Ndoa za kizaramo kulingana na mila na desturi zao

Wakili wa shetani

JF-Expert Member
Nov 22, 2022
1,689
3,259
Desturi ya kuoana kwao.​

Wazaramu wakitaka mke, kwanza huenda kwa mjomba wa yule mwanamke, akampa khabari—ya kama: "Mimi namtaka mpwa wako kumwoa." Na yule mjomba humjibu: "Vema, lakini nataka mkalio wangu wa maneno, ndipo nikujue kama wewe mkwe wangu." Basi yule mume hutoa reale moja au mbili akampa yule mjomba mkalio wake. Tena huenda kwa babaye mtu, akampasha khabari—ya kama: "Mtoto wako ametokea mchumba anataka kamwoa." Babaye mtu hujibu: "Miye sina mashauri, maneno yote yako kwenu." Tena hurudi kwake yule mjomba kumsikiliza siku atakayokuja yule mchumba. Desturi ya Wazaramu babaye mtu hana idhini juu ya mtoto wake, ila amri ya mtoto wa kizaramu kila neno juu ya wajomba zake. Atakapokuja yule mchumba, atatoa fedha ampe mjomba, naye atawaita ndugu zake na jamaa zake, wagawane fedha. Maana yake desturi ya Wazaramu mtoto hurithi kwa wajomba, kwa baba yake hapati kitu.

Khalafu watamwoza yule mtoto mume. Na kuoza kwao hawaendi kwa mwalimu kufunga khutuba, ila huoza kwa mila yao na lugha yao, humwambia: "Ninakupa mwanangu wewe, ndiwe mumewe, mkae mkisikilizane." Na mume huitikia maneno yale. Na arusi hawafanyizi karamu kupika wali na kuchinja ng'ombe, ila hufanya pombe, wakaalika watu kuja kunywa.

Kadhalika kila ngoma huja — kibende, sangara, kufurahia arusi. Wala hawana desturi ya kutembeza bikra kuonesha kila mtu, ila yule mume, baada ya kupewa mkewe, humla bikra taratibu kama siku anazotaka mwenyewe. Ila iwapo hafai, kila siku anamtazama macho, tena hampati baada ya miezi sita, atashtaki mwanamke kwa mapazi, ya kama huyu mwanaume hafai.

Na wakishaoana, hawana desturi sana ya kuwachana, hukaa miaka mingi, wakazaa watoto na wajukuu. Na mumewe akifa, haolewi na mume mwingine, ila ndugu ya mumewe, au ndugu za mumewe wawe radhi kuolewa na mume mwingine, huko ndiko kuoana kwao Wazaramu.



Desturi za kuachana kwao.​

Mwanzo wa ugomvi katika nyumba mwanamume huwa kazi ya kufanyiza kupata masurufu ya kumpa mwanamke kula na nguo hana, na kulima shamba hawezi. Yule mwanamke huvumilia siku nyingi. Akiona taabu sana, humwambia; "Wewe mwanamume kama huniwezi niache." Na mume hukataa kumuacha, mwanamke hushtaki kwa pazi, akasema, kama aibu aliyo nayo mwanamume. Tena atamwacha, lakini anapomwacha—asitokee mume mara kumuoa, itakuwa daawa kubwa, maana atasema: "Huyu mwanamke asingalitaka kuachwa, ila wewe—ndiye uliyemfitini."

Namna ya pili mwanamke kutaka kuachwa, akimwona mwanamume hafai, kila siku wanakula wakilala, mara atataka kuachwa au mwanamume ametoka kufanyiza biashara, amepata fedha, na ile fedha hamwonyeshi mkewe, kila siku anaifukia katika shimo,au hutia katika mfuko akajifunga kiunoni, basi mwanamume huyo hawana siku nyingi wataachana.

Na kuachana kwao kama kuoana kwao. Hawaendi kwa mwalimu kuandika talaka ila yule mwanamume akiona uzia mwingj, huenda kule kwa mjomba wake akamwambia: "Mimi na mke wangu hatupatani." Basi akiweza kuwapatanisha— atawapatanisha. Na kama hawezi, mwanamume atasema: "Mimi mwanamke amenishinda, sasa pokea mwanao, amefika kwako." Hiyo ndio talaka yao. Yamekwisha maneno ya talaka.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom