Mfungwa aliyeonekana mitaani auawa kwa mawe

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
HASIRA za Wananchi za kuwaona watuhumiwa wa unyang’anyi wa kutumia silaha waliokamatwa na baadaye kurejea mitaani, juzi iliangukia kwa mtu mmoja ambaye alifungwa miaka 30 jela na baadaye kuonekana mitaani.

Wananchi wenye hasira katika Kijiji cha Kitandu wilaya ya Moshi Vijijini, wamemuua Mwananchi mmoja aliyetajwa kwa jina la Uamuzi Spend au Massawe (24) huku wakihoji inakuwaje mtu aliyefungwa miaka 30 jela anakuwa mitaani.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro,Yusuph Ilembo, alisema jana kuwa tukio hilo la kujichukulia sheria mkononi lilitokea juzi saa 2:00 usiku na hadi hiyo jana hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na mauaji hayo.

Ilembo aliwaambia waandishi wa habari kuwa siku ya tukio, wananchi walimuona marehemu ambaye walikuwa wanamtuhumu kuwa miongoni mwa majambazi sugu akiwa nje ya duka la mfanyabiashara Raymond Miratu (60).

“Wananchi wakaanza kuulizana hivi huyu si alikuwa amefungwa miaka 30 jela inakuwaje amerudi tena kijijini?... kwa hiyo kwa jinsi wanavyomfahamu wakajua moja kwa moja anataka kuiba kwenye lile duka”alifafanua Ilembo.

Wananchi wakiwa katika kundi kubwa walimkimbiza na kumkamata marehemu na kuanza kumshambulia kwa silaha mbalimbali za jadi na mateke na ngumi hadi alipofariki dunia ambapo maiti yake imehifadhiwa hospitali ya Mawenzi.


Hata hivyo habari zaidi kutoka kijijini hapo zilieleza kuwa Wananchi hao walikuwa wakiwanyooshea kidole polisi na mahakama kwa kuwaachia watuhumiwa ambao wao wanaamini upo ushahidi wa kutosha kuthibitisha ni majambazi.


Kaimu Kamanda Ilembo aliwataka Wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi kwani hilo ni kosa mbele ya sheria na kusisitiza umuhimu wa wananchi hao kuheshimu utawaka wa sheria na si kujichukulia sheria kwa hisia.
 
Back
Top Bottom