Riwaya: Mji tulivu ulionipa gonjwa la milele

mzaramo

JF-Expert Member
Sep 4, 2006
6,371
5,174
IMEANDIKWA NA:GEORGE IRON MOSENYA

SEHEMU YA 1

IMEANDIKWA NAYE: George Iron Mosenya
SEHEMU YA KWANZA
Maisha wakati mwingine si jitihada pekee zinazoweza
kukutoa sehemu moja kwenda nyingine, kuna wakati
bahati inahusika katika maisha.
Si kwa wote lakini mimi nilibahatika kuwa mtoto
kutoka familia ya kimasikini ambaye baadaye nilienda
kusoma na kisha kupata kazi nzuri ambayo ilinitoa
katika umasikini na kunitupa katika daraja la kati na
baadaye nikawa tajiri.
Nikayabadili maisha ya kizazi changu na kuwaweka
katika mirija ya kujiendesha wenyewe.
Hadi ninafikisha miaka thelathini tayari nilikuwa
nimeyaweka maisha yangu sawa, nikiwa nimesaidia
ndugu zangu kwa kiwango cha uwezo wangu pamoja na
marafiki pia.
Baada ya kutimiza ndoto hizi ndipo kwa mara ya
kwanza nikafikiria juu ya utulivu wa hali ya juu
niliokuwa nauhitaji na niliwahi kuuota tangu nikiwa
nasoma, nilijiahidi kuwa nitakapomaliza kuinyanyua
familia yangu sasa nitaangalia vyema maisha yangu.
Niliwahi kuwa na marafiki wa kike lakini sikuwahi
kunyanyua kinywa changu na kuwatamkia kuwa nina
nia ya kuingia nao katika ndoa.
Nilikuwa nina deni, sikutaka nijiongezee majukumu
mengi yatakayosababisha nishindwe kutimiza vile
nilivyopanga kutimiza.
Katika mkesha wa mwaka mpya nilimpigia mama yangu
simu na kumweleza bayana kuwa ndoto mojawapo
katika mwaka unaoanza ni kuyabadili maisha yangu
kwa kujihifadhi katika mji tulivu.
Akaniuliza iwapo nataka kuhama Tanzania, nikacheka
na kumweleza kuwa sina wazo la kuhama Tanzania bali
nahitaji kuingia katika mji tulivu.
“Unataka kuoa?” mama aliniuliza.
Nikacheka bila kumjibu chochote, naye akacheka kisha
akanitakia kila la heri. Nikampongeza kwa kuelewa
maana yangu upesi sana!
_____
Mwaka ulianza vyema na shughuli zikiendelea kama
kawaida huku lile wazo likiwa kapuni kusubiri
utekelezaji wake.
Naomba niweke wazi kuwa nilikuwa aina fulani ya
mwanadamu ambaye napenda sana kufanya jambo
kadri ya wakati, maana niliwahi kufanya mambo mengi
kwa wakati mmoja na kujikuta nikiharibu ama
kutoyafanya kwa ufanisi mambo mengine.
Hivyo sikuwahi kupanga siku ya kuusaka mji ule
tulivu!!
Siku hii ikiwa ni miezi miwili baada ya mwaka kuanza
pale ofisini kwetu palikuwa na nafasi za kazi zilikuwa
zimetangazwa na watu wengi sana walikuwa
wameomba nafasi. Katika ile hatua ya awali ya usahili
walifika wasahiliwa mia moja na hamsini.
Nafasi zilikuwa tano tu zilizokuwa wazi. Katika ngazi
ya mwisho kabisa nd’o ambayo mimi na wakurugenzi
wenzangu tulikuwa tunahusishwa lakini hatua za awali
walisimamia wenzetu waliokuwa na vyeo vya chini.
Baada ya hatua za awali hii siku ndiyo ilikuwa ile ya
kupata mbivu na mbichi.
Wasahiliwa ishirini wa mwisho.
Katika usahili nilikuwa natazamwa sana, hakika
sikuwa mtu wa mchezo, ukifanya vibaya usitarajie
kuwa nitakubeba kisa tu u msichana ama umeonyesha
huruma ya aina yoyote.
Sikuwa mtu wa aina hiyo kabisa, na kilichokuwa
kinanifanya niwe hivi ni njia ambazo nilikuwa
nimepitia, hakuna njia ya panya yoyote niliyopitia
katika safari yangu ya kimasomo hadi kutafuta kazi.
Na pia nilikuwa nina hofu na Mungu!
Kitendo cha kumpitisha mtu asiyekuwa na vigezo na
kumwacha mwenye vigezo kungeisononesha nafsi
yangu sana.
Katika usahili nilikuwa naogopwa sana.
Hata siku hiyo nilikuwa yuleyule, maswali yangu
yalikuwa si magumu lakini yenye mitego. Maswali
yangu yakiwa na nia moja tu, kuupima uelewa halisi
wa msailiwa.
Walipita wasahiliwa wote katika hatua ya kwanza,
niliwanukuu majina yao.
Baada ya hatua zote za usahili kumalizika hatimaye
tuliwaeleza kuwa baada ya majuma mawili tutawapigia
simu katika nambari walizotuachia.
Tukawaaga wakaondoka!!
Masuala ya usahili yakaishia hapo…..
Nikaendelea na shughuli nyingine hadi majira ya saa
tatu usiku ndipo niliifunga ofisi yangu na kutoka nje
kuelekea katika gari langu.
Nilifungua mlango na kuiwasha gari nikaiacha
ikiunguruma kwa muda huku nikiwa nimewasha
kiyoyozi ili kuleta hewa safi, mara nikasikia hatua
zikijongea nilipokuwa. Nikatambua huyo atakuwa
aidha mlinzi ama kijana mwingine tu amekuja
kuniomba shilingi mia tano.
Nikaandaa hiyo pesa ili tusizungumze sana.
Sikuwa napendelea sana kusikiliza maelezo yao kwa
sababu huwa wanadanganya wana njaa kisha ukiwape
pesa wanaenda kujidunga madawa ya kulevya.
“Samahani kaka…” nikaisikia sauti ya kike.
Nikageuka upesi kumkabili anayeniita, sikuitarajia
kabisa sauti ya kike muda ule. Sikuwa na mazoea na
watoto wa kike kabisa. Mazoea ya kikazi yalitosha
kabisa!
“Nikusaidie nini?” nilimuuliza bila kuijibu salamu yake.
“Naitwa Nyambura…. Naitwa Nyambura Kone…”
alijitambulisha jina lake.
“Samahani sidhani kama nakufahamu..” nilimjibu huku
nikijiandaa kuingia garini ili niondoke.
Akajieleza kuwa siku hiyo alishiriki usahili katika
kampuni ninayofanyia kazi.
Aliposema vile jina likanikaa sawa kichwani.
Anataka kutoa rushwa!! Nilijiwazia huku nikimsikiliza
aendelee kuzungumza na hapo nikamwomba ajieleze
kwa haraka kidogo, kichwani tayari nikiwa nimepanga
shambulizi kubwa na kumpa ili nimuaibishe ikiwa
atanishawishi kunipa rushwa ya aina yoyote, tena
bora angezungumzia pesa ila akithubutu kunieleza
rushwa ya ngono hata vibao nitamchapa hadharani.
Akajikohoza kisha akazungumza.
“Naitwa Nyambura..” nikamzuia kwa mkono na kumsihi
aendelee kwani jina lake tayari alilitaja awali. Na
huku niliona ni kupoteza muda anakoelekea.
Yule binti aliyejitambulisha kwa jina la Nyambura Kone
akajieleza.
“Mimi ni mtoto wa tatu katika familia yangu…
nimetoka Musoma vijijini kuja jijini Dar es salaam kwa
ajili ya usahili huu, usahili ambao naamini kuwa kwa
leo hakika sijafanya vizuri, lakini hiyo sio tafsiri ya
jinsi nilivyo, ninauguliwa mama yangu na sijui hata
kama nitamkuta akiwa hai, sijala tangu nilipokula
jana mchana, zaidi ya yale maji mliyotupatia sijala
chochote….. nimekuja kwa miguu katika usahili na
nitarejea kwa miguu kama unavyoniona…. Nakusihi
sana na sijui kwanini nimekusudia kuonana na wewe
lakini nakuomba utakapofanya maamuzi basi nipe
nafasi ya upendeleo. Sipo kama nilivyojaribu kujieleza
katika usahili…. Nina matatizo makubwa sana
yananikabili… ni matatizo yangu na si ya kampuni
yenu lakini nakuomba kwa maelezo yangu haya mafupi
unisaidie uwezavyo. Mama yangu anakufa, lakini
wadogo zangu wanahitaji kula, achana na kusoma
maana imeshindikana tayari… mimi ni kila kitu kwao.”
Aliweka kituo yule binti. Akabaki kunitazama
Maneno yake hayakunishawishi sana, kwa sababu
ninaamini katika ushawishi wa katikati ya chumba cha
usahili na si vinginevyo.
Nikaitoa pochi yangu na kutoa noti tatu za shilingi
elfu tano nikampatia kama nauli na nikamweleza kuwa
nimesikia ombi lake.
Nilimweleza ilimradi tu kuyamaliza yale mazungumzo,
aondoke na mimi niondoke.
“Namba ya simu si yangu ni ya huyo aliyenipokea, ikiwa
nitapata nafasi ya kupigiwa simu utamwambia
anifikishie ujumbe.”
Akamaliza kunisihi huku akishindwa walau kutoa
shukrani kwa kiasi cha pesa nilichompatia.
Hakika jambo lile liliniudhi sana, nikahisi huyu ni
changudoa aliyebobea na kwangu mimi alitaka pesa
nyingi ili niununue mwili wake, sasa sijaununua na
nimempatia kiasi kidogo cha pesa.
Pesa zangu ziliniuma sana!
Niliondoka pale lakini sikwenda nyumbani moja kwa
moja, sikuwa nimeoa niliishi peke yangu. Hivyo
ilinilazimu kupita hotelini kupata chakula.
Kitendo cha kuondoka eneo lile nikamsahau na
kumpuuzia yule dada aliyejitambulisha kwangu kwa
jina la Nyambura!
Nilipomaliza kupata chakula, wakati nalipia bili ndo
nikamkumbuka tena Nyambura na kujisemea kuwa laiti
kama nisingempatia ile pesa basi ndo ningeitumia
kulipa ile bili ya chakula.
Niliondoka pale, sasa nilikuwa naelekea nyumbani.
Tofauti na siku zote, nilishangazwa na ile foleni
katika barabara ya Morogoro kutokea Kariakoo
nilipopitia, nilitazama saa yangu na ilikuwa saa nne
usiku. Foleni ilikuwa kubwa kiasi kwamba gari zilikuwa
hazitembei kabisa.
Taratibu taratibu hadi gari ikafikia kile chanzo cha
foleni, kuna ajali ilikuwa imetokea.
Nilipotambua kuwa ni ajali nikapandisha vioo vya gari
langu, kwani mazingira kama hayo kwa jiji la Dar es
salaam huwa vibaka nao wanaingia kazini.
Lakini nilibaki kutazama nione hiyo ajali kupitia kioo
kwenye kioo.
Hapo sasa gari zilikuwa hazitembei kabisa, nikashusha
vioo na kujaribu kuwauliza madereva waliokuwa
wameshuka.
Wakanieleza kuwa njia imefungwa kwa mbele, raia
wamegomea gari zisiondoke kwa sababu katika hii
foleni ipo gari iliyogonga!
Niliishiawa nguvu nikaamua kushuka na mimi garini.
Nilidadisi na kuelekezwa majeruhi alipokuwa.
Nilifika na kujikuta natazamana na mwanamke
aliyejivika mavazi mafupi sana yaliyouacha mwili wake
wazi, vijana wa pembeni wakawa wanamteta
wakisema kuwa ni changudoa alikuwa kazini. Mwil
wake ulikuwa umetokwa na fahamu na hakuonekana
kujeruhiwa sana…..
Maneno yale yakapenya na kunifikia, nami nikakiri
kuwa huenda kweli ni changudoa.
“Unasema changudoa… unamaanisha changudoa ana
haki ya kugongwa na gari akiwa upande wake sahihi….
Sharia ya wapi uliyoisoma wewe inayoruhusu mtu
kugongwa na gari kwa sababu tu ya shughuli zake….
Sikiliza kaka usipokuwa na uhakika na kitu ni heri
ukakaa kimya! Angekuwa dada yako ungesema sawa
afe kwa sababu ni changudoa!!!” ilisikika sauti kali ya
kike ikijibu mapigo kwa jazba.
Nikaguswa na maneno yake, kwa sababu nami na elimu
yangu nilikuwa nimekiri kuuwa ni sawa tu agongwe
kwa sababu ni changudoa.
Nikageuka kutazama ni nani anayetokwa na maneno
yale makali.
Nyambura!! Mungu wangu, nilishtuka sana.
Sijui ni kwanini nilishtuka vile, lakini kuna kitu kama
hofu kiliniingia.
Nikachelewa kubandua macho yangu kwake, mwishowe
nikajikuta natazamana naye.
NAKUSIHI!!
Usimuhukumu mtu yeyote kwa sababu ya muonekano
wake, kwa sababu ya kipato chake, kwa sababu ya
kabila ama imani yake kidini.
 
NA HII NI SEHEMU YA PILI

Baada ya yule dada kutonitambua sikupoteza wakati
zaidi eneo lile, nilihisi kuwa na yeye ni walewale.
Nikazikumbuka pesa zangu, na hapa nikakiri kuwa yule
binti alikuwa ananitaka kimapenzi hakuwa na lolote la
ziada, sasa Mungu kawapa pigo.
Nikajiondokea nikaingia kwenye gari na hapo foleni
ilikuwa inaanza kusogea. Bila shaka huko mbele
palikuwa pamesuluhishwa tayari.
Nilifika nyumbani kwangu nikiwa nimechoka sana
nikajitupa kitandani, kwanza nikapitiwa na usingizi
nikaja kuamka baadaye sana nikaoga na kulala tena.
Asubuhi nilikuwa nimemsahau yule dada na vimbwanga
vyake.
_____
BAADA YA JUMA MOJA, majina yalikuwa yametoka
tayari. Sikukumbuka wala sikujali juu ya yule dada
ambaye alihitaji nimsaidie aweze kuchomoza na kwa
jinsi nilivyompa alama chache katika ule usahili basi
ilikuwa lazima tu aanguke.
Kweli hakuwemo!
Nilikuwa ofisini kwangu nikapokea simu kutoka kwa
Hadija ambaye ni katibu muhtasi wangu, nikaipokea
upesi na kumsikiliza huku nikimsihi kuwa nitapenda
zaidi kama atazungumza kwa muda mfupi. Alinieleza
kuwa yupo mtu anahitaji kuonana na mimi na amesihi
sana kuwa ni muhimu.
Nikamruhusu aingie.
Zikapita sekunde kadhaa kabla mlango wangu
haujasukumwa.
Alisimama mbele yangu yuleyule binti, Nyambura!
“Shkamoo..” alinisalimia.
Nilisita kuitikia kwa sababu nilitambua wazi kuwa umri
wake haukuwa wa kuniambia mimi shkamoo.
Alisalimia tu kwa sababu ya nidhamu ya uoga.
“Habari yako…” nikamsabahi.
“Jina langu halipo katika orodha,” alisema kisha
akaendelea, “Ni kwa sababu haukuweza
kunisaidia…..” akajaribu kuzungumza lakini akakosa
cha kusema. Akabaki kutupatupa mikono hewani.
“Kuna jingine labda naweza kukusaidia…” nilimuuliza
huku nikipambana kuizuia hasira yangu isichukue
nafasi kubwa.
Maana niloiona yule binti ananichukulia mimi dhaifu
kama wanaume wengine….
Akazungumza huku akiwa amesimama, akanieleza
kuwa mama yake alikuwa amepoteza maisha tayari.
Akanisihi kama ninao msaada wowote ili aweze kufika
Musoma basi nimsaidie.
“Ujue ile siku ya kwanza nilipokusaidia sio kwamba
nilikuwa boya sana, naomba uondoke na kamwe usirudi
hapa….” Nilimkaripia huku nikisimama.
Akanikazia macho yake kisha akazungumza.
“Unaweza kunipiga kama utahitaji… mwili huu
umezoea suluba tayari.” Alinijibu kiujasiri.
Kisha akaendelea kuzungumza, alisema mengi sana
ambayo labda yangemgusa mwanaume wa kawaida,
lakini mimi yalionekana kama maigizo tu na hakuna
alichokuwa anamaanisha.
Hakika sikumsaidia kitu chochote.
“Naitwa Nyambura! Asante sana kaka kwa moyo
wako….” Alimaliza kisha akaondoka.
Alipoondoka nikatazama fungu la pesa lililosheheni
katika meza yangu pale ofisini, pesa ambayo niliipata
kwa kazi isiyokuwa ya kutoa jasho.
Kwani ningempa hata laki ningepungukiwa nini!
Nilijiuliza.
Nikanyanyua simu ya ofisini, nikampigia Hadija na
kumuuliza kama yule binti anaonekana pale amwite.
Akanambia kuwa amepita kasi huku akiwa analia sana.
“Kwani umemfanyaje?” aliniuliza.
Moyo ukaniuma, nikakata simu na kujikuta najuta.
Hivi ninakuwaje mimi! Sasa najuta nini? Si ni ukweli ni
malaya yule na ananiongopea tu hapa au!!
Nilijifariji lakini bado moyo wangu ulikuwa hauna
amani.
Ilikuwa kawaida yangu nikiwa naikosa amani ya nafsi
basi huwa nampigia mama yangu mzazi na ananishauri
ama kunitia moyo.
Hata siku hii nilimpigia pia.
Nikamweleza juu ya hali ile, ilimsikitisha pia lakini
mwisho alisema kuwa mjini pana mengi.
Huenda hata huyo ananiongopea tu!
Akanisihi niwe na amani.
Kweli amani ikatawala.
Nikaachana na Nyambura.
_____
Baada ya miezi miwili kupita afisa habari wa kampuni
alipoteza maisha kwa kile kilichosemekana alikula ama
kulishwa chakula chenye sumu, hivyo baada ya muda
fulani nafasi ya kazi ikatangazwa.
Na kitendo cha kuwa na afisa habari mmoja
kilisababisha wakurugenzi na bodi nzima wapendekeze
kupatikana kwa maafisa habari wawili yaani mtu na
msaidizi wake.
Nafasi za kazi zikatangazwa magazetini. Kama
kawaida wasahiliwa kutoka kila kona wakafika na
bahasha zao za kaki siku ya usahili.
Kwa sababu afisa habari alihitajika upesi sana usaili
huu ulifanyika siku mfululizo.
Hatimaye yakabaki majina sita ya mwisho.
Hawa walipangiwa siku yao, wanawake watatu na
wanaume watatu.
Ikafika siku yao ya usahili wa ziada kama ulivyo
utaratibu wa kampuni.
Wasahiliwa wakaingia mmoja baada ya mwingine.
Hatimaye wakalifikia jina la Neema Wilson.
Akaingia binti ambaye kimavazi alipangilia kama
ilivyostahili, nikatazama katika karatasi zangu, binti
yule alikuwa vizuri katika lugha tatu… kifaransa,
Kiswahili na kiingereza.
Nikaamua kuwa mchokozi nikachagua kuzungumza
naye kifaransa katika usahili wake.
Kwa sababu wenzangu walikuwa hawajui lugha hii
wakaniachia mimi mwenyewe.
Nikanyanyua uso wangu ili nimtupie swali la kwanza.
Mungu wangu! Nilikuwa natazamana ana kwa ana na
Nyambura, yule binti kutoka Musoma ambaye aliwahi
kufanya usahili katika kampuni yetu.
Swali nililopanga kuuliza likayeyuka nikajikuta
natokwa na swali ambalo sikutarajia.
“Wewe ni Neema ama Nyambura….” Nilimuuliza.
Akanitazama kwa sekunde chache akiwa hana mashaka
hata kidogo akanieleza kuwa yeye ni Neema.
Nikajaribu kujiweka sawa nikauliza maswali ya msingi
kwa kifaransa, akanijibu vyema.
Nikamruhusu atoke.
Lakini nikimweleza kwa kifaransa kuwa aningoje nje!
Akatii!
Baada ya usahili nikaonana naye na kumuuliza kwa
mara ya pili jina lake ni nani.
“Naitwa Nyambura!” alinijibu bila wasiwasi.
“Na kwa nini umejitambulisha kama Neema.”
Nilimuuliza kitafiti.
“Neema ni jina langu pia. Unaweza kunitambua kwa
yote ukihitaji….” Alinijibu kisha akaniaga na
kuondoka.
Lakini kabla hajafika mbali aligeuka.
“Hauamini kama mimi ni Nyambura…. Ulinipa elfu kumi
na tano mara ya mwisho na sasa sijakuomba hata
kunisaidia ili nipate nafasi katika kampuni yako…”
alinieleza kisha akaondoka zake, akianiacha nisijue
kuna kitu gani kinaendelea.
Upesi nkatika ofisi yangu nikapekua nyaraka kadhaa
za wasahiliwa wa wakati ule wa Nyambura.
Nikakutana na nyaraka zinazoelezea wasifu wa
Nyambura… nikabahatika kuona viambatanishi.
Cheti chake cha kidato cha nne kiliandikwa jina
NYAMBURA na cha kidato cha sita pia.
Nikaviweka kando na kutazama hivi vya sasa.
Jina lilikuwa NEEMA…..
Ni kitu gani anaficha huyu binti? Nilijiuliza huku
nikizidi kushangaa ile kasi ya kuingia katika akili yangu
ilivyokuwa inaongezeka.

NAKUSIHI!
Sio kila ukionacho kinang’ara basi ni dhahabu hiyo,
kuna ming’aro mingine inatengenezwa ing’ae kuliko
dhahabu. Ilimradi tu kukuchanganya wewe unayetaka
dhahabu halisi…….
 
WAKATI mwingine katika maisha sio kila kitu ukionacho
ukubali kuwaza kukimiliki.
Kile kitendo cha kuiruhusu akili yako kuwaza juu ya
kumiliki kitu fulani, unajiwekea deni katika akili yako
na hapo akili inaanza kukulazimisha ulilipe.
Na uombe sana deni hilo lisiwe mahusiano ya kimapenzi

NA HII NI SEHEMU YA TATU.

KWA jinsi Nyambura alivyojieleza katika usahili basi
lingekuwa jambo la ajabu kumnyima nafasi ya uafisa
habari katika kampuni yetu.
Niliunga mkono nafasi ile akabidhiwe binti yule.
Katibu muhtasi akapiga simu, Nyambura akaanza kazi
rasmi.
Uchapaji kazi wa Nyambura ulinifanya nijisikie hatia
sana nilipoyakumbuka maneno yake siku alipokuwa
ananisihi sana nimsaidie apate kazi kwa sababu anao
ndugu wanamtegemea kwa dhati sana.
Nakumbuka kuwa nilimpuuza na kumwona kuwa na
yeye ni walewale.
Wasichana wa kileo
Kwa sababu yeye alikuwa ni afisa habari wa kampuni
na mimi nikiwa katika bodi ya wakurugenzi,
hatukuweza kuonana mara kwa mara kwa sababu
kama ni habari angeweza kuzikuta kwa katibu muhtasi
wetu!
Habari ikiwa nyeti sana ndo angeweza kuonana na
mkurugenzi moja kwa moja.
Waswahili wanasema kizuri chajiuza, kibaya
chajitembeza.
Sifa za Nyambura zilisambaa upesi sana, alikuwa ni
mfanyakazi makini sana anayeijali ofisi yake na
asiyekuwa na mazoea kama ya wafanyakazi wengine
ya kuanza kutegea kazi pindi wanapoizoea ofisi.
Nyambura hakuwa hivyo!
Haikushangaza pale alipopewa zawadi na kampuni
kutokana na utendaji kazi wake.
Kuajiriwa kwa Nyambura kukaifanya kampuni yetu ya
kusambaa kwa kasi sana mkoa kwa mkoa.
Nyambura hakuchoka wala kuonyesha dalili ya
kuchoka, alizidi kuchapa kazi.
Nyambura alikuwa zaidi ya afisa habari!
Miezi mitatu baadaye Nyambura alikuwa amejenga
ushawishi hadi kampuni yetu ikafungua tawi kubwa
jijini Arusha. Ni katika ufunguzi huu wa tawi
nilichaguliwa kwenda kukata utepe nikiwa kama
mkurugenzi mtendaji.
Na hapa nikatakiwa kuongozana na afisa habari wa
kampuni!
Nyambura!!
Ndugu msikilizaji, licha ya kwamba nilikuwa nina pesa
za kutosha lakini sikuwa mpenzi wa kusafiri kwa njia
ya ndege. Safari kama hizo nilikuwa natumia gari
yangu binafsi, aidha ninaendesha mwenyewe ama
namchukua dereva wa kuniendesha.
Safari hii pia niliamua tusafiri kwa kutumia gari
langu.
Niliketi na Nyambura kwa dakika kadhaa kuzungumzia
kitu ambacho tunapaswa kwenda kufanya kule,
hasahasa wakati wa kuzungumza na watu wa Arusha
juu ya kampuni yetu iliyokuwa inahusika na mambo ya
usafirishaji wa mizigo ndani na nje ya nchi.
Ni hapa ndipo nilipokiri kuwa Nyambura alikuwa anajua
jinsi ya kuzipanga karata na kumfunga mpinzani
wake, alizungumza hadi nikatamani hiyo siku yeye ndo
asungumze na wakazi wa Arusha mimi niwe kando.
Yule binti alikuwa na akili halafu na kipaji cha ziada…
Alikuwa anajiamini na hatoi neno lisilokuwa na maana
mdomoni mwake.
Safari ya Arusha ikaiva!
Tukaondoka na dereva, mimi na Nyambura tukaketi
nyuma tukiendelea kupanga mikakati ya hapa na pale.
Mikakati ilipomalizika tukaanza kupeana stori za hapa
na pale kuhusu maisha.
Kisha utani kidogo, nikakumbuka kumwomba msamaha
kwa kumcheleweshea kazi alipokuja katika usaili siku
ya kwanza.
Nyambura akacheka kidogo! Kisha akanitazama na
kuzungumza huku akiwa anatabasamu.
“Mama yangu alikufa… na wadogo zangu wawili
wakamfuata nyuma. Lakini mimi nipo hai na ananiona
ninavyopambana huko alipo…” alizungumza huku lile
tabasamu likitoweka katika uso wake.
Sikutaka tuendelee kuzungumza sana juu ya jambo
lile, kwa sababu niliona waziwazi kuwa nilikuwa
upande wa hatia kwa sababu alinieleza awali na bado
sikutaka kumtetea ili aweze kuipata ajira.
Nikabadili mada!
______
SHUGHULI za kikazi Arusha zilienda vyema kabisa huku
Nyambura akizidi kunidhihirishia kuwa yeye ni moto wa
kuotea mbali.
Siku ya mwisho ya kuwa Arusha nilimwalika Nyambura
chakula cha usiku katika hoteli niliyokuwa nimefikia.
Tukakubaliana muda wa kukutana.
Nilifika majira ya saa mbili, yeye akafika nusu saa
baadaye….
Nilimuona kuanzia mbali alivyokuwa anatembea
kimadaha, vazi lake la usiku lilikuwa limeukamata mwili
wake na kuufanya urembo wake kuonekana bayana.
Hata kabla hajanifikia niliweza kutambua kuwa
manukato yake yalikuwa yanatoa harufu mwanana
sana.
Nikajiskia fadhaa sana kwa sababu nilikuwa nimevaa
kawaida sana.
Wakati Nyambura alikuwa amejipanga vyema.
Alifika na kunisalimia katika namna ya kunikumbatia.
Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nikajikuta
natamani mwanamke aendelee kunikumbatia kwa muda
mrefu zaidi!
Nyambura akaketi tukaagiza chakula na vinywaji huku
tukivunja kanuni ya chakula, tulikuwa tunazungumza
tena mazungumzo yalikuwa mengi kuliko mwendo wa
kula chakula.
Usingeweza kumdhania hata kidogo kuwa huyu
Nyambura ndo yule afisa habari machachari wa
kampuni yetu.
Kila sekunde zilivyozidi kusogea mbele nami nikajikuta
nazidi kutamani kuendelea kuwa pamoja na Nyambura.
Nikapiga moyo konde na kumsihi twende chumbani
kwangu ili tunywe pombe kwa tani yetu!
Awali alijaribu kupinga lakini nikasihi sana hadi
akanikubalia ombi langu.
Tukaingia chumbani, tulikunywa sana.
Nyambura akawa wa kwanza kulewa, lakini alikuwa
anajitambua.
Pombe zikamualika shetani katikati yetu, zaidi kwangu
mimi akanisukuma kumuhimiza Nyambura tuvunje amri
ya sita.
Nyambura akanikatalia huku akilia kilevilevi, nikasikia
kama anasema kuwa kamwe hajawahi kufanya kitendo
hicho.
Nikadhani zile ni pombe tu zinamsukuma kusema vile.
Nami mashetani yalikuwa yamenipanda na sikuweza
kujizuia.
La! Haula! yalikuwa maajabu makubwa sana kupata
kuyashuhudia!!
Nyambura alikuwa yu salama bado, alikuwa na
usichana wake!!
Alipambana sana na siku ile sikuweza kumfanya jambo
lolote lile.
Pombe zilipotutoka kichwani nikajikuta namtamkia
Nyambura kuwa ninampenda sana.
Hakuzungusha maneno sana badala yake alinijibu.
“Sina wazazi lakini nina baadhi ya ndugu, kama
unanipenda kanitolee mahari unioe!!” alijibu huku
amenikazia macho.
Jibu lile la Nyambura likanifanya nizidi kumtazama kwa
jicho la tatu kama msichana wa tofauti sana.
Na hapo rasmi nikajikuta naingia katika matamanio ya
kumuoa hasimu wangu wa zamani, Nyambura!!
Haikuwa safari nyepesi hata kidogo.
Na sikujua safari ile kama ingenifikisha pale
iliponifikisha!!!!
 
ni nzuri Mzaramo. Napenda hadithi unazozileta humu maana zote huwa zinafika mwisho... ila vipi kuhusu ile Asia digital mkuu?
 
Kujaribu kumsahau mtu unayempenda ni jambo gumu
sana, ni sawa kabisa na kujaribu kumkumbuka mtu
ambaye hata hujawahi kumuona.
Tazama jinsi ambavyo haiwezekani!!

HII NI SEHEMU YA NNE.

ILIANZA kama masihara, mara nikajikuta nazama
katika uhitaji wa kuwa karibu kabisa na Nyambura.
Walisema penzi ni kikohozi!
Ilikuwa hivi hata kwangu, wafanyakazi wakaanza
kutubadilisha majina hatua kwa hatua hatimaye
nikafungua kinywa na kuwaeleza kuwa ni kweli tupo
katika mahusiano na tunataka kuyabadili yawe ndoa
mapema sana.
Wengi walitupongeza na kututakia heri!
Kasoro rafiki yangu mmoja ambaye alikuwa yu katika
ndoa tayari, yeye aliniuliza ninamfahamu Nyambura
kiasi gani.
Sikutaka kujishughulisha na swali lake nikamweleza
kuwa tunafahamiana sana!
Akatabasamu kisha akanipongeza, nilijua wazi kuwa
hakuwa akimaanisha.
Siku mbili baadaye alinifuata ofisini, aliniomba
nimsikilize kwa dakika chache, akanielezea mashaka
yake juu ya uhusiano wa ghafla sana kati yangu na
Nyambura. Akanisihi sana nijipime upya tena kama ni
kweli nahitaji kuwa na yule binti kama mke wangu.
“Sikiliza Joshua, sikatai kuwa Nyambura ni mchapakazi
na kila mtu anampenda, kuhusu hilo sina swali kabisa
lakini je ana utayari wa kuwa mke kaka… au ndo
furaha uliyopata Arusha imekusukuma huko?”
aliniuliza yule rafiki yangu na mkurugenzi mwenzangu
pia kwa pale ofisini.
Niliyasikiliza vizuri sana maneno yake. Kuna namna
alimchambua Nyambura kwa ajinsi alivyomuona yeye,
sikuipenda ile hali na nikawa namjibu tu ilimradi
aondoke zake.
Mapenzi, yasikie tu mapenzi na uombe lisiwe penzi la
kwanza… penzi la kwanza maishani huwa lina kila aina
ya ubora. Kuaminiana kwa hali ya juu, hapa hujajua
maana ya kutendwa!
Nilimwalika Nyambura chakula cha jioni katika hoteli
moja ya kifahari, huko nikamweleza jinsi gani
Revokatus yule mkurugenzi mwenzangu anavyosema
kuhusu yeye.
Nilitarajia kuwa Nyambura atakasirika lakini haikuwa
hivyo, alinijibu kikarimu sana.
“Yule ni mwanandoa mzoefu tayari, unapaswa
kumsikiliza na usimkasirikie, hawezi kuwa na chuki
yoyote juu yetu…. Ni vyema kumsikiliza halafu kwa
vitendo sisi tutamwonyesha kuwa alivyowaza juu yetu
si sawa…”
Majibu ya Nyambura yalizidi kunifanya nimpuuzie Revo
na badala yake nikapiga hatua mbele siku ile
nikamtamkie tena Nyambura kuwa ninataka kumuoa na
ninahitaji kwenda rasmi kumtolea mahari,
akanielekeza kwa ndugu zake waliopo Musoma.
Kwa sababu mimi nilikuwa mkurugenzi, jambo la
ruhusa kwangu lilikuwa dogo sana.
Nisingeweza kukosa.
Nikazungumza na Revo aweze kunisindikiza akanieleza
kuwa mkewe anaumwa hivyo hataweza kwenda,
nikapata marafiki wawili wa kwenda nao pamoja na
mjomba wangu ambaye nilimtumia kama mshenga!!!
Baada ya siku nne mambo yalikuwa tayari, tukafanya
safari.
Tulipokelewa vizuri sana na ndugu zake Nyambura,
nilistaajabu kabisa jinsi mkoa wa Mara
unavyozungumzwa jijini Dar es salaam ni tofauti
kabisa na uhalisia tuliokutana nao.
Walitufanyia ukarimu sana, na sisi tukajishusha mno
ili tupate Baraka na kuachiwa mke.
Ile siku ya tatu wilayani Musoma mkoani Mara,
tukapokea simu kutoka jijini Dar es salaam.
Revo, yule rafiki na mkurugenzi mwenzangu alikuwa
hoi hospitali baada ya kula chakula kilichosadikika
kuwa kimewekewa sumu.
Tuliendelea kuwajulia hali mara kwa mara jijini Dar es
salaam hadi tulipopewa taarifa kuwa hali yake
inaendelea vizuri, hapo nasi tukapata ahueni.
Masuala ya Musoma yakamalizika hatimaye tukarejea
jijini Dar es salaam.
Ile nafika tu nikakutana na barua ofisini, Revo
alikuwa amenuia kuuza hisa zake na kuachana na
kampuni ile tuliyoianzisha wote kwa jasho sana!!
Hii ilinishtua sana, maelezo yake hayakuwa
yamenyooka sana, nilipatwa na ukakasi sana kuweza
kuelewa chanzo cha haya….
Nikampigia simu, akapokea na kunisisitiza kuwa
anahitaji kupumzika na mkewe waweze kulea watoto
wao mapacha.
Sababu ambayo sikuipima katika ujazo wa kusema
yawezekana ikawa ni sababu kuu.
Kama kawaida nikamtafuta Nyambura faragha na
kuzungumza naye.
Akanijibu kwa hekima kabisa kuwa ni heri nikazinunua
hisa za Revo ili niweze kuwa na umiliki mkubwa zaidi
wa ile kampuni inayotanuka.
“Wewe zinunue lakini ili kuboresha urafiki wenu
mweleze kuwa wakati wowote akihitaji kurejea katika
kampuni basi anakaribishwa!”
Nikayapokea vyema manenoya kinywa cha mwanamke,
nikayafanyia kazi.
Mwezi mmoja baadaye nikazinunua zile hisa na kisha
nikatangaza tarehe rasmi ya kufunga ndoa na
Nyambura!!
Nilipanga iwe ndoa ya kanisani.
Revo akasahaulika nami nikawa mmiliki mkubwa zaidi
wa kampuni ile, hapo nhikiwa na asilimia 90 ya umiliki.
Nilikuwa na sauti kubwa zaidi katika vikao vya
kampuni.
Katika kikao kimoja nikampandisha cheo Nyambura
kutoka kuwa msemaji mkuu wa kampuni hadi kuwa
msimamizi wa ofisi zote za kampuni yetu zilizoko
mikoani!!
Sikuwa najua ninachofanya kinaweza kuwa na
madhara yoyote, nilichotazama ni kwamba nafsi yangu
inafurahi huku ya Nyambura ikifurahi zaidi.
Baada ya maamuzi hayo, nikampigia mama simu na
kumfahamisha kuwa ule mji tulivu nilioapa kuwa
ninahitaji kuupata basi nimebakiza hatua chake kabla
ya kuingia.
Mama akanitakia heri!
Lakini hakusahau kutoa maonyo yale ya mzazi kwenda
kwa mtoto.
“Uwe makini baba eeh! Sisi wanawake hatutabiriki
kabisa….” Yalikuwa maneno ya mama…..
 
MASHAKA yakiingia katika ndoa yoyote ile iliyokuwa
imara hapo awali… huu ni mwanzo wa ndoa kugeuka
kuwa kama bomu lililotegeshwa na lisijulikane ni lini
litalipuka!

HII NI SEHEMU YA TANO

HATIMAYE ikawa kama nilivyopambana kwa udina
uvumba iwe. Nyambura akawa mke wangu halali kabisa
aliyetambulika kwa kila mtu.
Tuliendelea kufanya kazi katika kampuni
yangu….lakinihatukudumu sana, Nyambura akanieleza
kuwa anajiona utendaji kazi wake unashuka kwa kasi
kubwa sana, akaniweka chini na kunishauri kuwa kama
sitajali basi yeye ashughulike na biashara nyingine na
mimi niendelee kuwa mkurugenzi wa ile kampuni.
Wazo la Nyambura halikuwa baya, niliridhika kabisa na
maelezo yake na nikampa uwanja wa kuamua ni kitu
gani tunaweza kufanya.
Nilimpa nafasi ya kutulia na kuandika mchanganuo wa
chochote chenye manufaa ambacho anadhani ni sahihi
kufanya.
Wakati akiwa katika kuunda wazo lake la biashara,
mama yangu alipatwa na maradhi yaliyochangiwa na
utu uzima, sasa alikuwa analalamika kuwa
anasumbuliwa na vidonda vya tumbo.
Taarifa za ugonjwa wa mama nilimshirikisha Nyambura
pia, huku nikiacha kuzipa uzito mkubwa sana.
Usiku tukiwa mezani kwa ajili ya kuupitia mchanganuo
wa Nyambura, badala atoe makaratasi aliyoyatumia
kuandika mchanganuo ule, Nyambura alizungumza
maneno machache tu.
“Nitaenda kumuuguza mama kwanza!”
Sikutarajia hata kidogo kauli ile kutoka kwa
Nyambura, nilistaajabu.
Nikacheka nikijua anatania lakini alikuwa
anamaanisha kile alichokuwa anakisema.
Hakutaka biashara wala kitu kingine kile alisema kuwa
suala la afya ya mama lianze kwanza!
Ndugu msikilizaji kama mapenzi huwa yanaongezeka
uzito na yanaweza kupimika, basi Nyambura alikuwa
ameongeza kilo tano za mahaba yangu kwake.
Nikaukumbuka usemi usemao kuwa ukimpata
mwanamke ambaye anaweza kuwa mama kwako, mama
kwa watoto wako na mama kwa familia yako basi
mkamate kwa mikono miwili kamwe usimwache aende
zake.
Nami nikakiri kuwa Nyambura alikuwa na sifa hizi,
alinipenda mimi na familia yangu!!
Siku mbili baadaye alifunga safari kuelekea kijijini
alipokuwa akiishi mama yangu!
Nikabaki mjini peke yangu.
______
Sifa za Nyambura kutoka kwa mama zilinifanya nizidi
kuvimba kichwa na kila mara nikitabasamu na kujisifu
kuwa nilichagua mke ambaye wengi hawana!
Kwanza nilimkuta akiwa ni msichana bado, pili ana akili
sana na ni msikivu!
Hakika nilikuwa na kila sababu za kujisikia kuwa mimi
ni wa pekee zaidi.
Siku moja asubuhi niliamka kama kawaida, si unajua
tena mazoea hujenga tabia. Ilikuwa kawaida ya mke
wangu kuniandalia nguo za kuvaa, yaani ni yeye
aliamua leo navaa hiki na kesho kile. Alikuwa
ananyoosha nguo zangtu vyema na kuniwekea juu
kabisa ya nguo nyingine ama wakati mwingine alikuwa
akiziweka katika kochi, nikitoka kuoga nazivaa.
Siku hii hakuwepo basi kila kitu nikalazimika kufanya
mimi mwenyewe.
Nilipatwa na uvivu na kutamani hata kuvaa nguo
ambazo si za kunyoosha ila ofisini nilikuwa
nimekabiliwa na ugeni wa heshima sana nisingeweza.
Upesi nikaitafuta pasi ilipo, na baada ya kuiwasha
nikaliendea kabati la nguo, nikaanza kutafuta nguo,
nilivuruga hovyo!
Badala ya kupata nguo nikakutanana kitu kigeni kabisa
katika macho yangu ambacho sikutarajia kukutana
nacho.
Nilikutana an akaratasi jeupe sana huku likiwa
limeandikwa jina langu kwa kalamu nyekundu.
Hapakuwa na maelezo yoyote zaidi ya jina langu
kamili. Nilitumia dakika tano nzima kuitazama karatasi
ile ambayo haikuwa pale bahati mbaya bali ilikuwa
imehifadhiowa.
Sasa ni karatasi ya nini? Nilijiuliza…..
Na kwanini nimeandikwa jina langu kwa kalamu
nyekundu.
Nilitamani kumpigia simu mke wangu Nyambura ili
nimuulize nini maana ya karatasi ile lakini nikahofia
kuwa kinaweza kuzuka kizaaazaa wakati akiwa na
mama kule kisha nikaonekana kama mtu nisiyejua
kutafakari mambo kwa kina.
Nikalimezea lile jambo sikumgusia Nyambura kabisa.
Nikanyoosha nguo niliyoichagua nikavaa na kwenda
kazini, kinyonge kabisa huku akili yangu ikiwa
inahangaika kujiuliza ni nini kinaendelea.
Au ameniendea kwa mganga? Nilijiuliza punde tu
baada ya kuingia ofisini. Wazo hilo lililonipitia ghafla
kichwani lilinifanya nijisikie vibaya sana kwa sababu
katu maishani sijawahi kufanya mambo ya kishirikina
japokuwa siwezi kuapa kuwa kamwe sitashiriki.
Wakati nafikiria juu ya jambo lile mara ghafla moyo
wangu ukapiga kwa nguvu sana nikajikuta
nimesimama, mwili wangu ukikumbwa na joto kali licha
ya uwepo wa kiyoyozi.
Nilikuwa nimekumbuka kuwa nimeona kitu kingine cha
ziada katika lile karatasi ambacho sio cha kawaida
kabisa.
Katika yale majina yaliyoandikwa pale lilikuwa
limeambatanishwa pia jina langu la utotoni!!
Jina ambalo niliacha kulitumia miaka mingi sana huko
nyuma, jina ambalo lilisahaulika kabisa.
Fantom!!
Jina hili mke wangu alilitoa wapi, na aliliandika kwa
kalamu nyekundu ili iweje.
Niliumia sana kichwa, nikawaza na kuwazua.
Mwisho wa siku nikanyanyua simu na kumpigia katibu
muhtasi.
“Waambie sitaweza kushiriki mkutano leo, nitafutie
muwakilishi tafadhali!” nilimweleza na sikungoja
majibu, nikakata simu na kujilaza katika meza yangu
ya ofisi, nikishindwa kabisa kupata maana ya ile
karatasi katika kabati yangu!
“Au sio Nyambura aliyeiweka mle ndani…” nilijiuliza,
lakini nikalipuuza wazo lile, mle ndani tuliishi wawili
tu. Sasa iweje lile karatasi liingie biola kuingizwa?
Na kama sikuliingiza mimi basi ni Nyambura!
Sasa kwa nini?
Niliomba kimoyomoyo jambo lile liwe katika namna
zozote zile lakini isiwe mambo ya kishirikina, sikutaka
hata kidogo kuamini kuwa yawezekana Nyambura
amenipika na kunifanya anavyotaka.
Siku hii sikuweza kulala nyumbani, sikuwa na amani
kabisa nikaamua kulala nyumba ya kulala wageni,
Nyambura aliponipigia simu niliongea naye na
kumweleza kuwa nilikuwa nyumbani.
Nilipokata simu nafsi ilinisuta, kwa mara ya kwanza
nilikuwa nimemdanganya mke wangu!
Sikuupata usingizi siku hii, hadi majira ya saa nane
usiku bado nilikuwa macho tu.
Hakika lile karatasi lilikuwa limenichanganya sana na
sikujua nitaanza vipi kumueleza mke wangu ilimradi tu
tusigombane.
Nililala nikiwa nasumbuliwa na kisa kimoja…. Asubuhi
mambo yakapamba moto!
 
SEHEMU YA SITA

ASUBUHI majira ya saa nne nilikabidhi chumba kisha
nikaongoza njia kuelekea nyumbani, nia ikiwa kubadili
nguo kisha nielekee ofisini.
Nilianza kupuuzia juu ya karatasi lile lililoandikwa kwa
wino mwekundu majina yangu matatu, moja kati ya
jina hilo nikiwa nimeacha kulitumia kiwa miaka mingi
sana.
Nilipanga kuwa nitakapotoka kazini nitaenda nyumbani
kwa Revo rafiki yangu kumgusia juu ya jambo
lililotokea nyumbani kwangu, lakini nilipanga
kuyapanga maneno ili asije akapata pa kusemea eti
alinieleza kuwa nisiwe na papara katika kuoa na
sikutaka kabisa arejee lile swali aliloniuliza ikiwa
ninamjua vizuri Nyambura.
Nilifika nyumbani na kuingiza funguo mlangoni.
Ajabu! Mlango ulikuwa wazi tayari.
Ina maana nilisahau kuufunga au? Nilijiuliza huku
nikiingia ndani kwa tahadhari kubwa kabisa.
Nilianza kusikia dalili ya uwepo wa kiumbe hai pale
ndani. Upesi nikawahi kuchukua chupa tupu ya soda
pale sebuleni tayari kwa kukabiliana na yeyote
atakayethubutu kunikabili.
Nilienda hadi nikakifikia chumba, sasa nikasikia sauti
ya kike ikiwa katika kilio cha kwikwi.
Nyambura mke wangu yuko safarini, huyu ni nani
ndani ya nyumba yangu!
Nikaufungua mlango upesi huku nikitanguliza ile chupa
mbele.
Lahaula! Alikuwa ni Nyambura, akanitazama kwa jicho
kali jekundu lililoiva haswa kwa hasira.
Nilijikuta ile chupa inanitoka huku ikipasuka vipande.
“Ulikuwa na nani huko ulipolala?” aliniuliza huku
akisimama. Mikono yake ilikuwa inatetemeka sana,
alikuwa amevaa nguo ya kulalia pekee.
Michirizi ya machozi ilijionyesha dhahiri katika
mashavu yake.
Alikuwa ananisogelea, mimi nilikuwa katika pumbazo
nisijue nini cha kujibu.
Sikutarajia kabisa shambulizi lile la ghafla kiasi kile.
“Joshua ulilala na nani, hadi kufikia hatua
unaniongopea kuwa upo nyumbani kumbe unalala kwa
hawara zako, Joshua ni nini hiki unanifanyia eeh! Ni
nini Joshu….” Alilalama huku akibubujikwa na
machozi. Akashindwa kumalizia akanitazama
kidoleni….
“Na pete ya ndoa ukaona uivue kabisa, ukamwambia
kuwa hauna mke….wanaume sijui mnataka nini katika
maisha ya wanawake. Au Mungu alifanya makosa
kutuumba? Au kwa sababu tulitoka katika mbavu
zenu” Alizungumza huku akinitazama kidole changu
ambacho kilitakiwa kuwa na pete.
Aisee! Nilijisikia aibu sana, si kweli kwamba nilikuwa
nimeivua pete kwa sababu za kumsaliti mke wangu
lakini niliivua ili kuisafisha na nikasahau kuivaa tena.
Sasa ile bahati mbaya imegeuka kuwa kesi inayohitaji
majibu. Ningeyatoa wapi majibu!!
Mdomo ulikuwa mzito sana kana kwamba umedungwa
sindano ya ganzi.
“Umekuja lini?.” Nilijitutumua nikamuuliza huku
nikiwa sijiamini. Lilikuwa swali la kizembe sana
“Ulitaka nikueleze siku ambayo ninakuja ili uvae pete
na kuja kunipokea uwanja wa ndege na maneno
matamu kuwa unanipenda sana eeh!” alisema kwa
uchungu Nyambura, nikajaribu kumshika ili nimsihi,
akajitoa katika mikono yangu na palepale akaninasa
kofi kali usoni.
Niliumia lakini kwa hali aliyokuwanayo Nyambura
sikuwa na chochote cha kumfanya. Nilikuwa upande wa
mashtaka na yeye akiwa ni mshtaki.
Alizungumza mengi sana mwanamke yule kiasi kwamba
nikajikuta nikikosa walau doti ya ujasiri kuweza
kumshutumu juu ya kile kikaratasi chenye jina langu
katika wino mwekundu.
_____
KESI ile iliisha lakini Nyambura akiwa mnyonge kabisa.
Lakini hakuwa na budi kukubaliana na utetezi wangu,
maisha yakaendelea.
Ili kuyajenga tena upya mazoea ya kusahau kile
kilichotokea nililazimika kumpa mke wangu likizo fupi
kidogo ili aende nyumbani kwao kusalimia ndugu zake.
Licha ya kwamba alipoondoka nilimweleza kuwa
natamani abaki lakini kwa uhakika nilitamani sana
aondoke, sikuwa nikiishi kwa amani kabisa huku
Nyambura akiwa ameninunia.
Kuondoka kwa Nyambura kukairejesha amani yangu
lakini kukinifanya niwe mtu ninayeishi kwa tahadhari
sana ili nisije kufanya makosa katika hatua ninazopita
kisha nikamkwaza mke wangu kwa kitu ambacho si
kweli kabisa.
Napenda kukiri mbele yenu tena kuwa nilimpenda
Nyambura kwa dhati kiasi kwamba sikuwa napatwa na
msisimko wowote ule nikianza kumfikiria msichana
mwingine.
Labda hili ndo kosa kubwa zaidi ambalo niliwahi
kufanya katika maisha yangu, kupenda kwa dhati!!
Sijui kama maamuzi haya yalinifanya kuwa mjinga,
ama zezeta!
_____

Baada ya likizo ile fupi kuisha Nyambura alirejea tena
nyumbani tukiwa tumesahau kabisa yaliyopita…
tukaanzia tulipoishia nikampatia pesa ya mtaji na yeye
akaongezea akiba yake yake.
Wazo lililopitishwa ni biashara ya nguo za wanawake
na watoto kutoka China kuja Tanzania.
Hata sikuwa na mashaka juu ya mke wangu katika
suala la uelewa. Alikuwa mjanja sana na mwepesi
kuelewa hivyo nilijua kuwa safari ya kwanza na ya pili
pekee ndo atakuwa mikono nyuma lakini baada ya hapo
atakuwa mjuzi maraduhu.
Naam! Nyambura wangu akaanza kwenda China.
China ikawa China…… mimi sioni mabadiliko zaidi ya
kusifia kila nilichokuwa nakiona kuwa mke wangu
anapiga hatua kubwa sana kimaendeleo.
Mara zikapenyezwa habari kuwa Nyambura ana
mwanaume mwingine asiyekuwa mimi!
Yaani ananisaliti.
Nilijikuta nacheka tu, kwa sababu hayo maneno
nilishayazoea kila kukicha na kila nilipojaribu
kufuatilia majibu yalikuwa ni uongo mkubwa.
Kabla sijaendelea kukusimulia mkasa huu mpenzi
msikilizaji hapa nikugusie neno kidogo, katika maisha
yako kuna vitu hutakiwi kuviamini kwa asilimia nyingi.
Kimojawapo ni mwanamke mwenye hasira ama
aliyewahi kujeruhiwa!
Anaweza kufanya jambo ambalo wewe na halmashauri
ya kichwa chako nyote mkabaki kuduwaa.
Tetesi zilivyozidi nikaamua kufanya utafiti wa chini
kwa chini….
Nyambura alikuwa hachunguziki jama!
Sikuambulia kitu chochote, niliishia kuwa upande wake
na kuwacheka wale wanaosema kuwa ananisaliti.
Waswahili wanasema kuwa lisemwalo lipo njiani
linakuja. Nilijipa tahadhari na hapa nikajipa
tahadhari, na kwa mara ya kwanza nikatambua kuwa
namna nzuri ya kukabiliana na hali hii ya sintofahamu
ni kupata mtoto na Nyambura.
Hili litaleta heshima.
Alipotoka katika safari zake nikamsihi juu ya jambo
hili, mke wangu msikivu akalipokea kwa mikono miwili
na yeye akasema kuwa anatamani kupata mtoto na
mimi.
Wakati mimi nilidhani kuwa itakuwa ngumu sana
imekuwa nyepesi kuliko kawaida.
Nyambura akasitisha safari zake ili tutafute mtoto.
Hapa ndipo nilipoanza kupungua uzito siku kwa siku.
Jaribio la kwanza likashindikana, Nyambura akaingia
katika siku zake kama kawaida kumaanisha kuwa
nimegonga mwamba, jaribio la pili pia vilevile.
Tukajaribu tena mwezi wa tatu, hali ikawa vilevile.
Kuna shida mahali!
Nilijisemea huku nikiomba sana hiyo shida isijekuwa
ipo upande wangu. Kwa sababu ningedharaulika sana
na ikiwa Nyambura ataamua kusimulia kila mtu basi
nisingekuwa na uwezo tena wa kusimama mbele ya
watu na kuzungumza.
Tulipojaribu mwezi wa nne na shida kubaki palepale,
tulikubaliana kuwa iwe siwe tutalazimika kwenda
hospitali ili tujue kuna shida gani hadi inakuwa hivi??
Niliunga mkono jambo hili lakini bado maombi yangu
yalikuwa yakimsihi Mungu, lile tatizo lisijekuwa
upande wangu.
Vipimo vikachukulia, tukiwa kama wanandoa
tukakubaliana kuwa tutayachukua majibu yetu tukiwa
pamoja.
Muda ukawadia ndani ya chumba cha daktari,
alitutazama machoni kisha akalitazama faili
aliloshikiria akatuuliza majina yetu upya, kisha
akauliza ikiwa mmoja wetu amewahi kupata mtoto
katika maisha yake ya ujanani…
Sote hatukuwa tumewahi walau kuhusika katika
kusingiziwa walau mtoto hata kwa bahati mbaya.
“Ok! Mmesema kuwa ni wanandoa eeh!” alihoji tena.
Swali lake likanifanya nione kuwa anachelewa sana
kutoa majibu yake ambayo bila shaka sio mazuri hata
kidogo!
Alipomaliza swali lie akaanza kutoa majibu akianza na
Nyambura, ambaye hakuwa na mashaka kabisa……
 
SEHEMU YA SABA

Baada ya vipimo vile daktari alianza kuzungumza
mambo mengi sana kuhusiana na afya ya uzazi, na
mwisho ndipo akatoa majibu yetu.
Ndugu msikilizaji, Nyambura hakuwa na tatizo lakini
mimi nilionekana kuwa na tatizo.
Daktari alinifariji sana na kuelezea kuwa tatizo
nililonalo si kubwa kiasi cha kutisha na linatibika.
Sikuamiani maneno ya daktari kwa sababu
niliwatambua vyema kuwa nia yao siku zote si
kumkatisha tamaa mgonjwa bali kumpa moyo ili awe
imara zaidi.
Jasho lilinitoka sana, mawazo lukuki yakaniandama na
pepo la hofu likaniingia.
Hofu kubwa ikiwa kumpoteza Nyambura wangu,
angweza vipi kuishi na mimi bila ndoto ya kupata
mtoto?
Niliondoka pale nikiwa sijiwezi kabisa, nilimsihi
Nyambura aendeshe gari kwani mimi sikuwa sawa hata
kidogo.
Nyambura alinielewa, akaendesha gari tukafika
nyumbani akiwa hajasema neno lolote lile bado.
Ukimya wa Nyambura uliniumiza sana, nilijitahidi
kuwaza badala yake na nikaona kuwa anachowaza ni
kuanzisha maisha mengine bila kuwa na mimi.
Aliniandalia maji nikaoga, akaingia jikoni na
kuniandalia chakula nikipendacho.
Ugali dagaa na mboga za majani.
Tofauti na siku nyingine, siku hii chakula hakikulika,
nilikiona kichungu huku nikihisi hata harufu yake ni
mbaya.
Mawazo yalikuwa yamenikabili sana, yaani jitihada
zangu zote hizo nikose wa kurithi jasho langu kweli?
Iliniuma sana jama!
“Joshua mume wangu…. Nakupenda sana. Sijawahi
kukueleza ni kwanini nakupenda na kamwe sitakueleza
kwa sababu nakupenda kama ulivyo bna utakavyokuwa
hapo baadaye.” Hatimaye Nyambura alizungumza.
Sasa tulikuwa chumbani alikuwa ameniegemea huku
akizisukasuka ndevu zangu.
Nilifarijiwa sana na maneno yake yale ya kutia nguvu.
Nikapata faraja kwa mara ya kwanza lakini
haikumaanisha kuwa hofu yangu ilikuwa imeisha.
Tofauti na matarjio yangu kuwa itafikia wakati
ambao Nyambura atahitaji tena majadiliano juu ya
jambo lile, haikuwa hivyo.
Maisha yakaendelea kama kawaida, huku upendo wake
wa dhati nao ukizidi kuichukua nafasi yake.
Lakini katu sikuacha kuwaza juu ya lile jambo,
nilifahamu fika kuwa miaka itasogea marafiki
wataulizia mtoto lini, mama ataulizia mjukuu lini,
nitawajibu nini?
Hili nalo liliniumiza sana. Nikajiuliza ni kitu gani
nitafanya kukabiliana na jambo hili.
Sikupata majibu, nikajitoa muhanga na kurejea kwa
rafiki yangu Revo ambaye alikuwa ndoani
nikamshirikisha kiuwazi kabisa juu ya jambo hili
linalonitokea.
Alinisikitikia sana lakini zaidi ya kunisihi nisikate
tamaa hakuwa na ushauri zaidi.
Na zaidi alinikanya nisimshirikishe kila mtu maana si
kila mtu anayependa kuonamambo mazuri yakitokea
upande wangu.
Nikapokea ushauri wake.
Nilipotoka pale nilipita mahali na kupima uzito,
nikagundua kuwa nilikuwa nimepoteza jumla ya kilo
tano ndani ya majuma mawili tu.
Nilijisikitikia na kujiona mtu nisiyekuwa na bahati
kabisa. Lakini nilipoyasema haya mbele ya Nyambura
alinikumbusha kuwa nimejaliwa mengi ambayo wengine
hawajawahi kuyapata kabisa, akanielezea juu ya pesa
nilizokuwa namiliki pamoja na vitega uchumi, kisha
akanieleza kuwa nina bahati wazazi wangu bado
wanaishi wengine ni yatima tangu wana siku moja
duniani.
Maneno yake yaliniimarisha sana, na hapa akawa
ameichota akili yangu zaidi na kuona huyu ndiye
mwanamke wa maisha yangu yaani akitoka mama
yangu basi ni huyu anayefuatia.
Miezi ilikatika, takribani miezi miwili…. Nyambura
akarejea tenakatika zile biashara zake za kusafiri
huku na kule kama alivyokuwa amenieleza.
Nilimkubalia bila mashaka kabisa.
Nyambura akaanza kuishi mbali na mimi siku akisafiri,
upweke unanitawala na mawazo tele nikitamani kuwa
na mtoto.
Siku moja Nyambura akiwa safarini, nilitembelewa na
Revo yule rafiki yangu, aliniahidi kuwa atanitembelea
hivyo haikuwa jambo la kushtukiza.
Revo alinileza kwamba siku ile alishindwa kuzungumza
na mimi vizuri kwa sababu mkewe alikuwa amemvuruga
hivyo hakuwa sawa.
Na alikuwa amekuja hapo ili tujadiliane juu ya tatizo
linalonikabili.
Revo akaniuliza ikiwa nimejaribu tiba za jadi,
nikamweleza kuwa sijawahi kujaribu hata siku moja.
“Hizo tiba za hospitali zimekusaidia lolote?” aliniuliza,
nikatikisa kichwa na kumweleza kuwa hakuna
nilichofanikiwa hadi wakati huu.
Akanitazama kwa muda kisha akanieleza kuwa nijaribu
huko.
“Ujue kaka, unaweza kumwona Nyambura ni
mvumilivu, lakini elewa kuwa hawezi kuvumilia mkaisha
yote. Kaka pambana upate mtoto, hapa umefungwa tu
na mjinga mmoja asiyependa kuona unja furaha…
najisikia vibaya kwa haya yanayokutokea. Wewe ni
rafiki yangu tafadhali….” Alinisihi sana Revo, maneno
yake yalikuwa kweli tupu.
Ndoa ni mtoto… na Nyambura hawezi kuvumilia miaka
yote bila mtoto.
Kama hawezi kuvumilia basi hii inamaanisha kuwa
atatafuta njia nyingine kumpata.
Mwanaume mwingine!! Jibu hili likanijia kwa kasi
kubwa sana na kukiyumbisha kichwa changu,
nikafumba macho yangu na kumwona Nyambura wangu
akiingia kwenye mahusiano na mtu mwingine.
Hakuna kitu kinaumiza ndugu msikilizaji katika
mahusiano kumwona yule mpenzi wako ambaye moyo
wako unafarijika kuwa naye eti anaingia kwenye
mahusiano na mtu mwingine.
Sikuwa tayari kuupa fedheha kiasi hicho moyo wangu,
nikajikuta kwa mara ya kwanza natamani kufanya
jambo lolote lile ilimradi tu kumtunza Nyambura
wangu.
Nikamuuliza Revo juu ya huyo tabibu wa jadi ni wapi
nitakapompata. Akaniambia kuwa anaye rafiki yake
ambaye anafahamu wataalamu wazuri kabisa ambao
wanaweza kunifungua na kufanikiwa kupata mtoto.
“Kaka asijekuwa mtoto wa masharti halafu baadaye
wakaja kumdai!!” nilimpa tahadhari Revo huku
nikikumbuka filamu nyingi ambazo nimewahi
kuzitazama zikiwa na matukio kama hayo.
Akaniondoa hofu huku akinieleza kuwa kabla ya yote
tutamuuliza huyo tabibu atuhakikishie kabisa kuwa
mtoto atakuwa salama asiyekuwa wa masharti hata
kidogo.
Revo akaniaga huku akiniacha nikiwa nimekubali kabisa
kwenda kwa tabibu wa jadi ili niweze kuiokoa ndoa
yangu.
Punde tu baada ya Revo kuondoka, mama yangu
alinipigia simu na katika maongezi hayo aliulizia ni lini
aje mjini kulea mjukuu, nikajichekesha tu na
kumwambia kuwa ajiandae na nepi na kanga za
kumbembe mjukuu mgongoni.
Akanipa hongera!
Hongera ya mama iliniumiza sana kwa sababu alikuwa
anampa hongera mtu asiyekuwa na uwezo wa kuleta
mtoto duniani!
Chozi likanitoka!
Na hii ikaniongezea ujasiri wa kuzifuata tiba za jadi.
Nikatamani hiyo siku ya kwenda huko ifike.
Nikanyanyua simu na kumpigia Revo, nikamsisitiza
awasiliane na huyo rafiki yake upesi ikiwezekana
twende kabla Nyambura hajarejea. Akanijibu kuwa
tayari amemtumia ujumbe na anangoja majibu tu!
“Mama amenipigia simu Revo, nimejisikia vibaya sana
ameniuliza kuhusu mjukuu. Nimeumia sana Revo”
“Relax Joshua…. Mambo yote yanaenda kuwa sawa
muda si mrefu!” alinijibu kwa upole Revo. Kisha
tukaagana na kukata simu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom