Pukudu
JF-Expert Member
- Jan 7, 2011
- 3,148
- 2,220
- Ndugu wanahabari habari za leo
Kwanza nawashukuru kwa kuitikia wito huu wa kukutana na kuzungumza nanyi kuhusu mambo mbalimbali yanayoendelea kuhusu chaguzi za CCM pamoja na malalamiko ya wanaccm na wananchi kwa ujumla mkiwemo hata nyie wanahabari wenzangu.
Naomba nianze moja kwa moja,sababu kubwa iliyonifanya niwaite hapa ndugu zangu wanahabari ni kuzungumzia habari za uchaguzi wa CCM .
Watanzania wenzangu na wanahabari nachukua muda huu kumuomba mwenyekiti wa CCM taifa na rais wa Tanzania kwa mamlaka yake aliyonayo kutengua baadhi ya matokeo ya CCM ambayo yamekuwa yanalalamikiwa karibu na kila mwanachama,mshabiki,na mpenzi wa CCM lakini pia hata wananchi wa kawaida.
Miongoni mwa maeneo ambayo ninaomba matokeo yatenguliwe ni pamoja na NEC Monduli kwa sababu kilichofanyika hakiendani na kanuni za CCM kwa mbunge kuomba kuchaguliwa pamoja na kwamba kanuni inakataa hata kama aliomba kibali kwa chama na mkoa lakini habari zilizopo ni kwamba hakuwahi kuomba kibali katika ngazi ya CCM wilayani wala mkoani na katika kibali hicho hatukuwahi kusikia katibu wa CCM mkoa wa Arusha akizungumzia hilo.
Matokeo mengine ni ninayoomba yatenguliwe ni pamoja na mwenyekiti Mkoa wa Mara,Mwenyekiti wa umoja wa Vijana wa CCM Taifa pamoja na Makamu wake,na zile nafasi zote za kuwakilisha vijana kwenda katika NEC,pamoja na baraza kuu la Vijana na nafasi zingine zote zilizohusu umoja wa vijana kwa kuwa rushwa ilitawala kupitiliza,mbali na rushwa viongozi walioshindwa asilimia 98 ya vijana wa nchi nzima inawapinga kutokana na uwezo wao kuwa mdogo kulinganisha na siasa za wakati huu ambazo zinahitaji sana uwezo wa kubuni na kufikiri na kupambana kwa kila hali.
Pia nimemuomba mwenyekiti atengue matokeo ya umoja wa wanawake wa CCM Tanzania kwa kuwa huko nako kulitawaliwa na Rushwa kubwa ambayo haina kifani.Lakini pia tunamuomba mwenyekiti na vikao vya juu vya chama kutengua matokeo yote yaliyolalamikiwa katika ngazi ya kuomba mkutano mkuu Taifa kutokea Wilayani pamoja na NEC kutokea Wilayani.
Ndugu watanzania wenzangu na wananchi,ndugu wanaccm wenzangu ndugu wanahabari kuyakubali matokeo haya ni sawa na kuhalalisha Rushwa kwenye chama na katika Serikali,kwa hiyo kwa heshima kubwa naamini mwenyekiti atatumia busara na hekima kubwa aliyonayo na aliyopewa na mwenyezi Mungu kuhakikisha anafuta chaguzi zote zilizolalamikiwa.Hatuwezi kusema ni chaguzi zote hapana yapo maeneo ambayo chaguzi zake zilikwenda vizuri na hakuna malalamiko yoyote,na ninaomba maeneo hayo yabaki kama yalivyo.
KUFUKUZWA UANACHAMA KWA BAADHI YA WANACCM KUTOKANA NA KUKIDHOOFISHA CHAMA NA SERIKALI YA CCM RUSHWA NA UFISADI:
Ndugu wanahabri na watanzania wenzangu natumia muda huu kumuomba mwenyekiti wa CCM taifa na rais wa Tanzania pamoja na vikao vya juu vya chama kwa maana ya kamati ya maadili na usalama ya CCM,kamati kuu ya CCM,Halmashauri kuu ya CCM,kuwanyang`anya kadi za uanachama Mbunge wa Monduli Edward Lowasa,Andrew Chenge,Husein Bashe,Beno Malisa,Martin Shigela,Nassor Moyo,Mansour Yusuf HIMID,Mahamud Thabit Kombo,Vedasto Mathayo,Lemeck Lacairo na aliyekuwa mwenyekiti wa Vijana mkoa wa Mara Marwa ambaye chini ya uongozi wake kwa kushirikiana na kundi lake BENO MALISA,HUSEIN BASHE walifanya kikao cha siri MARA NA ARUSHA na kumtukana na kumkejeli waziwazi mwenyekiti wa chama taifa na ushahidi upo ,Pia tunaomba vikao vya maamuzi vya juu vya CCM viwape Onyo kali rais mstaafu wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar Amani Abeid Karume kwa kuwa miongoni mwa wanachama na viongozi wanaoleta vurugu Zanzibar.
Ndugu wanahabari namhakikishia mwenyekiti wa ccm taifa kuwa baada ya utafiti wangu kama mwanahabari na niliyekuwa mgombea wa NEC taifa kupitia Bunda,bado yeye binafsi kama mwenyekiti wa chama taifa anaungwa mkono na kundi kubwa la vijana,na wakiwemo wale wa ccm na wananchi kwa ujumla,na wengi wako pamoja naye na kama akifanya maamuzi sahihi ya kufuta chaguzi hizi pamoja na kuwanyang`anya kadi hawa wanachama wasio waadilifu atakuwa amefanya jambo kubwa sana na la msingi ambalo ni la kihistoria katika chama na taifa kwa ujumla,na katika uchaguzi ujao 2015 CCM itashinda kwa kishindo kutokana na ukweli kwamba atakuwa amerejesha imani kubwa sana kwa chama hiki kikubwa Tanzania,afrika,na duniani kwa ujumla.
Ndugu waaandishi na watanzania wenzangu wazalendo,hawa ndio chanzo cha matatizo yote ndani ya ccm na serikalini yake,kwani tayari wamekuwa wanashirikiana na wapinzani kuidhoofisha serikali ya ccm pamoja na CCM yenyewe kwa maslahi yao,kwa sasa wameingia makubaliano na baadhi ya vyombo vya habari wakiwemo wamiliki kuhakikisha hawawaandiki wala kuwatangaza vibaya,isipokuwa watangazwe vizuri tu kuelekea katika uchaguzi mwaka 2015 wakiwa wasafi,wamekuwa wanapita misikitini,makanisani,katika taasisi za umma na binafsi wakijisafisha na kutoa hela ambazo ni haramu.Ni miongoni mwa watanzania wafanya biashara haramu ambao hawalipi kodi,wanatumia hela ya kutolipa kodi wanaisambaratisha CCM na serikali yake bila hata aibu,wanaitafuta ikulu mwaka 2015 kwa kuhonga ni hatari sana,na hawa ni wa kuogopwa kama ukimwi na wala siyo ukoma.
Aidha Ndugu watanzania wenzangu wapinga rushwa,tunaomba atengue matokeo ya uchaguzi wa umoja wa vijana mkoa wa Mara kutokana na vurugu zilizojitokeza kwa wanachama na wajumbe wa uchaguzi huo kupigana viti hadharani mbele ya vyombo vya habari,pia atengue matokeo ya NEC wilaya ya Bunda kwa kutawaliwa na Rushwa,pamoja na atengue matokeo ya NEC wilaya ya Musoma Mjini.lakini pia atengue matokeo ya uchaguzi wa mwenyekiti wa vijana mkoa wa Shinyanga kwa kuwa kulitokea na vurugu kubwa ikiwemo kutekwa kwa mmoja wa wagombea Richard Luhende akapigwa na kuumizwa vibaya na kushindwa kutokea siku ya zoezi la uchaguzi ambapo uchaguzi ulifanyika yeye akiwa amelazwa hospitali.
Ndugu watanzania wenzangu waadilifu na wapenda nchi yao kwa dhati,kumekuwa na mpango wa kumchafua mwenyekiti wa CCM taifa na Rais wa Tanzania Mhe.Jakaya Kikwete na familia yake kupitia mitandao ya kijamii kama Facebook,Twiter,UTUBE na baadhi ya Mitandao inayotokana na Facebook lakini pia kupitia mitandao hii kumekuwa na kundi la vijana wanaotumwa na baadhi ya wanaCCM MAFISADI kwa kushirikiana na Chadema kuitukana na kuidharirisha CCM na Serikali yake,lakini pia vijana hao hao wakifanya kazi ya kuwasafisha MAFISADI pamoja na CHADEMA ambacho tayari wameingia makubaliano kutochafuana na mafisadi wa CCM wakiwemo hata wafanyabiashara wakubwa na baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari kuhakikisha mafisadi wa CCM waliokuwa wanatajwatajwa kwa rushwa na ufisadi hawawasemi tena kwa ufisadi na rushwa bali wawasafishe tu kwa kila hali.
Ndugu waandishi wa habari na watanzania wenzangu ninaomba Serikali iwe makini na mitandao ya kijamii kwani imeletwa Afrika kwa lengo la kufanya mapinduzi na kuleta migogoro,tusipokuwa makini na suala hili na kulichukulia kawaida tu ama utandawazi kama tulivyozoea kusema,Tanzania tutaingia vitani,ama katika vurugu kubwa.Serikali kupitia wizara ya habari,mambo ya ndani,na vyombo vya ulinzi na usalama wawe makini na mitandao hii,ni hatari kwa mustakabala wa taifa letu.Watanzania tumekuwa na mazoea ya kujisahau kuwa mambo kama haya hatuwezi kuyazuia kutokana na teknolojia ya sasa,hapa tunaweza kuyazuia,mbona Ulaya na Marekani kumekuwa na adhabu zinatolewa kwa wale wanaotumia mitandao kutukana na kudharirisha wenzao ama kuitukana serikali ama viongozi wan chi husika..
Tusipokuwa makini na kuchukulia kawaida Tanzania yaweza kuwa kama LIBYA,TUNISIA,MISRI,SYRIA,na Maeneo mengine ambayo yameingia katika vurugu kubwa kwa kudharau kama tunavyofanya watanzania..
Waswahili walisema mdharau Mwiba mguu huota Tende..