Ab-Titchaz
JF-Expert Member
- Jan 30, 2008
- 14,631
- 4,225
Ndege Yaanguka, Yaua Wanne Mlima Kilimanjaro
Ally Sonda na Rehema Matowo, Moshi
WATU wanne ambao ni raia wa kigeni wanaodhaniwa kuwa ni watalii wamefariki dunia papo hapo, baada ya ndege ndogo waliyokuwa wakisafiria kuanguka kwenye Mlima Kilimanjaro.
Habari zilizopatikana jana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng'hoboko zilisema kuwa ajali hiyo ilitokea jana kati ya saa 5:00 na 6:00 mchana.
Kamanda ameitaja ndege iliyopata ajali ni aina ya Cesna 206 inayomilikiwa na kampuni ya kukodisha ndege ya East Africa Air Charter ya jijini Nairobi nchini Kenya na kwamba ilikuwa na abiria wanne na rubani wake.
Alisema ndege hiyo iliyokuwa imebeba raia hao wa kigeni wakiwa na rubani mwenye asili ya kiafrika inadaiwa ilikuwa ikitokea Kenya kuja Tanzania.
Kamanda alisema watu waliofariki ni wanaume wawili na wanawake wawili wote raia wa kigeni na kwamba, hadi jana jioni majina yao na uraia wa nchi wanakotoka ilikuwa haijafahamika.
Majeruhi wa ajali hiyo ambaye ni rubani (naye jina halijafahamika) amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC kwa matibabu na hali yake ni mbaya sana na miili ya marehemu imehifadhiwa kwenye hospitali hiyo.
Taarifa zinaeleza kuwa ndege hiyo imeanguka jirani ya kilele cha Mawenzi ambacho ni sehemu ya Mlima Kilimanjaro mita 4,000 kutoka usawa wa Bahari.
Haijafahamika mara moja kama ndege hiyo ilivutwa na mvuto wa asili wa mlima huo au iligonga miamba kutokana na mawingu mazito yaliyopo mlimani ambayo ni hatari kwa usafiri wa anga.
Hata hivyo, Kamanda Ng'hoboko alisema uchunguzi wa ajali hiyo umeanza kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama vya Kenya pamoja na kufahamu uimara wa ndege hiyo.
Hii ni mara ya pili kwa ndege aina ya Cesna kuanguka mkoani hapa, mwaka huu mwanzoni ndege aina hiyo ilianguka kwenye Mtaa wa Viwanda mjini Moshi na kuua watu wawili akiwemo rubani na kujeruhi watatu.
Mwananchi Read News