Malawi - Tuhuma zaanza kuibuliwa dhidi ya utawala wa Mutharika

Candid Scope

JF-Expert Member
Nov 8, 2010
11,890
6,898
WAKATI aliyekuwa Rais Malawi, Bungu wa Mutharika akitarajiwa kuzikwa kesho, baadhi ya kasoro za utawala wake zimeanza kuwekwa hadharani huku wanaharakati wa haki za binadamu wakianza kuishinikiza serikali mpya ya Rais Joyce Banda kufanya uchunguzi wa utajiri wa kiongozi huyo. mMutharika ambaye siku ya kifo chake bado ina utata, anatarajiwa kuzikwa kesho katika shamba lake la Ndata, Wilaya ya Thloyo kusini mwa jiji la Blantyre katika mazishi ambayo yatahudhuriwa na wakuu wa nchi na Serikali wanane. Lakini zikiwa imebaki siku moja kabla ya kuzikwa kwake, utawala wake umeanza kuanikwa kuwa ulikiwa unakiuka haki za binadamu na vitisho vya wazi ambavyo aliwahi kuvitoa hata kwa wale aliowateua kushika madaraka pale walipomweleza ukweli kuhusu utendaji wa Serikali.

John Kapito ambaye ni Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu ya Malawi (MHRC) alisema alitishiwa kifo katika kikao baina ya wajumbe wa Tume yake na Rais Mutharika, lakini baada ya siku mbili tu alipata taarifa za kifo cha rais huyo. Kapito katika mahojiano yake na moja ya magazeti ya kila wiki alisema alipewa vitisho vya kuuawa mbele ya Mutharika katika kikao kilichokutana Ikulu, Lilongwe Aprili 3, 2012 wakati tume yake ilipokwenda kutoa taarifa kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Malawi. Gazeti hili lilizungumza na mwenyekiti huyo kwa siku akakiri kwamba mahojiano hayo ni ya kweli na kwamba hakuna kilichokosewa katika kile alichokisema. Mahojiano hayo nilifanya kwa maandishi kwa hiyo hakuna kilichopunguzwa wala kuongezwa kuhusu yale niliyosema,alisema Kapito ambaye anamaliza muda wake wa uongozi ndani ya MHRC, mwezi ujao.

Katika maeleo yake mwenyekiti huyo anamtuhumu Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Baraza la Mawaziri wa Malawi, Nicholaus Dausi kwamba alitamka wazi kuwa hata utawala wa kifalme wa Uingereza ulipobaini kwamba Dodi Alfayed na Princess Diana wanaisubua himaya ya malkia walimalizwa. Jana gezeti hili lilimtafuta Dausi kwa simu lakini alisema kwa kifupi: Katika hilo sina cha kusema, kisha akakata simu. Kapito alisema Daus alitoa tishio hilo baada ya Mutharika kuwa amemtuhumu yeye (Kapito) kwamba alikuwa akiifanya Malawi isitawalike kwa kushirikiana na wanaharakati wa ndani na nje ya nchi na kwamba alikuwa ameigeuza MHRC kuwa chama cha siasa cha upinzania.
Rais alinituhumu mimi binafsi na kwamba alilazimika kukutana na mimi kwa sababu tu ni Mwenyekiti wa MHRC, lakini vinginevyo hata tungekutana barabarani asingeweza kunisalimia,alinukuliwa Kapito. Hata hivyo, Mwenyekiti huyo wa MHRC alisema yeye alichukuliwa vitisho hivyo kama sehemu ya kazi yake kwani anatambua kwamba kazi anayoifanya inaweza kumfanya aozee jela au hata kuuwawa.

Machi mwaka huu, Kapito alikamatwa na polisi kwa tuhuma za kumiliki fedha nyingi za kigeni kinyume cha sheria na uchochezi, lakini hadi sasa hajafikishwa mahakamani huku kukiwa na taarifa kwamba tayari polisi wametupilia mbali mashtaka yake. Kapito alimnukuu Mutharika akisema yeye hakuhusika na kukamatwa kwake licha ya kwamba alithibitisha kumfuatilia kila alipokwenda iwe ndani au nje ya Malawi. Polisi pia wamekuwa wakitoa taarifa kwamba walimkamata Kapito kwa maelekezo ya wakubwa.

Uchunguzi wa mali
Katika hatua nyingine, jana jumuiya ya taasisi zisizo za kiserikali na haki za binadamu nchini Malawi zimeanza kuishinikiza Serikali ya Rais Joyce Banda kuanzisha uchunguzi wa kile zilizochodai kuwa ni utajiri wa kupindukia aliokuwa nao Mutharika. Mwito huo umekuja wakati kukiwa na taarifa kwamba rais huyo wa tatu wa Malawi alikuwa amejilimbikizia utajiri wa fedha ambazo ni mamilioni ya dola za Kimarekani na kwacha za Malawi katika benki za ndani na nje ya nchi hiyo.

Kadhalika kumekuwa na taarifa kwamba fedha nyingine zilikutwa katika Ikulu ya Malawi, Lilongwe na kwenye magunia zaidi ya 30 ya tumbaku ambayo yalikuwa yamehifadhiwa katika kasri yake aliyojenga katika, shamba lake la Ndata. Hata hivyo, hadi sasa vyombo vya usalama vya Malawi havijatoa taarifa yoyote kuhusu madai hayo ambayo watu wa kada mbalimbali nchini hapa wanataka yachunguzwe na taarifa zake zitolewe kwa umma. Profesa Masidizi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Chancellor, Edge Kanyongolo amenukuliwa akisema kuwa wasimamizi wa mali za Mutharika ndio wanaoweza kutoa maelezo kuhusu kile kinachodaiwa kuwa ni utajiri wake wa kupindukia.

Kuna uwezekano mkubwa wa Rais Banda kukubali kufanyika kwa uchunguzi huo kwani katika muda wa wiki mbili za uongozi wake ameunda Tume ya Kuchunguza mauaji ya aliyekuwa mwanafunzi wa mwaka wa nne katika Chuo cha Ufundi cha Chuo Kikuu cha Malawi, Robert Chisowa. Mwanafunzi huyo aliyekuwa mwanaharakati akiikosoa serikali ya Malawi kupitia jarida la chuo hicho alikutwa amekufa Septemba 24, mwaka jana katika mazingira ya kutatanisha lakini polisi walitoa taarifa kwamba Chisowa alijinyonga na kutoa ujumbe waliodai kwamba aliuandika yeye.

Juzi Rais Banda alitangaza tume ya kuchunguza kifo hicho na kuiapisha jijini Blantyre. Tume hiyo inaogozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Andrew Nyirenda huku wajumbe wake wakiwa ni Jaji wa Mahakama Kuu, profesa ambaye ni mtaalamu wa uchunguzi wa vifo vyenye utata na watumishi wengine wa umma wanaoheshimika nchini Malawi.

Utata siku ya kifo
Kumekuwa na utata kuhusu siku ya kifo cha Mutharika kutokana na kutofautiana kwa terehe ambazo zimekuwa zikiandikwa kwenye msalaba ambao uko mbele ya jeneza ulimowekwa mwili wake. Siku mwili ulipowasili Malawi, msalaba ulikuwa ukisomeka kwamba alifariki Aprili 7, 2012 na hata mwili wake ulipowekwa Ikulu kwa ajili ya kuagwa Jumamosi na Jumapili za wiki jana, msalaba ulikuwa ukosomeka hivyo. Hata hivyo, kulikuwa na mabadiliko ya tarehe wakati mwili huo ulipowekwa kwenye jingo la Bunge, Lilongwe kwa ajili ya umma kutoa heshima za mwisho kwani msalaba huo ulikuwa ukisomeka kwamba alifariki tarehe 5 Aprili 2012.

Aprili 5, ndiyo siku iliyotangazwa kwa mara ya kwanza na Ofisi ya Rais na Baraza la Mawaziri ya Malawi (OPC) katika taarifa yake iliyotangaza rasmi kisfo hicho Aprili 7, 2012 na kusainiwa Katibu Mkuu wake, Bright Msaka. Hata hivyo, mwili huo ulipopelekwa kaskazini mwa Malawi katika mji wa Mzuzu tarehe za kifo kwenye msalaba zilibadilika na kuandikwa Aprili 6, 2012, hivyo hadi sasa haifahamiki ni siku gani rasmi alipofariki Mutharika. Jana moja ya magazeti ya kila siku yalimnukuu mmoja wa makatibu wa OPC akisema kuwa tarehe iliyotangazwa na ofisi yake ndiyo rasmi, akimaanisha tarehe 5 Aprili.

Jana wananchi wa Blantyre na maeneo jirani katika kanda ya kusini mwa Malawi waliendelea kutoa heshima za mwisho kwa Mutharika katika Ikulu ya Sanjika na leo mwili wa kiongozi huyo unahamishiwa Ndata ili kuwapa fursa wananchi wa eneo hilo kumuaga rais wao.
 
Kwetu Tanzania Kikwete atakapomaliza muhula wake sitegemei kutokea yanayotokea Malawi, maana sisi tuna system yetu tofauti na yao.
 
Back
Top Bottom