Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,324
- 33,129
Rais wa Marekani, Barack Obama Thursday, September 10, 2009 11:14 PM
Rais Barack Obama wa Marekani, amekuwa rais wa kwanza wa Marekani kuambiwa muongo mbele ya maseneta wa bunge la kongresi. Rais Barack Obama wa Marekani, amekuwa rais wa kwanza katika historia ya Marekani kuambiwa muongo wakati akitoa hotuba yake kwenye bunge la kongresi la Marekani.
Seneta wa South Carolin toka chama cha upinzani cha Republican, Joe Wilson aliropoka kwa hasira "Unaongopa" kumwambia Obama wakati Obama alipokuwa akisoma hotuba yake kuhusiana na mageuzi anayotaka kuyafanya kuhusiana na masuala ya bima katika sekta ya afya ya Marekani.
Tukio hilo lilitokea wakati Obama akiwa amefikia karibia nusu ya hotuba yake ya dakika 40 wakati alipokanusha taarifa potofu zinazotolewa na wapinzani wake kuwa mageuzi hayo katika bima za afya yatatoa mwanya kwa wahamiaji holela.
Kwa mujibu wa gazeti la The Telegraph la Uingereza, Obama amekuwa rais wa kwanza wa Marekani kuambiwa muongo wakati akisoma hotuba yake kwenye bunge la kongresi la Marekani.
Kitendo hicho cha seneta Wilson kilizua kelele za "Aibu, Aibu" toka kwa maseneta wa chama cha Democratic.
Obama alimwangalia kwa mshangao seneta Wilsona na kusema "Sio Kweli" na kisha aliendelea na hotuba yake.
Mke wa rais Obama, Michelle Obama, akiangalia toka jukwaani alitingisha kichwa chake akionyesha kuchukizwa na kitendo hicho.
Hata baadhi ya maseneta wa Republican walionyesha kuchukizwa na kitendo cha Wilson kutoonyesha nidhamu kwa mkuu wa taifa hilo kubwa duniani.
Akiongea na CNN baada ya hotuba hiyo seneta wa Arizona, John McCain ambaye alikuwa mpinzani wa Obama katika uchaguzi wa urais uliopita, alisema kuwa kitendo cha Wilson ni cha aibu na aliongeza "Hakuna nafasi ya vitendo kama hivi kwa mtu yoyote yule, lazima amuombe radhi".
Wilson alikumbwa pia na hasira za wananchi na ilijitokeza kuwa watu wengi walianza kumsapoti mpinzani wake katika kiti cha useneta wa jimbo la South Carolin toka chama cha Democratic.
Baadae Wilson alimuomba radhi Obama kwa kitendo chake hicho akisema kuwa alishindwa kuzidhibiti hisia zake.
Wilson alijaribu kumpigia simu Obama kumuomba radhi lakini simu zake ziliishia kupokelewa na maafisa wa White House.
Kwa mujibu wa mageuzi ambayo Obama anakusudia kuyaleta katika mfumo wa afya wa Marekani, serikali ya Marekani itadhamini bima ya afya kwa wananchi wake wote na wastaafu watalipiwa bima zao na serikali.
Rais Obama kwa kukumbushia majaribio ya marais waliopita kufanya mageuzi hayo na kushindwa, alisema kuwa yeye siyo rais wa kwanza wa Marekani kujaribu kufanya mageuzi kwenye mfumo wa Afya lakini amejiandaa kuwa rais wa mwisho kufanya hivyo.
http://www.nifahamishe.com/NewsDetails.aspx?NewsId=3053954&&Cat=2