Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Sambusa ni tamu bwana,
Nyingine hakuna tena,
Wa kijiji ninanena,
Vingine sijaviona! - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Ukishaonja sambusa,
Vitumbua utasusa
Na utatumia mapesa,
Uje upate sambusa! - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Na zile zenye mafuta
Ulimini zinanata,
Na ladha ukishapata
Waweza tangaza vita - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Zipo zenye nyamanyama
Zaliwa Kijitonyama
Hata ukenda Dodoma
Sambusa hutojinyima - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Zipo zile zenye mboga
Zilochumwa kama boga
Wale wasio waoga
Wazila hata Msoga! - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Zipo zenye vitunguu
Zilotiwa karafuu
Ukila mluzi huu
Waimba "mikono juu" - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Na sambusa za Kihindi,
Utazikuta Malindi
Hata Mtwara na Lindi
Zinapikwa na mafundi! - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Uonje 'zopikwa Tanga
Ngonjera utazitunga
Ukipata za Iringa
Na baridi la Mafinga - sambusa ni tamu bwana, hasa zisizofanana!
Beti zangu nazifunga
Tungo nimeshazipanga,
Sambusa sitojivunga
Nayeya ninapuyanga
SAMBUSA NI TAMU BWANA, HASA ZISIZOFANANA!
Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)