Miili yetu inapojibu mawazo yetu kwa maradhi!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
Kuna wakati mtu anaweza kulala kitandani akiwa mgonjwa, wakati mwingine akiwa mgonjwa hoi kabisa. Anaweza kwenda au kupelekwa hospitalini na huko akaambiwa kwamba hana tatizo lolote. Jambo linalofuata baada ya taarifa kama hiyo, ni mtu huyo kudhani kwamba amelogwa.

Miili yetu huwa inaathiriwa kwa kiasi kikubwa sana na mawazo yetu. Tunapokuwa kwenye hali ambazo zinatupa mawazo mengi, hofu, wasiwasi na fadhaa, huwa kunatokea mabadiliko kwenye miili yetu. Mabadiliko hayo huwa yanatokea zaidi kwenye matumbo yetu, Misuli na mishipa midogo ya damu. Kuna ushahidi mkubwa kuhusu athari za mawazo yetu kwenye miili yetu.

Maradhi kama vile maumivu ya eneo la nyuma ya shingo, maumivu makali ya tumbo, kujaa hewa tumboni, kucheuwa sana, Kifua kubana, kukosa choo na maradhi mengine ya aina hiyo, kwa kiasi kikubwa yanaweza kuwa yanasababishwa na mawazo yetu na sio kitu kingine kilicho nje yetu.

Kwa hiyo, ni kweli kwamba mawazo yetu wenyewe yanaweza kabisa kutuuwa kwa kutupa maradhi ambayo yanaweza kuwa na ugumu mkubwa kutibika hospitalini. Licha ya maradhi, mawazo yetu pia yanaweza kutuingiza kwenye kukata tamaa au kutufanya tukaingia kwenye mambo ya hatari ambayo vinginevyo tusingeweza kuingia au kuyafanya.

Kuna ukweli kwamba jinsi tunavyowaza ndivyo jinsi ambavyo pia tunatenda. Tukiwaza vizuri tutatenda vizuri na tukiwaza vibaya tutatenda vibaya. Haijawahi kutokea mtu kuwaza vibaya na matokeo ya kila analolifanya kuwa zuri, wakati pia haijawahi kutokea mtu kuwaza vizuri na mambo yake yakaenda kombo.

Karibu kila kitu hapa duniani kiko kama kilivyo kutokana na kuwaza kwa binadamu.

Katika kitabu cha Secret mwandishi Rhonda Byrne anasema kwamba mawazo yetu ni kama sumaku. Kwa kawaida sisi wanaadamu tumezungukwa na nguvu ambazo hatuzioni lakini zipo kwa hiyo Kwa jinsi tunavyofikiri hayo mawazo yanakuwa na nguvu ambazo zinavuta kila kitu tunachowaza, kiwe kizuri au kibaya, ni lazima kitarudi kilipotoka, ambapo sipengine bali kwako wewe mwenyewe.

Rhonda anazidi kuabinisha utendaji wa mawazo yetu kwa kutoa mfano wa ufanyaji kazi wa Luninga.
Kama wote tunavyofahamu kuwa kituo cha kurusha matangazo ya Luninga kunakuwa na minara inayosafirisha mawimbi na kuyageuza katika mfumo wa picha na hivyo kutuwezesha kuona matangazo ya luninga tukiwa majumbani kwetu.

Wengi wetu hatufahamu mitambo hiyo inafanya kazi namna gani, lakini tunafahamu kwamba kila chaneli ina mawimbi yake ambapo kila tukichagua chaneli fulani tunapata picha katika luninga zetu.
Tunachagua mawimbi kwa kubadilisha chaneli na ndipo tunapopata picha za matangazo kutoka katika chaneli hiyo.
Kama tunataka kuona picha na matangazo tofauti katika luninga zetu tunabadilisha chaneli kwa kutafuta mawimbi ya chaneli nyingine.

Sisi kama wanaadamu tuko sawa na mnara wa kurusha matangazo ya luninga na tuna nguvu kuliko minara ya kurusha matangazo iliyowahi kuwepo hapa duniani. Mawimbi yetu ndiyo yanayoratibu maisha yetu na ndiyo yanayoifanya dunia iwe kama livyo leo, kwani tunatengeneza mawimbi kutokana na namna tunavyowaza.

Ile picha tunayopata au tunayoiona kupitia mawazo yetu, sio sawa na ile tunayoiona katika luninga zetu sebuleni kwetu, bali ni picha ya maisha yetu!
Mawazo yetu yanatengeneza mawimbi na yanavuta kila tunachokiwaza na kuwa ndio maisha yetu halisi.

Iwapo tunataka kubadili chochote katika maisha yetu, basi inatulazimu tubadili chaneli na mawimbi kwa kubadili namna yetu ya kufikiri.

Mwandishi huyo anaendelea kusema, kinachosabisha watu wengi wasipate kile wanachokitaka maishani ni kwa sababu wanafikiria zaidi kuhusu kile wasichokitaka badala ya kile wanachokitaka. Hebu tujaribu kuchunguza mawazo yetu na kauli zetu, tutagundua siri kubwa. Kwani nguvu ya mawazo ipo na inafanya kazi.

Ugonjwa mkubwa sana unaowakabili wanadamu hapa duniani karne kwa karne ni ugonjwa wa “sitaki” au “sipendi” anabainisha mama huyo
Watu wameendelea kuuacha ugonjwa huu uendelee kutawala katika mawazo yao, vitendo vyao na kauli zao, wakiendelea kuzingatia yale wasiyoyataka au wasiyoyapenda. Anasema mwandishi huyo.

Kwa hiyo tunatakiwa kuyaratibu mawazo yetu kwa kuzingatia zaidi yale tunayoyapenda kuliko yale tusiyoyapenda au kuyataka, na kama tukiamua kwa dhati kabisa tunaweza kubadili maisha tunayoisha na kuishi maisha tunayoyataka na tunayoyafurahia.

Kutokana na namna tunavyofikiri mtu anakuwa mbaya au mzuri kwetu, kitu kinaonekana chenye thamani au cha kipuuzi na hali inakuwa nzuri au yenye kukera kutokana na jinsi sisi tunavyofkiri kuhusiana na vitu au mambo hayo.

Haiwezekani kabisa tukawaza na kuamini kwamba fedha nikitu kibaya na tukahangaika kuitafuta kama ambavyo tunafanya hivi sasa ambapo tunaiona ni kitu cha thamani sana. Haiwezekani tukawafikiria wengine kuwa ni wabaya au wenye roho mbaya na bado tukawapenda. Lakini hao hao tunapowafikiria kuwa ni wema tunajikuta tunawapenda tu.

Kama miili yetu hupatishwa shida na mawazo yetu kwa kupewa mizigo ya maradhi, inakuwaje tusikubali kwamba inabidi tuanze upya kujifunza kufikiri vizuri. Kuna ubaya gani tukitambua kwamba kila kitu kiko katika hali yake ya utulivu na uzuri yakiwemo haya maisha yetu, bali ubaya uko kwenye mawazo yetu. Kwa nini tusijue, kwamba miili yetu huwa inajibu kile tunachokiwaza kwa miili hiyo kuendelea kuwa na afya au kuborongeka. Tukiwaza vizuri tunaisitiri na tukiwaza vibaya tunaiathiri.

Siyo vibaya nikisema kwamba kama mtu atajikuta anaumwa maradhi ambayo anaambiwa kwamba ‘hayaonekani’ huko hospitalini hasa kama ni maradhi ya yanayohusiana na tumbo, kusagwa kwa chakula,tumbo kujaa hewa, kuumwa na kichwa, maradhi ya ngozi na maradhi mengine ya aina hiyo, hana budi kujiuliza kuhusu kuwaza kwake.

Inawezekana kabisa mwili unakuwa kwenye matatizo hayo kwa sababu ya hofu, mashaka, wasiwasi na fadhaa alizonazo mtu huyo.

Tukumbuke kila siku kwamba mwili ni mtumwa wa mawazo yetu. Mbele ya mawazo yetu mwili unakuwa hauna maamuzi, mwili hujibu au kuonyesha kile kinachokwenda kwenye mawazo yetu kwa njia mbali mbali.

Unapoonyesha kile kiendacho mawazoni mwetu, kwa kutufanya tuwe wagonjwa, ina maana kwamba tunawaza vibaya. Tiba ya matatizo mkama hayo ni sisi kuanza kuwaza vizuri kama kweli tunataka kuihami miili yetu kutoka katika kuharibika.
 
nice article, nadhani mawazo yetu yana athiri sana miili yetu na utendaji kazi wetu, ila hawa dada zetu tunaowaita girl friends wanachangia kutupa stress sana. i wish i can live my life without having one, but i need love n to be loved
 
Very good analysis ya body functions.
Hivi tumewahi kujiuliza ni kwa nini binadamu wengine wakipata hofu kubwa sana huishia kuharisha au tumbo kulegea kiasi cha kutapika?
 
Kwa mimi niliye mlokole nakubaliana na hiyo article ambayo I can quickly summarise kuwa hayo maelezo yako ndani ya ulimwengu wa kiroho. Ulimwengu wa kiroho una sehemu kuu mbili. It is dualistic in nature. Kuna sehemu ya Mungu ambao ni ulimwengu wa Nuru na Mema na upande wa pili wa Ibilisi ambao ni ulimwengu wa Giza na Maovu. Sasa yale yaliyoko ulimwengu wa Roho ili mwanadamu ayapate kutegemeana anayataka yapi inabidi yajidhihirishe katika ulimwengu wa mwili (damu na nyama) ambao unaonekana kwa macho. Ukiwa umeokoka utayapata mema ya Mungu kama la utayapata ya Ibilisi. Hakuna neutrality kwenye masuala haya. Uamuzi unao wewe kutumia Nafsi yako.

Kwa hiyo unachokiwaza maana yake unakuvuta kutoka ulimwengu wa roho ambapo kutegemeana na unavyoamini nidivyo yanavyokuja kwa haraka zaidi kujidhirisha. Na ulimwengu huu wa roho una kanuni zake. Ukiwa upande wa Mungu huna budi kuzifahamu kanuni zake ili unufaike na usalimike. Wengi kwa sababu ya dhambi ya Adam ya asili tumekuwa wajinga na tumeangukia ulimwengu wa Ibilisi wa ghiliba na hila nyingi. Ndiyo maana unaweza ukaikuta nchi inaathirika na kulaanika wakati wale walio wake Mungu kupitia Kristo hawaathiriki.

Ni somo pana hili. But I certainly agree na Mtambuzi.
 
Very good analysis ya body functions.
Hivi tumewahi kujiuliza ni kwa nini binadamu wengine wakipata hofu kubwa sana huishia kuharisha au tumbo kulegea kiasi cha kutapika?


yote hii ni mawazo tu, unakuta mtu anaharisha mara baada ya kuwa kwenye situation flan.mawazo huchangia sana kutuharibu.

good article!!!maneno kama haya ndo tunayataka jf na si kupiga kelele!
 
Kwa mimi niliye mlokole nakubaliana na hiyo article ambayo I can quickly summarise kuwa hayo maelezo yako ndani ya ulimwengu wa kiroho. Ulimwengu wa kiroho una sehemu kuu mbili. It is dualistic in nature. Kuna sehemu ya Mungu ambao ni ulimwengu wa Nuru na Mema na upande wa pili wa Ibilisi ambao ni ulimwengu wa Giza na Maovu. Sasa yale yaliyoko ulimwengu wa Roho ili mwanadamu ayapate kutegemeana anayataka yapi inabidi yajidhihirishe katika ulimwengu wa mwili (damu na nyama) ambao unaonekana kwa macho. Ukiwa umeokoka utayapata mema ya Mungu kama la utayapata ya Ibilisi. Hakuna neutrality kwenye masuala haya. Uamuzi unao wewe kutumia Nafsi yako.

Kwa hiyo unachokiwaza maana yake unakuvuta kutoka ulimwengu wa roho ambapo kutegemeana na unavyoamini nidivyo yanavyokuja kwa haraka zaidi kujidhirisha. Na ulimwengu huu wa roho una kanuni zake. Ukiwa upande wa Mungu huna budi kuzifahamu kanuni zake ili unufaike na usalimike. Wengi kwa sababu ya dhambi ya Adam ya asili tumekuwa wajinga na tumeangukia ulimwengu wa Ibilisi wa ghiliba na hila nyingi. Ndiyo maana unaweza ukaikuta nchi inaathirika na kulaanika wakati wale walio wake Mungu kupitia Kristo hawaathiriki.

Ni somo pana hili. But I certainly agree na Mtambuzi.


Wale wanye neema ya kutambua mambo ya ulimwengu wa roho 2mekusoma, Karibu ufufuo na uzima.
 
Back
Top Bottom