Ndugu zangu,
Kuna tuliopata bahati ya kuyakumbuka tuliosimuliwa zamani. Ni mambo yenye elimu kubwa inayofaa maishani.
Naam, palipata kutokea nchi kwenye bahari ya giza. Nchi hiyo ilikuwa ikitawaliwa na mfalme maarufu sana. Aliitwa Mfalme Ihsani. Mfalme alikuwa mtu mwema. Alikaa vema na raia wake. Alikuwa ni mwingi wa hekima na busara.
Mara zote, Mfalme alikaa akitafakari namna ya kuwapatia raia wake mambo mema yenye kuwafaa. Akatafuta wataalam wa kuisukuma nchi mbele kimaendeleo. Akawaita waalimu, akajenga mashule watu wasome; mijini na vijijini.Naam. Mfalme alifahamu, kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila elimu.
Nchi ikawa na raia wenye maradhi mengi. Mfalme akatambua, kuwa nchi haiwezi kujengwa na wagonjwa. Ndio, duniani hakuna shamba la mgonjwa. Mfalme akatia jitihada za kusomesha matabibu. Kisha akajenga vituo vya tiba. Maradhi yakaanza kutoweka. Raia wakawa wenye wingi wa siha.
Nuru ikamulika katika nchi ile. Maendeleo yakaanza kuonekana. Sifa zikatapakaa, na mfalme akasifiwa kwa jitihada , hekima na busara zake katika uongozi. Lakini, Mfalme Ihsani hakutosheka na mafanikio hayo. Akatia jitihada zaidi. Akaumiza kichwa kufikiri shida za watu wake.
Akabaini, kuwa raia wake walipata tabu sana kufika shuleni na kwenye vituo vya tiba. Mfalme akaanzisha mpango wa ujenzi wa barabara, mijini na vijijini. Raia wakapata ajira na ujira pia katika kufanya kazi ya ujenzi wa barabara.
Watu wa dunia wakasikia sifa za nchi ya Mfalme Ihsani. Wakatamani kuishi katika nchi hiyo. Wengi wakahama nchi zao kuhamia nchi ya Mfalme Ihsani. Watu hao walikuja wakiwa na vipaji mbalimbali vya kazi za ufundi na mengineyo. Wengine wakafanya kazi za biashara kwa kufungua maduka. Majengo zaidi yakahitajika na mahitaji mengine ya kihuduma kwa raia. Watu wa nchi ya Mfalme Ihsani wakaanza kupata maisha bora.
Aaa! Fitina ikaanza kuingia. Ni fitina zilizosababishwa na watu wenyewe wa nchi ya Mfalme Ihsani. Chuki ikaingia, hivyo basi mifarakano na makundi. Njia ya maendeleo ikawa imewekwa vizingiti vya mawe makubwa. Naam, nyota mbaya ikawa imeanguka katika nchi ile kwenye bahari ya giza.
Kuna waliongiwa shauku ya kukamata mbingu kwa mkono wakitarajia makubwa kwa njia haramu. Kadri siku zilivyokwenda, basi, chuki, choyo, husuda na fitina vilitamalaki. Na kubwa zaidi kukawapo na ubaguzi wa kimakundi. Fujo na zogo la kijamii likatawala. Nchi ikaanza kuangamia.
Na nchi yetu Tanzania, kama ilivyo kwa nchi ya Mfalme Ihsani, nayo imeanza kuingiwa na sumu ya ubaguzi wa kisiasa , kidini na hata kikabila. Na yote hayo yanasababishwa na chuki, choyo, husuda na fitina. Yoye hayo ni matendo ya kifisadi. Ni uoza wa kimaadili- A moral decay- ni rushwa.
Pavumapo Palile, Si Kazi Kudamirika! Na hilo ni Neno La Leo.
Maggid
Sweden, Ijumaa, Julai 29, 2011
MJENGWA - Picha, Habari & Matangazo
Kuna tuliopata bahati ya kuyakumbuka tuliosimuliwa zamani. Ni mambo yenye elimu kubwa inayofaa maishani.
Naam, palipata kutokea nchi kwenye bahari ya giza. Nchi hiyo ilikuwa ikitawaliwa na mfalme maarufu sana. Aliitwa Mfalme Ihsani. Mfalme alikuwa mtu mwema. Alikaa vema na raia wake. Alikuwa ni mwingi wa hekima na busara.
Mara zote, Mfalme alikaa akitafakari namna ya kuwapatia raia wake mambo mema yenye kuwafaa. Akatafuta wataalam wa kuisukuma nchi mbele kimaendeleo. Akawaita waalimu, akajenga mashule watu wasome; mijini na vijijini.Naam. Mfalme alifahamu, kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila elimu.
Nchi ikawa na raia wenye maradhi mengi. Mfalme akatambua, kuwa nchi haiwezi kujengwa na wagonjwa. Ndio, duniani hakuna shamba la mgonjwa. Mfalme akatia jitihada za kusomesha matabibu. Kisha akajenga vituo vya tiba. Maradhi yakaanza kutoweka. Raia wakawa wenye wingi wa siha.
Nuru ikamulika katika nchi ile. Maendeleo yakaanza kuonekana. Sifa zikatapakaa, na mfalme akasifiwa kwa jitihada , hekima na busara zake katika uongozi. Lakini, Mfalme Ihsani hakutosheka na mafanikio hayo. Akatia jitihada zaidi. Akaumiza kichwa kufikiri shida za watu wake.
Akabaini, kuwa raia wake walipata tabu sana kufika shuleni na kwenye vituo vya tiba. Mfalme akaanzisha mpango wa ujenzi wa barabara, mijini na vijijini. Raia wakapata ajira na ujira pia katika kufanya kazi ya ujenzi wa barabara.
Watu wa dunia wakasikia sifa za nchi ya Mfalme Ihsani. Wakatamani kuishi katika nchi hiyo. Wengi wakahama nchi zao kuhamia nchi ya Mfalme Ihsani. Watu hao walikuja wakiwa na vipaji mbalimbali vya kazi za ufundi na mengineyo. Wengine wakafanya kazi za biashara kwa kufungua maduka. Majengo zaidi yakahitajika na mahitaji mengine ya kihuduma kwa raia. Watu wa nchi ya Mfalme Ihsani wakaanza kupata maisha bora.
Aaa! Fitina ikaanza kuingia. Ni fitina zilizosababishwa na watu wenyewe wa nchi ya Mfalme Ihsani. Chuki ikaingia, hivyo basi mifarakano na makundi. Njia ya maendeleo ikawa imewekwa vizingiti vya mawe makubwa. Naam, nyota mbaya ikawa imeanguka katika nchi ile kwenye bahari ya giza.
Kuna waliongiwa shauku ya kukamata mbingu kwa mkono wakitarajia makubwa kwa njia haramu. Kadri siku zilivyokwenda, basi, chuki, choyo, husuda na fitina vilitamalaki. Na kubwa zaidi kukawapo na ubaguzi wa kimakundi. Fujo na zogo la kijamii likatawala. Nchi ikaanza kuangamia.
Na nchi yetu Tanzania, kama ilivyo kwa nchi ya Mfalme Ihsani, nayo imeanza kuingiwa na sumu ya ubaguzi wa kisiasa , kidini na hata kikabila. Na yote hayo yanasababishwa na chuki, choyo, husuda na fitina. Yoye hayo ni matendo ya kifisadi. Ni uoza wa kimaadili- A moral decay- ni rushwa.
Pavumapo Palile, Si Kazi Kudamirika! Na hilo ni Neno La Leo.
Maggid
Sweden, Ijumaa, Julai 29, 2011
MJENGWA - Picha, Habari & Matangazo