Mifumo ya ubaguzi haipaswi kukumbatiwa

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,015
Jumapili Jan 25, 2009

• Mifumo ya ubaguzi haipaswi kukumbatiwa

Habari Zinazoshabihiana

Na Peter Masangwa
Majira​

INASIKITISHA Tanzania kugeuka uwanja wa mapambano kati ya wanafunzi wa elimu ya juu na Serikali yao wanayoipenda kwa dhati. Vijana wanaojaribu kuinusuru nchi wanaitiwa askari wa kutuliza ghasia maarufu kama FFU, hii inashangaza na haielezeki.

Migomo si jambo geni hapa duniani. Lilikuwa likitumiwa sana karne ya 19 kama njia ya kudai haki na maslahi ya watu hasa nchini Uingereza wakati wa mapinduzi ya viwanda. Migomo hiyo ilisaidia kwa kiasi kikubwa sana katika kuboresha maslahi na maisha ya Waingereza wakati huo na hata leo matunda yake yanadhihilika kwa Dunia yote.

Tanzania nayo imekumbwa na misukosuko kama hiyo hasa katika Serikali ya awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete yenye kauli mbiu ya kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania. Ikiwa maisha hayo mpaka sasa bado ni kitendawili kisicho tegeka kilichogubikwa na kero za namna yake pamoja na adha ya kila sumu ya ufisadi ndani ya utendaji.

Mwaka huu unaanza na kero hii ya wanafunzi wa elimu ya juu kwa kupinga sera ya uchangiaji wanayodai kuwa haina ukweli ndani yake na kuwa imejaa kila namna ya ufisadi, pia wamefikia hatua ya kumtaka Makamu Mkuu wa chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. Rwekaza Mkandara kujiuzuru kwa kushindwa kutekeleza wajibu wake hasa wa kuishauri Serikali katika kubadili sera hiyo ya uchangiaji huku akiwa anakili kuwa haina ukweli ndani yake inayolenga kuwagawa Watanzania katika matabaka kitu ambacho kinapingwa vikali na wanachuo hao.

Wanachuo hawa wa Mlimani wametangaza mgomo usio na kikomo kupinga kitendo cha baadhi ya wanafunzi kutokurudishwa kwa madai ya kutokamilisha kujaza ipasavyo fomu zilizotolewa na uongozi wa chuo hicho kwa masharti ya kurejea chuoni baada ya kuwa wamefungiwa kwa kufanya migomo na chuo kukifunga kwa kuhofia usalama wa wanafunzi na mali za chuo hicho.

Rai yangu kwa Serikali ni kuiomba itumie hekima na busara katika kutatua kero hii kwa wanafunzi hawa kwani wanachokipigania ni haki yao na wana kila sababu ya kufanya hivyo kwa maslahi yao na kwa wale wajao.

Sidhani kama wangekuwa na uwezo wa kulipa kiasi hicho cha uchangiaji wangediriki kufanya hayo wanayoyafanya, hivyo basi hii inadhihirisha kuwa hawana uwezo huo na hawana budi kusikilizwa.

Serikali haina budi kuendelea kufadhili elimu ya juu kwa asilimia 100 kama ilivyokuwa hapo awali ili kutoa fursa ya kila Mtanzania kupata elimu bora ili kuweza kunusuru nchi hii inayoendelea kushikilia mkia duniani kwa kuwa na uchumi mdogo.

Na hii itawezekana kama siasa uchwara zitafikia kikomo na wanasiasa hao kuamua kujenga nchi kwa maslahi ya Taifa zima na si kujinufaisha mmoja mmoja kwani hatutafika ng'o tunakotazamia kufika.

Chama tawala kimeingia na kauli mbiu yenye matumaini kwa kila mtu, katika kuleta maendeleo hivyo hayana budi kudhihirika dhahili kwa wanafunzi wa elimu ya juu kwa kuwadhamini bila madaraja yasiyo na ukweli wala hoja ndani yake isipokuwa ufisadi kwa lugha iliyojikita kwenye bongo za utawala wa awamu ya nne.

Takwimu zimeonesha mafanikio makubwa katika kila nyanja ya uchumi wa nchi hii hivyo Serikali haina namna ya kufadhili elimu ya juu ili kujipatia umaarufu zaidi ukizingatia fedha nyingi zinazofadhili elimu ya juu zinatoka kwa wahisani.

Kwenye maadhimisho ya siku ya mlipa kodi, TRA ilionesha kuvuka kiwango katika ukusanyaji kodi na kujinadi kuongeza ukusanyaji kwa mwaka huu maradufu. Kweli kwa hili wana kila sababu ya kujisifia.

Chakushangaza faida hizO hazijulikani zinaboresha nini baadaye badala yake zinaonekana kama takwimu tu katika kuwarizisha wananchi hasa tabaka kubwa la Watanzania ambao halina elimu ya kutosha.

Viongozi waliosoma bure sasa wanadiriki kuwanyanyasa vijana hawa kwa sababu kama unajua kuwa Watanzania hawana uwezo wa kuwasomesha watoto wao ndio maana elimu ya msingi ukaamuru itolewe bure, leo iweje elimu ya juu waigharimie au kuna matabaka yanaandaliwa ili wale wengi watakaoshindwa waendelee kuwa na maisha duni na kutawaliwa.

Ifike mahala Watanzania tuone haya na mifumo hii tunayoikumbatia ambayo ni kandamizi na baguzi kwa Taifa letu. Tuna kila namna ya kuunda mifumo ambayo itatusaidia na si kuiga kutoka nje. Elimu tunayo tena ya kutosha kwa nini tusiitumie kuondokana na adha hii. Hii ni aibu.

Naweza kuandika mengi na yakasomwa na wengi lakini wenye dhamana kama hawatakuwa na utayari wa kubadilika na kubadili mifumo mibaya katika kuisimamia maslahi ya waliowapa dhamana hizo nitamaliza wino bure. Kwani masikio hayawezi kuzidi kichwa.
 
Back
Top Bottom