Pengo amjibu Kilaini

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,013
bul2.gif
Awapasha viongozi wanaolinda mafisadi

bul2.gif
Asema wananufaika na uozo wao


Mwandishi Wetu
Raia Mwema
Juni 9, 2010

"Ukimwambia Rais wa nchi kuwa hili ni kosa lako anakataa na kusema hapana mimi ni msomi tu, ni hawa walio chini yangu ndiyo waliyo wabaya. Hiyo si kweli, ni kutowajibika tu,"

KATIKA hatua inayoweza kutafsiriwa kuwa uongozi wa juu wa Kanisa Katoliki nchini umechoshwa na ubabaishaji wa viongozi waandamizi serikalini, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amesema uongozi wa juu hauwezi kukwepa kuhusika na uozo wa watendaji wake kwa kuwa wana uwezo wa kuwang'oa vinginevyo hiyo ni ishara kuwa viongozi hao wananufaika na makosa ya watendaji na wasaidizi wao na pia ni sehemu ya udhaifu huo.

Kauli hiyo kali ya Kardinali Pengo, ambayo si tu imeelekezwa kwa wanasiasa waandamizi nchini na duniani kwa ujumla bali hata kwa mapadre wa kanisa hilo, inaweza kutafsiriwa kama hatua ya kupinga kauli nyingine ya hivi karibuni ya Askofu wa kanisa hilo, Dk. Methodius Kilaini ambaye alinukuliwa akisema Rais Jakaya Kikwete bado ni chaguo la Mungu, isipokuwa wanaomwangusha ni watendaji wake wasaidizi na akichaguliwa tena asiwateue watendaji hao.

Miaka minne iliyopita Askofu Kilaini alimuelezea Rais Kikwete kuwa ni "chaguo la Mungu" na hivi karibuni akarudia kusema kwamba hajabadili msimamo wake, japo akaongeza kusema kwamba wasaidizi na mawaziri wake wanamuangusha na hana budi kuachana nao iwapo atachaguliwa tena kuongoza nchi.

Kauli ya Kardinali Pengo aliitoa wakati wa akitoa Homilia katika Ibada ya Misa Takatifu ya Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam hivi karibuni, na ikapigiwa chapuo na Padre wa Kanisa hilo, Baptista Mapunda, alipokuwa akihubiri katika Kanisa Katoliki la Manzese kwenye maadhimisho ya Sikukuu ya Ekarist Takatifu.

Kwa mujibu wa gazeti rasmi la Kanisa Katoliki linaloitwa Tumaini Letu la Juni 4 hadi 10, mwaka huu, Kardinali Pengo anasema hatua ya viongozi wa ngazi za juu serikalini hapa nchini na duniani kwa ujumla ya kutowachukulia hatua viongozi wa chini yao wanaonekana kufanya vibaya katika utendaji wao wa kazi, ni kutaka kupata sehemu ya kutupia lawama.

Kardinali Pengo anakaririwa kueleza kuwa kutowachukulia hatua viongozi hao wanaofanya makosa mbalimbali serikalini kunalenga kulinda malsahi ya viongozi hao wa juu ili waendelee kuwapo na kujineemesha huku wakijua fika kwamba wanafanya makosa.

"Serikali za watu zimejaa mahangaiko na kero nyingi za kila aina. Watu masikini wanataabika, watu wanalia, wagonjwa wanakufa kwa ukosefu wa dawa na hawawezi wakapata hata msaada unaotakiwa halafu wewe unajilipa shilingi milioni tano.

"Huwezi kusema mama anayelia kwa maumivu ya kansa anakufa na hana hata dawa ya kutuliza maumivu kwamba hilo ni kosa la uchumi mbovu wakati viongozi wanajilipa mishahara mikubwa," alisema Kardinali Pengo na kufafanua kuwa kama viongozi hao wanadai kuwa hali ya uchumi ni mbaya, ni vema mahangaiko na mateso wanayopata wananchi na wagonjwa mbalimbali, viongozi hao wataabike pamoja nao ili kuthibitisha ukweli wa hali mbaya ya uchumi.

"Ukimwambia Rais wa nchi kuwa hili ni kosa lako anakataa na kusema hapana mimi ni msomi tu, ni hawa walio chini yangu ndiyo waliyo wabaya. Hiyo si kweli, ni kutowajibika tu," alisema.

Katika kuwaasa viongozi wenzake ndani ya Kanisa hilo, Kardinali huyo mwenye hulka ya kuzungumza kwa kuchuja maneno yake alitoa wito kwa mapadre wa kanisa hilo kuwa mfano wa kuigwa na kutambua majukumu yao ikiwa ni pamoja na jukumu lao.

"Sisi viongozi wa Kanisa hatujajifunza kusema samahani ni kosa langu. Tunapokataa kumwambia Mwenyezi samahani ndipo hapo mambo yanapokuwa mabaya zaidi. Sisi tusipojua kusema samahani tutawakokota wote kwenda Jehanamu nasi….tuombeeni sisi mapadre kuwa wa kwanza kukaa kwenye kiti cha kitubio na kupokea samahani zenu, kwani bila kuwa na moyo huo tutaangamia wote," alisema.

Kwa upande wake, Padre Mapunda katika kuonyesha kuunga mkono kauli za Pengo akiwa katika Kanisa Katoliki Manzese, Dar es Salaam, hivi karibuni, naye alisema kuwa matukio ya baadhi ya wananchi kujichukulia sheria mkononi ni ishara ya kuchoshwa na hali ya kukithiri kwa ubinafsi nchini akiweka bayana kuwa hali pia si shwari kwa viongozi wa dini.


Kwa tafsiri inayojitokeza kutokana na kauli yake hiyo; ni kwamba viongozi wa dini wameunda genge moja na baadhi ya viongozi wa kisiasa katika kupuuza maslahi ya wananchi.

"Kuna baadhi ya viongozi wa dini ambao wanakubali kupokea vijisenti vya wanasiasa kwa ajili ya kupindisha ukweli na kuongeza ushawishi kwa waumini ili wawachague katika nyadhifa zao. Hiyo ni dhamira kubwa ya kuliangamiza Taifa.

Viongozi lazima wakubali kuacha ubinafsi…hiyo ndiyo dhambi inayoteketeza Taifa. Wanawaacha wananchi waliowapa madaraka katika dimbwi la taabu na umasikini.

"Inasikitisha kumwoma Mcha Mungu akiuza utu wake kwa mtu binafsi eti kwa ajili ya kupata uongozi, ni muhimu kutambua kuwa viongozi wa mtindo huo hawatakiwi kabisa na ni lazima tuachane nao. "Sishabikii siasa bali ni wajibu wangu kuwaelimisha wananchi kuchagua kiongozi anayefanana na maadili ya Mungu ili kuweza kufikia malengo ya kiimani na maendeleo ya nchi kwa ujumla," alisema padri huyo.

Katika maelezo yake ya hivi karibuni, Askofu Kilaini, ambaye amehamishiwa mkoani Kagera kutoka Jimbo Kuu la Dar es Salaam, alinukuliwa akisema;

"Mwaka 2005 niliwahi kusema kuwa Kikwete ni chaguo la Mungu... kwa maana kwamba kiongozi yeyote anayechaguliwa na watu anakuwa amesimamishwa na Mungu. Miaka minne baadaye ameendelea kupendwa kwa kiasi kilekile na wananchi kwa kuwa kweli ni chaguo hasa ambalo Watanzania walilihitaji."

Akinukuliwa na gazeti moja nchini, Askofu Kilaini alisema: "Yapo mambo ambayo hayakwenda vizuri katika kipindi hiki, lakini ukiangalia yeye kama rais hawezi kujua kila kitu... anahitaji kusaidiwa na watendaji wake wa karibu na hawa wamekuwa wakimwangusha mara kwa mara."
 
Wakati mwingine waandishi wasipostulate vitu ambavyo havipo... kwani nilazima iwe Pengo amjibu Kilaini? kwanini isiwe Pengo naye ana msimamo wake ambao hauusiani na msimamo wa Kilaini. Sasa akija na shemasi akisema kitu kingine kwenye mada hiyo hiyo itakuwa anamjibu Pengo.. na huo mnyororo wa majibizano utaishia wapi?
 
tatizo la waandishi wanafikiri watamgombanisha pengo na kilaini,kumbe ni kitu kimoja. BINAFSI, nampongeza sana pengo, pengo ni mtu mwenye busara sana na kusema ukweli hata kama mi si mkatoliki, naheshimu sana mawazo yake na mchango wake kwa kanisa lake na kwa taifa la tz. pengo ni mtu makini sana na sehemu zote alizopita katika uaskofu wake amefanya mambo makubwa ajabu. izo radio, tv mabenki mashule mengi ajabu ni yeye anasimamia na kuyafanya..si mnafikinafiki.
 
Wakati mwingine waandishi wasipostulate vitu ambavyo havipo... kwani nilazima iwe Pengo amjibu Kilaini? kwanini isiwe Pengo naye ana msimamo wake ambao hauusiani na msimamo wa Kilaini. Sasa akija na shemasi akisema kitu kingine kwenye mada hiyo hiyo itakuwa anamjibu Pengo.. na huo mnyororo wa majibizano utaishia wapi?

MKJJ nadhani umeshindwa kuelewa dhana nzima,inaonekana hujui kuwa Kilaini na Pengo ni "wazito" ndani ya kanisa hilo la katoliki....Na kama unasoma katikatika ya msitari,utaona kuwa tayari kuna mgawanyiko,maybe Kilaini keshahongwa ila Pengo yeye bado ni mzalendo,na wote wana influence flani kwenye jamii ya wakatoliki na maybe even nje ya jamii hiyo kama alivyomention Ubungu Ubungo hapo juu,sasa kusema shemasi naye akijibu ni kutokuelewa issue nzima...
Bubu Ataka Kusmema said:
Kwa tafsiri inayojitokeza kutokana na kauli yake hiyo; ni kwamba viongozi wa dini wameunda genge moja na baadhi ya viongozi wa kisiasa katika kupuuza maslahi ya wananchi.

"Kuna baadhi ya viongozi wa dini ambao wanakubali kupokea vijisenti vya wanasiasa kwa ajili ya kupindisha ukweli na kuongeza ushawishi kwa waumini ili wawachague katika nyadhifa zao. Hiyo ni dhamira kubwa ya kuliangamiza Taifa.

Viongozi lazima wakubali kuacha ubinafsi…hiyo ndiyo dhambi inayoteketeza Taifa. Wanawaacha wananchi waliowapa madaraka katika dimbwi la taabu na umasikini.
 
wewe, wala usihangaike kuwajadili pengo na kilaini, hakuna kitu kama hicho, kama hulijui kanisa katoliki nyamaza. hakuna mgawanyiko wowote kwa hao watu wawili usijepoteza muda wako na mawazo yako bure kuwajadili kihivyo.
 
Habari ina ukweli ila sidhani kama inauhusuano mkubwa na Title. Anyways ni nzuri but md yo Babu in most cases Vichwa vya habari vyataka sana kuuza!
 
MKJJ nadhani umeshindwa kuelewa dhana nzima,inaonekana hujui kuwa Kilaini na Pengo ni "wazito" ndani ya kanisa hilo la katoliki....Na kama unasoma katikatika ya msitari,utaona kuwa tayari kuna mgawanyiko,maybe Kilaini keshahongwa ila Pengo yeye bado ni mzalendo,na wote wana influence flani kwenye jamii ya wakatoliki na maybe even nje ya jamii hiyo kama alivyomention Ubungu Ubungo hapo juu,sasa kusema shemasi naye akijibu ni kutokuelewa issue nzima...

hapo penye nyekundu mbona sikuelewi, Huyo kilaini ni mzito ndani ya ukatoliki (Kanisa katoliki Tanzania) au ana uzito kwenye jamii ya Tanzania
 
Kutofautiana kimawazo ni jambo la kawaida tu. Isipokuwa Pengo sidhani kama anamjibu Kilaini maana ana channel za kufanya hivyo. Ila kimsingi hoja za Kilaini zina utata wake kidogo.
 
Kama wana wafuasi wao basi watawaelekeza ni mtu gani wa kumchagua nk...Sasa kama hawana influence kwenye jamii ni kwanini mnamlaumu Kilaini kwa kusema JK ni chaguo la Mungu?Na sasa anapodai kuwa ni wasaidizi wake ndio wa kulauminiwa,then Pengo akaja na kusema si wasaidizi bali rais mwenyewe atakuwa amewajibu nyie?
Kama ni kweli kuna waliopokea vijisenti kama ilivosemwa hapo kwenye habari hii,hivyo vijisenti ni vya kusaidia nini zaidi ya wapiga kura?
Tumieni akili,hii JF imevamiwa na watu wenye kufikiri kiajabu mno,kweli nchi imeoza na watu wake.
 
hapo penye nyekundu mbona sikuelewi, Huyo kilaini ni mzito ndani ya ukatoliki (Kanisa katoliki Tanzania) au ana uzito kwenye jamii ya Tanzania
Kituko,haya ni yale yale niliyosema hapo juu,sikusema Kilaini pekee,nimesema wote pamoja na Pengo...Sasa kama ungesoma postings zilizopita kabla ya kukurupuka,basi ungetumia ubongo wako inavyotakiwa,nashangazawa sana na wabongo kujiita wabongo,na wakati ni bongoless,kama ufisadi ndo ubongo nani anuhitaji?Ama kama humu ndani ndo wasomi wetu?linchi linahitaji mapinduzi na watu ni wazembe na wajinga na wakurupukaji,wasiotafakari,wabinafasi,wachawi,ma extremist ya kidini,anything less ni wao....
Jibu kwenye swali lako hilo hapo chini,huyo alisema yeye si mkatoliki na kwahiyo jazia mwenyewe jibu kuhusu "uzito" na uache vituko next time.

Ubungo Ubungo said:
BINAFSI, nampongeza sana pengo, pengo ni mtu mwenye busara sana na kusema ukweli hata kama mi si mkatoliki,
 
Maoni ya gazeti la kanisa la Kiongozi yameijibu hiyo habari ya "Pengo kumjibu Kilaini" lakini hoja inakuja, Je, kama viongpzi hawa wawili ni "WAZITO" kama wanavyoelezwa hapo juu, nini maana ya kauli zao nzito kuhusiana na hali ya sasa ya nchi yetu. Mfano, "Kikwete Chaguo la Mungu" na kwamba "wanaomuangusha ni wasaidizi wake", halafu Mufti SImba naye anaenda Kigamboni anasema, "Lowassa ndiye kiongozi afaaye", anakuja Pengo anasema, "Ukimwambia Rais wa nchi kuwa hili ni kosa lako anakataa na kusema hapana mimi ni msomi tu, ni hawa walio chini yangu ndiyo waliyo wabaya. Hiyo si kweli, ni kutowajibika tu."... tunawaandalia nini wapiga kura wetu ambao sehemu kubwa ni wa dini hizi ambazo viongozi wake wanatoa matamko katika mwaka wa uchaguzi? TUTAFAKARI HOJA NZITO MBELE YETU NA SI VITU VIDOGO VIDOGO KAMA VICHWA VYA HABARI. TUNAWACHANGANYA WAUMINI AMBAO NDIO WAPIGA KURA WETU NA TUJUE IMANI ZA DINI ZINA UZITO WA KUTISHA. Sina hakika ule waraka wa KATOLIKI umeishia wapi na ule wa Waislamu umeishia wapi na ule wa KKKT na wengine umeishia wapi? ama ndio mbio zile zile? Au ndio mtandao mpya wa kuleta ushindi wa KISHINDO kuelekea MAISHA BORA KWA FAMILIA NA MASWAHIBA ZETU?
 
Kwa kweli tuwe makini na wanahabari. headings ziwe zinaranda na habari yenyewe. habari kama hiyo kwenye gazeti la udaku ni sawa lakini kwa serious paper kama hiyo ni noma. Tuzianze kutengeneza mnyororo wa mjibizano amabao mara zote huwa hauna manufaa kwa Taiafa. maoni ya kila mtu yawe yanajitegemea
 
Kwa kweli tuwe makini na wanahabari. headings ziwe zinaranda na habari yenyewe.
Wenye magazeti nia yao ni kuuza kwa wingi tofauti ni msimamao wa mhariri anayepitisha vichwa vya habari.
Kuhusu mada hii Kilaini anazungumzia kibiblia ya kuwa viongozi huteuliwa na Mungu. Na Pengo anataka kukazia tu kuwa japo wanateuliwa na Mungu, utendaji kazi wao, ni jukumu lao binafsi. Hawana sababu ya kurusha kiazi cha moto kwa watendaji walio chini yao kwani wana uwezo wa kuwteua na kuwaondoa, alimradi kusiwe na uonevu.
 
Wenye magazeti nia yao ni kuuza kwa wingi tofauti ni msimamao wa mhariri anayepitisha vichwa vya habari.
Kuhusu mada hii Kilaini anazungumzia kibiblia ya kuwa viongozi huteuliwa na Mungu. Na Pengo anataka kukazia tu kuwa japo wanateuliwa na Mungu, utendaji kazi wao, ni jukumu lao binafsi. Hawana sababu ya kurusha kiazi cha moto kwa watendaji walio chini yao kwani wana uwezo wa kuwteua na kuwaondoa, alimradi kusiwe na uonevu.

Hapa naona mjadala haujikiti kwenye hoja: Umejikita kwenye imani zaidi. Ina maana Kilaini anajua biblia kuliko Pengo? Biblia hutumika kufikisha ujumbe na anayeitumia huchagua kipengele kinachokidhi malengo anayokusudi kufikisha ujumbe kwa waumini na kwa hili ujumbe ulikuwa ni kumpigia kampeni JK, sasa je, ni haki Kilaini kutumia Jukwa la dini kufanya kampeni?

Jamani kwa walio karibu na PENGO wanajua WAZI kwamba Pengo na wengine ndani ya KANISA hakubaliani na kauli ya Kilaini kwamba Kikwete ni Chaguo la MUNGU tena katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu. Kwanza naon hao waandishi wameandika kiwoga yaliyomo ni mazito zaidi. Waumini wengi hawatofautishi mahubiri na maelekezo ya kwenda kupiga kura na kwa mantiki hiyo, Kilaini ameingia ktk yale yanayofanywa na wanasiada tena baadhi wa upinzani kuanza kampeni za JK. Hii ni HATARI, tuacheni USHABIKI tuangalie hali HALISI
 
Issue nzima ni kuwa nikweli kauli aliyotoa pengo ni sawa na kumjibu kilaini tena direct, Klaini kasema JK safi ila watendaji wake wanamuangusha, baadae Pengo anasema hapana JK hawajibiki na asisingizie watendaji wake wa chini, Sasa ukiangalia kwa makini utaona hizi ni kauli mbili zinazo kinzana sana toka kwa viongozi wa juu wa kanisa hili.
Hii yote inaletwa na tabia ya sasa ya viongozi wa dini badala ya kutumia muda mwingi ku chunga kondoo wa bwana wanatumia muda mwingi kuchambua maswala ya siasa, si vibaya viongozi kuwataadharisha waumini wao kuhusu siasa lakini hii imekuwa too much. zamani viongozi wa dini hasa wakristo walikuwa na baraza la maaskofu ambalo ndilo lilikuwa linatoa misimamo ya makanisa lakini sikuhizi sherehe zote au iwe ni mazishi ya mtu maarufu basi mahubiri ni siasa tu.
Pengo na Kilaini ni watu wenye ushawishi mkubwa sana, haipendezi kuanza kutofautiana katika matamko yao yahusuyo siasa wakati wao ni watumishi wanaopaswa kuwaongoza kondoo wao nasasa wanawachanganya kwa kauli zao.
 
Hapa naona mjadala haujikiti kwenye hoja: Umejikita kwenye imani zaidi. Ina maana Kilaini anajua biblia kuliko Pengo? Biblia hutumika kufikisha ujumbe na anayeitumia huchagua kipengele kinachokidhi malengo anayokusudi kufikisha ujumbe kwa waumini na kwa hili ujumbe ulikuwa ni kumpigia kampeni JK, sasa je, ni haki Kilaini kutumia Jukwa la dini kufanya kampeni?
Hadhara ya Pengo ilikuwa ya kiimani ndiyo maana itatazamwa hivyo. mfalme Daudi alikuwa chaguo la Mungu lakini uovu wake, k.m kumuua Uria Mhiti kwa tamaa zake, aliwajibishwa. Kwa hiyo pamoja na kuwa 'chaguo la Mungu' viongozi wanawajibika binafsi kwa kazi zao!!
 
Wakati mwingine waandishi wasipostulate vitu ambavyo havipo... kwani nilazima iwe Pengo amjibu Kilaini? kwanini isiwe Pengo naye ana msimamo wake ambao hauusiani na msimamo wa Kilaini. Sasa akija na shemasi akisema kitu kingine kwenye mada hiyo hiyo itakuwa anamjibu Pengo.. na huo mnyororo wa majibizano utaishia wapi?
Magazeti nayo si ni biashara mkuu
 
Back
Top Bottom