Maisha na Nyakati za Marehemu Edward Ngoyai Lowassa

Jana, Makamu wa Rais Dokta Philip Mpango aliwatangazia Watanzania kwamba Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa amefariki dunia jijini Dar es Salaam.

Tanzia hii inazungumzia matukio muhimukuhusu marehemu Lowassa ambaye alishika nyadhifa mbalimbali serikalini na kisiasa. Makala haitozungumzia wasifu mrefu wa marehemu Lowassa, kwa sababu hilo limeshafanyika mara kadhaa hata kabla hajafariki.

Kadhalika, matukio yatakayotajwa katika tanzia hii ni yale tu ambayo Jasusi anaamini kuwa yanaweza kusaidia kuieleza legacy ya mwanasiasa huyo.

Lakini itakuwa vema pia kutoa angalizo kabla ya kutaja matukio hayo, kwamba mila na desturi zetu zinakataza kuongelea mabaya ya marehemu. Hata hivyo, ni muhimu kuepuka “udikteta wa mila na desturi” hasa pale ambapo kuna haja ya kuweka kumbukumbu kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Kwahiyo, endapo baadhi ya matukio yatakayotajwa katika makala hii yatatafsiriwa kama “kumsema vibaya marehemu” basi ieleweke kuwa si kwa lengo baya.

Matukio muhimu katika maisha na nyakati za marehemu Lowassa
Pre-1995: Baada ya utumishi mrefu serikalini, marehemu Lowassa na aliyekuwa swahiba wake wakati huo, Jakaya Kikwete, walionyesha dhamira ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hata hivyo, Baba wa Taifa marehemu Mwalimu Julius Nyerere aliweka pingamizi kwa sababu ambazo hazijawahi kuwekwa hadharani. Hata hivyo, taarifa za kiintelijensia zilieleza wakati huo kwamba marehemu Nyerere alitatizwa na ukwasi kupindukia wa marehemu Lowassa.

Badala yao, chaguo la marehemu Nyerere lililikuwa marehemu Benjamin Mkapa ambaye alishinda urais katika uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995


1995-2005: marehemu Lowassa na Kikwete waliunda kundi la kisiasa lililofahamika kama “Mtandao” likiwa na lengo la kuingia Ikulu baada ya marehemu Mkapa kumaliza muda wake. Wawili hao walifahamika kama Boyz II Men wakilinganishwa na kundi maarufu la muziki la nchini Marekani

Licha ya marehemu Nyerere kutaka marehemu Mkapa kuwa rais mwaka 1995, pia ilifahamika kuwa chaguo lake kumrithi marehemu Mkapa pindi akimaliza urais wake mwaka 2005 lilikuwa kwa “kijana wake mwingine” Salim Ahmed Salim.

Hata hivyo, marehemu Lowassa na wana-Mtandao wenzie waliendesha kampeni chafu dhidi ya Salim, ikiwa ni pamoja na kudai kumhusisha na utawala wa Sultan uliotawala Zanzibar kabla ya mapinduzi.

Kadhalika, taarifa za kiintelijensia zilieleza kuwa marehemu Mkapa ambaye alikuwa na nia ya kutimiza matakwa ya marehemu Nyerere kwamba mrithi wake awe Salim, “aliwekwa mateka kisiasa” na kundi la Mtandao na kujikuta akiwa hana jinsi zaidi ya kulisapoti kundi hilo katika dhamira yake ya kuingia Ikulu.

2005-2008: Ndoto za urais za wanasiasa hao wawili hao zilitimia na Kikwete alichaguliwa kuwa rais mwaka 2005 na akamteua marehemu Lowassa kuwa Waziri wake Mkuu.

Japo hili hutolisikia sana, utawala wa Kikwete uliandamwa na skandali mbalimbali za ufisadi tangu ulipoingia madarakani, na Disemba 2005 kulianza kusikika fununu za ufisadi wa Richmond, huko marehemu Lowassa akituhumiwa kuwa mhusika mkuu.

Februari 2008: Kufuatia kashfa hiyo, marehemu Lowassa alilazimika kujiuzulu. Hata hivyo, taarifa za kiintelijensia zilibainisha kuwa marehemu Lowassa alikubali kujiuzulu ili kumkinga swahiba wake Kikwete.


2008-2010: kwa mujibu wa taarifa zisizo rasmi, inaelezwa kuwa kulikuwa na makubaliano kati ya Kikwete na marehemu Lowassa kwamba Waziri Mkuu huyo wa zamani “apokee kijiti cha urais” mwaka 2010. Hata hivyo, inadaiwa kuwa makubaliano mapya yalifikiwa kwamba marehemu Lowassa amwachie Kikwete amalize mihula miwili kisha yeye agombee mwaka 2015.

2010 - 2014: marehemu Lowassa alikuwa kama “rais anayesubiri tu muda wa kuapishwa” hapo 2015.

2014 - 2015: Taarifa zinaeleza kuwa kulijitokeza mfarakano kati ya Kikwete na marehemu Lowassa ambaye alikuwa anasubiri tu swahiba wake amalize muhula wake wa pili kisha yeye aingie madarakani. Kufuatia mfarakano huo, chaguo la Kikwete la mtu wa kumrithi likageuka kuwa marehemu Bernard Membe badala ya marehemu Lowassa.

2015: Licha ya tofauti zake na Kikwete, marehemu Lowassa aliendeleza kampeni zake za kuwania urais kwa tiketi ya CCM huku mpinzani wake mkuu akiwa marehemu Membe.

Hata hivyo, ndoto zake za urais kupitia CCM zilifikia kikomo baada ya jina lake kuchujwa na chama hicho tawala. Bila kuchelewa, marehemu Lowassa akaamua kujiondoa CCM na kujiunga na Chadema.

Wakati huo Chadema ilikuwa kwenye umoja wa vyama vinne, uliofahamika kama UKAWA, ambao uliafikiana kumsimamisha mgombea mmoja. UKAWA ikampitisha marehemu Lowassa kuwa mgombea wake.

Huko CCM, marehemu Membe aliishia kwenye “tano bora”

na hatimaye chama hicho kilimpitisha marehemu John Magufuli kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho.

Yayumkinika kutanabaisha kuwa Tanzania haijawahi kushuhudia mchuano mkali kwenye kinyang’anyiro cha urais kama ilivyokuwa kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, huku marehemu Lowassa na marehemu Magufuli wakionekana kuwa na takriban nafasi sawa za kuibuka washindi

Hata hivyo, hatimaye marehemu Magufuli alishinda uchaguzi huo. Japo awali marehemu Lowassa alionyesha kutoyatambua matokeo, baadaye suala hilo liliishia kimyakimya.

2019: Marehemu Lowassa arudi CCM.Kimsingi, tangu mwaka 2018 kulianza kujitokeza dalili kwamba ni suala la muda tu kabla mwanasiasa huyo hajaachana na Chadema na kurudi CCM.

Hata hivyo, inadaiwa kuwa uamuzi wa marehemu Lowassa kurudi CCM ulichangiwa zaidi na misukosuko aliyokumbana nayo kutoka kwa serikali ya marehemu Magufuli hususan kwenye biashara zake mbalimbali.

Jumamosi Februari 10, 2024: Waziri Mkuu huyo wa zamani Lowassa afariki.

Hitimisho
Kwa bahati mbaya – au pengine kwa makusudi – nafasi ya Marehemu Lowassa katika siasa za Tanzania haikuongelewa sana wakati wa uhai wake, na kwa bahati mbaya, “udikteta wa mila na desturi zetu unaotaka kuongelea mazuri tu ya marehemu” unaweza kuwa kikwazo kwa wachambuzi kuangalia pande zote mbili za mwanasiasa huyo mkongwe, na ambaye kwa wakati fulani, alikuwa mwanasiasa maarufu kuliko yeyote nchini Tanzania.

Moja ya mambo muhimu katika historia ya Tanzania, Chadema na marehemu Lowassa ambayo yayumkinika kusema “yamepuuzwa” ni swali hili: je ujio wa marehemu Lowassa huko Chadema ulikuwa ni asset au liability?

Swali la nyongeza: je Chadema kufanya vibaya sana kwenye uchaguzi wa madiwani wa mwaka 2019 na kupoteza takriban viti vyote kwenye uchaguzi wa wabunge mwaka 2020 kuna uhusiano na ujio wa marehemu Lowassa kwenye chama hicho?

Lakini pia kuna suala kubwa zaidi lililogubika uongozi wa marehemu Lowassa, ambalo ni ufisadi. Japo hakuwahi kufikishwa mahakamani kuhusiana na tuhuma hizo, tuhuma hizo zilitumiwa sana na chama chake cha zamani (wakati huo), CCM, dhidi ya kampeni za urais za marehemu Lowassa kwa tiketi ya UKAWA/Chadema.

Hata hivyo, habari njema kwake ni kwamba, Chadema ambayo ndiyo iliibua tuhuma za ufisadi wa Richmond, na iliwahi kumuita marehemu Lowassa kuwa ni “papa wa ufisadi” ililazimika kulamba matapishi yake na kuzunguka nchi nzima kumsafisha marehemu Lowassa

Pumzika kwa amani marehemu Lowassa
Hivi kumbe Kuna uchaguzi wa madiwani ulifanyika 2019 ? Kama hakuna basi bandiko lako lafaa lipuuzwe
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom