Serikali ya JK yapata kiwewe

MwanaFalsafa1

JF-Expert Member
Feb 26, 2008
5,565
836
  • BAJETI imeleta kiwewe.
  • Wabunge wamekuwa mbogo kwa kuikamia serikali
  • Kila mmoja anaongelea masuala ya jimboni mwake kana kwamba uchaguzi mkuu ni kesho.
Ndani na nje ya bunge, wabunge wanaonyesha wazi hisia zao za kutaka kukomboa majimbo yao na kwamba bajeti ya mwaka 2009/2010 iliyowasilishwa bungeni Alhamisi iliyopita “ni kitanzi.”

Michango ya wabunge wote, wale wa kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wale wa upinzani, inaashiria kukaba koo serikali, kuibebesha tuhuma na lawana ili wabunge kujiondolea uwezekano wa kutoaminiwa na kushindwa uchaguzi mwaka kesho.

Godfrey Zambi, mbunge wa Mbozi Mashariki (CCM), akizungumza nje ya Bunge alisema hakuomba kuchangia kwa kutoa hotuba bungeni, bali atachangia kwa maandishi.

Alisema, “Ni kweli kuna mambo mazuri katika bajeti hii, lakini kuna mambo mengi ambayo yakipita kama yalivyo yanaweka pabaya mustakabali wa mbunge.”

Kwa mfano, Zambi alisema serikali inaimba “Kilimo Kwanza,” lakini katika bajeti kilimo kimepewa kipaumbele cha nne na kutengewa Sh. 666.9 bilioni tu, huku elimu, afya na miundombinu vikiwa vinaongoza.

“Katika hali hii, huwezi kusema Kilimo Kwanza. Huu ni msemo tu, na tumekuwa na misemo mingi ya aina hii ambayo ni vigumu kutekelezeka. Tulikuwa na Azimio la Musoma na mengineyo mengi, lakini hakuna kitu,” alisema Zambi.

Mbunge wa Nzega (CCM), Lucas Selelii amefika mbali zaidi kwa kutaka baadhi ya mawaziri walaaniwe kwa kile alichoita, “Wamejiwa na roho mbaya.”

Alisema, “Mawaziri wa awamu ya nne wana roho mbaya. Mungu atawalaani. Wamekuwa wakiacha kutengeneza barabara zenye kuleta chachu za maendeleo na badala yake wamekuwa wanapeleka maendeleo katika maeneo wanayotoka.”

Alisema barabara zilizotengewa fedha ni zile ambazo tayari zina hali nzuri, lakini zile ambazo ziko katika hali mbaya, wameamua kuzipa kisogo.

Alisema, “Nanyi mliookaa mbele muone aibu (akimaanisha mawaziri na naibu mawaziri), na muyaogope makaburi. Kwa kuwa marehemu wanasema sisi tuliolala hapa tulikuwa kama ninyi. Mnajenga barabara za wilaya tu na kuacha za kuunganisha mikoa.”

Alisema, “Wallah, watu hawa wana hila na CCM. Nenda jimboni kwa Spika (Samwel Sitta), Tabora utafikiri unaenda jehanamu… Lakini Tabora imeachwa ukiwa. Ukiwauliza wanakwambia mipango ipo mbioni… Naamini hawa wana nia mbaya na wabunge wa CCM,” alisema kwa hasira Selelii.

Akichambua bajeti kifungu kwa kifungu, Selelii alisema barabara nyingi zilizotengewa fedha hazina makisio na makadirio na hivyo hazionyeshi zitamalizika lini.

Kuhusu kampuni inayoendesha Reli (RITES), Selelii alisema kampuni hiyo na menejimenti ya sasa havifai kuendesha Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) na kutaka serikali kuwafukuza mara moja.

Baada ya Selelii kumaliza kuchangia, alisimama mbunge wa Pangani (CCM), Rished Abdalah na kuomba mwongozo wa Spika kutokana na kile alichodai, mbunge mwenzake (Selelii) amevunja kanuni ya Bunge.

“Mheshimia Spika, Kanuni ya 68 ya Bunge inakataza mbunge kutoa kauli za kuudhi. Mbunge aliyemaliza kuchangia hivi sasa, ametoa kauli za kuudhi hasa pale alipotamka ‘Mungu awalaani mawaziri.’”

Hata hivyo, Spika Sitta aligoma kumtaka Selelii kufuta kauli yake; badala yake alisema ndani ya Bunge kuna uhuru mpana wa kuzungumza na kwamba hana uwezo wa kuzuia “hasira za wabunge.”

Alisema mbunge amepandwa na jazba na ametoa hisia zake. Kwanza, “Dua la kuku halimpati mwewe,” alisema Sitta katika hali ya kuliwaza mawaziri.

Awali Selelii aliomba mwongozo wa Spika akitaka kujua chanzo cha fedha zinazotumika kujenga barabara ya Chalinze–Segera–Tanga kabla ya bajeti kupitishwa.

Alihoji, “Mheshimiwa Spika, naomba mwongozo wako. Fedha zilizoombewa barabara hii ya Chalinze–Segera–Tanga bado hazijapitishwa. Sasa inajengwa kwa kutumia fedha zipi?”

Selelii pia alishauri uboreshaji huduma za bandari nchini na kusema kama serikali ingetumia vizuri fursa hiyo, taifa lingeendelea kwa kuwa Tanzania imezungukwa na nchi ambazo hazina bandari.

Aidha, alitaka serikali kuondokana na ukiritimba wa kampuni ya kupakia na kupakua mizigo bandarini (TICTS). Alisema, “Tuondokane na ukiritimba wa TICTS, sijui kwa nini tunainga’ng’ania…Yote haya yanakuja kwa ajili ya ufisadi,” alisema Selelii.

Naye mbunge wa Karatu (Chadema), Dk. Willibrod Slaa aliamsha hisia za wabunge juu ya sakata la ukwapuaji mamilioni ya shilingi katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA).

Alisema kwenye kitabu cha hali ya uchumi, serikali imesema imelipa asilimia 99 ya madeni ya ndani na nje, yakiwemo madeni ya waliokuwa wakidai kutoka akaunti ya EPA.

Katikati ya mshangao wa wabunge, Dk. Slaa aliuliza, vipi madeni hayo hayaonekani kwenye vitabu vya mwaka jana; na nani hasa wamelipwa.

Alitaka kujua serikali imelipa makampuni gani kutoka katika fedha za EPA, wakati maodita wanasema wadai hawapo.

Dk. Slaa alimbana Mkulo akitaka alieleze bunge ni kitu gani kilimzuia kuwachukulia hatua viongozi wa dini ambao walibainika kufanya ufisadi kupitia misamaha ya kodi.

Alisema kamwe hawezi kuunga mkono bajeti hiyo kwa kuwa serikali imeshindwa kuchukulia hatua baadhi ya viongozi wa dini na badala yake serikali imefuta misamaha ya kodi.

Alisema taasisi za dini, kwa miaka mingi, zimekuwa zikipeleka huduma mbalimbali kwa wananchi wa vijijini ambako serikali haifiki na kusema kuwa kitendo cha kuondoa msamaha huo ni cha kuwakatisha tamaa wao na wanaowasaidia.

Dk. Slaa alihoji kama ni kweli taasisi hizo za dini zilikuwa zikitumia vibaya misamaha hiyo, kwa nini watumishi wa serikali nao wasichukuliwe hatua kwani ni dhahiri walikuwa wakilifahamu hilo.

Pia alihoji ni kwa nini kabla ya kufutwa kwa kodi kwa upande wa makampuni ya madini, serikali ilijadiliana na viongozi wake, lakini haikufanya hivyo kwa viongozi wa taasisi za dini.

Akizungumzia kampuni ya RITES, alisema tangu wawekezaji hao wakabidhiwe menejimenti ya shirika hilo, hakuna chochote cha maana walichofanya zaidi ya serikali kuendelea kuwabeba kila kukicha kwa kulipa mishahara ya wafanyakazi na huduma nyingine.

Dk. Slaa alijenga mashaka kuwa huenda wawekezaji hao walipata zabuni hiyo “kwa njia ya pembeni. Hawa wafukuzwe hawafai kabisa. Tangu wameingia hatujaweza kuimaisha huduma zetu kwa kubeba mizigo mingi kutoka nchini Congo DRC, kwani kule kuna tani zaidi ya milioni 10, lakini mpaka sasa tunaendelea kusafirisha tani 400,000.

“Tutaendelea kulia umasikini na kutumia kisingizio cha mtikisiko wa uchumi, na hawa wachumi wetu wangekuja tuwashauri. Mheshimiwa Spika kweli inauma,” alisema.

Mbunge wa Lupa (CCM), Victor Mwambalaswa alisema kwa kuwa sehemu kubwa ya fedha zilizomo kwenye bajeti hiyo zitakwenda kwenye manunuzi, ameitaka wizara kujipanga vizuri ili kudhibiti matumizi ya fedha hizo.

Pia alipongeza kitendo cha serikali kutoa Sh. 7 bilioni kusaidia kampuni ya Artumas kuendelea na mradi wa umeme mkoani Mtwara, lakini alishauri serikali kununua hisa katika kampuni hiyo na kisha kuzikabidhi Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC).

Kwa upande mwingine, mbunge huyo aliiomba Mamlaka ya Nishati na Maji (EWURA) kuvifuatilia vituo vya mafuta vilivyopo kati ya Kibaha na Mlandizi, kwani vimekuwa na tabia ya kuchanganya dizeli, petroli na mafuta ya taa.

Alisema katika kipande hicho cha kilometa 20, kuna vituo 27 na kwamba nyuma ya vituo hivyo kuna maboma makubwa ambako kazi ya kuchanganya mafuta hayo inafanyika.

“Nawaomba EWURA wafuatilie, kwani kwa kufanya hivyo wanaikosesha mapato serikali na pia wanaharibu magari ya Watanzania. Pia huu ni ufisadi, hata Mungu hapendi. Naomba serikali iweke rangi katika mafuta ya taa, ili wakichanganya wabainike kwa urahisi, ” alisema.

Nayo hotuba ya upinzani kujibu mapendekezo ya bajeti ya serikali, imesema serikali imepunguza mgawo kwa Wizara ya Nishati na Madini na kwamba ndiyo maana Shirika la Umeme (TANESCO) limetahadharisha kuwa nchi inaweza kuingia gizani.

Akisoma hotuba ya upinzani, Dk. Slaa alionyesha kuwa mwaka huu wizara imetengewa Sh. 285.5 bilioni ikilinganishwa na Sh. 378.8 bilioni mwaka 2008/09. Fedha hii ni pungufu ya asilimia 24.6 ya bajeti iliyopita.

Sababu ya kupunguza bajeti ya wizara, alieleza Dk. Slaa ni “kumalizika kwa mikataba ya kuzalisha umeme kwa makampuni ya kukodi ya Dowans, APR na Aggrekko.”

“Hili ni jambo la ajabu, kwamba serikali inatenga fedha ikiwa kuna mikataba ya kuifilisi nchi, lakini haiwekezi katika kuzalisha umeme wa uhakika,” alisema.

Upinzani umeishangaa serikali kukopa fedha na kuikopesha kampuni ya kufua umeme wa gesi ya Artumas ili iendelee kutekeleza mradi wa kuzalisha umeme kwa mikoa ya Mtwara na Lindi, lakini fedha hizo hazionekani kwenye bajeti.

“Kama serikali ina fedha kwa nini isiingie ubia na kampuni hiyo? Ni serikali hii iliyokataa kuyapa ruzuku mashirika ya umma... Je, sasa inakuwa bora kuzipa sadaka kampuni binafsi kwa kisingizio cha hali mbaya ya uchumi duniani?” upinzani umehoji.

Upinzani umesema utaratibu wa “cash budget” – uliopewa jina la “malipo ya dirishani,” unadhoofisha sana nidhamu ya bajeti, umeeleza upinzani na kuongeza kuwa miradi ya maendeleo inaathirika sana kwa utaratibu huu kwani ndiyo huwa ya kwanza kupunguziwa matumizi.

Bajeti za dirishani siyo makini na haziheshimiwi, imeeleza hotuba ya upinzani na kuongeza kuwa, utaratibu huo unaacha mianya mipana ya rushwa hasa katika maeneo ya kulipa madeni, kufidia hasara na kudhamini mikopo ya makampuni.

Leo mjadala wa bajeti unaingia katika siku ya tatu.

Source: Gazeti la MwanaHALISI
 
Mbunge wa Mbozi, Ndugu Godfrey Zambi amesema kweli. Msemo wa "Kilimo Kwanza" ni uongo uliokolea. Hauna maslahi yoyote. Ukweli ni "Elimu kwanza". Watu wanalima bila Elimu ndio maana hawaendelei. Tuache kudanganyana kwamba tunaona ni "Kilimo kwanza".

Mbunge wa Nzega amemtaka Mungu awalaani Mawaziri. Ni sawa kabisa! Nashirikiana na Mungu kuwalaani hao mawaziri.

Mbunge wa Nzega anashangaaje kuona barabara za kwenda kwa Sitta ni mbaya? Nani alimwambia Sitta anajali kwao? Sitta is too busy protecting Meremeta to think about non-places like Tabora.

Kwani si Rostam alimwambia Sitta agombee Uspika? Sasa kama Sitta atashughulikia barabara badala ya kulinda Meremeta si Rostam atakasirika?
 
Ndefu sana ...great thinkers hu-summarise mambo. Katika habari yako yote sentensi muhimu haizidi moja. Habari ndefu kwenye magazeti huko. Eboo!
 
Intelligent Analysis and advise from Dr. Slaa; kama tungekuwa na akina Slaa hata 20 tu ndani ya hili bunge ingekuwa tofauti! Angekuwa CCM ningesema 'd be our future President!!
 
Ndefu sana ...great thinkers hu-summarise mambo. Katika habari yako yote sentensi muhimu haizidi moja. Habari ndefu kwenye magazeti huko. Eboo!

Great thinkers are also great readers. Don't blame others for your lack of interest to read things. Na siyo habari yangu ungekua msomaji ungegundua chini kuna source inayoonyesha kuwa inatoka kwenye hayo magazeti unayo sema wewe. Hebu angalia vizuri kabla ya kucomment bana unaishia kujiumbua pasipo sababu.
 
Mi naona wameona jamii inavyoheshimu wabunge wenye uthubutu na walio tayari kwa lolote,lakini la uchaguzi mwakani inaweza likawa changizo hulka ya binadamu nikutopenda kushindwa
 
bunge la safari hii ni very interestng...at least you can sense some mind and eyes opening from MPs, thanks to the oposition MPs, kuna wabunge walikuwa wanaona ni zambi kuikosoa au kuipinga serikali, and believe me pamoja na ujasili wao watakuwa na consequences...we know CCM very well...
Tatizo letu Tanzania, pamoja na kelele zote zile, maswali ya dr. Slaa, hoja za Selelii, hotuba ya upinzani...Nothing has changed and the budget was endorsed..inakuwa kama ni kelele za mpangaji...
lakini wabunge na CCM wajue kwamba..WATU WANAWATIZAMA, WANAONA, WANAWASIKIA KWALE WANAYOSEMA,WANAYOFANYA....tutawahukumu kwa hilo, wanakula pesa za walipa kodi halafu wanazani they can just get away with it...tusipouliza sisi watakuja kuuliza watoto wetu tunaowaachia umaskini ukiojengwa na wazee wao....
 
Back
Top Bottom