Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,322
- 33,127
Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)
Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), limesema makali ya mgawo wa umeme yaliyotangazwa juzi, yamepungua kutokana na mtambo wa Kihansi kutengemaa, hivyo kuongeza uzalishaji wa nishati hiyo.
Jumatano wiki hii, Tanesco ilitangaza kwamba, nchi imeingia tena kwenye mgawo wa umeme kutokana na kuharibika kwa mtambo mmoja kwenye vituo vya kuzalisha umeme.
Vituo hivyo ni vile vya Kidatu, Kihansi, Pangani na Ubungo, ingawa taarifa hiyo ya Tanesco haikueleza upungufu huo ni wa megawati ngapi.
Katika taarifa hiyo, Tanesco pia haikueleza mgawo huo utakoma lini.
Meneja Uhusiano wa Tanesco, Badra Masoud, alisema jana kuwa pia, mbali na mtambo wa Kihansi kutengemaa, Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), imeongeza uzalishaji, hivyo kuzidi kupunguza pengo lililopungua kwenye gridi ya taifa.
Alisema Tanesco bado inaendelea na juhudi za kushughulikia mitambo iliyopata hitilafu na ikitengemaa taarifa itatolewa kwa umma. Masoud alisema kutokana na unafuu huo, kuna maeneo, ambayo hayataguswa na makali ya mgawo wa nishati hiyo.
CHANZO: NIPASHE