinadi.Alikumbuka kumuona Patrick alivyovutiwa ghafla na kipindi hicho cha warembo.Toka Neema hakumbuki ni mrembo gani aliyefuatia kujinadi ila anachokumbuka ni kwamba Patrick alipiga ukelele mkubwa wa kushangaa kitu halafu akaanguka na kupoteza fahamu.
“Ni dhahiri ni mstuko ndio uliomfanya Patrick aanguke na kupoteza fahamu .Lakini je ni kitu gani hasa ambacho kilimstua Patrick kiasi cha kupoteza fahamu?Je mstuko huu una uhusiano wowote na kipindi kile tulichokuwa tukitazama ? hapana . Patrick nimekuwa naye muda mrefu sasa na tabia yake ninaifahamu vizuri.Kuhusu wanawake siwezi kumsemea vibaya hana tabia hiyo ya kuwa na wanawake wengine nje ya mahusiano yetu.Nina uhakika na hilo.Sasa ni kitu gani kilichomstua ? any way siwezi kupata jibu kwa sasa mpaka hapo atakaponiambia yeye mwenyewe kwani nina hakika hawezi kunificha kitu chochote.”
Alikuwa akiwaza Vero na taratibu usingizi ukamchukua akalala.

* * * *

Saa kumi na mbili asubuhi iliwakuta Vero ,Vick na mama yake vero tayari wakiwa hospitali.Hali ya Patrick ilikuwa ikiendelea vizuri .Alfajiri hiyo tayari alikwisha hamishwa toka katika chumba cha uangalizi maalum na kuwekwa katika chumba cha mapumziko ya kawaida.
Wakiongozwa na alois ambaye alilala hapo hospitali walielekea moja kwa moja chumbani na kumkuta Patrick tayari amekwishaamka.Bila kupoteza muda Vero akamkumbatia na kumpiga mabusu mfululizo.
“Pole sana my dear.Unajisiaje kwa sasa? akauliza Vero huku akitabasamu
“Najisikia vizuri sana” akajibu Patrick huku akijinyoosha nyoosha pale kitandani.Baada ya kusalimiana kilifuata kipindi cha vicheko na utani wa hapa na pale kisha Vick na mama yake Vero wakaomba waondoke kwa ajili ya kwenda kujiandaa na mishughuliko ya siku.
Vero alimwinua Patrick na kumpeleka bafuni ambako alimwogesha na kumrudisha tena chumbani ,akamwandalia kifungua kinywa .Patrick alijisikia faraja kubwa kwa namna binti huyu alivyokuwa akimjali na kumuhudumia.

* * * *

“Andrew kwa kipindi kirefu sasa umekuwa ni msiri wangu mkubwa.Mambo yangu mengi ambayo sihitaji mtu mwingine kufahamu wewe wayajua.Urafiki wetu ni zaidi ya undugu.Naomba sana kile nitakachokuambia hapa usimwambie mtu yeyote yule.Itabaki kuwa siri yako mpaka pale muda muafaka utakapofika.”
Patrick aliongea taratibu huku akijiweka vizuri sofani.Ni siku ya kwanza tangu ameruhusiwa kutoka hospitali kwa sababu ya mstuko uliopelekea apoteze fahamu.Andrew rafiki mkubwa wa Patrick alikuwa kimya akiwa na shauku kubwa ya kutaka kulisikia lile ambalo rafiki yake alikuwa tayari kumwambia.
“I saw Happy ”akasema Patrick kisha akatulia na kuyaacha maneno yale yamwingie Andrew.
“what !! ” akauliza Andrew kwa mshangao
“I saw Happy ”
Patrick alirudia tena kisha akainamisha kichwa chini na kuzama katika mawazo mazito.Andrew akainuka na kuanza kuzunguka zunguka mle chumbani huku akionekana dhahiri alikuwa ameshtushwa mno na kauli ile ya Patrick.
“Umemuona wapi?”andrew akauliza huku amejishika kichwa.
’‘Nimemuona kwenye luninga .Kulikuwa na kipindi cha kuwanandi warembo wanaoshiriki kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa Taifa .Happy ni miss Ilala.”
“are you sure” Andrew akahoji
“ I'm sure Andrew na hiyo ndiyo sababu iliyonifanya nikapata mstuko na kupoteza fahamu”
Andrew akavuta pumzi ndefu ,akainuka akaanza kuzunguka zunguka humo ndani kisha akakaa.Vijana hawa wote kwa sasa walikuwa katika wakati mgumu sana.Ni Andrew pekee aliyefahamu kilichokuwa kikiendelea kati ya Patrick na Happy na ndio maana alichanganyikiwa asijue afanye nini.Alimuonea huruma sana Patrick kwa wakati huu mgumu alionao.
“Vero aligundua chochote “Andrew akauliza tena
“sina hakika kama aligundua kitu chochote kwa wakati ule”akajibu Patrick
“ kwa hiyo tufanye nini sasa” Andrew akahoji.
Patrick akainuka na kwenda katika friji akjimiminia maji baridi kwenye glasi akapiga funda kubwa kisha akavuta pumzi ndefu na kusema.
“Nataka kuonana na Happy ”
Kimya cha sekunde kadhaa kikapita hapo sebuleni kisha Patrick akaendelea
“Nataka kabla ya kuonana naye kwanza tumfanyie uchunguzi anaishi wapi,na nani ,anafanya kazi gani,ana mchumba au hana,na chochote kile tunachoweza kukifahamu kuhusu yeye.Uchunguzi huu nataka uwe wa siri na yeye Happy asiweze kufahamu kuwa anachunguzwa.Ikiwezekana tunaweza hata kuajiri mtu wa kuifanya kazi hii niko tayari kumlipa kiasi chochote cha pesa anachohitaji.Nakukabidhi kazi hii Andrew nina imani itafanyika ipasavyo.Tuko pamoja? Akasema Patrick.Andrew akavuta pumzi ndefu na kusema
“Nimekuelewa Patrick lakini suala hili haliwezi kuathiri maandalizi ya harusi yako ambayo tayari yanaelekea mwishoni?
“Hahahah ! usihofu kuhusu hilo my friend.I know what I’m doing ,ok?” akasema Patrick huku akicheka
“Una maana gani Patrick unaposema unajua unachokifanya ?Ninafahamu kuwa ndoto zako za siku nyingi ni kuwa na Happy katika maisha yako na kwa sasa umekwisha kuwa na uhakika kuwa yupo na kwa wakati wowote unaweza kumuona . Nina wasiwasi sana na huu ujio wa Happy katikati ya maandalizi ya Harusi yako unaweza kutibua kila kitu." akasema Andrew kwa wasi wasi
“Kwa ajili ya Happy niko tayari kwa lolote linaloweza kutokea.All these years I’ve been hurting myself thinking about her na mpaka sasa nimeshindwa kabisa kuifuta kumbukumbu ya Happy moyoni mwangu.Siwezi kuendelea kuutesa moyo wangu Andrew.I have to face her.” Akasema Patrick
“Patrick nafikiri unahitaji kufikiri zaidi kuhusu suala hili, si suala jepesi kama unavyolifikiri.Ni suala ambalo linagusa hisia za watu wengi .Hi…..”
Andrew hakuendelea zaidi Patrick akadakia.
“Andrew I've made my decision and its final.Nilivyoamua nimeamua.Nitapambana kadiri ninavyoweza ili kuonana tena na Happy .I love her and I know she loves me too.” akasema Patrick.Andrew akamuangalai rafiki yake kwa makini na kusema.
“Patrick miaka mingi imepita tangu mpotezane na Happy na kila mmoja ameendelea na maisha yake.Tayari uko na Vero na kwa sasa bado kama mwezi mmoja na nusu hivi ufunge ndoa na Vero ,ndoa ambayo sehemu kubwa ya maandalizi yake yamekamilika.Huoni kuwa utakuwa unamnyima haki zake Vero kama ukihamishia mawazo yako yote kwa Happy .? Nina imani Vero anakupenda kwa dhati ya moyo wake na nina imani vile vile hata wewe unampenda Vero Kwa nini utake kumtesa Vero kiasi hiki ?
“Andrew nafahamu unachokisema .Ni kitu cha msingi sana lakini kama ungeigia viatu vyangu na kuona nini kilichomo ndani.Nina imani kubwa hata wewe ungefanya kama mimi ninavyotaka kufanya.Happy ni msichana wangu wa kwanza ambaye nilimpenda kupita ninavyojipenda mwenyewe.Ni kweli niko katika mahusiano na hivi karibuni ninatarajia kufunga ndoa na Vero lakini bado sura ya Happy haijaweza kunitoka moyoni mwangu.Please Andrew naomba msaada wako katika hili.Nisaidie nionane na Happy tafadhali.” akasema Patrick
“Nimekuelewa Patrick lakini bado moyo wangu una wasiwasi sana juu ya kinachoweza kutokea.hapo mbeleni.Nafahamu kuwa endapo utaingia matatizoni basi ni sisi sote tutakuwa katika matatizo.Tatizo langu ni lako na lako langu ndio maana tunahitaji sana kushauriana kwa kina kabla ya kufanya jambo.”
“Andrew najua una wasiwasi mwingi kuhusu mimi na Vero.Hilo ni kubwa linalokuumiza kichwa.Hata mimi sijisikii vizuri kumtesa Vero binti aliyeyatoa maisha yake kwangu.Binti anayenipenda kwa dhati ya moyo wake.Ni vero huyu huyu ndiye aliyeirudisha tena furaha ndani ya moyo wangu na kuliondoa wingu zito la ukiwa lililokuwa limenifunika.Nampenda Vero lakini ni lazima nionane na Happy .”akasema Patrick.
Andrew akainuka kitini akachukua chupa ya mvinyo na kujimiminia katika glasi akanywa mafunda kadhaa kisha akamgeukia Patrick.
“Ok Patrick kwa sababu umekwishaamua basi hatuna budi kufanya hivyo.Mimi nitaianza kazi hiyo kesho.Nitamtafuta mtu ambaye ataifanya kazi hiyo kwa ustadi mkubwa.Usijali kuhusu hili ndugu yangu”
Patrick alifurahi akainuka na kumkumbatia rafiki yake.

* * * *
Saa kumi na mbili za jioni Veronika alirejea katika shughuli zake na kumuaga mama yake kuwa alikuwa akaienda kumwangalia Patrick nyumbani kwake.Ni siku ya tatu sasa toka Patrick atoke hospitali.Hali yake haikuwa ikiendelea vizuri sana.Muda mwingi alikuwa akionekana ni mtu mwenye mawazo mengi .Hali hii ilimpa wasiwasi mwingi Vero kiasi cha kumfanya awe karibu naye kila wakati ili kujaribu kumchangamsha na kumrudisha katika hali yake ya kawaida.
Ingawa Patrick alijitahidi kwa kila jinsi ili Vero asione hali hii ya mawazo mengi aliyokuwa nayo lakini mara nyingi alishindwa na kujikuta akitoa machozi.Vero aliigundua hali hii na kwa kiasi kikubwa ikamuongezea udadisi juu ya kinachoendelea .alijua ni lazima liko jambo ambalo linamchanganya Patrick
“Haloo sweetie”Alisema Vero baada ya kuingia ndani kwa Patrick
“Haloo vero ”akasema Patrick
Vero akamfuata Patrick kitandani akamkumbatia na kumpiga busu zito.
‘Unaendeleaje mpenzi”
“Naendelea vizuri Mungu ananisaidia sana.Muda si mrefu nitapona kabisa”
Baada ya kujuliana hali Vero alimwandalia Patrick Juice kisha yeye akaelekea jikoni kufanya maandalizi ya chakula cha jioni.Patrick alipata faraja kubwa baada ya Vero kuwasili Ni wazi Patrick husikia furaha kubwa moyoni awapo na Vero.
Ilimuuma sana baada ya kugundua kuwa alimpenda Vero lakini kwa ghafla Happy ametokea na kuanza taratibu kuzihamisha hisia zake.
Chakula kilipokuwa tayari kikawekwa mezani,wakala kisha wakapumzika na baadae wakaelekea kulala.
“Vero dear tayari umekwisha kata tiketi za kuingia Miss Tanzania Jumamosi? Patrick akauliza
“Tayari mpenzi Nimekwishaziandaa . Utaweza kwenda na hali hii ?Naona kama hali yako inazidi kudhoofu siku hadi siku”
“Usijali mpenzi wangu lazima nihudhurie.Nina imani ndani ya siku mbili tatu zijazo hali yangu itakuwa shwari ”akajibu Patrick
Vero akanyamaza kimya akajaribu kuvuta kumbukumbu nyuma siku ile Patrick alipoanguka na kupoteza fahamu alikuwa akitazama kipindi cha wagombea wa miss Tanzania .Hakutaka kukubaliana kuwa kuna kitu chochote kinachoendelea baina ya Patrick na mashindano yale.Alijitahidi kuilazimisha akili yake ikubaliane na taarifa ya daktari kuwa Patrick alipoteza fahamu kwa sababu ya uchovu mwingi uliokuwa ukimkabili kiasi cha kuufanya ubongo wake ushindwe kufanya vizuri kazi yake.
“Lakini pamoja na taarifa ile ya daktari lakini kuna kitu kiko moyoni mwa Patrick ambacho kinamyima raha na kuisumbua akili yake .Ni kwa sababu hiyo tu ndiyo maana amepoteza furaha yote aliyokuwa nayo kabla.Chakula chenyewe mpaka abembelezwe.Mara kadhaa nimemfuma mwenyewe kwa macho yangu akilia.Ingawa anajitahidi sana kuificha hali hii lakini nimekwishafahamu .Anyway nitajitahidi kumuuliza ili anieleze kama kuna jambo lolote linalomsibu.”
Veronika alizama ghafla katika mawazo.
“Unawaza nini mpenzi wangu”Patrick akauliza
“Nothing.Siwazi chochote zaidi yako.Unajua Patrick hali yako kwa sasa inanipa wasiwasi sana.Tangu umetoka hospitali umebadilika.Ni kitu gani kinakusumbua mpenzi hebu niambie.Hali hii inanifanya hata mimi nihisi kama vile ninaumwa pia.Au kama kuna kitu nimekukosea niambie Patrick ili nijirekebishe.Tangu tumeanza mapenzi yetu sijawahi hata siku moja kukuona katika hali hii”
Vero akashindwa kujizuia akaanza kulia kwa kwikwi.
Patrick akamvutia Vero kwake akambusu na kumwambia
“Usihofu kitu baby hakuna kitu kingine kinachonisumbua .Kama daktari alivyosema kuwa natakiwa kupumzika sana .Uchovu ndio uliopelekea tatizo lile kutokea.”
Akasema Patrick huku akizichezea nywele laini za Vero.
‘Hapana dear najua lazima kuna kitu kinachokusumbua akili na hutaki kuniambia”
“ my dear angel ,wewe ndiye maisha yangu.Wewe ndiye uliyeyashika maisha yangu.Nimekukabidhi funguo za moyo wangu.Wewe ndiye mfariji wangu,wewe ndiye furaha yangu,wewe ndiye kila kitu kwangu sasa kwa nini nikufiche kitu?Hakuna kitu nimewahi kukuficha wewe mpenzi wangu na haitakuja tokea nikawa na tatizo nikashindwa kukwambia.Sasa nisipokwambia wewe nitamwambia nani tena?”
Patrick alijitahidi kumtoa Vero wasiwasi aliokuwa ameanza kuwa nao juu yake na mara moja akaazimia moyoni kubadilika kitabia ili Vero asije akaendelea kumdadisi.Taratibu akaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ya ucheshi na uchangamfu mkubwa kitu ambacho Vero alikifurahia sana.

TUKUTANE SEHEMU IJAYO…………..
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 3
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Usihofu kitu baby hakuna kitu kingine kinachonisumbua .Kama daktari alivyosema kuwa natakiwa kupumzika sana .Uchovu ndio uliopelekea tatizo lile kutokea.”
Akasema Patrick huku akizichezea nywele laini za Vero.
‘Hapana dear najua lazima kuna kitu kinachokusumbua akili na hutaki kuniambia”
“ my dear angel ,wewe ndiye maisha yangu.Wewe ndiye uliyeyashika maisha yangu.Nimekukabidhi funguo za moyo wangu.Wewe ndiye mfariji wangu,wewe ndiye furaha yangu,wewe ndiye kila kitu kwangu sasa kwa nini nikufiche kitu?Hakuna kitu nimewahi kukuficha wewe mpenzi wangu na haitakuja tokea nikawa na tatizo nikashindwa kukwambia.Sasa nisipokwambia wewe nitamwambia nani tena?”
Patrick alijitahidi kumtoa Vero wasiwasi aliokuwa ameanza kuwa nao juu yake na mara moja akaazimia moyoni kubadilika kitabia ili Vero asije akaendelea kumdadisi.Taratibu akaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ya ucheshi na uchangamfu mkubwa kitu ambacho Vero alikifurahia sana.

ENDELEA…………………………

Ni jumamosi angavu ndani ya jiji la Dar es salaam,jiji lililojaa kila aina ya pilika na purukushani.Jua lilikuwa likielekea magharibi na kulipisha giza lichukue nafasi yake.Jioni hii iliwakuta Patrick na Veronika wakiwa katika pilika pilika za kujiandaa kuelekea katika kinyang’anyiro cha kumsaka mrembo wa taifa katika ukumbi wa Diamong jubilee.
Patrick ndiye aliyekuwa katika pilika pilika nyingi zaidi jioni hiyo.Siku hii ilikuwa ni moja kati ya siku zake kubwa kabisa katika maisha yake.Ni siku ambayo aliamini ingemkutanisha tena na kiumbe ampendaye kwa dhati ya moyo wake.Alikuwa ndani ya suti nzuri ya gharama kubwa.Suti hii huwa anaivaa kwa nyakati maalum kama hizi.Hakika alikuwa amependeza vilivyo kijana huyu.Wakiwa katika harakati z a kumalizia kujiandaa simu yake ikaita.Alkuwa ni Andrew.
“Haloo Andrew”
“Hallo Patrick vipi mko tayari?aliuliza Andrew huku akicheka kichinichini.
“Tupo tayari Andrew na muda wowote toka sasa tunaweza kuanza safari ya kuelekea ukumbini”
“Ok Patrick sisi tayari tumekwishajiandaa na muda wowote tutakuwa njiani pia kuelekea huko na tutawasubiri nje ya ukumbi ili tuingie pamoja.Ila ndugu yangu nakuomba kitu kimoja katu usihamaki.Wala usionyeshe aina yoyote ya mstuko pindi utakapomuona Happy .Najua tu lazima kunaweza kutokea na kitu kama mstuko fulani utakaomuona Happy lakini naomba ujaribu kujizuia kwa sababu pale tutakuwa tuko na Vero na Vick kwa hiyo wanatakiwa wasihisi kitu chochote.Mimi nitakuwa macho kuhakikisha kuwa hakuna kitu chochote kitakachoharibika “
“Usihofu Andrew nalifahamui hilo na niko makini nalo sana..” akasema Patrick
Baada ya kumaliza kujiandaa na kuhakikisha kuwa wako safi wakaingia garini na kueleka Diamond Jubilee.

* * * *

Ukumbi wa Diamond jubilee ulikuwa umefurika watu pasi mfano.Pamoja na ukumbi kufurika watu bado watu walikuwa wakimiminika ukumbini hapo kwa lengo la kushuhudia mchuano wa kumtafuta mrembo wa Taifa atakayeliwakilisha Taifa katika mashindano ya dunia.
Patrick,Vero,Andrew na Vick waliwahi sana kuingia ukumbini na kuchukua moja kati ya meza za mbele kabisa.Patrick moyo ulikuwa ukimdunda sana usiku huo,.Andrew alilifahamu hilo na hivyo akawa makini sana katika kuhakikisha kuwa hakuna kitu kitakachoharibika .Toka wameingia ukumbini Patrick alikuwa kimya .
“Patrick are you ok?Vero akauliza baada ya kuona Patrick yuko kimya sana.
“Yes I’m ok Vero usihofu.”
Mara muongoza shughuli akatokea jukwaani na kuanza kutangaza.
“Mabibi na mabwana mliohudhuria mashindano haya makubwa ya urembo nchini napenda kuwakaribisha sana katika usiku huu wa pekee kabisa kwetu sote.Ni usiku wa pekee kwa sababu leo tutaandika historia mpya kabisa katika mashindano ya urembo hapa nchini na ulimwengu kwa ujumla.Kwa mwaka huu kamati nzima ya Miss Tanzania imeazimia kufanya mabadiliko makubwa sana na nyie wote mlioko hapa ndio mtakaokuwa mashahidi wa kile kitakachotokea usiku wa leo.Nasema karibuni sana katika usiku huu na tujumuike sote mimi naitwa Mc Thora kwa wale ambao hawanifahamu.."
“Mabibi na mabwana kabla hatujaendelea mbele na ratiba yetu ningependa kwanza kumkaribisha jukwaani mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainments ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu Mabibi na mabwana makofi kwa Mr Petty.s Woris”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainments akapanda jukwaani akiwa amevalia nadhifu kabisa.
“viongozi mbali mbali ,watazamaji wote mliohudhuria mashindano haya usiku huu mabibi na mabwana asalaam aleikhum.Ni furaha ilioje kwetu sisi kama Masimulizi entertainments kudhamini mashindano makubwa kama haya ya urembo hapa nchini.Kama wote mnavyoshuhudia mashindano ya mwaka huu yamekuwa na utofauti mkubwa na mengine yaliyotangulia.Maandalizi yake yamekuwa mazuri ,zawadi zimeboreshwa na ushindani miongoni mwa washiriki umeongezeka mara dufu.Kwa kuwa ni mara yetu ya kwanza kudhamini mashindano makubwa kama haya bado kunaweza kuwa na kasoro kadhaa ambazo nina imani kwa kushirikiana na wadau wote wa urembo hapa nchini tutasaidiana kuzitatua.Nina imani bado tutaendelea kudhamini na kuandaa matamasha mengi na makubwa zaidi hapa nchini ili kuzidi kuukuza wigo wa burudani hususani sanaa hii ya urembo.Mwisho kwa niaba ya uongozi na wafanya kazi wote wa Masimulizi entertainments napenda kuwatakia wote utazamaji mzuri wa mashindano haya usiku huu.Ahsanteni sana.”
Baada ya kumaliza kusema machache akarudisha kipaza sauti kwa muongoza shughuli kisha akashuka jukwaani.
“mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mkurugenzi wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano haya kwa mwaka huu..Mabibi na mabwana kwa mujibu wa ratiba yetu kinachofuata kwa sasa ni kuwatambulisha majaji wa mchuano huu ambao ndio watakaofanya kazi kubwa na ngumu ya kutuchagulia mrembo mwenye sifa ya kuwa mrembo wa taifa.Majaji tulionao usiku huu ni saba.Ningeomba jaji utakaposikia jina lako likitajwa basi usimame ili watu wakufahamu.Wa kwanza ni Mr Ernest Namesha,wa pili ni ndugu Mecky ,tunaye pia Mr Boniventure Gregory,anayefuatia ni Mr Samweli Nathaniel,tunaye pia dada yetu mpendwa usiku huu naye ni dada Esther mathias,pia tunaye Mrs Coletha brown,tunaye vile vile bi Susan Abrahams na wa mwisho ni ndugu Jacob Lyimo.Hawa ndio majaji wetu ambao watakuwa wakifanya kazi ngumu ya kumchagua mrembo wa Taifa usiku huu wa leo.”
“mabibi na mabwana baada ya kuwafahamu majaji wa mchuano huu wa leo sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 katika show maalum waliyoiandaa “
wimbo ukaanza kupigwa na warembo wakaanza kutoka huku wakicheza kwa staili yenye kuvutia sana.makofi nderemo na vifijo vikatawala ukumbini.Patrick alielekeza macho na akili yake yote jukwaani na bila kukosea alimuona Happy ambaye alikuwa amependeza kupindukia Jasho likaanza kumtiririka akatoa kitambaa na kujifuta.Alikuwa kimya kabisa.
Baada ya show ya warembo kukamilika ziliendelea burudani nyingine toka kwa wasanii mbali mbali kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana baada ya kupata burudani hizo zakukata na shoka sasa naomba niwalete kwenu warembo wote 26 ili muwatambue.Watapita hapa jukwaani mmoja mmoja .”
Warembo wakaanza kutoka nyuma ya jukwaa na kuanza kupita mbele ya watazamaji.Kidogo Patrick atamke kitu baada ya kusikia jina la Happy likitajwa .Happy akapita jukwaani huku kelele za shangwe zikisikika.Happy alikuwa akionekana kama malaika usiku huu.Alikuwa amependeza vilivyo.Kila mtu aliustaajabia uzuri wa binti huyu mwenye kila sifa ya kuwa mrembo wa Taifa na dunia.Kelele zile za mashabiki zilizidi kumchanganya Patrick na kumfanya ahisi kuchanganyikiwa.Andrew alikuwa makini sana kwa lolote ambalo lingeweza kutokea.
Baada ya kupita jukwaani kujitambulisha kwa mashabiki zikafuata burudani za aina yake toka kwa wanamuziki.Kisha Muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana mambo yanazidi kupamba moto.Mambo ni bam bam na kama nilivyowaeleza toka mwanzo kuwa Masimulizi entertainment wameleta mageuzi makubwa katika mashidano ya mwaka huu .Kwa sasa napenda kuwaleta kwenu warembo wote 26 wakiwa katika vazi la ufukweni.Mhh ! hapa pana kazi kweli kweli .mabibi na mabwana hebu tuwashangilie hawa warembo wetu watakapokuwa wakipita jukwaani katika vazi la ufukweni.”
Warembo wakaanza kupita jukwaani wakiwa katika vazi la ufukweni.Siyo siri walikuwa wamependeza vilivyo.Baada ya kumaliza kupita na vazi la ufukweni zikafuata tena burudani halafu warembo wote wakapita tena kwa mara nyingine na vazi la ubunifu.Kelele zilikuwa kubwa sana kila walipopita warembo Neema wa Arusha na Happy wa Ilala.Warembo hawa walionekana kuchuana vilivyo.Kisha pita na vazi la ubunifu muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana tayari tumewashudia warembo wetu 26 wakipita hapa mbele yetu wakiwa katika mavazi tofauti tofauti.Kwa sasa ule wakati mliokuwa mkiusubiri kwa hamu kubwa unaelekea kuwadia.Kwa hivi sasa tutakwenda kuwafahamu warembo 10 bora ambao wameonekana kufanya vizuri zaidi .Naomba sasa nimkaribishe Mrs Coletha brown ili aje atutangazie wale warembo wetu kumi waliofanya vizuri zaidi.Karibu sana mama.”
Mrs Coletha brown akapanda jukwaani akiwa na karatasi yenye majina ya warembo kumi waliofanya vizuri na ambao wataendelea na mchuano.
“mabibi na mabwana napenda kuchukua nafasi hii kwanza kuwapongeza waandaaji wa mashindano haya ambayo kwa mwaka huu yameboreshwa kwa kiwango cha juu kabisa.
Mabibi na mabwana kazi yetu usiku wa leo imekuwa ni ngumu sana .Warembo wote wako katika hali ya ushindani wa hali ya juu mno.Lakini tumeweza kuwapata wale kumi ambao ni bora zaidi na ambao nitaenda kuwataja hivi punde.Nambari 12 Nelea shulo,nambari 9Saida abdi,nambari 4 Upendo timelo,Nambari 20 Neema ,Nambari 11 Esther stevens,Nambari 6 Happy Kibaho,nambari 22 Elimeena kimuo,nambari 26 bahati udhoka,nambari 16 Winifrida mwasajuki,na mwisho ni namba 13 genevieve alphonse.”
Kelele za kushangilia zikasikika ukumbini.Warembo waliofika hatua ya kumi bora wakajipanga mstari.wakapiga picha ya pamoja kisha zikafuata burudani .baada ya burudani mc akapanda tena jukwaani.
“Mabibi na mabwana bado tunaendelea na mchakato wetu wa kuifikia ile hatua kubwa kabisa ambayo kila mmoja wetu aliyeko hapa ana hamu ya kuishuhudia.Kila mmoja anatamani amfahamu mrembo wetu mpya wa Taifa.Kwa sasa tutaenda kuwatafuta wale watano bora ambao kutoka kwao tutampata mrembo wetu.Atapanda tena Mrs Coletha kuja kututangazia warembo watano bora .”
mrs Coletha akapanda tena jukwaani akiwa ameongozana na watu wawili wa miraba minne wanaomlinda.
“mabibi na mabwana kama nilivyowaambia awali kuwa kazi yetu leo imekuwa ngumu sana hasa kutokana na jinsi warembo wote walivyo na vigezo vya juu mno kiushindani.Lakini pamoja na wote kuwa na ushindani wa juu tumeweza kufanikiwa kuwachuja na kupata wale watano ambao wameonekana kuwa ni bora zaidi.
Warembo waliopita hatua ya tano bora ni mrembo nambari 16 Winifrida mwasajuki,nambari 20 Neema i,nambari 13 Genevieve alphonse,nambari 26 Bahati udhoka na mwisho ni nambari 6 Happy Kibaho .”
Kelele kubwa zikasikika zikishangilia.Kila mtu pale ukumbini alikuwa ameridhika na kazi waliyoifanya majaji.Hakukuwa na aina yoyote ya upendeleo.Baada ya kuwatambua warembo wote waliofanikiwa kuingia hatua ya tano bora hatimaye kikafuata kipindi cha maswali.Ni Happy kibaho tena ndiye aliyejibu swali vizuri zaidi na kuwafanya watu wote ukumbini kumshangilia kwa nguvu.Kila mtu aliamini kuwa Happy ni lazima angeibuka kuwa mrembo wa Taifa.Patrick jasho lilikuwa likimtiririka mwilini.Alijitahidi kwa kila alivyoweza ili asiweze kuonyesha hali yoyote ya utofauti pale mezani.Baada ya kipindi cha maswali kumalizika ikafuata burudani moja kisha muongoza shughuli akapanda jukwaani.
“mabibi na mabwana ule wakati uliokuwa ukisubiriwa na kila mtu hapa ukumbini naona sasa umewadia.Huu ni wakati wa kumtambua mrembo wetu mpya wa Taifa.Napenda nichukue fursa hii kuwashukuru sana majaji kwa kazi ngumu waliyoifanya usiku huu kwa kutuchagulia mrembo mpya wa Taifa.Kabla sijamkaribisha jaji mkuu kuja kutangaza mshindi wa shindano hili napenda kumkaribisha mrembo anayemaliza muda wake ili aweze kuongea machache na kuwaaga rasmi kabla hajalivua taji la Miss Tanzania.”
Helen Daudi mrembo anayemaliza muda wake alipanda jukwaani huku akishangiliwa vilivyo.Alipewa kipaza sauti na kusogea mbele.
“mabibi na mabwana ,wageni waalikwa,waheshimiwa majaji ,waandaaji na wadhamini wote wa mashindano haya habari za usiku.Napenda kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha mimi kutimiza moja ya ndoto zangu nayo ni kuwa mrembo wa Tanzania.Nawashukuru vile vile wazazi wangu na ndugu zangu kwa kunipa moyo toka katika hatua za awali za kinyang’anyiro hiki hadi nilipobahatika kuchukua taji.Mabibi na mabwana kulivaa taji la Miss Tanzania ni mzigo mkubwa.Nimeshuhudia mimi mwenyewe uzito wa taji hili kubwa la urembo hapa nchini.Yapo mengi ambayo unapaswa kulifanyia taifa hili ukiwa kama mrembo wa Taifa.Kuna mazuri na magumu yake.Zipo changamoto nyingi ambazo yakubidi upambane kufa na kupona ili uweze kushinda.Napenda kuishukuru kamati nzima ya Miss Tanzaina kwa ushirikiano mkubwa walionipa katika kipindi chote nilichokuwa nimevaa taji hili.Sintaweza kumtaja mmoja mmoja lakini napenda niwashukuru wote kwa ujumla.Napenda niwashukuru vile vile wadau wote wa sanaa hii ya urembo hapa nchini kwa sapoti yao kubwa waliyonipa.Wamenisaidia sana kuifahamu sanaa hii ya urembo vizuri.Nawashukuru pia wananchi wote wa Tanzania kwa kunikubali Nawapenda wote na ninaahidi kushirikiana na mrembo atakayevaa taji hili usiku huu katika yale yote mazuri niliyokuwa nimeyafanya kwani kulivua taji hili si mwisho wa kuendeleza yale yote niliyokwisha yafanya wakati niko na taji.Mwisho kama binadamu kuna wakati naweza kuwa nimemkosea huyu na yule kwa namna moja au nyingine.Napenda kuchukua nafasi hii kwa dhati kabisa kuwaomba msamaha wale wote niliowakosea.Tusameheane na kuanzia usiku huu tuanze maisha mapya.Ahsanteni sana.”
Alimaliza kutoa machache mrembo huyu akarudi katika kiti chake cha heshima huku akishangiliwa na watu.’
“naam mabibi na mabwana huyo alikuwa ni mrembo anayemaliza muda wake.Na sasa ule wakati tuliokuwa tukiusubiri kwa hamu kubwa ndio umewadia.Ni hivi punde tutaenda kumfahamu mrembo wetu mpya.Naomba sasa nimwite Mr Jackob Evarist ili aweze kututajia washindi wetu.”
Mr jacob akapanda jukwaani.
“Mabibi na mabwana kama alivyotangulia kusema Mrs Coletha brown kuwa mchuano wa leo ulikuwa mgumu sana.Tunamshukuru Mungu kuwa tumeweza kumpata mrembo wa taifa licha ya kuwa na wakati mgumu hasa kutokana na kila mrembo alivyokuwa amejiandaa.Mabibi na mabwana nitaanza kuitangaza nafasi ya tatu hadi moja.”
Alitulia kidogo kisha akaendelea.
“Nafasi ya tatu imekwenda kwa mrembo nambari 16 winifrida mwasajuki”
alitulia kwanza na kumpisha mrembo huyu apite mbele huku akishangiliwa.
“nafasi ya pili imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 20 Neema Jaspa”
Kelele za shangwe zikasikika.Miss Arusha Neema Jaspa binti mwenye ngozi nyeusi yenye kung’aa akapita jukwaani akiwa ndani ya tabasamu kubwa.
“Na sasa mabibi na mabwana ni nafasi ya kwanza.Nafasi ya kwanza imekwenda kwa mrembo mwenye nambari 6 Happy .”
Tangu ukumbi wa Diamond jubilee ujengwe hakujawahi tokea shangwe kubwa kama hii ya usiku huu ya kuushangilia ushindi wa Happy .Mrembo huyu alifanikiwa kuzikonga nyoyo za watu vilivyo.
Patrick alishindwa kujizuia akainuka na kushangilia kwa nguvu sana.
Jukwaani Happy machozi yalikuwa yakimtoka.Hakuamini kama ni yeye ndiye aliyetangazwa mshindi wa shindano hili hasa kutokana na upinzani mkubwa uliokuwepo miongoni mwa washiriki.Watu waliKumbatiana na kupeana mikono ya hongera kuashiria kukubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji ya kumchagua Happy kuwa mrembo wa Taifa.Kila mmoja aliamini kuwa Happy alistahili kulitwaa taji lile.
Baada ya kama dakika kumi hivi za hoi hoi na nderemo muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana nafikiri hoi hoi na nderemo hizi zote ni kuonyesha jinsi gani wote kwa pamoja tunavyokubaliana moja kwa moja na maamuzi ya majaji.Happy kibaho ndiye miss Tanzania wetu mpya.Kinachofuata sasa ni mrembo anayemaliza muda wake kulivua taji na kumvisha mrembo mpya.”
Zoezi hili likafanyika huku likishangiliwa kwa nguvu sana.na baada ya zoezi hili kukamilika muongoza shughuli akapanda tena jukwaani.
“mabibi na mabwana tukio linalofuata sasa ni la kumkabidhi Miss Tanzania funguo za gari lake.Tunamuomba mkurugenzi mkuu wa Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu apande jukwaani na kumkabidhi Miss Tanzania funguo hizo.”
Petty woris mkurugenzi wa Masimulizi entertainment akapanda jukwaani na bila kupoteza muda akamkabidhi Happy funguo za gari ambalo ni zawadi ya kwanza kwa miss Tanzania.Akiwa katika tabasamu pana sana alipita jukwaani huku akizipunga funguo hewani .Kelele za kushangilia zilisikika.
Baada ya zoezi hilo zikafuata burudani mbili kisha mashindano yakafungwa rasmi na taratibu umati wa watu ukaanza kuondoka maeneo hayo ya Diamond jubilee kila mmoja akiwa amesuuzika vilivyo na ushindi wa Happy kibaho.
Happy sasa alikuwa akipiga picha na watu mbali mbali huku akisongwa na waandishi wa habari wakitaka kufahamu mawili matatu ingawa mkurugenzi wa Miss Tanzania alijitahidi kuwazuia kwani Happy angefanya mkutano na waandishi wa habari hapo kesho lakini haikusaidia kitu.
Patrick ambaye alionekana kuchanganyikiwa kadiri muda unavyosonga alitoa simu yake na kuanza kubonyeza namba kisha akajitenga na akina Andrew ambao kwa sasa walikuwa wamesimama wakijiandaa kuondoka.Patrick aliitumia njia ile ya kujifanya anapiga simu ili aweze kuondoka mahala pale bila kutiliwa mashaka kwani lengo lake kuu lilikuwa kujaribu kupata nafasi ya kuonana na Happy .Andrew alielewa mara moja nini kilichokuwa kikiendelea akawaomba Vero na Vick waondoke mahala pale waelekee katika magari.Lengo lilikuwa kuwatoa wasiwasi akina Vero.
Patrick alikuwa akipigana vikumbo na waandishi wa habari waliokuwa wakichukua picha na kumuuliza Happy maswali mawili matatu.Alijitahidi sana kupenya na hatimaye akajikuta yuko mahala ambako anaweza kumuona Happy kwa ukaribu.Jasho lilikuwa likimtiririka na moyoni alikuwa na wasi wasi mwingi lakini hii haikukumkatisha tamaa ya kuonana na Happy .Alijisogeza taratibu na hakuna mtu yeyote aliyeweza kuwa na shaka naye kuwa si mwandishi wa habari tena toka katika chombo cha habari kikubwa hapa nchi au nje ya nchi kutokana na muonekano wake.
“Hongera sana Happy madame Tanzanie”Akasema Patrick wakati huo akiwa uso kwa uso na Happy .Happy kwa wakati huo hakujua aliyekuwa akiongea naye .Alijua wote ni waandishi wa habari.Lakini neno lile “Madame Tanzanie”likamstua na kumfanya ainue uso wake na kumtazama vizuri mtu yule aliye mpa salamu ile.Kwanza alihisi sauti ile ni kama si ngeni masikioni mwake .mbele yake alikuwa amesimama kijana nadhifu akiwa ndani ya tabasamu lenye kuonyesha aina Fulani ya wasi wasi.macho yake yakakutana na macho ya Patrick na kwa kasi ya umeme kumbukumbu ya ghafla ikamjia kichwani
“Noooooo!!!!!!!!!!! Pa………..t…………….”
Akaanguka na kupoteza fahamu.
Kizaa zaa cha ghafla kikatanda hapo ukumbini.Kwa sekunde kadhaa ikatokea taharuki kubwa.Kila mtu akapatwa mstuko kwa kitendo cha Miss Tanzania kupoteza fahamu ghafla.
Haraka haraka walinda usalama wakamwinua na kumkimbiza katika gari la wagonjwa ambalo lilikuwa nje tayari kabisa kwa dharura kama hii.Kwa kasi ya ajabu gari lile likaondoka kuelekea Hospitali.
Watu waliokuwa bado wako ukumbini hawakuamini kilichotokea ghafla vile.Waandishi wa habari wakalichukua tukio lile kama lilivyotokea.
Patrick nusura akili imruke kwa kitendo cha Happy kupoteza fahamu.Taratibu alihisi kuishiwa nguvu lakini tayari Andrew alikuwa ameshafika ,akamshika mkono na kumtoa nje ya ukumbi .
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 4
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Hongera sana Happy madame Tanzanie”Akasema Patrick wakati huo akiwa uso kwa uso na Happy .Happy kwa wakati huo hakujua aliyekuwa akiongea naye .Alijua wote ni waandishi wa habari.Lakini neno lile “Madame Tanzanie”likamstua na kumfanya ainue uso wake na kumtazama vizuri mtu yule aliye mpa salamu ile.Kwanza alihisi sauti ile ni kama si ngeni masikioni mwake .mbele yake alikuwa amesimama kijana nadhifu akiwa ndani ya tabasamu lenye kuonyesha aina Fulani ya wasi wasi.macho yake yakakutana na macho ya Patrick na kwa kasi ya umeme kumbukumbu ya ghafla ikamjia kichwani
“Noooooo!!!!!!!!!!! Pa………..t…………….”
Akaanguka na kupoteza fahamu.
Kizaa zaa cha ghafla kikatanda hapo ukumbini.Kwa sekunde kadhaa ikatokea taharuki kubwa.Kila mtu akapatwa mstuko kwa kitendo cha Miss Tanzania kupoteza fahamu ghafla.
Haraka haraka walinda usalama wakamwinua na kumkimbiza katika gari la wagonjwa ambalo lilikuwa nje tayari kabisa kwa dharura kama hii.Kwa kasi ya ajabu gari lile likaondoka kuelekea Hospitali.
Watu waliokuwa bado wako ukumbini hawakuamini kilichotokea ghafla vile.Waandishi wa habari wakalichukua tukio lile kama lilivyotokea.
Patrick nusura akili imruke kwa kitendo cha Happy kupoteza fahamu.Taratibu alihisi kuishiwa nguvu lakini tayari Andrew alikuwa ameshafika ,akamshika mkono na kumtoa nje ya ukumbi .

ENDELEA…………………….

Saa kumi na moja asubuhi miss Tanzania Happy alizinduka.akaangaza huku na huku akatambua kuwa alikuwa hospitali.Taratibu akaanza kukumbuka kilichotokea na kumfanya awepo pale hospitali mida ile.Akalikumbuka tukio zima lililotokea usiku.
“ that’s him..I saw him ”Happy akajikuta akiongea kwa sauti na kuwastua watu waliokuwemo mle chumbani.Miongoni mwa watu waliokuwa wakifuatilia kwa karibu hali ya Happy ni mdogo wake Margreth .Alikuwepo pia mkurugenzi wa Miss Tanzania pamoja na watu wengine kadhaa.Mara tu waliposikia kuwa ameamka mkurugenzi wa Miss Tanzania akamwita daktari ambaye alikuja na kumpima.Baada ya vipimo vyote kuonyesha hakuna tatizo zaidi ya mstuko wa kawaida daktari alimuomba Happy aendelee kupumzika na asibughudhiwe.Daktari akawaomba wote waliokuwa pale Hospitali kwa ajili ya Happy waende kupumzika na kumwacha mgonjwa apumzike kwani bado alihitaji mapumziko ya kutosha.Ni margreth pekee ndiye aliyebaki ili kumsaidia dada yake.Baada ya watu wote kutawanyika Happy akageuza kichwa na kumwita margreth.
“ Pole sana Happy.Unaisikiaje sasa ”akasema Margreth
“I’m ok magie." akajibu happy.Margreth akamuangalia kwa makini kisha akamuuliza
" happy kitu gani kilitokea mpaka ukapoteza fahamu?..Happy akamuanglai mdogo wake usoni halafu akasema
" Maggie I saw Patrick yesterday”
“Whaaaaat!!!!!!!!!!!!!!!!”akauliza margreth kwa mstuko.
' Patrick !!....Patrick yupi ? akauliza Margreth
" Patrick mpenzi wangu wa zamani" akasema Happy
" happy Patrick is dead....hakuan namna ambayo ataweza kurudi.Inawezekana ulimafananisha na mtu" akasema Margreth.
" hapana margreth..I saw him with my own eyes.It was him.." akasisitiza Happy“Sister are u ok?Magie akauliza tena.
“Sina tatizo magie ni kweli nilimuona Patrick jana wakati nikiongea na waandishi wa habari Alikuja mbele yangu na kunisalimu .Alitamka maneno Fulani ambayo yalinifanya nistuke na nilipomtazama vizuri alikuwa ni yeye.Nina hakika ni yeye kwani ni mtu ambaye yuko moyoni mwangu kwa miaka mingi na kila siku ninaangalia picha yake hivyo siwezi kuwa nilimfananisha.Ninaamini nilimuona Patrick na ndio maana nikastuka hadi kupoteza fahamu.I’m confused Maggie .Totaly confused.”
Kimya kikatanda mle chumbani .
“Margreth tafadhali usimwambia mtu yeyote juu ya habari hii.”
“Usijali sister siwezi mweleza mtu" akasema Margreth.
“Sasa maggie naomba unisaidie kitu kimoja.”Akasema Happy .
“Nikusaidie nini Happy?” akauliza Margreth.
‘nataka kuonana na Patrick”Akasema Happy huku macho yake yamefunikwa na machozi.
“Pumzika kwanza sister ukitoka Hospitali tutaongea kwa undani juu ya suala hili.Kwa sasa bado unahitaji mapumziko ya kutosha na huhitaji kuwaza sana juu ya suala hili.”akasema Margreth.
“Thanks Maggie I understand “akasema Happy.
mara mlango wa chumba alimolazwa Happy ukafunguliwa wakaingia wazazi wa Happy ambao walikuwa safarini lakini kutokana na matatizo aliyoyapata mtoto wao ikawabidi waahirishe safari yao na kurudi Tanzania haraka.Mama yake akamkumbatia huku machozi yakiwatoka wote .Baada ya kusalimiana Happy akawahakikishia wazazi wake kuwa kwa sasa alijisikia mzima kabisa na pengine mchana wa siku hiyo angeruhusiwa kurudi nyumbani.
Wakiwa katika maongezi akaingia muuguzi akiwa na sinia la dawa.akawaomba radhi wote waliokuwa mle ndani kuwa alihitaji kumuhudumia mgonjwa hivyo akawaomba watoke nje kwa dakika kadhaa.Alipohakikisha wote wametoka akamkaribia Happy .
“Samahani dada Happy nina ujumbe wako ambao nimeambiwa ni wa muhimu na nyeti sana .Aliyenipa ujumbe huu amenionya kwamba nisikupe mahala penye watu .”
“Nani aliyekupa ujumbe huu?
“simfahamu ila ni kijana mmoja alikuwa amevaa suti nyeusi na hakujitambulisha jina lake .yeye alisema ukishausoma tu utakuwa umefahamu.”
Yule muuguzi akatoa bahasha toka katika mfuko wake wa koti na kumpatia.Baada ya kumpatia dawa muuguzi yule alitoka na kumwacha Happy jasho likimtiririka.Hakujua ni nani aliyeleta ujumbe ule.
Aliishika bahasha ile na kuifungua taratibu.Ilikuwa ni kadi nzuri iliyomtakia uponaji wa haraka.Ndani ya kadi ile kikaanguka kikadi kidogo .Akakiokota na kukisoma.Nusura apatwe na wazimu baada ya kuisoma kadi ile.Margreth akaingia mara akastukia dada yake amesimama ghafla na kumkumbatia.
“dada kuna nini?akauliza margreth kwa mshangao.
“Its Patrick”
“Patrick !!!!!!!!!!!!!!!”
“Yes .Look at this” akasema Happy akimuonyesha Margreth ile bussines card
“Mhhh”margreth akaguna
Wakati margreth akiisoma ile kadi mlango ukagongwa na likaingia kundi la warembo.wote wakafurahi baada ya kumkuta Happy ni mwenye furaha namna ile.

* * * *
MISS TANZANIA AZIMIA JUKWAANI , HAPPY KIBAHO MISS TANZANIA MPYA , ZENGWE LATAWALA UKUMBINI MISS TANZANIA AZIRAI,Hivyo vilikuwa ni baadhi ya vichwa vya habari vilivyotanda katika magazeti mengi kwa siku hiyo.Karibu magazeti yote yalijaribu kuandika kwa kina juu ya tukio la kuzimia kwa miss Tanzania ukumbini,lakini hakuna hata gazeti moja lililoweza kuandika au kuufahamu ukweli juu ya tukio lile.
Akiwa katika kibanda cha kuuzia magazeti asubuhi hiyo Andrew alinunua karibu kila gazeti lililotoka siku hiyo na kupitia habari ya kuanguka kwa Happy .Lengo lake kubwa ni kutaka kufahamu kama kuna mtu yeyote aliyeweza kumtilia shaka Patrick kuwa ndiye aliyekuwa chanzo cha tukio lile la kuanguka Happy ukumbini.katika magazeti yote hakukuta habari yoyote iliyomuhusisha Patrick na tukio lile.
Akatoa simu yake na kumpigia Patrick.Simu ikapokelewa na Vero
“Hallo shemeji”akasema Vero.
“Shemeji mambo vipi?habari za toka jana ?Andrew akauliza
“nzuri tu shemeji”
“Vipi jamaa bado kalala?
“Ameingia maliwatoni kidogo anakuja sasa hivi”
Muda huo huo Patrick akatokea Vero akampa simu na kumwambia Andrew anahitaji kuongea naye.
Hallow Andrew vipi ? Akasema Patrick
“Poa Patrick vipi maendeleo yako ?
“Nashukuru Mungu Andrew naendelea vizuri.Hebu nipe habari’
“Habari ni ndefu kidogo lakini kwa ufupi tu ni kwamba leo sijalala kabisa.Baada ya kuachana pale ukumbini nikamrudisha Vick kwake halafu nikaanza kufuatilia Happy alipelekwa hospitali gani.Kwa msaada wa rafiki yangu mmoja mwandishi wa habari nilifanikiwa kujua mahala Happy Alikopelekwa.Unajua walificha juu ya mahala alikopelekwa Happy kwa kuwakwepa waandishi wa habari.Alipelekwa katika hospitali moja ya kanisa maeneo ya msasani.Mpaka saa kumi na mbili nilikuwa pale hospitali na ndipo nilipopata taarifa kuwa tayari Happy alikuwa amezinduka.Kuna muuguzi mmoja anafahamiana na Vick pale na ndiye huyo aliyenipa msaada mkubwa sana.Nilimpa kiasi Fulani cha pesa yule muuguzi na kumuomba aipeleke business card yako kwa Happy na kumwambia apige namba zile zilizoandikwa katika business card hasa muda wa mchana.Yule muuguzi akajitahidi na kuifikisha kadi ile .Baada ya kuhakikisha tayari Hapy ameipata mimi nikaondoka.Kabla sijafika nyumbani nikaona nipite kwanza katika kibanda cha magazeti ili nione magazeti yanasema nini lakini hakuna chochote kibaya.Kwa hiyo Patrick nina imani muda wowote Happy anaweza akakupigia simu.Mimi kwa sasa nakwenda nyumbani kupumzika tutaonana baadae ila be carefull brother’ akasema Andrew
Patrick akavuta pumzi ndefu kisha akasema
“Sijui nikushukuruje Andrew kwa msaada huu mkubwa . thanks a lot.Dont worry I’ll be careful. see you later”
Patrick akakata simu kisha akaelekea jikoni ambako Vero alikuwa akiandaa stafstahi akamsaidia kuandaa mlo wa asubuhi kitendo ambacho Vero alikifurahia sana

* * * *

Saa sita kamili mchana Happy akaruhusiwa kutoka hospitali.Akiwa na furaha isiyokifani huku ameongozana na mama yake pamoja na mdogo wake kipenzi Margreth bila kumsahau mwenyekiti wa kamati ya Miss Tanzania pamoja na wajumbe kadhaa wa kamati hiyo na ujumbe wa watu toka Masimulizi entertainment ambao ndio wadhamini wakuu wa mashindano hayo walilakiwa na kundi kubwa la warembo waliokuwa wakisubiri atoke kwani walikwisha taarifiwa kuwa angeruhusiwa mchana.Walitumia kama robo saa kusalimiana na kupongezana vile vile kupeana pole kwa yaliyotokea. Kisha akapanda gari na kuelekea nyumbani kwao.Happy alikuwa ni mwenye furaha sana mchana huo.Ni margreth pekee ndiye aliyefahamu siri ya furaha ile aliyokuwa nayo dada yake.Akiwa garini Happy akafumba macho kana kwamba amelala lakini alikuwa amezama katika mawazo na mara akajikuta akitamka kwa sauti.
"Thanks God I found him"
Mama yake aliyekaa kiti cha mbele aligeuka na kumuangalia mwanae bila kusema kitu.
Margreth yeye alikuwa katika lindi la mawazo na hasa akijaribu kuvuta taswira ya kinachoenda kutokea huko mbeleni.Anafahamu wazi kuwa katika dunia hii Patrick ndiye mwanaume pekee ambaye Happy anampenda .Licha ya kupotezana kwa muda mrefu lakini bado taswira ya Patrick haikufutika moyoni mwake.Kwa sasa Happy tayari ana pete ya uchumba ambayo amevishwa na mchumba wake aitwaye Mike cambell raia wa Marekani.Mike ni kijana anayependwa sana na kila mtu katika familia ya akina Happy .Pamoja na kuwa na pete ya uchumba kidoleni bado Happy ameshindwa kuifuta kabisa kumbukumbu ya Patrick moyoni mwake.Kuonekana kwa Patrick ni wazi kunaweza kusababisha mvurugano mkubwa ambao ni vigumu kujua hatma yake itakuwa nini.Ni wazi Mike alimpenda Happy kupita maelezo.Hiki ni kitu kilichomuumiza kichwa Margreth.
Baada ya mzunguko mrefu hatimaye wakawasili nyumbani ambako walilakiwa na kundi jingine la warembo,ndugu jamaa marafiki na waandishi wa habari wote walifika kumpongeza na kumpa pole Happy .Kisha salimiana na kupongezana Happy akaomba aachwe kidogo apumzike.
Happy akaoga na kupata chakula kisha akaingia chumbani kwake kupumzika.Kitu cha kwanza kabisa ambacho alikifanya ni kuitazama tena ile business card kwa makini .akaichukua simu yake na kuandika namba zile zilizoandikwa pale juu kisha akapiga.Mapigo ya moyo wake yalikuwa yakienda kwa kasi ya aina yake alipoiweka simu sikioni akaisikia ikiita.Mikono ilianza kuloa jasho kwa wasi wasi.Hakujua angeongea nini baada ya kuisikia sauti ya Patrick.Hakujua Patrick angekuwa katika hali gani mara atakapoisikia sauti yake.Wakati akisuburi kujibiwa na sauti ambayo aliamini moja kwa moja ingekuwa ni ya Patrick akasikia kitu ambacho hakukitarajia.Ilikuwa ni sauti ya mwanamke ndiye aliyepokea simu ile ya Parick.
“hallow”Ikasema sauti ya upande wa pili.
Happy mikono ilimtetemeka,akapatwa na kigugumizi cha ghafla kilichomfanya ashindwe kuongea.
“hallow naongea na nani? ”ikauliza tena ile sauti ya mwanamke.
Happy akashindwa ajibu nini akabaki ameiweka simu sikioni.
“Haloo nani mwenzangu?Ikauliza tena..Tayari Happy chozi lilikuwa likimtoka.Mara akasikia simu ikikatwa.Kitendo kile kikamuuma akajitupa kitandani machozi yakimtoka.
“Oooh Lord why me?? Why me God? I love Patrick .Yes ni yeye tu ndiye mwanaume ninayempenda kwa dhati ya moyo wangu .Nimetengana naye muda mrefu sana na sielewi maisha yake kwa sasa nadhani tayari ana mke .Sielewi kama ninaweza vumilia nikisikia Patrick ana mke.’akawaza Happy
“Patrick I’ll fight for you and I must win you back.You are mine Patrick .I lost you once and now I’ve found you I’ll never loose you again”
Happy alikuwa akiongea peke yake maneno haya huku machozi yakimchuruzika.
* * * *
Patrick leo huamki? akasema Vero huku akimtingisha Patrick ambaye alikuwa amelala tangu alipokula chakula cha mchana.Patrick akajigeuza na kuangalia saa kubwa ya ukutani.Ilionyesha ni saa kumi na moja za jioni.
“Oh nimelala sana” akasema Patrick kwa uchovu
“Ni vizuri hata hivyo ukipata mapumziko ya kutosha” akasema Happy
Happy akaelekea jikoni akaleta juice na kummiminia Patrick katika glasi.
“Halafu nimekumbuka kuna mtu alikupigia simu nikaipokea lakini cha ajabu hakutaka kuongea kitu chochote .Nimemuuliza zaidi ya mara mbili yeye ni nani lakini hakunijibu.” akasema Happy na kumfanya Patrick astuke. Mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi..Kijasho kikaanza kumtoka .akaichukua simu na kuziangalia namba zile zilikuwa ni ngeni kabisa kwake.Hakufahamu zilikuwa ni namba za nani lakini akahisi huenda Happy ndiye aliyepiga.Kwa mujibu wa maelezo ya Andrew ni kwamba alimuelekeza Happy apige mida ya mchana.Vero akainuka akatoka mle chumbani,Patrcik akaitumia nafasi hiyo kupia zile namba.Simu ikaita bila kupokelewa,ikakatika.Akapiga tena mambo yakawa ni yale yale.Akapiga kwa mara ya tatu simu ikapokelewa.
“Hallow”Ilikuwa ni sauti tamu sana ya mtoto wa kike.Sauti hii Patrick hajaisahau mpaka hvi sasa.Ni sauti ya Happy.Kabla Patrick hajaongea lolote simu ikakatika.Patrick akaipiga tena na safari hii akaambiwa kuwa simu anayopiga haipatikani tena.Akajaribu kupiga tena na tena lakini simu haikuwa ikipatikana.
Patrick akaitupa simu kitandani kwa hasira .Hakuelewa sababu ya Happy kumkatia simu.Sauti aliyoisikia ilikuwa ni ya Happy.Patrick akasimama na kuzunguka zunguka humo chumbani Vero akarejea na kumshangaa kwa namna alivyobadilika ghafla..Vero akamtazama akapatwa na wasiwasi.
“Patrick dear kuna kitu gani kibaya mbona umebadilika ghafla hivyo?
Patrick akastuka na kumtazama Vero..
“Usiogope Vero.Mimi niko sawa kabisa." akasema Patrick lakini ndani ya moyo wake Vero alifahamu kabisa kwamba kuna ambo linamsumbua Patrick.
“Relax my dear jitahidi usiumize kichwa chako kwa mawazo .Kaa chini tuendelee kupanga mipango ya harusi yetu.”
Patrick akastuka kwa ndani baada ya kuisikia habari ile ya harusi.Toka amemuona Happy alisahau kabisa kama anatakiwa kuendelea na mipango ya harusi yake na Vero.Kijasho kikamtoka.
" Vero naomba niendelee kupumzika nitakapoamka tutaendelea na majadiliano." akasema Patrick na kupanda kitandani.Akafumba macho na kurejesha kumbu kumbu za nyuma. Akakumbuka toka siku ya kwanza aliyokutana na Happy.
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 5
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Patrick dear kuna kitu gani kibaya mbona umebadilika ghafla hivyo?
Patrick akastuka na kumtazama Vero..
“Usiogope Vero.Mimi niko sawa kabisa." akasema Patrick lakini ndani ya moyo wake Vero alifahamu kabisa kwamba kuna ambo linamsumbua Patrick.
“Relax my dear jitahidi usiumize kichwa chako kwa mawazo .Kaa chini tuendelee kupanga mipango ya harusi yetu.”
Patrick akastuka kwa ndani baada ya kuisikia habari ile ya harusi.Toka amemuona Happy alisahau kabisa kama anatakiwa kuendelea na mipango ya harusi yake na Vero.Kijasho kikamtoka.
" Vero naomba niendelee kupumzika nitakapoamka tutaendelea na majadiliano." akasema Patrick na kupanda kitandani.Akafumba macho na kurejesha kumbu kumbu za nyuma. Akakumbuka toka siku ya kwanza aliyokutana na Happy.

ENDELEA……………………….


MALANGALI SEKONDARI -IRINGA

Ni ijumaa iliyotawaliwa na kiubaridi cha asubuhi.Hakukuwa na dalili zozote za kuchomoza kwa jua ingawa mida hiyo ilipata saa nne za asubuhi.Anga lote lilifunikwa na mawingu.Pamoja na hali hii ya hewa lakini shughuli ziliendelea kama kawaida.Kwa watu wa eneo hili hali hii walikwisha izoea.
Saa nne na dakika kumi basi linalofanya safari zake kati ya Mbeya na Iringa lilifunga breki katika kijiji cha Mbalamaziwa.Dakika kama mbili hivi tangu basi lile lisimame kijana mmoja akashuka akiwa na mabegi matatu.Ilionyesha dhahiri kuwa kijana yule alikuwa mwanafunzi.Baada ya kuhakikisha kuwa mizigo yake yote iko salama basi likaondoka na kumwacha kijana yule akiangaza angaza macho kana kwamba kuna kitu alikuwa akikitafuta.Muda ule ule jamaa mmoja akamfuata.
“ dogo unaelekea Malangali? akauliza yule jamaa
“Ndiyo kaka “akasema yule kijana.
“ gari lile pale inakwenda Malangali muda si mrefu.Tunasubiri watu wawili watatu halafu tunaondoka.”
Jamaa yule kumbe alikuwa ni dereva.Akamsaidia kubeba mizigo hadi katika gari dogo aina ya Toyota pick up.Kutoka hapo Mabalamaziwa hadi kijiji cha Malangali usafiri unaotumika ni huu wa gari ndogo.Gari lile halikuwa na abiria yeyote ndani zaidi ya mizigo.
“ mbona hakuna abiria yeyote ?”Akauliza kijana yule
“ watu wapo si unaona mizigo yao hiyo hapo.Wote wanasubiri muda ufike .Nikipiga honi tu watakuja wote.Wale wote unawaona ni abiria wengine wanakunywa chai kule na muda wa kuondoka ukifika basi watakuja..Unaweza kwenda kupumzika pale kwa yule dada naye ni mwanafunzi anaelekea huko huko Malangali wakati tunasubiri watu wawili watatu”
Katika kibanda kimoja cha biashara kilichokuwa hakitumiki msichana mmoja alikuwa amekaa akisoma kitabu chake cha hadithi.Alikuwa amekiinamia kitabu hali iliyoonyesha kuwa alikuwa amenogewa sana na kilichoandikwa kitabuni.
“Dada habari yako” Dada yule alistuliwa na sauti ya kijana yule .Kwa sekunde kadhaa alikaa kimya akimtazama yule kaka .Sijui ni kwa nini alifanya vile lakini ni wazi alionyesha mstuko Fulani.
“Nzuri habari yako?akajibu kwa sauti laini na ya taratibu sana.Sauti ile ilionyesha kuwa dada yule hakuhitaji kusumbuliwa kwa wakati ule kwani baada tu ya kuitikia salamu ile akainama na kuendelea kusoma kitabu chake.Akiwa amesimama pembeni yake alimtazama yule dada kwa sekunde kadhaa na kugundua ni kwa nini alikuwa vile.Dada yule alikuwa na uzuri wa kipekee.Alikuwa mweupe ,mwenye nywele ndefu zilizorudishwa nyuma vizuri na kumfanya avutie zaidi.Alikuwa ni mwembamba na mrefu wastani.Binti huyu alijaaliwa sura nzuri yenye uzuri wa kipekee.
“Mhh ! hii shule ninayoenda kusoma inaonekana si mchezo.Kama kuna watoto wazuri kama huyu.Anaonekana ana nyodo kweli lakini ngoja nimuulize maswali mawili matatu akikataa kunijibu basi nitaachana naye .”akawaza yule kijana
“dada samahani nimeambiwa na yule dereva wa lile gari kuwa na wewe unaelekea malangali .Na wewe ni mwanafunzi pale? akauliza yule kijana
Dada yule akainua uso wake na kumtazama yule kijana kama alivyofanya mwanzo.
“Ndiyo. kwani vipi?akauliza
“ nilitaka tu kufahamu kwa sababu mimi ni mgeni na ninaelekea huko huko Malangali na ni mara yangu ya kwanza nafika huku hivyo nilihitaji kuyafahamu mazingira ya shule yenyewe kabla sijafika”
dada yule akamtazama tena .Macho ya binti huyu yalikuwa meupe na makali kiasi kwamba unaweza ukakwepesha macho yako asikuangalie.
“Wewe unatokea wapi? akauliza yule dada
“Natokea Mazwi secondary Sumbawanga”
“Uko kidato cha ngapi?Akauliza tena yule binti
“Kidato cha tatu”akajibu yule kijana
“hata mimi niko kidato cha tatu”Akajibu yule dada.
“Kumbe tuko kidato kimoja?”
“Yeah .Ila pale kuna michepuo.Mimi niko mchepuo wa sanaa. wewe je ?
“hata mimi ninasoma sanaa.Vipi unaionaje shule kwa ujumla ? ufundishaji wao ukoje ? Akauliza kijana yule nadhifu
“wanajitahidi kufundisha.Kumetulia na ni sehemu nzuri kwa kusoma.Mi napapenda sana”akajibu yule binti
“aisee kumbe nilifanya chaguo zuri”
‘hata mimi mwanzoni nilidhani kuwa nilikosea kuhamia shule hii .Mwanzoni nilipata shida sana kuzoea lakini mpaka sasa nimeshazoea na nimetokea kupapenda sana ”Akajibu yule dada
“Kumbe hata wewe ulihamia?Yule kijana akauliza
“Yes .Nilikuwa nasoma Mbeya secondary nikahamia huku.Sikutaka kusoma mjini nilitaka kusoma mahala tulivu mbali na nyumbani ” akasema yule dada
“Umehamia mwaka huu? akauliza yule kijana
“Hapana toka mwaka jana”
Taratibu walianza kuzoeana.Binti yule kumbe alikuwa mcheshi na muongeaji mzuri.Kwa upande wake naye alifurahia sana uchangamfu wa yule kijana.
“lakini kwa ujumla unaniambiaje kuhusu mazingira ?kijana yule akauliza.
“mazingira siyo mabaya.Mabweni ni mazuri kwa ajili ya wavulana .Sisi wasichana tunalala hosteli.Ni hosteli nzuri ya kanisa.Wale wasiopenda kulala hosteli wanapanga vyumba kijijini.Maisha ni mazuri ukisha zoea ila kwa wewe nadhani utapata shida kidogo mwanzoni.” Akasema yule dada huku akicheka.
“kwa nini unahisi ninaweza kupata shida?akauliza kijana yule.
“hahahaha! " akacheka yule dada
" muonekano wako unaonyesha hujazoea maisha ya shida”akasema huku akicheka.
Kijana yule naye akacheka sana kisha akasema
“sasa mimi na wewe nani anayeonekana hajazoea shida?
“hahahaha ! hata mimi mwanzoni nilipata shida sana lakini kwa kiasi Fulani naweza kusema kwa sasa nimeshaanza kuizoea hali halisi ya mazingira”akasema yule msichana.
Kimya kikapita cha kama dakika mbili hivi kila mmoja akiwaza lake.Yule kijana akauvunja ukimya.
“Kwani wewe dada waitwa nani?
Binti yule akatabasamu kisha kama anajishauri aseme au asiseme akajikuta akitamka
“naitwa Happy Happy Kibaho ..Wewe unaitwa nani?
“Mimi naitwa Patrick ”
“Happy nimefurahi sana kukufahamu.Na kama hutajali nitafurahi ikiwa utakuwa mwenyeji wangu” akasema Patrick.
“Hilo tu usijali.Nitakufundisha jinsi ya kunywa uji na maandazi yanayoumuliwa kwa ulanzi” akasema Happy na wote wakacheka.
“Ulanzi ! Mbona nasikia ulanzi ni pombe? akauliza patrick
“Yes ni pombe tena kule iko nyingi sana.Unakunywa pombe?”
" Hapana sinywi pombe" akajibu patrick.

“Kwa hiyo sasa hivi umetoka wapi happy ? Patrick akauliza.
“Niliomba ruhusa ya wiki moja.Nilikwenda nyumbani mara moja nilikuwa na matatizo kidogo na leo ndio narudi shuleni.Twende pale kibandani tukapate chai unajua niliondoka asubuhi bila hata kunywa chai” Happy akasema
Wakainuka pale kibandani walikokuwa wamekaa na kuelekea katika moja ya vibanda vinavyouza chai
.
* * * *

“Haya wale wanafunzi wa Malangali tumefika.”akasema utingo wa lile gari walimokuwa wamepanda akina Patrick.Yeye na Happy walikuwa wanafunzi pekee katika ile gari wakashuka..
Mida hiyo ilipata saa saba za mchana.Safari ilikuwa ni ndefu kidogo hasa kutokana na barabara .
" Patrick tushuke” Akasema Happy akiwa wa kwanza kushuka kisha akaanza kupokea mizigo ya Patrick. Happy akatoa pesa na kumlipa yule utingo .
“kata nauli ya watu wawili”
“No Happy nina nauli yangu hapa”akasema Patrick
“Usijali Patrick just keep it”akasema Happy huku akitabasamu.
Abiria wote waliokuwamo katika ile gari macho yao yalikuwa kwa binti huyu mrembo.Kwa muonekano wake alionyesha dhahiri kuwa alitoka katika familia yenye uwezo mkubwa kifedha.wote walistaajabia uzuri wa binti huyu.
“Poa mrembo karibu tena siku nyingine” akasema utingo huku akimminyia Happy jicho moja gari ikatimua vumbi na kuondoka Patrick akageuza shingo na kutazama majengo ya shule.Idadi kubwa ya wanafunzi waliokuwa katika mapumziko ya mchana walikuwa wamesimama wakiwaangalia .Patrick alishangaa kidogo kwa namna walivyokuwa wakiangaliwa.Taratibu akaanza kujiuliza maswali juu ya kuangaliwa kule.Je ni kwa sababu alikuwa na Happy ?Au ni kawaida kwa mwanafunzi mgeni kuangaliwa namna ile?
“Patrick beba begi hilo mimi ngoja nikusaidie hili hapa.”akasema Happy na kumstua Patrick
" Ahsante Happy lakini utaweza kulibeba hilo ni zito sana.Beba hili dogo.”
Wakabeba mabegi yale na kuanza kuelekea katika ofisi za shule.Ili kufika ofisini ni lazima upite katikati ya shule.Bado wanafunzi walikuwa wakiwaangalia na wengine wakisemezana.Kitendo hiki cha wanafunzi kuwaangalia kisha kuanza kusemezana wao kwa wao kilimzidishia Patrick ushawishi wa kutaka kufahamu kulikoni.
“Happy mbona wanafunzi wanatuangalia sana ?
“Just ignore them”akasema Happy kwa kifupi.
Wakafika katika ofisi za shule mizigo ikawekwa chini.
“Hapa ndio ofisi ya mkuu wa shule msaidizi .Ingia ndani ye ndiye atakayekusajili na kukupa maelekezo yote.Bye tutaonana baadae pengine tunaweza kuwa darasa moja’akasema Happy huku akichanua tabasamu pana na kuyaonyesha meno yake meupe na mwanya wa kupendeza katika meno ya juu.
“Nashukuru sana Happy tutaonana baadae” akasema patrick na Happy akaondoka .Patrick akagonga mlango na kuruhusiwa kuingia.
“Welcome gentleman.where are you from ? Ilikuwa ni sauti ya ukakamavu ya mtu ambaye Patrick aliamini moja kwa moja kuwa ndiye alikuwa mkuu wa shule msaidizi.
“From Mazwi secondary school sir ”Patrick akajibu.
“Ohh ! Mazwi!
Patrick akasajiliwa kisha mwalimu yule akatoka nje na kumwita mwanafunzi mmoja na kumuomba ampeleke Patrick katika bweni la Shaaban Robert.Mwanafunzi yule akamsaidia mizigo na kumpeleka katika bweni hilo lililo upande wa juu kabisa wa shule hii.
Pale bwenini akapata kitanda kilichokuwa wazi akaweka mizigo yake.akajilaza kitandani huku akijaribu kuwaza jinsi atakavyoweza kuyakabili maisha mapya ya shuleni pale..Hakuwahi kusoma katika shule ya bweni na hii ilikuwa mara yake ya kwanza.
“lakini Happy yupo atanisaidia kuyazoea maisha ya hapa.Kama yeye mtoto wa kike amezoea kwa nini mimi nishindwe ? Nitazoea tu.Halafu shule hii inaonekana ina wanafunzi washamba sana kwa nini walikuwa wakituangalia vile wakati tumeshuka mchana.Au mimi ninaonekana niko tofauti na wao? akawaza Patrick
Mawazo yake yakastuliwa na sauti ya mwanafunzi mmoja aliyeingia bwenini humo kwa kelele.Akamsogelea Patrick na kumsalimu kisha akaelekea katika kitanda chake kupumzika.

* * * *

Saa kumi na moja jioni Patrick akaamua kuzunguka zunguka maeneo ya hapo shuleni.Ilikuwa ni mwishoni mwa wiki hivyo kulikuwa na pilika pilika nyingi.Ni wanafunzi wachache tu waliokuwamo madarasani jioni hii wakijisomea.
Alipofika katika bwalo la chakula akamuuliza mwanafunzi mmoja yalipo madarasa ya kidato cha tatu .Alitaka kutembelea na kuangalia madarasa atakayo kuwa akisomea.
Yalikuwa ni madarsa yaliyofuatana.Yaani kidato cha tatu A B na C.Yeye alikuwa amepangiwa kusoma kidato cha tatu C.Akayapita madarasa ya A na B akaelekea katika darasa la C .Mlango haukuwa umefungwa akaingia ndani na mara macho yake yakagongana na macho ya Happy .
“Happy !! ..”akaita Patrick kwa mshangao.Hakutegemea kama angemkuta happy mle darasani.
“Patrick ! Naona umeshaanza kuwa mwenyeji" akasema Happy huku akitabasamu
Patrick akacheka.
" niambie unaendeleaje ? umeshaanza kuzoea?Umepangiwa bweni gani?”
Happy akauliza maswali mfululizo huku akifunika vitabu vyake.
“Nimepangiwa bweni la Shaabani Robert na darasa ni hili hili C”
Happy akatoa tabasamu pana sana.
“karibu sana hata mimi ninasoma humu humu.”
“nafurahi sana kufahamu kuwa tutakuwa wote darasani.Vipi mbona uko hapa peke yako?
“Nimeamua tu kuja kukaa huku kwa sababu kule hosteli ninaboreka sana.Mara nyingi hupenda kuja huku kujisomea mwenyewe.sipendi kelele.”
“nimeambiwa kuwa kuna maktaba huku “Patrick akauliza.
“Yes ipo lakini mimi sipendi kwenda huko.Mara nyingi huwa nakuja huku darasani.Sipendi kusoma na watu wengi.Patrick naomba tuwe tukisoma wote” akasema Happy.Patrick akatabasamu kisha akasema.
“Usijali Happy tutasoma wote ”
waliongea mpaka ikafika mida ya saa kumi na mbili Happy akaomba Patrick amsindikize kurudi hosteli kwao.Bila hiyana Patrick akakubali.wakatoka wote darasani wakaanza kupanda kilima kuelekea hosteli ya akina Happy .Kila mwanafunzi waliyekutana naye alikuwa akiwatazama.Patrick akaamua kumuuliza Happy
“Happy mbona kila mtu tukikutana naye anatuangalia sana kwa nini?Toka tumefika mchana naona watu wakitushangaa mno !!
Happy akatabasamu kisha akajibu
“Achana nao Patrick ,Jali mambo yako.Kamwe usiwasikilize wanafunzi wa hapa wana mambo ya kipuuzi sana. wakiona mtu mgeni sijui wanakuwaje. ukitaka kuishi kwa amani mahala hapa jitahidi kufuata kile kilichokuleta yaani masomo”Happy akasema kwa sauti ambayo haikuwa ile yake ya kawaida.Patrick hakutaka kuuliza tena kuhusu suala hilo.
“Patrick kesho jumamosi kuna mnada hapo kijiji cha mbele vipi ungependa kwenda kutembea ?
“Yes ni vizuri kama nikienda ili nianze kuyazoea mazingira”
“Ok nitakupitia basi mida ya saa tano ili tukashinde huko mpaka jioni .Huwa ni pazuri sana.Unajua sku za mwisho wa wiki hapa shuleni panakuwa kimya mno.Halafu kama utakuwa tayari , jumapili tutaenda sehemu moja inaitwa stone beach.Ni pazuri pia.Mi hupenda kwenda kutulia kule siku kama hizi za weekend.” akasema Happy
" usijali Happy tutakwenda huko kote unakotaka twende” akajibu Patrick.
Hatua chache mbele yao wakaliona geti la kuelekea hosteli ya wasichana wakaagana na Patrick akarejea bwenini.
Saa nne na nusu asubuhi siku iliyofuata alikuja mpishi katika bweni alilokuwa akilala Patrick na kuanza kumuulizia.
“wewe ndiye Patrick? akauliza mzee yule wa makamo baada ya Patrick kujitokeza.
“ ndiyo mimi”Patrick akajibu
“Nimeagiziwa na binti mmoja anaitwa Happy kuwa anahitaji kukuona sasa hivi .Panda na barabara utamkuta pale mbele karibu na kanisa anakusubiri.”
“Ok mzee nashukuru”
Mzee yule akaondoka kisha Patrick akavaa viatu vyake akaondoka kuelekea mahala alipoagiziwa na Happy .siku hii alikuwa amependeza vilivyo.alikuwa amevaa kaptura ya jeans rangi nyeupe,juu akavaa fulana nzuri yenye mistari ya kijani na nyeupe halafu akavaa na mkufu wake wa dhahabu uliomfanya avutie zaidi.Chini akavaa raba nzuri nyeupe na soksi nzuri .Mwisho kabisa akajipulizia uturi wenye harufu nzuri .Kwa ujumla alikuwa amependeza sana kijana huyu.Wakati akitoka alisikia baadhi ya wanafunzi waliokuwa hapo bwenini wakifanya usafi wakinong’onezana.
“alaaa kumbe ndo huyu !” akasema mmoja wao
“Du bonge la brother maskini .haelewi “akadakia mwingine.
Patrick hakutilia maanani sana minong’ono ile akawapuuza na kuondoka zake.Alitamani sana kuonana na Happy kwani aliamini ni yeye tu ndiye anayeweza kumfanya akazoea mazingira yale magumu.Tangu amewasili bado hajapata rafiki wa karibu kama Happy .
Kwa mbali alimuona Happy amekaa chini ya mti amejiinamia.Moyo ukafurahi baada ya kumuona tena binti yule mrembo.Kwa mbali tu aliweza kutambua utofauti katika muonekano wa Happy .
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 6
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Nimeagiziwa na binti mmoja anaitwa Happy kuwa anahitaji kukuona sasa hivi .Panda na barabara utamkuta pale mbele karibu na kanisa anakusubiri.”
“Ok mzee nashukuru”
Mzee yule akaondoka kisha Patrick akavaa viatu vyake akaondoka kuelekea mahala alipoagiziwa na Happy .siku hii alikuwa amependeza vilivyo.alikuwa amevaa kaptura ya jeans rangi nyeupe,juu akavaa fulana nzuri yenye mistari ya kijani na nyeupe halafu akavaa na mkufu wake wa dhahabu uliomfanya avutie zaidi.Chini akavaa raba nzuri nyeupe na soksi nzuri .Mwisho kabisa akajipulizia uturi wenye harufu nzuri .Kwa ujumla alikuwa amependeza sana kijana huyu.Wakati akitoka alisikia baadhi ya wanafunzi waliokuwa hapo bwenini wakifanya usafi wakinong’onezana.
“alaaa kumbe ndo huyu !” akasema mmoja wao
“Du bonge la brother maskini .haelewi “akadakia mwingine.
Patrick hakutilia maanani sana minong’ono ile akawapuuza na kuondoka zake.Alitamani sana kuonana na Happy kwani aliamini ni yeye tu ndiye anayeweza kumfanya akazoea mazingira yale magumu.Tangu amewasili bado hajapata rafiki wa karibu kama Happy .
Kwa mbali alimuona Happy amekaa chini ya mti amejiinamia.Moyo ukafurahi baada ya kumuona tena binti yule mrembo.Kwa mbali tu aliweza kutambua utofauti katika muonekano wa Happy

ENDELEA.........................

" Happy mambo vipi ”akasema Patrick
“Poa tu Patrick , mzima? Akasema Happy halafu akainua macho
Patrick akastuka kisha akauliza
“Happy kulikoni mbona macho mekundu na inaonyesha ulikuwa ukilia.Unaumwa?
Happy akanyamaza na kuanza kulia kwa kwikwi.Patrick akajua lazima kuna kitu kimemsibu binti yule.akatoa kitambaa na kumpatia
“Chukua hii futa machozi”
Happy akachukua kitambaa kile na kufuta machozi.
“Niambie Happy kitu gani kimekusibu mpaka ukawa katika hali hii?
“Patrick naona nitashindwa.”
“kwani kuna nini Happy ?.Niambie kama una tatizo ili tuone namna ya kulitatua.”
“Patrick hapa shuleni mimi nina matatizo makubwa. wenzangu wananichukia sana sijui nimewakosea kitu gani.Mara waseme eti mimi ninaringa sana ,wanasema eti ninajidai kwa kuwa familia yangu ina pesa nyingi,eti ninajifanya mtoto wa tajiri.Hiyo ni sababu ambayo imewafanya wanitenge na hakuna mtu anayetaka hata kushirikiana nami kitu chochote.Hata kusoma huwa nasoma peke yangu.Kwa hivi sasa shule nzima wanajua eti mimi nimeathirika na virusi vya ukimwi..Habari hizo zimesambaa kila mahala na hii ndio imenifanya nikose hata rafiki.Mimi silijali hilo kwa sababu ninafahamu mimi mwenyewe kuwa mambo hayo si ya kweli.Hata baadhi ya walimu wanaamini hivyo .Kuna siku walikuja watu wa afya na kuwataka watu wapime afya zao na karibu wanafunzi wote wakapima kasoro mimi.Nilikataa kupima kwa sababu nimekwisha pima toka huko nilikotoka na zaidi ya yote ninajiamini mimi mwenyewe kuwa sina ugonjwa huo wanaosema ninao.Kwa kipindi hicho walichokuja kupima nilikuwa ninasumbuliwa na kifua basi baada ya kukataa kupima afya , ikawadhihirishia watu kuwa ni kweli nina ugonjwa huo.Mimi sioni ajabu kwa sababu hata huko nilikotokea mambo haya yalinikuta na ndiyo sababu kubwa iliyonifanya nihame.Huku nako nikakuta mambo ni kama yale yale .Nilipata taabu mwanzoni lakini ikafika mahala nikazoea.Nimejaribu kuwa wazi kuwa mimi sisumbuliwi na ugonjwa huo wanaodai ninao lakini hakuna anayeniamini na hasa ukichukulia huu mwili wangu jinsi ulivyo basi kila mtu anajua ninaumwa.Namshukuru Mungu kwa sababu kwa sasa nimekwisha pona lakini hakuna mtu anayetaka hata kuchangamana nami.Pale tulipokutana nilikuwa nimetoka tena kufanya vipimo ili kujua kama ugonjwa ule wa kifua ulionisumbua kwa muda mrefu umekwisha kabisa au vipi.na kwa bahati nzuri madaktari wakanithibitishia kuwa tayari nimepona .Wewe mwenyewe jana uliona wanafunzi walivyokuwa wakituangalia wakati nakusindikiza i.wote walikuwa wanakusikitikia wewe.”
Happy akanyamaza na kufuta machozi yaliyokuwa yakitoka.Patrick akawa kimya kabisa kumsikiliza.Kijasho kilikuwa kikimtiririka.Happy akaendelea.
“Kibaya zaidi ni leo asubuhi.Nilikuwa nimeenda kuoga nikasahau kufunga sanduku langu .Niliporudi nikakuta pesa zangu zote karibu laki moja na ishirini na tatu elfu hazipo.Nimejaribu kuuliza lakini hakuna mtu yeyote anayejua zimeenda wapi.Ninaelewa hizi ni njama za wazi za watu wasionipenda.”
Patrick akavuta pumzi ndefu na kumwangalia Happy kwa makini .alimuonea huruma sana binti yule kwa matatizo anayoyapata.Sasa alipata jibu kwa nini wale wanafunzi walikuwa wakimwangalia sana na hata kusemezana wao kwa wao kila walipomuona yuko na Happy .Roho ikamuuma kumuona binti mrembo kama yule akitoa machozi.Ni wazi hakustahili kufanyiwa vile hata kama angekuwa ameathirika kama wanafunzi hao wanavyodai..
“Hawa watu wa namna gani ambao wanawafanya wenzao namna hii?Hivi ndio tunavyofundishwa kuhusu mapendo kwa wenzetu? kama wao waa tabia hizi mimi sijafundishwa namna hii.Wazazi wangu wamenifundisha kuwa na upendo kwa watu wote.Lazima nionyeshe mfano kwa watu hawa na nitaanzia kwa Happy ”Aliwaza Patrick akiwa na fundo la hasira moyoni.
Taratibu akamuinamia Happy na kumshika mikono.akamwangalia usoni kwa sekunde kadhaa kisha akasema.
“Happy usijali ,nyamaza kulia I’m here for you.I’ll be on your side.Hutalia tena.Hata kama dunia nzima itakutenga na kusimama mbali nawe I’ll be there for you.Hata kama ungekuwa na maradhi hayo wanayosema unayo nisingeweza kukutenga.”
Happy akapatwa na furaha ya ghafla baada ya kuambiwa maneno yale akainuka na kumkumbatia Patrick kwa nguvu.
“Thanks very much Patrick.Nadhani ni Mungu kakuleta ili uweze kunipa faraja.Baba alitaka kunihamisha na kunipeleka mbali lakini nilikataa kwa sababu nayapenda mazingira haya ya huku.Napenda sana kuwa katika sehemu tulivu kama hii.sikujua kumbe kuna mtu ana kuja ambaye atakuwa ni faraja yangu.”
Akasema Happy huku machozi yakimtoka.hakuamini kwa mazingira yale kama kuna mtu angeweza kumtamkia maneno ya faraja kama yale.
“Usijali Happy .Hutalia tena.Usijali kuhusu pesa zako kupotea.kama ilikuwa ni njama zao basi wameshindwa.Mimi bado nina kiasi cha kutosha cha pesa nitakugawia na kiasi kitakachobaki tutaendelea kukitumia taratibu.Usijali you are more than a friend to me.To me you are like my sister.”
“Thanks Patrick.You are more than a brother to me”akasema Happy
‘Thanks. vipi kuhusu ile safari yetu ya mnadani bado ipo au ndio umeshaifuta? Patrick akauliza
“Mimi nilikuwa nimeshaifuta kwa sababu hata kama ningeenda huko ningenunua vitu na nini?wamechukua pesa zote.”
“Pole sana. hebu nisubiri kidogo hapa nakuja sasa hivi”
Patrick akamwacha Happy pale na kutembea kwa kasi kurudi bwenini..akafungua sanduku lake kubwa na kutoa bahasha Fulani aliyokuwa ameificha .akaiweka mfukoni akafunga sanduku lake na kuondoka kurudi kule alikomwacha Happy .
“Happy chukua hii ni laki moja na nusu itakusaidia ila kuwa makini sana wasije wakakuibia tena siku nyingine.”akasema Patrick wakati akihesabu pesa toka katika ile bahasha aliyokwenda kuichukua kule bwenini.Happy hakuamini macho yake.hakuamini kama katika dunia hii bado kuna watu wenye moyo wa huruma kama wa Patrick.
“ jamani Patrick Naomba kidogo tu sasa ukinipa hizi zote na wewe je utabakiwa na nini?
“Usijali Happy bado nina akiba ya kutosha”Patrick akajibu
“No Patrick siwezi kuchukua zote.”
“Happy kumbuka ulikuwa ukilia kwa kuibiwa na sasa narudisha kiasi kile kilichokuwa kimeibiwa ili ufute kabisa suala hilo moyoni mwako”
Happy akapokea pesa zile.
“nashindwa hata kupata neno la kukukushukuru litakalokufaa Patrick.Thanks very much “
“you are welcome" Patrick akasema kisha kikapita kimya kifupi.
“Patrick thanks again unajua nilikuwa nawaza sana jinsi ya kumwambia daddy kuwa nimeibiwa kwa sababu si mara ya kwanza namwambia hivyo ananitumia pesa Ila kwa sasa sijui ningesemaje.You are my angel.”akasema Happy
“usihofu kitu Happy muda wowote utakaokuwa na tatizo usisite kunitaarifu.I will help you.”Patrick akasema kwa kujiamini.alijisikia vizuri sana kumsaidia binti yule mwenye matatizo aliyekuwa ametengwa .
Taratibu wakaondoka mahali pale na kuelekea mnadani.

* * * *
Maisha ya Patrick na Happy yaliendelea kama kawaida shuleni malangali.Kila mara walikuwa pamoja.Waliachana tu pale Happy alipokwenda hosteli kwao.Walisoma pamoja na maendeleo yakawa mazuri sana.Happy akawa ni mtu mwenye furaha kila siku .Ni kweli hakulia tena kama Patrick alivyomuahidi.Alizidi kupendeza na kuwa mrembo zaidi.Kwa muda mfupi urafiki wa Patrick na Happy ukawa gumzo pale shuleni.Wapo waliosema kuwa Patrick na Happy ni ndugu,wengine wakadai kuwa ni wapenzi ilimradi kila mtu akasema lake.Chuki dhidi ya Patrick na Happy ikaongezeka.Na kwa sasa ikawa wazi wazi.Maneno yalitamkwa bila kificho .Wengine wakadai eti Patrick anaringa ,wengine wakadai ana majivuno,wengine wakasema kuwa anaringia pesa za Happy wengine wakamwita mwanaume kama binti na majina ya kila aina.Hii ilimfanya Patrick akose rafiki wa karibu ambaye angeweza hata kumweleza matatizo yake .Rafiki yake mkuu alikuwa ni Happy .Si kwamba alipenda hali hii lakini ilijitokeza yenyewe na ikafika mahala akajikuta akiizoea.Alipenda sana kuwa na marafiki wengi lakini angewapata vipi?kila mtu hakuwa tayari kushirikiana naye.
Kwa upande wake Happy naye alikumbana na visa kama alivyokumbana navyo Patrick.Hii haikuwasumbua hata kidogo.Maneno mengi yakasemwa lakini mwisho wa siku ukweli ukabaki pale pale kuwa Patrick na Happy hawawezi kutengana.Maneno ya watu pamoja na visa walivyotendewa vilikuwa ni changamoto kubwa kwao.Siku zote walipeana moyo na ujasiri wa kutokukata tama.Waliongeza juhudi katika masomo na kila mara walionekana kufanya vizuri na kupata alama za juu.Taratibu walimu wakaanza kuwapenda kutokana na juhudi walizozionyesha darasani.Hii ikazidisha chuki miongoni mwa wanafunzi .

*******************

Ilikuwa ni saa sita na robo siku ya jumatano.Darasani hapakuwa na mwalimu kilikuwa ni kipindi cha kujisomea.Happy akatoka na kwenda msalani.Wakati akirejea kwa bahati mbaya akaligonga daftari la mwanafinzi mmoja wa dawati la mbele kabisa na daftari lake likaanguka chini.Happy akaomba samahani na kuinama kuliokota daftari lile.
“Wewe usiguse daftari langu usije na mimi ukaniambukiza magonjwa yako”akasema kwa sauti yule binti aliyeangushiwa daftari lake na Happy .
Happy akapandwa na hasira kali kwa kauli ile.Siku zote alivumilia kashfa za kila aina lakini hii ya leo ilimuuma mno.Wanafunzi wakaanza kucheka kwa kejeli.Kitendo hiki kikamzidishia hasira akainuka na kumzaba kofi yule binti na mara ukazuka ugomvi.
“Apigweeee huyo !!!… anaringa sanaaa…!!!!!!! acheni afundishwe adabu..”yalikuwa ni maneno ya wanafunzi wakishangilia .Wengine waliinuka na kumsaidia yule binti kumpiga Happy .Patrick ambaye alikuwa katikati ya darasa alikishuhudia kitendo kile wazi wazi naye kama ilivyokuwa kwa Happy akapandwa na hasira zisizomithilika.Akapanda juu ya meza na kuruka meza nyingine kama mbili hivi na kufika mahala pale ulipokuwa ukitokea ugomvi.Akaingilia kati na kuwaamua.Wanafunzi wawili wa kiume walipoona Patrick ameingilia kati ugomvi ule nao wakainuka na kuanza kupigana na Patrick.Kelele zikawa nyingi na zikamfikia mwalimu aliyekuwa darasa la karibu ambaye alifika haraka kuona kuna nini akakuta kuna ugomvi mkubwa.Wanafunzi walipomwona mwalimu wakakimbia kila mmoja katika kiti chake kasoro Patrick na Happy .Patrick alikuwa amevimba kwa hasira.
“haya wote mliokuwa mnagombana pita mbele”
Yule binti aliyekuwa akigombana na Happy akasimama na kupita mbele.
“Si huyu peke yake nimewaona wengi tu piteni wote mliokuwa hapa mnagombana”
Akasema mwalimu yule kwa ukali na kuwafanya wanafunzi waogope na kuanza kupita mbele .wakachukuliwa wote na kupelekwa kwa mwalimu wa darasa.
“haya nipeni sababu za kugombana”Akasema mwalimu yule mkali
Yule binti aliyekuwa akigombana na Happy akasema
“Ni huyu hapa ndiye mkorofi.ameangusha daftari langu makusudi kabisa badala ya kuliokota akaanza kunitolea maneno ya kashfa.Mimi nikamwambia kama hataki kuliokota nakuja kushtaki kwa mwalimu yeye akaninasa kibao na kusema kuwa nenda kaseme kwa huyo mwalimu wako tuone atanifanya nini.Muda huo huo huyu hapa sijui ndugu yake akainuka naye akaja wakaanza kunichangia ndio hawa wenzangu wakaja kuniokoa.”Akadanganya yule binti
Mwalimu yule akawaangalia Patrick na Happy kwa macho makali.Akawageukia wale wanafunzi wengine watano.
“Eti nyie ni kweli haya maneno aliyoyasema mwenzenu?
“kweli kabisa mwalimu” wakajibu
Haya nyie wote nendeni nitabaki na hawa watukutu wanaojifanya matajiri wa shule.”
Wanafunzi wale wengine wakaondoka na kuwaacha Patrick na Happy katika mikono ya mwalimu ambaye alikuwa ameshika fimbo kubwa .
“ leo mtanieleza nyie watoto kwa nini mnasababisha ugomvi darasani?Kwanza wewe binti hebu nyoosha mkono wako hapa”
Happy huku akilia akanyoosha mkono ili mwalimu aanze kumchapa.
“No ! Happy .Usinyooshe.”Patrick akapiga kelele na kwenda kusimama mbele ya Happy .
“ kumbe wewe ndiye unayemfundisha kiburi mwenzako.leo utanieleza . haya lala chini haraka.”akafoka mwalimu
“Hapana mwalimu silali”Patrick akajibu kwa hasira ..Happy machozi yalikuwa yakimtoka.
“Unaonekana una kiburi sana wewe."akadakia mwalimu mwingine aliyetokea ghafla..
“Wewe unajifanya tajiri na vihela vyako leo utaimba “Akasema mwingine huku akisogea akiwa na fimbo mbili mkononi
“ walimu hali hii mpaka lini? Uonevu huu mpaka lini ? Kwa nini hamtaki kutupa na sisi nafasi ya kujieleza? Patrick akasema
“Unajifanya kujua sheria ? nakwambia leo utaona”mwalimu yule akamsogelea na kutaka kumchapa Patrick mgongoni.Patrick akadaka Fimbo.
“Unataka tupigane ? ”Mwalimu yule akatupa fimbo na kukunja ngumi.
Ofisi ikageuka kituko.Mara mkuu wa shule msaidizi akapita akasikia kelele ofisini
“wamefanya nini hawa? akauliza
“wamepigana na wenzao darasani na hawataki kuadhibiwa.”
“Siyo hivyo mwalimu.Huu ni uonevu.Huyu mwalimu kapewa maneno ya uongo naye kwa chuki zake anaamua kutuadhibu bila kosa.Chuki za wazi wazi zitakwisha lini?.Happy ananyanyaswa na shule nzima wanasema eti ana ukimwi.Hata kama angekuwa nao hivi ndivyo wanafunzi wanavyofundishwa kuishi na wenzao wagonjwa?”Patrick akaongea maneno mfululizo kwa hasira.
“Kwa hiyo mmepigana au hamjapigana" akauliza mkuu wa shule msaidizi
“Ukweli ni kwamba Happy alikuwa akitoka msalani na kwa bahati mbaya akaligonga daftari la mwenzake likaanguka chini.Akainama ili aliokote lakini wakati anataka kuliokota yule binti akasema aache daftari lake asije akamuambukiza maradhi yake.Happy akakasirika na kumnasa kibao lakini halikuwa kusudio lake.Hata kama ungekuwa ni wewe nafikiri usingevumilia.Ungejisikiaje kama huyu angekuwa mwanao na unasikia anaambiwa maneno kama yale ?
Mwalimu yule msaidizi akakaa kimya kisha akawaamuru Happy na Patrick wamfuate ofisini kwake
“Enhee vijana hebu niambieni nini kilichotokea”akasema mwalimu baada ya Patrick na Happy kufika katika ofisi yake.Happy ndiye aliyeanza kueleza
" mimi nilitoka msalani , kwa bahati mbaya nikaligonga daftari la Mwantumu likaanguka chini.Nikamuomba samahani nikainama ili niliokote.Wakati nikiliokota akasimama na kuniambia “acha daftari langu usije ukaniambukiza magonjwa yako”.Kwa kweli mwalimu kauli hii mimi iliniuma sana hasa ukizingatia kuwa hapa shuleni mimi nimekuwa nikitengwa na wanafunzi wanadai eti nimeathirika na ugonjwa wa ukimwi.Mwalimu hata kama ningekuwa na maradhi hayo wanayodai kwa nini basi wanitenge?Kwanini waninyayapae namna hii?Na kwa nini wanizushie kitu ambacho si cha kweli?Inauma sana mwalimu.Kila mwanafunzi ananichukia hapa shuleni na.Kibaya zaidi hata walimu nao wameungana na wanafunzi katika kuoyesha chuki zao za wazi kwangu.”
Mwalimu akakaa kimya na kutafakari kisha akasema.
“halafu kuna kitu nataka kuwauliza..Kuna tetesi nimezisikia kuwa nyie wawili ni wapenzi.Ni kweli?
Wote wawili wakakaa kimya .Hili lilikuwa ni swali ambalo hawakukulitegemea kabisa..Walikaa kimya kwa sekunde kadhaa bila kujibu .
“Mbona hamjibu ina maana ni kweli?”Akasema mwalimu kwa ukali.Happy alikuwa akitetemeka mwili.Ni kweli hajawahi kuwa na mpenzi mpaka hapa alipo Hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuambiwa kuwa ana mpenzi.Patrick yeye alikaa kimya akitafakari ajibu nini.
“Mwalimu sisi si wapenzi kama ulivyosikia .Sisi ni marafiki na muda wote tuko pamoja Kitu kinacho fanya watu wahisi kuwa sisi ni wapenzi ni kwa vile tuko karibu karibu sana.Tunasaidiana karibu katika kila jambo.Tunaishi kama ndugu.Maendeleo yetu ni mazuri.Mwalimu hizo ni chuki tu za watu wasiotutakia mema.Naomba uniamini kuwa sisi si wapenzi kama watu wanavyodhani..”Patrick akasema.Happy machozi yalikuwa yakimtoka.Mbele ya mwalimu mkuu msaidizi .
“haya nendeni nitakaa kikao na walimu ili kujadili suala lenu.”
Happy na Patrick wakatoka ofisini huku Happy akilia.Patrick akatoa kitambaa mfukoni na kumfuta machozi.
“Nyamaza Happy kila kitu kitakuwa sawa,Usilie.”
Moja kwa moja wakaelekea darasani.Walipoingia tu darasani minong’ono ikaanza.Happy akashindwa kuvumilia akachukua vitabu vyake na kutoka darasani macho yakiwa yamefunikwa na machozi.Patrick naye akatoka na kumkimbilia .
“Happy please hebu nyamaza.Unajua ni kwa kiasi gani unawapa ushindi wale wote wasiokupenda.tayari wanaona wamekwisha kushinda.Be strong Happy .Pambana na utashinda.I’m on your side.i’ll fight for you”Patrick akasema kwa msisitizo.
Happy akafuta machozi akatabasamu na kusema.
“Ahsante sana Patrick .Nafahamu kuwa uko pamoja na mimi.Naomba kwa sasa nikapumzike tutaonana baadae.Nasikia kichwa kinaniuma .”
Patrick akamtazama Happy usoni kisha akasema.
“Ok Happy nenda kapumzike tutaonana baadae.”
Wakaacha na Patrick akarejea darasani.Ilikuwa ni siku ndefu na ngumu kwa Patrick.Kila mara alikuwa akitafakari juu ya tukio la leo.Ni tukio ambalo lilimuuma sana na kumfanya afikie hatua ya kupigana.Toka amezaliwa hajawahi kupigana na mtu yeyote.Hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kupigana .Ilimuuma sana.
“lakini sikuwa na jinsi.Ni lazima nimtetee Happy .Kwa gharama yoyote ile.Kwa nini binti yule anyanyasike bila kosa?Nitahakikisha katika uwepo wangu hapa shuleni ninamsaidia kwa kila hali.Lazima siku moja heshima itapatikana..” akawaza Patrick huku ameinama chini .Mawazo yalikuwa yakija na kupita kwa kasi.Mara akakumbuka kitu.Akakumbuka swali waliloulizwa na mkuu wa shule msaidizi.
“halafu kuna kitu nataka kuwauliza..Kuna tetsi nimezisikia kuwa nyie wawili ni wapenzi.Ni kweli? Patrick akatabasamu alipoyakumbuaka maneno haya ya mwalimu mkuu
“Kumbe siku zote watu wanahisi kuwa sisi ni wapenzi .Nadhani hii ni mojawapo ya sababu inayopelekea watu kuwa na chuki zaidi kwetu kwani Happy ni binti mrembo kupita maelezo.Na kadiri siku zinavyozidi kusonga anazidi kupendeza na kuwa kama malaika.Sasa kama wao hawaupendi ukaribu huu wangu na Happy basi wameumia .Tutaendelea kuwa karibu zaidi ya hapa.Lakini kuna dalili zozote za mapenzi kati yetu?.Hapana. Nadhani tunapenda kama marafiki wa kawaida .Sijui ya huko mbele kwa sababu naona urafiki wetu umekuwa mkubwa sana na unazidi kukomaa kadiri siku zinavyosonga mbele.”.
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 7
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“lakini sikuwa na jinsi.Ni lazima nimtetee Happy .Kwa gharama yoyote ile.Kwa nini binti yule anyanyasike bila kosa?Nitahakikisha katika uwepo wangu hapa shuleni ninamsaidia kwa kila hali.Lazima siku moja heshima itapatikana..” akawaza Patrick huku ameinama chini .Mawazo yalikuwa yakija na kupita kwa kasi.Mara akakumbuka kitu.Akakumbuka swali waliloulizwa na mkuu wa shule msaidizi.
“halafu kuna kitu nataka kuwauliza..Kuna tetsi nimezisikia kuwa nyie wawili ni wapenzi.Ni kweli? Patrick akatabasamu alipoyakumbuaka maneno haya ya mwalimu mkuu
“Kumbe siku zote watu wanahisi kuwa sisi ni wapenzi .Nadhani hii ni mojawapo ya sababu inayopelekea watu kuwa na chuki zaidi kwetu kwani Happy ni binti mrembo kupita maelezo.Na kadiri siku zinavyozidi kusonga anazidi kupendeza na kuwa kama malaika.Sasa kama wao hawaupendi ukaribu huu wangu na Happy basi wameumia .Tutaendelea kuwa karibu zaidi ya hapa.Lakini kuna dalili zozote za mapenzi kati yetu?.Hapana. Nadhani tunapenda kama marafiki wa kawaida .Sijui ya huko mbele kwa sababu naona urafiki wetu umekuwa mkubwa sana na unazidi kukomaa kadiri siku zinavyosonga mbele.”.

ENDELEA……………………..

Kwa upande wake Happy baada ya kutoka darasani mchana ule akaenda mpaka katika hosteli yao akajitupa kitandani na kuanza kutafakari.juu ya tukio zima la leo.
“sikuwahi hata siku moja kuwaza kuwa nitakuja kugombana na mtu .Nimevumilia mambo mengi lakini hii ya leo ilivuka mipaka..Kwa nini wananichukia namna hii?Mbona mimi sina tabia ya maringo kama wanavyodai?Mbona sijivuni japokuwa wazazi wangu wana uwezo?Nafikiri ni kwa sababu wengi hawaupendi ukaribu wangu na Patrick.Wasichana wenzangu wana chuki hawapendi sana jambo hili.Nadhani hii ni sababu kubwa ya kuwa na visa vya wazi wazi.Kumbe tayari wamepeleka maneno hadi kwa walimu kuwa mimi na Patrick ni wapenzi.Mhh jamani!!.Maskini Patrick anaonewa bure kaka wa watu.Wangejua jinsi alivyo wala wasingezusha tuhuma hizo.Lakini hata kama ingekuwa ni kweli kwani wao inawahusu nini?Wivu wao unawasumbua tu..Nasema Patrick simuachi na nitazidi kuwa rafiki yake wa karibu.Patrick ni mtu pekee ambaye amenifikisha hapa nilipo sasa.Nilikwisha kata tamaa kabisa hata ya kuendelea kusoma hapa lakini ni yeye aliyenipa moyo na kunisaidia katika kila kitu .Amenipa msaada mkubwa kimasomo.Ni yeye tu ambaye amekuwa nami siku zote pale ambapo jamii nzima imenikataa.Potelea mbali watakavyosema na waseme.Mimi sijali .Mbona wao wana wanaume kila kona mimi siwafuatiliii mambo yao .Kwa nini basi wao wafuatilie ya kwangu.?.Lakini hata kama ingekuwa ni kweli ,kuna ubaya wowote mimi na Patrick kuwa wapenzi?Nadhani hata kama nikiamua kuwa na mpenzi basi ni wazi ni lazima atakuwa ni Patrick .Kwani ni yeye pekee mpaka sasa hivi ambaye amekuwa ni mtu wangu wa muhimu sana.Ni yeye pekee ambaye anaweza kunikosesha usingizi kwa kutomuona.Je ni kweli kuwa hii ni dalili ya kuchipua kwa penzi kati yetu? Inaweza kuwa kweli kwa sababu sijawahi kuwa karibu na mvulana yeyote zaidi ya Patrick.Ni yeye ambaye amenifundisha nini maana ya kuwa rafiki wa dhati.nadhani hizi ni dalli njema.lakini hata kama nikiamua kumchagua Patrick kuwa mpenzi wangu nitamwambiaje?Mhh ! ngoja niachane na haya mambo huu si wakati wake." akawaza happy.

* * * *

Kengele ya dharura ikagongwa ikiashiria kuwa na jambo ambalo si la kawaida.Wanafunzi wote wakatoka darasani kwa haraka kama inavyotakiwa mara tu inaposikika kengele hii.Kwa haraka haraka mistari ikapangwa na huku kila mwanafunzi akiwa kimya akisubiri kusikia ni nini kitakachojiri.Walimu wote walikuwa wamejipanga na mara akatokea mkuu wa shule.Wanafunzi mioyo ikawaenda mbio kwani ni nadra sana kwa mkuu wa shule kuonekana katika eneo hilo la mkusanyiko.Mara zote anapoonekana eneo hilo huwa ni kwa sababu maalum tu.
“Habari za asubuhi wanafunzi” Akasalimu wanafunzi.
“Nzuri shikamoo mwalimu”
“Wanafunzi nimesimama mbele yenu asubuhi hii ili kuzungumzia mustakabali mzima wa maendeleo ya shule yetu.kwa siku za karibuni shule yetu imekuwa na mambo ambayo katu hayafurahishi na ambayo yanaenda kinyume na maadili mazima ya mwanafunzi.
Kwanza kabisa kumekuwa na vitendo vya ubaguzi.Wanafunzi mmeanza kubaguana.Mnawanyanyasa na kuwabagua wenzenu ambao ni wagonjwa.Hivi ndivyo mnavyofundishwa na wazazi wenu majumbani? Kuna binti mmoja nimepata malalamiko yake kuwa yeye ametengwa na wanafunzi wenzake eti kisa ni mgonjwa.Hii ni aibu kubwa kwa shule yetu..Sasa ninasema hivi kuanzia sasa wewe ukibainika kuwa unafanya kitendo chochote cha kibaguzi adhabu yake ni kufukuzwa shule.Sintataka kukuona tena katika shule yangu.Kuweni makini sana na hilo.Jambo la pili ninalotaka kulizungumza leo ni nidhamu .Kumekuwa na uvunjaji mkubwa sana wa sheria za shule.Imefikia mahali sasa ambapo mwanafunzi anaweza akamgomea hata mwalimu .Mwanafunzi anaweza akafanya kitu chochote anachotaka bila kuogopa.Hivi kweli wewe mwanafunzi unaweza ukabishana na kutaka kupigana na malimu wako?mwalimu wako ni sawa na mzazi wako hapa shuleni.Nasema kuwa kuanzia sasa sheria na taratibu za shule zitafuatwa kwa ukaribu sana.Endapo utakwenda nje ya taratibu basi tutakushughulikia kikamilifu.Kwa sasa naomba nitakaowataja wapiti mbele haraka: Patrick Charles,Happy kibaho.Mwantumu ramadhani.Pius augustinie,Pili Juma,Maria asey,Steven amanuli na Benson Chiteu.”
Wanafunzi wale walioitwa ,wakajipanga mbele ya alipokuwa amesimama mkuu wa shule,halafu akaendelea.
“Hawa mnaowaona mbele yenu mnajua wamefanya nini? Akauliza mkuu wa shule.wanafunzi wote wakawa kimya .Hakuna mtu aliyethubutu kusema kitu ingaa walkuwa wakifahamu juu ya ugomvi uliotokea.
“Wanafunzi hawa walioko mbele yenu walivunja sheria za shule kwa kugombana darasani.Baada ya kukutwa wkipigana mwalimu aliyewakamata akawapeleka kwa mwalimu wa darasa Patrick na mwenzake Happy ambao ndio kiini cha ugomvi wakagoma kuadhibiwa.Kibaya zaidi ni kwamba Patrick alikuwa tayari kupigana hata na mwalimu wake wa darasa.Sijui jeuri hii mnaitoa wapi ninyi watoto..Mwanafunzi unataka kupigana na mwalimu wako kweli? Hii tabia mbaya ambayo katu haitavumiliwa katika shule yetu.Kingine ni kwamba Patrick na Happy ambao wote ni wanafunzi wa darasa moja wamekuwa wakijihusisha na masuala ya kimapenzi wakiwa shuleni kitu ambacho ni kinyume kabisa na sheria na taratibu za shule.Bodi ya shule imekaa na imeamua yafuatayo.Moja wanafunzi Mwantumu Ramadhani,Pius Augustine,Pili Juma,Maria asey ,steve amanuli,na Benson chiteu watapata adhabu ya kung’oa kila mmoja visiki vitatu kwa muda wa siku sita kuanzia leo.Wanapata adhabu hii kwa kosa la kupigana darasani.Hili ni fundisho kwa wengine .Wanafunzi Patrick charles na Happy Kibaho wao wanasimamishwa masomo kwa muda wa mwezi mmoja.Hii ni kwa sababu wamesababisha ugomvi ,wamapigana darsani,wakagomea adhabu ya mwalimu na zaidi ya yote wanajihusisha na mahusiano ya kimapenzi wakiwa shuleni.Adhabu hii ni fundisho kwa wanafunzi wengine.Ninasema kuwa kuanzia sasa tutakuwa wakali mno kwa yeyote yule ambaye atajaribu kwa namna yoyote kuvunja sheria za shule.Nasema ole wenu ,ole wenu.” Mkuu wa shule akamaliza na kuondoka zake.mwalimu wa zamu akawatawanyisha wanafunzi warudi madarasani.Sehemu kubwa ya wanafunzi walkikuwa wakifurahia adhabu ile waliyoipata Patrick na Happy .Kwao uilikuwa ni alama ya ushindi mkubwa.Katika darasa la akina Patrick ilikuwa ni kama sherehe.Wanafuzi walikuwa wakipongezana.
Happy macho yalijaa machozi.Alikuwa akilia.Hakuamini kuwa kosa lille lingepelekea yeye na Patrick wasimamishwe masomo.Hakuwahi kuota kama iko siku atakuja kusimamishwa masomo.Mbaya zaidi aliumia moyo kwa uongo wa wazi kabisa .Ni wazi ulikuwa ni ukandamizaji mkubwa.Zilikuwa ni chuki za wazi .Patrick alikuwa katika hali ya mstuko kutokana na adhabu ile ambayo kwa kiasi kikubwa haikuwa ya haki.Ulikuwa ni uonevu mkubwa.Walikuwa wamesingiziwa uongo mkubwa .Ilimuuma Patrick kwa kiasi kikubwa lakini hakuwa na la kufanya .tayari maamuzi yamekwisha fanywa na kilichobakia ni utekelezaji.Kwa muda huu mfupi shule hii ilikuwa imeanza kumchosha.Taratibu akamsogelea Happy na kumshika mkono.Akatoa kitambaa mfukoni na kumfuta machozi .
“Happy be strong.Najua inauma sana lakini hatuna jinsi.Tusiwape faida maadui zetu.Wanapotuona tuko na huzuni ni furaha kwao.Let us act kama vile hakuna chochote kilichotokea.

* * * *

“Patrick ninasikia uchungu sana ..Kusingiziwa kitu ambacho sijakifanya inauma mno .Inaniuma sana Patrick”Happy akashindwa kuvumilia akaanza kulia .Ilikuwa ni majira ya saa kumi na moja za jioni walipokutana katika hoteli moja kijijini baada ya kuachana mchana na kila mmoja akaenda kupumzika na kutuliza akili.Happy macho yalikuwa yamemvimba na mekundu kwa kulia..
“Kinachoniuma zaidi ni wewe kusimamishwa masomo.wewe hukustahili kwa namna yoyote ile kuipata adhabu hii.Mimi ndio chanzo cha haya yote.Mimi ndiye niliyekusababishia matatizo haya .Ni bora ningesimamishwa masomo peke yangu.Nasikitika sana Patrick .Naomba unisamehe kwa hilo.Haikuwa adhma yangu na wewe uingie katika matatizo haya .Najua hustahili adhabu hii………………….” Akasema Happy huku machozi yakimtoka lakiniPatrick akamzuia na kusema
“Shhhhhhhhhhhhhhhhhhhh………….”Patrick akamfumba Happy mdomo kwa kidole.
“Happy usiseme hivyo.Ninafurahi kupata adhabu hii .Ninastahili.Ulikuwa ni wajibu wangu mimi kukutetea.Nimetimiza wajibu wangu.Kumbuka niliahidi kuwa nawe katika kila jambo.Niliahidi kupambana na yeyote yule ambaye angekufanya ulie.Nimefanya nilivyopaswa kufanya..Usijilaumu Happy ninastahili adhabu hii .”Parick akasema kwa kujiamini.Akamuangalia happy kwa makini na kusema
“Happy si hapa duniani tu hata nikiwa Mbinguni sintavumilia kuona mtu yeyote akikusumbua.Nitapambana naye.”
Kwa mara ya kwanza Happy akacheka kwa kauli ile ya Patrick..Patrick akatabasamu kwa kuifanya sura ya Happy ikajaa tabasamu tena.
“ Umeanza vituko vyako.Mbinguni hakuna uonevu wa namna hii” akasema Happy huku akicheka
“nimesema hivyo kukuthibitishia kwamba sintakuwa tayari kuona mtu yeyote yule akikunyanyasa Happy..” akasema patrick na kumfanya Happy atabasamu tena
“Happy hii ni vita na sisi ni wapiganaji. kuna msemo wa kiingereza unaosema winners never quit.Na sisi ndio washindi hivyo tusikate tamaa.Kukata tamaa ni kuwapa ushindi wale wote wasiotupenda,wasiotutakia mema.Wao wanapamba na sisi lakini sisi tupambane na muda.tumeelewana?”
“sawa Patrick nimekuelwa.nashukuru sana Patrick sijui hata nipate neno gani la kukushukuru kwa jinsi ulvyojitoa mhanga juu yangu.Sidhani kama kuna mwanaume ambaye anaweza kufanya haya uliyoyafanya kwangu.Kama wapo basi ni wachache mno.”
Patrick akatabasamu na kusema...
“Happy utaanzaje kuwaeleza wazazi wako juu ya tukio hili mpaka wakakuelewa.? Manake kwa mujibu wa barua zilivyoandikwa za kuwapelekea wazazi mhh ni hatari tupu.”
Happy akakaa kimya kwa muda kisha akasema.
“Patrick hilo suala linaniumiza kichwa kupita kiasi..unajua baba yangu ananiamini sana na hajawahi kusikia sifa yangu mbaya hata siku moja .Siku zote nimekuwa mfano hata kwa wenzangu , leo akisikia nimesimamishwa masomo mhhh !! sidhani kama kutakuwa na amani nyumbani.Kuna hatari akakataa hata kunipokea kwa jinsi baba yangu alivyo mkali.Nilikuwa nafikiria niende kujificha kwa shangazi yangu Morogoro mpaka adhabu itakapokwisha.Shangazi yangu ni mwelewa na nina imani nikimwelezea atanielewa.Sitaki baba yangu afahamu kuhusu suala hili.Akijua tu nimekwisha.Wewe je umepanga nini? Patrick akafikiri kidogo na kusema
“mimi sina tofauti na wewe hata kidogo.Mzee wangu hatavumilia akisikia nimesimamishwa masomo.Hata mimi nilikuwa ninafikiria niende mahala nikatulie mpaka adhabu hii itakapoisha.Mwezi mmoja si mrefu.”
Kimya kikapita Patrick ambaye alikuwa ameinama akiwaza akainua kichwa na kusema.
“Happy kuna jambo nimelifikiria.Kwa kuwa sisi sote tuna wazo moja la kutotaka kuzifahamisha familia zetu juu ya adhabu hii tuliyopata ,kwani hata kama ukienda kwa shangazi yako anaweza akamweleza tu mzee wako na hapo ndipo itakuwa mbaya zaidi. kama ni hivyo kwa nini basi tusitafute mahala tukaenda kukaa kwa muda wa huo mwezi mzima mahala ambako hakuna mtu anayetujua,na tutakaa kwa raha mstarehe huku tukipata nafasi ya kutosha ya kusoma hadi muda wa adhabu utakapoisha?
Happy akatabasamu lile tabasamu lake adimu sana.
“That’s a good idea Patrick.Wewe una akili sana.Ni wazo zuri Patrick .Sasa ni wapi ambako unafikiri tunaweza kwenda kukaa kwa muda huu wote bila ya kufahamika? Akauliza Happy na Patrick akakaa kimya kidogo akafikiri kisha akasema
“Umewahi kwenda Bagamoyo?”Patrick akauliza.
“hapana sijafika huko”
“Basi ninafikiria twende huko.Kule tutapumzika vya kutosha.Hakuna mtu yeyote anayetufahamu.Tutakaa kwa raha mustarehe.Tutapata nafasi nzuri ya kujisomea.Tutatembelea sehemu mbali mbali za kihistoria.Tutajifunza mambo mengi sana tukiwa kule.Usijali kuhusu gharama bado nina akiba ya kutosha ya pesa na wala hatutapata shida kwa muda kwa huo wote wa mwezi mmoja.Nafikiri hii itatusaidia sana kutoka nje ya ulimwengu huu wa watu wasiokuwa na upendo hata chembe”
Furaha ya wazi ikajidhihirisha usoni mwa Happy .Hakuwa amewaza jambo kama lile hapo kabla.Huzuni yote aliyokuwa nayo ikayeyuka ghafla.
“ Patrick nashindwa hata nisemeje.You are my Hero.Toka nimefahamiana na wewe maisha yangu ytamekuwa na furaha sana.Najihisi niko slama muda wote ukiwa pembeni yangu.Nafurahi kwa kuwa najua niko na rafiki anayeyenijali na kunithamini.Sina kitu cha kukulipa Patrick kwa wema wako huu ”akasema Happy.Patrick akatabasamu.
“ Sifanyi hivi kwa kuhitaji malipo Happy.Ninafanya hivi kwa sababu moyo wangu umenituma” akasema Patrick.Walijhadiliana mambo mengi hadi ilipotimu saa moja za jioni wakaondoka kwa ajili ya kwenda kujiandaa na safari ya kesho yake ya kuelekea Bagamoyo
Ulikuwa ni usiku mrefu sana ambao Happy hakuwahi kuupata hapo kabla.Alitamani asubuhi ifike haraka ili aweze kuondoka hapa shuleni.Tayari alikwisha maliza kufunga baadhi ya vitu vyake muhimu ambavyo angevihitaji katika safari yake ya kuelekea Bagamoyo.Vingine vilivyobaki akavikabidhi kwa mkuu wa hosteli.Wanafunzi wenzake walikuwa wakimshangaa sana kwa hali aliyokuwa nayo.Badala ya kuwa na huzuni kwa kusimamishwa masomo yeye alikuwa na tabasamu muda wote.
“Me and Patrick together in bagamoyo” Neno hili lilijirudia rudia kichwani mwake mara nyingi.
“Nashukuru nimepata nafasi ya kuwa na Patrick peke yangu kwa mwezi mzima..Walau nitajitenga na karaha za shule hii kwa muda.Nafikiri baada ya kurudi nitakuwa na mabadiliko makubwa.Safari hii ya Bagamoyo nina imani itanisaidia sana kisaikolojia.Nitakuwa mtu mpya tena.”Aliwaza.
kwa upande wake Patrick alikuwa akifikiria jinsi atakavyomaliza mwezi mzima akiwa na Happy . “Ni vipi ikija kugundulika kuwa kwa mwezi mzima tulikuwa tumejificha Bagamoyo?Hii itadhihirisha wazi kuwa kuna kitu kinaendelea baina yetu.Lakini potelea mbali hata kama ikigundulika siogopi tena .na hata kama tukiwa wapenzi hakuna mtu anayehusika katika kuamua masuala ya maisha yetu .”Akawaza Patrick.

* * * *

Kengele ya mlangoni ikalia na kumwamsha Patrick toka katika usingizi mzito.Taratibu akainuka na kwenda kuufungua mlango.Alikuwa ni Happy akiwa ndani ya tabasamu pana.Ni siku yao ya kwanza katika mji wa Bagamoyo.Walifika jioni ya siku iilyotangulia na kupanga vyumba viwili katika nyumba ya kulala wageni yenye hadhi ya kawaida lakini yenye ulinzi wa kutosha na huduma nzuri.
“Mhh ! Patrick amka basi uoge tunywe chai .Nimeenda kununua chai katika mgahawa wa mama mmoja hapo jirani.Kwa kuwa tutakuwepo hapa Bagamoyo kwa muda mrefu amenipa chupa ya chai na baadhi ya vyombo ambavyo tutakuwa tukitumia katika muda wote tutakaokuwepo hapa ”akasema Happy .
“ Happy kumbe umeshaamka !Ahsante kwa kuniamsha nilikuwa nimeshajisahau kabisa.” Patrick akasema huku akijiinuataratibu pale kitandani.
“Nimekwisha amka kitambo Patrick..Jiandae ninakusubiri tunywe chai ” akasema Happy.Patrick akaelekea bafuni akaoga na kisha wakapata kifungua kinywa.
Baada ya kupata chai wakatoka na kuanza kuzunguka katika mji wa kihistoria wakifurahia mandhari yake .Walizunguka sana na mchana wakaenda kupata chakula katika mgahawa uliomilikiwa na mama mmoja wa makamo.Walimuomba mama yule awe akiwatengenezea chakula kwa muda wote watakaokuwa pale Bagamoyo.Mama yule akakubali kuwahudumia bila matatizo.Kisha pata chakula wakarudi hotelini kupumzika hadi saa kumi jioni halafu wakaanza kusoma.
“Happy tunatakiwa tuutumie muda wetu mwingi hapa Bagamoyo kwa ajili ya kusoma ili kuwa sawa na wenzetu waliobaki shuleni .Tutakaporudi shuleni tutakuwa tunakaribia kipindi cha mitihani na lengo langu mimi ni sisi kufanya vizuri zaidi ili wale wote ambao wanatuonea wivu waone aibu.”
“Usijali Patrick nina imani tutasoma na tutafanya vizuri.”akajibu Happy .
Saa mbili usiku wakaenda kupata chakula cha usiku kisha wakarejea tena kusoma hadi saa tano za usiku halafu kila mmoja akaenda kulala.Hii ilikuwa ndiyo ratiba yao kubwa kila siku.Jumamosi na jumapili walizitumia kutembelea sehemu mbali mbali za kihistoria hapo Bagamoyo.
Ilikuwa ni jumamosi angavu .Kijua kilikuwa kikali .Ni siku ya ishirini tangu wamewasili Bagamoyo. Saa sita mchana iliwakuta Patrick na Happy katika sehemu moja maarufu sana hapa Bagamoyo.Ni Patrick ndiye aliyeweka msisitizo mkubwa kuwa ni lazima wafike mahali hapa kabla hawajarudi shuleni.Hapa ni sehemu inayojulikana kama kaburi la wapendanao.Sehemu hii ni sehemu maarufu sana na watu wengi hupenda kwenda mahali hapa wakiwa na wapenzi wao na kuwekeana ahadi mbali mbali mbali katika safari nzima ya mapenzi hasa kutokana na historia ya watu hao waliozikwa hapo.
“Happy hii sehemu ndiyo inaitwa kaburi la wapendanao.Waliozikwa hapa inasemekana ni watu waliokuwa wamependana kwa dhati .”
Happy akatabasamu ,na huku akiogopa ogopa.
Patrick akamsogelea Happy akamsika mikono yote miwili kisha akamwangalia machoni
“Happy toka tumekuja Bagamoyo tumetembelea sehemu mbali mbali za kihistoria.Tumejifunza mambo mengi.Hii nilitaka iwe ni sehemu ya mwisho kwa sisi kutembelea tukiwa hapa Bagamoyo.” Akanyamaza kidogo kisha akaendelea
“Nina sababu kubwa ya kuamua kuja eneo hili.Happy waliolala hapa chini ni watu ambao inasemekana upendo wao ulikuwa wa kweli.Hii ndio sababu kubwa ambayo watu wengi na hasa wapenzi hupenda kuja mahali hapa na kuwekeana ahadi mbali mbali katika safari yao nzima ya kimapenzi.Nadhani utajiuliza kwamba na sisi je nini kilichotuleta hapa? Happy nimeamua kukuleta hapa leo hii ili niweze kudhihirisha jinsi gani ninavyokupenda.Nakupenda sana Happy .Toka tulipokutana na kuwa marafiki niliona ishara na kuamini kuwa wewe ndiwe pekee uliyeumbwa kwa ajili yangu.Tafadhali Happy naomba unikubalie ombi langu .Naomba uwe mpenzi wangu.Nakuahidi mbele ya watu waliolala hapa chini kwamba siku zote nitakupenda ,nitakujali na kukuthamini hadi kifo kitakapotutenganisha.Hata siku moja sintakutoa machozi” akasema Patrick akimtazama Happy usoni huku ameishika mikono yake
Taratibu Happy akaiachia mikono ya Patrick,akiwa kama vile mtu aliyepigwa na bumbuwazi.Akamtumbulia macho Patrick kana kwamba ni kwa mara ya kwanza kumuona.Moyo ukamwenda mbio kijasho kikamtiririka.Akafumbua mdomo kutaka kusema kitu lakini akajikuta anashindwa.Patrick ambaye leo hii alikuwa na ujasiri wa aina yake akamsogelea ,akamshika mkono.,akamwangalia usoni.
“Happy I’m sorry.Sikutegemea kama ningekuudhi.naomba vile vile ufahamu kuwa sina lengo baya na wewe,sina lengo la kukuharibia masomo au maisha yako.Naheshimu ndoto zako ,naheshimu maisha yako na ninakuheshimu wewe pia.Natambua kuwa una ndoto zako nyingi siku za usoni na hata mimi nina ndoto zangu pia na ambazo ni lazima nizitimize na moja kati ya ndoto zangu kubwa ni kuwa na wewe.You are my dream Happy .Lakini naona kama vile nimekukwaza na kauli yangu hivyo naomba usahau.Just pretend I didn’t say anything.Naomba kauli yangu hii ya leo isije ikavuruga urafiki wetu .I’m sorry.Happy” Patrick akasema .
Happy machozi yalikuwa yakimtoka.Mashavu yake yote yalikuwa yamelowa machozi.Alitamani kusema neno lakini midomo ilikuwa ikicheza cheza na kushindwa kuongea.Akajikaza na kusema
“Patrick ! siyo hivyo unavyofikiri.Patrick huwezi jua jinsi gani ulivyoustua moyo wangu.Sikutegemea kama ungeweza kunitamkia maneno haya leo…
“Shhhhhhhhhhhhhh!!!!!!!!!!!.I’m sorry Happy .Nilishindwa kuvumilia .Nimeshindwa kupigana na hisia zangu kwako .Sahamani sana” Patrick akasema
“No Patrick usinifikirie vibaya.Simaanishi hivyo unavyofikiria wewe.Ni kwamba sikuwa nimetegemea kama utakuja kuniambia kitu kama hiki leo.Naomba niwe wazi kuwa nimekuwa nikiumia sana moyoni kwa muda mrefu nikisubiri siku kama hii ya leo ambayo ungeniambia maneno haya.I love you Patrick.I love you so much.Th…….”Akashindwa kuendelea akaanza kulia kwa kwikwi.Patrick akatoa kitambaa na kumfuta machozi .Happy akamtazama Patrick usoni kwa sekunde kadhaa kisha wakakumbatiana kwa nguvu..
“Thank you so much Happy kwa kunipenda.I promise you that I’will never hurt you.Nakuahidi hapa mbele ya kaburi la wapendanao kuwa sintakubali kitu chochote kitutenganishe .Naomba kifo tu ndicho kiwe kitu pekee cha kuweka kutufanya tutengane.Naomba hata kama tukitenganishwa na kifo basi kama kuna uwezekano tufe sote na kuzikwa pamoja kama watu hawa hapa chini.” Patrick alitamka maneno haya kwa umakini mkubwa na ni wazi yalitoka ndani kabisa mwa moyo wake.Happy macho yalikuwa yamemjaa machozi wakati akisikiliza maneno ya Patrick.
“Patrick hata mimi nashukuru sana kama hisia zako kwangu ni za kweli .Ninaichukua ahadi yako kama ilivyo na kuihifadhi moyoni mwangu.Na mimi kama ulivyofanya wewe nakuahidi kuwa sintakuwa radhi kutengana nawe.Naahidi kuwa hakuna chochote kitakachoweza kututenganisha zaidi ya kifo..Ila naomba hapa tuwekeane ahadi kuwa pamoja na kwamba tumekubaliana kuwa wapenzi lakini hatutafanya mapenzi mpaka hapo tutakapokuwa tumemaliza masomo yetu.Niahidi hivyo Patrick”akasema Happy
Patrick akamwangalia Happy kwa tabasamu kubwa kisha akasema.
“Nalifahamu hilo Happy .Ndio maana nikasema kuwa nitakuheshimu na kuziheshimu ndoto zako.Nafahamu hatari za mapenzi shuleni hivyo niko makini sana na suala hilo.Usitie shaka natumai tutakuwa na muda mzuri baada ya kumaliza masomo yetu.”
Happy akatabasamu na kumkumbatia Patrick.Walibaki wamekumbatiana kwa takribani dakika kama tano hivi huu ulikuwa ni mwanzo wa ukurasa wao mpya

******************

Siku mbili kabla ya adhabu yao kumalizika Patrick na Happy wakarejea shuleni.Mara tu baada ya kuwasili kwao shuleni tayari maneno ya chini chini na vijembe vikaanza.Muda huu walioutumia wakiwa Bagamoyo uliwajenga na kuwafanya wawe majasiri hivyo hali hii haikuwatia hofu.Uhusiano wao ukaendelea kama kawaida na safari hii wakawa karibu zaidi.Muda mwingi waliutumia kusoma pamoja hivyo kuwafanya wanafunzi wenzao kuongeza udadisi zaidi.
Ilikuwa ni wiki ya tatu siku ya jumamosi tangu Patrick na Happy warejee toka katika adhabu.Siku hii kulikuwa na tamasha la michezo lililojumuisha shule ya Malangali na shule ya sekondari Ifunda.Lilikuwa ni tamasha kubwa na lililopendeza sana.Uongozi wa shule uliamua kufanya tamasha hili ili kuwaburudisha wanafunzi kabla ya kipindi cha mitihani ya kumaliza muhula wa pili kuanza.
Tamasha lilianza saa nne asubuhi kwa michezo mbali mbali kama vile kukimbia ,kucheza ngoma ,sarakasi nk.Kisha maliza awamu ya kwanza ,wanafunzi wakaenda kupata chakula cha mchana kabla ya kuanza kwa awamu ya pili mchana huo.
Saa nane mchana ikaanza awamu ya pili.wanafunzi wote wakakusanyika katika viwanja vya michezo.Michezo iliyokuwa ikifanyika mchana huu ni mpira wa kikapu,wavu,pete na mwisho kabisa mpira wa miguu.
Karibu katika kila mchezo shule ya sekondari Ifunda ikachukua ushindi.Na sasa ushindani ukahamia katika mpira wa miguu.Wanafunzi wote wakahamia katika uwanja wa mpira wa miguu.
Patrick na Happy walikuwa wakishuka taratibu sana wakielekea katika uwanja wa mpira ili kushuhudia mtanange huo wa kukata na shoka.Hawakuwa wamehudhuria mchezo wowote toka tamasha lilipoanza.Walikuwa wamejificha mahala akijisomea.Wote wawili hawakuwa wapenzi sana wa michezo.
Kiujumla walikuwa wamependeza mno siku hii ya leo na kila aliyepisha nao hakukosa kugeuka kuwatazama.Hawakujali macho ya watu ,wakafika uwanjani na kutafuta sehemu moja iliyokuwa na msingi wa nyumba wakakaa.Waliamua kujitenga kabisa na wenzao.
Mpira ukaanza kwa kasi sana.Dakika ya kumi na moja ya mchezo Ifunda wakapata bao la kuongoza.Mpira ukaendelea na dakika ya arobaini wakapata tena bao la pili.Mpaka mapumziko Ifunda walikuwa wakiongoza kwa mabao mawili.Ilikuwa ni simanzi kubwa kwa upande wa malangali kupoteza kila mchezo.
Kipindi cha pili kikaanza kwa kasi.Dakika ya tisa ya kipindi cha pili Malangali wakapata bao lakini refa akakataa kwa madai kuwa mfungaji wa bao lile likuwaameotea.Wanafunzi wa Malangali wakavamia uwanja na ikazuka vurugu kubwa.Wachezaji wa Ifunda wakatoka uwanjani na kuanza kukimbia wakijaribu kujiokoa na ile vurugu.Mawe,fimbo ,chupa vikawa vikirushwa uwanjani.
“Happy tuondoke mahali hapa si salama tena”Akasema Patrick huku akimshika mkono Happy lakini kabla Happy hajamaliza kuvaa viatu vyake vya kuchomeka alivyokuwa ameviweka kando ya miguu yake jiwe kubwa lililorushwa upande wao likampiga kichwani akaanguka chini huku damu nyingi ikimmwagika.
“Nooo..!!!!!!!.........” Patrick akapiga ukelele mkubwa baada ya kumuona Happy akiwa amelala chini huku damu nyingi ikimvuja kichwani.
Akamwinamia Happy kwa haraka huku machozi yaliyoambatana na hasira yakimtoka.Mwalimu Vicent ambaye alikuwa karibu na mahali pale aliliona tukio lile naye akakimbia haraka kuja kuangalia hali ya Happy .alistuka kwa hali aliyoikuta.haraka haraka akakimbia na kwenda kumwita dereva wa shule akaja na gari na kwa haraka wakampakia Happy wakamwahisha katika kituo cha afya cha karibu.Patrick hakuongea kitu machozi yalikuwa yakimchuruzika.
Kituo cha afya Malangali hakikuwa mbali sana na shule.Kwa bahati mbaya wakati walipofika pale hakukuwa na daktari.Alikuwepo muuguzi mmoja tu.Kwa dakika kama mbili hivi hawakujua wafanye nini kwani hata muuguzi yule alionekana kuwa na hofu kutokana na hali aliyokuwa nayo Happy.
“I have to do something” Patrick akawaza.ghafla akatoka mbio kuelekea kijijini.Hakuna mtu yeyote aliyejua Patrick anakwenda wapi.Dakika kama kumi baadaye gari moja aina ya Toyota pick up ikaja kwa kasi kubwa maeneo hayo ya hospitali huku ikiwa imewasha taa.Watu waliokuwepo hapo nje wakaanza kuingiwa na wasi wasi labda kuna maafa mengine yametokea.Gari ikafunga breki kali na mara bila kutegemea Patrick akashuka.
Mpaka muda huo bado Happy alikuwa ndani ya gari akiwa hana fahamu huku mwalimu na yule muuguzi wakizuai damu kuendela kuvuja huku wakijadiliana jinsi ya kumpata daktari ambaye kwa wakati huo hawakujua alikuwa wapi.
“Haraka haraka,nisaidieni kumbeba.”Akasema Patrick akiwaambia watu wawili aliokuja nao katika ile gari.Huku mwalimu na muuguzi wakishangaa Happy akashushwa toka katika gari ya shule na kupakiwa katika ile gari ndogo aliyokuja nayo Patrick.
“Patrick unafanya nini??.................Alipaaza sauti mwalimu akiwa haelewi nini Patrick alikusudia kufanya.
“Dereva ondoa gari achana na huyo mwalimu”Patrick alisema huku akifunga mlango .
gari ikaondolewa kwa kasi ya ajabu kila mtu akibaki ameduwaa.
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 8
MTUNZI : PATRICK.CK
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“I have to do something” Patrick akawaza.ghafla akatoka mbio kuelekea kijijini.Hakuna mtu yeyote aliyejua Patrick anakwenda wapi.Dakika kama kumi baadaye gari moja aina ya Toyota pick up ikaja kwa kasi kubwa maeneo hayo ya hospitali huku ikiwa imewasha taa.Watu waliokuwepo hapo nje wakaanza kuingiwa na wasi wasi labda kuna maafa mengine yametokea.Gari ikafunga breki kali na mara bila kutegemea Patrick akashuka.
Mpaka muda huo bado Happy alikuwa ndani ya gari akiwa hana fahamu huku mwalimu na yule muuguzi wakizuai damu kuendela kuvuja huku wakijadiliana jinsi ya kumpata daktari ambaye kwa wakati huo hawakujua alikuwa wapi.
“Haraka haraka,nisaidieni kumbeba.”Akasema Patrick akiwaambia watu wawili aliokuja nao katika ile gari.Huku mwalimu na muuguzi wakishangaa Happy akashushwa toka katika gari ya shule na kupakiwa katika ile gari ndogo aliyokuja nayo Patrick.
“Patrick unafanya nini??.................Alipaaza sauti mwalimu akiwa haelewi nini Patrick alikusudia kufanya.
“Dereva ondoa gari achana na huyo mwalimu”Patrick alisema huku akifunga mlango .
gari ikaondolewa kwa kasi ya ajabu kila mtu akibaki ameduwaa.

ENDELEA……………………

“ahsanteni sana ndugu zanguni nashukuru mmenisaidia”Patrick akawaambia dereva na yule msaidizi wake baada ya kufika katika hospitali ya Makambako na Happy kuanza kupatiwa matibabu.
“Usjali dogo siku yoyote ukiwa na tatizo unasema.sisi sote binadamu lazima tusaidiane.”akasema dereva.
Baada ya kuwalipa pesa zao wakaondoka kurudi malangali na kumwacha Patrick hapo hospitali.Giza tayari lilikwisha ingia.Happy alikuwa katika chumba cha upasuaji akishonwa jeraha lake la kichwa.Lilikuwa ni jereha kubwa lililompelekea apoteze damu nyingi .Bado alikuwa hajarejewa na fahamu.Patrick bado alikuwa nje ya chumba hicho akisubiri kujua hali ya Happy itakuwaje .Moyoni bado alikuwa na fundo kubwa lililomkaa juu ya kilichokuwa kimetokea.Alianza kuvuta picha ya jinsi tukio lile lilivyotokea .Alikumbuka wakati vurugu imeanza na mawe kuanza kurushwa.hadi jiwe lile kumpata Happy kichwani, ni wazi tukio lile lilikuwa limedhamiriwa.
“Naanza kupata picha kuwa mrushaji wa jiwe lile alikuwa amedhamiria kabisa kumjeruhi Happy au mimi.”akawaza Patrick.akiwa katika lindi la mawazo mara mlango wa chumba cha upasuaji ukafunguliwa na machela ikatoka.
“Kijana hali ya mwenzio inaendelea vizuri .Tumeshona jeraha lake na sasa tunampeleka wodini .Tutamuongezea damu kwa sababu amepoteza damu nyingi sana.wewe unaweza kwenda kupumzika .Uje asubuhi”Alisema daktari mama wa makamo ambaye alionekana kuwa na roho ya huruma.
“Ahsante daktari kwa kazi kubwa mliyoifanya.Lakini nitabaki hapa hapa mpaka asubuhi kwa sababu tayari imeshakuwa usiku na mimi hapa Makambako ni mgeni”
“Nyie mmetokea wapi” Akauliza yule daktari
“sisi ni wanafunzi wa shule ya sekondari malangali” patrick akajibu.Baada ya mahojoano mafupi na yule mama akamwangalia Patrick kwa sekunde kadhaa kisha akasema.
“Umefanya kitendo cha kijasiri sana ..kama ungeendelea kukaa pale shuleni hali ya mwenzio ingekuwa mbaya zaidi na hata kupoteza maisha.Nitamwambia dereva wetu akupeleke nyumbani kwangu ukapumzike hadi kesho.Umeonyesha moyo wa ujasiri sana wa kumsaidia mwenzako..Nisubiri hapo hapo” Alisema yule mama na kuingia ndani.
Patrick aliendelea kumwomba Mungu kimoyo moyo hali ya Happy iwe nzuri.
“Twende” akasema yule daktari wakaondoka na kisha Patrick akapanda gari la hospitalina kupelekwa nyumbani kwa yule daktari
.

* * * *

Saa kumi na mbili asubihi ilimkuta Patrick tayari amekwisha fika hospitali.Hakuweza kupata usingizi usiku huo licha ya kuhakikishiwa kuwa hali ya Happy ilikuwa nzuri.Moyo ulikuwa ukimwenda mbio.Aliingia katika wodi aliyolazwa Happy kwa wasi wasi mwingi.Lakini ghafla akakutana na sura angavu yenye matumaini ya Happy .tayari alikwisha pata fahamu toka usiku.Patrick akafumba mdomo kwa kiganja cha mkono wake akionyesha mshangao.kwa haraka akakimbia na kumkumbatia Happy pale kitandani.
”Pole sana Happy ”
‘ahsante Patrick.nashukuru sana kwa msaada wako”
“Usijali Happy ulikuwa ni wajibu wangu kufanya hivyo”akajibu Patrick.
“ nilikuwa na wasi wasi mwingi wakati fahamu zimenirudia nikiwaza nilifikaje fikaje hapa..Muuguzi mmoja aliyekuwapo zamu ya usiku akaniambia kuwa kuna rafiki yangu mmoja anaitwa Patrick pamoja na watu wengine wawili ndio waliokuleta hapa.Nilifurahi sana kusikia hivyo.nashukuru sana Patrick.Kwa sasa naamini kuwa upendo wako kwangu ni wa kweli.”
Patrick hakujibu kitu akatabasamu.
“sasa Patrick nina imani nitazidi kuwepo hapa hospitali kwa siku kadhaa hivyo nitakupa namba hizi za simu umpigie mama yangu na umweleze mkasa mzima jinsi ulivyokuwa ili aje anihudumie kwa kipindi hiki chote nitakachokuwa hapa hospitali. Kwa sababu wewe unatakiwa kwa sasa uanze kujiandaa na mitihani ambayo haiko mbali sana.”
Patrick akakubaliana na ushauri ule na kuzichukua zile namba.
“ Happy ungependa kula ni ni asubuhi hii”Patrick akauliza
“Mimi nimeshashiba kwa kukuona wewe tu.Patrick wewe ni chakula tosha kabisa.Usisumbuke Patrick sintakula kitu .Jitahidi ukawasiliane na mama najua atanihamisha hapa na kwenda kutibiwa Mbeya.”
Waliongea mambo mengi asubuhi hiyo hadi muda wa kuwaona wagonjwa ulipoisha kisha Patrick akamuaga Happy kuwa anaenda kupiga simu.

****************************

Saa tano na dakika ishirini na saba gari moja ndogo yenye vioo vyeusi lilifunga breki katika hospitali ya Makambako .Mama mmoja akiongozana na binti mmoja ambaye ni wazi alionekana kuwa ni mwanae walishuka ndani ya gari lile na kuelekea mapokezi.Waliongea na wauguzi waliokuwapo pale mapokezi kisha wakapelekwa kwa mganga mkuu.Baada ya muda wakatoka wakiwa wameongozana na mganga mkuu na kuelekea maeneo ya wodi za wagonjwa.
Patrick alikuwa nje ya wodi aliyokuwa amelazwa Happy .Hali ya hewa ilikuwa ya kiubaridi baridi kama ilivyo ada ya hali ya hewa ya Makambako.Kijua kilichomoza na kuzima.Hii haikumsumbua sana kwa sababu alikuwa bado amevaa suti aliyokuwa ameivaa jana yake.Mara akawaona mama mmoja na mwanae wakiwa wameongozana na daktari mkuu.
“Mhhhh!!” Patrick akaguna.Akazidi kuwaangalia kwa makini watu wale wakija .
“Yule msichana mbona kafanana sana na Happy ? anaweza akawa ndiye yule ndugu yake ? hata yule mama amefanana sana na Happy” Patrick akaendelea kuwaza huku akiwatazama yule mama na yule binti wakielekea katika wodi aliyokuwa amelazwa Happy..
Mama yule ,binti yake pamoja na daktari mkuu wakampita Patrick pale nje na kuelekea moja kwa moja katika wodi ile aliyokuwa amelazwa Happy wakaingia ndani.
“Nahisi ni wenyewe hawa.nahisi huyu ndiye mama yake Happy .”Akawaza Patrick huku akijiweka sawa kwani alitegemea ni lazima wangeonana..Dakika kama tano hivi toka yule mama aingie mle wodini alikuja muuguzi na kumwita Patrick ndani.
“mama huyu ndiye Patrick ni rafiki yangu na ndiye aliyeyaokoa maisha yangu kwa kunileta hapa hospitali haraka.”
Akasema Happy baada ya Patrick kuingia
“ooh ! Ndiye huyu ! Ndiye huyu aliyenipigia simu asubuhi?”
“Ndiye mimi mama.Shikamoo” Patrick akasema kwa adabu
“Marahaba mwanangu.nashukuru sana kwa msaada wako.”
“Ahsante mama”Patick akajibu.
Mama yake Happy alikuwa ni mtu mchangamfu na mcheshi sana.
“Patrick huyu ni mdogo wangu anaitwa Margareth.” Happy akasema
“Nafurahi sana kukufahamu margareth.”Akasema Patrick huku akishikana mikono na Margareth.Mama yao alikuwa akitabasamu akasema
“Patrick tunashukuru sana kwa msaada wako lakini itabidi Happy tumuhamishe hospitali.Tutaenda naye Mbeya akatibiwe kule.Kwa hiyo wewe unaweza ukarejea shuleni.Utapewa barua na mganga mkuu wa hapa ili uipeleke shuleni ya kuthibitisha ugonjwa wa mwenzio.”
“sawa mama” akajibu Patrick
Saa saba na nusu za mchana Patrick akawasili shuleni na moja kwa moja akaelekea katika ofisi ya mkuu wa shule msaidizi.
“Patrick !!.. akasema mkuu wa shule msaidizi baada ya Patrick kuingia ofisini kwake.
“Naam mwalimu”
“Umefanya nini tena? Hata wiki mbili hazijaisha toka utoke kwenye adhabu leo tena unarudia mambo yale yale? Akasema mwalimu kwa ukali
“Sikiliza mwalim…………………..”
“noo !! sitaki kusikiliza upuuzi wako.kwa nini ukamchukua mgonjwa na kukimbia naye mahala kusikojulikana?Sisi kama walimu ndio walezi wenu ninyi mkiwa hapa shuleni . tutajibu nini kwa wazazi wake pindi tatizo kubwa likimpata? Akaendelea kufoka mwalimu mkuu msaidizi
‘.Mwalimu,siku ile ya mashindano baada ya kutokea vurugu Happy alijeruhiwa na jiwe kichwani akapoteza fahamu.damu nyingi ikawa ikimvuja.Mimi na mwalimu Steve pamoja na dereva wa shule tukampakia garini na kumpeleka zahanati .pale hakukuwa na daktari na muuguzi tuliyemkuta pale alikuwa akisita hata kumuhudumia Happy .Mimi sikuridhika na hali ile ikanibidi nikodi gari kwa pesa zangu na kumuwahisha Happy hospitali ya Makambako ambako alipatiwa matibabu,akashonwa jeraha lake ,akaongezewa damu pia.na hii hapa ni barua toka kwa mganga mkuu wa hospitali ya Makambako.”
Mkuu wa shule msaidizi akaichukua barua ile na kuisoma kisha akamwangalia Patrick kwa sekunde kadhaa.
“Ulifanya jambo jema Patrick .Uliokoa maisha ya mwenzio lakini siku nyingine unatakiwa ushauriane kwanza na sisi na siyo kuchukua maamuzi yako binafsi .Mashitaka yaliyoletwa hapa kwangu ni kwamba ulifanya vurugu na kumchukua Happy .Hivi sasa tulikuwa katika maandalizi ya kuripoti suala hili katika vyombo vya usalama vitusaidie kukutafuta na kukuchukulia hatua.Haya nenda ukapumzike ila kuwa mwangalifu sana kwa sasa unafuatiliwa kwa kila unachokifanya” akasema mwalimu
“Ahsante sana mwalimu nitakuwa mwangalifu”
Patrick akatoka ofisini kwa mkuu wa shule msaidizi na kuelekea bwenini.Akaoga na kujilaza kitandani.

* * * *

Mwezi wa kwanza mwaka uliofuata shule zikafunguliwa na ikawa ni awamu mpya kwa Patrick na Happy .Kwa sasa walikuwa kidato cha nne na walifahamu nini walichokuwa wakihitajika kukifanya hivyo hawakuwa na mzaha katika kusoma.Walisoma kwa bidii kubwa kwa lengo moja tu la kutimiza ndoto zao.Wawili hawa kwa ghafla waka ni mfano wa kuigwa na wengine.Tofauti na mwaka uliotangulia kwa sasa wakaanza kuwa na marafiki wengi wa madarasa ya chini yao ambao mara nyingi walipewa msaada mkubwa katika masomo.Kitendo cha kuheshimiwa na wanafunzi wa vidato vya chini kilizidi kuwapa wakati mgumu wale wanafunzi adui zao ambao walikuwa hawawatakii mema.
Ilikuwa ni tarehe 14/03 siku ya jumamosi ambapo wanafunzi walikuwa wametangaziwa kuwa siku hiyo kungekuwa na burudani ya muziki.Burudani kama hizi huja mara chache sana hapa shuleni,hivyo wanafunzi walikuwa wamejiandaa vilivyo.Patrick na Happy nao walishauriana na kukubaliana kuwa wangeingia ukumbini japo kwa muda mchache tu halafu waendelee na ratiba yao za kujisomea.
Baada ya mlo wa jioni milango ya ukumbi ikafunguliwa na wanafunzi wakaanza kujitoma ndani.Disko likafunguliwa rasmi na wanafunzi wakaanza kuserebuka.Patrick na Happy wakaingia ndani ya ukumbi lakini hawakukaa sana kutokana na joto ,wakatoka na kwenda kupunga upepo nje.Wakiwa nyuma ya bwalo la chakula wakipunga upepo huku mbalamwezi ikumulika mara ghafla likatokea kundi la vijana waliokuwa wamefunika nyuso zao wakiwa na mapanga matatu wakawazingira.Happy akaogopa na kumkumbatia Patrick
“Mama yangu !!!!,”Happy akasema kwa mstuko
“ kaa kimya na usijaribu kupiga kelele kwani tutawaua sasa hivi.”Akasema jamaa mmoja aliyekuwa na sauti nzito .Happy alikuwa akitetemeka.Patrick naye mikono ilikuwa ikimtetemeka.
Kundi lile lilikuwa na vijana zaidi ya kumi na wote walikuwa wamefunika nyuso zao.
Mmoja ambaye ndiye aliyeonekana kuwa kiongozi wao aliwasogelea na kumshika mkono Happy .
“Tuna shida na huyu binti” Akasema yule jamaa huku akimvuta Happy kwake.
Patrick akainua mkono lakini kabla hajafanya lolote akapigwa na chuma kizito shingoni akaanguka chini na kuona giza, yule jamaa akamshika Happy kisha kwa haraka wakamjaza vitambaa mdomoni ili asiweze kupiga kelele.
“Haya jamani haraka haraka tumalize kazi.Leo ni leo.Keo nenda kaangalie kama kuna mtu yoyote anakuja maeneo haya .Ukiona kuna mtu anakuja tufahamishe haraka.”
Akaamrisha yule jamaa ambaye alionekana kuwa ndiye kiongozi wa genge lile
Happy alikuwa ameshikwa bara bara kiasi cha kutoweza kufurukuta akabebwa juu juu na kupelekwa katika kichaka cha karibu.Kwa kasi ya aina yaka yule jamaa kiongozi akaichana blauzi nyepesi aliyokuwa ameivaa Happy na kuyashuhudia matiti machanga ya kimwana huyu.Udenda ukamtoka.Happy alikuwa akilia lakini sauti yake ilikuwa haisikiki kutokana na vitambaa walivyomuweka mdomoni.
Fedhuli yule akaishusha suruali yake hadi magotini na kuanza kumsogelea Happy huku uume wake ukiwa umesimama wima.Akaivuta suruali ya Happy na kuishusha chini kisha akaivuta nguo ndogo ya ndani aliyokuwa ameivaa na kuichana Akaitupa pembeni akawaamuru wale watu waliokuwa wamemshika Happy wampanue miguu.
“Hii niyo dawa yake mshenzi huyu.Halafu anaonekana bado bikira.Hii ndiyo dawa ya wasichana kama wewe wenye maringo”
Akasema yule jamaa huku akiuchezea uume wake tayari kumwingilia Happy kwa nguvu
Taratibu Patrick akapata fahamu na kuhisi maumivu makali sana maeneo ya shingoni na mara kumbu kumbu zote zikarudi.Akakumbuka kuwa walikuwa wamevamiwa na yeye akapigwa na kitu kizito shingoni.
“Happy yuko wapi?” Akajiuliza na mara akakumbuka kwamba wale wahuni waliowavamia walimchukua kwa lengo la kumtenda vibaya.Akajikaza na kuamka pale alipokuwa amelala huku akihisi maumivu makali mno.Happy hakuwapo na wala wale jamaa waliowavamia hawakuwapo.Hasira ikampanda .
“ I must do something immediately kabla hawa jamaa hawajatekeleza mpango wao” AkawazaPatrick.Pale chini akakiona kile chuma alichopigwa nacho akainama na kukiokota kisha akaanza kunyata kuelekea mahala aliposikia minong’ono ya watu.Alinyata taratibu akiwa amefura kwa hasira.
Ndani ya kichaka Happy alikuwa ameshikwa barabara kiasi kwamba hakuweza kufurukuta wala kupiga kelele kutokana na matambara yaliyojazwa mdomoni.Kiongozi wa genge lile alikuwa akijiandaa tayari kabisa kutekeleza kitendo cha kumbaka Happy .Ni machozi pekee ndiyo yaliyokuwa yakimtoka binti huyu mrembo .Roho ilimuuma sana kwa kushuhudia kitendo kile alichotaka kufanyiwa.Vile vile aliumia sana roho baada ya kumfikiria Patrick.Hakuwa na uhakika kama atakuwa salama kwani alishuhudia yeye mwenyewe kwa macho yake Patrick akipigwa na chuma kizito akaanguka chini.Ni uchungu ambao hauwezi kuelezeka aliokuwa nao binti huyu.Hakuwa na tumaini la kupata msaada wa aina yoyote kwa wakati ule.Msaada pekee alikuwa ni Patrick na ambaye aliamini kuwa kwa pigo lile lazima atakuwa katika hali mbaya ya kutokujitambua kama sio kufa kabisa
Wakati jamaa yule akiuchezea uume wake mkubwa ,Happy huku machozi yakimtoka akafumba macho na kuomba
“Ee Mungu najua sina ubaya wowote na mtu yeyote yule hadi kufanyiwa kitendo hiki.Ee baba kama sistahili kufanyiwa hivi basi na isiwe lakini kama …….
Hakumaliza maombi yake mara ghafla yule jamaa aliyekuwa tayari kumwingilia akapiga ukelele mkubwa na kuanguka chini.Kilichofuata hapo ni kusikia vishindo vya watu wakikimbia.Ulikuwa ni muujiza ambao Happy hakuutegemea katu.Kijana mmoja ambaye hakuweza kumtambua kwa haraka kutokana na giza alikuwa amesimama mbele yake na kisha akamwinamia.
“Happy are you ok?” Ilikuwa ni sauti ya Patrick ambaye aliongea akiwa katika maumivu makali sana.
Happy hakusema kitu ni machozi tu ndiyo yaliyokuwa yakimtoka .Hakuamini kabisa kwa alichokuwa akikiona.
Patrick akamtoa yale matambara aliyokuwa amewekewa mdomoni kisha akambusu.
“Patrick you are my Hero.” Ni neno hilo tu ambalo Happy aliweza kulisema kwa wakati huu.Mwili wote ulikuwa ukimtetemeka.
“Hawajakufanya kitu chochote washenzi hawa? Akauliza Patrick
“Hwakuwahi, ulifika kwa wakati muafaka kabisa bado walikuwa hawajatimiza azma yao.Ahsante Patrick”Akasema Happy huku machozi yakimtoka
Pale chini alikuwa amelala yule kiongozi wa genge lile la wahuni akivuja damu kichwani mahala alipopigwa na chuma .Patrick akamwangalia kwa hasira sana.
“Patrick huyu jamaa ni mzima kweli? Happy akauliza
“I don t know Happy .Sijui kama atakuwa mzima.Nilimpiga kwa nguvu zangu zote nilizokuwa nazo..Hiyo ni adhabu yake” akajibu Patrick
Ghafla wakasikia makelele ya watu wakija kwa kasi kule mahala walikokuwa.
“Happy lets get out of here.wasije wakatukuta hapa hawa watu.tayari wamekwisha ambizana.” Akasema Patrick na kumshika Happy mkono wakaanza kukimbia kushuka katika korongo.Hawakufika mbali wakamulikwa na tochi usoni.
“Hey ! simameni hapo hapo,mkikimbia ninaachia mshale huu”Ilikuwa ni sauti nzito ya mwanaume.Patrick na Happy wakasimama.Walikuwa ni watu wanne waliokuwa na mbwa .Watu hawa walikuwa ni wawindaji waliokuwa wakifuatilia mitego yao porini.
“Tafadhali jamani naomba mtuache tuondoke tuna matatizo makubwa” Akasema Patrick
“Hapana kwanza ninyi mnaonekana ni wanafunzi.Usiku huu mnafanya nini porini?Haya anzeni kuongoza tunawarudisha mpaka shuleni” Akaamuru jamaa mmoja ambaye alionekana kuwa ndiye kiongozi wa wale wawindaji.
Jitihada za Patrick an Happy kuomba waachiwe hazikuweza kuzaa matunda,jamaa wakaanza kuwaongoza kuwarudisha shuleni.
Hawakuwa na ujanja tena zaidi ya kufanya vile walivyoamriwa.

* * * *

“wameuaaaaaa !!!....wauajiiiiiiiiii!!!!!!......wauaweeeee!!!!!!!!!!” Hizo ni kelele zilizoufunika mji wa Malangali kwa muda huu wa usiku.Patrick na Happy walikuwa katika mikono ya polisi kwa ajili ya usalama wao.Yule jamaa aliyepigwa na chuma kichwani na Patrick alikuwa amekufa.
Karibu kijiji chote kilikuwa kimeamka kutokana na makelele ya wanafunzi na kukusanyika shuleni.Wote walitaka washuhudie ni wanafunzi gani waliofanya mauaji.Baada ya kuingizwa katika kituo kidogo cha polisi kilicho pembezoni mwa shule ikawabidi polisi kupiga risasi za moto juu ili kuwatawanya wanafuzi ambao walikuwa wameanza kurusha mawe wakitaka watuhumiwa waachiwe ili wauawe pia.Ilikuwa ni kazi kubwa kuwatawanya lakini hatimaye walifanikiwa baada ya kupiga risasi kadhaa hewani.
Happy machozi yalikuwa yakimtoka.Hakutegemea kama siku moja angeweza kuingia katika dhahama ile.Hakuwahi kuota kama siku moja angeitwa muuaji.
“Nyamaza Happy ,usilie mambo yameshatokea..Jipe moyo Mungu yupo na yeye ndiye anayeufahamu ukweli.” Patrick akambembeleza Happy
“Patrick nina uchungu mwingi sana .Ni bora ningekuwa mwenyewe lakini sasa nimekuingiza na wewe katika matatizo makubwa namna hii.tayari nimekwisha kuharibia mwelekeo mzima wa maisha yako……….”
“Shhhhhhhh..!!!....Usiseme hivyo Happy .I did the right thing.Hata nikinyongwa nitakuwa na amani kwamba niliua kwa ajili ya kukulindia heshima yako.Hakuna mwanaume yeyote anayeweza kukubali kuona mpenzi wake akifanyiwa kitendo cha kinyama kama walichotaka kukufanyia hawa jamaa.nadhani nilifanya kitu sahihi.Sijutii kosa langu kwa sababu nimefanya kwa ajili ya mtu nimpendaye”
Happy akamkumbatia Patrick kwa nguvu huku akilia .
Kwa ajili ya usalama wao usiku huo huo wakapakiwa katika gari la polisi na kupelekwa kituo kikuu cha polisi Iringa mjini

* * * *

Karibu kijiji chote kilikuwa kimeamka kutokana na makelele ya wanafunzi na kukusanyika shuleni.Wote walitaka washuhudie ni wanafunzi gani waliofanya mauaji.Baada ya kuingizwa katika kituo kidogo cha polisi kilicho pembezoni mwa shule ikawabidi polisi kupiga risasi za moto juu ili kuwatawanya wanafuzi ambao walikuwa wameanza kurusha mawe wakitaka watuhumiwa waachiwe ili wauawe pia.Ilikuwa ni kazi kubwa kuwatawanya lakini hatimaye walifanikiwa baada ya kupiga risasi kadhaa hewani.
Happy machozi yalikuwa yakimtoka.Hakutegemea kama siku moja angeweza kuingia katika dhahama ile.Hakuwahi kuota kama siku moja angeitwa muuaji.
“Nyamaza Happy ,usilie mambo yameshatokea..Jipe moyo Mungu yupo na yeye ndiye anayeufahamu ukweli.” Patrick akambembeleza Happy
“Patrick nina uchungu mwingi sana .Ni bora ningekuwa mwenyewe lakini sasa nimekuingiza na wewe katika matatizo makubwa namna hii.tayari nimekwisha kuharibia mwelekeo mzima wa maisha yako……….”
“Shhhhhhhh..!!!....Usiseme hivyo Happy .I did the right thing.Hata nikinyongwa nitakuwa na amani kwamba niliua kwa ajili ya kukulindia heshima yako.Hakuna mwanaume yeyote anayeweza kukubali kuona mpenzi wake akifanyiwa kitendo cha kinyama kama walichotaka kukufanyia hawa jamaa.nadhani nilifanya kitu sahihi.Sijutii kosa langu kwa sababu nimefanya kwa ajili ya mtu nimpendaye”
Happy akamkumbatia Patrick kwa nguvu huku akilia .
Kwa ajili ya usalama wao usiku huo huo wakapakiwa katika gari la polisi na kupelekwa kituo kikuu cha polisi Iringa mjini .

* * * *

Uchunguzi wa kesi ya mauaji inayowakabili wanafunzi wawili wa kidato cha nne Patrick na Happy ulianza kwa kasi .Wazazi wa happy wakishirikiana na wale wa Patrick waliweka mawakili sita wa kuwatetea watoto wao.Pamoja na jitihada hizo zote za kuhakikisha kuwa watoto wao wanaachiwa huru na mahakama bado kesi ikaonekana kuwa ngumu kutokana na ushahidi mkubwa wa wanafunzi kuwakandamiza Patrick na happy.Wanafunzi zaidi ya kumi walikubali kusimama mbele ya mahakama na kutoa ushahidi kuwa Patrick na Happy kwa pamoja walishirikiana katika mauaji ya Angatile mmoja kati ya wanafunzi watukutu hapo shuleni.
Baada ya miezi miwili Happy akaachiwa huru na mahakama alipoonekana hakuwa na kesi ya kujibu.Patrick ambaye alionekana kuwa ana shataka la kujibu akabaki gerezani huku kesi yake ikiendelea kusikilizwa.Huo ukawa ni ukurasa mpya wa maisha yake gerezani.
Miezi ilizidi kukatika Patrick akiwa bado gerezani akiendelea kushikiliwa kwa shitaka la mauaji.Happy ambaye alikubaliwa na uongozi wa shule yao kuwa ataruhusiwa kurudi kufanya mtihani wake wa kidato cha nne aliendelea na masomo jijini Mbeya..Alidhoofu kwa mawazo na ukiwa aliokuwa nao.Furaha yote aliyoipata kwa muda mfupi ilikuwa imetoweka.Hakuwa tena na rafiki Rafiki yake mkuu alikuwa ni Patrick ambaye kwa sasa alikuwa gerezani.Kila siku alikuwa akilia na kumuomba Mungu amsaidie Patrick aweze kutoka gerezani .Moyoni alijua ni yeye ndiye aliyesababisha Patrick kuwapo gerezani .Patrick aliua wakati akijaribu kumtetea yeye asibakwe.Aliumia sana kila alipolifikiria suala hili.
Kila mwishoni mwa wiki alikwenda kumtazama Patrick na kumpelekea vitu mbali mbali.Wazazi wa Happy halikadhalika walikwenda mara kwa mara kufuatilia maendeleo ya kesi ya Patrick na kumjulia hali.Happy alikwisha waeleza kwa kina juu ya kilichosababisha Patrick kuwepo gerezani.Wazazi wa Patrick walijitahidi kwa kila walivyoweza ikiwa ni pamoja na kuongeza mawakili maarufu wa kujitegemea katika jopo la mawakili wanaomtetea Patrick.Kilikuwa ni kipindi kigumu sana kwa familia zote mbili .
Hatimaye kikafika kipindi cha kufanya mitihani ya Taifa ya kumaliza kidato cha nne Patrick akiwa bado gerezani.Siku tatu kabla ya mtihani huo kuanza Happy akamtembelea gerezani ambako waliongea mambo mengi.
“Patrick mpenzi nasikia uchungu sana kwa hali hii.Tulikuwa na malengo mengi sana ya maisha yetu kwa siku za usoni lakini yote yameyeyuka.Sijui lini utatoka gerezani mpenzi wangu…………” Happy akashindwa kujizuia akaanza kulia ,Patrick akamkumbatia na kumbembeleza.
“ Nyamaza Happy .Hutakiwi kulia.Be strong.Haya ni mambo ya kawaida.Kila kitu hutokea kwa sababu maalum Huwezi kujua kwa nini sisi yametutokea haya.Maandiko matakatifu yanatuasa tushukuru katika kila jambo linalotufika.Sijutii kuwapo hapa kwa sababu niko hapa kwa ajili ya mwanamke nimpendaye.Kitu kimoja tu ninachokuomba jiandae vyema na mitihani yako na Mungu akujalie ufanye vizuri.Mimi nipo na Mungu atanisaidia siku moja nitatoka.Nitakuwa nimepoteza muda mwingi na mwelekeo mzima wa maisha yangu lakini nitakuwa na furaha kuwa nilipigana kiume kulinda heshima ya mtu nimpendaye duniani.Ila nakuomba kitu kimoja Happy ………”Patrick akanyamaza akavuta pumzi ndefu ,akamwangalia Happy kwa sekunde kadhaa ,akamfuta machozi .
“Happy naomba kabla muda wetu wa maongezi haujakwisha unihakikishie kitu kimoja kwamba pamoja na kuwa sijui lini nitatoka gerezani,pengine nitanyongwa lakini naomba kusikia kutoka kwako leo hii kuwa hautakuwa na mwanaume mwingine zaidi yangu pamoja na hali yangu hii kwa sasa.Naomba haya yote yaliyotokea yasipotee bure,naomba uendelee kuheshimu ahadi zetu tulizowekeana,naomba ue……………..”Patrick akashindwa kujizuia kutokwa na machozi.
“Patrick mpenzi wangu ,nyamaza kulia.Najua inauma sana na ni ngumu kuibeba adhabu hii kubwa lakini naomba nikuhakikishie kuwa kwa namna yoyote ile sintadiriki kuwa na mwanaume yeyote zaidi yako.Nitakusubiri kwa muda wote mpaka utakapotoka ili tuweze kutimiza ndoto zetu pamoja.I promise.”
Akasema Happy kisha wakakumbatiana kwa hisia kubwa huku kila mmoja machozi yakimdondoka.Muda ukaisha Happy akaombwa aondoke.

* * * *

Muda ulikwenda kwa kasi .Na hatimaye matokeo ya kidato cha nne yakatoka na Happy akachaguliwa kuendelea na kidato cha tano na sita katika shule ya Sekondari ya wasichana ya Iringa.Alifurahi sana kwa kuchaguliwa kwenda pale kwani atakuwa bado karibu na Patrick ambaye kwa sasa alikuwa ni sehemu ya maisha yake .Ingawa bado hakukuwa na matumaini yoyote ya Patrick kutoka gerezani kutokana na mwenendo wa kesi kuwa mgumu,lakini bado Happy alizidi kumpenda na kumpa moyo.Kila wiki alikuwa akienda kumtazama gerezani na kumpa faraja..
“Patrick matokeo yametoka “Alisema Happy alipokwenda kumtembelea Patrick gerezani mara baada ya matokeo kutoka.
“Hizo ni habari njema sana.Unakwenda shule gani ? Patrick akauliza
“nimechaguliwa kuendelea na masomo hapa hapa Iringa.Nitasoma Iringa girls.Nilikuwa nikiomba Mungu nisipangwe shule yoyote ya mbali ili isiwe vigumu kuja kukutembelea.Patrick wewe ni sehemu ya maisha yangu na kamwe siwezi kuvumilia kuwa mbali nawe.Nashukuru Mungu amesikia kilio changu .” Happy alisema huku amemkumbatia Patrick .
“Happy nimefurahi sana kusikia hivyo.Mungu bado anatupenda.Pamoja na misuko suko yote iliyotukumba lakini bado umeweza kufanya vizuri na kufaulu mtihani wako.Hongera sana Happy.Kumbuka kama imeandikwa kuwa mimi na wewe tutakuwa pamoja maishani hakuna ambaye anaweza kututenganisha.” Patrick akasema
Ilikuwa ni siku ya furaha sana kwao.
Mpaka Happy anamaliza kidato cha sita bado Patrick alikuwa akisota katika mahabusu ya gereza kuu la Iringa.Kesi yake ilikuwa ikisomwa na kuahirishwa mara kwa mara.Tayari Patrick alikwishazoea maisha ya kukaa mahabusu.Afya yake ilikuwa imedhoofu kutokana na maisha magumu ya gerezani.Faraja pekee aliyokuwa nayo ni Happy aliyekuwa akienda kumtazama kila jumamosi pamoja na wazazi wake.Upendo wa Happy haukupungua hata kidogo.Kila siku upendo wake kwa Patrick ulikuwa ukiongezeka.
Jumamosi moja Happy alienda kumtembelea Patrick kama ilivyo kawaida yake.Kwa sasa tayari alikwisha maliza shule na alikuwa akisubiri matokeo ya kidato cha sita.Wakati wakiongea Patrick akamtazama Happy usoni kwa makini na kusema.
“Happy mpenzi naomba nikufahamishe kuwa Jumatatu ndo ile siku yangu ya Hukumu .Nashukuru Mungu kwani baada ya kusota gerezani kwa muda mrefu hatimaye nitaenda kusomewa hukumu yangu.Sijui nini kitatokea.Mwenendo mzima wa kesi yangu unaonesha kuwa nina hatia japokuwa kesi ilibadilishwa na ikawa ni kuua bila kukusudia...Siyo siri ninaogopa.Sijui kama nitafungwa maisha au nitahukumiwa miaka mingapi gerezani.Mungu anajua kuwa sikukusudia kufanya vile lakini nilifanya kwa sababu ya kumlinda mtu nimpendaye asidharirishwe na wahuni wale.Happy naomba usiwepo mahakamani siku hiyo ya hukumu.Sitaki uumie.Ni wewe tu ndiye unayeufahamu ukweli hivyo kusikia hukumu nitakayoipata najua itakuumiza mno.Ila kumbuka vyovyote vile itakavyokuwa naomba ujue kuwa nakupenda sana.I love you so much Happy .Wewe ni mtu pekee ambaye ninayatoa maisha yangu kwake.Sintapenda mtu mwingine kama ninavyokupenda wewe…………….”Patrick akasema kwa hisia kali
Huku akitokwa na machozi Happy akasema
“Patrick nashindwa hata niseme nini.Siku zote tumekuwa tukiomba siku hii ifike haraka ili tujue hatma yako lakini kwa sasa naona kama vile siku hii isije.lakini siwezi kuizuia isifike.I’ll be strong.Nitajitahidi kuwa jasiri na kuwepo siku hiyo ya hukumu.I must be there Patrick.I mus………………” Happy akaangua kilio.
Ilichukua muda kumbembeleza Happy .Huzuni kuu ilitanda kwa vijana hawa.Hawakuongea sana walikuwa wamekumbatiana huku kila mmoja akiwa kimya.Kila mmoja akiwaza lake.

* * * *

Ni siku ya Jumatatu mahakama ilifurika watu.Wote walikuja kushuhudia hukumu ya Patrick,kijana mwanafunzi aliyemuua mwanafunzi mwenzake.
Ndugu za Patrick wote walikuwa wamewasili mapema sana hapa mahakamani.Si wao tu hata familia nzima ya akina Happy ilikuwa imewasili kusikiliza hukumu hii.Familia ya Happy na ile ya Patrick kwa sasa zilikuwa zimekwisha fahamiana na wote walikuwa kitu kimoja katika kumsaidia Patrick.
Saa mbili kamili juu ya alama gari lililowabeba washtakiwa wa kesi za mauaji ambao walikuwa wakisomewa hukumu zao liliwasili eneo la mahakama.Simanzi kuu ikatanda eneo hilo baada ya watuhumiwa wale kuwasili.Happy alishindwa kujizuia kudondokwa na machozi pale aliposhuhudia Patrick akishushwa toka katika gari maalum la kubebea mahabusu maarufu kwa jina la karandinga..Margreth na mama yake walijitahidi kumbembeleza na kumtaka ajikaze.Happy akanyamaza.
Hatimaye ule muda uliokuwa mgumu sana katika historia ya Patrick ukawadia.Muda wa hukumu.Patrick akapandishwa kizimbani akiwa ni mwenye majonzi makubwa .Macho yake yalikuwa hayaoni vizuri kutokana na machozi yaliyokuwa yanamtoka.Baadhi ya watu ambao hawakumuona kwa muda mrefu walikuwa wakimsikitikia kijana huyu kwa jinsi alivyodhoofu.Akiwa kizimbani mara akagonganisha macho yake na mama yake akajikaza na kutabasamu.Si mbali sana na alipokaa mama yake akakutanisha macho na Happy .Happy akatoa tabasamu la kulazimisha lenye kuonyesha kukata tamaa.Macho yake yalikuwa yamevimba kwa kulia.
Akapata faraja kubwa baada ya kugundua kuwa ndugu zake wote walikuwa wamekuja kusikiliza hukumu yake.
Jaji kutoka mahakama kuu akaanza kusoma historia ya kesi na baada ya masaa matatu ukafika ule wakati mgumu kupita wote ,wakati wa jaji kuisoma hukumu..Happy moyo ulikuwa ukimwenda mbio.Mwili wote ulikuwa ukimtetemeka.Jasho lilikuwa likimtiririka.mama yake Patrik midomo ilikuwa ikimcheza kwa uoga .Kila mtu alikuwa akiuogopa sana wakati huu.Patrick yeye alikuwa ameinama akisali kimoyo moyo akimwomba Mungu ampe ujasiri wa kuweza kuipokea adhabu yoyote atakayopewa.
Mahakama iliridhika na ushahidi wa pande zote yaani upande wa mashtaka na upande wa utetezi.Kutokana na ushahidi uliotolewa na pande zote mbili mahakama ikaridhia kuwa Patrick alikutwa na hatia ya kuua bila kukusudia hivyo akahukumiwa kwenda jela miaka mitano.
Mara tu baada ya hukumu kusomwa Happy akazimia na kutolewa nje kwa ajili ya huduma ya kwanza.Mama yake naye alishindwa kujizuia na kuangua kilio baada ya kumwona mwanae akipakiwa katika gari tayari kwenda kuanza kukitumikia kifungo chake cha miaka mitano.Patrick akajikaza kiume asilie ingawa alikuwa amepatwa na mstuko mkubwa .
Gari lililowabeba mahabusu likaondoka mahakamani hapo na kuacha vilio vikiendelea.mama yake Patrick naye alikuwa amezirai.Ni tukio ambalo lilivuta hisia za watu wengi. Hatimaye Patrick akayaanza maisha mapya ya gerezani katika gereza kuu Iringa.
 
MISS TANZANA
SEHEMU YA 9
MTUNZI : PATRICK.CK

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
Mahakama iliridhika na ushahidi wa pande zote yaani upande wa mashtaka na upande wa utetezi.Kutokana na ushahidi uliotolewa na pande zote mbili mahakama ikaridhia kuwa Patrick alikutwa na hatia ya kuua bila kukusudia hivyo akahukumiwa kwenda jela miaka mitano.
Mara tu baada ya hukumu kusomwa Happy akazimia na kutolewa nje kwa ajili ya huduma ya kwanza.Mama yake naye alishindwa kujizuia na kuangua kilio baada ya kumwona mwanae akipakiwa katika gari tayari kwenda kuanza kukitumikia kifungo chake cha miaka mitano.Patrick akajikaza kiume asilie ingawa alikuwa amepatwa na mstuko mkubwa .
Gari lililowabeba mahabusu likaondoka mahakamani hapo na kuacha vilio vikiendela.mama yake Patrick naye alikuwa amezimia .Ni tukio ambalo lilivuta hisia za watu wengi.
Patrick alianza maisha mapya ya gerezani katika gereza kuu Iringa.

ENDELEA.....................

Tayari Patrick alikwisha kuyazoea mazingira ya gerezani humo.Hayakuwa mageni sana kwani amekwisha sota mahabusu kwa miaka kadhaa kabla ya kuanza rasmi kutumikia kifungo kwa hiyo hali nzima alikwisha ifahamu.na kuizoea.Tayari alikwisha zoeana na wafungwa wengi Wengi walimpenda kutokana na busara zake.Alikuwa ni kijana mdogo lakini mwenye busara za hali ya juu.Aliheshimika na kila mtu gerezani.
Kila mwishoni mwa wiki alikuwa akitembelewa na ndugu na jamaa zake.Happy ni mtu pekee ambaye hajawahi kukosa kila mwisho mwa wiki kuja kumtembelea mpenzi wake.Kufungwa kwa patrick bado hakukuwafanya watengane.Bado waliendelea kupendana kwa kiwango cha juu .Alijitahidi kwa kila alivyoweza kumwonyesha upendo wa pekee Patrick kwani aliamini yeye ndiye sababu kubwa kwa Patrick kuwapo pale gerezani.
mwaka wa kwanza ulikatika ukaanza wa pili na hatimaye Happy akamaliza masomo yake ya kidato cha sita.Pamoja na kumaliza masomo yake lakini bado alikuwa akiendelea kumtembelea na kumjulia hali Patrick kila mwisho wa wiki..Ilikuwa ni siku ya jumapili ,Happy alikuja kama ilivyo kawaida yake akiwa katika sura iliyoonyesha simanzi kubwa.Patrick akamshika mkono na kutaka kujua kitu kilichopelekea yeye Happy akawa katika hali ile.Huku akilia Happy akasema
“Patrick nashindwa kuelewa ni kwa nini kila wakati mimi ninakuwa katika majaribu makubwa.Niko katika majaribu makali sana Patrick” Happy akainama na kuanza kulia.
“Kwani kuna nini ? Hebu nieleze Happy ” Patrick akahoji
Happy akasita kidogo kisha akasema
“Baba amenitafutia Chuo nchini Marekani .natakiwa niende kuanza masomo katika chuo cha Howard university “
Kilipita kimya cha ghafla humo ndani.Wote wawili walizama katika lindi zito la mawazo.Patrick akahisi kitu kama kisu kinaukata moyo wake.Hakuwa ameota kama iko siku atakuja kusikia kitu kama hiki.Hii kwake ilikuwa ni taarifa yenye uchungu zaidi kuliko hata wakati ule alipokuwa akisomewa hukumu yake.Kidonda kilichokuwa kimeanza kupona kikatoneshwa .Patrick alishindwa kujizuia machozi yakamtiririka.Happy hakuweza kumwangalia Patrick usoni .Naye alikuwa akilia.
“ooh God why me every time?Why me? God What I have done that you cant forgive me? Why I’m always hurt? Am I not suppose to love?Am I ……..ooh !!!!!Patrick hakuweza kuendelea akainama chini.Happy ambaye alikuwa karibu yake akamshika bega na kumwinua shingo yake.
“Patrick nisikilize.Najua ni kwa kiasi gani habari hii imekuumiza.Ulivyoumia wewe na ndivyo hivyo hivyo nilivyoumia .Nimeumia sana Patrick.Na mpaka sasa kuna ugomvi mkubwa kati yangu na baba.Nimekataa kwenda Marekani.Siwezi kwenda na kukuacha hapa peke yako.I cant leave you alone Patrick.”
Patrick akageuza sura yake na kumwangalia Happy ambaye naye macho yake yalikuwa yamejaa machozi.Akatumia vidole vyake kumpangusa machozi kisha kwa sauti ya taratibui na upole akasema.
“Happy mpenzi wangu najua kuwa unanipenda sana .nafahamu pia kuwa unaelewa ni jinsi gani ninavyokupenda.Nafahamu haya yote yanayotokea hivi sasa ni majaribu tu ambayo iko siku yatapita na kutuacha sisi bado tunapendana.Nakuamini sana Happy na sina shaka yoyote juu yako kuhusu upendo wako kwangu.Sitaki Happpy ugombane au kushindwa kuelewana na wazazi wako kwa ajili yangu.Alichoamua mzazi ni kwa faida yako kwa siku za usoni. Kwa mantiki hiyo nakupa ruhusa ya kwenda kusoma Marekani.Mimi nipo na nitaendelea kuitumikia adhabu yangu hadi hapo nitakapomaliza.Natmai pindi ntakapomaliza adhabu yangu ,nawe utakuwa umemaliza au unakaribia kumaliza masomo yako na hivyo tutaungana tena na kuwa pamoja”
Patrick alitamka maneno haya ingawa moyoni alikuwa na uchungu mwingi.
Happy ambaye alikuwa amemshikilia Patrick akamwachia na kumtazama kwa mshangao
“Patrick are you out of your mind? Hivi kweli na wewe unakubali mimi niondoke na kukuacha hapa peke yako wakati uko hapa gerezani kwa sababu yangu???
Patrick akatabasamu na kumshika Happy mkono.
“Happy kama nilivyokwisha kueleza kuwa nakuamaini sana na wala sina wasi wasi wowote juu ya penzi lako kwangu.Uamuzi huo wa kwenda kusoma ni wa wazazi wako hivyo ni lazima tuuheshimu.Happy mimi ninafurahi kwa sababu unaenda kutengeneza msingi bora wa maisha yako na yetu kwa siku za usoni.Mimi nipo na siku zote nitakuombea na kukutakia mafanikio mema katika masomo yako.Ila naomba tu uniahidi kitu kimoja kuwa hutakuwa na mwanaume mwingine yeyote huko Marekani au kwingineko kokote zaidi yangu mimi.Niahidi kuwa utanisubiri mpaka nimalize adhabu yangu ili tuweze kutimiza ndoto zetu pamoja.”
Happy akatabasamu kisha akasema.
“Patrick nimekwisha kuahidi mara nyingi tu kuwa chini ya jua sintakuwa na mwanaume mwingine yeyote ambaye si wewe.Wewe ni wa kwanza na wa pekee.Na kuahidi hivyo .Nashukuru sana kwa kuridhia mimi nikasome Marekani .Naenda huko ingawa moyo wangu hautaki kabisa.Najua utabaki mkiwa kwa kunikosa.Pamoja na kwamba nitakuwa mbali nawe kimwili lakini moyo wangu naucha hapa kwako ubaki nao.”

***************

Pamoja na umbali mawasiliano kati ya Happy na Patrick yaliendelea kuwa mazuri.Happy alikuwa akiandika barua kwa Patrick kupitia kwa mkuu wa gereza na kisha soma Patrick hujibu na kumkabidhi mkuu wa gereza ambaye ndiye aliyejitolea kuhakikisha mawasiliano kati ya vijana hawa yanakuwa mazuri.Mkuu huyu wa gereza alisikia historia ya wawili hawa ikamgusa na kumfanya aahidi kuwasaidia kwa kila alivyoweza.. Chuoni Howard university Happy alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi wachache kutoka bara la Afrika .Alikuwa ni binti mpole kupita wote chuoni hapo na kwa muda mfupi aliweza kujulikana sana kwa upole wake.Muda mwingi alipenda kuwa peke yake katika sehemu tulivu.Hakupenda kujiunga na makundi ya wenzake na wala hakushiriki katika burudani yoyote ile.Mawazo yote yalikuwa Tanzania gerezani alikomwacha Patrick akitumikia kifungo chake.
Hali hii ilivuta udadisi mkubwa miongoni mwa wanafunzi wenzake.Wapo waliodhani labda ni hali ya ugeni,wengine wakadhanii labda ni uoga na wengine wakadiriki kumwita mshamba.
Siku moja profesa Adelin shawlight ambaye ndiye anayehusika na maendeleo na mienendo ya wanafunzi akamwita Michelle ,msichana anayeishi na Happy chumba kimoja na kumuhoji juu ya tabia za Happy
“Hata mimi nimekuwa nikijiuliza sana juu ya hali ya mwenzangu huyu.Toka tumefahamiana hatujawahi kuzungumza mambo yoyote zaidi ya salamu.Tunaishi chumba kimoja lakini mpaka leo hii sijui hata ametokea nchi gani.Akiwa chumbani huwa mkimya sana na kuna siku kama mara tatu hivi nimemkuta akiangalia picha Fulani huku akilia.Mi naona kuna jambo ambalo linamsumbua akili yake na pengine anahitaji msaada wa kisaikolojia zaidi
Profesa Adellin akakubaliana na Michele kuwa ni lazima kuna tatizo linalomsibu Happy na wakaweka nia ya kumsaidia ili aweze kuwa ni mtu mwenye furaha kama wenzake.
Siku moja jumapili Michelle akatembelewa na kaka yake aitwaye Mike cambell anayefanya kazi katika wizara ya mambo ya nje ya Marekani.Mike na Michelle ni watoto pekee kwa wazazi wao waishio katika jimbo la California.Michelle alimchukua Mike na kwenda naye hadi chumbani kwao wanakoishi yeye na Happy .Baada tu ya kuingia chumbani humo Mike akapigwa na butwaa baada ya kukutanisha macho na Happy ambaye alikuwa amejlaza kitandani akiwa na kompyuta yake ndogo.
“Wow how beautiful the gal is.Looks like a black angel…….”Mike akawaza.
“Hi “ Mike akamsalimu Happy .
“Hi “ Happy akajibu na kuendelea na shughuli zake.
Michele akafungua vinywaji toka katika friji lililokuwapo humo chumbani akamkaribisha Happy lakini akakataa.
Mike alikuwa akisumbuliwa na kitu moyoni mwake.Uzuri wa Happy ulikuwa umemstua sana.
Baada ya kuongea na dada yake akaomba aondoke .
“Bye baby” Mike Akamuaga Happy
“Bye” Happy akajibu bila hata kugeuza shingo yake
“Michelle hebu niambie yule mwenzio ametokea nchi gani?Akauliza Mike wakati wakishuka ngazi
“Mimi sijui .tangu tumekutana hatujawahi ongea lolote zaidi ya salamu.Ulivyomuona ndivyo alivyo vile vile.Haongei na mtu na wala hataki urafiki na mtu yeyote.Ni mkimya mno.Lakini nahisi kuna kitu kinachomsumbua”
“Michelle unakosea.” Akasema Mike
“Ki vipi Mike.”
“Wewe ndiye unayetakiwa kuwa karibu naye zaidi kwa sababu mnalala pamoja na hata kama tatizo likimtokea wewe ndiye utakayeweza kumsaidia.Wewe unatakiwa uwe mwenyeji wake hapa marekani.Pengine ni ugeni unaweza kuwa unamsumbua”
“Si ugeni Mike,nahisi kuna kitu anakificha.”
“sasa sikiliza Michelle,Jitahidi kwa jinsi yoyote ile kuwa naye karibu sana.Jitahidi uweze kumzoea na hapo ndipo utakapoweza kumsaidia.Nasikitika sana kumuona binti mrembo kama yule akiwa katika ukiwa wa namna ile”
“Mbona unaongea kwa msisistizo Mike ,kunani?
“Anavutia yule binti ,ningependa kumfahamu zaidi “
“kama ndio hivyo basi hakuna shida nitajitahidi sana niwe naye karibu.ili hata kama unamhitaji basi iwe rahisi.Hata hivyo ni binti mzuri hata mimi ananivutia sana kwa urembo wake.”
“Nitafurahi sana Michelle kama utafanikiwa kuwa karibu na binti yule.Utakuwa umenifanyia kitu kikubwa sana katika maisha yangu.”Mike akasisitiza.
“Usihofu kaka nitajitahidi “
Waliagana kisha Michelle akarudi chumbani kwao akiwa ni mwingi wa mawazo jinsi gani atakavyoanza kumzoea Happy msichana ambaye alikuwa hataki mazoea namtu yeyote yule.
Aliingia chumbani akajimiminia kinywaji katika glasi na kuanza kunywa huku akimtazama Happy kwa makini sana.
“Excuse me my dear sister” Michelle akajikaza na kumsemesha Happy ambaye bado alikuwa busy na kumpyuta yake
“Yes ,what’s up “ Akasema Happy bila kumuangalia Michelle.
“Sister unajua tangu tumepangwa kuishi wote katika chumba hiki hatujawahi kuongea hata siku moja,hatujawahi hata kufahamiana.Binafsi sipendezwi na staili hii ya maisha tunayoishi.Tuko katka chumba kimoja yatupasa tuishi kama ndugu,tupendane na kusaidiana.Mimi naitwa Michelle camblle natokea California.”
“Naitwa Happy Kibaho ,natokea Tanzania”
“Uuugh ! nafurahi sana kusikia unatoka Tanzania.I love Tanzanians.Nasikia ni watu wapole na wakarimu sana.mama yangu amewahi kwenda Tanzania kupanda mlima Kilimanjaro na aliporudi akatuhadithioa kuwa hajawahi kukutana na watu wakarimu kama watanzania.”
Happy akatabasamu .Ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Michelle kumuona happy akitabasamu.
“Happy you are so pretty.Unajua sikuwahi kukuangalia vizuri.You are amazing” Michelle akajibu na kumfanya Happy afurahi.
Huo ukawa ni mwanzo wa urafiki mkubwa kati ya Happy na Michelle.

****************

Urafiki kati ya Happy na Michelle uliendelea kuimarika siku hadi siku.Michelle alijitahidi kadiri alivyoweza kuwa karibu na Happy .Kila mwisho wa wiki walitoka na kwenda sehemu mbali mbali za starehe na kujiliwaza.Pamoja na mambo hayo yote ambayo Michelle alijitahidi kufanya ili kumfanya Happy awe na furaha lakini haikuweza kumsahauliasha kuhusu Patrick hata nukta moja.Alijitahidi kila awezavyo ili asiweze kumsahahu kijana huyu mwenye upendo wa ajabu kwake.
Ili tokea siku moja chuo kikafungwa kwa muda wa wiki mbili,Michelle akamuomba Happy wazitumie wiki mbili hizo kwa kuitembelea familia yao huko California.Happy akakubaliana na mwaliko huo na kesho yake wakapanda ndege na kuelekea California.Walipewa mapokezi mazuri na familia ya akina Michelle.Ilikuwa ni furaha iliyoje kwao kumpata mgeni aliyetoka Tanzania. .
Siku mbili tu baada ya kuwasili kwao hapo nyumbani ,Mike naye akawasili akitokea jiji la New York anakofanya kazi.Tayari alikwisha taarifiwa na mdogo wake Michelle kuwa tayari Happy alikuwa hapo nyumbani kwao.Mike aliwasili mida ya mchana na kuwakuta familia nzima ikiwa imejipumzisha.Akasalimiana na wote kisha akaelekea chumbani kwake.Kijasho kilikuwa kikimtiririka hasa baada ya kulishuhudia kwa mara ya kwanza tabasamu pana la Happy .Alikaa kitandani na kujaribu kuwaza ni jinsi gani atakavyoweza kujiweka karibu na binti huyu mwenye urembo ulotukuka.Alishindwa kupata jibu akaamua kwenda kuoga kisha akaelekea bustanini ambako Michelle na Happy walikuwa wamepumzika kwa muda huo.
Mara tu baada ya Mike kuwasili hapo bustanini ,Michelle akainuka na kwenda ndani kuongeza vinywaji,akawaacha Mike na Happy .Mike moyo ulikuwa ukimdunda .Ilihitaji ujasiri wa aina yake kuanzisha maongezi na binti huyu mwenye uzuri wa malaika.Baada ya kimya cha sekunde kadhaa toka amefika pale Mike akajikaza kiume na kuanzisha maongezi.
“Happy unanikumbuka?”
:Happy akanyamaza kidogo kana kwamba anajaribu kukumbuka kitu kisha akajibu.
“hapana”
“Nilikuja siku moja chuoni kweni nikakukuta uko busy na kompyuta yako”
“Oooh ! sasa nimekukumbuka.kumbe ni wewe ! Samahani siku ile sikuwa katika hali nzuri ndio maana sikukujibu vizuri.”
“Its’s ok Happy.hata mimi nilijua haukuwa katika halinzuri kwa sababu siku hazifanani.” Mike akasema huku akatabasamu baada ya kumuona Happy akitabasamu
“Vipi unaionaje hali ya Marekani”Mike akauliza
“Mhh ni nzuri,Marekani kuzuri,kila kitu kizuri ,but I miss home”
“Tanzania? Mike akauliza
‘Yes ! nani kakwambia kuwa natokea Tanzania?
‘Michelle” Mike akajibu .Happy akatabasamu
“Hata mimi” Mike akaendelea “naipenda sana Tanzania.Nasikia ni nchi ya amani na watu wake ni wakarimu mno.”
“Nafurahi kusikia hivyo.Umekwisha wahi tembelea nchi yoyote ya Afrika?
“Hapana bado ila nina mpango wa kufanya ziara Afrika na nchi ya kwanza kutembelea itakuwa Tanzania.”
“Nini kinakuvutia mpaka uifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza kuitembelea? Happy akauliza
“Just to see pretty women” Mike akajibu na wote wakaangua kicheko.
Ilikuwa ni wiki nzuri sana kwa Happy .Alifurahi kukutana na familia yenye watu wakarimu kama hii ya akina Michelle.Kwa kiasi Fulani ziara hii ya California ilisaida kumuondolea msongo wa mawazo uliokuwa ukimkabili.Mike na Michelle walijitahidi kwa kila walivyoweza kuhakikisha kuwa Happy anakuwa na furaha kwa muda wote atakaokuwa hapo kwao.
Jumapili Mike akamuomba Happy watoke kwa ajili ya matembezi.Michelle alikuwa hajisikii kutoka.Jioni ya siku hiyo wote wawili wakiwa wamependeza vilivyo walipanda gari na kutoka.Safari iliishia katika klabu moja kubwa na maarufu .Ilikuwa ni sehemu tulivu na yenye mandhari ya kuvutia mno.Waliagiza vinywaji na kuanza kunywa taratibu.
“Happy leo ni siku ya furaha sana kwangu kuwa karibu nawe katika mahali tulivu kama hapa na ni siku muhimu vile vile kwa kuwa nimedhamiria kuutua mzigo mzito unaonikabili kwa muda mrefu sasa”
Happy akastuka kidogo lakini akamuacha Mike aendelee.
“Happy nina furaha moyoni mwangu kukutamkia kuwa u mwanamke pekee ambaye umeweza kuuteka moyo wangu kwa kiasi ambacho siwezi elezea.Kwa ufupi Happy nakupenda sana na tafadhali ninaomba uridhie ombi langu la mimi na wewe kuwa wapenzi.Naomba unielewe Happy kuwa penzi langu kwako ni la dhati lenye lengo la kuja kuishi nawe kama mume na mke pindi utakapomaliza masomo yako.”
Happy akaiweka glasi chini ,akamuangalia Mike kana kwamba ni mara ya kwanza anamuona.Mike naye akamuangalia Happy kwa makini Happy akatabasamu ,tabasamu ambalo kwa kiasi kikubwa linamchanganya Mike.
“Mike you are very handsome” Happy akasema
“Oh ! thank you Happy” mike akasema huku akitababasamu na kuirekebisha tai yake aliyokuwa amevaa.
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 10
MTUNZI: PATRICK CK
CONTACT: 0764294499

ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
“Happy nina furaha moyoni mwangu kukutamkia kuwa u mwanamke pekee ambaye umeweza kuuteka moyo wangu kwa kiasi ambacho siwezi elezea.Kwa ufupi Happy nakupenda sana na tafadhali ninaomba uridhie ombi langu la mimi na wewe kuwa wapenzi.Naomba unielewe Happy kuwa penzi langu kwako ni la dhati lenye lengo la kuja kuishi nawe kama mume na mke pindi utakapomaliza masomo yako.”
Happy akaiweka glasi chini ,akamuangalia Mike kana kwamba ni mara ya kwanza anamuona.Mike naye akamuangalia Happy kwa makini Happy akatabasamu ,tabasamu ambalo kwa kiasi kikubwa linamchanganya Mike.
“Mike you are very handsome” Happy akasema
“Oh ! thank you Happy” mike akasema huku akitababasamu na kuirekebisha tai yake aliyokuwa amevaa.

ENDELEA...............................

“ Mike wewe ni mtu ambaye kila mwanamke angependa uwe naye.Una kila sifa za kijana bora.U mcheshi,mchangamfu na unayevutia.Nashukuru kwa kuwa wazi na hisia zako.Ila samahani kaka yangu mimi tayari nina mtu ambaye sijui hata nielezeje ili unielewe kwamba ninampenda Kijana huyu ndiye aliyeyashika maisha yangu.yeye ni kila kitu kwangu.Nampenda Patrick kuliko ninavyojipenda mimi.Kama nisingekuwa Patrick nisingekukataa Mike.” Happy alisema kwa kujiamini.
Mike akainama chini kwa sekunde kadhaa akiwaza.tayari alikwisha uona ugumu uliopo mbele yake.katika kumshawishi Happy akubali ombi lake la kuwa naye katika mahusiano.
“Happy naheshimu mawazo yako na ninauheshimu sana uhusiano wa mtu.Si lengo langu kuvuruga uhusiano wako.Kwa kuwa tayari una mpenzi anayekupenda na wewe unampenda basi naomba kitu kimoja tu kutoka kwako.”
“Kitu gani hicho” Happy akauliza
“ nataka tuwe marafiki wa kawaida”
“Kwa hilo Mike hakuna shida.nashukuru sana kwa kunielewa.Nitakuombea ili uweze kumpata msichana kama mimi ambaye nina imani utampenda zaidi yangu.”
“nafurahi kusikia hivyo Happy ” Mike akasema katika hali ya unyonge.
Maisha yaliendelea vizuri na baada ya wiki mbili kumalizika Michelle na Happy wakarudi chuoni Mike akarejea kazini kwake New york

*****************

Maisha gerezani yaliendelea kama kawaida.Siku moja Patrick akaitwa na mkuu wa gereza na kuambiwa ajiandae kwa safari alikuwa akihamishwa gereza.Hii ilikuwa ni taarifa ambayo ilimvunja moyo sana kiasi cha kumfanya adondoshe machozi.Ni wafungwa watatu tu ndio waliokuwa wakihamishwa.
Haikuweza kufahamika mara moja sababu ya kuhamishwa kwao Wakati wakijiandaa na kuondoka ,hakukuwa na mfungwa mwingine wa karibu ambaye angeweza kumwachia ujumbe wowote.Hakujua anahamishiwa gereza gani.Alimkumbuka Happy na kulia sana.Alizoea kila wiki kupokea barua za Happy .Hakujua angewezaje kumfahamisha juu ya uhamisho ule wa ghafla.
Safari ilianza bila kuchelewa .ILikuwa ni safari ndefu na yenye kuchosha.Gari walilopanda lilikuwa na madirisha madogo juu kwa ajili ya kuingiza hewa .hivyo kutokutambua ni wapi walikokuwa wakielekea.
Wakiwa wamepitiwa na usingizi walistuliwa na sauti ya kufunguliwa kwa mlango.Walifunguliwa pingu walizokuwa wamefungwa mikononi na kuamriwa kushuka.Walikuwa wamechoka kupita kiasi.Ilikuwa ni safari ndefu na njaa ilikuwa ikiwauma kupita maelezo.Tangu wapewe chakula mchana ambacho kilikuwa ni chipsi kavu na maji ya kunywa hawakula tena chochote.
Tayari giza lilikwisha tanda angani.Hawakujua ilikuwa ni saa ngapi mida hiyo.hali ya mahala hapo ilikuwa ni ya baridi kali.Wote walikuwa wakitetemeka.Walisimamishwa hapo kwa takribani dakika ishirini kisha askari mmoja ambaye alionekana kuwa na cheo akatoka ndani akawaangalia na kuamuru wapelekwe ndani wakapumzike.Waliongozwa na askari wawili wenye silaha hadi ndani ya gereza.Kila mmoja akaonyeshwa chumba chake cha kulala.Hili lilikuwa ni gereza jipya kabisa na la kisasa lililokuwa limejengwa mjini songea kwa msaada wa watu wa Marekani.Lilikuwa ni gereza la kwanza nchini Tanzania kuwa na ubora wa hali ya juu.Patrick alishukuru Mungu kwa kuletwa hapa .Kutokana na uchovu wa safari aliokuwa nao akajitupa kitandani na kulala.
Saa kumi na mbili asubuhi king’ora kikalia .Patrick mwili wote ulikuwa ukimuuma kwa uchovu na alihisi njaa kali.
“Hey amka best” Akastuliwa na sauti ya mtu aliyekuwa akimtikisa.Akafumbua macho na kukutana na macho ya kijana mdogo mwenye sura ya upole.
“Vipi husikii king’ora hicho?” Akaendelea kusema yule kijana.
Kiuvivu Patrick akainuka na kukaa kitandani.baada ya kama dakika tatu hivi alikuja askari akafungua geti la chumba chao na kumrushia Patrick nguo mpya kabisa za kifungwa.Hakusema kitu akazikunjua na kuvaa .
“Kwa hiyo nini kinaendelea saa hizi? Utaratibu wa hapa ukoje ?” Patrick akamuuliza yule kijana waliyekuwa wakilala wote chumba kimoja.
“huu ni muda wa kujiandaa,kunawa au kuoga kama unataka .Kitapigwa king’ora kingine tutaenda kupata mlo wa asubuhi halafu baada ya hapo tutapangiwa kazi.”
Patrick akaonyeshwa sehemu yenye mabafu akaingia na kujimwagia maji baridi.King’ora kingine kikalia na wote wakakusanyika katika bwalo la chakula kwa ajili ya kifungua kinywa.i.Walikuwa wafungwa wachache kama arobaini hivi.
Baadaye kazi zikapangwa na Patrick na wenzake wakapangiwa sehemu ya kufyeka.Miongoni mwao alikuwemo yule kijana anayelala naye chumba kimoja.Walifanya usafi huku wakisimuliana mambo mengi na kupeana moyo.taratibu wakaanza kuzoeana na kujenga urafiki.
Usiku wa siku hiyo Patrick na yule kijana ambaye alikuja kumfahamu kama Andrew waliutumia katika kusimuliana mikasa mbali mbali ya maisha yao.Andrew alimsimulia Patrick kisa cha yeye kuwapo pale gerezani.Kifungo chake kilikuwa cha miaka mitatu na kilitokana na kusababisha ajali wakati akiendesha gari huku akiwa amelewa.
Patrick naye alimsimulia hadithi yake na mpaka anamaliza Andrew alishindwa kujizuia kudondokwa na mchozi.
“Pole sana Patrick hayo yote ni majaribu katika maisha .Ni wazi Patrick una upendo wa dhati na wapekee sana kwa huyo Happy .Usikate tama Mungu atakusaidia utamaliza kifungo chako.”
“Ahsante sana Andrew kwa kulitambua na kunipa moyo.Lakini kitu ambacho bado kinaniumiza sana kichwa ni jinsi nitakavyoweza tena kuwasiliana na Happy .Katika gereza lile nilikotoka ,mkuu wa gereza alikuwa amejitolea kunisaidia kwa kutuma barua zangu kwenda kwa Happy na kupokea zitokazo kwa happy na kuniletea..Ningeweza kuwatumia wazazi wangu lakini bado hawajui kama nimehamishwa gereza
“Usijali Patrick .Mimi binamu yangu atakuja wiki ya kwanza ya mwezi ujao kuja kuniona .Hivyo tutamtumia huyo ataenda kuposti barua kwenda kwa Happy na utamuelekeza happy kuwa umehamishwa gereza. na hata kama ukipenda majibu yapitie kwake itakuwa sawa tu..Nina imani hata Happy naye atakuwa anasononeka sana kwa kukosa barua zako.Ila hilo lisikupe shida sana kwani bado miezi minne nimalize kifungo changu hivyo nikiwa uraiani nitakusaidia katika suala la mawasiliano kati yako na Happy. “ Akasema Andrew.

*****************

Siku moja Patrick akapangiwa kwenda kufanya usafi katika nyumba ya mkuu wa gereza.Huko alipangiwa kufyeka na kurekebisha viunga vya maua .
Katika dirisha lililoelekea upande wa mbele ya nyumba dada mmoja mrembo sana alikuwa amekaa mkono shavuni kwa takribani dakika kumi na tano akimuangalia Patrick bila yeye kujua kama alikuwa akiangaliwa.Alistaajabu kwa kumuona kijana kama yule ambaye kwa mbali tu alionekana ni kijana mpole,mtaratibu na mwenye kuvutia ,akiwa gerezani.
“ama kweli jela haina mwenyewe.How such a handsome guy be in prison?.Alifanya nini kijana yule i? Mhh ! hebu mwangalie vizuri halafu anaonekana ana mawazo mengi.Namuonea huruma mhh…..jamani ..” Akawaza mwanadada yule.
Dada yule akaenda jikoni na kutengeneza chai akaweka katika sinia akabeba na kuelekea mahali alipokuwa Patrick.
“kaka habari za kazi? Patrick akastushwa na sauti tamu,laini ya mwanadada.Akageuka na ghafla akajikuta akiangusha fyekeo.Macho yake yakakutana na binti ambaye uzuri wake wa asili ulikuwa unasisimua.Hakuamini kama angeweza kukutana na binti mrembo vile maeneo yale.
“Pole na kazi “ Alisema tena binti yule baada ya kuona Patrick akimuangalia tu bila kusema kitu.
‘Nzu…r..rii tu dadangu” Akajibu.
“pumzika basi walau upate kikombe cha chai kwani toka asubuhi nakuona ukiwa unachapa kazi”Alisema yule dada akamkaribia Patrick na kuweka lile sinia chini.
“Nashukuru sana dadangu lakini naogopa mkuu akinikuta hapa patakuwa hapatoshi”
“Usihofu kaka yangu ,mjomba hayupo amekwenda Dar leo asubuhi na hata mkewe naye hayupo atarudi kesho”akajibu yule dada
Patrick anamkazia macho yule dada baada ya kusikia kauli ile.”Ina maana binti huyu ni mjomba wake na mkuu wa gereza?Mhh si mwanae huyu?Du si mchezo mtoto ameumbika vilivyo.Ananikumbusha sana mpenzi wangu Happy .”
Patric hakujivunga tena akaa chini na kunawa mikono
“Karibu” yule dada akamkaribisha
“Ahsante lakini mbona kikombe chenyewe ni kimoja?we hunywi? Patrick akauliza
“Usijali kakangu mi tayari hii ni kwa ajli yako”
Patrick akaanza kunywa chai ile nuri .Akamaliza kikombe cha kwanza na kuongeza tena cha pili na hatimaye cha tatu.Kimoyo moyo alimshukuru sana yule dada mrembo kwa chai ile kwani ni wazi alihisi njaa kali asubuhi hiyo.
Wakati Patrick akinywa chai ile,yule dada aliingia ndani na kwenda kukaa katika lile dirisha akiendelea kumwangalia Patrick.
“Anateseka kaka huyu.Namuonea huruma kweli.Halafu mpole.Sijui alifanya kosa gani huyu kaka manake haonekani kama mhalifu “ Akawaza yule dada
Patrick akamaliza kunywa chai akakusanya vyombo na kwenda kugonga mlango.Yule dada akafungua mlango na kuvipokea.
“Ahsante sana dada Mungu akubariki” Akasema Patrick
Patrick akaendelea na kazi yake yake ya usafi .Kila dakika taswira ya yule dada mpole mwenye roho ya huruma ilikuwa ikimjia na kumfanya atabasamu.”Kumbe duniani bado kuna watu wenye upendo “ Akasema taratibu huku akiendelea na kazi yake ya kurekebisha bustani ya maua. Imezoeleka katika jamii yetu kila mfungwa ni mnyang’anyi
hivyo kufanya wafungwa kutokuthaminiwa,kutokuhurumiwa,na hata kutokusaidiwa lakini bado wako watu wachache wenye huruma na upendo kwa wafungwa kama huyu dada alivyofanya leo.Aliwaza Patrick.Wakati akiendele na usafi dada yule akatoka tena na kisinia kilichokuwa na glasi mbili za juice.
“Kaka karibu upumzike upate juice”
Patrick aliingiwa na wasiwasi iwapo wakuu wake wangekuja na kumkuta amekaa .
“ahsante sana dadangu ila naogopa iwapo hawa wakuu wetu watakuja na kunikuta nimekaa nakunywa hiyo juice” Patrick akasema huku akiwa na wasi wasi lakini ni wazi alikuwa akiitamani sana juice ile.Huku akitabasamu dada yule akasema
“Usihofu kaka nimekwambia mjomba wangu hayupo na hata mkewe hayupo kaenda Iringa .Hapa nipo mimi tu .Kaa upumzike kaka yangu unajua upatapo nafasi ya kufanya usafi katika nyumba hizi za wakuu ndio nafasi yako ya kupumzika.Kazi zenu ni ngumu sana” Akasema dada yule
“Ni kweli usemayo dada yangu lakini inategemea na mahali penyewe.Unajua kwa sisi wafungwa jamii inatuchukulia kama wote ni wanyang’anyi kumbe sivyo.Nimekuwa nikifanya usafi katika baadhi ya nymba za maafisa wakubwa na wadogo lakini hakuna hata siku moja niliyowahi kupewa hata glasi ya maji.Lakini kumbe kuna watu wana roho za utofauti sana na mmoja wao ni wewe.U mkarimu sana dada yangu.”
Taratibu Patrick akajikuta akikaa chini kwenye bustani huku ameikamata glasi ya juice.Juice kama hii alizowea kuipata wakati Happy hajaondoka.Siku hii ya leo inamkumbusha mbali sana.Alishindwa kuyazuia machozi kudondoka mara alipomkumbuka Happy
“Vipi kaka yangu mbona unalia?
“Unajua Juice hii imenikumbusha mbali sana”
“Basi usilie kaka yangu Mungu yupo na atakusaidia uweze kumaliza kifungo chako”
Kilipita kimya cha seunde kadhaa Patrick akauliza
“lakini dada yangu inaonyesha wewe si mwenyeji kabisa wa maeneo haya”
Huku akitabasamu dada yule akajibu
“kwa nini unasema hivyo”
“Inaonyesha tu.Mwonekano wako haufanani kabisa na mazingira haya”
Dada yule akacheka kicheko kikubwa kisha akajibu.
“Una uwezo mkubwa wa kuweza kumsoma mtu na kumwelewa kwa haraka.Ni kweli mimi si mwenyeji wa hapa .Mi naishi Dar es salaam.Mzee Joel mkuu wenu wa gereza ni mjomba wangu na nimekuja mara moja kumletea mizigo yake iliyotumwa na dada toka Ulaya.Ingawa sintakuwa na muda mrefu hapa lakini nimetokea kupapenda sana.Pana hewa nzuri na nimazingira tulivu sana.”
Alitulia kidogo akanywa mafunda mawili ya Juice kisha akaendelea.
“ Kwa jina naitwa Veronika .Veronika Rugi sijui kaka wewe unaitwa nani?
Patrick akanyamaza na kutafakari iwapo amweleze jina lake au vipi.Mwishowe akaamua kumtajia jina lake
“Naitwa Patrick “
“Uh ! nafurahi sana kukufahamu Patrick.Unajua toka nimekuona asubuhi ukifanya usafi moyo wangu haukutulia kabisa.Nilikuwa na hamu sana ya kutaka kukufahamu.U mpole sana na haufanani na wafungwa wengine”
Patrick akacheka.
“Kweli kabisa patrick,haufanani na wafungwa tuliozoea kuwaona.Mtu yeyite akikuona mara moja atahisi kuwa uliingizwa gerezani kimakosa.Sura yako haioneshi kuwa unaweza ukafanya kosa katika jamii ambalo lingepelekea wewe kufungwa gerezani”
Patrick akacheka tena na safari hii kicheko kikubwa zaidi,Vero akatabasamu.
“Patrick nitafurahi sana kama utaungana nami kwa chakula cha mchana leo hii.Unajua niko mwenyewe hapa nyumbani na kama ujuavyo chakula cha peke yako katu hakina utamu”Akasema Vero
“Hamna shida Veronika “Patrick akajibu .Alikwisha anza kumzoea binti yule mrembo.Veronika akamkaribisha Patrick ndani sebuleni na kumuwashia Tv kisha yeye akaelekea jikoni kuandaa chakula.Patrick alijisikia faraja kubwa kwa kukalia tena sofa nzuri kama zile.
“Du ! Veronika ni binti mzuri ,mrembo mwenye kila sifa inayohitajika kwa binti mrembo .Ni mwelewa na ana huruma sana.Nafurahi kukutana na binti huyu japo kwa muda mfupi.Nina imani vile vile anaweza kunisaidia kurejesha mawasiliano kati yangu na Happy .
Patrick akastuliwa kotoka katika mawazo mazito na sauti ya Vero
“Hello Patrick ,mbona unaonekana mnyonge hivyo?Usihofu .Unaonekana umezama kwenye dimbwi la mawazo.Just relax.Hakuna mtu atakaye kuja kukusumbua.Pumzika mpaka muda wa kurudi ndani utakapofika.”
“Ahsante Vero,nashukuru sana dada yangu”
Waliongea mambo mengi na kujikuta wakifahamiana na kuzoeana zaidi.Patrick alimsimulia Vero hadithi nzima ya maisha yake inayomfanya Veronika atokwe na machozi.
Hatimaye muda ukafika kwa wafungwa kurejea gerezani wakaagana huku Vero akiahidi kufanya kila njia ili waonane kabla hajaondoka kurudi Dar.

******************

Ulikuwa ni usiku mgumu sana kwa Vero.Hakujua ni kwa nini Patrick alikuwa ameingia moyoni mwake kwa kasi ya ajabu namna ile.
“Sielewi ni kwa nini Patrick amenigusa ghafla hivi .Ni kijana mpole ,mtaratibu na mwenye kuvutia hata akiwa katika mavazi ya kifungwa.Namuonea huruma sana Patrick nitajitahidi niweze kumsaidia katika kipindi chote atakachokuwepo gerezani.Namwonea wivu huyo Happy kwa kumpata kijana mwenye upendo wa dhati kama Patrick.Toka nimezaliwa sijawahi kuguwa moyo wangu na kijana yeyote kama alivyonigusa leo Patrick na hadithi ya maisha yake.Ni mapenzi mazito aliyonayo kwa Happy ndiyo yaliyopelekea mpaka kijana wa watu anasota gerezani.Natamani kama angekuwa ni mpenzi wangu.Ningejitahidi kwa kadiri niwezavyo kuweza kumfanya mwenye furaha daima.I’m real dreaming for a man like Patrick.Ana karibu kila kitu ninachokihitaji kwa mwanaume wa ndoto zangu.Lakini mhh…wait…are my feelings ok? Mbona naanza tena kuwaza mambo ya ajabu ajabu?Ni kwa nini siwezi kupitisha hata dakika moja sijamuwaza? Mhh nahisi tayari ameanza kuingia moyoni mwangu taratibu.Ooooh My God help me with these feelings.Ae they right?”Veronika akawa katika mawazo mazito
“Ingekuwa ni mimi ndiye niliyepelekea Patrick akafungwa nisingekubali kabisa kwenda Ulaya na kumwacha mtoto wa watu akiteseka gerezani peke yake.Stupid girl Happy .nitafanya kila niwezalo ili Patrick awe ni mtu mwenye furaha daima.Nitahakikisha anakuwa msafi,anakula vizuri na kupata raha zote.Mkuu wa gereza ni mjomba wangu.Nitamweleza ukweli ili aweze kunisaidia.Nitamuomba kila siku Patrick awe akipangiwa kufanya kazi kwa mkuu wa gereza ili aweze kupata nafasi ya kula vizuri na kupumzika.
Wakati Veronika akiwa katika wakati mgumu kwa mawazo usiku huo hali haikuwa nzuri sana kwa upande wa patrick .Mchana wa siku hiyo ulimkumbusha mbali sana.Ulimkumbusha kipindi alichokuwa katika mapenzi mazito na Happy . Alizikumbuka nyakati zile za furaha alizokuwa nazo .alihisi kuhitaji furaha ile tena.
Ghafla ikaja picha ya Veronika akiwa na sinia lenye chai .Akakumbuka toka wakati akinywa chai ile na Vero na jinsi alivyokula chakula kitamu siku hiyo .
“Mhh haya ni majaribu makubwa sana” Akawaza
“Bado nampenda sana Happy lakini mbona Veronika naye anakuja kwa kasi sana katika mawazo yangu.Mhh hapana labda ni kwa ajili ya ule ukarimu wake.Unajua toka nimefungwa sijawahi kukutana na binadamu ambaye si mtu wangu wa karibu mwenye roho ya huruma na upendo kama Veronika.Veronika hatofautianai sana na Happy .Nahisi hii ni sababu inayonifanya niwe nikimuwaza sana kwa sababu kila nikimkumbuka namkumbuka Happy
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 11
MTUNZI :pATRICK.CK
CONTACT: 0764294499
ILIOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
Wakati Veronika akiwa katika wakati mgumu kwa mawazo usiku huo hali haikuwa nzuri sana kwa upande wa patrick .Mchana wa siku hiyo ulimkumbusha mbali sana.Ulimkumbusha kipindi alichokuwa katika mapenzi mazito na Happy . Alizikumbuka nyakati zile za furaha alizokuwa nazo .alihisi kuhitaji furaha ile tena.
Ghafla ikaja picha ya Veronika akiwa na sinia lenye chai .Akakumbuka toka wakati akinywa chai ile na Vero na jinsi alivyokula chakula kitamu siku hiyo .
“Mhh haya ni majaribu makubwa sana” Akawaza
“Bado nampenda sana Happy lakini mbona Veronika naye anakuja kwa kasi sana katika mawazo yangu.Mhh hapana labda ni kwa ajili ya ule ukarimu wake.Unajua toka nimefungwa sijawahi kukutana na binadamu ambaye si mtu wangu wa karibu mwenye roho ya huruma na upendo kama Veronika.Veronika hatofautianai sana na Happy .Nahisi hii ni sababu inayonifanya niwe nikimuwaza sana kwa sababu kila nikimkumbuka namkumbuka Happy .

ENDELEA.....................

Urafiki kati ya Patrick na Veronika ulikua kwa kasi sana.Vero kwa kupitia mjomba wake ambaye ndiye aliyekuwa mkuu wa gereza alihakikisha kuwa patrick anapangiwa kufanya kazi mbali mbali nyumbani kwa mkuu wa gereza.Joel armendo mkuu wa gereza hilo aligundua urafiki mzito ulioanza kujengeka baina ya Patrick na veronica .Baada ya kuligundua hilo mara moja akaanza kufanya uchunguzi juu ya kijana huyu ambaye jarada lake linaonyesha kuwa alihukumiwa kifungo kutokana na kesi ya kuua bila kukusudia.Hakuridhika sana na maelezo yale siku moja akamwita Patrick ofisini kwake na kuanza kumuhoji mambo kadhaa ikiwa ni pamoja na kutaka kufahamu historia kamili ya Patrick.Hadithi ya Patrick ilimkuna sana Joel na kufungua ukurasa mpya.Alimpenda sana kijana huyu hasa kutokana na tabia yake nzuri na kujituma.Familia nzima ya Joel Armando ilitokea kumpenda Patrick na kadiri siku zilivyozidi kwenda taratibu wakaanza kumhesabu kama mmoja wa wanafamilia.Kila siku alishinda nyumbani kwa mkuu wa gereza na kusaidia kazi mbali mbali mpaka muda wa kurudi gerezani ulipowadia.Hakuhitaji tena kusimamiwa .Alikuwa ni mfungwa ambaye alitokea kuaminiwa mno siyo tu na wakuu tu bali hata wafungwa wenzake na askari magereza wote.
Urafiki na ukaribu baina ya Patrick na Veronika ukaongezeka maradufu.Veronika alifurahi mno kwa ukaribu ule kiasi kwamba hakuwa na hamu hata ya kurudi nyumbani kwao Dar es salaam..Mama yake akashangaa sana kwa binti yake kuchukua muda mrefu namna ile kurudi nyumabni wakati makubaliano yalikuwa akae wiki mbili tu lakini sasa ni wiki ya tatu.Akaamua kumpigia simu kaka yake ambaye ndiye mjomba wa Vero na kumwomba amwambie Vero arudi haraka sana dare s salaam kwani shughuli nyingi zilikuwa zikimsubiri.Veronika ndiye msimamizi mkuu wa miradi na shughuli zote za familia yao.Veronika alilia sana usiku huo kwa kuachana na Patrick kijana ambaye tayari alikwisha mzoea kwa kiasi kikubwa na alikuwa na matumaini makubwa ya kuwa iko siku Patrick angebadili mawazo yake kwa Happy na kumpenda yeye.
Siku iliyofuata alimweleza Patrick kuwa mama yake anamwitaji arudi Dar mara moja.
“Usihofu Patrick pamoja na kwamba ninaondoka lakini nitajitahidi walau kila mwisho wa mwezi niwe nakuja hapa kukutazama.Niambie kitu kimoja Patrick..”
“kitu gani hicho Veronika” Patrick akauliza
“Will u miss me ?! “
Patrick akatabasamu ,akamsika mkono Vero na kusema.
“ Very much.I’ll miss you very much Veronika”
Veronika akatoa tabasamu pana sana baada ya kusikia kauli ile.
“Lakini usijali kama nilivyokwambia nitajitahidi kuja mara kwa mara kukuangalia.Isitoshe familia ya mjomba ipo nawe hivyo hutajisikia mkiwa hata kidogo na hapa kuna simu nitakuwa nakupigia kila siku tunaongea .Nadhani hutanimiss sana”
“Vero usijali sana .Unajua toka siku ya kwanza tumeanza urafiki nilijua tu iko siku utaondoka.Tayari nilikuwa nimekwisha jiweka tayari kwa hilo.Usihofu chochote juu yangu,mimi nimekwisha zoea kuumia.Siyo siri Vero kuondoka kwako ni jeraha jingine kubwa katika moyo wangu.Umekuwa mtu wangu wa karibu sana na kunifanya nisahau mateso na mchungu yote ya gereza japo kwa muda mfupi……………..”Patrick akasema
“Patrick najua una uchungu sana kwa mimi kuondoka.Hata mimi ninaumia vile vile kwa kukuacha peke yako hasa katika kipindi kama hiki ambacho ni wazi unahitaji sana mtu wa kukufariji na kukupa moyo.Lakini usijali nitarudi .”
“Nimekuelewa Vero.Ila naomba unisaidie kitu kimoja”
“Kitu gani hicho Patrick niambie niko tayari kukusaidia”
“Kama unavyofahamu kuhusu kinachoendelea baina yangu na Happy .Nina imani Happy hajui kama nimehamishwa gereza.Wazazi wangu pamoja na mkuu wa gereza nilikotoka ndio waliokuwa na kazi ya kuniunganisha na Happy lakini mpaka sasa hivi hawajaja kunitazama.Kwa hiyo sifahamu nini kinachoendelea.Ninachohitaji toka kwako ni msaada wako ili niweze tena kuwasiliana na Happy .Nitaandika barua na kumweleza Happy kila kitu na nitaomba ukanisaidie kuiposti kwa haraka.”
Akionyesha uso wa furaha Veronika akajibu
“Usihofu Patrick .Nimekwisha kueleza toka awali kuwa nipo kwa ajili yako,hivyo usisite kunituma jambo lolote lile na nitakusaidia kwa uwezo wangu wote”
Siku hiyo Patrick akaandika barua ndefu na kumfahamisha Happy juu ya uhamisho wake na kuzidi kumsisitiza juu ya ahadi zao walizowekeana..
“Kazi kubwa bado ninayo” Aliwaza vero usiku kabla ya siku ya kuondoka kwake.
“Ninampenda Patrick lakini bado inaonyesha mapenzi yake yako kwa Happy .Mapenzi yao ni ya dhati kabisa.Ni ndoto yangu ya siku nyingi ya kumpata kijana mwenye mapenzi ya kweli kama Patrick.Hata hivyo bado sikati tamaa.Happy yuko mbali na mimi niko karibu na Patrick nani alisema fimbo ya mbali inaua nyoka? Kwa kuwa ninampenda Patrick nitapambana .Kwanza ni lazima niuvuruge uhusiano huu wa Patrick na Happy baada ya hapo utazaliwa uhusiano mpya kati ya Patrick na veronica.”
Kwa hasira akaifungua barua ile aliyopewa na Patrick ili akaiposti kwenda kwa Happy akaanza kuisoma.alipomaliza akairudia tena na tena.Ilikuwa ni moja kati ya barua zenye msisimko wa hali ya juu.
“Siwezi kuituma barua hii.Maneno aliyoyaandika humu yanaweza kumfanya mgonjwa aliye mahututi kupona ghafla.Ni maneno yenye mahaba mazito.I deserve a guy like him.He must be mine.” Vero akasema mwenyewe kwa hasira huku akiichana katiikati ile barua aliyopewa na patrick.

******************

Ni siku moja tu tangu Veronika aondoke ,Patrick akatembelewa na wazazi wake.Ilikuwa ni siku ya furaha kubwa mno .Aliruka na kufurahi,alitamani kama Vero ngekuwepo ili awafahamu wazazi wake.
Kitu kikubwa ambacho alikitarajia na kukisubiri kwa hamu ni iwapo kulikuwa na barua yoyote toka kwa Happy .Aliamini wazazi wake watakuwa wamekuja na barua kwa sababu kimepita kipndi kirefu sasa toka alipopokea barua ya happy kabla hajahamishwa gereza..Patrick hakupoteza muda akauliza iwapo wamekuja na barua yoyote toka kwa Happy .Baba yake akajibu kwa masikitiko
“Patrick ninasikitika kukwambia kuwa nilipata uhamisho wa ghafla wa kwenda Dar es salaam na ndiko tunakoishi kwa sasa.Toka tumehama hatujapata mawasiliano yoyote toka kwa Happy .Kama atakuwa ametuma barua basi zitakuwa zimetua katika mikono ya watu wengine.Nasikitika vile vile kwa kutomfahamisha juu ya kuhama kwetu ili asiendelee kutumia anwani ile tuliyokuwa tukiitumia awali “.
Patrick akainama kwa sekunde kadhaa akitafakari.
“Oh My God” Akajikuta akitamka kwa nguvu.Alihisi ni kama kitu chenye ncha kali kikiupenya moyo wake.Akahisi maumivu makali.
“Patrick mwanangu “Akasema mama yake baada ya kumuona mawnae amedhiifika ghafla.
“Nafikiri ni wakati sasa wa kusahau yote yakiyopita na kuanza maisha mapya.Nakuomba jitahidi toka moyoni mwako uweze kumsahau Happy .Nakuomba umsahau na uuvunjilie mbali urafiki kati yako na huyo Happy .Bila Happy usingepatwa na matatizo haya mwanagu. ,Happy kakusababishia matatizo halafu yuko wapi sasa? huyo yuko Ulaya anasoma ! Wewe unasota gerezani,umepoteza masomo na kila kitu.Angalia mateso unayoyapata mwanangu.Mimi na baba yako hatulali tunakuwaza wewe mwanetu.Kama ni kweli angekuwa anakupenda na kukuthamini basi asingekubali kwenda Ulaya na kukuacha peke yako hapa gerezani ukiteseka.Sisi wazazi wako tunasema hatutaki tena kuusikia urafiki kati yako na Happy .yaliyotokea yametokea tunashukuru. Na tunamwachia Mungu lakini hatutaki tena kusikia wala kumwona Happy mtoto asiye na fadhila hata kidogo.’
“ No mama !!!!!! Patrick akapiga kelele.
“kamwe sintathubutu kufanya kitu kama hicho maishani mwangu.Siwezi kumuacha Happy hata iweje.Nilipambana kwa ajili yake na kwa ajili ya kuulinda utu wake na yote hii ni kwa sababu nampenda.Nikumuacha leo haya yote niliyoyafanya kwa ajili ya upendo wangu kwake yatakuwa ni bureWazazi wangu siwezi hata kwa sekunde moja kumsahau Happy.Hakuna mtu anayejua thamani ya sadaka hii niliyoitoa kwa ajili tu ya upendo wangu kwake.”Akasema Patrick huku machozi yakimtoka.
“Patrick sisi ni wazazi wako na ndio wenye tamko la mwisho.Sasa tunasema kuwa hatutaki kumsikia Happy masikioni mwetu.narudia tena hatutaki kabisa kumsikia binti huyo.” Akasema baba yake kwa hasira kisha akatoka nje.
Hili likawa tena ni pigo jingine la kutenganishwa na mtu aliyempenda kupita kiasi.Alikuwa njia panda je achague kuwa na Happy au wazazi wake? Mama yake akaendelea kumbembeleza mwanae ausikie ushauri wao ili amani iweze kudumu kwani ndugu wote walikuwa wamepitisha azimio hilo kuwa hawataki kuusikia urafiki wa Happy na Patrick.

*****************

Veronika akafika nyumani kwao Dar na kulakiwa na mama yake.Ilikuwa ni furaha sana kwa mama huyu kumuona tena mwanae ampendaye.Jioni hiyo wakiwa katika mlo wa jioni mama yake Vero akaanzisha mazungumzo.
“Enhe Vero hebu niambie kisa cha kukaa kwa mjomba wako siku zote hizi hali makubalianao yetu yalikuwa ni wiki mbili tu.Unafahamu fika kabisa kuwa hapa nipo peke yangu sina mtu mwingine wa kunisaidia.Msaidizi wangu ni wewe.”
“mama samahani sana kwa kukaa siku zote hizi kwa mjomba na kukuacha peke yako.Sikuwa nimetarajia kufanya hivyo ila ilitokea nikapata dharura ikanibidi nikae.Nashukuru hata ulivyonipigia simu kwani bila hivyo nadhani ningeendelea kukaa zaidi.”
“Dharura gani hizo we mtoto hebu niambie.”
“mama pamoja na kwamba wewe ni mzazi wangu lakini umekuwa ndiye mshauri wangu na zaidi ya yote umekuwa ni rafiki yangu wa karibu sana.Ni kutokana na juhudi zako wewe za kunifundisha maadili mema ndio maana leo hii nimekuwa ni binti mwenye mafanikio na kukuletea heshima kubwa.Katika mambo ambayo umekuwa ukiniusia kila siku na kunionya ni kujikita katika mahusiano ya kimapenzi.Yes nimekuwa nikilifuatilia hilo na ndio maana mpaka umri huu najivunia usichana wangu.Kweli mama simjui mwanaume mpaka leo hii.Lakini mama mapenzi ni kitu ambacho hakikwepeki.Yapo na kila mtu kwa wakati wake anajikuta yu mapenzini kama nilivyojikuta mimi.”
Alisita kidogo baada ya kumuona mama yake akimtazama .
“Nikiwa kwa mjomba kule Songea nilifanikiwa kukutana na mvulana wa maisha yangu.”
Alitulia tena na kuyaacha yale aliyoyasema yazame kabisa kwa mama yake.
Kisha akamsimulia kisa kizima,jinsi alivyokutana na Patrick na hadithi nzima ya maisha ya Patrick .
Mambo yalikuwa tofauti na jinsi Veronika alivyowaza.Yeye alitegemea labda mama yake angemgombeza na kumkanya juu ya jambo lile lakini ikawa tofauti.
“Vero mwanangu nimefurahi sana kwa kuwa wazi na hisia zako.Ni wazi mapenzi haya kwepeki.Yapo na kila mtu anapenda.Mimi nafurahi kusikia kuwa kijana huyo unampenda kwa dhati.Anaonekana ni kijana mtaratibu sana na mwenye mapenzi ya kweli.Mimi nakuunga mkono na niko tayari kukusaidia kwa lolote lile ili uweze kufanikiwa kumpata kijana huyo umtakaye.Kwani lengo langu ni wewe uishi maisha ya furaha na si karaha.” Waliongea mambo mengi kisha wakaagana na kila mmoja akaenda zake kulala.
Hakuweza kupata usingizi usiku huo.alikuwa na furaha kubwa sana baada ya mama yake kukubali kumsaidia ili aweze kumpata Patrick.
“Sasa kinachofuata ni kuharibu kabisa kila kitu baina ya Happy na Patrick.” Akasema kimoyomoyo halafu akachukua kalamu na karatasi akakaa mezani na kuanza kuandika barua ambayo alipanga aitume kwa Happy .

Kwako dada Happy
Ni matumaini yangu kuwa unaendelea vizuri na masomo huko uliko.
Naomba kabla yote nijitambulishe kuwa mimi ni jirani wa akina Patrick hapa Sumbawanga.Tumeishi vizuri na familia yao na baadaye nikahamia mkoani Mbeya.Kwa jina naitwa Grace.Nilisikia matatizo yaliyomkumba Patrick.Nikasikitika sana.
Si lengo langu kusema haya yote lakini dhumuni kuu la barua hii ni kukufahamisha kuwa Patrick mpenzio Amefariki dunia kwa ugonjwa wa kuhara akiwa gerezani.
Dada yake ndiye aliyenipa anwani yako na kunitaka niwasiliane nawe na kukufahamisha juu ya kifo hicho.Anadai kuwa hawawezi kukufahamisha kwa sababu familia yao haitaki kukusikia kabisa hasa baada ya kumsababishia matatizo mtoto wao na kumwacha akiteseka gerezani hali wewe ukipata maisha mazuri i na kuendelea na masomo yako huko Marekani.
Pole sana dada ,haya ndiyo mambo ya dunia.Ulimpenda sana Patrick lakini Mungu kampenda zaidi.Jipe moyo na utampata kijana mwingine kama Patrick
Pole sana
Grace

Aliipitia tena na tena barua ile na kuhakikisha iko safi na siku iliyofuata akadamka na kwenda kuiposti.

**********************

Akiwa katika tafakari nzito juu ya hatma ya uhusiano wao kwa ujumla .Mlango ukagongwa .Kwa uvivu Happy akainuka na kwenda kuufungua .alikuwa ni mtumishi wa chuo aliyekuwa na bahasha mkononi.Akamkabidhi Happy barua ile kisha akaondoka.
Happy aliitazama barua ile kwa wasi wasi .Alitazama muhuri ulikuwa wa Tanzania.Mwandiko juu ya bahasha hakuufahamu ulikuwa ni wa nani.
Kwa muda wa miezi miwili sasa amekuwa akiandika barua mfululizo kwa Patrick kupitia wazazi wake bila kupata majibu.Hii ilimpa wasiwasi mkubwa .aliumia sana kila alipofikiria Patrick atakuwa katika hali gani.aliujutia uamuzi wake wa kwenda Marekani na kumwacha Patrick peke yake.Alijiuliza maswali mengi juu ya ukimya huo uliotokea ghafla.
Taratibu akaifungua barua ile na kuanza kuisoma kwa makini.Kabla hajamaliza akapiga ukelele mkubwa sana,akaanguka chini na kupoteza fahamu.
Ukelele ule ulikuwa mkubwa kiasi cha kuwastua wenzake waliokuwa katika vyumba vya jirani.Watu walifika hapo chumbani na kumkuta Happy amezimia.haraka haraka wakamchukua na kumkimbiza katika hospitali ya hapo chuoni kwa ajili ya huduma ya kwanza.
Hakuna aliyeweza kufahamu mara moja sababu ya Happy kupiga ukelele ule na kupoteza fahamu.
Saa saba za usiku Happy akazinduka na kujikuta akiwa hospitali.Michelle pamona na wanafunzi wengine walikuwa pembeni ya kitanda.Alifumbua macho akatazama pande zote kisha akalala tena.Baada ya kama nusu saa akaamka tena na kukaa kitandani.Daktari akafika ,akampima na kumwomba aendelee kupumzika.
Alijilaza kitandani na kuanza kukumbuka mambo yaliyotokea .Alikumbuka barua ile aliyotumiwa na kuanza kulia.Michelle ambaye kwa sasa ni rafiki mkubwa wa Happy alifanya kazi ya ziada kumbembeleza
“siwezi kunyamaza Michelle,kilio hiki hakiishi leo,ni kilio cha milele.Nimempoteza mtu muhimu sana mishani mwangu.”akasema Happy kisha akaendela kulia.
“ Umempoteza nani,baba,mama au ndugu?
“Michelle its Patrick.Patrick amekufa”
“Whaat? Michelle naye akastuka.
Yes Patrick is dead” Happy akazimia tena.
Baada ya masaa mawili akazinduka.Safari hii aliweza kutazama lakini hakuweza kuongea .Alijaribu kufungua mdomo lakini maneno hayatoki.Ni machozi tu ndiyo yaliyokuwa yakitiririka..Wazazi wake wakataarifiwa juu ya ugonjwa wa mtoto wao na kwa haraka ikawabidi waende kumtazama.Ilikuwa ni siku ya sita tangu amelazwa hospitalini hapo wazazi wake walipowasili.Aliwaeleza kilichotokea wote wakastuka sana.
Wiki ya kwanza ikakatika bila ya Veronika kutokea.Patrick akaanza kupatwa na wasiwasi kwani Vero alimuahidi kuwa atakuwa akimtembelea karibu kila wiki.Alkuwa na hamu sana ya kutaka kupata walau ujumbe wowote toka kwa Happy kwani Vero aliahidi pamoja na barua ile ambayo Patrick alimtuma akaiposti ,angempigia simu .Alijipa moyo na kuendelea kusubiri.Wiki ya nne toka alipoondoka pale Vero akarudi Songea kwenda kumjulia hali Patrick.
Patrick alifurahi mno kumuona tena Vero.Vero naye alifurahi sana kumuona Patrick kijana ambaye amekuwa akimkosesha usingizi.Bila ya kupoteza muda Patrick akataka afahamu kama kuna habari yoyote kutoka kwa Happy .
Veronika akamwangalia kwa sekunde kadhaa akakohoa kidogo kisha akasema
“Patrick nimekuja na habari Fulani ambazo si nzuri “
Patrick akastuka na kuuliza.
“habari gani hizo Vero”
Vero akatulia kidogo kisha akaendelea
“Patrick nimechelewa kuja kukuona kama nilivyokuwa nimekuahidi lakini kilichonichelewesha ni suala hili hili la Happy .”
“Happy ? Kafanya nini tena? Patrick akauliza kwa hamaki
“Patrick you are strong I know but you need to be strong more stronger to hear this” Vero akasema
“Vero nakuwa sikuelewi .Mbona unanichanganya?Go straight to the point”
Vero akajiweka sawa akakaza sura ili asije onekana anadanganya
“Patrick ! Nilipiga simu chuoni kwa Happy kama tulivyokuwa tumekubaliana na nikaambiwa kuwa Happy alikuwa amehama chuo hicho muda mrefu.Sikuchoka nikaomba nielekezwe alikuwa amehamia chuo gani nikasaidiwa nikakipata chuo alichokuwa anasoma kwa sasa nikapiga simu na kweli nikampata lakini nilipojitambulisha tu kuwa ninaujumbe muhimu toka kwa Patrick akakata simu.Nilistuka sana lakini sikukata tamaa.Kwa muda wa siku mbili mfululizo nikawa napiga simu lakini haipokelewi.basi nikaamua kumtumia binamu yangu mmoja ambaye naye anasoma huko huko lakini chuo kingine tofauti na hiki cha Happy .Yeye akafanya uchunguzi wake na baada ya siku kama tano hivi akaniambia kuwa amefanikiwa kumfahamu Happy lakini kwa bahati mbaya Happy amepata bwana ambaye anaishi naye na inavyosemekana tayari ana ujauzito wa mzungu huyo.Niliumia mno nikapiga tena simu kwa hasira nikaongea naye bila aibu akanijibu hivi “ sitaki kusikia habari yoyote juu ya Patrick .Kama ni gerezani alitaka kwenda mwenyewe.mwacheni akae atatoka atatafuta maisha yake.Mimi nina mtu wangu kwa sasa na sitaki usumbufu hata kidogo na wala huko Tanzania sitegemei kurudi..Halafu akakata simu.Nikaj………………..” Hakumalizia sentensi yake Patrick akaanguka chini na kupoteza fahamu.Vero akapiga kelele kuomba msaada na mara wakaja askari magereza na kumbeba Patrick na kumpatia huduma ya kwanza.
Veronika akachanganyikiwa na kijasho kikamtoka.Alijilaumu sana moyoni kwa kutunga uongo ule mkubwa kiasi cha kuhatarisha maisha ya wawili hawa waliopendana.Hakutegemea kama hali ingekuwa vile
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 12
MTUNZI : PATRICK CK
CONTACK: 0764294499
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
Kwa muda wa siku mbili mfululizo nikawa napiga simu lakini haipokelewi.basi nikaamua kumtumia binamu yangu mmoja ambaye naye anasoma huko huko lakini chuo kingine tofauti na hiki cha Happy .Yeye akafanya uchunguzi wake na baada ya siku kama tano hivi akaniambia kuwa amefanikiwa kumfahamu Happy lakini kwa bahati mbaya Happy amepata bwana ambaye anaishi naye na inavyosemekana tayari ana ujauzito wa mzungu huyo.Niliumia mno nikapiga tena simu kwa hasira nikaongea naye bila aibu akanijibu hivi “ sitaki kusikia habari yoyote juu ya Patrick .Kama ni gerezani alitaka kwenda mwenyewe.mwacheni akae atatoka atatafuta maisha yake.Mimi nina mtu wangu kwa sasa na sitaki usumbufu hata kidogo na wala huko Tanzania sitegemei kurudi..Halafu akakata simu.Nikaj………………..” Hakumalizia sentensi yake Patrick akaanguka chini na kupoteza fahamu.Vero akapiga kelele kuomba msaada na mara wakaja askari magereza na kumbeba Patrick na kumpatia huduma ya kwanza.
Veronika akachanganyikiwa na kijasho kikamtoka.Alijilaumu sana moyoni kwa kutunga uongo ule mkubwa kiasi cha kuhatarisha maisha ya wawili hawa waliopendana.Hakutegemea kama hali ingekuwa vile

ENDELEA..........................

Hatimaye miezi ikatika bila ya mawasiliano yoyote baina ya Patrick na Happy .Wakati Happy akiamini kuwa Patrick ni marehemu ,Patrick kwa upande wake yeye alikuwa bado ana hasira moyoni kwa kusalitiwa na Happy .alijiona mjinga sana kwa kuhatarisha maisha yake kwa mtu asiyekuwa na thamani kwake hata chembe.Alilia usiku na mchana kwa kitendo hiki cha Happy .Happy yeye alikuwa akimlilia Patrick kila siku.Kila alipoiona picha yake alikuwa hakaukwi na machozi.
Taratibu kila mmoja kwa upande wake akaanza kukubaliana na matokeo kuwa hayakuwa mapenzi ya Mungu wao kuwan pamoja.Kila mmoja akamweka mwenzie kama kumbukumbu ya pekee maishani.Pamoja na kukubali huko kuwa Patrick alikuwa amekufa lakini Happy alikuwa na dhamira moyoni ya kuja kulitafuta kaburi la Patrick na kutoa heshima zake kwa mtu pekee aliyempenda na kumthamini.
Wakati Happy akiwa na wazo la kuja kudhulu kaburi la Patrick pindi atakaporejea nyumbani Patrick yeye aliamua kumsamehe kwa maamuzi aliyoyafanya na kuamua kusonga mbele na maisha yake.Ingawa ni kitu ambacho kilimuumiza akili kila siku lakini alijitahidi aweze kumsahanu Happy na kuanza maisha yake mapya bila ya kiumbe huyu aliyempenda zaidi .
Ni katika wakati huu mgumu aliokuwa nao Patrick ndipo Veronika alipozidisha ukaribu wake kwa Patrick.Patrick kwa kiasi Fulani alishukuru sana kwa kufahamiana na Vero kwani yeye ndiye mfariji mkuu wake mkuu katika kipindi hiki kigumu alichokuwa nacho.Ni vero pekee ambaye anaonyesha kumuelewa na kumjali.Ukaribu wao ukaongezeka mara dufu na tayari kukaanza kuwa na kila dalili za kuibuka kwa uhusiano mzito baina yao.
“Vero ni msichana mrembo ,ambaye ni wazi anaonyesha ana mapenzi ya kweli.Vero amekuwa ndiye mtu wangu wa karibu.Ni yeye tui ambaye anaonyesha kunielewa na kunisaidia.Ni kwa sababu ya Vero ndio maana naona hata maisha yangu hapa gerezani yamekuwa mazuri kwani ninaishi kama niko nyumbani.Mjomba wake Vero mkuu wa gereza ananjali mno na kunithamini.Yote hii ni kwa sababu ya Vero.vero amenifanya nisijione mkiwa tena,ameniondolea lindi la mawazo mazito niliyokuwa nayo juu ya Happy .Vero amenisaidia kurudisha tena matumaini ya ndoto zangu ambazo tayari zilikuwa zimeanza kufutika,kwa haya yote aliyoyafanya Kwa nini basi nisimpe nafasi aliyokuwa nayo Happy ? Nilitambua toka awali kuwa Vero ananipenda lakini ikawa vigumu kuipata nafasi ndani ya mioyo wangu kwa sababu wakati huo funguo ya moyo wangu alikuwa nayo Happy .Ninakubaliana na hisia zangu kuwa Vero ndiye msichana pekee ambaye anaweza kuliziba pengo la Happy .Patrick akawaza kwa kina sana juu ya suala hilo na akadhamiria kumtamkia wazi wazi Vero juu ya adhma yake ya kutaka wawe wapenzi.

*******************

Ingawa alihuzunika sana kwa kusikia kuwa Patrick mpenzi wa Happy amefariki dunia kwa upande mwingine Mike Cambell alikuwa na furaha isiyokifani kwani aliamini kuwa sasa anaweza kuipata nafasi hii ya Patrick toka kwa Happy .Aliamini kuwa kwa sasa Happy hatakuwa tena na kisingizio cha kumkataa .Alihama toka New york city hadi Washington DC ambako Happy alikuwa akisoma.Lengo likiwa ni kujaribu kujenga ukaribu kati yake na Happy .
Taratibu akaanza kujenga mazoea ya kuwa karibu na Happy na kumfariji kwa kumnunulia maua n.k.Yeye na dada yake Michelle wakajitahidi kwa kadiri walivyoweza katika kumfariji na kumuondolea Happy majonzi yasiyokwisha.Walitoka kila mwisho wa wiki na kwenda sehemu mbali mbali za kuvutia na burudani lengo likiwa ni kujaribu kumsahaulisha juu ya msiba wa Patrick.Baada ya miezi minne kupita tayari Happy alikwisha anza kurudia hali yake ya kawaida.Tayari ukaribu mkubwa ulikwisha jengeka kati yake na Mike kiasi kwamba hakusikia raha kupitisha siku bila kumuona kijana huyu ambaye ametokea kuwa mfariji wake mkubwa hasa katika kipindi hiki cha msiba mkubwa uliompata.
Pamoja na ukaribu huo uliojengeka baina yao bado ilikuwa ngumu kwa Happy kuitoa nafasi ya Patrick kwa mtu mwingine.Kwa mapenzi mazito aliyokuwa nayo kwa Patrick alikuwa radhi aishi peke yake kwa heshima ya kijana huyu.Suala hili liliendelea kumuumiza kichwa Mike kwa muda mrefu lakini hakukata tamaa.Alizidi kuonyesha mapenzi ya wazi na nia dhahiri ya kutaka kuwa na Happy .
Siku moja wakiwa katika klabu ya usiku Mike akaamua tena kumkumbushia Happy juu ya ombi lake la kutaka wawe wapenzi.
“Happy naomba kwanza nitangulize samahani kwa jambo ninalotaka kukueleza kwa sababu najua unaweza usilipende.” Akanyamaza kidogo huku Happy akimtazama kwa macho maangavu.
“Najua bado uko katika kipindi kigumu cha kufiwa na mpenzi wako.Kusema ukweli ni kipindi kigumu kwetu sote kwa sababu wewe ni rafiki yetu wa karibu na hivyo huzuni yako ni yetu pia.Pamoja na yote yaliyotokea ambayo ni kazi ya Mungu,lakini maisha hayana budi kuendelea.Ninachokusihi ni kuyasahau yote yaliyotokea na kuanza maisha mapya” Akanyamaza akamtazama Happy usoni halafu akaendelea.
“Happy nimeona nikueleze tena kile nilichokueleza muda mrefu uliopita.Happy napenda kwa mara nyingine tena kukuhakikishia kuwa wewe ni mwanamke pekee ambaye umeweza kutua katika moyo wangu na kukataa kutoka kama vile nyuki anavyong’ang’ania ua lenye asali tamu..Toka mara ya kwanza nilipokutia machoni sura yako imejichora moyoni mwangu kiasi ambacho haitaweza kufutika kamwe.Happy nakupenda kupita ninavyojipenda mwenyewe.Naomna kwa mara nyingine tena unipe nafasi ndani ya moyo wako ya kuwa nawe.Ninaomba unipatie nafasi ya Patrick .Wewe ni mwanamke mrembo ambaye unahitaji mtu mwenye mapenzi ya dhati na ya kweli kama alivyokuwa Patrick.Siwezi kuwa kama Patrick lakini ninakuhakikishia kuwa upendo wangu kwako ni wa kweli na wa dhati .Niko tayari kufanya lolote lile katika dunia hii ilimradi tu niwe na wewe.Tafadhali Happy naomba unielewe ninaposema kuwa moyo wangu unateketea kwa penzi lako.Naomba unipe nafasi ndani ya moyo wako “
Mike akasema na kumtazama Happy ambaye alikuwa amenyamaza huku machozi yakimtoka kwa mbali.Akatoa kitambaa katika pochi yake akajifuta uso halafu akakaa vizuri na kusema
“Mike kwanza napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe na Michelle kwa kuwa watu wangu wa karibu.Sio siri mmenisaidia sana na hasa katika kipindi hiki kigumu nilichokuwa nacho.Bila uwepo wenu sijui ningekuwa katika hali gani.Mmekuwa na mimi katika kila hali,kila dakika.Mmefanya kila mliloweza kunifariji na mpaka leo hii ninaendelea vizuri.Sioni kitu cha kuwalipa zaidi ya maneno haya machache Ahsanteni sana.Kuhusu suala ulilonieleza ,naomba unipe muda wa kutosha wa kutafakari na kufanya maamuzi.Nitakapokuwa tayari nitakujibu”

*******************

Hatimaye siku ya kihistoria katika maisha ya Patrick iliwadia.Ni siku ambayo Patrick alihitimisha adhabu yake ya kutumikia miaka mitano gerezani.Tangu asubuhi ya siku hiyo ya kutoka kwake Patrick alikuwa ni mtu mwenye furaha sana.Aliwaaga wafungwa wenzake wote huku akiwa mwingi wa tabasamu.Wakati Patrick akiwa mwingi wa furaha kwa upande mwingine ilikuwa ni simanzi gerezani kwa kuondokewa na kijana kama huyu ambaye alipendwa karibu na kila mtu.Alikuwa mstari wa mbele katika kuwapa moyo na kuwafariji wale waliokata tamaa,vile vile alikuwa ni kiungo kikubwa katika kuwasaidia wenzake kupata vitu kama sigara,sabuni n.k kwa sababu yeye muda mwingi alikuwa akishinda nyumbani kwa mkuu wa gereza hivyo kuvipata vitu hivyo kwake ilikuwa rahisi..Kuondoka kwake lilikuwa ni pigo kubwa kwa wale wafungwa waliokuwa wakimtegemea .
Saa tatu na nusu juu ya alama Patrick aliitwa katika ofisi ya mkuu wa gereza ambako alitaarifiwa rasmi kuwa kuanzia muda huo alikuwa huru.Aliombwa awe raia mwema huko aendako ili asije rudishwa tena gerezani.Hii ilikuwa ni kama ndoto.Hakuamini hadi pale mkuu wa gereza alipompa mkono na kumwambia kuwa yuko huru na kumtakia kila la heri katika maisha yake .
Katika lango la kuingilia hapo gerezani kundi kubwa la watu likongozwa na wazazi wake lilikuwa likimsubiria kwa hamu kubwa.Walikuwepo ndugu na baadhi ya rafiki zake akiwemo rafiki yake ambaye walikutana hapo gerezani lakini yeye aliwahi kutoka Andrew.Alikuwepo pia binti mrembo ambaye urembo wake leo hii ulizidi mara dufu.Alikuwa amependeza zaidi ya maelezo.Huyu ni Veronika ambaye yeye pamoja na ndugu zake na mama yake waliungana na familia ya akina Patrick katika kusherehekea tukio hili kubwa .Tayari Patrick na Vero walikwisha kuwa wapenzi na urafiki wao ulikuwa na baraka ya pande zote mbili yaani upande wa akina Patrick halikadhalika mama na ndugu zake Veronika hawakuwa na kipingamizi chochote juu ya urafiki huu.
Taratibu lango likafunguliwa na Patrick akaruhusiwa kutoka nje akiwa huru.Alitumia sekunde kadhaa kulitazama gereza hilo ambalo amekaa takribani miaka mitatu.
Huku akitiririkwa na machozi mama yake alikuwa mtu wa kwanza kumkumbatia mwanae,kisha wakafuata wengine wote waliokuwapo hapo .Zilikuwa ni dakika chache zenye furaha kubwa .Wote wakapanda katika magari yaliyoandaliwa na kuanza safari .Patrick alipanda katika gari maalum lililokuwa likiendeshwa na Andrew rafikiye mkuu pamoja na mfariji wake na hatimaye mpenzi wake ,Veronika.ambaye kwa sasa alikuwa ni kila kitu kwake .
Ndani ya gari Patrick na Vero walikuwa wamekumbatiana wote wawili machozi yakiwatoka.Patrick alikumbuka toka alivyoonana na Vero siku ya kwanza,wakazoeana na kuwa marafiki na hatimaye kwa sasa ni wapenzi.Alimshukuru sana Mungu kwa kumrudishia furaha iliyokuwa imepotea baada ya kumpoteza Happy .Mwanzoni aliamini kuwa Happy ndiye ilikuwa furaha yake lakini baada ya Happy kuondoka akatokea Vero na kuirudisha tena furaha hiyo.Veronika alionyesha mapenzi ya kweli na uvumilivu mkubwa katika kipindi chote walichofahamiana mpaka leo.
“Veronika nashukuru sana kwa yote uliyonifanyia.Nashukuru kwa upendo wa ajabu ulionionyesha”Akasema Patrick kwa kunong’ona.
“ahsante pia Patrick kwa kuufungua moyo wako na kunikubali .Najiona ni mwenye bahati sana kuwa na mtu kama wewe.”

******************

Hatimaye Happy naye baada ya kumaliza masomo yake akarejea nyumbani Tanzania.Toka akiwa safarini alikuwa na shauku moja tu ya kutaka kufahamu mahala alipozikwa Patrick .Tayari alikwisha kuwa na mahusiano ya kimapenzi na Mike cambell.
Familia yake yote ilikuwapo uwanja wa ndege kumlaki.tayari baba yake alikwisha staafu kazi na sasa wanaishi jijini Dar es salaam.
Siku tatu tu baada ya kuwasili nchini Happy akafunga safari hadi mjini Sumbawanga ambako ndiko Patrick alikuwa akiishi.Kule alitaarifiwa kuwa familia hii ilikwisha hama muda mrefu na walihamia jijini Dar es salaam. Hakukata tamaa akaondoka na kuelekea Iringa katika gereza ambalo Patrick alikuwa amefungwa mwanzo.Lengo lilikuwa ni kupata ukweli juu ya kifo cha Patrick.Pale gerezani alitaarifiwa kuwa Patrick alihamishwa na kupelekwa katika gereza jipya huko Songea.Toka hapo hawakuwa na kumbukumbu naye zozote.
Happy hakukata tamaa akafunga safari tena hadi Songea katika gereza jipya ambako ndiko Patrick alihamishiwa.Pale akaonana na mkuu wa gereza na kumweleza kilichompeleka.Mzee yule akamwangalia kwa mstuko .
“wewe ndiye Happy kibaho?
“Ndiye mimi mzee “Happy akajibu
Mkuu huyu wa gereza ambaye ni mjomba wa Veronika alikwisha hadithiwa hadithi nzima ya mkasa uliomkuta Patrick ndio maana alistuka kwa kumuona Happy pale.
“Happy ina maana hamkuwa mkiwasiliana wakati ukiwa masomoni?
“Tulikuwa tukiwasiliana lakini mawasiliano yakakata ghafla sana na siku moja nikapokea taarifa kuwa Patrick alifariki kwa ugonjwa wa kuhara akiwa gerezani.”
Mkuu wa gereza akstuka sana alipopata taarifa ile .Kwa kiasi fulani taarfa ile ikamchanganya kwa sababu kwa mujibu wa taarifa aliyoipata ni kwamba Happy akiwa masomoni nchini Marekani alipata bwana mwingine na kuolewa naye na kumsahau Patrick kitu kilichopelekea Patrick ampe nafasi Veronika.
Iliimlazimu mzee yule akae kimya akitafakari kisha akasema
“Happy kwanza nakupa pole sana kwa yote yaliyotokea kati yako na Patrick.Ni kweli Patrick alihamishiwa katika gereza hili akitokea Iringa.Patrick alikuwa ni mmoja kati ya wafungwa bora kabisa ambaye hajawahi kutokea katika gereza hili.Tulimpenda sana.Kila mtu alimpenda.Alikaa hapa gerezani hadi alipomaliza kifungo chake na kuachiwa huru.Hapa gerezani alitoka salama salimini .Kama ni kufariki basi atakuwa amefariki baada ya kutoka hapa kwa sababu mimi ndiye niliyeidhinisha kuachiwa huru baada ya kumaliza kifungo chake.”
Maneno yale yakamfanya Happy atetemeke mwili .Aliinama chini akashindwa kuyazuia machozi kumtoka.Hakuyaamini maneno yale ikambidi aulize tena.
‘Mzee sijakuelewa vizuri.Umesema nini?
“Nimesema kuwa Patrick alimaliza kuitumka adhabu yake akiwa mzima wa afya na mimi kama mkuu wa gereza ndiye niliyemuachia huru baada ya kumaliza kifungo chake.Kama ni kufariki basi alifariki baada ya kutoka hapa gerezani.Nasikitika sana kwa kumpoteza kijana kama yule.”
“mzee mbona taarifa niliyoipata mimi inasema kwamba Patrick alifariki akiwa gerezani? Tena inasema kuwa alifariki kwa maradhi ya kuhara? Happy akasema huku machozi yakimdondoka
“Taarifa hiyo ulipewa na nani? Mkuu wa gereza akauliza
“Taarifa hiyo nilitumiwa na mtu nisiyemfahamu akidai kuwa yeye anamfahamu Patrick kwa sababu walikuwa ni majirani kule Sumbawanga.Dada huyo alisema kwamba familia ya Patrick haikuweza kunifahamisha juu ya msiba wa mtoto wao kwa madai kwamba nilimtelekeza mtoto wao gerezani nikaenda kusoma ulaya,wakati yalikuwa ni makubaliano yetu mimi na yeye.Sikuwa nataka kumwacha Patrick peke yake na mimi nikaenda kusoma Marekani hasa ukichukulia mim ndiye chanzo cha yeye kufungwa,lakini ni Patrick huyo huyo ndiye aliyenishawishi nikubaliane na uamuzi wa baba wa kunipeleka Marekani kusoma.”
“Pole sana Happy.Jipe moyo.Haya ni mambo ya kawaida Jitahidi sana uyaruhusu maisha yako yaendelee.”Mkuu wa gereza akasema
“Nashukuru sana mzee kwa msaada ulionipa.Japokuwa bado kuna utata mkubwa juu ya kifo hicho lakini namuachia Mungu.Kama amekufa kweli nitamuombea kwa Mungu apumzike kwa amani lakini kama hajafa kweli huko aliko atambue kuwa maumivu anayonisababishia ni makubwa kiasi ambacho siwezi kuelezea.”
Happy akaagana na mkuu wa gereza ,akapanda gari lake na kuondoka huku machozi yakiendelea kumtoka.Akashindwa kuendesha gari akapaki pembeni akainamia usukani.
“ Nina kila sababu ya kuamini kuwa Patrick hajafa.Kutokana na maelezo ya mkuu wa gereza ni kwamba Patrick alimaliza kifungo chake na kutoka gerezani salama.Na katika ile barua niliyoandikiwa ilisema kwamba Patrick alifariki akiwa gerezani.Mbona mambo haya yananichanganya? Je Patrick alinifanyia hila nijue kuwa amekufa? Kama ni kweli kwa nini Patrick amenifanyia hivi mimi??”Happy akajiuliza huku akiupiga usukani kwa hasira. .
“Nilimkosea nini Patrick hadi akamua kunidanganya na kuniacha niteseke miaka yote hii?Moyo wangu hauna amani hata kidogo yote hii ni kwa ajili yake .Au labda kitendo cha mimi kuondoka kwenda kusoma Marekani yeye hakikumfurahisha?Anyway nitakutafuta Patrick hata kama itanigharimu maisha yangu I promise I’ll find you because you left me at the time I needed you most “
 
MISS TANZANIA
SEHEMU YA 13
MTUNZI : PATRICK.CK
CONTACT : 0764294499
ILIPOISHIA SEHEMU ILIYOPITA
Happy akaagana na mkuu wa gereza ,akapanda gari lake na kuondoka huku machozi yakiendelea kumtoka.Akashindwa kuendesha gari akapaki pembeni akainamia usukani.
“ Nina kila sababu ya kuamini kuwa Patrick hajafa.Kutokana na maelezo ya mkuu wa gereza ni kwamba Patrick alimaliza kifungo chake na kutoka gerezani salama.Na katika ile barua niliyoandikiwa ilisema kwamba Patrick alifariki akiwa gerezani.Mbona mambo haya yananichanganya? Je Patrick alinifanyia hila nijue kuwa amekufa? Kama ni kweli kwa nini Patrick amenifanyia hivi mimi??”Happy akajiuliza huku akiupiga usukani kwa hasira. .
“Nilimkosea nini Patrick hadi akamua kunidanganya na kuniacha niteseke miaka yote hii?Moyo wangu hauna amani hata kidogo yote hii ni kwa ajili yake .Au labda kitendo cha mimi kuondoka kwenda kusoma Marekani yeye hakikumfurahisha?Anyway nitakutafuta Patrick hata kama itanigharimu maisha yangu I promise I’ll find you because you left me at the time I needed you most “

ENDELEA.................................

Miaka sita sasa imekwisha pita toka Patrick toke gerezani na tayari Patrick amekwisha maliza shahada yake ya kwanza ya uandishi wa habari na tayari ni mwajiriwa katika kituo kimoja kikubwa cha Televisheni nchini.
Pamoja na kwamba ni muda mrefu umepita lakini picha ya Happy bado haijafutika kabisa moyoni mwake.Huja na kufutika na wakati mwingine humuacha katika huzuni kubwa.
Uhusiano kati yake na Vero umekomaa ukakubaliwa na ndugu wa pande zote mbili na hatimaye ukafikia hatua ya uchumba .Aliamua kumvisha pete ya uchumba Vero baada ya kuamini kuwa tayari Happy hakuwa na nafasi tena katika maisha yake.Aliamini Vero ndiye mwanamke pekee aliyepewa na Mungu ili awe mke wake.Vero ndiye aliyekuwa naye katika kipindi kirefu cha mahangaiko,Vero amemsaidia kufuta majeraha ya moyo na kuanza maisha mapya,Vero amekuw ani kila kitu kwake.
Kwa upande mwingine baada ya Happy kugundua kuwa Patrick hakufa gerezani na kuamini kuwa bado yu hai alikumbana na shinikizo kubwa toka kwa wazazi na ndugu zake la kutaka amsahau kabisa kijana huyu na kuolewa na Mike cambell ,kijana mmarekani mweusi ambaye mapenzi yake kwa Happy hayana kifani.Mike amekuwa ndiye mfariji mkubwa wa Happy toka alipopata taarifa kuwa Patrick amefariki dunia.Ni yeye na dada yake Michelle ndio walioweza kumfuta Happy machozi aliyokuwa akilia kila uchao akimlilia Patrick.Ni Mike ndiye aliyejitolea kila alichoweza kukifanya kuhakikisha binti huyu mwenye uzuri uliotukuka anarejea katika maisha ya kawaida.Pamoja na ugumu uliokuwepo wa Happy kumsahau Patrick lakini Mike alivumilia na kuamini kuwa iko siku Happy atamsahau Patrick na yeye kupewa nafasi ndani ya moyo wa binti huyu mwenye sura ya kimalaika..Hatimaye baada ya kujishauri kwa muda mrefu akaamua kumkubali Mike awe mpenzi wake na bila kupoteza muda akakubali kuvishwa pete ya uchumba na Mike Cambell katika sherehe kubwa iliyohudhuriwa na umati wa watu.
Pamoja na kuamini kuwa Patrick hakuwa ridhiki yake,kitu kilichompelekea akubali kuvishwa pete ya uchumba na Mike lakini bado Happy alikuwa na kitu moyoni juu ya Patrick.Kuna kitu ambacho hakuweza kukifuta moyoni mwake.Na hiki kilizidi kumtesa siku hadi siku licha ya kujitahidi kwa kadiri alivyoweza kumsahau Patrick.

********************

Veronika akamtazama Patrick kwa macho makali na tayari akagundua kuna kitu kinachomsumbua mpenzi wake.Kilichomuumiza roho zaidi ni kwa nini kama Patrick ana tatizo asimwambie?
Akapanda kitandani na kukaa karibu ya Patrick akamkumbatia .
“Patrick mpenzi kwa siku chache sasa nimegundua mabadiliko Fulani kwako.Hauko kawaida.Kuna jambo gani linalokusumbua hebu niambie mpenzi wangu.Unajua ninapokuona katika hali hiyo hata mimi ninapata wasiwasi mwingi.Nimezoea kuiona sura yako iliyojaa tabasamu kila wakati lakini kwa sasa unajilazimisha kutabasamu na unaonekana u mwingi wa mawazo.Au kuna kitu nimekuudhi Patrick?
Aliongea maneno haya taratibu machozi yakimlenga hali kichwa chake amekilaza kifuani kwa Patrick
“Vero mpenzi hakuna jambo lolote linalonisumbua.Nahisi ni hizi dawa ninazotumia ndiyo zinanifanya niwe katika hali hii lakini usijali si muda mrefu nitarudia hali yangu ya kawaida.”Akasema Patrick huku akimsugua Veronika mgongoni.
“Patrick mimi ni mchumba wako na nimekuwa karibu nawe kwa muda mrefu sasa.Sidhani kama kuna mtu mwingine anayekufahamu kiundani zaidi yangu.Nina imani kabisa kuna kitu kinakusumbua akili yako .Nina jua kabisa ni wakati gani unakuwa na furaha na ni wakati gani unakuwa na matatizo.lakini sikulazimishi kuniambia.Kama unaona tatizo hilo halina ulazima wa mimi kulijua basi hakuna neno.Ila kumbuka muda wowote utakapohitaji msaada wangu nipo tayari kukusaidia.”
Vero akambusu Patrick kisha akatoka nje.
Saa saba za usiku Patrick akastuka toka usingizini .Vero alikuwa pembeni yake amelala .Akamwangalia mpenzi wake kwa dakika kadhaa.akapatwa na uchungu mwingi baada ya kuyaona mapenzi makubwa aliyokuwa nayo binti huyu kwake.
“Ni wazi vero amekuwa ni msichana wa pekee maishani mwangu ambaye ameweza kunionyesha mapenzi ya kweli na kunisaidia kupata uelekeo mpya wa maisha yangu.Nampenda Vero na nina imani ndiye mwanamke atakayenifaa maishani.lakini huyu Happy ……………mhhh …naye kajitokeza tena katika hatua za mwisho kabisa za kukamilisha ndoa yangu na Veronika.Yes ! nilimpenda Happy kuliko kitu chochote kile lakini alinitenda kitu kibaya nikamwondoa katika moyo wangu.Lakini ni kwa nini siachi kumuwaza ?Kila dakika sura yake inanijia akilini….ooh Mungu wangu nisaidie katika mtihani huu mguu nilionao.Lakini pamoja na yote yaliyotokea baina yetu lazima nimtafute Happy .Ni lazima nionane naye .Lazima nifahamu ni kwa nini alinitenda vile?
Patrick akamtazama tena vero akamkumbatia kwa nguvu.
Asubuhi na mapema aliamka akaoga kisha akamuaga Happy kuwa anakwenda kumuona Andrew.Vero hakuwa mbishi akamwacha aende
Akiwa ndani ya gari Patrick alijaribu tena kupiga ile namba ya simu ambayo aliamini kabisa itakuwa na uhusiano Fulani na Happy lakini bado ikawa haipatikani.
“Yawezekana labda alipopiga simu jana mchana ikapokelewa na Vero ,walitoleana lugha chafu .Pengine labda walitukanana ,kitendo kilichomfanya akasirike na kuizima kabisa simu yake.”
Akawasili nyumbani kwa Andrew mishale ya saa moja na dakika ishirini hivi
“ooh Patrick mbona asubuhi hivi.Kuna usalama kweli? Akauliza andrew kwa shauku ya kutaka kufahamu kama kulikuwa na tatizo lolote.
“Si kwema andrew” akasema Patrick huku akiketi sofani.
“Enhe ! kulikoni ? Akauliza tena Andrew
Patrick akatulia kidogo akavuta pumzi kisha akasema
“mambo katu si mazuriAndrew.Jana mchana mimi nikiwa nimelala mtu ambaye nahisi atakuwa ni Happy akalipiga simu ,basi si ikapokelewa na Vero?
“Mhh usiniambie Patrick.Enhee ikawaje? Andrew akauliza huku akionyesha hali Fulani ya mstuko
‘Sasa sielewi waliongea nini kwa sababu kwa mujibu wa maelezo ya Vero ni kwamba mtu huyo hakuongea chochote.Nikajaribu kupiga mimi mwenyewe simu ikapokelewa na sauti niliyoisikia ni dhahiri ni ya Happy .Sidhani kama ninaweza kuipotea sauti yake japokuwa hatujaonana kwa kipindi kirefu.Baada tu ya kuitikia akakata simu na kuizima kabisa na hadi muda huu tunapoongea simu yake haipatikani.Nimechanganyikiwa Andrew sijui hata nifanye nini ndio maana nimekuja hapa kwako asubuhi hii ili tuone tufanye kitu gani.”
Andrew akavuta pumzi ndefu akasimama na kuzunguka zunguka humo sebuleni kisha akasema.
“Patrick hata mimi naanza kuhisi kuwa kuna kitu waliongea na Vero ambacho kimemfanya awe na hasira na asitake tena hata kuiwasha simu yake.lakini bado hatuna haja ya kukata tamaa,kitu tunachotakiwa kukifanya kwa sasa ni kutafuta mahala anapoishi Happy .kazi hiyo niachie mimi nitaifanya kikamilifu.Baada ya kupafahamu anapoishi itakuwa rahisi kwetu kumpata”
‘Ahsante sana Andrew kwa kunisaida.” Baada ya dakika chache za maongezi Patrick akaaga na kiondoka.

******************

Happy alistuliwa toka katika usingizi mzito na hodi iliyogongwa mlangoni.Alijiinua kiuchovu na kuangalia saa.Ilikuwa ni saa nne asubuhi.
“Mhh ! dada mbona umelala hivyo? Mi nimepatwa na wasiwasi pengine unaumwa.” Akasema Margreth.Happy hakujibu kitu akageuka na kukaa tena kitandani huku akiyafikicha macho yake ambayo kwa sasa yalionyesha hali ya kuvimba kutokana na kulia kwa muda mrefu.
“Happy hebu niambie kitu gani tena kinakufanya uwe katika hali hiyo? Na Patrick vipi ulimpigia simu?
“Ah ! acha tu Margreth.Nilimpigia simu lakini ikapokelewa na mwanamke.Nilishindwa kuongea jambo lolote nikakata simu.nahisi Patrick tayari atakuwa ameoa”
Happy akashindwa kuvumilia machozi yakamtoka.
“Hebu nisikilize dada.Hupaswi kulia.Ninaimani hizo ni hisia zako tu kwamba Patrick tayari ana mke.Huwezi jua pengine labda ni ndugu yake ,dada yake au hata katibu muhtasi wake.hata hivyo ni muda mrefu sasa umepita toka mlipopotezana na mlipotezana katika mazingira yenye kutatanisha sana huku kila mmoja akiwa bado anampenda mwenzake,nina imani kabisa kuwa pendo lile bado liko hai.Najua ndio maana unahisi kuumizwa na hisia kuwa Patrick tayari ana mke kwa sababu bado unampenda.Yawezekana labda atakuwa ameoa au pengine ana mchumba lakini hilo lisikupe shaka.Tutalifahamu muda si mrefu.”
Maneno yale ya Margreth yanampa moyo sana Happy .
“nashukuru sana mdogo wangu kwa kunifariji.Pamoja na hayo naomba tafadhali hii iwe ni siri yako na asijue mtu mwingine yeyote yule.”
“Usijali Happy Hakuna mtu yeyote atakayefahamu juu ya Patrick.leo nataka nimfuate Patrick ofisini kwake kama hii kadi yake ya biashara inavyoonyesha.”

******************

Saa tano na nusu ilimkuta Margreth katika jengo lenye ofisi anakofanyia kazi Patrick .Akashuka garini na na kupanda lifti kuelekea ghorofa ya saba ziliko ofisi hizo alizokuwa akizitafuta.
Aliposhuka tu katika lifti akakutana na bango kubwa linaloelekeza zilipo ofisi hizo.Taratibu na kwa mwendo wa madaha kama ilivyokawaida yake alifika mpaka katika chumba cha mapokezi akakutana na akina dada wawili warembo,Akajitambulisha na kuoma kuonana na Patrick.
“Patrick kwa sasa yuko mapumzikoni nyumbani kwake.Alipatwa na matatizo ya moyo hivi karibuni hivyo amepewa muda wa kupumzika .Labda tukuelekeze nyumbani kwake kama kuna ulazima wa kumuona yeye mwenyewe ”
Margreth akaelekezwa nyumbani kwa Patrick kisha akaaga na kuondoka.
Ilimchukua kama masaa mawili hivi kuipata nyumba ya Patrick.Kwa mujibu wa ramani aliyopewa alitumaini pale palikuwa ni penyewe kabisa.Taratibu akalisogelea geti kubwa la mbele na kubonyeza kitufe cha kengele.Baada ya kama dakika nne hivi dada mmoja mrembo ,aliyevalia nadhifu akafungua mlango.
“Karibu dada” Yule dada akasema
“ahsante sana” Margreth akajibu
“sijui nikusaidie nini?
“Samahani dada ,sijui hapa ndio nyumbani kwa Patrick?
“Yes ndio hapa.Una shida naye ?
“Yes nina shida naye ya kiofisi.Kuna mzigo wake ulipitia katika ofisi zetu.Baada ya kuona kimya kingi tukaona tumtafute.Nimekwenda ofisini kwake wakanieleza kuwa Patrick ni mgonjwa na wakanielekeza hapa nyumbani kwake.”
“Kweli dada ,Patrick ni mgonjwa ana wiki ya pili sasa anamumwa.Ana matatizo ya moyo kwa hiyo amepewa muda mwingi wa kupumzika.Hivi tunavyoongea amelala lakini ninaweza kumwamsha kama kuna ulazima wa kuonana naye sasa hivi.”
“Usijali dada ni masuala madogo tu ya kiofisi hivyo sioni kama kuna haja yoyote ya kumsumbua mgonjwa.Ila atakapoamka mwambie kuwa Margreth Kibaho alifika hapa.”
“Sawa dada Margreth karibu sana.Mimi naitwa Veronika.karibu basi hata ndani upate walau glasi ya maji.”
“Nashukuru sana dada Vero siku nyingine nitaingia ndani.Haya kwa heri”
Margreth akaondoka maeneo hayo huku kichwa chake kikiwa kizito mno kwa mawazo aliyokuwa nayo.
“Je yawezekana kweli Patrick akawa na mke?Inawezekana Vero akawa ndiye mke wa Patrick?Sasa nimepata picha kamili.Naona siku ile Happy alipopiga simu ya Patrick ikapokelewa na Vero na ndio maana akashindwa kupata kitu cha kuongea.Ok nitamshauri tujaribu tena kumpigia Patrick leo jioni.Aliwaza Margreth akirudi nyumbani.

*************************

Saa kumi na moja jioni Margreth akarejea nyumbani kwao na mtu wa kwanza kukutana naye alikuwa ni mama yake ambaye akamwita na kumuuliza
“margreth ,naomba unieleze kwa undani bila kunificha ni kitu gani kinachomsumbua dada yako?Nina imani ni lazima utakuwa unafahamu kinachomsumbua dada yako.Kutwa nzima amejifungia ndani,hajala kitu na wala hataki kuonana na mtu yeyote.wakuu wake wa Miss Tanzania wamekuja kuonana naye leo hii mchana lakini ameshindwa kuonana nao.na hata waandishi wa habari wamekuja kutaka kumuhoji lakini hao ndio kabisaaa hataki hata kuwasikia.Sasa hebu niambie kitu gani kinachomsumbua mwenzio?
“Mama hakuna jambo lolote alilonieleza mimi.Nimekuwa nikijaribu toka jana kumshawishi ili anieleze ni kitu gani kinachomsumbua lakini amekuwa mgumu kunieleza.Ni wazi hata mimi naona kuna kitu kinamtatiza .naomba uniachie kazi hiyo mama nitajitahidi kumdadisi.”
“sawa Margreth jitahidi mwanangu.hali ya dada yako si nzuri na inatia shaka.”
“tena mama nipeni chakula nimpelekee nitamkoroga mpaka atakula tu.”
Haraka haraka akapewa sinia la chakula na kwenda hadi mlangoni kwa Happy .Akasimama hapo mlangoni kwa takribani dakika moja akatega sikio na kwa mbali akaisikia sauti ya Happy akilia.Aliumia sana moyoni mwake kuona jinsi dada yake anavyoteseka namna ile kwa sababu ya mapenzi.
Akagonga mlango kisha taratibu mlango ukafunguliwa akaingia ndani.Ni wazi Happy alionyesha hali ya kukata tamaa kwa jinsi alivyosawajika.Macho yalikuwa yamemvimba kwa kulia.
“Happy jaribu kuwa jasiri dada yangu.Unajua mambo yanaweza kuwa magumu zaidi iwapo hautaonyesha ujasiri .Hebu kwanza nyamaza kulia ule chakula.Mama anawasiwasi sana juu yako.”
Happy akamtazama mdogo wake usoni kisha akasema
“Najua ni rahisi kutamka hivyo kwa sababu wewe hayajakukuta.Ungekuwa katika mahala pangu , sijui ungefanya nini.Huwezi jua ni maumivu kiasi gani niliyonayo moyoni .Naumia sana Margreth.Patrick amekitonesha tena kidonda kilichokuwa kimeanza kupona.”
“Ok Dada Happy tulia basi ule halafu nikwambie habari za leo”
“Hebu nieleze kuna habari gani huko utokako? Akauliza Happy
Margreth akavuta pumzi ndefu akajiweka sawa na kusema.
“Nilipotoka hapa nikaelekea moja kwa moja katika zilizo ofisi za Patrick kwa mujibu wa wa hii businesscard inavyoonyesha.Nilifika katika ofisi hizo na nikaambiwa kuwa Patrick hayupo anaumwa .amepatwa na mstuko wa moyo na hivyo yuko nyumbani kwake anapumzika.Wakanielekeza nyumbani kwake nikaenda nikamkuta dada mmoja anaitwa Veronika .Akanikaribisha ndani na kutaka kwenda kumwamsha Patrick lakini sikuingia ndani nikamuachia ujumbe kuwa akiamka amwambie kuwa nilifika pale.Kwa ufupi ndiyo hivyo.” Akasema Margreth.
Happy alibaki ameshika tama asiamini alichokisikia kutoka kwa Margreth.Kilichomfanya anyong’onyee ni kusikia kuwa Margreth alikuta msichana pale nyumbani kwa Patrick.
“Najua kabisa huyu ndiye aliyeipokea simu siku ile nilipopiga.Yawezekana akawa ni mke wake? Au mchumba wake? Ni lazima nimpate Patrick ili nipate ukweli toka kwake.Yes ni muda mrefu umepita lakini…….”Alikuwa katika mawazo mazito wakati simu ya Margreth ilipolia.Alikuwa ni Mike Camble mchumba wa Happy .
“Ni mike” Akasema Margreth huku akimtazama Happy.
“Mwambie sipo “ Akasema Happy huku amejishika kichwa.
Alichanganyikiwa ghafla.Tayari alikuwa amekwishaanza kukubali matokeo kuwa Mike ndiye mtu wa maisha yake lakini Ghafla sana ametokea Patrick na kumfanya Happy achanganyikiwe.Margreth akaweka sauti kubwa ili Happy asikie watakachoongea.
“hallow Mike”
“hallow margreth mambo vipi?
“safi tu Mike habari ya huko?
“Huku kwema vipi huko?
“Huku nako kwema tu”
“Hebu niambie Margreth mbona Happy simpati katika simu?Nimejaribu sana kuitafuta simu yake lakini haipatikani kabisa.nilipata taarifa kuwa amefanikiwa kulitwaa taji la Miss Tanzania lakini akapatwa na mstuko akaanguka na kupoteza fahamu.Mara ya mwisho alinipigia simu kabla hawajaanza mashindano toka hapo sijapata mawasiliano yoyote toka kwake.Hebu nieleze margreth nini kimetokea?
Margreth akamtazama Happy kisha akasema
“Happy alipatwa na mstuko kidogo baada ya kutangazwa mshindi.Lakini kwa sasa anaendelea vizuri.Kuhusu mawasiliano ni kwamba simu yake bado hata hakumbuki aliiweka wapi ngoja kwanza atulie kabisa atakupigia Mike”
“Ok nimekuelewa margreth upo karibu naye hapo walau niongee naye kidogo?
“Hapana niko mbali naye kwa sasa.Labda ujaribu kupiga tena baadae”
“Ok margreth nimeomba wiki mbili za dharura ili niweze kuja Tanzania kukaa naye katika kipindi hiki kigumu alichonacho.Kesho nitaanza safari.Lakini usimwambie chochote .Nataka nimshangaze kidogo.Nitakujulisha kabla sijaanza safari yangu.
“Ok Mike bye”Margreth akajibu na kukata simu.
Happy alijilaza kitandani mikono ikiwa kichwani.
“why me ?Nampenda Mike .Yes nimeshakubali kuvishwa pete ya uchumba na Mike sasa ni kwa nini Patrick ametokea na kufanya akili yangu iyumbe namna hii?
Happy alijikuta tena katika mtihani mgumu.Ni wazi alimpenda Mike lakini baada ya kutokea Patrick taratibu ameanza kuonyesha dalili za kuanza kumsahau Mike
 
Back
Top Bottom